Kocha Diego Simeone anaonekana kama amekata tamaa na timu yake ya Atletico Madrid katika mbio za LaLiga kwa sababu ya kiwango cha nyota Barcelona, Lionel Messi.
Atletico imepunguza tofauti na kubaki tisa kati yake na vinara wa ligi hiyo Barca baada ya kushindi juzi bao 1-0 dhidi ya Deportivo La Coruna wakati ligi ikiwa imebaki michezo nane.
Barca ilionekana kama ingepoteza pointi kwa mara ya kwanza kabla ya Lionel Messi kuingia akitokea benchi na kuisawazishia timu yake kutoka kuwa nyuma kwa mabao 2-0 na kumaliza kwa sare 2-2 dhidi ya Sevilla.
Simeone anafikiri nyota huyo ndiye anayeleta tofauti kubwa kati ya timu hizo mbili kwa sasa.
"Tumekuwa katika wakati mzuri kwenye ligi msimu huu. Tumeona nini kilichotokea kwa Sevilla," alisema kocha huyo.
"Bila ya Messi, Sevilla wangeshinda 2-0. Kwa Messi kuwepo uwanjani, Barca imeshinda 2-0, japokuwa matokeo ya mwisho yalikuwa ni sare 2-2.
"Messi ni sababu ya mabadiliko hayo. Tunataka kuendelea kufanya vizuri zaidi ya ilivyokuwa msimu uliopita."
Atletico ambayo ilimkosa nyota wake Antoine Griezmann anayetumikia adhabu, ilipata ushindi mwembamba dhidi ya vibonde Deportivo, shukrani kwa bao penalti ya Kevin Gameiro katika kipindi cha kwanza.