21/4/2007
Ndugu Jakaya Mrisho Kikwete
Rais
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ikulu
Dar es Salaam
Mheshimiwa:
RAI YA VIJANA KWA RAIS KUHUSU SUALA LA MIKOPO YA ELIMU YA JUU
Aprili 17, 2007 Uongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam(UDSM) uliwasimamisha masomo wanafunzi wote wa shahada ya kwanza kutoka kampasi ya Mlimani, Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu cha Changombe, Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu cha Mkwawa, Chuo Kikuu Kishiriki cha Ardhi na Taaluma ya Usanifu wa Majengo, na Taasisi ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano ya Umma. Aidha Chuo Kikuu cha Sokoine (SUA) nacho kimechukua uamuzi kama kwa wanafunzi wake. Sababu ikiwa ni migomo ya wanafunzi kupinga uchangiaji wa asilimia 40 ya gharama ya elimu pamoja na ada ya matibabu (laki moja kwa upande wa UDSM). Baada ya vyuo kuchukua uamuzi huo kauli mbalimbali zimetolewa kupitia vyombo vya habari na uongozi wa wanafunzi (kupitia DARUSO, TAHLISO, SUASO), Serikali ( Wizara inayohusika, Waziri Mkuu nk), wanafunzi, wazazi, Asasi za Kiraia (LHRC, TANLET nk), vyama vya siasa (CUF, NCCR,TLP, UPDP), wabunge (wakiwemo wa CHADEMA), wazazi, viongozi wa dini na baadhi ya wananchi kwa ujumla. Kwa kipindi cha zaidi ya wiki moja CHADEMA tumelifuatilia kwa karibu suala zima na kutafakari matukio yaliyotokea na hoja mbalimbali zilizotolewa. Tunatoa rai kwa kuzingatia zaidi matukio na misimamo kuhusu suala hili katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam tukiamini kwamba maamuzi ya utatuzi wa suala hili katika chuo hiki yatahusisha pia vyuo vingine vya umma. Kwa barua hii vijana wa CHADEMA tunawasilisha kwako Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania rai kwa ofisi yako ili kuchukua hatua na kutoa mwelekeo kuhusu suala hili kwa kuzingatia yafuatayo:
1. Ofisi yako iweze kuwasiliana na Uongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam ili kusimamisha(suspend) utaratibu na masharti yaliyotolewa kwa wanafunzi ambayo wanapaswa kuyatimiza kabla ya Mei 4, 2007 ili kuweza kuendelea na masomo. Masharti ambayo yameelezwa kwamba kama mwanafunzi hayatimiza hapaswi kuandika barua chuoni wala kurejea masomoni. Serikali isitishe utaratibu wa malipo ya wanafunzi kuchangia 40% (wa mwaka wa kwanza), na kulipa ada ya matibabu (laki moja) na wanafunzi kwa ujumla wao warudishwe bila masharti. (Masharti haya na mengine yalitolewa na UDSM kwa taarifa yake kwa vyombo vya habari la Aprili 18, 2007).
2. Kama Uongozi wa Chuo hauwezi kusitisha masharti hayo (hususani Sharti la Wanafunzi kulipa 40% na ada ya Matibabu kupitia benki na kuwasilisha hati ya malipo(pay-in-slip) pamoja na barua kabla ya Mei 4, 2007 kama kigezo cha Msingi cha kurudishwa masomoni), basi ofisi ya Rais itoe maelekezo kwa wanafunzi wa vyuo wasio na uwezo ni wapi wawasilishe maombi yao ya kusaidiwa kukopeshwa 40% na ada ya matibabu na kupewa hati za malipo(pay-in-slip) mapema iwezekanavyo ili wawahi kuwasilisha barua zao waweze kuendelea na masomo yao. Hii ni kwa sababu Mheshimiwa Rais uliahidi Februari 3, 2007 kwamba hakuna mwanafunzi atakayeshindwa kuendelea na masomo kutokana na michango hiyo na Waziri Mkuu amerudia kusisitiza kwamba Serikali itatekeleza ahadi hiyo (Rejea hotuba ya Waziri Mkuu alipoahirisha Kikao cha Bunge cha Aprili,2007).
