Simulizi: Niliyoyaona Darfur yanatisha

Simulizi: Niliyoyaona Darfur yanatisha

SEHEMU YA 11

Kwa muonekano wa harakaharaka, Sudan haikuwa miongoni mwa nchi zilizokuwa na amani kama Tanzania, katika kila kona, magari ya kijeshi ya Umoja wa Mataifa pamoja na yale ya Umoja wa Afrika yalikuwa yakionekana.

Ukiachana na magari hayo ya jeshi, vile vile kulikuwa na magari makubwa ambayo yalikuwa yakitumika kupeleka vyakula katika nchi hiyo.

Sudan ilikuwa na njaa, watu walikuwa bize kuyakimbia makazi yao hasa wale ambao waliishi sehemu za nje ya Jiji la Khatoum.

Mashambani, wakulima hawakufika huko kulima kwa sababu waliogopa. Vyombo vingi vya habari vilikuwa vikitangaza mara kwa mara vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyokuwa vikiendelea kutokea nchini humo.

Darfur ndio ilikuwa sehemu iliyokuwa na mapigano makubwa. Japokuwa sikuwa nimefika huko lakini nilijua tu kwamba sehemu hiyo ilikuwa ni ya hatari mno, kama ungeingia unatembea basi kile ambacho kingerudishwa kingekuwa ni mwili wako tu bila pumzi.

Nilikaa na kuiangalia televisheni na habari za mauaji ambazo zilikuwa zikiendelea kutokea Darfur, niliporidhika, nikainuka na kulifuata begi langu. Nikalifungua na kuanza kutoa kitu kimoja baada ya kingine.

Nikaitoa kamera na kuiweka juu ya meza huku nikiwa nimeiseti sawasawa na pale nilipokaa.
Hapo ndipo ambao nikaanza kujirekodi, makala ambayo nilikuwa nimekwenda kuifanya Darfur ikaanzia hapo.

Niliongea maneno mengi kwa Lugha ya Kingereza huku nikiwataka watazamaji wawe makini kuangalia kila kitakachokwenda kuonekana pamoja na kukisikia kile ambacho nilikuwa ninatarajia kukiongea.
Nilipoona inatosha, nikaizima kamera.

Nikatoa vitu vingine zaidi na zaidi, kazi ambayo ilikuwa mbele yangu ilikuwa kubwa tena ya kujitoa mhanga lakini sikujali, nilichokijali ni kuajiriwa katika moja ya makampuni makubwa ya habari tu. Siku hiyo sikutaka kufanya mambo mengi, nikalala.
 
SEHEMU YA 12

Kelele zilikuwa zikisikika nje, nikashtuka kutoka katika usingizi mzito. Kitu cha kwanza kabisa nilianza kujiuliza ni mahali gani nilipokuwa, baada ya akili kukaa sawa na kukumbuka nilikuwa nchini Sudan, nikainuka kitandani na kwenda dirishani kuchungulia ili kujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea huko.

Niliwaona watu wakikimbia huku na huko, wanajeshi wa Serikali walikuwa wameingia mitaani huku lengo lao likiwa ni kuwatafuta wanajeshi wa kikundi kilichojiita DLF (Darfur Liberation Front) ambacho kilikuwa kinyume na Serikali ambayo ilikuwa madarakani.

Haraka sana nikaichukua kamera yangu kwani kile kilichokuwa kikiendelea kilinivutia mno, nikaanza kurekodi kupitia dirisha la chumba changu.

Mule nilipokuwa nilihisi kama siridhiki hivyo kwa haraka sana nikavaa suruali yangu, nikachukua kitambulisho changu cha bandia ambacho kilinionyesha kuwa ni mwandishi wa habari kutoka katika Shirika la Habari la Al Jazeera na kuelekea nje huku kamba yake nikiwa nimekining’iniza shingoni.

Nilipofika nje, nikaanza kurekodi, nilikuwa nikiendelea kurekodi kimoja baada ya kingine, jinsi wanajeshi wa serikali walivyokuwa wakiwatafuta watu hao na mambo mengine mengi tu.

