UTAJIRI WENYE UCHUNGU
0718069269
Sehemu ya Ishirini na Mbili.
Muda wote Dylan na mkewe walionekana kuwa na furaha tele, hawakuamini kilichokuwa kikiendelea kwamba mwanamke huyo alishika ujauzito ambao kadiri siku zilivyokuwa zikizidi kwenda mbele, tumbo lake likaanza kuonekana.,
Dylan hakuamini kama mwisho wa kila kitu, mkewe angepata ujauzito na hivyo yeye kuitwa mwanaume kamili kama ilivyokuwa wengine. Kila alipopita, mikono yake aliitanua, ofisini kwake, kila wakati alikuwa akiwaambia wafanyakazi wenzake ni jinsi gani alikuwa na furaha na jinsi alivyohangaika kumfanya mke wake kushika ujauzito huo.
Hakumfikiria mwanaume ambaye alizitoa mbegu zake kwa ajili ya mke wake, alichokifikiria kwa wakati huo ni mkewe tu, tena kwa kujitapa kwamba watoto walikuwa wake.
Kwa Katty, muda wote alikuwa na furaha hakutaka kutoka nyumbani kwake, kila siku alibaki ndani, alihisi kwamba anaweza kupata ajali na kufariki, alijichunga na kadiri siku zilivyokuwa zikienda mbele, Marekani nzima wakajua kwamba mke wa bilionea Dylan alikuwa mjauzito.
“Mimi kidume Christina, nilikwambia, ukabisha,” Dylan alimwambia ndugu yake wakati wakiongea kwenye simu.
“Safi sana, umefanya kazi kubwa, tunahitaji kupata watoto wetu sasa,” alisema Christina huku kwa sauti yake tu, ilionyesha ni jinsi gani alikuwa na furaha.
Siku zikaendelea kukatika, Dylan akashindwa kuvumilia, alichokifanya ni kumnunulia mkewe zawadi ya gari la thamani aina ya Buggati ambalo hilo alitaka alitumie kipindi alichokuwa akienda hospitalini.
“Nashukuru sana mume wangu! Unanifanya nijisikie kupendwa sana,” alisema Katty pasipo kufahamu kilichotokea nyuma ya pazia.
Mimba tu ikaanza kuwaweka pamoja na kwa ukaribu mkubwa. Dylan akawa mtu wa kuwahi kurudi nyumbani, kuliona tumbo la mkewe, ilimpa furaha kubwa.
“Daktari amesemaje?” aliuliza Dylan.
“Amesema nina mapacha! Wa kike na wa kiume.”
“Unasemaje?”
“Nina mapacha mume wangu!”
Dylan hakuamini, hapohapo akamkumbatia mkewe, akashindwa kuvumilia, machozi ya furaha yakaanza kumtiririka mashavuni mwake. Shukrani zake zote zilikuwa kwa Dk. Fabian ambaye ndiye aliyefanikisha suala zima la upachikaji wa mbegu katika yai la mkewe.
“Nashukuru kwa kila kitu!”
“Asante na wewe pia! Hakika najisikia faraja sana kuona zoezi langu limefanikiwa,” alisema Dk. Fabian huku akiwa na furaha mno.
Baada ya miezi tisa, Katty akaanza kujisikia uchungu wa kuzaa. Siku hiyo, Dylan alikuwa nyumbani kwake, ilikuwa ni saa sita usiku. Wakati mkewe akilalamikia uchungu, tayari gari lilikuwa tayari nje kwani alijua kwamba kitu kama hicho kingetokea kutokana na muda kufika.
Alichokifanya ni kumbeba na kumpeleka ndani ya gari na safari ya kuelekea hospitalini kuanza. Njiani, alikuwa na furaha tele. Hawakuchukua dakika nyingi, wakafika ambapo manesi wakaleta machela na yeye kuanza kuifuata kule manesi walipokuwa wakiisukumia, walipofika katika chumba kilichoandikwa ‘Labour’ akatakiwa kusubiri kwenye viti vilivyokuwa nje ya chumba hicho.
