DP WORLD: Mkataba wa Bandari kwa Kiswahili (tafsiri isiyo rasmi)

FaizaFoxy

Platinum Member
Apr 13, 2011
92,883
109,212
MAKUBALIANO YA KISERIKALI KATI YA:

ΤHΕ UNITED REPUBLIC 0F TANZANIA

AND
THE EMIRATE 0F DUBAI

DP Mkataba.png



UTANGULIZI

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,
iliyowakilishwa ipasavyo na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi (“Tanzania”) na SERIKALI YA DUBAI, iliyowakilishwa ipasavyo na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Bandari, Forodha na Ukanda Huru (“Dubai”);

(Tanzania na Dubai baadaye zinarejelewa kama “Nchi Wanachama” (kila moja kama “Nchi Mwanachama”):

(A) KWA KUZINGATIA ziara ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Falme za Kiarabu, Dubai Expo 2020 na kikao alichofanya na Mtawala wa Dubai Februari 2022 kuhusu fursa za uwekezaji nchini Tanzania;

(B) KWA KUZINGATIA Mkataba wa Makubaliano (MoU) kati ya Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na DP World (DPW) uliosainiwa katika ziara ya Mh. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Maonesho ya Dubai 2020 (Dubai Expo) tarehe 28 Februari, 2022;

(C) KWA KUZINGATIA matakwa yaliyotolewa katika Mkataba wa Makubaliano kuhusu maeneo ya ushirikiano kati ya TPA na DPW kwa ajili ya kuendeleza na/au kuboresha uendeshaji na usimamizi wa miundombinu ya kimkakati ya Bandari za Bahari na Maziwa Tanzania, kanda maalum za kiuchumi, hifadhi za usafirishaji na ukanda wa kibiashara wa Serikali ya Tanzania;

(D) KWA KUTAMBUA nia ya Serikali ya Tanzania ya kuhimiza uwekezaji ili kuendeleza na kuboresha utendaji na ufanisi wa bandari za bahari na maziwa ili kuendana na dira ya Serikali na mwenendo wa kimataifa wa huduma za usafiri
wa baharini;

(E) KWA KUZINGATIA matakwa ya Serikali ya Tanzania kutumia fursa na kufaidika na eneo lake la kijiografia katika usafiri wa baharini na kufungua uwezo wake wa soko katika ukanda huu kwa kuhudumia nchi zilizounganishwa na ardhi kupitia kuimarisha ushindani wa bandari na kuboresha shughuli za kijamii na kiuchumi;

(F) KWA KUTAMBUA uwekezaji mkubwa wa Serikali ya Tanzania uliofanywa katika kuboresha miundombinu na miundo mikuu ya aina mbalimbali nchini Tanzania ikiwa ni pamoja na Mradi wa Dar es Salaam Maritime Gateway (DMGP) na Standard Gauge Railway (SGR) na matakwa yake ya kufikia faida katika uwekezaji huo, kuimarisha utendaji wa bandari na kuchochea ukuaji wa uchumi kwa ajili ya ustawi wa watu wa Tanzania na ukanda huu;

(G) KWA KUTHAMINI mabadiliko ya huduma za usafiri wa baharini yaliyofanywa na Serikali ya Dubai kupitia DPW ambayo yalisababisha huduma za usafiri wa baharini kuwa mchangiaji mkubwa wa Pato la Taifa la Dubai (GDP)

(H) KWA KUTAMBUA kwamba DPW ni kampuni yenye uzoefu na yenye sifa na uwezo wa kimataifa katika ukuzaji wa bandari, usimamizi, uendeshaji na mtoaji wa suluhisho la ugavi;

(I) KWA KUZINGATIA mikataba mbalimbali ya miradi inayokusudiwa na Nchi Wanachama kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali itakayokubaliwa kupitia Mikataba ya Serikali Mwenyeji (HGAs), mikataba mahususi ya maafikiano au
mikataba mingine ya miradi kati ya Tanzania na kampuni husika za mradi;

(J) KWA KUZINGATIA kuwa Nchi Wanachama zinataka kuingia katika Mkataba huu ili kuweka mfumo shuruti wa manunuzi na utekelezaji wa Miradi mbalimbali inayokusudiwa katika Mkataba huu.

KWA HIYO SASA, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai zinapenda kuingia katika Mkataba huu ili kuwezesha malengo ya pande zote za Nchi Wanachama kama ilivyoainishwa hapa chini

