Siku za Mkurugenzi Tanesco zahesabika
Siku za Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Nchini (Tanesco), Dk Idris Rashid kuendelea kushika wadhifa huo sasa zinahesabika baada ya baadhi ya Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika hilo kuanza mikakati ya chini chini kuhakikisha mkataba wake unaomalizika Septemba mwaka huu, hauongezwi.
Wajumbe hao waliliambia Nipashe kuwa kitendo cha Dk Rashid (pichani), kukaidi maagizo yao na kutangaza katika magazeti mpango wa kununua mitambo ya Dowans, ni kosa ambalo Bodi yao haiwezi kulivumilia.
``Tumedhamiria kwamba mara baada ya kumaliza muda wake wa miaka mitatu, kamwe sisi wajumbe wa Bodi hatutakubali kumpa kipindi kingine ili aiongeze tena Tanesco,`` alisema mmoja wa wajumbe wa bodi hiyo.
Alisema Dk Rashid alikaidi maagizo ya Bodi hiyo na kuamua kwenda kwenye Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma ya Bunge kinyume na maagizo waliyompa.
Uteuzi wa Dk Rashid kushika wadhifa huo wa Ukurugenzi wa shirika hilo ulitangazwa na Bodi hiyo mwishoni mwa mwaka 2006.
Dk Rashidi alichukua nafasi ya kuongoza shirika hilo kufuatia Serikali kuamua kuachana na Kampuni ya Net Group Solutions ya nchini Afrika Kusini ambayo nayo ilimaliza mkataba huku ikiliacha Tanesco likiwa taabani.
Kampuni hiyo ilihitimisha mkataba wake Desemba 31, mwaka 2006 baada ya kuliongoza Tanesco kwa takriban miaka minne mfululizo kuanzia Mei, mwaka 2002.
Mkataba wa kwanza wa miaka miwili kati ya kampuni hiyo na Serikali, ulisainiwa Mei, mwaka 2002 na kumalizika Agosti, mwaka 2004.
Hata hivyo, mkataba huo uliongezwa tena kuanzia Agosti mwaka 2004 na kumalizika Desemba 31, mwaka 2006 ambapo Serikali iliamua kutoendelea na kampuni hiyo hivyo shirika hilo nyeti kuwa chini ya uongozi wa wazalendo.
Wakati hayo yakijiri, Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, inatarajia kumhoji Mkurugenzi huyo wa Tanesco na Waziri wa Wizara ya Nishati na Madini, William Ngeleja kutokana na madai ya Mkurugenzi huyo kukosa nidhamu.
Akizungumza na Nipashe kwa njia ya simu jana Mwenyekiti wa Kamati hiyo, William Shelukindo alisema wanataka Dk Rashid ajieleze kwanini aendelee na wadhifa wake, ili hali ameonyesha dharau kwa vyombo vilivyomuweka madarakani yaani serikali na Bodi ya Shirika hilo.
Shelukindo alisema kauli ya vitisho kwa Watanzania iliyotolewa na Dk Rashid aliyekaririwa akisema Nchi itaingia gizani na Tanesco tusilaumiwe`` ni yakibabe na ukosefu wa nidhamu wa hali ya juu.
Alisema inaonekana wazi Mkurugenzi huyo ana kiburi ambacho haijulikani kinatoka wapi.
Akifafanua, Shelukindo alisema kama Mkurugenzi aliona hatari iliyo mbele, alipaswa kupeleka taarifa kwa Serikali au Bodi ya Wakurugenzi ya Tanesco.
``Lakini cha kushangaza inaonekana Dk. Rashid amekuwa ndiye Waziri na pia anajifanya yupo juu ya bodi, hali hii hatuikubali,``alisema.
Alipoulizwa wanapendekeza adhabu gani dhidi ya Mkurugenzi huyo, Shelukindo alisema hawezi kutamka kwa sasa kwa vile wanaamini kabla ya kuwekwa `kiti moto` tayari mamlaka zitakuwa zimechukua hatua.
Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, Estherina Kilasi ambaye pia ni Mbunge wa Mbarali (CCM), alisema pia hakubaliani na jinsi Dk Rashidi alivyotangaza mpango wa kujitoa katika sakata la kununua mitambo hiyo ya Dowans.
Alisema kauli yake ya vitisho kwamba nchi itaingia gizani na wao (Tanesco) wasilaumiwe, sio ya kiungwana na haikupaswa kutolewa na mtu anayeongoza Shirika linalowahudumia Watanzania.
Kilasi alisema kauli hiyo inaweza kutafsiriwa kuwa Mkurugenzi huyo alikuwa na usongo wa kununua mitambo hiyo kufa na kupona.
