STORY: MPAKA KIELEWEKE
MTUNZI: NIRA SIARE
SEHEMU YA TANO
Ilipoishia....
“niko mbali sana na hapo mlipo, ingawa naweza kuwaona na kuituma sauti yangu mpaka hapo mlipo” iliongea sauti ile nami nikapata shauku ya kujua jambo nikauliza “unaweza kuona na kupeleka sauti mpaka Muifufu?” nikajibiwa “ndio ninao uwezo huo ingawa huwa naishia kuangalia nini kinaendelea huko Muifufu lakini huwa situmi sauti kwa maana huwa sitaki baba yangu ajue kama huwa naona kinachoendelea huko na kwa kutuma sauti atajua mara moja. “tafadhali niangalizie kama mke wangu yuko salama huko” nilijikuta nimetoa ombi na sauti ikanijibu “nadhani ingekuwa bora uangalie na umuone mwenyewe”.....
Endelea....
“Nitashukuru sana kama utanisaidia kwa hilo” nilijibu huku sauti yangu ikionyesha waziwazi kiherehere cha kutaka jambo hilo litokee haraka. “kifaa kinachoniwezesha kutekeleza jambo hilo kiko hapa kwangu na hakiwezi kutoka hapa, itakubidi uje huku ili uweze kuona” ilielezea sauti ya mzee yule nami nikamjibu “haina shida mzee, nielekeze nije sasa hivi” ... “huwezi kufika kwangu mpaka mimi nikulete, nitakuja kukuchukua usiku kama kweli uko tayari” ilisema ile sauti nami nikakerwa kidogo na tabia ile ya kutaka kila jambo lichelewe kutendwa, nikajikuta nimeuliza kwa mara nyingine “kwani hauwezi kuja kunichukua asubuhi hii nikaja huko?” sauti ile ikatulia kwa muda kisha ikanijibu “kua mchawi kunataka subira, kuna mambo mengi ya kuyafanya kwa upole na ukiwa na haraka kama hii yako utajikuta umepoteza kila kitu, kama kweli unataka kuwa mchawi jifunze hilo” hapo nikakumbuka tena kuwa napaswa kua mchawi, jambo ambalo hata sijui litafanikishwaje. “kwanini ni lazima awe mchawi ila kutekeleza haya majukumu?” safari hii ni baba ambaye aliuliza.. “kwa sababu bila ya kua mchawi hatoweza kufanya chochote ndani ya Muifufu, atakuwa anajipeleka kuuawa tu. Ili kufanikiwa anapaswa kuwa mchawi, tena mchawi hasa ili aweze kushindana na wachawi wa huko wenye uwezo mkubwa mno” baba akauliza tena “ wewe ni mchawi tayari, kwanini usitusaidie tu mara moja kwa hili?” sauti ile ikajibu, tena ilionesha kukasirshwa kama sio kuchoshwa na maswali yale.. “naona kama tunarudi nyuma kila baada ya kupiga hatua moja, kua mchawi sio jambo kubwa kama ambavyo ninyi mnaliona! Ni swala la kujua tu mbinu na kuzitumia, sio lazima uanze kuua au kuwangia watu, kila mtu anaamua jinsi ya kuutumia ujuzi anaoupata!. Ndio maana nikasema nakuachia siku nzima ya leo kisha kesho utafanya maamuzi” sauti ile ilitulia nasi tukawa kimya, baadae nikavunja ukimya “mimi niko tayari mzee, wala haina haja ya kungoja kesho ili nifanye maamuzi” sauti ile ikacheka kisa ikasema “tumerudi nyuma tena, jifunze kuwa na subira kama kweli unataka kuwa mchawi, tutaonana usiku” kisha kimya kikatawala.
Tulibaki pale tukiwa tumeduwaa, hakuna ambaye alikuwa akiongea! Nadhani kila mmoja alikuwa akijaribu kuwaza na kuwazua kama ambavyo nilikuwa nikifanya mimi. “Bado mna mpango wa kwenda kwa mganga?” mzee Miale alivunja ukimya na mimi nikamuangalia baba kama ishara ya kumtupia yeye swali hilo ili afanye maamuzi baada ya ambacho tumekiona.. “tujifunze kuwa na subira” alijibu baba akiigiza ile sauti tukacheka kisha tukaaga na kuondoka.