3. Ofisi yako ielekeze Wizara inayohusika kuendesha mjadala kuhusu Uchagiaji wa Elimu ya Juu nchini kabla ya Bunge kujadili bajeti ya Mwaka wa Fedha 2007/2008 ili kuepusha migogoro katika vyuo vya elimu ya juu nchini ambayo kwa kiasi kikubwa inasababishwa na suala hili. (Rejea taarifa ya Tume iliyoundwa na serikali miaka ya hivi karibuni kuchunguza vyanzo vya migomo na migogoro katika elimu ya juu). Baadhi ya mambo muhususi yanayopaswa kushughuliwa ni: Mifumo ya Uchangiaji wa gharama za elimu ya juu; Kusitisha mapendekezo ya mabadiliko ya Sheria na. 9 ya mwaka 2004 yenye kulenga kuimarisha uwekaji wa madaraja na viwango vya asilimia katika uchangiaji wa elimu juu; Haja ya kupandisha madaraja ya utoaji mikopo na kuweka stahili ya mikopo kwa wote wenye kupata udahili (admission); mifumo ya kutambua uwezo wa wanafunzi (means testing); Kiwango cha ruzuku na menejimenti/uendeshaji wa bodi ya mikopo na mifumo ya urejeshaji wa fedha za mikopo kwa wanafunzi. Tuko tayari kutoa maoni yetu ya ziada pindi utaratibu utakapotangazwa.
MISINGI YA RAI YETU:
Msingi wa Rai yetu ni masuala yafuatayo:
1. Mfumo wa uchangiaji uliopo hivi sasa unakinzana na Sera, Sheria na ilani ya Uchaguzi ya Chama kilichopo madarakani :
Mfumo wa uchangiaji uliopo hivi sasa unakinzana na Sera, Sheria na ilani ya Uchaguzi ya Chama kilichopo madarakani. Sera ya Elimu ya Juu ya Mwaka 1999 inazungumza kuhusu uchangiaji wa elimu kwa maana ya serikali kuwa na mchango wake na wananchi kuwa na mchango wake. Kwa mfumo ulioko hivi sasa mwananchi anabeba mwenyewe mzigo wa gharama ya elimu ya juu kwa asilimia 100%. Kupitia mfumo huu hivi sasa mwanafunzi anakopeshwa 60% (ambazo anawajibika kuzirejesha) na anapaswa kutoa 40%. Hivyo mfumo huu ni ubebaji wa gharama (cost bearing) na si uchangiaji wa gharama (cost sharing). Kwa upande mwingine, sheria na. 9 ya mwaka 2004 (sheria ya bodi ya mikopo ya elimu ya juu) haitamki uwepo wa mfumo wa kutoa mikopo kwa asilimia na madaraja badala yake inatamka kwamba wanafunzi wahitaji waliopata udahili wanastahili kupatiwa mikopo. Serikali imekiri kwamba sheria hii inatoa haki zaidi ya sera ya elimu lakini cha kushangaza katika kikao kilichomalizika cha Bunge imeahidi kuirekebisha sheria hii (kwa misingi ya mapendekezo ya awali yaliyotolewa na wizara husika mabadiliko hayo yanalenga kuhalalisha maamuzi yaliyokwisha kuchukuliwa hali ambayo itarudisha nyuma kasi ya kuongeza elimu ya juu nchini). Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (Uk 44. Imeahidi kuwezesha 12.5% ya wahitimu wa kidato cha Sita kufika Elimu ya Juu) pamoja na ahadi yako Mheshimiwa Rais wakati wa Kampeni (Mchinga ,Lindi Tarehe 23/8/2005 na maoeneo mengine), kwamba mtawezesha vijana wa kitanzania wapya 30,000 kuingia Chuo Kikuu kwa Mwaka. Katika mwaka 2005-2006 ahadi hii haijatekelezwa kwa ukamilifu wake (mfumo uliopo wa uchangiaji utakwamisha zaidi utekelezaji wa ahadi hii). Huu ni mkataba na wapiga kura na ni muhimu ahadi hii ikatekelezwa kwa kuwa tafiti zimeonyesha uwekezaji wa kina na makini katika elimu ya juu kwa mwaka mmoja huongeza pato la Taifa kwa asilimia 0.63 (Rejea Hotuba ya Bajeti ya Wizara husika 2006/2007) na kwamba ni msingi muhimu katika kutekeleza MKUKUTA na kutimiza Malengo ya Maendeleo ya Milenia (MDGs). Tunaamini busara zako katika suala hili zitalirudisha taifa letu katika mstari wa sheria na kutimiza matarijio ya wananchi.
