BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,769
- 288,283
- Thread starter
- #441
Idrisa Rashid Dowans imekupa nini?
Na Mbasha Asenga
Mwanahalisi~Maslahi ya Taifa Mbele
Na Mbasha Asenga
Mwanahalisi~Maslahi ya Taifa Mbele
TANZANIA yetu isiyoishiwa sakata, safari hii imethibitika kwamba lile sakata la Richmond ambalo lilirithiwa na Dowans katika mradi wa kuzalisha umeme wa dharura wa megawati 100, halijafa na kwa kweli limekataa kufa.
Ni jambo la kustaajabisha kusikia kwamba Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umeme nchini (Tanesco), Dk. Idriss Rashid, amewasilisha hoja mbele ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma, akitaka uamuzi wa serikali utazamwe upya.
Serikali kupitia Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, ilitangaza kwamba imejitoa katika mchakato wa tenda ya kununua mitambo ya Dowans.
Ama kweli Dowans imekataa kufa. Haifi na wanaotaka kuiuwa watakufa wao! Naam. Juhudi zimeanza na sasa zimeshika kasi kuhakikisha kwamba kwa vyovyote Dowans haiwezi kupata hasara katika mkataba uliovunjwa.
Wanataka mambo mawili, Tanesco wakubali yaishe wanunue mitambo yake, au wasubiri kulipa fidia baada ya kesi iliyofunguliwa dhidi ya serikali kuamuliwa.
Awali, Richmond ilipouza mkataba wake kwa Dowans tena katika mazingira tatanishi, Watanzania waliambiwa habari ya Richmond imefungwa, hakuna tena tija kuijadili kwa sababu tayari umeme ulikuwa unazalishwa.
Waliokuwa na akili zao kichwani wakatulia na kutafakari, inakuwaje bwana mkubwa wakati huo, Edward Lowassa, anasema maneno hayo? Mambo yakafunikwa kama ambavyo imekuwa kawaida ya nchi hii.
Lakini mwishowe jipu likaiva na Richmond ikatumbuka vibaya. Baraza la Mawaziri lote likaenda na maji. Katika hali ya kawaida, Dowans ingeogopwa, ingekimbiwa kwa kuwa ni nondo mbaya, lakini wapi, watu wameendelea kuikumbuatia.
Miezi kadhaa ilipita tangu Februari 2008 maazimio ya Bunge yalipopitishwa hadi mkataba wake ulipovunjwa rasmi Agosti. Tangu kuvunjwa kwa mkataba huo, juhudi imekuwa ni moja tu, Tanesco ibebe Dowans kama si moja kwa moja basi hata kwa mlango wa nyuma.
Mwaka jana joto la Tanesco la kutaka kununua mitambo ya Dowans likapanda hadi pale wabunge walipotoa angalizo kwa Waziri wa Ngeleja, kwamba kununua mitambo ya Dowans ni kuvunja azimio la Bunge na kukiuka sheria ya manunuzi ya umma (PPRA).
Miezi mitatu tu imepita tangu serikali kupitia kwa Waziri Ngeleja itamke kwamba imejitoa katika mchakato wa zabuni ya kununua mitambo ya Dowans, lakini katika ujasiri wa aina yake Dk. Rashid anaweka wazi kwamba bado wana matamanio hayo. Je, ujasiri huu ni wa nini, na unatokana na nini?
Tanesco shirika ambalo linahemea hewa ya ziada kutokana na kukabiliwa na matatizo makubwa ya kiundeshaji, ikiwa haina hata uwezo wa kutosheleza wakazi wake wa mjini kwa umeme achilia mbali vijijini, inapata ujasiri wa kutaka kuendesha ligi ya kugombea mitambo ya Dowans ambayo ina kila shaka kwamba ni biashara chafu!
Kwa nini Dk. Rashid ana ujasiri huu? Si siri tena kwamba kiongozi huyu aliyepata kuongoza taasisi nyeti za fedha nchini, kuanzia Mkurugenzi Mkuu wa iliyokuwa Benki ya Taifa Biashara na hatimaye Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), amethibitika kushiriki katika mchezo mchafu.
