STORY : MPAKA KIELEWEKE
MTUNZI : NIRA SAIRE
SEHEMU YA KUMI
Ilipoishia...
Nikatoroka na kuelekea nyumbani ambapo nilijilaza na kumngojea Mnaro kwakuwa sikua hata nikijua namna ya kumpata, ulikuwa ni lazima aje yeye kama ulivyo utaratibu wetu siku zote.
Niliendelea kujilaza pale mpaka usingizi ukanipitia ambapo nilikuja kushtuka mlango wa chumba changu ukigongwa. Nilikurupuka na kuangalia saa ya ukutani pale chumbani ambayo ilionesha kuwa ilikuwa saa mbili na dakika kumi asubuhi.. "khaaaaaa" nili hamaki sana baada ya kugundua kulikuwa kumekucha bila kurudi mahabusu.
Endelea....
Nilikurupuka nikaenda moja kwa moja na kufungua mlango. Alikuwa ni baba akiniamsha na kunipa taarifa juu ya mama yangu kuumwa, alisema mama alikuwa amelazwa akiwa na hali mbaya sana. Tukakubaliana kuwa yeye aondoke kwenda kumuuguza mama huku akiniacha mimi nikiendelea na jukumu la kumtafuta mke wangu, baba akaondoka.
Nilibaki pale ndani nikijiuliza cha kufanya juu ya kutoroka kwangu mahabusu, mpaka sasa lazima watakuwa wamegundu kutokuwepo kwangu, lazima watakuwa wameshangazwa na jambo lile kwa maana niliondoka nikiacha chumba kile cha mahabusu kikiwa kimefungwa kama ambavyo walikiacha. Je nirudi mahabusu? Lakini nitawaeleza nini iwapo watanikuta mule ndani wakati wamegundua tayari kuwa sikuwepo?
Au niache tu kwenda? Hili pia ni jambo gumu kwa maana nilitoa maelezo yote kunihusu mimi, tena kwa usahihi kabisa, hivyo wana uwezo wa kunipata iwapo watanihitaji.. niliendelea kujiuliza maswali mwisho nikaamua kutoenda mahabusu, liwalo na liwe kwanza serikali haiutambuwi uchawi, niliwaza.
Nilipumzika pale nyumbani mpaka majira ya saa tano asubuhi kisha nikaamua kwenda benki nikatoe pesa kwa maana nilikuwa karibu kuishiwa.
Nikatoka na kwenda benki, nikachukua pesa na kisha kuamua kuingia kazini angalau nikawaone watu wangu kwa maana sasa ulikaribia mwezi toka niombe likizo ile ya bila malipo.
Nilifika kazini nikakutana na wafanyakazi wenzangu, tukaongea mengi huku wengi wakinipa pole na kunitaka nirundi kazini. Kwa muda ule mfupi wa kuongea na wafanyakazi wenzangu nilijikuta nikipata ari ya kufanya kazi. Ninaweza kufanya kazi na mambo mengine yakaendelea, isitoshe mchana nakuwa bila kazi kwa maana mambo mengine hufanyika usiku, niliwaza na kufikia maamuzi kuwa nirudi kazini.
Nikaamua kwenda kwenye ofisi ya mkuu wa kitengo ili kuzungumza naye juu ya kurudi kwangu kazini. Tukaongea na kukubaliana, kisha nikabaki tukiongea mengine kuhusu maisha kwani alikuwa rafiki yangu pia. Tulipomaliza maongezi nikatoka nikikusudia kwenda nyumbani lakini secretary wa mkuu wa kitengo akanipa taarifa "kaka Abuu, kuna wageni wako mapokezi" wageni wangu mapokezi? nani anaweza kuwa mgeni wangu ikiwa sikuwepo kazini kwa muda wote huu?, nilijiuliza huku nikielekea mapokezi kuonana na hao wageni wangu.
Sasa nilikuwa nikiutizama mlango wa mapokezi lakini kabla sijaingia ndani akili ikaniambia nimeingia mtegoni, nilipokamatwa na polisi niliwapa maelezo yote kunihusu ikiwa ni pamoja na mahala pangu pa kazi, kivyovyote baada ya kutoroka sehemu ya kwanza kutafutwa ingekuwa hapa kazini kwakuwa hawana taarifa kuwa sipo kazini.
Baada ya kupata wazo hilo nikaamua kugeuka haraka ili kutoka nnje ya ofisi lakini nilikutana na askari polisi akiwa ndani ya sare "bwana Abubakar Saire uko chini ya ulinzi" niliishiwa nguvu, mwili ukanyong`onyea na kujuhisi kama sina uzito. Askari yule akaja na kunitaka kumpatia mikono yangu kisha akanifunga pingu na kuwaita wenzake kwa simu nao wakaja kutokea mapokezi, safari ya kuelekea kituoni ikaanza huku wafanyakazi wenzangu wakibaki wamepigwa na butwaa wasielewe nimefanya kosa gani la kuwindwa na polisi.