2. Elimu ya Juu ni hitaji la Wananchi na Serikali yetu inao uwezo wa kuweka mazingira ya wanavyuo kuweza kusoma elimu juu :
Sababu inayotolewa ya kutokuwapatia udhamini (kwa kuwakopesha) kamili wanafunzi ni kwamba nchi yetu haina uwezo na kwamba kama uchumi wetu ukikua basi serikali itabadili maamuzi yake. Hayati baba wa Taifa-Mwalimu Nyerere aliwahi kutuasa wakati wa mjadala wa uchangiaji wa elimu kwamba kama taifa hatuwezi kujua gharama ya elimu mpaka tutakapojaribu ujinga ! Tunapaswa kujiuliza-kipi kinaaza elimu ama uchumi au vyote kwa pamoja ? Kama nchi ambazo zina uchumi wa chini kuliko ya kwetu zinawekeza katika elimu ikiwemo ya juu zaidi yetu ni kwa vipi tutaendelea kwenda mbele zaidi yao ?(Mathalani rejea viwango vya idadi ya wanafunzi katika nchi za SADC-Afrika Kusini 9.11%, Kenya 1.47, Uganda 1.23, Lesotho 0.98, Malawi 0.42, Msumbiji 0.33, Tanzania 0.27). Nchi za Asia Mashariki (The Tigers) walikuwa na nguvu ya kiuchumi kama sisi katika miaka ya 1960 lakini kwa pamoja na mambo mengine kuwekeza katika elimu ya juu wameweza kufikia hatua waliyoko sasa, kwa nini sisi tuendelee kutumia umaskini wetu kama sababu ya kutowekeza kwenye elimu ? Kama Mheshimiwa Rais ulitamka ukiwa kwenye ziara ya nchi za Scandnavia kwamba nchi yetu haina wataalamu wa kutosha wenye uwezo ndio maana tunaingia katika mikataba mibovu kwa nini tusielekeze nguvu katika kuwa na wataalamu wetu wenye uwezo wengi zaidi ?. Lakini sisi tunaamini kwamba nchi yetu inao uwezo hata katika bajeti hii inayoendelea kutumika hivi sasa. Kama ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) inaonyesha kwamba kwa mwaka 2005/06 shilingi bilioni 700 hazieleweki matumizi yake na tayari tumeshazidisha bajeti kwa bilioni 900. Kama serikali kwa kipindi hiki imeweza kusamehe kodi na kwa kiasi kikubwa kwa wafanyabiashara wakubwa kwa takribani bilioni 400. Kama tumeweza kuilipa kampuni ya Dowans (kampuni iliyotokana na Richmond) shilingi zaidi ya Bilioni 100(pamoja na kwamba mpaka sasa hawajaweza kutupatia umeme wa megawatts 100 kama ilivyokuwa katika mkataba). Kama tumeweza kuongeza idadi ya magari ya thamani (mashangingi) na semina elekezi. Ni dhahiri kwamba uwezo tunao ! Katika mwaka wa fedha 2005/06 (wakati ambapo hakukuwa na uchangiaji wa 40% wala madaraja katika utoaji wa mikopo) serikali ilikopesha jumla ya wanafunzi 42,729 ambayo ni sawa ya jumla ya shilingi bilioni 62.9 (Rejea Hotuba ya Waziri wa Elimu ya Juu akiwasilisha makadirio ya Bajeti ya Serikali 2006/07). Hivyo elimu ya juu ni gharama ambayo kama taifa tunaweza kuimudu. Kwa mantiki hiyo basi baada ya serikali kulipa 60% tunaamini kwamba