Makachero wa Uingereza wa kikosi cha Kuchunguza makosa makubwa ya jinai (SFO) wamemtaja Dk. Rashid sambamba na aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali wakati wa utawala wa Rais Benjamin Mkapa na pia Waziri katika serikali ya Awamu ya Nne, Andrew Chenge, kuwa wana harufu ya rushwa ya rada ya Tanzania.
Dk. Rashid anatuhumiwa kupokea kutoka kwa Chenge Dola za Marekani 600,000 zinazohisiwa kuwa mgawo wa watu walioshiriki kufanikisha ununuzi wa rada hiyo iliyogharimu serikali ya Tanzania fedha za walipa kodi Sh 40 bilioni.
Je, kweli kiongozi wa nama hii, yaani Dk Rashid pamoja na kujua wazi kwamba anachunguzwa kwa tuhuma hizo, na hata baada ya kuelezwa na kusoma magazetini kuhusu tuhuma hizi, amemaua kukaa kimya, lakini kibaya zaidi akiendelea kukalia ofisi umma.
Dk Rashid anadaiwa kuwa na uhusiano wa karibu na mmiliki wa Dowans, mbunge wa Igunga na mfanyabiashara, Rostam Aziz. Uhusiano wao unakwenda ndani katika uendeshaji wa shughuli za kibiashara kwenye kampuni moja nyeti nchini.
Kwa maana hiyo kuendelea kwa shinikizo la kutaka Dowans inunuliwe bila kuzingatia maslahi ya taifa, ni kielelezo kwamba mbinu chafu zimejichimbia ndani ya Tanesco.
Ujasiri huu pia wa Tanesco kupitia kwa Dk. Rashid wa kutaka kununua Dowans, ni sawa na jaribio la kutikisha Bunge.
Ndiyo kutikisa Bunge! Jaribu kutafakari. Bunge limetoe azimio kutaka Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Johnson Mwanyika, Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Edward Hosea na waliokuwa mawaziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi na Dk. Ibrahim Msabaha wachunguzwe.
Je, kama sio kile kinachoitwa, "ujasiri wa kifisadi" Dk Rashid anapata wapi ujasiri wa kuendelea na matamanio ya Dowans?
Huu ni ujasiri ambao hauwezi kuelezewa katika sura ya kiuwajibikaji ndani ya shirika la umma, ni jambo linalohitaji utafiti zaidi kubainisha nguvu hizi zimejiegemeza wapi?
Kwa upeo wangu ni nguvu za fedha, ni nguvu za kutaka kuvuna, liwe liwalo ni lazima Tanesco ikamuliwe hadi ibaki hoi bin taaban.
Inawezekana Dk. Rashid na Tanesco yake wana hoja, lakini katika dunia hii hivi mitambo ya kufua umeme kwa kutumia gesi ni ya Dowans tu? Kwa nini anaing'ang'ania Dowans kwa kiwango hiki?
Je, kuna asilimia ngapi za kamisheni kama za rada? Ipo shida moja ndani ya nchi hii. Ujasiri wa ajabu; kukosa soni; kufanya uhalifu wao kweupe kana kwamba wamepewa kibali cha kutokuwajibishwa kwa maovu yao.
Hali hii ndiyo inawafanya wote wanaotuhumiwa makosa makubwa ya kuikosea jamii, kujitafutia njia nyepesi na za kitoto kabisa kujisafisha; wengine kusajili magazeti ili kujisafisha na kuandama wengine eti kulipiza kisasi; wengine kutaka jamii iamini kwamba Tanzania haina mtu safi hata mmoja.
Nafikiri wakati sasa umefika kuamua kuzaliwa upya kwa taifa hili, na hakika halitazaliwa bila kwanza wahalifu wote, watuhumiwa wote waikosoe jamii katika mikataba kama ya rada, Richmond, IPTL na mingine mingi kufikishwa mahakamani na kufilisiwa ili kutoa ujumbe mmoja tu kwamba WIZI HAULIPI.
Hatua ya Dk. Rashid na serikali kung'ang'ana na Dowans ni dalili tosha ya kwamba kuna "Wizi mtupu."