Zitto, mimi ninakusikia vizuri sana na ninashare sentiments zako. Lakini tukumbuke:
HALI HALISI
a. Tatizo la Nishati siyo geni.
Wewe kama mimi na Watanzania wengine wengi tunajua kuwa tanzania ina tatizo la nishati ya umeme. Tunajua pia kuwa tatizo la nishati ya umeme ya Tanzania siyo kutokana na kukosekana kwa 'vyanzo' vya umeme. Tunavyo vyanzo vya kutosha kabisa. Tunajua kabisa kuwa umeme wa kutumia maji unategemea majira na hali ya hewa. Hili tunalifahamu. Tunafahamu pia kuwa uchumi wetu unakua na matumizi ya umeme yameongezeka. Haya yote tunayafahamu.
Serikali ya CCM inafahamu juu ya hali hii kwa miaka 45!
b. Kwamba licha ya kujua ukweli wa hali halisi ya umeme nchini tumeishia kufanya vitu hivi: (1) kujenga vibwawa hapa na pale (natumia neno vibaya kumaanisha vimiradi vidogovidogo vya umeme wa maji) na (2) kukodisha au kuingiza hawa IPPs ili tuweze kuongeza umeme nchini. Haya ndiyo masuluhisho pekee ambayo tunayo na tunayoyatekeleza.
c. Umeme wa Jua na wa Upepo
Licha ya (b) tunatumia umeme wa upepo na umeme wa jua sehemu mbalimbali (nilikosooma sekondari tulikuwa tunatumia umeme wa jua). Kwa nchi iliyoko kwenye eneo la Ikweta jua siyo tatizo. Kuna maeneo yana upepo sana wa kutosha kuweka majenereta ya umeme wa upepo. Kati ya hivyo viwili (jua na upepo) Upepo ndiyo wenye gharama ya chini kidogo, ni rahisi kukusanya uwezo wake. Hadi hivi sasa hatujathubutu kufanya mradi mkubwa wa umeme wa upepo ukizingatia kuwa (a) hapo juu ni kweli.
d. Vyanzo vinazalisha chini ya kiwango chao.
Pia inafahamika kuwa vyanzo mbalimbali hasa vya maji vinazalisha chini ya uwezo wake. Mara nyingi tunaambiwa vinazalisha chini ya uwezo wake kwa sababu ya maji kupungua lakini hata maji yakiwa yamejaa bado vinazalisha chini ya uwezo wake. Sababu tuliambiwa na Karamagi kuwa ni kwa sababu mitambo mingi imechakaa na kuikarabati yote kuirudisha katika kiwango chake cha juu kutaligharimu taifa dola bilioni 1.3
Katika hotuba yake ya bajeti ya 2007/2008 alisema hivi: Hata hivyo, tatizo la kukatika umeme mara kwa mara kwenye gridi ya Taifa limeendelea kutokana na
uchakavu wa miundombinu ya usafirishaji na usambazaji wa umeme. Gharama za kukarabati mfumo mzima wa umeme kwa kipindi cha miaka mitano ijayo zinakadiriwa kuwa Dola za Marekani bilioni
1.3."
Hiyo namba ni muhimu nitaonesha hapa chini. Kwa maneno mengine ni kuwa kuanzia 2007 hadi 2012 tukiamua kukarabati mitambo yote hiyo tutatumia kiasi hicho cha fedha. Lakini tukikamilisha tutakuwa tumerudisha uwezo wa mabwawa yote kuzalisha to their maximum capacity ambayo ni 560MW na yale ya mafuta n.k vyote vitafikia karibu MW900 hivi.
Sasa hayo yote hapo juu ni mambo ambayo yanafahamika; yanafahamika na Tanesco, yanafahamika serikalini, yanafahamika na wataalamu n.k Hakuna geni hata moja. Hayo niliyoyasema Mheshimiwa ni mambo ambayo tunayajua, hayana hisia, ni halisia.