SEHEMU YA I
UFAFANUZI, TAFSIRI NA UPEO

KIFUNGU I
UFAFANUZI NA TAFSIRI

  1. Ufafanuzi wa Maneno na Tafsiri

(a) Ufafanuzi wa maneno​
Maneno yenye herufi kubwa yaliyotumika katika Mkataba huu (pamoja na Dibaji na Viambatisho), na ambayo hayajafafanuliwa vinginevyo, yatakuwa na maana ifuatayo:​
“Mshirika” itamaanisha, kuhusiana na chombo chochote ama chombo kingine chochote ambacho, moja kwa moja au isivyo moja kwa moja kupitia mpatanishi mmoja au zaidi, kinaongozwa ama kiko chini ya udhibiti wa pamoja na chombo hicho.​
“Utawala wa Kifedha Uliokubaliwa” utajumuisha utaratibu wa kodi na tozo nyinginezo (ikiwa ni pamoja na utaratibu wa kutoza, kusimamia na kupinga kodi na tozo hizo) zinazotumika kwa Miradi, kwa mujibu wa sheria za Tanzania;​
“DPW” au “DP World” inamaanisha DP World MEA Ports FZE, kampuni inayomilikiwa na serikali ambayo inamilikiwa kikamilifu na PCFC ambayo inamilikiwa kikamilifu na Emirate ya Dubai, iliyoanzishwa katika Eneo Huru la Jebel Ali katika Umoja wa Falme za Kiarabu, yenye ofisi iliyosajiliwa kwa anuani ya P.O. Box 17000, Emirate ya Dubai, Falme za Kiarabu, ambayo itaanzisha Kampuni moja au zaidi za Miradi nchini Tanzania kwa madhumuni ya​
kutekeleza Shughuli za Mradi;​
“Dubai” itakuwa na maana ikama ilivyoelezwa kwenye utangulizi katika utambulisho wa Nchi Wanachama.​
“Shughuli ya mwanzo ya Mradi” itamaanisha Shughuli yoyote ya Mradi iliyofanywa kabla ya uamuzi wa mwisho wa uwekezaji kuhusiana na Mradi, na haswa kazi muhimu ya kiufundi kwa muundo wa mbele wa uhandisi, unaohusiana na hatua ya awali ya muundo, ujenzi na ukuzaji wa mfumo (ikiwa ni pamoja na, jiotekiniki ya nchi kavu na nje ya nchi, jiofizikia, topographical, bathymetric, offshore current, cadastral na uchunguzi mwingine wa kimazingira na kijamii na/au upimaji na ujenzi wa barabara hizo za kuingilia kutoka barabara kuu hadi maeneo ya Mradi kama itakavyohitajika kwa Shughuli zingine za mwanzo za Mradi; “Shughuli ya Mwanzo ya Mradi” itamaanisha yoyote kati ya hizo.​
“Taasisi” maana yake ni kampuni yoyote, shirika, kampuni yenye dhima yenye mipaka, ubia, biashara, ubia wa pamoja, ubia usiojumuisha, chama, amana au taasisi nyingine ya kisheria, shirika au biashara iliyopangwa kwa mujibu wa mkataba au chini ya sheria za nchi yoyote au kitengo chochote.​
“Serikali” maana yake ni Serikali ya Dubai, inayowakilishwa na Shirika la Bandari, Forodha na Eneo Huru la Dubai (PCFC), Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na “Serikali” itamaanisha yoyote kati ya hizo.​
“Usalama wa Serikali” utakuwa na maana iliyoainishwa kwake chini ya Kifungu cha 12 (1) cha Mkataba huu.​
“HGAs” au Mikataba ya Serikali Mwenyeji (Host Government Agreements) itamaanisha makubaliano yatakayoingiwa kati ya Tanzania na Kampuni ya Mradi kuhusiana na Shughuli za Mradi zinazozingatiwa katika Mkataba huu (au, ikiwa aya ya (b) ya Ibara ya 1 (2) (Ahadi ya kuingia katika HGA)) inatumika, kati ya Tanzania na DPW na baadaye kuhamisha haki na wajibu wao kwa Kampuni ya Mradi itakapoundwa); na “HGA” au Mkataba wa Serikali Mwenyeji itamaanisha mojawapo.​
“Viwango vya Haki za Binadamu” vitamaanisha (i) sheria na kanuni za kitaifa kuhusu haki za binadamu na (ii) haki za binadamu zanazo tambulika kimataifa na viwango vinavyotumika nchini Tanzania vikihusishwa na Shughuli za Mradi.​
“Kamati ya Ushauri ya IGA” itakuwa na maana iliyoainishwa kwayo katika Kifungu cha 3(2) cha Mkataba huu.​
“IGA” au Mkataba itamaanisha Mkataba huu, ikijumuisha Viambatisho vyake vyote.​
“Mwekezaji” itamaanisha (i) Kampuni ya Mradi (na tawi lolote au kampuni tanzu ya Kampuni ya Mradi iliyosajiliwa kufanya Mradi kwa niaba ya Kampuni ya Mradi); (iii) mtu yeyote anayeshikilia moja kwa moja aina yoyote ya usawa au maslahi mengine ya umiliki katika Kampuni ya Mradi.​
“Haki za Ardhi” itamanisha haki zote (bila kujumuisha haki za umiliki wa ardhi nchini Tanzania) juu ya ardhi inayohusiana na uchunguzi, upimaji na tathmini, uchambuzi, ukaguzi, ujenzi, matumizi, umiliki, ugawaji wa udhibiti na starehe (ikiwa ni pamoja na kukodisha, haki za njia, urahisi na haki za kumiliki ardhi) kama inavyohitajika kutekeleza Shughuli za Mradi.​
“Mtu” itamaanisha mtu yeyote wa asili au chombo;​
“Mradi” itamaanisha shughuli yoyote au mradi wowote unaofanywa na Mwekezaji au Kampuni ya Mradi au Washirika wao au wakandarasi ili kufikia malengo yoyote ya Mkataba huu.​
“Shughuli ya Mradi” itamaanisha shughuli yoyote inayofanywa na Mwekezaji au Kampuni ya Mradi au Washirika wao au wakandarasi kuhusiana na Mradi;​
“Mkataba wa Mradi” utamaanisha makubaliano yoyote, mkataba, makubaliano au hati nyingine, isipokuwa Mkataba huu, ambao Tanzania, Mamlaka yoyote ya Nchi, au Mwekezaji au Kampuni ya Mradi au Washirika wao wanashiriki au baadaye kuwa sehemu inayohusiana na Shughuli za Mradi (ikiwa ni pamoja na Haki za Ardhi), kwa kuwa mkataba wowote kama huo, mkataba au hati nyingine yanaweza kurefushwa, kuanzishwa upya, kubadilishwa, kurekebishwa au vinginevyo kurekebishwa mara kwa mara;​
“Idhini ya Mradi” itamaanisha kibali chochote, idhini, leseni, usajili, au uwasilishaji unaohitajika wakati wowote na mshiriki yeyote wa mradi kuhusiana na Miradi;​
“Kampuni ya Mradi” itamaanisha DPW au kampuni iliyosajiliwa Tanzania (ikiwa ni Mshirika wa DPW) ambayo imeingia katika Mkataba wa Mradi ili kufanya Shughuli za Mradi;​
“Mamlaka ya Nchi” itamaanisha kila Serikali na kila mamlaka ya kiserikali au mamlaka nyingine katika kila ngazi inayohusiana na eneo la Nchi Mwanachama;​
“Nchi Mwanachama” itakuwa na maana inayohusishwa nayo katika utambulisho wa wanachama katika utangulizi;​
“Tanzania” itakuwa na maana inayohusishwa nayo katika kutambulisha Nchi Wanachama kwenye utangulizi;​
“Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania” kwa kifupi chake “TPA” maana yake ni mamlaka iliyoanzishwa chini ya kifungu cha 4 cha Sheria ya Bandari SURA ya 166 na kwa madhumuni ya Mkataba huu maana yake ni taasisi inayomilikiwa na serikali yenye jukumu la kuingia mikataba na Kampuni ya Mradi kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za Mradi;​
“Eneo” kuhusiana na Mkataba huu itamaanisha eneo la nchi kavu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ikijumuisha eneo lake la bahari, anga, na maeneo ya baharini ambayo Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatekeleza mamlaka yake na haki zake za kujitawala kwa mujibu wa Sheria ya Kimataifa ya Umma;​
(b) Tafsiri:​
(i) Mgawanyo wa Mkataba huu katika vifungu na sehemu nyingine na uwekaji wa vichwa vya habari ni kwa ajili ya kurahisisha marejeleo pekee na hautaathiri mpangilio au tafsiri yake.​
(ii) Isipokuwa ikiwa imeonyeshwa vinginevyo, marejeleo yote ya “Kifungu” au “Kiambatisho” kinachofuatwa na nambari au herufi hurejelea Kifungu, Nyongeza au Kiambatisho kilichobainishwa cha Mkataba huu.​
(iii) Isipokuwa imeonyeshwa vinginevyo, rejeleo la “Utangulizi” inarejelea utangulizi wa mkataba huu.​
(iv) Isipokuwa kama imeonyeshwa vinginevyo au muktadha unahitaji vinginevyo, maneno “Mkataba huu”, “hapajuu,” “hapandani” na “hapa chini” na maneno kama hayo yanarejelea Mkataba huu, ikijumuisha Nyongeza na Viambatisho, na sio Kifungu chochote au kingine.​
(v) Marejeleo yoyote katika Mkataba huu kwa Nchi Mwanachama kutekeleza wajibu katika HGA husika au kukubali kwamba kifungu chochote mahususi kitajumuishwa katika HGA hiyo haimaanishi kuweka mipaka ya maudhui ya HGA husika kwa ahadi au masharti hayo na HGA hiyo inaweza kujumuisha ahadi na masharti mengine kama yatakavyokubaliwa na wahusika.​
(vi) Isipokuwa imeonyeshwa vinginevyo, marejeleo yote ya “Mkataba huu” au “Mkataba” au “hati” yanarejelea Mkataba huu au Mkataba au hati husika, kama ilivyorekebishwa, kuboreshwa au kuongezwa mara kwa mara.​
(vii) Isipokuwa imeonyeshwa vinginevyo, marejeleo kwa Mtu yeyote yatajumuisha wahamishwaji wake wanaofuata, warithi wake na waliokabidhiwa.​
(c) Mipangilio​
(i) Isipokuwa imeonyeshwa vinginevyo, maneno yanayoingiza umoja yatajumuisha wingi na kinyume chake na maneno yanayoingiza jinsia yoyote yatajumuisha jinsia zote.​
(ii) Isipokuwa kama imeonyeshwa vinginevyo, “udhibiti” utamaanisha kumiliki, moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja, mamlaka ya kuongoza au kusababisha mwelekeo wa usimamizi na sera za Mtu, iwe kupitia mamlaka ya kisheria au ya udhibiti juu ya Mtu huyo (katika kesi ya taasisi ya Serikali), umiliki wa wengi au maslahi mengine ya udhibiti katika usalama wa kupiga kura, usawa au maslahi mengine ya umiliki katika Shirika, kwa mujibu wa sheria au kwa makubaliano kati ya Watu wanaotoa mamlaka au haki hizo za kupiga kura.​
2. Ahadi ya kuingia kwenye HGA​
(a) Tanzania inaahidi kuhitimisha HGA na Kampuni ya Mradi husika (au itakavyokuwa, Mwekezaji husika) kuhusiana na kila Mradi husika unaotekeleza kanuni zilizoainishwa katika, na masharti husika ya, Mkataba huu na yenye masharti mengine kama vile Nchi Mwanachama na Kampuni ya Mradi husika au Mwekezaji anaweza kuamua.​
(b) Iwapo Kampuni ya Mradi haijajumuishwa wakati wa kutia saini HGA husika, HGA inaweza kusainiwa na Tanzania na DPW au Mshirika (pamoja na mtia saini huyo akiwa na haki ya kukabidhi HGA kama hiyo kwa Kampuni husika ya Mradi mara itakapoanzishwa).​
(c) Tanzania inakubali kwamba kila HGA husika na kila Mikataba ya Mradi husika ambayo yenyewe au Mamlaka ya Nchi inashiriki yatakuwa mfumo wa kimkataba wa Tanzania na haki za kimkataba za Mamlaka ya Nchi, makubaliano na ahadi chiniya au zinazohusiana na Mradi husika.​


