This is the Wassira I used to know
Jasusi
Serikali yaparaganyika
Mwandishi Wetu
Aprili 21, 2010
Mawaziri, watendaji kila mtu na njia yake
Dk. Slaa asema ni dalili za mwanzo za ufalme uliogawanyika
IKIWA katika maandalizi ya kuomba kura kurejea tena madarakani, Serikali ya Rais Jakaya Kikwete, haiko pamoja, ushahidi wa hili ukiwa matukio kadhaa likiwamo la karibuni zaidi la mawaziri kupingana waziwazi nje katika suala lililopitishwa ndani ya Baraza la Mawaziri, Raia Mwema limebaini.
Wiki iliyopita Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Steven Wasira akichangia katika muswada wa Sheria ya Madini wa mwaka 2010 aliupinga muswada huo akisema kwamba haukuwa na maslahi kwa umma wa Watanzania.
Wasira alifanya hivyo mbele ya Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, na mbele ya wabunge wengine na wadau mbalimbali wa madini nchini katika mkutano wa wadau hao wa madini uliokuwa umeitishwa kuudurusu muswada kabla ya kuuwasilishwa bungeni. Miswaada huwasilishwa bungeni baada ya Baraza la Mawaziri kuiridhia.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Sera, Bunge na Uratibu, Philip Marmo, ameiambia Raia Mwema kuwa muswada huo wa Sheria ya Madini wa mwaka 2010, ulijadiliwa kwa kina kwenye Baraza la Mawaziri.
Lakini katika maoni yake nje ya Baraza la Mawaziri, Wasira ambaye ni Mbunge wa Bunda, Mara alihoji: "Nchi inapata nini na wananchi watapata nini?" na baada ya kuhoji alishauri kuwa lazima muswada wa sheria hiyo kwa makusudi ulenge kusaidia wachimbaji wadogo ambao ndio msingi mkubwa wa maendeleo ya sekta ya madini.
Waziri huyo ambaye alisema wazi kuwa alikuwa akizungumza kama mdau wa madini akiwa hana elimu ya sheria, alisema suala la madini ni suala nyeti nchini na kwa hali yoyote sheria inayotarajiwa kutoa mwongozo wa madini, lazima ijibu hoja muhimu za manufaa kwa Taifa na wananchi.
"Haya mapendekezo yanatofautiana hata na Sera ya Taifa ya Madini," alisema Wasira huku akifungua ukurasa wa 16 wa kitabu cha sera hiyo cha Septemba 2009, kilichotiwa saini na Waziri Ngeleja na kusoma sehemu iliyoandikwa Policy Statement.
Katika sehemu hiyo, kipengele cha ii cha kitabu hicho ambacho gazeti hili limefanikiwa kupata nakala yake inasema: "Serikali itachukua hatua za lazima kuwawezesha Watanzania kushiriki katika uwekezaji wa kati na mkubwa wa uchimbaji madini (
The Government will take necessary measures to enable Tanzanians to participate in medium and large scale mining.)"
"Je, haiwezekani kuwawezesha watu masikini, wawekezaji wa ndani?" alihoji Wasira akitoa mfano wa Sweden ambayo uchumi wake unategemea madini kutokana na kuwezesha wachimbaji wadogo wazawa.
Waziri Wasira alisema wazi kuwa sheria lazima ijibu hoja za sera, na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ambavyo vinataka wachimbaji wadogo kuendelezwa na kuwa msingi wa uchumi mambo ambayo katika muswada huo hayakujionyesha.
Lakini wakati Wasira akisema hayo hasa Muswada huo wa madini kushindwa kujibu Sera ya Taifa ya Madini, Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka, naye anabaini kuwa muswada huo umekwenda kinyume cha Sera ya Taifa ya Madini na hasa katika kipengele cha kutaka migodi ya madini ya vito kuendeshwa na wazawa kwa asilimia isiyopungua 50.
"Sera inataka Watanzania waweze kuendesha migodi ya vito kwa asilimia isiyopungua 50 lakini sheria inataka miaka 25 kwa migodi mikubwa. Hii si sahihi na ni kinyume cha sera," alisema Sendeka ambaye anatoka katika jimbo lenye mgodi wa madini pekee duniani wa Tanzanite, ulioko mkoani Manyara.
Ukurasa wa 18, sehemu 5.7 kitabu hicho cha muswada inazungumzia maendeleo ya madini ya vito, ambako msingi mkuu wa sehemu hiyo unatajwa kuwa ni kuwawezesha Watanzania kushiriki katika uchimbaji wa madini ya vito. Katika sehemu ya policy statement kuhusu sehemu hiyo kipengele cha ii kinasema; "Serikali itahakikisha uchimbaji mkubwa wa madini ya vito unakuwa mikononi mwa Watanzania kwa asilimia isiyopungua 50."
