Chuo cha vijana cha Liverpool FC (Liverpool Academy) kinatarajiwa kufanyiwa mabadiliko makubwa, huku mipango ikitangazwa ya kufanya ukarabati zaidi wa miundombinu ya kituo hicho kilichopo Kirkby.
Uwanja wa sasa katika kituo cha vijana utajengwa juu yake jengo lenye dome litakalounganishwa na jengo la sasa la Academy, na litakuwa na uwanja wa ndani wa kwanza kabisa wenye ukubwa kamili kwa ajili ya matumizi ya mazoezi.
Uwanja mpya wa nyasi utajengwa eneo la nje ukiwa na jukwaa lenye uwezo wa kuchukua mashabiki 500, na hivyo kuwa kitovu kipya cha mechi zitakazochezwa hapo.
Mabadiliko yajayo pia yatakujumuisha maboresho makubwa kwenye huduma za kitabibu na sayansi ya michezo ili kusaidia maendeleo ya wachezaji chipukizi wa klabu.
Liverpool FC itawasilisha maombi ya kibali cha ujenzi muda si mrefu, huku lengo likiwa ni kukamilisha kazi hizo kufikia mwaka 2028.
Mkurugenzi wa Academy, Alex Inglethorpe, alisema kuhusu mradi huo:
“Huu ni ujumbe mkubwa.
“Wamiliki wameanzisha miradi kadhaa ya miundombinu katika miaka ya hivi karibuni, ikiwemo ukarabati wa majukwaa mawili Anfield, ujenzi wa Kituo cha Mafunzo cha AXA ili kutuweka wote kituo kimoja hapa Kirkby, na pia kukiboresha Melwood ili timu ya wanawake iweze kukitumia.
“Sisi kama academy tumekuwa wavumilivu siku zote tukijua nafasi yetu ipo wapi kwenye mpangilio, lakini sasa huu ndio wakati wetu na ni jambo la kusisimua sana.
“Hatujawahi kuwa na uwanja wa ndani wa ukubwa kamili unaolingana na vituo vingi vya washindani wetu. Ingawa napenda vijana wakue wakikabiliana na upepo na mvua za Kirkby, kuna siku nyingi tunalazimika kufuta mazoezi au ubora wa mazoezi kuathirika. Hii italeta mabadiliko makubwa sana.”
Awamu hii ya mabadiliko inafuata nyongeza kadhaa ambazo tayari zimefanyika katika Academy.
Kwa sasa kuna viwanja vidogo vilivyotengenezwa mahsusi kwa mechi za wachezaji wachache, eneo la ukuzaji wa uwezo wa mwili, eneo la mazoezi ya ujuzi binafsi, na pia uwanja wa padbol — mchezo maarufu unaochanganya soka, tenisi, mpira wa wavu na squash.
Taa mpya za mwanga (floodlights) pia zimewekwa ili kuhakikisha viwanja vyote katika eneo hilo vinaweza kutumika hadi nyakati za jioni katika kipindi chote cha mwaka.
“Tayari tunaanza kunufaika na mabadiliko yaliyofanyika majira ya kiangazi yaliyopita,” alisema Inglethorpe, ambaye amekuwa sehemu ya mfumo wa vijana wa The Reds tangu mwaka 2012. “Ni muhimu kwa wavulana na familia zao kuona uwekezaji huu.
“Siku zote tunajaribu kutathmini na kuleta ubunifu. Wavulana wanakuja hapa wakiwa na umri wa kuanzia miaka sita, mara nne kwa wiki – huwezi kupoteza ile haiba ya kipekee, lazima upate njia mpya za kuwafanya wapende kuwa hapa. Uwanja wa padbol unatumika vizuri, na vivyo hivyo na vile viwanja vidogo vya mazoezi.”
Mipango ya uboreshaji wa baadaye imetokana na utafiti wa kina uliofanyika kote Ulaya, ambapo Julian Ward – mkurugenzi wa kiufundi wa Fenway Sports Group – alitembelea zaidi ya vilabu 25 ili kukusanya taarifa na mbinu bora zaidi.
Baada ya hapo, mipango iliandaliwa kwa ajili ya ukarabati mkubwa zaidi wa Academy tangu ilipofunguliwa mwaka 1998.
“Nimemfahamu Julian kwa miaka 13 sasa na moja ya faida ya yeye kurejea si tu maarifa yake, bali pia ukweli kwamba ana uthamini wa kina kwa kile tunachofanya,” aliongeza Inglethorpe.
“Ameleta ushawishi chanya sana na amekuwa msaada mkubwa kwetu pale tulipoona kuna mapungufu kwenye miundombinu.
“Kiwango kimepanda sana sasa. Unachohitaji kufanya ni kuangalia tu muundo wa kikosi kwa sasa ukilinganisha na miaka 10 iliyopita. Ni vigumu kutambua kwa jinsi ubora na upana ulivyoongezeka, na hivyo changamoto kwa Academy zimekuwa kubwa zaidi – lakini ni jambo tunalolifurahia.
“Tamko letu kuu la dhamira ni kuwaandaa vijana kuingia kikosini wakiwa na uwezo wa kushindania mataji makubwa. Uwekezaji huu bila shaka utatusaidia kufanikisha hilo.”