Wakili wa Moyo-19
ILIPOISHIA:
Nimekuelewa.
Brenda alikata simu na kumgeukia shoga yake aliyekuwa na kimuhemuhe cha kutaka kujua Hans alikuwa akisemaje.
Vipi mzushi alikuwa akisemaje?
SASA ENDELEA...
Brenda alimweleza mazungumzo yote waliyozungumza na Hans.
Mmh! Anataka kuniambia nini?
Sijui, wewe ndiyo unajua mlizungumza nini katika ahadi ya penzi lenu.
Uhuu! Mage alishusha pumzi na kusema:
Brenda unanishauri nini? Mage alionekana kama ametahayari kusikia taarifa za Hans.
Kwa vile upo katika hatua nzuri za harusi, huu si muda wa kuzungumza na Hans unaweza kuharibu kila kitu ukakosa bara na pwani, Brenda alimtahadharisha rafiki yake.
Eti eeh, sijui Hans anataka kuniambia nini?
Achana naye.
Mmh! Sawa.
Kwa vile muda ulikuwa umekwenda sana, kila mmoja aliingia kwenye gari lake kurudi nyumbani.
***
Brenda alipofika nyumbani kwao alikwenda kuoga na kupata chakula kisha alijifungia chumbani kwake na kuwasha Ipad yake na kuanza kuchati na marafiki zake kwenye Twiter na Skype.
Akiwa anaendelea kuchati simu yake iliita, namba ilikuwa ngeni aliipokea.
Haloo.
Haloo Brenda.
Abee, nani?
Brenda unaniuliza nani wakati tumetoka kuzungumza muda si mrefu.
Hans? Brenda aliuliza.
Ndiyo.
Unasemaje?
Brenda samahani sana.
Bila samahani.
Naomba unikutanishe leo na Mage.
Hans, si tumeisha ongea?
Hapana Brenda, kuna kitu cha muhimu sana nataka nizungumze naye kabla siku ya kesho.
Samahani Hans, nipo Bagamoyo sitarudi leo.
Naomba hata umpigie simu ili anisikilize hata kwa sekunde tano tu.
Hans kwanza samahani, hapa nipo na boy friend wangu, ana wivu sana naomba tuzungumze kesho, Brenda alidanganya.
Samahani, ila utakacho kisikia kesho usishangae najua Mage atafurahi.
Unataka kufanya nini Hans?
Nilitakiwa kumweleza Mage mwenyewe, kwa heri.
Hans alikata simu na kumfanya Brenda abakie na simu mkononi kama anatazama kitu cha kumshangaza. Alijikuta akijiuliza.
Hans anataka kufanya nini? Au anataka kujiua? Mmh! Ngoja nimweleze Mage maana sasa imekuwa kazi. Lakini kipi cha ajabu Mage akiolewa? Kwani alitaka akae vile mpaka lini? Hivi Hans ana shida na Mage au anataka kumvurugia maisha tu.
Brenda alijikuta akiwaza peke yake, wakati huo simu aliyopiga ilikuwa ikiita. Ilipokelewa upande wa pili.
Haloo shoga lete stori, Mage alipokea.
Mmh! Mtu wako ananisumbua sana.
Nani?
Hans.
Kakupigia tena? Mage alishtuka.
Ndiyo.
Brenda achana naye, kwa nini unamsikiliza?
Mage siwezi kumkatia simu kwa vile sina mgomvi naye.
Yaani hivi najiandaa kwenda kwa Colin, tulikuwa tuna chati tukaona haitoshi, tukaongea vilevile tukaona haitoshi, nimeamua kwenda kabisa kuonana naye uso kwa macho.
Duh!
Brenda, nimeamini Colin ananipenda sana.
Sasa ndiyo utulie.
Brenda, lazima nitulie Colin kaniahidi vitu vingi sana baada ya ndoa. Nina imani ndoto zangu nilizoziota kwa Hans zitakuwa mara kumi.
Basi ndiyo hivyo mtu wako, roho ya Mungu anatapatapa kama mfa maji.
Kwani alikuwa akisemaje?
Brenda alimweleza yote aliyoelezwa na Hans na alivyomdanganya, Mage baada ya kumsikiliza alishusha pumzi na kusema:
Kwani Hans anataka kuniambia nini? Mage aliuliza.
Akwambie nini! Yule mharibifu, huu si muda wa kumsikiliza, ukirogwa kumsikiliza tu ndoa huna.
Mmh! Nimekuelewa japo moyo unatamani kumsikiliza ili nijue anataka kusema nini?
La kusema hakosi, anaweza kukuvuruga akili na ndoa yako ukaiona chungu. Najua bado unampenda sana Hans, kama utampa nafasi narudia tena ndoa hakuna, Brenda alimtahadhalisha Mage.
Hata siku moja, labda siyo Mage mimi. Siwezi kuumizwa mara ya tatu, mbili zinatosha.
Basi ndiyo hivyo kuwa makini na Hans, kwa nini muda wote akae kimya, kusikia unataka kuolewa ndiyo ajifanye anakupenda sana.
Nimekuelewa basi wacha niwahi kwa mahabuba wangu.
Mambo si hayo.
Brenda alikata simu na kuendelea kuchati na mashoga zake.
***
Mlio wa simu ulimshtua Brenda aliyekuwa bado amelala. Alipoangalia ilikuwa namba ngeni, aliipokea.
Haloo.
Haloo, nazungumza na Brenda?
Ndiyo, nani mwenzangu?
Naitwa Ndubi rafiki mkubwa wa Hans.
Ndiyo Ndubi.
Kuna habari siyo nzuri.
Habari gani?
Hans amepata matatizo makubwa sana, nilijaribu kumpigia Mage simu yake haipatikani nikaona nikupigie wewe ili umjulishe.
Mmh! Matatizo gani?
Jana usiku wamevamiwa na majambazi nyumbani kwake. Mkewe na mwanaye wameuawa na yeye hatujui kama yupo hai.
Mungu wangu! Yupo wapi kwa sasa?
Yupo Hospitali ya Muhimbili, chumba cha wagonjwa mahututi.
Mungu wangu! Ngoja nimjulishe Mage.
Itakuwa vizuri.
Baada ya simu kukatwa, Brenda alimpigia simu Mage aliyekuwa bado yupo kwa mchumba wake Colin. Baada ya simu kuita kwa muda ilipokelewa upande wa pili.
Haloo Brenda mbona unaharibu pozi za watu, Mage alisema kwa utani.
Brenda hakupoteza muda alimweleza taarifa aliyopokea asubuhi ile. Taarifa ile ilimshtua sana Mage.
Mungu wangu! Yupo wapi?
Muhimbili.
Nakuja sasa hivi twende.
Noo, tutakutana hospitali.
Mage alinyanyuka kitandani na kupitia nguo zake na kuvaa bila kuoga.
Itaendelea..............