SEHEMU YA II
WAJIBU WA JUMLA

KIFUNGU CHA 2
LENGO LA MKATABA

  1. Madhumuni ya Mkataba huu ni kuweka mfumo wakisheria wa maeneo ya ushirikiano kwa ajili ya maendeleo, uboreshaji, usimamizi na uendeshaji wa bandari za bahari na maziwa, kanda maalum za kiuchumi, hifadhi za usafirishaji, korido za kibiashara na miundombinu mingine ya kimkakati ya bandari nchini Tanzania. Maeneo ya ushirikiano pia yanajumuisha kujenga uwezo, uhamisho wa ujuzi, utaalam na teknolojia, kuimarisha taasisi za mafunzo na msaada wa utafutaji wa masoko.​


KIFUNGU CHA 3
USHIRIKIANO

  1. Utekelezaji wa Mradi​

(a) Nchi Wanachama zitashirikiana ili kuweka na kudumisha hali zinazofaa na mazingira bora kwa ajili ya utekelezaji wa Shughuli za Mradi.​
(b) Wawakilishi wa kila Nchi Mwanachama watakutana kwa nia njema wakati wote unaofaa na mara nyingi inavyohitajika na moja ya nchi mwanachama kwa madhumuni ya kujadiliana na kuingia mikataba mingine kadri itakavyofaa kati ya Nchi Wanachama, ili kuidhinisha, kuwezesha na kusaidia utekelezaji wa Shughuli za Mradi.​

2. Kamati ya Ushauri ya IGA​
(a) Nchi Wanachama zitaanzisha Kamati ya Ushauri ya IGA ambayo itakuwa na jukumu la kuratibu shughuli za Wanachama zinazohusiana na utekelezaji wa Mkataba huu na Kamati ya Ushauri ya IGA itaripoti kwa Katibu Mkuu anayehusika na Usafiri wa Majini wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania.​
(b) Kamati ya Ushauri ya IGA itajumuisha mwakilishi aliyehitimu ipasavyo wa kila Nchi Mwanachama na kutumika kama chombo ambacho Nchi Wanachama zinaweza kubadilishana habari na kushauriana kuhusiana na utekelezaji wa Mkataba huu au jambo lingine lolote ambalo linaweza kutumwa kwayo kwa mujibu wa hadidu za rejea zilizokubaliwa kati ya Nchi Wanachama.​
(c) Majukumu, mikutano ya mara kwa mara, mfumo wa kuripoti na mambo mengine yanayohusiana na utendakazi wa Kamati ya Ushauri ya IGA yataelezwa katika hadidu za rejea zitakazokubaliwa kati ya Nchi Wanachama.​
3. Ukaguzi na Taarifa​
(a) Nchi Wanachama zitakubaliana kupitia HGA na Mikataba ya Miradi kuhusu masuala ya ukaguzi yanayo husiana na uendeshaji wa Shughuli za Mradi.​
(b) Nchi Wanachama zitahakikisha ubadilishanaji sahihi wa taarifa kati yao zinazo husiana na Miradi. Taarifa zozote za siri zitakazotolewa kutoka nchi moja kwenda nchi nyingine hazitafichuliwa zaidi na nchi inayopokea taarifa bila kibali cha nchi iliyotoa taarifa hiyo​
KIFUNGU CHA 4
UPEO WA USHIRIKIANO NA VYOMBO VYA UTEKELEZAJI


1. Upeo wa Mkataba huu ni kuwezesha utekelezaji wa maeneo ya ushirikiano yaliyoainishwa katika Kiambatisho cha 1 cha Mkataba huu.​
2. Tanzania itaarifu serikali ya Dubai juu ya fursa nyingine zozote zinazohusiana na bandari, maeneo huru na sekta ya usafirishaji nchini Tanzania ili kuruhusu nchi au taasisi za Dubai kuonyesha nia na kuwasilisha mapendekezo ya kuzingatiwa kuhusiana na fursa hizo nyingine.​
3. Serikali ya Tanzania inathibitisha kuwa TPA itawajibika juu ya utekelezaji wa maeneo ya ushirikiano kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na mkabidhiwa yeyote au mrithi wa TPA atalazimika kuzingatia kanuni na masharti yaliyoainishwa katika Mkataba huu.​
4. Serikali ya Dubai inaiteua DPW na Washirika wake kama chombo cha kutekeleza Shughuli za Miradi.​
5. DPW na taasisi tanzu zitawajibika kutafuta ufadhili kwa Makampuni ya Miradi husika kwa ajili ya kuendeleza Shughuli za Miradi.​
KIFUNGU CHA 5
HAKI ZA KUENDELEZA, KUSIMAMIA AU KUENDESHA