Tulifika kituoni nikaingizwa mahabusu, lakini kilikuwa ni chumba tofauti na kile ambacho niliingizwa mwanzo.
Nilitamani sana kutoroka mule mahabusu ila nilishindwa kutoka kutokana na kutokuwa na vijiti vile ambavyo vingeniwezesha kupenya kichawi.
Nikakaa humo kwa nusu saa kisha wakaja askari watatu na kuanza kunihoji, askari wale walikuwa wakiamini kuwa kutoroka kwangu kituoni pale kulitokana na kusaidiwa na askari mmojawapo mule ndani na walikuwa wakitaka kumjua askari huyo "bwana, sisi unachotaka kujua ni kimoja tu, nani alikusaidia kutoka mahabusu na si kingine chochote" alisema askari mmoja ambaye alikuwa akizungumza lafudhi ya Kihaya na alionekana mwenye roho ya kikatili.
Kwa haraka haraka sikuwa na jibu la kutoa nikabaki nikiwaangalia tu kitendo ambacho walikitafsiri kama dharau. "Tumewahi kukutana na wajeuri kuliko wewe lakini walitii bila kupenda, hakuna ambaye huingia humu akaacha kutupa habari ambazo tunazitaka" alisema askari yule Muhaya akionekana amekasirika, "kwanini mpaka uumizwe? Bora useme mapema tu kwa maana kusema lazima utasema" aliongea askari mwingine lakini bado niliendelea kuwa kimya, niwajibu nini sasa? Kuwa nilitoroka kichawi? Kwanza hawawezi kuniamini, niliwaza.
Ghafla nilizabwa kofi kali la shavuni na yule askari ambaye hakuwa ameongea chochote toka ameingia mule ndani, lilikuwa kofi zito kiasi kwamba sikuamini kuwa lilitoka kwa askari yule ambaye nilimuona kuwa alikuwa mpole kuliko wale wengine, ama kweli umdhaniae ndie kumbe siye. Damu zilikuwa zikinitoka puani kutokana na kofi lile ambalo lilinifanya pia Nikapatwa na kizunguzungu cha hali ya juu. "Uko tayari kusema ama show iendelee?" Aliuliza askari yule ambaye aliyenizaba kofi ambaye alikuwa ni mdogo wangu kiumri, lakini kwa mara nyingine nilikuwa kimya akanizaba kofi lingine kali mpaka nihisi harufu ya damu kisha akanibaki akinikazia macho kama ambaye anangoja nitoe majibu lakini sikuwa na chakusema, nikamuona akinyanyua mkono wake ili kuninasa kibao kingine nikasimama na haraka huku nikikinga mikono kuzuia kofi lile zito ambalo lilitua juu ya mikono yangu.. askari wale wote watatu wakanikabili kunidhibiti kila mmoja akipiga alipopaona mpaka nikaanguka chini.
Askari mmoja akatoka na kurudi mara moja akiwa amebeba kiti cha mbao na kamba, wakaninyanyua na kunikalisha kitini kisha wakanifunga wakinishikanisha vyema na kiti kile kutia mikono yangu ambayo ilizungushwa nyuma ya kiti na kukazwa na kamba vizuri kisha miguu nayo ikafungiwa viziri kwenye miguu ya mbele ya kiti kile.
"Tunakuuliza kwa mara ya mwisho, nani alikutorosha kituoni jana" aliongea askari ambaye sasa nilimgundua kuwa alikuwa miongoni mwa wale ambao walinikamata usiku na kunileta pale kituoni kabla sijatoroka kichawi..
Nilitamani kujieleza ili adhabu ile iondoke lakini nini niseme ndio tatizo ambalo sikujua kulitatua.
"Endelea afande" alizungumza askari aliyenifunga kamba baada ya kuona sitoi maelezo na askari yule mtaalamu wa kupiga makofi akanisogelea tayari kwa muendelezo wa adhabu ile..
"NGOJENI JAMANI NASEMAAA" nilijikuta nikisema kwa sauti kubwa yenye hofu ndani yake.. "kusema tunajua utasema tu unataka ama hutaki" alisema askari yule mdogo lakini katili huku akinizaba kofi lingine zito nikajihisi kuchanganyikiwa.. "haya sema sasa" aliamuru askari mwingine, wakati huu damu zilikuwa zinazidi kutoka puani, na mdomo wangu wa chini ulikuwa umevimba kutokana na kupatwa na kofi mojawapo, lakini nilijikaza nikaanza kujieleza harakaharaka kabla askari yule asiyerudi nyuma akiamua kupiga hajaamua tena.. "jamani mimi nilitoroka kichawi, nilipenya kwenye ukuta" nilijieleza lakini kama ambavyo nilitegemea askari wale hawakuniamini, waliangalian, wakacheka kisha wakanirudia "wewe ni mchawi? toroka sasa uende" alisema askari mmoja kimzaha huku wenzake wakicheka.
