Bishop leo it's your day ukipata mda tutupie episode za kutosha tusherehekee birthday [emoji847]
Umesikika
Shunie wangu, ngoja niongeze episodes 2...
Kizungumkuti! - 62
Na Bishop Hiluka
ASP Komba alijilaumu sana kwa kushindwa kumpata Joram Mbezi akiwa hai kwani aliamini kuwa Joram ndiye alikuwa kiungo kikubwa kati ya mtu aliyejiita Belinda Jackson na Yusuf na sasa kazi ilianza kuwa ngumu pasipo Joram.
Alikuwa amebakiwa na kazi moja tu, kumbana Yusuf ili amweleze uhusiano wake na wale watu wawili, Joram Mbezi ambaye sasa alikuwa marehemu na Belinda Jackson, ambaye hawakuwa na taarifa zake hadi muda huo. Alipaswa kupata majibu ya uchunguzi wake haraka iwezekanavyo.
Endelea...
ASP Komba alionekana kuchoka sana asubuhi ile alikumbuka kuwa baada ya kurudi tu ofisini mkuu wake wa kazi, Kamanda wa Polisi wa kanda maalumu alimuuliza, “Unadhani kuna haja ya kukuongezea mtu mwingine katika kazi hii?”
“Hapana, afande! Naamini sisi wawili tunatosha. Nikihitaji msaada, nitakujulisha,” ASP Komba alijibu.
Picha ya maiti ya Joram Mbezi iliyokuwa imefumuliwa kichwani iliendelea kumjia ASP Komba akilini mwake, baada ya uchunguzi wa mwili wa Joram Mbezi waliwahoji takriban watu watano, wakiwamo wale watoto wawili waliopewa madafu katika eneo la tukio.
Watu hao watano, watatu wakiwa watu wazima ambao kati yao mmoja alikuwa mwanamume na wawili wanawake, walichukuliwa hadi kituo cha polisi na kuhojiwa na ASP Komba, wote walieleza kuwa walimwona muuza madafu kwa mbali na wala hawakumtilia maanani, hivyo wasingeweza kumtambua endapo wangemuona tena.
Ila wale watoto waliopewa madafu walikiri kumwona kwa ukaribu yule muuza madafu akitumia bastola. Walieleza kuwa waliitambua bastola kwa kuwa waliwahi kuona zikitumika kwenye sinema walizoziangalia kwenye mabanda ya video.
Baada ya mahojiano, wale watu wazima watatu, isipokuwa wale watoto, waliachiwa. ASP Komba na Sajenti Mapambano wakabaki peke yao na wale watoto.
ASP Komba aliwatazama kwa macho ya upole wale watoto. Aliamini kuwa ilikuwa ni mara yao ya kwanza kushuhudia mauaji na kufikishwa kituo cha polisi kutoa maelezo. ASP Komba alikumbuka kuwa pamoja na mambo mengi aliyowauliza wale watoto lakini alitaka kujua kama wangeweza kumtambua yule mtu aliyewapa madafu endapo wangemuona kwenye picha.
“Mkimwona tena yule baba aliyekupeni madafu mtaweza kumtambua?” ASP Komba aliwauliza wale watoto.
“Sura yake?” aliuliza mtoto mmoja aliyeonekana mjanja zaidi.
”Ndiyo, sura yake”
“Naweza,” yule mtoto alijibu pasipo hata kufikiria mara mbili.
“Hata ukimuona kwenye picha?” ASP Komba alimuuliza kwa upole huku akimkazia macho.
“Ntamjua.”
ASP Komba aliinuka akafungua kabati moja la chuma lililokuwa ukutani na kuvuta droo iliyokuwa ndani yake upande wa kulia, akatoa faili lililokuwa na picha kadhaa za wahalifu, akawawekea mbele wale watoto.
“Angalieni vizuri kama picha ya huyo mtu imo humo. Msifanye haraka,” ASP Komba aliwaeleza kwa sauti ya upole.
Pamoja na kuchukua muda mrefu kufunua na kuziangalia zile picha kwa utulivu mkubwa, wakipitia kila moja kwa msaada lakini hawakuweza kumuona mtu waliyekuwa wakimtafuta. Jambo lile likazidi kumuumiza ASP Komba.
* * * * *
“
I killed Kisu, he had to die…” (Nimemuua Kisu, alipaswa kufa…) maneno ya Carlos ambayo bado yaliendelea kupita kichwani mwa Jacky na kumsumbua. Baada ya kuambiwa maneno yale Jacky hakusema lolote, alijiondosha pole pole pale alipokuwa amesimama akaketi juu ya sofa.
Uso wake ulionesha mchanganyiko wa huzuni na hasira. Alimtazama Carlos huku akipumua kwa nguvu. Carlos alimtazama Jacky kwa mshangao, akapitisha ulimi wake chini ya midomo yake. Hakuweza kuelewa mara moja ni kipi kilichomkera Jacky.
Carlos alimsogelea Jacky, akaketi karibu yake huku akimtulizia macho yake usoni akimtazama kwa makini.