1. Nchi Wanachama zinakubali kwamba DPW itakuwa na haki ya kipekee ya kuendeleza, kusimamia na/au kuendesha Miradi kama ilivyoainishwa katika Kiambatisho cha 1 Awamu ya 1, moja kwa moja au kupitia Washirika wake chini ya Mkataba huu kama itakavyoainishwa zaidi katika Mikataba ya Mradi husika na HGAs husika.​
2. Nchi Wanachama zinakubali kwamba utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya Miradi na DPW inategemea kuhitimishwa kwa Mikataba ya uhakika ya Mradi, Haki za Ardhi na HGAs kwa kila Mradi husika.​
3. Baada ya kusainiwa kwa Mkataba huu, DPW itatayarisha na kuwasilisha mapendekezo ya utekelezaji wa miradi chini ya maeneo ya ushirikiano yenye taarifa na nyaraka kama itakavyokubaliwa kati ya TPA na DPW.​
4. Nchi Wanachama zinakubali kwamba Miradi ya Awamu ya 1 (kama ilivyofafanuliwa katika Kiambatisho 1) itakuwa ndiyo miradi ya kipaumbele katika kuiendeleza na kuitekeleza. Serikali ya Tanzania itahakikisha kwamba TPA haitaongeza mapendekezo mengine yoyote ya Miradi yoyote ya Awamu ya 1 kuanzia Tarehe ya Kusainiwa hadi tarehe ambayo majadiliano kati ya DPW na TPA kwa Miradi ya Awamu ya 1 yamesitishwa au baada ya kumalizika muda wa miezi 12 kutoka Tarehe ya kusainiwa kwa Mkataba huu, yoyote iliyo ya mapema​
KIFUNGU CHA 6
MIKATABA YA SERIKALI NA VIBALI VYA SERIKALI


1. Serikali ya Tanzania itahakikisha kwamba Kampuni ya Mradi husika inapewa vibali vyote muhimu vya kiserikali, ridhaa, haki za ardhi, vivutio vya uwekezaji na misamaha inayohitajika kwa ajili ya utekelezaji wa Mikataba ya Mradi na mikataba yoyote ya ziada kwa mujibu wa sheria husika.​
2. Kwa kupitia DPW au Kampuni ya Mradi husika, Serikali ya Tanzania itasaidia kuzuia na/au kukomesha uingiliaji wowote usio halali au usioidhinishwa katika ununuzi au utekelezaji wa Miradi husika kwa mapendekezo ya DPW yaliyoidhinishwa na mamlaka yoyote au mtu wa tatu isipokuwa tu uingiliaji huo uwe ni muhimu kwa sababu za kiulinzi na kiusalama zinazoeleweka na kukubalika na Nchi Wanachama.​
KIFUNGU CHA 7
VIBALI VYA MRADI


1. Serikali ya Tanzania, kwa wakati ufaao, itatoa, itaruhusu, itadumisha au kuhuisha (au itasababisha kutolewa, kuruhusiwa, kudumishwa, au kuhuishwa) vibali vyote vinavyohitajika na kila Kampuni ya Mradi na/au TPA kwa ajili ya utekelezaji wa mapendekezo yaliyoidhinishwa.​
2. Serikali ya Tanzania inatambua na kukubaliana kwamba kutoa, kuruhusu, kutunza au kuhuisha vibali hivyo kwa wakati, ni muhimu kwa mafanikio na kwa utekelezwaji wa mapendekezo yaliyoidhinishwa na itahakikisha kwamba mamlaka au wakala wa nchi husika itawezesha na kuharakisha utekelezaji wa mapendekezo hayo, baada ya kupokea maombi au mapendekezo kutoka kwa DPW, TPA au kampuni ya mradi husika kwa ajili ya kutoa, kuruhusu, kudumisha au kuhuishwa kwa vibali hivyo.​
3. Iwapo vibali vikisha tolewa kwa mradi wowote havitoweza, kubatilishwa, kubadilishwa, kurekebishwa, au kushindwa kuhuishwa au kuongezwa na Serikali ya Tanzania au mamlaka husika ya serikali au wakala bila ya mashauriano ya awali na PCFC inayowakilisha Serikali ya Dubai ikiwa ubatilishaji kama huo, mabadiliko, urekebishaji au kushindwa kuhuisha au kuongezwa kunaweza kuwa na athari mbaya kwa Miradi (au yoyote kati ya hizo).​
KIFUNGU CHA 8
HAKI ZA ARDHI


1. Serikali ya Tanzania itachukua hatua zote zinazohitajika ili kuhakikisha upatikanaji na utoaji wa haki za ardhi kwa DPW au kampuni ya mradi husika ili:-​
(a) kupata, kumiliki na kutumia ardhi inayohusiana na kila Mradi (“Haki za Ardhi”);​
(b) Kutunza na kumiliki Haki hizo za Ardhi; na​
(c) kulinda haki hizo za ardhi kwa mujibu wa sheria na taratibu husika za utoaji na utumizi wa haki za ardhi kwa DPW.​
2. Serikali ya Tanzania itachukua hatua zote zinazohitajika kwa mujibu wa sheria ili kuhakikisha kuwa Haki za Ardhi zinaendelea kupatikana wakati wote na kwamba ubora wa Miradi hautoathiriwa na miundombinu yoyote ya baadaye ambayo inaweza kuvuka au kuendelezwa karibu na Miradi hiyo. Dhamana na gharama za uvukaji na uendelezaji wa baadaye zitakuwa chni ya mwendelezaji mwingine na si DPW au kampuni ya mradi husika.​
3. Serikali ya Tanzania itahakikisha kwamba Haki za Ardhi kwa Shughuli za Miradi ni:​
(a) zinatambuliwa kwa uwazi, kwa kuzingatia ukodishaji uliosajiliwa bila vikwazo vyovyote kama, dhamana, usalama au haki nyingine ya wahusika wengine, na kutoka kwa dai lolote, ushindani, au kutekelezwa na mtu mwingine yeyote;​
(b) zinatolewa kwa kampuni ya mradi kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa;​
(c) zinapatikana kwa kipindi kilichoainishwa katika hati ya kukodi; na​
(d) zinatolewa bila kizuizi kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi.​
KIFUNGU CHA 9
MOTISHA ZA UWEKEZAJI


1. Nchi Wanachama zinakubaliana kwamba uwekezaji wa DPW nchini Tanzania utakuwa wa kiwango na upeo mkubwa ambao utaleta manufaa mapana ya kijamii na kiuchumi yanayothibitisha utoaji wa motisha za uwekezaji zinazohusiana na Shughuli mahususi za Mradi.​
2. Nchi Wanachama zinakubaliana kwamba motisha za uwekezaji zitatolewa kwa mujibu wa sheria husika pamoja na taratibu zilizowekwa nchini Tanzania na kama itakavyoelezwa katika HGA husika na Mikataba ya Mradi.​
KIFUNGU CHA 10
USIRI


1. Nchi Wanachama hazitatoa kwa wahusika wengine kwa madhumuni yoyote taarifa yoyote inayohusiana na Mkataba huu au mapendekezo yake ambayo ni ya siri au ya binafsi (ikiwa ni pamoja na, bila kizuizi, taarifa yoyote inayohusiana na mapendekezo ya kiufundi na yakifedha) ambayo inakubaliwa kuwa taarifa hiyo ni ya siri na nyeti kibiashara kwa nchi zote mbili, isipokuwa kama itaarifiwa vinginevyo na/au kuidhinishwa kwa maandishi na DPW na TPA.​
2. Mmoja wa Nchi Mwanachama hatatumia taarifa yoyote inayotokana na Nchi Mwanachama mwingine au uchunguzi wowote unaostahili au taarifa nyingine iliyotolewa chini ya Mkataba huu (ikiwa imekubaliwa kuwa taarifa hizo ni za siri kabisa na ni nyeti kibiashara kwa Pande zote mbili) au kutumia taarifa hiyo kuomba ofa yoyote kutoka kwa wahusika wengine au kufanya zabuni yoyote ya ushindani inayohusiana na Shughuli za Miradi.​
KIFUNGU CHA 11
VITENDO VISIVYO VYA KIBAGUZI