Kwa maoni yake, Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Wilbroad Slaa hali hii ya Waziri Ngeleja kuwasilisha muswada wenye vipengele vinavyopingana na sera aliyotoa takriban miezi minane tu, bila watendaji wa wizara hiyo kubaini kasoro hiyo na kisha Baraza la Mawaziri kujadili muswada huo bila kubaini kasoro na hatimaye Waziri Wasira kukosoa, ikizingatiwa kuwa ni mjumbe wa Baraza la Mawaziri, ni dalili za ufalme uliogawanyika.
"Hii inathibitisha kuwa masuala mengi (yakiwamo ya sera) yanabaki kuwa ya kisiasa zaidi kuliko utekelezaji unaozingatia maslahi ya nchi. Kwanza , wadau wamezungumza na imebainika kuwa hawajapata muda wa kutosha kujadili muswada huu, ambao maswali ni mengi zaidi kwa kuwa umeletwa kwa hati ya dharura, upitishwe bungeni kumbe unapingana hata na sera waliyotunga wenyewe," alisema Dk. Slaa katika mahojiano na Raia Mwema.
Dk. Slaa aliunganisha tukio hilo la mawaziri kupishana na mmoja wao kuwasilisha muswada unaotofautiana na sera, na tukio la hivi karibuni la Rais Jakaya Kikwete, ambaye ni Mwenyekiti wa CCM, kumteua Husna Mwilima aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake wa CCM aliyefukuzwa kwa hoja kuwa ni mtendaji asiye na uwezo kikazi, hoja iliyoshangiliwa na Mwenyekiti wa Umoja huo, Sofia Simba, ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utawala Bora ni mkanganyiko mwingine na dalili ya ufalme uliogawanyika.
Raia Mwema ilizungumza na Waziri Marmo katika viwanja vya Bunge mjini Dodoma kuhusu masuala mawili ya msingi. Kwanza ni kutaka kujua kama muswada huo ulijadiliwa kwenye Baraza la Mawaziri, lakini pili azungumzie mkanganyiko huo kwa kuhusisha umakini wa Baraza hilo la Mawaziri katika kuchambua masuala ya nchi. Mazungumzo hayo yalikuwa hivi:
Raia Mwema: Waziri huu Muswada wa Sheria ya Madini wa mwaka 2010, pamoja na ule wa Sheria ya Mifugo wa Waziri Dk. John Magufuli ambao ulikataliwa bungeni, yote ilipitia mchakato wa kujadiliwa katika Baraza la Mawaziri?
Waziri Marmo: Ooh! hiyo sawa, yote ilijadiliwa kwa kina katika Baraza la Mawaziri.
Raia Mwema: Kuna mambo mawili yamejitokeza. Kwanza, muswada umebeba vipengele tofauti na matakwa ya sera ya madini, pili, mawaziri licha ya kuwa na fursa ya kujadili, wametofautiana hadharani mbele ya wadau na kwa kawaida, kikao cha Baraza la Mawaziri kinaongozwa na Rais au Makamu kama Rais hayupo, au hata Waziri Mkuu kama wote wawili hawapo. Unazungumziaji umakini wenu na mgongano wa mawaziri?
Waziri Marmo: Mhh! Hiyo hapana bwana, siwezi kuzungumzia…achana na mambo hayo.
Mbali na Wasira, muswada huo pia ulipingwa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige ambaye hata hivyo haingii kwenye Baraza la Mawaziri. Wanaoingia kwenye vikao vya baraza hilo ni mawaziri pekee.
Pamoja na viongozi hao, wadau wengine pia walipinga muswada huo, wengi wakitaka kutoundwa kwa chombo cha ushauri wa masuala ya madini kama inavyopendekezwa na muswada huo na badala yake, iundwe mamlaka ya madini, itakayokuwa na jukumu la kusimamia sekta yote ya madini huku ikiwa huru nje ya minyororo ya Serikali.
Katika mkutano huu wa Bunge, Waziri mwingine aliyeonja ‘kibano' kutokana na kutojiandaa kwa kuzingatia matakwa ya wadau ni Magufuli ambaye alilazimika ‘kuchomoa' muswada wake bungeni baada ya wabunge kuujadili kwa hoja kali, zenye tafsiri kuwa muswada huo utakwenda kinyume cha maslahi ya wafugaji na Taifa kwa ujumla.
Baada ya kuchomoa muswada huo, Magufuli alilazimika kufanya semina kwa kuwashirikisha wadau ili kuwasilikiza upya na kuingiza mapendekezo yao . Semina hiyo ilifanyika siku moja na ile ya Nishati ya Madini kuzungumzia muswada wake wa sheria ya madini wa mwaka 2010.
Lakini hali kama hiyo pia iliwahi kumpata Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utawala Bora, Sofia Simba, ambaye katika mkutano wa uliopita wa Bunge, mkutano wa 18, aliwasilisha Muswada wa Sheria ya Usalama wa Taifa, ambao ulipingwa na wabunge wengi, wakiwamo wabunge waandamizi wa CCM kama John Malecela. Simba alichomoa muswada wake na kwenda kujiandaa upya.