Matatizo ya sasa:
Mheshimiwa matatizo ya sasa pia siyo mageni. Kuanzia mwaka 2006 tumeandika kuhusu suala la nishati na ninyi wawakilishi wetu mmelijadiri hili Bungeni kwa kina wakati mwingine kwa jazba na pia kwa utamu wote wa kushawishi akili. Miaka mitatu sasa tunajua kuwa tuna mapungufu ya nishati ya umeme.
a. Richmond
Tatizo la mgogoro wa Richmond lilikuwa ni hilo hilo. Kwamba licha ya nchi kuingizwa kwenye mkataba huu kwa sababu ya "dharura" majenereta hayakufanya kazi na hawakuingia kwa muda kwa karibu mwaka mzima. Na walipoingia (chini ya Dowans) na kuanza kuzalisha tatizo la nishati ya umeme iliyolazimisha mkataba huo halikuwepo tena.
Hii ina maana dharura iliyokuwapo 2006 na kusababisha blackouts na usumbufu mkubwa haikulipigisha magoti taifa! Hatukuona mamilioni ya watu wetu wakifa mahospitalini, au wanafunzi kushindwa kabisa kusoma; na hatukuona mamia ya viwanda yakifungwa kwa kushindwa kuzalisha. Tulihimili na tukasalimika. Gharama yake kwenye uchumi ikiwa bado ni kubwa mno.
b.Richmond/Dowans
WAliporithisha mkataba wao kinyemela kwa Dowans kampuni ambayo ni ya kitapeli (and I can say with authority ni kampuni ya kitapeli kama ilivyo Richmond) wabunge wetu mling'aka na kukataa. Mlipinga kwa nguvu zote na matokeo yake Waziri Mkuu akajiuzulu na baraza la mawaziri kuvunjika. Tukaamini kuwa Serikali imejifunza, na Tanesco imejifunza kitu.
Sasa mazingira ya kupewa richmond mkataba ndiyo yale yale ambayo yanakuja tena leo.
-. Richmond iliiingia kwa sababu kuna dharura; Dowans imeingia kwa sababu kuna dharura
-. Richmond haikujulikana wamiliki wake; Dowans haijulikani wamiliki wake
-. Richmond ilipigiwa debe na viongozi serikalini; Dowans inapigiwa debe na viongozi serikalini
-. Richmond ilitangazwa ndiyo mkombozi; Dowans inatangazwa kuwa ni mkombozi
- Richmond ikaingia mkataba mbovu kabisa; Dowans ilirithi mkataba mbovu vile vile na kuingia mkataba mbovu na Tanesco
Tofauti iliyopo katika sakata hili na lile la Richmond ni kile ambacho umekirudia hapa na Kasheshe naye amekirudia nacho ni kuwa wakati kwenye Richmond Tanesco walionekana kupinga, katika hili la Dowans Tanesco wako tayari kulikumbatia. Hii ndiyo tofauti pekee. Kwamba kwa vile Tanesco sasa hivi wanakubali na kutaka kununua basi tukubali nia yao nzuri bila kuihojia au kuangalia motivations nyuma yake.
1. Tanesco kutafuta suluhishi la tatizo la nishati.
Tutakuwa hatuwatendei haki Tanesco na serikali kama hatutatambua uzito wa hali iliyopo mbele yetu. Tutakuwa hatukiri ukweli uliopo. Hata hivyo binafsi naamini kinacholetwa mbele yetu ni suluhisho la kukwepa kushughulikia tatizo halisi la umeme nchini. NI suluhisho la kufunika kidonda kwa kitambaa bila kuweka dawa ya kuzuia vijidudu zaidi. Ni suluhisho jepesi la tatizo gumu.
Sikubaliani na wazo la wabunge kwenda kutafuta majenereta ya umeme kwani kwa kufanya hivyo wanavuka mpaka wa watunga sheria na wasimamizi wa serikali na kuwa watendaji. Hili nalo ni "no no".