1. Nchi Wanachama zinakubaliana kwamba mamlaka zinazohusika nchini Tanzania zitafanya:​
(a) kutoza kodi, ushuru, na tozo nyinginezo kwa kampuni ya mradi ya mradi husika, Shughuli za Mradi au watu (ikiwa ni pamoja na wasambazaji au watoa huduma) kwa mujibu wa Kanuni ya Fedha Iliyokubaliwa; na​
(b) kutumia sheria na kanuni hizo kwa nia njema na kwa ufanisi, uwazi na uratibu wa njia ambayo ni ya haki na isiyo ya kibaguzi.​

KIFUNGU CHA 12
ULINZI NA USALAMA

1. Nchi Wanachama zinakubaliana kwamba ulinzi na usalama hautaathiriwa kwenye Shughuli za Mradi ikijumuisha Ardhi ya Mradi, mifumo, watu, bidhaa na vifaa vililivyo kwenye, chini, juu, au katika Ardhi ya Mradi na Majengo au usakinishaji katika eneo la Mradi au katika Shughuli za Mradi ndani ya Eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na masuala mengine yote ya ulinzi na usalama ambayo Tanzania inawajibika, (“Usalama wa Serikali”).

2. HGA itahusika katika:

(a) kuweka mfumo wa wazi wa mgawanyo wa majukumu na utendaji wa Usalama wa Serikali;​
(b) kufafanua hatua zinazohusiana na vipengele hivyo vya ulinzi na usalama wa Mradi ambao Kampuni ya Mradi inawajibika kwayo (“Usalama wa Kampuni ya Mradi”);​
(c) kujumuisha masharti yanayohitajika na nchi mwanachama na Kampuni ya Mradi kushauriana, kushirikiana na kuratibu juu ya maendeleo na utekelezaji wa hatua zote za ulinzi na usalama zinazohusiana na Mradi, ikiwa ni pamoja na Usalama wa Serikali na Usalama wa Kampuni ya Mradi;​
(d) kutambua miingiliano kati ya hatua zinazohusiana na Usalama wa Serikali na Usalama wa Kampuni ya Mradi kulingana na Viwango vya Haki za Kibinadamu; na​
(e) kuweka hatua zinazohusiana na Usalama wa Serikali kwa kuzingatia Viwango vya Haki za Kibinadamu.​
KIFUNGU CHA 13
MAUDHUI YA NDANI, AJIRA NA WAJIBU WA KIJAMII WA KAMPUNI

1. Mkataba wa Mradi husika utajumuisha masharti yanayohusiana na yafuatayo:​
(a) kutambua na kutengeneza Mipango ya Maudhui ya Ndani ya Miradi husika;​
(b) ahadi za Kampuni ya Mradi zinazohusiana na utekelezaji wa programu za uwajibikaji kwa jamii; na​
(c) ahadi za Kampuni ya Mradi zinazohusiana na kubakiza kazi zilizopo, ajira za raia wa Tanzania na programu za mafunzo na maendeleo kwa wafanyakazi hao wa Kitanzania wa Kampuni ya Mradi husika.​
2. Kuhusiana na Shughuli za Mradi zinazofanywa na Kampuni ya Mradi, Mpango wa Maudhui wa Ndani utajumuisha, pamoja na mambo mengine, kutoa:​
(a) kipaumbele kwa mashirika ya ndani na watu juu ya ununuzi wa bidhaa, kazi, ushauri na huduma zisizo za ushauri ambapo mashirika na watu kama hao wanapatikana, na wanakidhi viwango vinavyohitajika;​
(b) mikataba iliyotengwa kwa ajili ya bidhaa na huduma fulani zitakazotolewa kwa makampuni ya ndani, taasisi zilizosajiliwa na raia wa Tanzania;​
(c) ubora unaohitajika, afya, usalama, mazingira, utaalamu na viwango vingine vya bidhaa na huduma zitakazo nunuliwa ndani ya nchi;​
(d) mpango wa ajira na mafunzo kwa raia wa Tanzania;​
(e) utekelezaji wa Mpango wa kuajiri na kutoa mafunzo kwa raia wa Tanzania;​
(f) Msaada kwa taasisi za ndani za mafunzo katika uwanja wa huduma za usafiri wa majini na vifaa; na​
(g) Mpango wa utafiti na maendeleo, na uhamisho wa teknolojia.​
Hii itazingatia kilawakati kwamba bidhaa, huduma na rasilimali zingine kulingana na mapendekezo na hifadhi iliyotajwa hapo juu ni yenye ubora na wingi unaokubalika na Kampuni ya Mradi (iwapo busara itatumika) na zinapatikana kwa viwango vya ushindani wa soko.​
3. Utekelezaji wa Mpango wa Maudhui ya Ndani na ahadi nyingine zilizoainishwa hapo juu zinazohusiana na uwajibikaji wa shirika kwa jamii, mafunzo na maendeleo na uhifadhi wa ajira na kujenga uwezo kwa raia wa Tanzania utategemea mkataba kati ya Kampuni ya Mradi na TPA katika Mikataba ya Mradi husika.​
KIFUNGU CHA 14
UTAIFISHAJI WA MALI


1. Tanzania inathibitisha kwamba Shughuli za Mradi ni za kibinafsi, uwekezaji au mali za washirika wa mradi katika Mradi huu, ikiwa ni pamoja na Mifumo ya Miradi au mali nyingine yoyote inayoonekana au isiyoonekana ya Kampuni ya Mradi au hisa katika, au mikopo kwa Kampuni ya Mradi inayohusiana na Mradi, au mali inayoonekana au isiyoonekana ya Mshirika wa Mradi au hisa katika, au mikopo kwa Mshirika wa Miradi yeyote anaye husiana na Miradi huu ( kuhusu “Unyang'anyi”) kwamba haina nia yakunyang'anya, kutaifisha, kuchukua au kujimilikisha mali yoyote kwa lazima ama hatua nyingine zenye athari sawa za moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja, nzima au kwa sehemu.​
2. Tanzania inakubali kwamba, endapo Serikali ya Tanzania itaamua kufanya utaifishaji, utaifishaji huo utakidhi masharti yafuatayo: (i) hatua za utaifishaji huo zitachukuliwa kwa maslahi ya umma na kwa mujibu wa taratibu za kisheria; (ii) hatua hizo si za kibaguzi; na (iii) hatua za ulipaji wa fidia zitachukuliwa papo hapo, madhubuti na ya kutosha kwa watu walioathirika, kwa mujibu wa kanuni ambazo zitawekwa katika HGA husika na Mikataba ya Miradi husika.​
KIFUNGU CHA 15
VIWANGO VYA MAZINGIRA, AFYA MAHALI PA KAZI, MAMBO YA KIJAMII NA
USALAMA