Usiku wa siku hiyo tulikuwepo nyumbani mapema, tukala na kuingia vyumbani mwetu! Yalikuwa kama majira ya saa tatu na sikuwa na usingizi hata kidogo, nilikuwa na hofu kidogo huku nikimgoja mzee yule nikiwa sina uhakika kama atakuja ama laa!..
Sijui hata saa ngapi nilipitiwa na usingizi ila nilikuja kujikuta nikiisikia sauti ya mtu ikiniita kwa mbali kama naota vile, niliposhituka nilijikuta katika mzingira ambayo sikuwa nikiyajua. Mbele yangu alikuwa amesimama mtu ambaye sikuwa nimewahi kumuona! Alikuwa ni mwanume wa makamo tu, hakuwa mzee wala hakuwa kijana. “karibu bwana, hapa ndipo ambapo napatikana” aliongea bwana yule lakini ilikuwa ni sauti ile ambayo ilitutembelea kwa mzee Miale na hata ambayo alikuja nayo mzee aliyenifuata nyumbani! “wewe ni Mnaro?” niliuliza baada ya kuhisi kuwa alikuwa yeye “ndio” alijibu kwa kifupi nami nikashangaa kwa maana sio yeye ambaye alikuja kwangu usiku ule. “na yule mzee ambaye alikuja kwangu alikuwa nani?” niliuliza naye akanijibu huku akiwa ameshughulika kufanya shughuli ambazo hazikueleweka, alikuwa akihamisha hamisha vitu kama vile ambaye alikuwa akikipanga upya chumba kile ambacho kilijaa makorokoro.. “nilikuwa ni mimi pia” akawa amenichanganya lakini akaendelea na kunipa mwanga “ninao uwezo wa kuonekana kama kijana, kama mzee, kama mtoto, kama mwanamke au hata kama mnyama yoyote yule” sasa alikuwa amesogeza mbele yangu kitu kama beseni kubwa sana ambalo lilikuwa limetengenezwa kwa matirio kama ya mbao hivi, kuangalia ndani ya beseni lile kulikuwa kuna kimiminika cha rangi nyekundu. “sasa ni wakati wa kumuona mkeo” aliongea mzee yule nami nikayalengesha macho yangu zaidi ndani ya beseni lile lakini hakukuwa na chochote ambacho kilionekana! Lakini akaanza kunyunyizia ungaunga ambao ulikuwa ukionekana kama majivu kisha akachukua kipande cha kitambaa na kuanza kukisemea maneno kisha akanikabidhi, nilipokiangalia vizuri niligundua kuwa kilikuwa kipande cha nguo ambayo aliivaa mke wangu siku ile ambayo alipotea, nikashangaa nguo ile aliipata wapi mzee yule kwa maana nilijua kua nguo ile ilikuwa nyumbani. “ili kumuona mtu hapa unatakiwa kuweka humo nguo yake ambayo aliivaa na haijafuliwa, ukitaka kumuona mkeo weka humo kipande hicho cha nguo yake” alisema yule mzee nami nikauliza “lakini mbona nguo yake iko nyumbani?” yule mzee akaniangalia kisha akaniuliza baadala ya kunijibu “kwani wewe ulikuwepo hapa? Haukuwa nyumbani?” nikabaki bila jibu wala swali lingine la kuuliza kisha nikawa nakiingiza kitambaa kile ndani ya kimimkinika kile ambacho nilianza kudhani kuwa kilikuwa damu. Mara niliona kimiminika kile kikianza kuchemka polepole, huku kikiongeza kasi ya kuchemka kadri muda ulivyozidi kwenda na mara kikaanza kuzunguka ndani ya beseni lile kubwa la mbao kisha nikaona kama macho yangu yanavutwa ndani ya beseni lile nikawa najaribu kujivuta kurudi nyuma lakini sikuweza kushindana na nguvu ile nikajiona kama ambaye napoteza fahamu!......