Huku nje, alikuwa na presha kubwa, muda wote alikuwa amesimama, alitembea huku na kule, alitaka kusikia watoto wakilia ndani ya chumba hicho. Watu wote waliokuwa katika eneo hilo walibaki wakimwangalia, walimfahamu, alikuwa bilionea mkubwa Marekani, utajiri ambao aliachiwa na baba yake aliyekuwa amezeeka na hivyo kuhitaji msimamizi.
Baada ya dakika arobaini na tano, akajikuta akianza kurukaruka kwa furaha, hakuamini hata kidogo kile alichokisikia ndani ya chumba hicho. Sauti za watoto zikaanza kusikika. Akajikuta akitoka mbio na kuwakumbatia madaktari waliokuwa mahali hapo, tena kwa zamu. Kile kilichotokea, kilidhihirisha kwamba yeye naye alikuwa mwanaume rijali.
****
Walibaki wakiangaliana, macho yao tu yalionyesha kila kitu kilichokuwa kikiendelea mioyoni mwao. Watu wengine walibaki wakiwaangalia Mike na msichana Aisha, hawakuonekana kuwa mahali hapo, mawazo yao yalikuwa yamehama na yalikwenda sehemu nyingine kabisa.
Mwenyekiti wa mkutano huo akajikoholesha kama njia mojawapo ya kuwaambia watu hao kwamba walitakiwa kuacha kile kilichokuwa kikitokea kwao na wamsikilize yeye.
Hiyo ilisaidia, Mike akamgeukia mwenyekiti huyo lakini muda wote macho yake yalikuwa kwa msichana huyo. Siku hiyo, tena kwenye kikao hicho kazi ilikuwa ni kuangaliana kwa zamu tu.
Mapenzi mazito yakawaingia wote wawili, hawakuamini kama ingechukua muda mfupi kiasi hicho mpaka macho yao kuzoeana. Mkutano uliendelea, ulipomalizika, Mike akashindwa kuvumilia, akamfuata msichana huyo.
“Unaniangalia sana....” alisema Aisha.
“Kwa sababu u mzuri sana, siamini kama duniani kungekuwa na msichana mrembo kama wewe,” alisema Mike, macho yake tu yalionyesha ni kwa kiasi gani alikubaliana na uzuri wa msichana huyo.
“Kweli?”
“Ndiyo!”
“Asante!”
Aisha hakutaka kukaa sana kuzungumza na Mike, alizijua sheria za nchi hiyo, haukutakiwa kupendana na kuishia njiani, kama kweli mlipendana basi ilikuwa ni lazima kuoana na si kuchezeana, sheria nyingine ni kwamba hamkutakiwa kufanya ngono mpaka pale mtakapoona, vinginevyo, mkigundulika mnapigwa mawe hadharani mpaka kufa.
“Aisha...” aliita Mike. Aisha akageuka.
“Unasemaje?”
“Una macho mazuri sana, naomba unitafute...” alisema Mike, akampa kikaratasi kilichokuwa na namba yake na kisha kila mmoja kuondoka.
Hotelini, bado Mike alikuwa amechanganyikiwa. Sura ya mtoto wa Kiarabu ilimchanganya mno, hakuamini kama kweli angekutana na msichana huyo nchini Kuwait.
Usiku hakulala, alibaki akimfikiria msichana huyo mrembo kiasi kwamba akajisahau kabisa na mawazo kuhusu ndoa yakaanza kumuandama. Kwa sababu alimpa namba ya simu, alichokuwa akikisikilizia kipindi hicho ni kupigiwa simu tu.
Ilipofika saa tatu usiku, simu yake ikaanza kuita, hakuamini, namba ilikuwa ngeni hivyo harakaharaka akaichukua na kuipokea.
“Aisha...” alijikuta akiita baada ya kupokea.
“Umejuaje?”
“Hakuna mwenye namba yangu ambaye anaweza kupiga muda huu zaidi yako mrembo,” alisema Mike huku akiachia tabasamu pana kana kwamba msichana huyo alikuwa mbele yake.
