Dowans wakamatwe
2008-07-02 09:49:36
Na Raymond Kaminyoge
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahimu Lipumba, ameitaka serikali na menejimenti ya TANESCO kuibana kampuni ya kufua umeme ya Dowans kurudisha fedha iliyokwishachukua kwa mkataba ambao si halali.
Kampuni ya Dowans `ilichukua mikoba` ya Kampuni ya Richmond Development Company LLC iliyoingia mkataba wa kuiuzia umeme Tanesco.
``Naipongeza serikali na menejimenti ya TANESCO kwa uamuzi wake wa kuvunja mkataba na kampuni ya Dowans, wamesikia kilio chetu,`` alisema Profesa Lipumba jana jijini Dar es Salaam alipozungumza na Nipashe.
Alisema kitu cha kufanya sasa iwe ni kudai fedha walizokuwa wakichukua kila mwezi kwa sababu mkataba huo haukuwa halali na wameshachukua mamilioni ya fedha.
``Wameshachukua fedha nyingi za walipakodi wa Tanzania kupitia mkataba wa kisanii. Huu ni muda mwafaka wa kuelekeza nguvu za kuhakikisha fedha hizo zinarejeshwa,`` alisema.
Aliongeza kuwa sambamba na hatua hiyo, waliohusika katika mkataba huo wanatakiwa kufikishwa kwenye vyombo vya sheria ili waweze kushughulikiwa kwa maovu waliyoyafanya.
Alisema walioingia mkataba huo ndiyo wamekuwa wakisababisha bei ya umeme kuendelea kupanda kila wakati na hivyo gharama za maisha kuendelea kupanda.
Aidha, Profesa Lipumba, alisema serikali kwa kutumia wanasheria wake waangalie namna wanavyoweza kuvunja mkataba mwingine wa kampuni ya IPTL na TANESCO.
``Mkataba huu pia unaonyesha ulikuwa na dalili za rushwa, hivyo ili kuwasaidia wananchi mkataba huu pia unatakiwa kuvunjwa na wahusika kufikishwa mahakamani,`` alisema.
Juzi TANESCO ilitangaza kuvunja mkataba na kampuni Dowans kuanzia Agosti mosi, mwaka huu baada ya kubaini kuwa haukuwa halali.
Wakati huo huo, Mary Edward wa PST anaripoti kutoka Dodoma kwamba baadhi ya wabunge wameipongeza serikali kwa hatua nzuri iliyochukua ya kuvunja mkataba na kampuni ya kuzalisha umeme ya Dowans.
Hata hivyo, wamesema hatua hiyo haitoshi bali inatakiwa pia kuwachukulia hatua wote waliohusika katika kuingizia hasara kubwa nchi kwa kupoteza mamilioni ya fedha.
Wakizungumza katika mahojiano maalumu na PST katika viwanja vya Bunge, baadhi ya Wabunge hao walisema, Watanzania wanasubiri kuona inakwenda mbali zaidi kwa kuhakikisha wale wote waliohusika katika utapeli huo wanafikishwa mahakamani, ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.
Mbunge wa Mkanyageni (CUF), Bw. Habibu Mohamed Mnyaa, alisema anaishukuru serikali kwa kuyafanyia kazi maoni ya Watanzania, lakini ni lazima ihakikishe uzembe wa namna hiyo haupewi nafasi tena.
Hata hivyo, alisema serikali ni lazima ijifunze sasa kwa hayo yaliyotokea ili isije ikafanya tena makosa katika mikataba mengine itakayokuja hapo baadaye.
Alisema serikali ilikuwa na uwezo wa kupata mitambo kama ile tena kwa bei nafuu na ikainunua na kuwa ya kwake, kuliko hasara kubwa iliyoingia.
Bw. William Shelukindo, Mbunge wa Bumbuli (CCM), ambaye pia alikuwa ni mmoja wa wajumbe wa kamati ya Mwakyembe, alisema kamati yao ilipendekeza kuvunjwa kwa mkataba huo kutokana na uchafu uliokuwepo.
``Tunashukuru serikali kuona kwamba imeyazingatia maoni ya kamati yetu japo wengine walianza kuzusha mambo kwamba tumewaonea, sisi tulifanya kazi tuliyotumwa, kama kuna watu wanasema tumewaonea basi waende mahakamani.``
Bw. Shelukindo, alisema hivi sasa hawazungumzii masuala ya Richmond kwa kuwa kazi hiyo imekwisha na kuahidi kuwa, wataendelea kuisaidia serikali pale inapoonekana kuna maovu.
Bw. John Cheyo, Mbunge wa Bariadi Mashariki (UDP), alisema: ``Hatua iliyochukua serikali sio ya kuvunja mkataba kwa kuwa hapakuwa na mkataba wowote pale, isipokuwa wameamua kutekelezamambo ambayo tulikuwa tunayazungumza tangu zamani.``
Alisema baada ya hatua hiyo sasa iangalie namna ya kuwachukulia hatua wale wote waliohusika na udanganyifu huo.
Alisema hakuna kilichovunjwa kwani hakukuwa na mkataba. Hasara imeshapatikana na haijulikani serikali itafanya nini juu ya hao waliosababisha hasara.
Naye Mbunge wa Karatu (CHADEMA), Dk. Wilbrod Slaa, alisema: ``Sawa, serikali imechukua hatua, lakini hiyo haitoshi. Tunataka kuona walioizamisha serikali katika hasara kubwa kama hii wanachukuliwa hatua kali za kisheria.``
Mbunge wa Jimbo la Nzega (CCM), Bw. Lucas Selelii, alisema serikali imechelewa kupata ukweli kuhusu Dowans Tanzania Limited kwani ilikuwepo tangu mwaka 2006.
Aidha Mbunge wa Bukoba Vijijini (CCM), Bw. Nazir Karamagi, ambaye alikuwa Waziri wa Nishati na Madini, akizungumzia hatua hiyo aliendelea kukana kuwa hahusiki hata kidogo katika sakata hilo.
``Mimi nilirithi Wizara ya Nishati toka kwa aliyekuwa waziri wa Wizara hiyo (akimaanisha Ibrahimu Msabaha, Mbunge wa Kibaha vijijini -CCM) na wala sikuhusika kwa namna moja au nyingine katika kusaidia mkataba huo, hivyo kama serikali imechukua hatua ni vyema, nami naipongeza.
``Mimi sikutetea mkataba huo isipokuwa nilikuwa najaribu kusema kwamba, wakati mkataba huo unafanyika nchi ilikuwa katika matatizo, hivyo katika hali ya kawaida, ilikuwa ni lazima watu wachanganyikiwe,`` alifafanua.
Akizungumzia hatua zitakazochukuliwa, Waziri wa Nishati na Madini, Bw. William Ngeleja, alisema: ``Hii ni hatua ya kwanza tuliyoichukua baada ya kujiridhisha, hatma ya wahusika ni hatua nyingine``
Aidha, alisema kilichofanyika kwa serikali sio kuvunja mkataba kwa kuwa hapakuwa na mkataba wowote walioingia kwa mujibu wa wanasheria na kwamba hapatakuwa na fidia yoyote ya kuwalipa Dowans kwa vile hakuna mkataba uliovunjwa.
``Msingi wa maamuzi haya ni kwamba, hakukuwa na kampuni yoyote ya Richmond Development Company LLC iliyokuwa imesajiliwa na kuingia mkataba na TANESCO... Haipo,`` alisema.
SOURCE: Nipashe