Akili iliporudi sawa nikajikuta nimesimama katika mazingira ambayo sikuwa nikiyajua, kulikuwa na miti mingi sana kama pori fulani hivi kisha nikasikia sauti ikiniita nyuma yangu, nilipogeuka nikakutana na sura ya Mnaro lakini kitu cha ajabu kilikuwa ni kichwa tu kikielea hewani bila kiwiliwili, kitu kingine cha kushangaza ilikuwa ni mchana wakati nilikuwa nikikumbuka vyema kabisa kuwa dakika chache zilizopita nilikuwepo kwa Mnaro na ilikuwa ni usiku. “tembea ukifuata njia hiyo unayoiona mbele yako kisha utakuwa umetoka nje ya pori hili na utakutana na nyumba za watu na watu mbalimbali wakifanya kazi zao kama kawaida, pita kote mpaka utakapokuta nyumba ambayo mlango wake ukiwa umetandwa na mwanga mkubwa, ingia hapo utamkuta mkeo, lengo ni kumuona na sio kumsemesha. Ukiongea umeharibu kila kitu, sawa?” kilielekeza kichwa kile cha Mnaro baada ya mimi kuwa nimegeuka kufuata sauti yake aliponiita nami nikaitikia kwa kukubali kisha nikauliza “sasa watu hao ambao nitawakuta wakiwa wanaendelea na shughuli zao hawatonisumbua?” kichwa cha Mnaro kikajibu.. “sisi hatupo hapa, tuko huko kwenye dunia yetu ya kawaida hivyo hakuna ambaye anakuona, ila ukiongea watakusikia” alimaliza kutoa maelezo nami nikaridhika na kuanza safari ya kufuata ile njia ambayo ilikuwa inanitoa nje ya pori lile kwa maelezo ya Mnaro.
Nilifanikiwa kutoka ndani ya pori lile na kwa mbali nikaanza kuziona nyumba, zilikuwa nyumba za kizamani sana, yani yalikuwa kama mazingira ya kijijini au sehemu ambayo haijaendelea sana. Nilianza kusikia sauti za watu na mifugo ikilia, kilikuwa ni kijiji kikubwa chenye shughuli mbalimbali. Watu wa eneo lile walionekana kuwa ni wachapakazi kila mmoja akiwajibika panapomuhusu. Nilipita nikiwavuka watu wote wale lakini sidhani kama kuna ambaye alikuwa akioniona kwa maana hakuna hata mmoja ambaye alikuwa akiniangalia ingawa nilikuwa nikiwapitia mbele yao kabisa, nikawa nikitembea nikijaribu kuitafuta nyumba ambayo mlango wake una mwanga lakini sikuiona, nikazidi kwenda mbele mpaka nikakaribia kukata tamaa lakini nikaona nyumba moja kubwa ambayo mlango wake ulikuwa wazi lakini kulikuwa na nuru kali kiasi cha kunifanya kushindwa kuona ndani yake, nikaamini Mnaro alimaanisha nyumba ile nami nikaenda na kuingia kwenye mlango ule, baada ya kuvuka mlangoni ndani hakukuwa na mwanga mkali sana nikaona watu wakiwa wamekaa kwenye mkeka eneo lile la wazi wakila chakula, nikazidi kusogea karibu na kugundua kuwa walikuwa wamekaa juu ya ngozi ya mnyama ambaye sikumjua, nilipojaribu kuwatazama vizuri nikagundua kuwa mmoja wao alikuwa mke wangu..
Alikuwa anakula kwenye sahani ya peke yake ingawa wengine walikuwa wakila kwenye sinia moja , nikasogea karibu zaidi nikaona alikuwa anakula wali na nyama ambayo sikujua ni ya mnyama gani, pembeni yake pia kulikuwa na sahani yenye matunda, niliweza kugundua kulikuwa na ndizi, machungwa na matunda mengine sikuyajua. Alikuwa na maji ya kunywa pia kwenye kikombe kikubwa cha mbao. Nilikuwa nimeduwaa nikimuangalia akila kwa upole nikaingiwa na huruma sana nikitamani nimchukue na kuondoka naye. Nikatembea kwa kasi mpaka pale alipo na kutaka kumshika mkono kumnyanyua lakini sikuweza kukamata mkono wake, mkono wangu ulikuwa ukiuvuka wake kama moshi unavyopita mbele ya mtu, roho ikaniuma sana na wakati huu machozi yalikuwa yakinitoka nikafungua mdomo wangu na kutaka kumwambia tuondoke “mke wa...” kabla sijamalizia nikakabwa kabali kubwa ya shingo....
Usikose sehemu ya sita.
Kwa maswali, maoni au ushauri unaweza kunipata kupitia:
+255653686008
nirasaire@gmail.com