“Mmmh! Aya! Niambie unataka kuniambia nini?” aliuliza Aisha.
“Nataka twende sehemu, tukakae na kuzungumza,” alijibu Mike.
“Sehemu gani?”
“Yoyote ile ya siri! Tukutane kisiri na tuzungumze...” alisema Mike.
“Mmh! Si Marekani hapa, ni Kuwait, hilo jambo haliwezekani,” alisema msichana Aisha.
“Kwa hiyo inakuwaje?”
“Labda tukutane sehemu nyingine.”
“Wapi?”
“Dubai! Huko kidogo sheria hazibani!” alijibu msichana huyo.
“Hakuna tatizo! Nataka twende kesho!”
“Ila si kuna mkutano mwingine!”
“Achana nao! Wewe ni muhimu kuliko hata huo mkutano!” alisema Mike. Aisha akacheka kidogo, wakakubaliana na simu kukatwa.
Kilichofuata ni Mike kuwa na presha kubwa ya kukutana na msichana huyo huku akijua kwamba watakapofika Dubai, hakuna sehemu yoyote ambayo wangekutania zaidi ya hotelini ambapo huko angemaliza kila kitu.
“Lazima...lazima, sijawahi kumpata Mwarabu...lazima,” alijisemea huku akivua nguo zake kwa ajili ya kulala. Hata usingizi haukumpata kwa wakati, kila wakati alimfikiria Aisha tu.
*****
Dylan hakuamini kama mke wake alikuwa amejifungua watoto mapacha, pale nje alipokuwa alikuwa akirukaruka kwa furaha huku akimkumbatia kila mtu aliyepita mbele yake.
Alibaki mahali hapo kwa dakika zaidi ya arobaini na ndipo baadaye mkewe alipotolewa na kupelekwa katika chumba cha mapumziko ambapo huko kulikuwa na wanawake wengi waliokuwa na watoto wao.
Hakutaka mke wake awe huko, alikuwa bilionea mkubwa hivyo alichokitaka ni mke wake kupelekwa katika chumba kingine cha peke yake, na hicho ndicho kilichofanyika haraka sana.
Dylan alibaki akimwangalia mkewe, alionekana kuwa na furaha muda wote, hakuamini kama kweli leo hii alikuwa akiitwa baba. Alichukua simu yake na kumpigia baba yake na kumpa taarifa hizo, baba yake alifurahi kwa kupata wajukuu.
Hakuishia hapo tu bali alichokifanya ni kuwapigia marafiki zake wengine akiwemo Catherine na kumwambia kile kilichokuwa kimetokea, msichana huyo hakutaka kubaki nyumbani, japokuwa ilikuwa ni usiku wa manane, akaamka na kuelekea hospitalini.
“Wa kiume ataitwa Patrick, na wa kike ataitwa Patricia,” alisema Dylan huku uso wake ukiwa kwenye tabasamu pana.
Kitu cha kwanza alichokifanya ni kumshukuru mke wake kwa zawadi nzuri aliyompa ambayo hakuweza kuifikiria kabla. Kila alipomwangalia, kwa furaha aliyokuwa nayo, machozi yakaanza kumbubujika mashavuni mwake.
“Nashukuru sana mke wangu,” alisema Dylan huku akimwangalia Katty usoni.
“Asante kwa kushukuru...nililia sana kwa ajili ya hawa watoto,” alisema Katty.
Wala haikuchukua muda mwingi, Catherine akaingia ndani ya chumba hicho, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kuwafuata watoto wale, akawaangalia, moyo wake ukaridhika, furaha ya ajabu ikampata moyoni mwake.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa furaha ya familia hiyo. Dylan akajipa likizo ya mwezi mzima, hakutaka kutoka ndani ya nyumba yake, alibaki huko huku muda wote akiwa pembeni ya watoto wake.