1. Nchi Wanachama zinakubaliana kwamba utekelezaji wa Shughuli za Mradi utazingatia sheria zilizopo Tanzania zinazosimamia Viwango vya Mazingira, Afya mahali pa kazi, mambo ya Kijamii na Usalama (EOHSS), ilimradi tu Kampuni husika ya Mradi haijazuiliwa kutekeleza matakwa yoyote ya kuzingatia viwango vingine vyovyote vya kimazingira na kijamii vilivyowekwa na wakopeshaji wa kimataifa au wafadhili wa Miradi.​
2. Kampuni inayotekeleza Mradi itazingatia Viwango vya Kimataifa vya kuzuia uchafuzi wa baharini ikijumuisha Mikataba ya IMO kama vile MARPOL, Kanuni ya Usalama wa Meli na Bandari (ISPS) na viwango vingine vya kimataifa vya shughuli za bandari.​
KIFUNGU CHA 16
VIWANGO VYA KIUFUNDI


DPW na TPA zitashirikiana na kubadilishana taarifa za utekelezaji wa Shughuli za Mradi kuhusu viwango vya kiufundi vya kubuni, kuendeleza, ujenzi, uendeshaji, matengenezo, ukarabati, ubadilishwaji, ukuzaji wa uwezo au upanuzi na matengenezo ya miundombinu au miundo mikuu na uendeshaji wa Shughuli za Mradi kwa mujibu wa taratibu za uendeshaji wa kimataifa kama zitakavyoainishwa katika Mikataba ya Mradi husika. DPW na TPA zitashauriana pamoja na Kampuni ya Mradi mara nyingi inapohitajika katika mchakato wa kufafanua na kukubaliana juu ya viwango hivyo vya kiufundi.​
KIFUNGU CHA 17
HAKI ZA WAFANYAKAZI


Nchi Wanachama zinakubaliana kwamba wakati wa utekelezaji wa Shughuli za Mradi hatua zote za Kampuni ya Mradi au watu wanaohusisha matumizi ya nguvu zinafanywa kwa njia inayolingana na Mazingira, Afya ya Kazini, Kiwango cha Kijamii na Usalama na Viwango vya Haki za Kibinadamu.​
SEHEMU YA III
UTAWALA WA FEDHA

KIFUNGU CHA 18
KODI, USHURU NA TOZO NYINGINEZO


1. Nchi Wanachama zinakubaliana kwamba kodi, ushuru na tozo zingine zitatozwa kwa mujibu wa sheria zilizopo za kodi za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na masharti mengine na motisha kama itakavyokubaliwa katika HGA husika na Mikataba ya Miradi kwa kuzingatia sheria za Tanzania.​
2. Motisha wa uwekezaji na misamaha ya kodi, ushuru na tozo zingine (inapohitajika) vitatolewa kwa kuzingatia sheria za kodi za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na masharti yatakayokubaliwa katika HGA husika na Mikataba ya Miradi kwa kufuata sheria za Tanzania.​
SEHEMU YA IV
MASHARTI YA MWISHO
KIFUNGU CHA 19
MABADILIKO YA UONGOZI WA NCHI


Iwapo uongozi wa Nchi Mwanachama utabadilishwa au kurithiwa na uongozi wa awamu nyingine kutokana na majukumu ya mahusiano ya kimataifa ya nchi yote au sehemu ya Eneo lake, uongozi utakaorithi utachukuliwa kuwa mhusika wa Mkataba huu kuanzia tarehe ya mabadiliko au urithi, ikiwa uongozi huo, ndani ya muda ufaao kuanzia tarehe hiyo, utaarifu Nchi Mshirika kuhusu nia yake ya kuwa sehemu ya Mkataba huu.​
KIFUNGU CHA 20
UTATUZI WA MIGOGORO


1. Usuluhishi wa kirafiki
Migogoro inayotokana na, au inayohusiana na, Mkataba huu itatumwa na Mwanachama kwa utatuzi wa kirafiki kupitia njia za kidiplomasia au, ikiwa Mwanachama atachagua, kwa Kamati ya Ushauri ya IGA, kwa makubaliano yoyote yaliyoandikwa kwa maandishi. Ikiwa mzozo hautasuluhishwa kwa njia ya kirafiki ndani ya siku tisini (90) kuanzia tarehe ya kuwasilishwa kwa mgogoro huo kupitia njia za kidiplomasia au Kamati ya Ushauri ya IGA, Mshirika yeyote anaweza kuarifu Upande mwingine kwamba kuna mgogoro uliotangazwa (“Mgogoro Uliotangazwa”).​
2. Usuluhishi wa kimahakama
(a) Ikiwa Mgogoro Uliotangazwa upo, Wanachama wanakubaliana kwamba Upande wowote unaweza, baada ya notisi iliyoandikwa kwa Mshirika mwingine, kuwasilisha suala hilo kwenye usuluhishi chini ya Kanuni za Usuluhishi za UNCITRAL.​
(b) Kila Upande utateua mjumbe mmoja (1) wa mahakama ndani ya siku thelathini (30) baada ya kupokea notisi ya maandishi kama ilivyoelezwa katika Kifungu cha 20(2)(a) hapo juu. Wajumbe hao wawili (2) watachagua raia wa nchi nyingine ambapo, baada ya kupitishwa na Nchi Wanachama, atateuliwa kuwa Mwenyekiti wa mahakama hiyo. (c) Mwenyekiti atateuliwa ndani ya siku thelathini (30) kuanzia tarehe ya uteuzi wa mjumbe wa pili.​
(d) Iwapo ndani ya muda ulioainishwa katika Ibara ya 20(2)(b) hapo juu, uteuzi unaohitajika haujafanywa, upande wowote unaweza, bila ya kuwepo makubaliano mengine yoyote, kumwalika Katibu Mkuu wa Mahakama ya Kudumu ya Usuluhishi kufanya uteuzi wowote wa muhimu ndani ya siku thelathini (30) baada ya ombi kufanywa.​
(e) Kwa madhumuni ya Mchakato wa Usuluhishi:​
(i) kiti cha usuluhishi kitakuwa Johannesburg, Jamhuri ya Afrika Kusini;​
(ii) eneo la usuluhishi litakuwa Johannesburg, Jamhuri ya Afrika Kusini;​
(iii) lugha ya usuluhishi itakuwa Kiingereza; na​
(iv) hukumu itakuwa ya maandishi na itaeleza sababu za uamuzi wa mahakama.​
3. Migogoro chini ya Mikataba ya Mradi na HGAs pia itatatuliwa kupitia usuluhishi wa kimataifa katika ukumbi na kiti kisichoegemea upande wowote.​


KIFUNGU CHA 21
SHERIA INAYOONGOZA

Sheria itakayo ongoza Mkataba huu itakuwa Sheria ya Uingereza ambapo sheria ya uongozi wa kila HGA na Mikataba ya Mradi husika itakuwa ni kwa sheria za Tanzania.

KIFUNGU CHA 22
MAREKEBISHO YA MKATABA

Mkataba huu unaweza kurekebishwa wakati wowote, kwa maandishi, kwa makubaliano ya pande zote za Nchi Wanachama. Hakuna marekebisho ya Mkataba huu yatakayotumika bila makubaliano hayo kwa kutia saini na kuridhiwa na/au kupitishwa kwa hati zinazofaa na Nchi Wanachama.

