Polisi wabeza ushahidi wa kifo cha Wangwe
Shadrack Sagati
Daily News; Thursday,August 07, 2008 @00:01
Polisi imebeza ushahidi uliowasilishwa kwao juzi na viongozi wakuu watatu wa vyama vya upinzani juu ya utata wa kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe (Chadema), kwa maelezo kuwa ushahidi huo ni wa kuokota mitaani.
Kamishna wa Polisi Paul Chagonja ambaye alipokea ushahidi huo juzi, aliliambia gazeti hili kuwa kilichowasilishwa na viongozi hao sio ushahidi bali ombi la kutaka jeshi hilo lifanye uchunguzi wa kina wa kifo cha Wangwe, kwa maelezo kuna utata.
Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia na Mwenyekiti wa TLP, Augustine Mrema, juzi walikwenda ofisini kwa IGP kuwasilisha kile walichosema ni ushahidi juu ya ujasusi na umafia wa Deus Mallya aliyekuwa na Wangwe wakati ajali iliyosababisha kifo chake (Wangwe) ilipotokea eneo la Pandambili, Dodoma, siku 10 zilizopita.
Mallya, kwa sasa yuko rumande baada ya kufikishwa mahakamani Ijumaa iliyopita, akituhumiwa kwa makosa matatu ya kusababisha kifo cha Wangwe, kuendesha gari kwa kasi na bila leseni. Kabla ya kwenda Polisi, viongozi wa upinzani waliwaambia wanahabari kuwa wana ushahidi, kuwa Mallya yuko kwenye mtandao wa Mafia na ana mafunzo ya ujasusi, hivyo wanaamini atakuwa amehusika kwenye ajali ya Wangwe.
Waliahidi kumpatia ushahidi huo IGP ili aufanyie kazi. Ni kweli wamekuja tukaonana, lakini hakuna cha ushahidi wowote juu ya yale waliyowaambia waandishi wa habari juu ya Deus Mallya na utata wa ajali. Wameniomba suala hilo polisi tutumie busara kubwa kutokana na utata uliopo, lakini hakuna ushahidi mwingine
kitu walichonisisitizia ni kwamba ajali ile ina maslahi kwa taifa, kwa Chadema hasa kutokana na maneno yanayosemwa, alisema.
Alisema kutokana na hali hiyo, viongozi hao walimwomba aamuru Polisi wafanye uchunguzi wa kina wa suala hilo na katika kipindi kifupi walimaliza mazungumzo. Kwa mujibu wa Chagonja, kwa vile viongozi hao hawakuwapo eneo la ajali Polisi wanaamini kuwa walichowaeleza ni mambo ya kusikia mitaani.
Kwa mujibu wa Kamishna huyo, Polisi wameridhika kwa kiasi kikubwa na uchunguzi uliofanywa na madaktari na taarifa ya madaktari wa familia. Aliongeza yeye binafsi alitarajia kupokea ushahidi mzito lakini badala yake viongozi hao hawakuuwasilisha na muda mwingi walizungumzia kuishukuru Polisi na Mkuu wa Mkoa wa Mara Issa Machibya, kwa busara walizotumia wakati wa vurugu kwenye msiba wa Wangwe.
Chagonja alisema; Waliniomba nifikishe shukrani zao kwa mamlaka za mkoa wa Mara. Kamishna huyo aliongeza kuwa baada ya majadiliano hayo, baadaye Mrema alianza kutoa maombi yake ya kutaka Polisi imrudishie vifaa vyake ambavyo vilikamatwa miaka kadhaa iliyopita. Mrema aliomba kama kesi dhidi yake imemalizika ni heri wamrudishie vifaa hivyo kwani ana kazi navyo, alisema.
Kamishna Chagonja alisema baada ya kupata maelezo hayo yeye aliwataka wao kama viongozi wa vyama vya siasa kutofanyia kazi mambo yanayosemwa mitaani. Chagonja alisisitiza kuwa ajali iliyotokea ni ajali ya kawaida na kwa kuwa viongozi hao hawakuwapo eneo la tukio hawawezi kukusanya ushahidi wa mitaani juu ya tukio hilo.
Kamishna huyo alisema baada ya kuona ushahidi huo hauisaidii Polisi, aliwaeleza kuwa busara wanayotaka polisi waitumie ni kwa wao kama viongozi wa watu kutofanyia kazi maneno yanayoweza kuhatarisha amani. Kuhusu tamko la familia, Chagonja alisema kuwa tamko hilo halijafikishwa ofisini kwa IGP, hivyo hawezi kulizungumzia.
Sisi tunasema kama kuna watu wana ushahidi wakiwemo wana familia wajitokeze waje tuzungumze, watusaidie namna ya kupata ushahidi wa kile wanachodai". Bosi huyo wa Polisi alivitaka vyombo vya habari pia kuwa makini katika kuripoti masuala hayo, kwani baadhi ya mambo yanayoandikwa yanaweza kuzidisha chuki miongoni mwa jamii.