Alisema maneno ambayo yamemkariri Mwenyekiti wao (Zitto Kabwe) yalikuwa maoni yake binafsi na wala sio ya kamati kwa vile hakuna hata kikao kimoja ambako walikubaliana na ombi la kununua mitambo hiyo.
``Wala hatujawahi kutoa ushauri wowote juu ya suala hilo, zaidi ya kuwaelekeza Tanesco walifikishe kwa kamati husika ya Nishati na Madini,``alisema
Akifafanua, alisema kilichotokea siku hiyo ni semina ambayo Tanesco waliiandaa na kuwakaribisha wajumbe wa Kamati hiyo kwa lengo la kuwaelezea mipango ya kununua mitambo ya Dowans kwa kuwa wana kiasi cha Sh. bilioni 60 kwa ajili hiyo.
``Sisi tuliwahoji kama mnazo Sh Bilioni 60 mnashindwajwe kuongezea kidogo ili mnunue mitambo mipya? Vilevile tukawahoji hivi mambo haya mnayotuambia kwenye semina wameyapeleka kwa wahusika ambao ni Kamati ya Niashati inayoongozwa na William Shelukindo?,`` alisema Kilasi na kuongeza:
``Baada ya hapo tuliwashauri suala hilo walifikishe kwa wahusika (Kamati ya Madini) na hakuna hata mahali pamoja tulipolitolea uamuzi suala hilo kwa vile halituhusu.``
Mbunge huyo alisema kufuatia kauli za Zitto ambazo zimezua malumbano, na kuifanya Kamati yao ionekane ina `walakini` wanamsubiri kwa hamu arejee ili wamuweka kiti moto.
``Unajua baada ya semina ile mimi nilienda Zambia, huku nyuma ndo nikasikia malumbano, lakini baada ya kurejea nimewauliza wenzangu na hasa makatibu wanaoandika muhtasari, kama kuna kikao kingine kimeketi na kutoa uamuzi, lakini wakasema hapana. Sasa tunamsubiri Zito arejee safarini ili tumuulize kulikoni? ``Alisema.
Naye Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustine Mrema amemtaka Rais Jakaya Kikwete kuingilia kati malumbano yaliyozuka wiki tatu sasa kati ya Kamati mbili za Bunge, Spika Samuel Sitta na Tanesco kuhusu hoja ya kununua mitambo hiyo ya Dowans.
Akizungumza na waandishi wa habari makao makuu ya TLP, jijini Dar es Salaam jana, Mrema alisema anatoa rai hiyo kwa vile anaamini kuwa Rais Kikwete amesikia hoja za kila upande kupitia malumbano hayo kuhusu suala hilo.
``Nchi ina uongozi, haiwezekani mambo yakajiendea ovyo, ninachoweza kusema ni kwamba, Rais Jakaya Kikwete asaidie kuondoa utata, asiache watu wakatoana macho,`` alisema Mrema.
Alisema huko nyuma wakati akiwa serikalini, ilikuwa linapotokea jambo, haraka wanalishughulikia kwa vile hawakuona kuwa ni busara kuacha kushughulika na mambo mengine ya kujenga taifa na kusalia kwenye kushughulikia jambo moja pekee kila uchao.
``Haiwezekani kila tukiamka asubuhi ni Tanesco, huyu anakuja na taarifa kwamba, nchi itakumbwa na giza na mwingine anakuja na hili katika jambo moja, halafu Rais wala Waziri Mkuu hawasemi lolote,`` alisema Mrema.
Wengine waliojitosa kwenye malumbano hayo ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Shelukindo, ambaye ni Mbunge wa Kyela (CCM), Dk. Harrison Mwakyembe na Mbunge wa Karatu (Chadema), Dk. Willibrod Slaa.
Chimbuko la Dowans ni mkataba wa mradi wa ufuaji umeme wa dharura wa megawati 100 kati ya serikali, Tanesco na kampuni ya Richmond uliofikiwa mwaka 2006.
Hatua hiyo ilikuja baada ya Richmond kushindwa kutekeleza mradi huo iliuza mitambo hiyo kwa Dowans.
Mkataba huo ulizua mvutano mkubwa kiasi cha kusababisha Bunge kuunda kamati teule kuchunguza, ikiongozwa na Dk Mwakyembe, na ripoti yake kusababisha Edward Lowassa kujiuzulu wadhifa wa Waziri Mkuu.
Vilevile Nazir Karamagi alijiuzulu Uwaziri wa Nishati na Madini) na Dk Ibrahim Msabaha wa Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki kutokana na kashfa hiyo.
SOURCE: Nipashe