A
Anonymous
Guest
Katika video inayoonyesha tukio hilo, Inspekta huyo anaonekana akivuka barabara na kumfuata mwandishi kwa lengo la kumpora kamera.
Tukio hilo lilitokea wakati Wananchi wakishuhudia kibaka aliyekuwa amechomwa moto, ambapo Waandishi walikuwa kazini kama kawaida kurekodi na kuripoti tukio hilo.
Baada ya kushindwa kutekeleza azma yake kufuatia kelele za Wananchi, askari huyo alikimbilia kwenye gari, huku akiwa anaashiria kuwa huenda alikuwa amelewa. Waandishi walijaribu kumjulisha Kamanda wa Polisi kuhusu tukio hilo kwa kumpigia simu, lakini mara tu walipojitambulisha kuwa ni Waandishi, simu ilikatwa ghafla.
Baada ya tukio hilo, Waandishi walichukua hatua ya kuelekea Kituo cha Polisi cha Central kufungua jalada dhidi ya askari huyo, lakini walizuiwa getini na askari aliyekuwa na silaha pamoja na OCCD.
Walipomweleza kuhusu tukio hilo, OCCD ambaye pia alikuwepo eneo la tukio usiku huo, alidai kuwa hakushuhudia askari huyo akijaribu kupora kamera.
Waandishi walipoomba kufungua jalada, waliambiwa warudi kesho, jambo lililowafanya waulize kama kuna muda maalum wa kufungua jalada Polisi badala ya kupatiwa majibu ya msingi, waliambulia kufukuzwa kituoni kama watu wasio na haki.
Kutokana na hali hiyo, tunaomba kujua hatua gani zitachukuliwa dhidi ya Inspekta huyo, kwani ni jambo la kusikitisha kuona usalama wa waandishi ukivunjwa na wale wanaopaswa kuwalinda.
Ushirikiano kati ya askari na Waandishi ni muhimu, lakini vitendo kama hivi vinavuruga uhusiano huo na kuibua maswali