Hapo niligundua kwamba nilikuwa nikifanya kosa, kwa sababu ile ilikuwa ni makala ihusuyo mambo mbalimbali yaliyokuwa yakiendelea nchini Sudan, yalihitaji maelezo ili kila atakayeiangalia aielewe.

Kwa haraka sana macho yangu yakaanza kuangalia huku na kule na kutua kwa kijana mmoja ambaye alishika madaftari, umri wake bila shaka nilikuwa nimemzidi kidogo.

Nikamfuata kujitambulisha kwamba nilikuwa mwandishi wa habari na hivyo nilihitaji msaada wake.
Hakufahamu Lugha ya Kingereza vizuri lakini tuliweza kuelewana.

Nilichokifanya ni kumpa kamera ile na kuanza kunirekodi kwa malipo ya paundi mia tano za Sudan.
Kazi ikawa imeanza, nilikuwa nikielezea kila kilichokuwa kikiendelea huku kijana yule aliyejitambulisha kwa jina la Majeed akiendelea kunirekodi.

Mahali pale sikuwa mimi peke yangu, waandishi wengine wa BBC, CNN walikuwahapo huku nao wakichukua habari juu ya kila kilichokuwa kikiendelea mahali pale.
 
SEHEMU YA 13

Kitendo cha kuwaona waandishi wale wa habari kiliniuma sana, niliwaonea wivu mno kwa kuwa walikuwa wakifanya kazi katika mashirika ambayo yalinifanya kusafiri mpaka nchini Sudan kwa ajili ya kutengeneza makala yangu.
Majeed aliendelea kunirekodi mpaka pale hali ilipotulia.

Haraka sana mkuu wa majeshi nchini humo akawaita wananchi na waandishi wa habari na kuanza kuzungumza nasi. Moyoni nilijisikia furaha kupita kawaida, sikuamini kama nilifanikisha kuanza kile ambacho nilikuwa nimekipanga kukifanya.

Siku hiyo ndiyo ilikuwa siku ya kwanza kukutana na Majeed ambaye aliniahidi kunisaidia katika kila kitu ambacho nilitakiwa kukifanya huku yeye akiwa kama mshika kamera wangu.

Nilifurahi sana, nilichokifanya ni kuahidiana na malipo ya siku hasa kwa wiki nzima ambayo ningekwenda kuitumia nchini humo na kurudi nyumbani japokuwa viza yangu ilionyesha nilikuwa na uwezo wa kukaa kwa miezi mitatu.

Sikutaka kukaa hapo Khatoum, lengo langu la kufika nchini Sudan lilikuwa ni kufika huko Darfur kulipokuwa na machafuko makubwa. Nilitaka nimwambie Majeed, nilijua angekataa au kuhofia lakini sikutaka kujali, ilikuwa ni lazima nimwambie ili twende huko.

“Nitataka twende Darfur,” nilimwambia Majeed, akashtuka kama nilivyotegemea.
“Kufanya nini?” aliniuliza huku akionekana kuwa na hofu.
“Kufanya kazi ambayo ilinileta mahali hapa.”

“Mh! Mbona kama inakuwa ngumu.”
“Ugumu wake upo wapi hapo?”
“Mauaji. Huko pamejaa damu, watu wanauawa kila siku,” Majeed aliniambia kwa kuhisi kama ningehofia.

“Hayohayo mauaji ndiyo ninayotaka kuyarekodi. Vipi upo tayari twende hiyo kesho?” nilimwambia na kumuuliza.
“Hapana. Siku tayari,” alinijibu.

Majeed alionekana kuwa msaada mkubwa kwangu hapo baadaye, nilimuhitaji sana kwa ajili ya ile kazi ambayo nilitaka kuifanya mahali hapo, alinikatalia katakata ila kwa sababu nilijitambua kwamba mimi ni Mtanzania, tena mwenye maneno mengi, nikaanza kuutumia uongeaji wangu na ushawishi mkubwa kumlaghai Majeed.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom