Simulizi: Niliyoyaona Darfur yanatisha

Simulizi: Niliyoyaona Darfur yanatisha

SEHEMU YA 06

Nilijisikia vibaya sana hasa mara baada ya wazazi wangu kunikatalia kile ambacho nilitaka kukifanya kwa wakati huo.

Nilichukia sana na wala sikutaka kuongea nao, niliwaona kuwa kama wasaliti katika maisha yangu ambao hawakutaka kuniruhusu kufanya kitu ambacho kingenifanya kufaidika katika maisha yangu.

Siku iliyofuata nikaanza kuondoka kuelekea nyumbani alipokuwa akiishi Hamza, rafiki yangu ambaye alikuwa mtaalamu na mambo ya Graphic.

Nilimkuta Hamza na hivyo kumtaka anionyeshee kitambulisho cha mwandishi wa habari wa shirika la habari la Aljazeera na kisha kunionyeshea.

Kitambulisho kile kilionekana kutengenezwa katika utaalamu wa hali ya juu, japokuwa kilikuwa kikionekana kwenye kompyuta lakini kilionekana kuvutia sana.

“Kwa hiyo jina niweke Thomas Chilongani kama kawaida au?” Hamza aliniuliza.
“Nope. Weka Iqram Ibrahim” Nilimwambia.
Pale pale Hamza akabadilisha na kisha kuliweka jina lile.

Kichwani mwangu nilikwishajua kwamba katika kipindi kile nilikuwa nikielekea katika nchi ambayo ilikuwa na waumini wengi wa dini ya Kiislamu, hivyo nilihakikisha kwamba nafanya kila jitihada ili nionekane kuwa mtu wao ili hata kama nitahitaji vitu fulani kutoka kwao basi niweze kuvipata kwa urahisi.

Siku hiyo nilikamilisha kila kitu kilichokuwa kikihitajika na kisha kuondoka kuelekea nyumbani.

Nilichokifanya kwa wakati huo ni kuelekea katika mashine ya ATM na kisha kuchukua kiasi cha fedha cha shilingi milioni mbili na kuanza kuelekea Posta kwa ajili ya manunuzi ya kamera.

Nikapata kamera mbili ambazo zilionekana kuwa bora na kuanza kurudi nyumbani.

Kwa wakati huo, nilitaka kufanya mambo yangu kwa siri sana, sikutaka mtu yeyote nyumbani afahamu kwani kwa kuwafanya wafahamu basi wangeweza kunizuia kwenda kwa kutumia maneno yao ya kunikatisha tamaa na kunitisha.
 
SEHEMU YA 07

Maandalizi yangu yaliendelea zaidi na zaidi, baada ya miezi miwili, nikawa nimekwishagongewa viza ya kukaa kule kwa muda wa miezi mitatu.

Bado siri iliendelea kuwa siri tu, sikuwaambia wazazi wangu na wala sikumwambia mpenzi wangu, Myra kwani nilimuona msichana huyo kuwa kama wazazi wangu tu.

Kiu ambayo nilikuwa nayo katika kipindi hicho ni kuwa mwandishi mkubwa wa kimataifa, mwandishi ambaye ningeweza kufanya kazi ya uandishi katika mashirika makubwa duniani, sikutaka kuonekana kujali au kuhofia kuuawa, kwangu niliamini kwamba nafsi zote zingeonja mauti, haijalishi kama ni Mchungaji au Imamu, wote wangeonja mauti.

Ingawa nilifahamu fika kwamba nchi ya Sudan haikuwa na usalama mkubwa katika maisha yangu lakini katika kipindi hicho sikuonekana kuhofia kitu chochote kile, yaani nilijiona kwamba ningeweza kufika salama na kurudi salama nchini Tanzania ambapo ningeendelea na maisha yangu huyku nikianza kuipeleka makala yangu katika mashirika mbalimbali ya habari.

Naikumbuka sana siku hii ya tarehe 12/11/2005 siku ambayo nilianza safari yangu ya kuelekea nchini Sudan. Moyo wangu ulikuwa na furaha kubwa sana, sikuamini kama katika kipindi hicho nilikuwa nimeweza kuondoka nchini Tanzania na kuelekea nchini Sudan kwa ajili ya kutengeneza makala moja ambayo kila mtu ambaye angeiangalia basi angeonekana kushangaa sana.

Ndani ya ndege nilikuwa na mawazo mengi, nilikuwa nikiwafikiria wazazi wangu ambao nilikuwa nimewaambia kuhusiana na safari hiyo lakini hawakuonekana kuwa radhi kuniruhusu kuelekea katika nchi hiyo ambayo vita vya wenyewe kwa wenyewe vilikuwa vikiwasumbua sana.

Ukiacha na wazazi wangu, pia nilikuwa nikimkumbuka mpenzi wangu, Myra ambaye nae wala hakutofautiana sana na wazazi wangu, kwani nae hakutaka nielekee katika nchi hiyo.

Nilijiona nikiwa nimefanya maamuzi magumu sana, maamuzi ambayo baadae yangeweza kuleta lawama za kila aina, sikutaka kujali kuhusiana na lawama ambazo ningezipata, nilichokuwa nikikitaka ni kuwa mwandishi mkubwa sana ambaye ningeonekana kuifanya dunia kuelewa kwa undani kile ambacho kilikuwa kikiendelea ndani ya nchi ile.
 
SEHEMU YA 08

Ingawa nchi ambayo nilikuwa ikielekea katika kipindi hicho ilionekana kuwa nchi ya hatari, lakini moyoni mwangu wala sikuonekana kuwa na wasiwasi wowote ule, nilikuwa nikizidi kujipa matumaini kwamba kila kitu kingekwenda kama ambavyo kilitakiwa kiwe.