kiwango cha 40% kilichobaki serikali inaweza kukimudu ndani ya bajeti inayoendelea hivi sasa kwa kubadilisha mafungu ya bajeti ama kuahirisha ulipaji (isipokuwa suala la kuwalipa wanafunzi kikamilifu kwa ajili ya kwenda mafunzo kwa vitendo ambalo lipaswa kufanyika sasa) mpaka mwaka wa fedha 2007/08. Izingatiwe kuwa fedha hizi ni mkopo kwa hiyo sio gharama zinazozama (sunk cost) ni uamuzi wa kutunisha mfuko wa bodi ya mikopo ambao kwa msingi wake wa kisheria fedha zake ni za mzunguko(revolving). Ikumbukwe kwamba elimu (ikiwemo elimu ya juu) ni hitaji kipaumbele kwa wananchi na taifa kwa ujumla. Ni dhahiri kwa muktadha wa Ripoti ya Hali ya Umaskini na Maendeleo ya Watu Tanzania (Poverty and Human Development Report) watanzania walio wengi hususani wa vijijini hawana uwezo wa kuchangia 40% ya elimu ya juu ambayo ni kati ya 500,000 na 1,500,000 ( ukijumlisha ada ya masomo, matibabu, gharama za mafunzo kwa vitendo na michango mingine).
3. Madai ya wanafunzi yameanza kutolewa mapema, na ahadi za kuyatatua nazo zikatolewa, ni vyema sasa yakapatiwa ufumbuzi :
Sera ya Uchangiaji wa Elimu ya Juu ilianza kutekelezwa kwa awamu kwa kuanzia awamu ya kwanza mwaka 1992 na awamu ya pili mwaka 2004/5 hivyo katika hali ya kawaida maandalizi ya utekelezaji wa awamu ya tatu yalipaswa kuanza mapema. Utekelezaji awamu hii ulianza kuleta migogoro tangu hatua za awali. Serikali iliahidi kulipatia ufumbuzi suala hili kwa pamoja na mambo mengine kuanza kutumia mifumo ya kutambua wanafunzi wahitaji wa mikopo na kuweka viwango (Means Testing) katika mwaka wa fedha 2006/07(Rejea hotuba ya Bajeti ya Wizara husika). Kushindwa kwa wizara husika kuweka utaratibu bora wa kuwatambua wahitaji na viwango mpaka sasa hakupaswi kuwa sababu ya kuweka mazingira ya wanafunzi wasio na uwezo kushindwa kuendelea na masomo na wala kuwataka wanafunzi wawasilishe hati ya malipo (pay-in slip) ndani ya siku 10 haiwezi kamwe kuwa njia bora ya kupima uwezo wa wazazi kuchangia elimu juu. Mara baada ya bajeti, utekelezaji wa uchangiaji wa awamu hii ulizua migogoro. Na hatimaye wanavyuo wakalazimishwa na utawala kusaini fomu za kukubaliana na utaratibu wa kulipa 40% kwa ahadi kwamba utaratibu utawekwa kwa ajili ya wasio na uwezo. Oktoba 22, 2006 Vijana wa CHADEMA tulitoa rai kwa wizara inayohusika kushughulikia suala zima mapema ili kuepusha migogoro na kuweka utaratibu ambao utawasaidia watanzania wasio na uwezo. Baada ya hapo zilifuata safari za wanafunzi wa vyuo mbalimbali kwenda Bodi ya Mikopo kuwasilisha hoja zao kuhusu kushindwa kulipa 40% (mathalani 16/1/2007 Wanafunzi wa SUA). Tarehe 28 Januari, 2007 Wanafunzi