“
Why you look so serious?” (Vipi, mbona unaonekana hivyo?) Carlos alimuuliza Jacky huku akiendelea kumkazia macho.
Jacky alimtazama Carlos, akashusha pumzi ndefu za ndani kwa ndani, “
There was no reason to kill Kisu,” (Hapakuwa na sababu ya kumuua Kisu) alisema, uso wake akiwa kaukunja, kisha akaongeza, “
We agreed to bring him here, give him his share and then let him leave the country,” (Tulikubaliana kuwa umlete hapa, umkatie chake kisha atoroke nchi).
Carlos alitazama kando akaonekana akiwaza kwa kitambo kifupi kisha akayarudisha macho kwa Jacky, “
So, is this what makes you so distressed?” (Kwa hiyo, ndicho kinachokukera sana?)
“Kwani wewe hakikukeri?” Jacky alimuuliza huku aakimtulizia macho.
“Kinikere kwa vipi? Carlos aliongea kwa sauti iliyoanza kuonesha dalili za hasira. “Si alikuwa akisakwa na polisi kwa udi na uvumba, na ilibaki kidogo tu wangemtia mbaroni, sasa weweulitakaje?”
Jacky alibaki kimya akimtazama Carlos kwa makini, kisha alitazama kando, akashusha pumzi za ndani kwa ndani.
“
I don't understand, what are you trying to tell me, Jacky?” (Sijaelewa, unajaribu kuniambia nini, Jacky?) Carlos alimuuliza Jacky huku akimkazia macho yaliyokuwa yanawaka kwa hasira.
“
Listen, Carlos. We have everything that man has to have that can buy anything, I didn't see a reason to start killing people who helped us!” (Sikiliza, Carlos. Tuna kila kitu ambacho binadamu anatakiwa kuna nacho ambacho kinaweza kununua chochote, sikuona sababu ya kuanza kufanya mauaji kwa watu waliotusaidia!) Jacky alisema huku akiminya midomo yake.
Carlos aliachia tabasamu la mbali, akatingisha kichwa taratibu, “Jacky,” alisema kwa sauti ya upole. “Hivi tangu lini mwenzangu umeanza kuwa mlokole?”
“Nani mlokole?” Jacky alimuuliza Carlos huku akitoa macho. “Yaani mimi niwe mlokole,
are you kidding?”
“Kama si mlokole basi ni nini hiki unachomaanisha?” Carlos alisema huku akimkazia macho Jacky.
”Basi tuyaache hayo, tayari yameshatokea na hakuna namna ya kumrudishia Kisu uhai wake,” Jacky alisema huku akiinuka pale kwenye sofa. Akaingia jikoni. Carlos alimsindikiza kwa macho kisha akainuka na kutoka nje.
Baada ya kuandaa kifungua kinywa, Jacky alitoka na kuelekea sebuleni, hakumkuta Carlos, akaanza kuita akidhani labda Carlos alikuwa chumbani, kimya. Akaamua kuchukua simu yake na kumpigia simu lakini simu ilikuwa inaongea na simu nyingine na baada ya muda alipokea ujumbe mfupi, “
Nimetoka kidogo, nitarudi baada ya nusu saa…”
Saa tano asubuhi Jacky alikuwa amejipumzisha kwenye kochi kubwa la sofa pale sebuleni, hadi muda huo Carlos hakuwepo nyumbani. Jacky hakuwa na furaha kabisa kama alivyozoea siku zote, alijikuta akiwa na mawazo mengi yaliyokuwa yakizunguka kichwani kwake kiasi cha kutaka kumtia wendawazimu.
Jacky alikwisha anza kuchoshwa aina ile ya maisha waliyokuwa wakiyaishi yeye na mumewe Carlos, alijiona ni mtu mwenye hatia kuishi maisha kama yale, ya kuuza utu wake na hata kuhatarisha maisha kwa sababu ya kutaka kuendelea kupata mabilioni ya fedha.
Alianza kujishangaa, kwa nini aendelee kuishi maisha ya uhalifu wakati tayari walikuwa na fedha nyingi za kutosha kufanya chochote na hata kuishi nchi yoyote!
Nyumba waliyokuwa wakiishi lilikuwa kasri lililokuwa na thamani kubwa ya zaidi ya mabilioni ya fedha na walikuwa na nyumba nyingine tatu jijini Dar es Salaam, zenye thamani ya mabilioni ya fedha na miradi kadhaa iliyokuwa ikiwaingizia fedha nyingi, japo hazikufikia mabilioni. Pia walikuwa na magari kadhaa ya kifahari.
Kila alipofikiria mambo aliyokwisha yafanya na wanaume kadhaa kwa maelekezo ya mume wake Carlos, alianza kuona kinyaa na kujiona mjinga kukubali kutumika kama chambo cha kuingiza mabilioni ya fedha. Alishusha pumzi ndefu za ndani kwa ndani huku akihisi thamani ya utu wake ilikwisha toweka siku nyingi na sasa alikuwa akiishi maisha ya majonzi!
Itaendelea...