Askari wale waliona kama nimepania kutomtaja ambaye alinitorosha hivyo wakaamua kunining`niniza kweye kamba ambayo iliifunga mikono yangu ikiiunganisha pamoja na kisha askari yule mpenda kupiga akawa ananishindilia ngumi nzito za tumbo huku akisema mchezo ule ungesita iwapo nitawaeleza nilitorokaje mahabusu..
"Kama hutomtaja ambaye alikusaidia kutoka mahabusu utakufa kwa adhabu humu ndani" alisema askari ambaye alionekana yeye ndiye mwenye kuagiza wenzake lakini yeye hakuwa akifanya chochote zaidi ya kuongea.
"Kwanini unaacha niteseke ikiwa unajua ni wewe ambaye ulinitorosha, nirudishie pesa zangu basi" niliropoka kumwambia askari yule akabaki mdomo wazi huku askiri aliyekuwa akinipiga akisitisha zoezi ya kumgeukia askari mwenzao, wakawa wanamtazama bila kusema neno naye akagutuka na kutaka kuniamia lakini wenzie walimdhibiti wakamtoa mule chumbani.. "kumbe tunapoteza muda ikiwa unajua ulichokifanya" alisema askari yule aliyekuwa akinipiga wakati wakimvutia nnje askari mwenzao ambaye nilimvika kesi isiyomuhusu ili mimi nipumzike na kipigo kile.
Nikabaki pekeyangu kwenye chumba kile ambacho niligundua kuwa kilikuwa cha mateso, huku nikiwa nimening`inizwa kwa kamba nikiwa na maumivu makali.
Nikawa nikiwaza juu ya hatma yangu, nilitamani kutoroka lakini sikuwa na vifaa, Mnaro pia sikuwa nimemuona toka nipatwe na matatizo yale ya polisi na sikujua kama alikuwa anajua kama nilikuwa polisi. Mipango ya kumkomboa mke wangu itafanikiwaje kwa mimi kiwemo mule ndani, na roho iliniuma sana na nikauchukia uchawi kwakua haukua na chakunisaidia.
Baada ya kama dakika ishirini aliingia askari yule mwenye lafudhi ya Kihaya akanifungua na kunihamishia kwenye chumba kile cha mahabusu ambacho nilitoroka. "Tulikuwa tunajua yule bwana ndiye ambaye atakuwa amekutorosha, hatukua na ishahidi tu, ila hakuna askari mwingine angeweza kufanya kitu cha aina hiyo hapa" alisema askari yule akinibwaga chini, nikagumia kwa maumivu ya tumbo.. "ungetueleza haraka wala yasingekupata hayo, sisi tulikuwa tunamtaka mpumbavu huyu ambaye anataka kututia matatizoni kwaajili ya tamaa zake, alisema askari yule huku akiondoka..
"Sasa nini hatma yangu afande?" Nilimuuliza polisi yule naye akajibu "tunawapeleka mahakamani kesho, wewe ni mshtakiwa namba moja na huyo mwenzio ni mshtakiwa namba 2" alisema askari yule akatoka nnje na kuniacha nikimuonea huruma polisi yule ambaye nimemsababishia matatizo.. lakini sikuwa na jambo la kufanya zaidi ya lile, pengine mpaka sasa ningekuwa bado napigwa. Niliwaza.
Mida ya saa 8 wafanyakazi wenzangu wawili walikuja kiniona wakaniletea na chakula. Walijaribu kuniwekea dhamana nitoke ila ikashindikana, ikanibidi kulala pale bila mpango wowote juu ya kutoka kwangu.
Asubuhi tulipelekwa mahakamani nikiwa na askari yule ambaye nilimvika kesi, tukasomewa kesi ya kujaribu kutoroka nguvuni mwa polisi, tukakana shtaka..
Nilishangaa kukuta hakimu aliyekuwa akisikiliza kesi yetu akiwa yule bwana ambaye alinijia nyumbani akiwa amempoteza binti yake na kuniachia business card.
Baada ya kukana shtaka tukapelekwa kwenye mahabusu ya gereza kuu huku tukipangiwa kesi ile kusikilizwa tena baada ya wiki mbili.
Niliyaona maisha ya jela yakiwa magumu ndani ya siku moja tu. Nilikuwa nimekaa muda mrefu, tena chini mpaka makalio yakawa yanauma sambamba na maumivu ya kipigo cha kule polisi hali ikawa mbaya. Nilijiona wazi wazi kuwa siyawezi maisha ya mule gerezani.. wiki mbili za kuwemo mule mpaka siku ya kusomwa tena kesi nilianza kuziona kama mwaka mzima.
"Abubakar Saireee, kuna mgeni wakooo" ilikuwa ni sauti ya askari ikinishtua kutoka katikati ya dimbwi kubwa la mawazo. Nikasimama na kumfuata askari yule..
Usikose sehemu ya 11
Kwa maswali, maoni au ushauri. Unaweza kunipata kupitia:
+255653686008
nirasaire@gmail.com