NYEMO CHILONGANI
UTAJIRI WENYE UCHUNGU
Sehemu ya Ishirini na Tisa.
"Tunaondoka, nadhani hautorudi tena huku," alisema Sam huku akimwangalia Aisha ambaye uso wake ulikuwa na tabasamu pana.
"Na sitotaka kurudi tena, hata kama nikifa, ni bora kuzikwa hukohuko," alisema msichana huyo huku tabasamu lake likiendelea kuwepo usoni mwake.
****
Hali ya mawingu haikuwa nzuri hata kidogo, anga ilichafuka, hakukuwa na amani hata kidogo. Marubani wawili waliokuwa wakiiendesha ndege hiyo walichanganyikiwa, hawakuamini kama kweli anga hiyo ilichafuka kiasi hicho.
Walifanya kazi ya urubani kwa zaidi ya miaka ishirini, hata anga ilipokuwa ikichafuka kwa kujaa mawingu huku mvua iliyoambatana na upepo mkali inaponyesha, hawakuwa wakiogopa lakini kwa siku hiyo, hali ilionekana kuwa tofauti kabisa.
Radi zilikuwa zikipiga kila kona, waliogopa, walihisi kwamba ndege hiyo ingepoteza muelekeo, walijitahidi kuiweka sawa kwani upepo mkali uliokuwa ukivuma ulikuwa ukiiyumbisha ndege ile kupita kawaida.
Tayari hali ya hatari ikaanza kuonekana, walichokifanya ni kuitoa ndege ile kutoka katika usawa wa nchi kavu na kuipeleka katika usawa wa bahari ya Atlantiki.
Hali ya hewa haikutulia, siku hiyo ilionekana kuwa na mkosi kwao, juhudi zao za kuiweka sawa ndege ile zilikuwa zikiendelea zaidi, mbaya zaidi, kitu kilichowatisha ni kuona injini moja ya ndege ile ikianza kuzima na kuwaka mara kwa mara.
"Vipi?" aliuliza rubani mmoja.
"Injini inazima na kuwaka, Mungu wangu! Tuombe Mungu, hali hii sijawahi kuiona tangu nazaliwa," alisema rubani mwingine.
"Hebu tuishushe ndege chini kidogo, inaweza kusaidia," alisema rubani huyo na hivyo kuanza kufanya hivyo.
Walichokuwa wakitaka ni kutoka katika wingu zito ambalo liliambatana na upepo mkali, wakaishusha ndege ile kwa chini kidogo, kama mita hamsini kutoka baharini, yote hiyo walifanya ili kuepukana na upepo huo mkali lakini cha ajabu, injini ile iliyokuwa ikiwaka na kuzima, ikazima kabisa.
"Mungu wangu! Injini imezima..." alisema rubani.
"Unasemaje?"
Huku nyuma, kila mtu alikuwa akishangaa, hali iliyokuwa ikionekana ilimtisha kila mmoja, Aisha alibaki akipiga kelele, hewa safi ya oksijeni ikaanza kupotea hivyo kuvuta mipira ya hewa safi na kujivisha midomoni na puani mwao.
"Tunakufa..." alisema Aisha huku akianza kulia.
"Hatuwezi kufa....hebu tuchukue maboya," alisema Shawn.
Hicho ndicho walichofanya, walijua kwamba kwa namna moja au nyingine marubani wale wasingeweza kuirudisha ndege ile katika hali ya kawaida kutokana na upepo mkali kuendelea kuvuma hivyo walichokifanya ni kuchukua maboya kwa kuamini kwamba kama ndege hiyo ingeanguka basi ingeangukia baharini.
"Vaa haraka Aisha...injini imezima," alisema Shawn huku akimsisitiza Aisha kuvaa boya lile. Hata kabla hawajakaa sawa, ndege ile ikaanza kushuka baharini kwa kasi, kila mtu akaogopa, tayari walikiona kifo kuwa mlangoni, baada ya sekunde kadhaa, kilichosikika kilikuwa ni puuuuu, ndege ikaangukia baharini na kuanza kuzama.
