Mrema umekua msemaji wa Kikwete?
Irene Mark
NAAMINI Augustino Lyatonga Mrema, Mwenyekiti Taifa wa Tanzania Labour Party (TLP), ameamua kuwa msemaji asiye rasmi wa Rais Jakaya Kikwete kutokana na sababu za siri anazozijua mwenyewe.
Ndiyo maana kwa siku za hivi karibuni, ameamua kujipa madaraka ya usemaji wa rais japokuwa anakanusha hadharani tena kwa msisitizo, jambo linalonifanya niamini kwamba dhamira yake inamsuta kwa kujitwika msalaba wa Kurugenzi ya Mawasiliano ya Ikulu na kuendelea kunishawishi kwamba anachokifanya si kingine bali ni ‘kumsafisha' Kikwete na kujijengea mazingira bora zaidi ya kisiasa.
Ukweli ni kwamba, hivi sasa Mrema huyu hauziki. Amepauka kisiasa ndiyo maana anatafuta pa kutokea. Anahisi amepata lakini hali halisi iko wazi, amekalia kuti kavu ndani ya chama anachokitawala cha Tanzania Labour (TLP).
Kwa kauli yake hadharani, Mrema anasema, "Sijaingia katika mtandao wa serikali, nimezungumza hayo leo kama mwananchi mzalendo, kwani kuna ubaya gani kusema hayo? Mtendeeni haki Rais Kikwete jamani."
Ni kweli kama anavyosema kwamba hajaingia kwenye mtandao wa serikali kwa sababu hakubaliki huko na yeye anafahamu hilo. Mrema anaishawishi jamii kumtendea haki Kikwete, anasahau kwamba hata kukosolewa pia ni haki tena iliyoainishwa kikatiba?
Mrema ameingia kwenye mtandao binafsi wa Kikwete na wapambe wake ambao wako tayari kwa lolote kuhakikisha sifa mbaya na nzuri za Kikwete zinapata mapokeo chanya machoni pa jamii.
Hapa kuna mambo mawili, kwanza ni Kikwete kama mtu binafsi, anasimama kwa kuwa ndiye mgombea uras kwa tiketi ya CCM kwenye uchaguzi mkuu ujao na huko ndiko tuendako.
Pili, serikali ni ile inayomtambua rais kama mkuu wa taasisi muhimu kwa ustawi wa taifa bora lenye mkusanyiko wa watendaji wakiwemo usalama wa taifa, jeshi, polisi na idara nyingine.
Wachambuzi makini wa siasa, wanashtushwa na kauli hiyo ya Mrema aliyekuwa mwiba mkali kwa wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na watawala wa serikali inayotokana na chama hicho katikati ya miaka ya 1990 hasa baada ya kuingia rasmi kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini.
Mrema huyu ambaye ni mwenyekiti wa taifa wa TLP alianza kampeni za kujikita kwenye kundi la utetezi wiki chache zilizopita alipokaririwa akisema utendaji wa Kikwete (hakusema serikali) kwa kipindi cha miaka minne, umekua bora sana hasa katika mapambano dhidi ya ufisadi.
Kwa Mrema, hii ina maana kwamba Kikwete anaweza bila urais alionao sasa. Kwangu si kweli, ndiyo maana alishindwa kupambana nao alipokuwa Waziri wa Mambo ya Nje kwa miaka 10 mfululizo kwa sababu mafisadi wa leo, hawajazuka tu, wameanzia mahali ambapo Kikwete anapafahamu.
Siku moja baada ya mnajimu, Sheikh Yahya Hussein, kutumbukia kwenye mtego huo kwa lengo la kubadili mwelekeo wa wananchi kuhusu utawala wa Serikali ya Awamu ya Nne inayoongozwa na Kikwete, Mrema alinukuliwa akiushabikia utabiri na kuwaonya wanasiasa wengine kutafuta kazi za kufanya kipindi hiki ili kumpisha Kikwete amalizie muda uliobaki.
Sheikh Yahya aliwaogopesha watu kwamba atakayempinga Kikwete, atakufa ghafla. Mrema akaunga mkono kwa asilimia 100 kisha akawashauri wale wanaofikiria kuwania urais kwenye uchaguzi ujao kuacha kiherehere.
Wote tunafahamu kwamba kifo kipo na kila mwenye pumzi lazima atakufa. Lini, wapi na kwa sababu gani, hilo ni fumbo kutoka kwa Mungu. Lakini sheria za nchi haziruhusu mtu kumwambia mwingine atakufa. Huko ni kutishana kusikostahili.
Yote yaliyosemwa na Sheikh Yahya, vyombo vya usalama wa taifa na polisi vimenyamaza kimya. Hivi leo, mnajimu huyo angeamua kusema Kikwete atakufa, sina hakika kama angeendelea kulala usingizi mnono nyumbani kwake. Angekamatwa na sheria ingechukua mkondo wake.
Sasa uko wapi usawa kwa raia wote. Wale wanaotaka kutumia haki zao kama John Shibuda kugombea urais wanatishiwa kifo na hakuna anayewatetea, halafu tunajinasib kwamba tunaongozwa kwa utawala wa sheria. Si kweli.
Kwangu, Sheikh Yahya anastahili kukamatwa na kufunguliwa mashtaka ya jinai kwa kutishia kuua kwa maneno. Mshtakiwa wa pili kwenye kesi hiyo ni Mrema. Adhabu yao ni kifungo kisichozidi miezi 12; faini ama vyote kwa pamoja.
Hivi, ni kipi hasa kinachomsukuma Mrema kujitwika majukumu mazito ya ‘upambe' kwa Kikwete wakati huu wa kuelekea kwenye uchaguzi ilhali mambo si shwari ndani ya chama chake? Kwa nini asitumie nguvu hizo kuwahutubia wana wa Vunjo anaotarajia kuwaomba ridhaa ya kuwawakilisha?
Binafsi, hoja za Mrema katika kujenga utetezi dhidi ya Kikwete ni dhaifu. Hazina mashiko wala ushawishi kwa jamii. Namshauri ajipange kwa ajili ya kampeni zijazo ili ajiweke kwenye nafasi nzuri ya kuwa mbunge wa Vunjo kwa mara nyingine kuliko kupoteza muda kumtetea mwenyekiti wa CCM taifa. Naamini kwamba wananchi ambao ndiyo wenye maamuzi makubwa, wana uwezo wa kumpima Kikwete mwenyewe, iwapo amefanikiwa ama la, si Mrema wala Shekhe Yahaya.