wa UDSM waliandamana mpaka Uwanja wa Jangwani kuwasilisha madai yako lakini siku hiyo hiyo, Waziri wa wizara husika-Prof Peter Msolla akasisitiza kwamba kuchangia asilimia 40 ni suala la lazima. Hatimaye ukafuata mkutano wako na wanafunzi wa vyuo vikuu vya Dar es salaam kama sehemu ya maadhimisho ya miaka 30 ya CCM tarehe 3 Februari 2007 katika Ukumbi wa Diamond Jubilee ambapo (baada ya kusikiliza risala ya wanafunzi) uliahidi (kama mwenyekiti wa chama tawala) kwamba utawasiliana na chama chako kutafuta ufumbuzi wa suala hili na kwamba taarifa zingetolewa baada ya mwezi mmoja kuhusu hatua ambayo ingefikiwa. Hatahivyo ukasisitiza pia kwa namna ya pekee kwamba hakuna mwanafunzi atayeshindwa kuendelea na masomo kwa kushindwa kulipa 40%. Machi 3, 2007 mwezi mmoja ulipotimia Chuo Kikuu kiliitisha mkutano na kueleza kwamba suala hilo bado linaendelea kushughulikiwa. Lakini cha kushangaza mwezi mmoja baadaye (3-6 Aprili 2007) Waziri Msolla akiwa katika Ziara ya Vyuo Vikuu Zanzibar alisisitiza kwamba serikali haina fedha za kutosha kulipia asilimia 40 ya gharama za elimu ya juu nchini na kwamba utaratibu wa kuchangia utaendelea ( Rejea Nipashe 7/4/2007). Kwa mzazi na mwanafunzi yoyote kauli hii ilitoa picha ya namna gani ahadi yako ya Machi 3 ilikuwa ikielekea kutelekezwa badala ya kutekelezwa !. Matukio yote haya yalitokea kipindi ambacho wanafunzi walikuwa wanakaribia mitihani yao ya kufunga semista huku katika baadhi ya vyuo matamko yakitolewa na utawala wa vyuo kwamba wanafunzi ambao hawatalipa 40% hawatapewa matokeo yao. Wakati malalamiko ya 40% yakiwa bado yanafukuta yakaibuka masuala mengine ambayo kwa maoni yetu yalichangia kuongeza kasi ya mgogoro : Mosi, wanafunzi kutakiwa na uongozi wa chuo kulipa ada ya matibabu shilingi laki moja (ambayo hata haikuwepo katika mkataba). Pili, wanafunzi walitakiwa kujiandaa kwenda katika mafunzo ya vitendo (field) lakini wakaelezwa kwamba watalipwa 3,600 kwa siku badala ya 6,000 kwa siku ambayo imekuwa ikitolewa (tofauti ya 2,400 ikiwa ni 40% ambayo wanafunzi walipaswa waongeze wenyewe). Ikumbukwe kwamba kwa lengo la kuboresha ubora wa wahitimu na utalaamu (professionalism), mafunzo haya kwa vitendo hufanyika nje na makazi ya kawaida ya mwanafunzi hivyo mwanafunzi hulazimika kugharamia usafiri, malazi, chakula nk ! Viongozi wa wanafunzi wakakutana na Katibu Mkuu wa wizara husika na kuelezwa kwamba hata waende popote, uamuzi wa wanafunzi kulipwa shilingi 3,600 utabaki palepale. Kwa maneno mengine suala la kuahirisha malipo ya 40% mpaka mwaka ujao wa fedha likawa halipo tena kama inavyoelezwa kwa sababu wanafunzi wanapaswa kwenda