KIFUNGU CHA 23
MUDA NA UTARATIBU WA KUSITISHA MKATABA

1. Kwa mujibu wa aya ya 2 ya ibara hii ya 23, Mkataba huu utaendelea kutumika hadi pale itakapotokea mojawapo ya yafuatayo: (i) kusitishwa kabisa kwa shughuli zote za mradi; au (ii) kumalizika muda kwa HGA zote na Mikataba yote ya Mradi (pamoja na ya nyongeza yoyote ya muda itakayo fanyika) na utatuzi wa migogoro, ikiwa ipo, kama inavyoelezwa hapochini.​
2. Iwapo HGA itasitishwa kabla ya muda wake kuisha, Mkataba huu utaendelea kutumika kwa muda huo, na kwa kiwango kinachohitajika na Nchi yoyote Mwanachama au Kampuni ya Mradi kudai haki zozote zinazotokana na, kulinda maslahi yoyote yanayohatarishwa na au kuleta shauri lolote linalotokana na kusitishwa kwa HGA. Kusitishwa au kuisha muda kwa HGA hakutaathiri haki zozote zilizopatikana, madeni au masuluhisho ya Mwanachama yeyote chini ya HGA hiyo au Mikataba ya Mradi inayohusiana au Mkataba huu.​
3. Kusitishwa kwa Mkataba huu kutategemea idhini ya awali ya Nchi Wanachama, idhini hiyo haipaswi kuzuiliwa bila sababu.​
4. Nchi Wanachama hazitakuwa na haki ya kushutumu, kujiondoa, kusimamisha au kusitisha Mkataba huu katika hali yoyote, hata ikitokea ukiukwaji wa mkataba (material breach), mabadiliko ya kimsingi ya hali, kuvunjika kwa uhusiano wa kidiplomasia au kibalozi, au sababu zingine zozote zinazotambuliwa chini ya sheria ya kimataifa. Bila kujali yaliyotajwa hapo juu, mgogoro wowote kati ya Nchi Wanachama kuhusiana na hali kama hizo utashughulikiwa kulingana na mahitaji ya Ibara ya 20 ya Mkataba huu.​

KIFUNGU CHA 24
KUTORIDHISHWA, LUGHA NA VIAMBATANISHO

1. Nchi Wanachama hazijaonyesha kutoridhishwa na kifungu chochote cha Mkataba huu.​
2. Viambatisho vyote au nyongeza kwa Mkataba huu, ambazo Nchi Wanachama zinaweza kutia saini mara kwa mara, zitakuwa sehemu muhimu ya mkataba huu.​
3. Mkataba huu umeingiwa katika lugha ya Kiingereza. Kwa kuzingatia matumizi ya Mkataba huu (ikiwa ni pamoja na, taarifa zote, madai, maombi, taarifa au nyaraka nyingine au mawasiliano chini ya Mkataba huu) Nchi Wanachama zitatumia lugha ya Kiingereza.​

KIFUNGU CHA 25
KUINGIA KWENYE UTEKELEZAJI

1. Mara tu baada ya kutiwa saini kwa Mkataba huu na bila kuathiri wajibu mwingine wowote wa Nchi Wanachama katika Mkataba huu, Nchi Wanachama zitachukua hatua zote za kiutawala na udhibiti ambazo ni muhimu ili kuhakikisha kuwa Shughuli za Mradi wa Mapema zinaweza kufanywa na kutekelezwa kisheria na au kwa niaba ya mmoja au zaidi ya wawekezaji au Kampuni ya Mradi kwa mujibu wa sheria za Tanzania.​
2. Serikali ya kila Nchi Mwanachama, ikiwa itahitajika chini ya sheria zao za ndani, ndani ya siku thelathini (30) baada ya kutiwa saini kwa Mkataba huu, itaanza mchakato wa kuridhia Mkataba huu na chombo chake cha kisheria kilichoidhinishwa ipasavyo au chombo cha mahakama ili kufanya hili kuwa ni wajibu wa lazima kwa kila Nchi Mwanachama chini ya Sheria ya Kimataifa.​
3. Nchi Wanachama zinakubali kwamba masharti ya Mkataba huu na HGAs yatatumika kwa Shughuli zote za Mradi, ikiwa ni pamoja na zile zilizofanywa kabla ya kusimikwa kwa Mkataba huu au HGA husika, inapobidi.​
4. Mkataba huu utaanza kutumika baada ya kubadilishana hati za uidhinishaji chini ya sheria za kila Nchi Mwanachama, isipokuwa kwa mujibu wa ibara ndogo ya 1 na 2 hapa juu, ambayo itaanza kutumika baada ya kutia saini Mkataba huu na kila Nchi Mwanachama.​

KIFUNGU CHA 26
KUINGIZA IGA KWENYE SHERIA YA NCHI

Bila kuathiri Ibara ya 25, Serikali ya kila Nchi Mwanachama itachukua hatua zote zinazohitajika kwa haraka ili kufanya Mkataba huu na HGA husika kutumika chini ya sheria yake ya ndani kama mfumo wa kisheria uliopo kuhusiana na Miradi inayopendekezwa, ikijumuisha, pale inapobidi, kuwasilisha rasimu ya sheria zote wezeshi zinazohitajika, na itatumia juhudi zake zote kupata, haraka iwezekanavyo, kupitishwa kwa sheria wezeshi. Serikali za kila Nchi Wanachama zitafahamishana kwa wakati kuhusu hatma ya sheria hiyo wezeshi.

KIFUNGU CHA 27
UHUSIANO KATI YA MKATABA HUU NA MAJUKUMU MENGINE YA KIMATAIFA NA YA NDANI KWA NCHI WANACHAMA

Kila Nchi Mwanachama inawakilisha na kuthibitisha kwamba, baada ya kusimikwa kwa Mkataba huu na sheria zote wezeshi, haitakuwa sehemu ya mikataba au ahadi yoyote ya ndani au ya kimataifa, au kulazimika kufuata au kutekeleza sheria yoyote ya ndani au ya kimataifa, kanuni, au makubaliano, ambayo yanakinzana na au kuingia au kutekeleza Mkataba huu au HGA husika na Mikataba yoyote ya Mradi huu ambayo Nchi hiyo Mwanachama inashirikishwa.

KIFUNGU CHA 28
UWEZO WA NCHI WANACHAMA NA WATIA SAINI WAO

Kila Nchi Mwanachama inawakilisha na kuthibitisha kwamba utekelezaji na utendaji wa Mkataba huu uko ndani ya mamlaka ya Serikali yake, na kwamba Mkataba huu umesainiwa rasmi na mamlaka ya juu ya umma, inayo tawala kwa mujibu wa mamlaka zilizowekwa kisheria na kufuata taratibu zilizowekwa katika sheria zao za kitaifa za kuingia kwenye Mikataba ya kimataifa ya aina hiyo kwa niaba ya Nchi Mwanachama.

KIFUNGU CHA 29
UTENDAJI NA UFUATILIAJI WA IGA NA MIKATABA MINGINE IYOHUSIANA NA MSAADA KWA SHUGHULI ZA MRADI.