****
Mike alichanganyikiwa, hakuelewa ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, mara ya mwisho kuzungumza na Shawn alimwambia kwamba walikuwa ndani ya ndege wakiivuka Bahari ya Atlantiki ila kitu kilichomshangaza ni kwamba kwa kipindi hicho, simu ya mtu huyo haikuwa ikipatikana.
Hali hiyo ilimpa hofu moyoni mwake na kuhisi kwamba inawezekana kuna kitu kibaya kilichotokea, akili yake ikamwambia kwamba inawezekana kulikuwa na ajali ndiyo maana simu haikuwa ikipatikana.
Alichanganyikiwa mno, alichokifanya ni kuwasiliana na watu wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa JFK wa hapo New York ili kuona kama walikuwa na mawasiliano na marubani waliokuwa wakirusha ndege hiyo.
“Una hofu ya nini?” alisikika mwanaume mmoja akiuliza kwenye simu.
“Kuna ndege yangu ilikuwa ikitoka Dubai, nashangaa siwapati kwenye simu, kuna tatizo lolote?” aliuliza Mike huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Ndege aina gani?”
“Ndogo!”
“Aina?”
“Ultra-long-range G550.”
“Asante! Nitakupigia tafadhali.”
Simu ikakatwa, bado Mike alikuwa na hofu moyoni mwake, alikuwa na uhakika kwamba kulikuwa na kitu kilikuwa kimetokea, kila alipokaa, moyo wake ulikosa amani kabisa, hakutaka kukubali, alichokifanya nii kuondoka kuelekea huko uwanja wa ndege.
Alipofika huko, moja kwa moja akaelekea katika uongozi wa uwanja huo na kuwaambia kilichokuwa kimetokea hivyo kuchukua simu na kuwapigia watu wa mawasiliano ili waambie mahali ndege hiyo ilipokuwa kwa kipindi hicho.
“Hakuna mawasiliano...” alisema jamaa mmoja mara baada ya kujaribu kuwapigia marubani waliokuwa ndani ya ndege hiyo.
“Hamuwapati kabisa?”
“Ndiyo mkuu! Labda kuna tatizo la hali ya hewa, tutaendelea kuwatafuta,” alijibu jamaa wa upande wa pili.
Mike hakutaka kuondoka mahali hapo, alitaka kufuatilia mpaka mwisho, alihitaji kufahamu ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea, moyo wake ulikuwa mzito mno, kuna kipindi alisikia sauti ikimwambia kwamba ndege hiyo ilipata ajali lakini wakati mwingine alipiga moyo konde na kusema kwamba hayo yalikuwa mawazo ya kijinga tu.
Muda ulizidi kwenda mbele, baada ya saa mbili, matokeo wala hayakubadilika, yaliendelea kubaki vilevile kwamba marubani hao hawakupatikana.
“Kuna tatizo?” aliuliza Mike.
“Inawezekana ndege imepata ajali na kuzama baharini. Ngoja tuwasiliane na watu wa usalama wa majini,” alisema kiongozi wa mahali hapo na kuanza kuwasiliana.
Uchunguzi ukaanza kufanyika haraka sana, baada ya saa sita, wakapewa taarifa kwamba kulikuwa na ndege iliyokuwa imepata ajali na kuanguka baharini, walipoambiwa wataje iliandikwa vipi kwa nyuma, wakasema G550.
“Ndiyo yenyewe....” alisema Mike, akajikuta miguu ikiishiwa nguvu na kukaa chini.
Machozi yakaanza kumtoka, hakuamini kilichokuwa kimetokea, alimsubiri kwa hamu mpenzi wake, alitaka kumsubiri, ampokee kwa mabusu mfululizo, sasa ilikuwaje ndege aliyopanda ipate ajali, tena katika siku ambayo kwake ilionekana kuwa ya thamani kuliko siku nyingine.
Walichokifanya ni kuwasiliana na watu wa majini na kwenda huko kufuatilia kama kuna mtu yeyote aliyepona. Mike hakutaka kukubali, hakutaka kuletewa taarifa tu bali alichokifanya na yeye kuelekea huko ili kujionea mwenyewe.
