Kifo cha Wangwe: Chadema yataka polisi wafanye uchunguzi wa kina
*Aliyekuwa na marehemu awekwa chini ya ulinzi
*Akiri kutembelea Libya, hana mafunzo ya kijeshi
*Anukuu maadiko: Kufa ni zawaidi kuishi ni Ukristo
Na Muhibu Said, Dar na Ramadhan Semtawa, Dodoma
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimelitaka Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina kuhusu kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe, kwa kujibu maswali saba yanayomhusu kijana aliyekuwa na marehemu wakati wa ajali iliyosababisha kifo chake.
Kijana huyo, Deus Mallya (27) (pichani), ambaye ni shuhuda wa kwanza wa ajali hiyo, juzi alikaririwa na gazeti hili akieleza kwa ufasaha namna ajali hiyo ilivyotokea katika eneo la Pandambili, Wilaya ya Kongwa, mkoani Dodoma, Jumatatu wiki hii na kusababisha kifo cha mbunge huyo aliyekuwa machachari.
Chadema imetoa maswali hayo, kupitia barua yake Kumbukumbu namba C/HQ/ADM/SG/02/85 ya Julai 30, mwaka huu, kwenda kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, kwa madai kwamba, mazingira ya ajali hiyo, yamegubikwa na utata.
Barua hiyo, ambayo imesainiwa na Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, imetaja sababu nyingine ya kutaka uchunguzi huo ufanyike kuwa ni kutokana na wabunge wa Chadema kupata taarifa za vitisho na kuzushiwa vifo kupitia ujumbe mfupi wa simu za mkononi (sms) na ujumbe huo kusambazwa.
Mnyika, ambaye pia ni Mkurugenzi wa Vijana Taifa wa chama hicho, ameeleza katika barua hiyo kuwa taarifa hizo za vitisho, ziliwahi kuripotiwa kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, ambaye pia, ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe.
Nakala ya barua hiyo iliyotumwa kupitia mtandao wa kompyuta, imenakiliwa kwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Lawrence Masha, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai nchini (DCI), Robert Manumba.
Mnyika amedai kuwa maelezo yaliyotolewa na Mallya kuhusiana na jinsi ajali hiyo ilivyotokea na kiti ambacho alikuwa amekaa wakati ajali inatokea, yameongeza utata.
Mnyika alidai kabla ya Mallya kutoa maelezo hayo, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Slaa, katika mahojiano yake na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC1) kupitia kipindi cha 'Jambo Tanzania', alielezea utata huo na kutaka Jeshi la Polisi lifanye uchunguzi wa kina.
Alidai taarifa ambazo zimetolewa na watoto wa marehemu walipohojiwa na vyombo vya habari, yakilinganishwa na maelezo ya Mallya, yanahitaji kupatiwa majibu ya kina.
Alisema Chadema kama mwathirika wa ajali hiyo, haiwezi kufumbia macho suala hilo, hasa baada ya kufuatilia kwa kina maelezo yaliyotolewa kwa nyakati na watu tofauti kuhusu ajali na hatimaye msiba huo na kwa vile ina maslahi ya karibu katika uchunguzi huo.
Kutokana na hali hiyo, alilitaka Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya usalama kufanya uchunguzi wa kina kuhusu mambo mbalimbali, ikiwamo kijana huyo (Mallya) aliyekuwa na Wangwe kwenye gari lake wakati anafariki dunia, ni nani na anafanya shughuli gani.
Pia, (Mallya) alienda Dodoma kufanya shughuli gani na ana uhusiano gani na marehemu na au familia yake (marehemu).
Vilevile, (Mallya) alikuwa amekaa kwenye kiti gani wakati ajali inatokea, ni nani alikuwa anaendesha gari wakati ajali na hatimaye umauti unamkuta Wangwe na mazingira gani yaliyosababisha ajali hiyo kutokea.