1. Kila Nchi Mwanachama inajitolea kutimiza na kutekeleza kila moja ya majukumu yake chini ya Mkataba huu, HGA ambayo ni mshirika na Mikataba mengine yoyote ya Mradi ambayo inashiriki mara kwa mara. Kwa kiwango kamili cha utekelezaji wa mamlaka yake halali, kila Nchi Mwanachama itahakikisha kwamba Mamlaka zake za Serikali zinatenda kulingana na, kukidhi, majukumu ya Nchi Mwanachama chini ya Mkataba huu na HGA husika.​
2. Kwa kiwango kamili cha utekelezaji wa mamlaka yake halali, kila Nchi Mwanachama itaunga mkono kikamilifu utekelezaji wa Mradi na utekelezaji wa Shughuli za Mradi na itahakikisha kwamba Mamlaka zake za serikali zinachukua hatua zote zinazohitajika kwa utekelezaji huo.​

KIFUNGU CHA 30
UTULIVU

1. Nchi Wanachama zinakubali kwamba mazingira ya kisheria na ya kimkataba yanayohusiana na Miradi yatadhibitiwa kwa namna ambayo ni sawa na ya kuridhisha kwa Nchi Wanachama na Kampuni ya Mradi. Maelezo ya uimarishaji huo yatakubaliwa kati ya DPW au Kampuni husika ya Mradi na TPA na pia kuonyeshwa katika HGA husika. Utulivu huo utatumia tarehe ya kutia saini IGA kama tarehe ya marejeleo ya uimarishaji, ili kushughulikia mabadiliko yoyote katika Sheria au mabadiliko ya kodi yanayoathiri Miradi husika.​
2. Tanzania itachukua hatua zote zinazohitajika au zinazofaa kufanya, kutoa au kutekeleza ndani ya Eneo lake sheria zote wezeshi na hatua nyingine za kisheria zinazohitajika ili kuwezesha na kutekeleza ahadi zilizoainishwa katika Mikataba ya Mradi na HGAs.​

KIFUNGU CHA 31
KUBADILISHANA HATI ZA MIKATABA

Mkataba huu na vyombo vyote vya uidhinishaji utabadilishanwa kati ya Nchi Wanachama.

Habari zaidi, soma:
  1. Sakata la DP WORLD: Rais Samia asema Serikali itatafuta mbia wa kuiendesha bandari ya Dar, sasa kuchangia robo tatu ya bajeti ya nchi
Mkataba DP.png


KIAMBATISHO 1: MAENEO YA USHIRIKIANO​

AWAMU​
MAELEZO​
Awamu ya 1
Miradi​
1.
2.
3.
4.
5.
6.
7.​
Maendeleo, usimamizi na uendeshaji wa Kituo cha RoRo (Berth O), General Cargo Terminal (Berth 1 hadi 4) na Container Terminal (Berth 5 hadi 7) ya Bandari ya Dar es Salaam.
Uendelezaji wa Dhow Wharf Terminal na Kituo cha Abiria cha Bandari ya Dar es Salaam kuendeshwa na TPA.​
Maendeleo, usimamizi na uendeshaji wa Eneo lililoteuliwa la Kwala Inland Container Depot na Kuras[ni bandari kabla ya lango.
Maendeleo, usimamizi na uendeshaji wa Kituo kipya cha Container katika RoRo & General Cargo Berths, ikiunganisha yadi ya RoRo kwa eneo lililoteuliwa na EPZA kwa kujenga Hifadhi ya Gari ya Multi Storey na Kuboresha yadi ya RoRo kwa General Cargo & Container Yard.
Kutoa Mifumo ya kisasa ya TEHAMA inayotakiwa na TPA ili kuwapa wadau wote wa Tanzania ufanisi na uonekanaji katika uendeshaji wa bandari mbalimbali Tanzania.
Kutoa huduma za kisasa za baharini za darasa la dunia kwa Bandari ya DSM kwa msingi wa kawaida wa mtumiaji.
Mafunzo na msaada wa maendeleo yatakayotolewa kwa TPA na DPW ili kuongeza uwezo wa watumishi wa TPA kuendesha mtandao wa bandari zilizo chini ya udhibiti wao.​
Awamu ya 2
Miradi​
1.​
2.​
Maendeleo ya majukwaa ya vifaa, maeneo maalum ya kiuchumi, mbuga za viwanda na miundombinu mingine ya vifaa ili kusaidia ukuaji na maendeleo ya biashara na njia za usafirishaji zinazohudumia nchi zilizofungwa katika Mashariki na Kusini
Afrika.​
Maendeleo, usimamizi na uendeshaji wa bandari za ziada za bahari na/au ziwa kupitia kuboresha na kuendeleza bandari nchini Tanzania pamoja na kuunganishwa na biashara kati ya Tanzania na Nchi zilizounganishwa na Ardhi kama inavyopendekezwa na TPA na kukubaliana na DPW.


KIAMBATISHO 2: CHOMBO CHA NGUVU KAMILI

DP Samia.png





BARUA YA UTEUZI

DP Dubai.png

 

Attachments

  • MKATABA WA KISERIKALI DP WORLD.pdf
    235 KB · Views: 20
Hakuna mkataba mbovu umewahi kutokea kama huu duniani

Samia akishirikiana na waziri na katibu mkuu wameiuza Tanganyika kwa waarabu

Watanganyika amkeni muitete nchi yenu wajukuu na vitukuu vyenu vitazaliwa km watumwa chini ya nchi ya waarabu ambao wameuziwa nchi

Mkumbuke viongozi waliofanya haya wananufaika na uuzwaji huu wa nchi
 
Mkataba nimeuweka kwa Kiswahili kwa msaada wa tafsiri ya Google, kama ulivyo.

Kama kuna makosa ni ya kimtandao, muyaainishe tutayafanyia marekebisho (editing) kidogo kidogo.


Naona Watanzania tunadanyana sana hapa JF. Sasa kila mmoja wetu avione na avisome vipengele vyote walivyokubaliana serikali mbili na tutowe maoni yetu. Tuyajadili kiheshima.

Binafsi nauunga mkono huu mkataba wa maendeleo.


Mama anaupiga mwingi Kimataifa.
 
Mimi nakubali serikali waingie mkataba na hii kampuni ya kitapeli sina tatizo, ombi langu tu waondolewe kinga za kutoshitakiwa kwa maamuzi ya hovyo hapo baadae.
Huu mkataba siyo wa kampuni, usome hata mwanzo wake tu, unaonesha kuwa ni mkataba wa nchi na nchi.

Wacha kusema uongo.


Mama anaupiga mwingi Kimataifa.
 
Hiki kipengere ni hatari kuliko hatari yenyewe, yaani hata isipo perform hakuna mtu kujitoa, ni kama ndoa ya kikristo hadi kifo kiwatenge.

“Nchi Wanachama hazitakuwa na haki ya kukemea, kujiondoa, kusimamisha au kusitisha Mkataba huu katika hali yoyote, ikiwa ni pamoja na katika tukio la uvunjaji wa nyenzo, mabadiliko ya msingi ya hali, kukatizwa kwa uhusiano wa kidiplomasia au wa kidiplomasia, au sababu nyingine yoyote inayotambuliwa chini ya sheria ya kimataifa”.
 
😊😊
Kwa nini Watu hawaamini Akili na maamuzi ya viongozi wao?
1. Uhuru umepitiliza
2. Ujuaji mwingi
3. Njaa (Kuna wakosoaji wengine wanatumika na maadui zetu kuhakikisha hatupigi hatua) rejea battle la Bwawa la mwl Nyerere na ujasiri wa mwendazake.
4. Kutafuta kutrend na kuonekana (wanasiasa wanaingia hapa)
 
Back
Top Bottom