MVUTANO mkali uliibuka jana katika kikao cha Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma na maafisa wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kuhusiana ombi la kununua mitambo ya kuzalisha umeme inayomilikiwa na Kampuni ya Dowans.
Baadhi ya wabunge wa kamati hiyo iliyokuwa chini ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe waliwabana maafisa wa Tanesco waliokuwa wakiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Dk Idrisa Rashid ili waeleze sababu iliyowafanya waamue kununua mitambo chakavu ya Dowans badala ya mipya.
Wabunge hao walionyesha wasiwasi wao kufuatia nia ya Tanesco kutaka kununua mitambo hiyo huku wakijua kuwa sheria ya manunuzi inazuia ununuzi wa mitambo chakavu.
Mbunge wa Bukombe, Emmanuel Luhahula, alihoji iwapo Tanesco na serikali hawana wazo mbadala zaidi ya kununua mitambo ya Dowans.
Zitto alimtaka Mkurugenzi wa Tanesco aieleze kamati mitambo ile inayotaka kununuliwa na shirika hilo ina ubora wa kiasi gani.
Akijibu baadhi ya hoja za wabunge, Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Dk Idriss Rashid kwa kushirikiana na timu ya wataalam wake, alisema mtambo mmoja ni mpya na mingine imetumika kwa takribani saa 800 kila mmoja.
Alisema mitambo hiyo inao uwezo wa kufanya kazi kwa miaka 10 bila kufanyiwa ukarabati na kwamba ikifanyiwa ukarabati inaweza kufanya kazi kwa miaka mingine 10 na kufikisha miaka 20.
Dk Rashid aliongeza kuwa shirika lake lilipata mkaguzi kutoka Ujerumani ambaye aliikagua mitambo na kutoa taarifa kuwa mitambo hiyo ni mizima na inao uwezo wa kuzalisha umeme.
Alisema jambo kubwa linaloisukuma Tanesco kushinikiza ununuzi wa mitambo hiyo ni hali ya ukame inayotarajia kuikumba nchi katika kipindi cha miezi kadhaa ijayo.
Zitto alipomtaka Mkurugenzi huyo aeleze mbadala endapo bunge halitaridhia ununuzi wa mitambo hiyo, Dk Rashid alisema hakuna chaguo jingine ni ama kununua mitambo hiyo au nchi kuingia katika giza.
Nafikiri suala hili ni la kitaifa, tunapaswa kuliangalia kwa uzito wake, au tuendelee hivi tulivyo na kuwa na shortage (upungufu) ya umeme au kununua mitambo iwe ya Dowans au mingine yoyote, lakini tukumbuke kuwa tukiamua kukodi itabidi kuendelea kulipia capacity charges (gharama ya mitambo), alieleza Dk Rashid.
Alisema mitambo hiyo inauzwa kwa Sh60 bilioni, huku wakiamua kununua mitambo mipya, mbali na kulipia Sh90 bilioni, lakini mchakato huo utachukua muda mrefu hadi kukamilika hali aliyosema italiingiza taifa kwenye uhaba wa umeme.
Kwa upande wake, Mbunge wa Kigoma Mjini (CCM), Peter Serukamba alitetea ununuzi wa mitambo hiyo akisema kuibana Tanesco ni kuionea kwani hali iliyopo ni kuwa shirika hilo limefungwa kamba na serikali.
Tayari wametuambia, kuna shortage (uhaba) ya umeme, tunatakiwa kununua mitambo au tuingie kwenye shortage, sasa tunataka nini tena? Tatizo letu sisi tumeamua kuiacha siasa ndio itoe maamuzi, ukiisoma hii taarifa yao hutakuwa na swali lolote la kuwauliza, aliongeza Serukamba.
Alipokumbushwa azimio la bunge lililokataza kununua mitambo hiyo, mwanasheria wa shirika hilo, Subira Wandiba alisema hana kumbukumbu zozote azimio hilo isipokuwa anachojua yeye sheria hairuhusu kununua mitambo chakavu.
Hata hivyo, baada ya mvutano mkali kamati hiyo iliamua suala hilo lijadiliwe na Kamati ya Nishati na Madini ili waweke msimamo wa pamoja kuhusu mitambo ya Dowans, IPTL, Mradi wa Umeme wa Upepo Singida, Mradi wa Kinyerezi na ule wa Mtwara.