Mdau, binafsi nakupongeza kwa kuliona hilo na kuona kwamba ipo haja ya kutoa angalizo kwa kile ulichokisikia kupitia redio hiyo inayomilikiwa na taasisi ya dini ya Kiislam.
Kwangu mimi, cha msingi ninachokiona kwenye mada yako ni kuhusu uchochezi wa kidini unaofanywa na Redio hiyo na maafa yanayoweza kulikumba taifa letu kama hatua za haraka hazitachuliwa kudhibiti hali hiyo. Mimi binafsi sina tatizo na hoja yako. Kimsingi ni angalizo linalopaswa kuungwa mkono na kila mpenda amani. Hata hviyo, ninachotaka kuongeza hapa ni kwamba, hali ya mustakabali wa kidini katika Tanzania kwa sasa ni tete. Na hili halina ubishi hata kidogo, labda iwe kwa mtu mwenye hulka ya kubishia kila jambo ndiye pekee anayeweza kupingana na ukweli huu.
Hali tuliyo nayo sasa hapa nchini haishirii dalili njema hata kidogo mbele ya safari. Zinahitajika hatua za maksudi kabisa katika kukabiliana na hali hii kabla bomu halijalipuka. Ni vema watanzania tukatambua kwamba machafuko yenye sura kama hizi za kidini mahali popote yalipopata kutokea duniani, hayakuja kama mvua au kwa bahati mbaya, la hasha!. Machafuko yalianza kama masihala kwa njia kama hizi hizi za chochoko, malumbano,na uchochezi wa chini kwa chni kama tunavyoanzashudia hapa kwetu Tanzania.
Binafsi sipendi kuhukumu kwamba ni dini gani hasa ndio inayoonesha dalili za kutaka kutupeleka kwenye machafuko ya kidini ambayo ni machafuko mabaya kupita machafuko mengine yoyote katika dunia hii. Nasita kufanya hivyo kwa sababu imani yangu inanizuia kukuhukumu na kusisitiza zaidi kuchunguza boriti ndani ya jicho langu kabla ya kutoa kibanzi katika mboni ya jicho la mwenzangu. Hata hivyo, natambua dhahiri shahri kwamba mustakabli wa hali ya kidini hapa nchini imekuwa tete tangu mchakato wa uchaguzi Mkuu wa mwaka jana. Hivyo basi, ni wajibu wa kila mtanzania mwenye dini na asiye na dini kuliona hilo na kuchukua hatua kwa nafasi yake ili kuzuia dalili mbaya zinajitokeza katika taifa letu.
Na mwisho ninapendekeza kwamba, kama ilivyo hitaji la watanzania kuwa na Katiba Mpya, basi halikadhilika iwe hivyo hivyo katika jambo la kidini. Sio vibaya tukawa na mjadala wa kitaifa kuhusu hatma ya mivutano ya kidini iliyoanza kujitokeza hapa nchini. Na kwa njia hiyo pekee ndipo tutaweza kutoa fursa kwa kila upande utoe dukuduku lake na kisha kufikia muafaka wa pamoja. Lakini, tukiendelea kupuuza, kukejeliana,kutukanana na kushutumiana bila kuchukua hatua zozote haitatusaidia. Tukumbuke kwamba panapofuka moshi lazima pana moto!!
Mungu ibariki Tanzania na watu wake!!!