"Tunataka Polisi wachukue hatua stahiki za kisheria ili Deus Mallya akaisaidie polisi na kuhojiwa kwa kina juu ya suala hili kwani maelezo yake yana utata mkubwa sana. Jeshi la polisi liitoe ripoti ya uchunguzi huo mapema na kuiweka ripoti hiyo hadharani," alisema Mnyika kupitia barua hiyo na akaongeza:
''Tunapendekeza hatua hizo zichukuliwe mara moja kwani tunaamini kuwa kifo hiki kimegubikwa na utata mkubwa sana na haswa kutokana na maelezo ambayo yamekuwa yakitolewa na aliyeshuhudia ajali (Deus Mallya) pamoja na watoto wa marehemu.''
''Tunaamini kuwa utatupatia ushirikiano wa kina ili kuhakikisha kuwa hatua za haraka na za dharura zinachukuliwa mara moja kwa ajili ya kuujua ukweli wa kifo hiki tata.
"Tunaomba wabunge wetu wapatiwe ulinzi na pia taarifa hizo zifanyiwe kazi kwa kina,'' alisema Mnyika kupitia barua hiyo.
Akizungumza na Mwananchi mjini Dodoma jana, Mallya alisema anajuana na viongozi wa Chadema na kueleza kwamba, yeye ni mfanyabiashara.
Pia alisema anajuana na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na anamiliki kampuni ya uchapishaji wa majarida na vitabu, iitwayo Visitor Print, iliyoko Kinondoni, jijini Dar es Salaam.
Mallya, ambaye yuko chini ya ulinzi wa polisi, mjini Dodoma, alisema mara ya mwisho alipanga kusafisha picha za Wangwe alizopiga akiwa na nywele zilizosukwa kwa mtindo wa rasta ili aziweke kwenye jarida la marehemu.
Pia alidai anafahamiana na Zitto na kwamba, mara ya mwisho alimchapishia mbunge huyo jarida linaloitwa "Wajibu Wangu".
Alipoulizwa kuhusu kupata mafunzo ya kijeshi nchini Libya, Mallya, ambaye hana makovu licha ya jicho lake kuonekana limevia kwa mbali, alikiri kufika nchini humo, lakini akasema alikwenda na akawapo huko kwa siku nne kati ya Juni na Julai, mwaka jana.
Alisema katika safari hiyo, alikuwa pamoja na Mufti wa Tanzania, Sheikh Mkuu, Issa bin Shaaban Simba, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Makongoro Nyerere, Mbunge wa Iramba Magharibi, Juma Killimbah na kusisitiza kuwa mbunge huyo anamfahamu.
Kuhusu kupata mafunzo ya kijeshi, alisema hajawahi hata kuwa sungusungu wala mgambo.
Alisema baada ya kutoka Libya, alikwenda Uswisi na baadaye akarejea nchini.
Mallya, alisema fani ya usanifu aliipata Nairobi, nchini Kenya katika Chuo cha Mtakatifu Hubert baada ya kumaliza sekondari kidato cha nne.
Alisema aliacha kuendesha gari tangu alipokuwa chuoni hapo baada kupata ajali kubwa kati ya mwaka 1999 hadi 2001.
Alisema amesikitishwa na taarifa za watoto wa Wangwe kwamba ndiye aliyekuwa akiendesha gari kabla ya ajali iliyosababisha kifo cha baba yao kutokea.
''Inawezekana watoto walishinikizwa, lakini mimi ni jasiri, ni mkweli, na nitaendelea kuwa mkweli,'' alisema.
Kuhusu tuhuma kwamba ametumiwa kumhujumu Wangwe, alisema anachojua yeye ni kuwa kilichotokea ni ajali na si vinginevyo.
''Mimi ni mhubiri mzuri wa injili, ninamwamini Yesu na Paulo aliwahi kusema kufa ni zawadi na kuishi ni Ukristo,'' alisema Mallya.
Hata hivyo, kwa sasa Mallya yuko chini ya ulinzi katika hospitali ya mkoa wa Dodoma daraja la kwanza na askari anayemlinda alisema wamemweka chini ya ulinzi ili kuangalia asihujumiwe na pia kusaidia taarifa nyingine kutoka kwake kama watazihitaji.
Source: Mwananchi