Helkopta ikaandaliwa na ndani ya dakika chache walianza safari ya kuelekea huko. Njia nzima Mike alikuwa akilia tu, hakuwa akiamini kile kilichokuwa kikiendelea kwamba mpenzi wake na mtoto wake mtarajiwa walikuwa wamekufa.
“Hivi ni kweli Aisha amekufa?” alijikuta akiwauliza watu aliokuwa nao humo ndani.
“Hatujui, lakini hakuna aliyekufa, kama kweli ilipata ajali muda saa chache zilizopita, wote watakuwa salama,” alijibu jamaa mmoja, maneno yake yalikuwa yenye kutia moyo ila kwa Mike, yaligonga mwamba.
Walichukua saa mbili mpaka kufika mahali ambapo ndege hiyo ilipokuwa imepata ajali alfajiri ya siku hiyo. Walipofika hapo, waliikuta ndege hiyo, lakini kitu cha ajabu hawakukuta mwili wa mtu hata mmoja zaidi ya nguo za marubani ambazo zilionekana kuraruliwa hali iliyoonyesha kwamba walikuwa wametafunwa na papa.
“Kitu cha kwanza ni kutafuta kiboksi cheusi,” alisema jamaa ambaye alionekana kuwa kongozi wao.
Vijana wawili waliokuwa na mitungi ya hewa safi wakaingia ndani ya maji, huko, wakaanza kutafuta hicho kiboksi cheusi ambacho waliambiwa wakitafute, wala hawakuchukua muda mwingine wakakipata na hivyo kuanza kuitafuta miili miili ya watu waliokuwa ndani ya ndege hiyo.
Zoezi hilo lilikuwa kubwa na gumu, walitafuta zaidi na zaidi, walikwenda huku na kule lakini hawakuweza kuiona miili hiyo kitu kilichowafanya kuwa na wasiwasi mno.
Kati ya watu wote waliokuwa mahali hapo, Mike ndiye alionekana kuwa makini, alikuwa akiangalia huku na kule, moyo wake ulimuomba sana Mungu kwamba afanikiwe kumuona mpenzi wake lakini hilo wala halikuwezekana.
Walikaa huko kwa saa tatu lakini hawakufanikiwa kitu, hivyo Mike kuhisi kwamba mpenzi wake na watu aliokuwa amewatuma, wote walikufa katika ajali hiyo, hivyo wakarudi nchini Marekani huku akiwa na uchungu mkali moyoni mwake.
****
“Usiogope Aisha....usiogope...” ilisikika sauti kutoka kwa Shawn.
“Ninakufa...ninakufa...niokoe...” alipiga kelele Aisha.
“Huwezi kufa, hauwezi kufa....”
Walikuwa kwenye maji, walijitahidi kujitoa ndani ya ndege ile na wote wanne kuanza kuogelea. Hawakujua marubani walikuwa wapi, walichokuwa wakikiangalia kwa wakati huo ni kuyaokoa maisha yao tu.
Waliendelea kuogelea, maboya waliyoyavaa yaliwasaidia sana kuogelea. Mawimbi yalikuwa yakipiga huku na kule, kwa Shawn na wenzake hakukuwa na tatizo lolote lile lakini kwa Aisha, ilibidi ashikwe ili asiweze kupelekwa na mawimbi hayo.
Waliendelea kuogelea kwa zaidi ya saa moja na nusu na ndipo kwa mbali sana wakaweza kukiona kisiwa, hawakujua kilikuwa kisiwa gani, kilikuwa kidogo sana, hivyo wakaanza kuelekea huko.
“Ni lazima twende kule,” alisema Shawn.
“Baridi litaniua...”
“Usife...huwezi kufa, jitahidi kuvumilia Aisha. Ukifa wewe, safari yetu ya kuja Kuwait itakuwa bure kabisa, vumilia,” alisema Shawn huku akiwa amemshika mkono Aisha, waliendelea kusonga mbele kukifuata kisiwa kile.