2. Kuzungumza na Watengenezaji
Makampuni mbalimbali ya majenereta ikiwemo GE yana in stock majenereta ambayo yako tayari kupelekwa sehemu yoyote duniani. GE hali yake kiuchumi siyo nzuri sana kwa siku za hivi karibuni na kutokana na kumomonyoka kwa uchumi duniani. Endapo serikali yetu ikizungumza na GE moja kwa moja kutokana na dharura n.k nina uhakika GE watafurahi sana kuhakikisha tunapata majenereta mapya kabisa wakijua kuwa within hours watakuwa na dola karibu milioni 30! Basically we will give them some kind of a bailout while they are bailing out our energy sector!
WAbunge wetu tunaomba muishawishi serikali na watendaji kuzungumza moja kwa moja na watengenezaji na kuona nini kinaweza kufanyika sasa hivi kuondoa tatizo linalokuja. Kama Watanzania waliweza kusubiri kwa mwaka mzima suala la Dowans nina uhakika watawala wakiwaambia wananchi wasubiri miezi mitatu au sita kwa majenereta mapya kabisa kwa bei nzuri na kutoka kwa watengenezaji wenyewe wananchi wataelewa. Tatizo hakuna aliyejaribu njia hiyo wamebakia leo kulitisha taifa na kama kutuchukua mateka wanatuambia viwanda vyetu vitafungwa, na mahospitali kusitisha huduma. That is unacceptable!
Hivyo tatizo la nishati ya sasa hivi linaweza kabisa kutatuliwa bila kusababisha athari kama ile ya Richmond. Nakuomba usimamie pendekezo hilo kwani hili la Dowans ni No no. Ihamasisheni serikali na Wizara au tanesco kuzungumza na GE au makampuni mengine.
3. Wanachoogopa kuprocure moja kwa moja toka Marekani ni nini?
Kwa mara kadhaa sasa tumeona watawala wanakwepa kuzungumza na Wamarekani moja kwa moja na matokeo yake wanazunguka kwa madalali. Walilifanya hili pia kwenye suala la Rada na hata ndege ya Rais. Matokeo yake ni kuzunguka sheria za Marekani.
Wamarekani wanasheria inayokataza makampuni ya Marekani kujihusisha vitendo vya kifisadi kwenye nchi za kigeni. Sheria hiyo ya Forein Corrupt Practices ni tishio kwa wanasiasa na watendaji wetu. Leo hii tunavyozungumza kuna jamaa wa Nigeria amefikishwa mahakamani kwa kuwa dalali wa kifisadi alipojaribu kujihusisha na ufisadi kwa niaba ya kampuni za Kimarekani. Sheria hiyo ni mwiba mkubwa na ni tishio. Ndiyo maana ni rahisi kwa watawala wetu kwenda UAE na Costa Rica kutuletea Dowans.
Hata ile Richmond wengine tulipendekeza karibu miaka miwili iliyopita kwa serikali yetu kuiomba serikali ya Marekani kuishughulikia Richmond Printing ya Houston under that ACT kwani ingefumua mengi. Of course hawakusikiliza.
Kama tunataka uwazi na ukweli twendeni tuzungumze na watengenezaji moja kwa moja.
Baadhi ya taarifa tayari zimepitishwa kwa watendaji kadhaa huko nyumbani juu ya hili na kuwahakikishia kuwa watu kama wa GE wako tayari kuzungumza nao.
4. Kiza kijacho kitatokana na uzembe na siyo sababu tumepinga Dowans.
Mheshimiwa Zitto kama kutatokea kiza nchini si kwa sababu hatukununua majenereta ya umeme toka Dowans. Itakuwa ni makosa makubwa kusema kuwa ati nchi kuwa giza ni kwa sababu hatukuwasikiliza Tanesco, Kamati yako au Waziri. Hapana.
Nchi ikiingia gizani ni kwa sababu viongozi wetu wameshindwa. Kwa sababu wamejaribu kutafuta suluhisho la kiraka.
5. Mradi wa Stiglers
Mwaka jana Rais Kikwete mwenyewe akizungumza kwenye hafla ya kuzawadia tuzo ya Rais kwa Wazalishaji wa mwaka inayoandaliwa na CTI alisema wazi kuwa mradi huo ndiyo utaondoa tatizo la upungufu wa nishati nchini. Mradi huo una uwezo wa kuzalisha hadi MW2100.