kwenye mafunzo kwa vitendo kabla ya bajeti ya Mwaka ujao wa Fedha. Makamu Mkuu wa Chuo-Profesa Rekwaza Mukandala akaweka wazi katika kikao cha Bunge la Wanafunzi kwamba hakuna namna yoyote ya kuwasaidia (zaidi ya kupunguza idadi ya siku au kuwapangia wanafunzi mafunzo kwa vitendo maeneo ya karibu makazi yao-hoja ambazo zilikataliwa kwa kigezo cha kupunguza ubora wa taaluma) na kama watagoma basi watafukuzwa. Hatimaye wanafunzi wakagoma (kiasi kikubwa kwa amani ukilinganisha na miaka mingine) na hata kabla ya kutimia siku 3 mfululizo za kutafuta ufumbuzi kama kanuni za UDSM zinavyoelekeza, wanafunzi wakasimamishwa masomo na Chuo kikafungwa. Kipindi hiki chote hakiwezi kuitwa kutoa siku mbili kwa serikali kama ambavyo baadhi ya viongozi wamekuwa wakilaumu. Mheshimiwa Rais, kwa kuwa umewahi kuwa Kiongozi wa Wanafunzi UDSM, ukipitia mtiririko wote wa matukio na kauli, utabaini jambo lililodhahiri ni kwamba wanafunzi wameingizwa katika mazingira ya misongo (pressure) hivyo taifa linapaswa kuwasaidia zaidi wa kuwalaani na katika kushughulikia suala hili viongozi wa wanafunzi wanapaswa kushirikishwa badala ya kutolewa kafara.
HITIMISHO :
Mheshimiwa Rais tunatambua kwamba wewe ni kiongozi uliyeahidi hususani katika hotuba yako ya kuzindua Bunge Disemba 30 mwaka 2005 kwamba utaongozwa kwa kushirikisha wananchi na kufuata ushauri wa makundi mbalimbali ya kijamii ikiwemo vyama vya siasa kwa kutanguliza mbele maslahi ya Taifa. Aidha Mheshimiwa Rais kwa nafasi yako ni Mwenyekiti wa Baraza la Mawaziri, hivyo tunaamini muongozo wako unaweza kutoa mwelekeo mwafaka kwa wizara na taasisi zinazohusika. Kwa upande mwingine, ni mwenyekiti wa chama kilicho madarakani hivyo ahadi zako ni msingi wa mwelekeo wa serikali iliyoko hivi sasa. Tunaamini utaichulia rai yetu kwa uzito unaostahili kabla ya tarehe ya mwisho iliyotolewa na Chuo kwa wanafunzi kuweza kutimiza masharti yaliyoelezwa. Tunaamini katika hatua ambayo suala hili limefikia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ndiye unayeweza kuwaepusha wanafunzi wa vyuo kushindwa kuendelea na masomo yao kwa sababu ya uchangiaji wa elimu ya juu nchini kama ulivyoahidi tukiamini kwamba kwa kuwa umepata wasaa wa kuzunguka nchi nzima unaielewa hali hali ya Taifa na wananchi wake na hivyo utachukua hatua za haraka kuepusha matabaka na migogoro katika elimu ya Juu nchini.
Tunatanguliza shukrani tukitarajia utaifanyia kazi Rai Yetu
John Mnyika
Mkurugenzi wa Vijana na Kaimu Katibu Mkuu
0754 694 553
vijana@chadema.net
www.chadema.net
Nakala : Makamu wa Wakuu wa Vyuo (UDSM, SUA) ; Rais wa Wanafunzi (DARUSO, SUASO) ; Vyombo Vya Habari