****
Hali ilikuwa mbaya kisiwani, baridi kali lilikuwa likipiga kupita kawaida, muda wote Aisha alikuwa akitetemeka, alitoka katika nchini Kuwait, moja ya nchi za kiarabu iliyokuwa na joto kali kutokana na hali ya jangwa iliyokuwepo huko.
Kwa Shawn na wenzake, hali haikuwa mbaya sana, walichokifanya ni kuelekea katika kipori kidogo kilichokuwa kisiwani humo na kisha kuchukua kuni na kurudi.
Walizungukwa na maji kila kona na kila walipoangalia, hakukuwa na dalili za meli au mtumbwi wowote ule. Walipelekwa huko bila kutaka, hawakujua Mashariki ilikuwa upande gani, Magharibi wala upande wowote ule.
Wakawasha moto kwa njia za kusaga mawe na kisha kuanza kuota moto. Hakukuwa na aliyelala, usiku mzima walikuwa mahali hapo, walichoka, njaa iliwauma lakini hawakuwa na jinsi, walikuwa wakisubiri msaada wowote ule, uwe meli, boti au chochote kile.
Siku ya kwanza ikakatika, walikuwa hapohapo kisiwani, siku ya pili nayo ikaingia lakini hakukuwa na dalili zozote zile. Walionekana kukata tamaa, wakati mwingine Aisha aliyaona mateso ya kukaa kisiwani hapo kuwa makubwa, ilikuwa ni afadhali kuuawa kule Kuwait kuliko kukutana na mateso makali aliyokuwa akikutana nayo mahali hapo.
Siku ya tatu ikaingia, napo hali ilikuwa mbaya zaidi, hakukuwa na chakula chochote kile, miili yao ikaanza kudhoofika, ikaanza kukosa nguvu kwani kama maji, walijitahidi kuyanywa hayohayo japokuwa yalikuwa ya chumvi lakini kuhusu chakula, hawakuwa na jinsi, waliendelea kubaki njaa hivyohivyo.
“Hatuwezi kuvumilia, ni lazima tuvue samaki,” alisema Shawn huku akiwaangalia wenzake.
“Hatuna nyavu!”
“Kwani kuvua samaki mpaka nyavu? Hakuna, hata kwa kutengeneza mikuki, tutaweza kuvua,” alisema.
Hicho ndicho walichokifanya, walikuwa majasusi, wenye mafunzo mengi, walifunduishwa namna ya kupambana katika kipindi kigumu kama hicho hivyo kitu walichokifanya kilikuwa ni kukata miti, wakaichonga kwa kutumia meno yao, walipoona kidogo imepata ncha kali, wakaingia baharini.
Uvuaji huo ambao ulitumika sana katika nchi zisizoendelea ndiyo walioutumia. Ulikuwa mgumu sana lakini waliweza kuufanya hivyohivyo. Siku hiyo ya kwanza ilikuwa ngumu kwao lakini wakafanikiwa kupata samaki waliowatosha na hivyo kurudi kisiwani na kuwachoma kisa kula.
Maisha yalikuwa hivyohivyo, hakukuwa na chakula kingine zaidi ya samaki ambao waliwala pasipo chumvi, hapo hawakuangalia ladha, walichokiangalia kilikuwa ni kushiba tu.
Mpaka siku ya nne inaingia, wakipigwa baridi kali nyakati za usiku lakini hakukuwa na msaada wowote ule uliokuja, waliendelea kuishi humohumo mpaka kuyazoea maisha ya humo kisiwani.
“Tutachukua muda gani mpaka kuondoka hapa?” aliuliza Aisha.
“Inategemea.”
“Na nini?”
“Na msaada tutakaoupata, kama utachukua siku kumi, tutakaa kwa siku hizo, kama utachukua mwaka mzima, hatuna jinsi,” alijibu Shawn.
Aisha alikata tamaa, alichokuwa akikitaka ni kufarijiwa na Shawn kwamba hata kama walijua kusingekuwa na msaada wowote ule lakini aambiwe tu kwamba msaada ungepatikana.
