Jamani someni hapa muone jinsi Spika alivyomgeuka Zitto. Hii iko kwenye gazeti la serikali, Habari Leo la kesho asubuhi.
============
SPIKA SAMWELI SITTA NA DOWANS
Spika wa Bunge, Samuel Sitta, ameitahadharisha Serikali juu ya athari zinazoweza kujitokeza iwapo itapuuza ushauri wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na kuamua kuendelea na mchakato wa kununua mitambo ya umeme ya kampuni ya Dowans.
Ameunga mkono ushauri uliotolewa na kamati hiyo unaoitaka Serikali isinunue mitambo hiyo ya Dowans, kwani kwa kufanya hivyo ni sawa na kufufua sakata la Richmond na badala yake itumie nguvu ilizonazo kuhakikisha inamaliza tatizo la umeme kwa kununua mitambo mipya.
Aidha, Spika amesema Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma, imekiuka kanuni za Bunge kwa kutoa maoni yake juu ya ununuzi wa mitambo ya Dowans hadharani, hali ambayo imejenga taswira kwamba Bunge lina ushauri unaokinzana kuhusu suala hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari leo ofisini kwake Dar es Salaam juu ya mwongozo wake na ushauri anaoutoa kwa Serikali juu ya suala hilo, Spika Sitta, aliitaka Serikali kutosahau kwamba Dowans ni kampuni iliyopatikana kwa kurithishwa mradi na kampuni ya Richmond katika mazingira yenye utata, ambayo hadi leo ni kitendawili.
"Uhalali wa utaratibu wa Richmond kumkabidhi mradi Dowans ulitiliwa shaka na kamati teule ya Bunge. Dowans na Richmond ni mtu na binamu yake na si vigumu kukubali kuwa bado wao ni wabia hadi sasa," alisema Sitta.
Alisema ikiwa ni kweli Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), lina dola za Marekani milioni 69 sawa na Sh bilioni 90, ingetazamiwa shirika hilo litumie fedha hizo kununulia mitambo mipya badala ya kununua mitambo ya Dowans iliyochakaa.
Sitta alisema pamoja na hayo, Tanesco wanatakiwa wakumbuke kuwa Dowans wamewashitaki kwenye Baraza la Kimataifa la Usuluhishi Paris, Ufaransa na kwamba gharama za mitambo na za kuikodi haziwezi kuepukwa kuwa ni sehemu ya shauri hilo Paris.
"Ni kwa mantiki ipi kesi baina yao iendelee na papo hapo mdaiwa (Tanesco) anunue mitambo kutoka kwa mdai (Dowans)? Ikumbukwe kuwa Tanesco walipoikodi mitambo ya Dowans, Tanzania ilikuwa inalipa Sh milioni 152 kwa siku sawa na dola za Marekani milioni 42 kwa mwaka," alisema.
Spika alisema mkasa wa Richmond haupaswi kufufuliwa upya kupitia Dowans, Serikali haina budi kuelekeza nguvu zake katika kutafuta njia mbadala za kulipatia Taifa umeme wa dharura, badala ya kung'ang'ania mitambo ya Dowans ambayo imejaa utata.
Alisema suala la uchakavu wa mitambo ya Dowans si la mzaha, kwani mitambo hiyo ni ya mwaka 2006. "Kwani mtu ukienda dukani kununua gari jipya na anayenunua gari chakavu wako sawa? Jamani tafsiri ya mitambo ya 2006 na ya sasa ikoje? Mambo mengine nawaachia mtayatafakari wenyewe," alisema.
Alisema pamoja na hayo Serikali ina haki ya kupuuza ushauri wa Bunge, ila iko siku wakati Bunge hilo likitathmini utendaji wa Serikali, ikibainika hitilafu itabidi sababu za kukaidi ushauri huo zifahamike.
Akizungumzia mvutano uliopo baina ya Kamati za Bunge za Nishati na Madini na Hesabu za Mashirika ya Umma, alisema Bunge ni chombo ambacho kazi yake kubwa ni kusimamia na kutoa ushauri kwa Serikali kwa kuzingatia kanuni za Bunge ambazo zimetungwa na chombo hicho.
Alisema kwa mujibu wa kanuni hizo, kamati za Bunge zenye madaraka ya kushughulikia taarifa za utendaji unaofanywa na wizara za serikali na vyombo vilivyo chini ya wizara hizo, ni kamati ya kudumu ya kisekta, pamoja na kwamba kamati nyingine za Hesabu hazizuiwi kutafakari mambo yanayogusa sekta husika, lakini si kwa kusema hadharani.
Alisema kwa mujibu wa kanuni hizo, kamati husika ya hesabu inapokuwa na maoni kuhusu suala la sekta linalosimamiwa na kamati nyingine, haina budi ipitishe ushauri na maoni yake kwenye kamati ya kisekta.
Alisema mvutano unaoendelea kwa sasa hauna sababu yoyote na wala hakuna haja ya yeye Spika kuzikutanisha kamati hizo mbili ili kurejea upya maoni na uamuzi juu ya suala hilo, kwa kuwa ushauri kwa Serikali kutonunua mitambo hiyo ulikwishatolewa kwa Wizara na Kamati ya Bunge tangu Desemba mwaka jana. "Huo ndio ushauri rasmi na sahihi wa Bunge ninaoutambua."
Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja alikaririwa na baadhi ya vyombo vya habari juzi, akishikilia msimamo wa serikali kununua mitambo hiyo ya Dowans kutokana na hali halisi ya nishati nchini na kwamba uamuzi huo ndio sahihi kwa wakati huu na hauhusiani na ufisadi wowote.
Alisema suala la kununua mitambo mipya litachukua zaidi ya miaka miwili wakati kwa sasa mahitaji ya umeme ni makubwa kuliko kiwango halisi kinachozalishwa na Tanesco, hali ambayo inahitaji kufanyika kwa juhudi za dharura kunusuru hali ya umeme nchini.
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, Zitto Kabwe, hakupatikana leo kuzungumzia suala la kamati yake kutoa ushauri wao juu ya suala hilo hadharani. Kwa muda mrefu baadhi ya wanasiasa na kamati hizo, wamekuwa wakilumbana kuhusu uamuzi wa Tanesco kutaka kununua hiyo mitambo wakidai kwamba Sheria ya Manunuzi inakataza kununua vitu vilivyotumika.