Japokuwa usiku walikuwa wakilia sana, hakujali, kelele zao zilikuwa ni furaha tele kwake. Yeye ndiye aliyekuwa na jukumu la kuwabadilisha nguo, yeye ndiye alikuwa na jukumu la kuzifua nguo zao kwani hakutaka kabisa wafanyakazi wafanye kitu chochote kwa ajili ya watoto wake.
Mwezi ulipokatika, hapo ndipo alipoanza kwenda kazini. Huko, hakuwa mkaaji sana, ilikuwa ni lazima arudi nyumbani mapema mno. Kila mtu aliyekuwa akimtazama, alionekana dhahiri kuwa na furaha kubwa moyoni mwake, alimsalimia kila mtu na kila aliporudi nyumbani, ilikuwa ni lazima awe na mfuko uliojaa nguo kwa ajili ya watoto wake.
“Nitahakikisha nawapa kila kitu,” alimwambia mke wake.
“Kweli?”
“Ndiyo! Nimekuwa na furaha mno, maisha yangu yamebadilika, wameniletea kitu moyoni mwangu ambacho sikuwa nikikifikiria kabla,” alisema Dylan huku akiwa na Patricia mikononi mwake.
Siku ziliendelea kukatika, miezi ikaenda mbele mpaka mwaka ulipokatika, bado biashara yake ilikwenda vizuri, mafanikio yaliendelea kumiminika. Mwaka wa pili ukaingia, wa tatu mpaka wa nne ambapo mapacha hao wakaanza kusoma chekechea.
Jukumu la kuwapeleka shuleni lilikuwa lake, hakutaka mtu yeyote achukue jukumu hilo. Watoto hao walikuwa wazuri wa sura, walifanana mno. Patricia ambaye ndiye alikuwa Kulwa, sura yake iliwachanganya watu wengi, urembo wake uliwafanya watu kuona kwamba mtoto huyo angekuwa msichana mrembo mno siku za usoni.
Shule waliyokuwa wakisoma ilikuwa ni St. Pius International School, hiyo ilikuwa miongoni mwa shule za matajiri, watoto waliokuwa wakisoma shuleni hapo, wazazi wao walikuwa matajiri au viongozi wa serikali kama mawaziri.
Mbali na utajiri, pia serikali iliwasomesha watoto waliokuwa na uwezo kiakili shuleni hapo. Ilikuwa ni shule ya vipaji lakini upande wa pili ilikuwa ni shule ya matajiri.
Kila siku ilikuwa ni lazima kwa Dylan kuwapeleka shule watoto wake na kuwarudisha nyumbani. Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake ya kila siku, hakutaka kuona wakipata tabu yoyote ile, kwake, watoto wake ndiyo walikuwa kila kitu.
Miaka haikumsubirii mtu yeyote ile, baada ya kufikisha miaka nane, uzuri wa Patricia ukazidi kuongezeka, vijana wengi shuleni hapo wakamtolea macho, japokuwa alionekana kuwa mtoto lakini umbo lake lilikuwa kubwa, vijana wengi wakaanza kuweka mazoea na kijana wa kwanza kabisa kuwa karibu naye aliitwa Tenny Andrew.
Huyu alikuwa mtoto wa waziri mstaafu nchini Marekani, Bwana Carthbert Andrew. Alikuwa miongoni mwa watoto waliokuwa na akili nyingi shuleni hapo. Kila mmoja alitamani kuwa karibu na kijana huyo ambaye kama ingekuwa Tanzania, basi tungesema kwamba kijana huyo alikuwa darasa la saba huku Patricia akiwa darasa la tano.
Ukaribu wao ulianza taratibu, watu wengi wakaanza kuhisi kwamba nyuma ya pazia kulikuwa na kitu kinaendelea. Walimu hawakutaka kukaa kimya, walichokifanya ni kumuita Tenny na kuzungumza naye, walimwambia kabisa kwamba ukaribu wake na msichana Patricia uliwatia shaka lakini yeye mwenyewe hakutaka kukubaliana nao.