“Wiki moja imekatika, bado tupo hukuhuku kisiwani!” alisema Aisha huku mwili wake ukiwa umekonda kwa ajili ya mawazo na tabu za mule kisiwani.
“Ndiyo hivyo Aisha! Ninajaribu kuwatafuta kwenye simu, hakuna network,” alisema Shawn.
Walikuwa na simu, yenye uwezo mkubwa ambayo haikuwa ikipitisha maji, haikutumia betri la umeme bali sola hivyo ilivyofika mchana ilikuwa ni lazima kuichaji.
“Nahisi tutakufa hapa,” alisema Aisha huku akionekana kukata tamaa kabisa.
“Haiwezekani! Hatuwezi kufa hapa!”
“Tutaupata wapi msaada?”
“Sijui! Lakini kufa hapa! Haiwezekani Aisha, tutapata msaada tu.”
Wiki ya tatu ilipoingia, Aisha akaanza kujisikia vibaya, kizunguzungu kikaanza, tumbo likaanza kumuuma mno. Alilia siku nzima, Shawn na wenzake ndiyo waliokuwa wakimpoza na kumsaidia katika kila kitu.
Hakukuwa na dawa mahali hapo, walichokifanya ni kutumia mizizi ya miti iliyokuwa kisiwani hapo kama dawa za kumtibu Aisha ambaye kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele, hali yake iliendelea kuwa mbaya sana.
“Vipi Shawn?” aliuliza Sam.
“Network inakuja na kukata, inakuja na kukata....” alijibu Shawn.
Hiyo ilikuwa ni saa kumi alfajiri, hawakulala usiku mzima, ni Aisha tu ndiye aliyelala tena kwa usingizi wa mang’amung’amu. Wao walikesha wakiiangalia simu ambayo ilikuwa inashika network na kupotea.
“Fanya kitu kimoja.”
“Kipi?”
“Mtumie meseji Mike.”
“Hakuna network.”
“Wewe mtumie, kama network ikija, meseji itakwenda tu.”
Hakuwa na jinsi, alichoambiwa kilikuwa sahihi kabisa hivyo kutuma meseji hiyo ambayo wala haikwenda kutokana na eneo hilo kukosekana kwa network.
****
Mike alichanganyikiwa, hakuamini kama kweli alimpoteza msichana aliyekuwa akimpenda kwa moyo wote lakini kilichomuumiza zaidi ni kupotea kwa mtoto wake ambaye angetarajiwa kuzaliwa miezi michache ijayo.
Akakosa furaha, akawa mtu wa kulia tu, kila siku akawa anaomboleza, wakati mwingine aliona kama Mungu akimuonea tu. Alitumia gharama kubwa mno kumuokoa Aisha kutoka katika kifo nchini Kuwait mpaka huko lakini mwisho wa siku, hata kabla hajaingia nchini Marekani, tayari msichana huyo alikufa njiani.
“Mungu! Mlaze mpenzi wangu mahali pema peponi,” alisema Mike.
Hakuwa na jinsi, moyo wake ulimwambia kwamba alimpoteza mpenzi wake, hakukuwa na kingine alichokifanya zaidi ya kumtaka Mungu amlinde Aisha huko alipokuwa.
Wiki ya kwanza ikakatika, hakukuwa na taarifa zozote zile, wiki ya pili ikakatika, hakukuwa na taarifa zozote kutoka huko walipokuwa. Ilipofika wiki ya tatu, tena katikati, saa mbili asubuhi akiwa ofisini kwake huku akiwa na mawazo, akasikia mlio wa meseji ukiwa umelia kuashiria kwamba kuna meseji imeingia.
Akaichukua simu yake na kuifungua meseji hiyo, akakutana na ujumbe mfupi ulioandikwa ‘WE STILL ALIVE IN THE ISLAND’ (BADO TUPO HAI KISIWANI) Mike akashtuka, alipoangalia namba, ilikuwa ni ya Shawn.
Je, nini kitaendelea?