Nimesema hapo nyuma juu ya gharama ya kukarabati vyanzo vya sasa kuwa ni dola bilioni 1.3 za Kimarekani. Hayo ni kwa mujibu wa Karamagi. Mradi wa Stiglers jinsi unavyokadiriwa sasa utagharimu dola bilioni 2! Yaani, ni
lazima tuchague aidha kutumia dola bilioni 1.3 kupata MW1000 hivi au kutumia bilioni 2 kupata MW2100!
Kwenye taifa lenye viongozi wenye kuthubutu uchaguzi hapo wala si mgumu. Kwanini basi hakuna mkazo wa mradi mkubwa kama huu? Yawezekana kuna siasa na matatizo yake, lakini huu ni mradi pekee ambao tunaweza kuutekeleza hata kwa fedha zetu wenyewe! Kwanini hatujauchangamkia? Sijui kama Chadema mna sera ya kuendelea mradi huo mkipata madaraka, CCM wao wana sera ya nishati lakini hawajathubutu kuuweka mradi huu kwenye vipaumbele!
Kwanini?
Sababu ni kuwa kujengwa kwa Stiglers kutaondoa kabisa masuala ya vimiradi hivi vidogo vidogo vya ulaji! Vitaondoa kina Richmond na Dowans, na miradi mingine yenye sura ya kifisadi. It is not in the interest of a small group of people kuwa na Stiglers Dam! Kwanini wahangaikie mradi ambao utakuwa ni mwisho wa kula kwao?
Tatizo basi hapa ni kuwa hatuna viongozi wenye kuthubutu kufanya "maamuzi magumu" kama alivyosema Dr. Idris. Tuna viongozi (baadhi yao anyway) ambao kufanya mradi mkubwa itaonekana ni "hatuna fedha" lakini vimiradi hivi vya kuchezea akili fedha ipo! Tuna tayari dola milioni 260 (vitambulisho na hizi za Dowans), tuna milioni 40 za Dowans, tuna zile zilizoenda Deep Green, Mwananchi, Meremeta na Tangold..!! Hatuna viongozi wenye kuthubutu kukomalia hayo yote tupate fedha za kukomboa sekta yetu ya nishati!
Sasa, nakubaliana na wewe kuwa ipo haya ya kuziba pengo la nishati. Tatizo ni kuwa Dowans isiwe sehemu ya suluhisho hilo. Inasikitisha kuwa Tanesco katika kugonganisha vichwa vyao wameshindwa kupata suluhisho jingine isipokuwa Dowans! Kwamba Watanzania na wataalamu wote walioko Tanzania wote wameshindwa kufikiria njia nyingine mbadala isipokuwa Dowans.
Nakubaliana na kauli yako:
I want to state here in explicit terms that, I, Kabwe Zuberi Zitto (MP), Chairman Public Investments Committee of Parliament of Tanzania, stand with TANESCO on their desire to acquire gas fired turbines to improve electricity generation to the country.
Hii haina utata. Tatizo langu liko kwenye njia ya pekee na moja tu nayo ni Dowans! Sidhani kama kuna mtanzania mwenye akili timamu ambaye anapinga Tanesco kuongeza uwezo wa nishati. Hoja zao tumezisikia lakini wakati umefika wa hatua za makusudi kuchukuliwa.
a. Kuepusha tishio la kiza kwa sasa hivi, na suluhisho hilo liwe nje ya Dowans, watoto wake au shemeji zake.
b. Kuandaa mkakati na kuanza kuutekeleza ili ndani ya miaka kati ya 5-7 ijayo Tanzania isiwe kabisa na tatizo la nishati.
Nje ya hapo tutazungushana kwenye mambo haya kila mwaka hadi tuchoke.
Mwisho swali kwako:
Unachukuliaje kauli ya Dr. Rashid ambayo wananchi (mimi mmojawapo) tumeichukulia kuwa ni tishio kwa nchi, kwamba bila Dowans giza laja, viwanda kufungwa, mahospitali kukosa huduma na wanafunzi kutosoma?
NB: Don't mind my numbering system kwani hadi nimefika mwisho sijui where is "a"~!