Hongera Kikwete kwa kazi nzuri AU
Mhariri
Daily News; Sunday,February 01, 2009 @21:15
Tanzania leo inamaliza uenyekiti wake wa mwaka mmoja wa Umoja wa Afrika (AU) uliokuwa ukishikiliwa na Rais Jakaya Kikwete, tangu Februari mwaka jana. Rais Kikwete anamaliza muda wake wakati wa mkutano wa kawaida wa viongozi wa nchi na serikali wa Afrika watakapoanza rasmi mkutano wao leo mjini Addis Ababa, Ethiopia, yalipo makao makuu ya AU.
Rais Kikwete anafanya hivyo kutokana na utaratibu wa kawaida wa Katiba ya AU ambayo inaeleza kuwa nafasi hiyo itakuwa ya kuzunguka baina ya nchi wanachama kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Tanzania chini ya Rais Kikwete inakabidhi uenyekiti huo wa AU, ikiwa na mengi ya kujivunia iliyoyafanya wakati wa mwaka wake mmoja wa kushika wadhifa huo mzito na wenye majukumu mengi. Rais Kikwete amefanya mengi ya kukumbukwa chini yake akiwa Mwenyekiti wa AU.
Tanzania, kwa msaada wa AU ilikwenda katika kisiwa cha Anjouan nchini Comoro ambako iliweza kumwondoa madarakani kiongozi muasi, Kanali Mohamed Bakar baada ya kujitangazia madaraka kinyume cha Katiba katika kisiwa hicho.
Majeshi hayo ya Tanzania ya vijana 700 waliweza kuhakikisha muasi huyo anaondoka nchini humo na anawaacha wananchi wa Anjouan wakifurahia maisha katika kisiwa chao kwa amani, bila ya umwagaji damu. Hongera Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ). Hongera Rais Kikwete.
Si hilo tu. Kwa juhudi zake na kwa kuwa mstari wa mbele, Rais Kikwete alikwenda Kenya na kumaliza mzozo na machafuko yaliyotokana na Uchaguzi Mkuu wa Desemba 2007, ambao ulisababisha mauaji ya Wakenya zaidi ya 2,000.
Mwenyekiti huyo wa AU kwa busara na uwezo wake, alizishawishi pande zilizokuwa zikivutana katika mzozo huo wa uchaguzi, kukaa meza moja na kufikia makubaliano ambayo sasa Kenya ni moja na wanaijenga nchi yao.
Jingine alilolifanya katika kuleta amani ni suala la mgogoro wa muda mrefu wa Burundi ambako amewezesha kusitishwa kwa mapigano na kufikiwa kwa mkataba wa amani baada ya mauaji na vita ya muda mrefu kati ya waasi na jeshi la serikali.
Juzi, siku chache kabla ya kukabidhi madaraka leo, alikuwa Afrika Kusini, ambako kwa wadhifa wake wa uenyekiti wa AU, alishirikiana na viongozi wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kuzishawishi pande zinazovutana Zimbabwe kutekeleza makubaliano ya kugawana madaraka yaliyofikiwa Septemba mwaka jana baada ya uchaguzi uliokuwa na kasoro.
Yapo pia ya kuleta mabadiliko katika Sekretarieti ya AU mjini Addis Ababa ambako kwa mujibu wa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Rais Kikwete amemaliza tatizo la muda mrefu lililokuwa likiwakabili watumishi katika Sekretarieti ya AU kwa kufanikisha kuongezwa mishahara ikiwamo kulipwa malimbikizo, posho za matibabu na elimu ambazo walikuwa wanadai kwa miaka mitano iliyopita.
Tunajua kuwa yapo masuala kadhaa ambayo pengine aliahidi au yalipaswa kutekelezwa katika kipindi chake cha uongozi wa mwaka mmoja, lakini ni ukweli usiofichika kuwa Rais Kikwete amefanya makubwa katika kipindi hicho.Ikumbukwe kuwa chini ya uongozi wake, ameweza pia kuifanya Tanzania na Afrika kwa ujumla, kuwa na sauti katika medani ya kimataifa, hali ambayo imeongeza ushawishi wa mataifa makubwa kwa Afrika.
Tunaamini Rais Kikwete anamaliza uenyekiti wa AU akiwa ametekeleza kwa ufanisi mkubwa na kwa umakini majukumu yake, kiasi kuwa ameliweka jina la Tanzania na Afrika kwa ujumla katika ajenda za mataifa makubwa. Tunampongeza Rais Kikwete kwa kazi nzuri na kumtakia kila la heri katika jukumu lake la kuwahudumia Watanzania baada ya jukumu kubwa na zito la kuwaongoza Waafrika kwa mwaka mmoja uliopita.