“There is nothing is going on, trust me,” (hakuna kinachoendelea, niamini) alisema Tenny.
Huku nyumbani, Bwana Dylan hakutaka kuvuruga ratiba yake. Kila siku ilikuwa ni lazima kuwapeleka watoto wake shuleni na kisha kuwarudisha kila ilipofika mchana.
Siku ziliendelea kukatika mpaka pale ambapo Bwana Dylan alipotaka kuwafanyia sapraizi watoto wake kwa ajili ya siku yao ya kuzaliwa.
Siku hiyo hakutaka kuwapeleka shuleni, alipotoka ofisini mapema sana, akapitia supamaketi ambapo akawanunulia keki kubwa, zawadi nyingine na kisha kurudi nyumbani.
Alipofika huko, akamuita mke wake na kumwambia kile alichotaka kukifanya. Kilionekana kuwa kitu kizuri sana. Ili kitu kile kikamilike, ilikuwa ni lazima dereva ndiye awafuate shuleni huko siku hiyo.
Akawasiliana na dereva na hivyo kwenda kuwachukua. Yeye na mkewe walibaki nyumbani, waliandaa mazingira mazuri, wakawaita watu wengine kwa ajili ya kusherehekea nao.
Muda ukaanza kwenda, ulikwenda na kwenda, kitu ambacho kiliwashangaza na kuwashtua ni kwamba watoto hao hawakufika nyumbani. Haikuwa kawaida, shule haikuwa mbali na nyumbani hapo, wakampigia simu dereva ili kumuuliza walikuwa wapi na kitu gani kilikuwa kikiendele, kilichowatisha, simu ya dereva huyo haikuwa ikipatikana.
“I can’t reach him on the phone,” (Simpati kwenye simu) alisema Bwana Dylan.
“What?” (Nini?) aliuliza mkewe.
“I can’t reach him,” (Simpati)
Kila mmoja alichanganyikiwa, kile walichokisikia hakikuaminika kabisa, walichokifanya ni kuondoka nyumbani hapo, seherehe ile iliyoandaliwa, ikavurugika kwa muda. Bwana Dylan akaingia ndani ya gari, aliendesha gari yeye mwenyewe na tena kwa kasi kubwa.
Wakafika shuleni, hakukuwa na mwanafunzi yeyote yule, wakaelekea mpaka katika ofisi ya walimu na kuwauliza kama dereva alifika shuleni hapo. Wakaambiwa kwamba alifika, aliwachukua watoto hao na kuondoka nao.
“Kwani nyumbani hawakufika?” aliuliza mwalimu mmoja.
“Hawakufika! Aliwachukua muda gani?”
“Kama saa moja lililopita!”
“Watakuwa wapi?”
“Hata sisi tunashangaa...”
Kweli walichanganyikiwa, hawakujua ni kitu gani kilikuwa kimetokea, walichokifanya ni kujaribu tena kumpigia simu dereva, kama kawaida majibu yalikuwa yaleyale, simu haikupatikana. Walichanganyikiwa, dakika ziliendelea kusonga mbele, waliogopa hivyo walichokifanya ni kuwasiliana na polisi.
“Hatujui walipo...”
Hivyo ndivyo walivyosema, polisi wakaanza kuwatafuta. Waliwatafuta kwa kuanzia kamera zao za barabarani, hawakupatikana. Walichanganyikiwa, hawakujua watoto hao walipelekwa wapi na dereva huyo.
Muda wote Katty alikuwa akilia tu, hakuwa akiamini kilichokuwa kikiendelea, Dylan, japokuwa yeye mwenyewe alikuwa na uchungu lakini hakutaka kuuonyesha waziwazi, hivyo akajitahidi kumliwaza mke wake. Mpaka inafika saa mbili usiku, polisi hawakumpata dereva wala watoto. Wakazidi kuchanganyikiwa.
Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumapili.
Tunasubiria kujua upande Wa pil kilichojir
Yeah!!.....tuone nn kimetokea kwa Aisha!Tunasubiria kujua upande Wa pil kilichojir