Nilipanga kuandaa makala moja kubwa na ya maana sana katika kila chombo cha habari ambacho kingediriki kuonyesha makala hiyo ambayo ilikuwa imeandaliwa na kijana mbunifu ambaye alikuwa na uwezo wa kuelezea mambo mengi kwa undani zaidi, Thomas Chilongani.
Saa 11:15 jioni, ndege ikaanza kutua kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Khartoum uliokuwa katika jiji la Khartoum.

Hali ya hewa haikuwa nzuri sana, joto liionekana kuwa juu kwa kiasi fulani. Mimi pamoja na abiria wenzangu tukaanza kutoka nje ya uwanja ule.

Macho yangu yalikuwa yakiangalia katika kila upande, nilijitahidi kutaka kuyazoea mazingira ya jiji lile.

Watu wengi ambao walikuwa wakionekana katika macho yangu walikuwa wamevaa kanzu pamoja na vilemba vichwani, mavazi yale ndio yalionekana kuwa makubwa sana katika nchi ile.

Nilipofika nje ya uwanja ule, moja kwa moja nikamfuata dereva wa teksi na kutaka aniepeleke sehemu yoyote ambayo ingeniwezesha kubadilisha fedha zangu na kuwa paundi, fedha ambayo ilikuwa ikitumiwa nchini humo.

Baada ya kumwambia kitu nilichotaka kukifanya, akaniambia niingie ndani ya gari lake na kisha safari kuanza.

Mji wa Khatoum haukuwa mzuri sana, majengo yao yalikuwa kama ya kizamani sana, kwa jinsi ulivyokuwa ukionekana mji ule, hali ilionyesha dhahiri kwamba sehemu kubwa ya nchi ile ilikuwa ni jangwa.
 
SEHEMU YA 09

Mitaa ya jiji lile ilikuwa katika mpangilio mzuri japokuwa haukuwa ukivutia sana. Kwa kila mtu ambaye nilikuwa nikimuona alikuwa akionekana kuwa na kanzu jambo ambalo likanifanya hata mimi pia kutamani kununua kanzu ili nionekane kuwa mmoja wapo.

Safari yetu ile iliishia njie ya duka moja kubwa ambalo nikaingia ndani na kisha kutoa kiasi cha shilingi milioni saba na kisha kunibadilishia katika fedha zao za paundi ya Sudan ambayo walikuwa wakiitumia.

Kutokana na nchi ile kubwa imeanguka sana katika uchumi, fedha zangu nilizozipata zilikuwa nyingi sana.

Kitu cha kwanza nilichokifanya ni kumlipa dereva fedha zake na kisha kumtaka kunipeleka katika hoteli yoyote ambayo haikuwa na gharama kubwa.

Huku tukiwa njiani kuelekea katika hoteli hiyo, nikamwambia kwamba nilikuwa na uhitaji wa kununua kanzu na kiremba na yeye kuniita muuzaji na kununua, sikutaka kuchelewa, nikanunua na kisha kuvivaa pale pale.
“How do I look? (Naonekana vipi?)” Nilimuuliza dereva yule.

“Like a Sudanese (Kama Msudani)” Dereva alinijibu huku akionyesha tabasamu pana.
 
SEHEMU YA 10

Kutokana na nchi ile kuwa katika mapigano ya wenyewe kwa wenyewe ambayo yalikuwa yakiendelea, wanajeshi wa majeshi ya Umoja wa Mataifa walikuwa wametapakaa katika kila kona huku wakiwa kwenye magari yao ambayo yalionekana kutengenezwa kwa ajili ya vita tu.

Si wanajeshi wa Umoja wa Mataifa tu ambao walikuwa wakirandaranda mitaani bali hata wanajeshi wa Umoja wa Afrika (A.U) nao walikuwa wametapakaa katika mitaa ile, kwa picha ambayo ilionekana, sehemu ile haikuonekana kuwa ya usalama hata kidogo.

Baada ya dakika chache dereva akasimamisha gari lile nje ya hoteli moja ndogo iliyoitwa Selima Oasis.

Nikateremka, nikamlipa dereva kiasi ambacho alikuwa ameihitaji na kisha kuelekea katika sehemu ya kaunta na kukutana na msichana mrembo. Nikaanza kumuuliza kuhusu vyumba na kisha kulipia na kupelekwa katika chumba ambacho nilitakiwa kukaa katika siku ambazo ningekuwa hapo Sudan.

Sehemu ambayo nilitamani sana kufika tayari nilikuwa nimekwishafika. Sikujali kama wazazi wangenitafuta na kunikosa, nilichokuwa nikikijali kwa wakati huo ni kutengeneza makala yangu tu. Nilibaki chumbani mule huku nikianza kuifikiria safari yangu ya kuelekea Darfur, magharibi mwa nchi hiyo ya Sudan.

Ingawa ilionekana kuwa sehemu iliyokuwa na hatari lakini wala sikuonekana kujali kabisa, sikuwa na woga wowote moyoni mwangu, nilikuwa nimedhamiria kwa moyo mmoja kwamba ilikuwa ni lazima nifanye kazi ambayo ilikuwa imenleta mahali pale, sikujali kupigwa risasi, kuchomwa moto au kuchinjwa, kile nilichokuwa nikikihitaji kwa wakati huo ni kufanya kazi yangu ambayo niliiona kuwa bora na kuniingizia fedha na kunitambulisha kama mwandishi wa habari wa Kimataifa.


*
*
*
Itaendelea.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom