Simulizi: Namtaka mpenzi wangu arudi

Simulizi: Namtaka mpenzi wangu arudi

SEHEMU YA 74 •


“Najua! Inawezekana Mungu alipanga hivi, hata kama umepooza, nakuahidi kitu kimoja kwamba sitokuacha,” alisema Dickson huku akiwa ameukaribisha uso wake karibu na wa Nandy.
“Unanipenda pamoja na hali niliyokuwanayo?”

“Ninakupenda sana Nandy! Siwezi kukuacha kwa kuwa umepooza, nitakupenda hata kama kuna siku utaondoka ndani ya dunia hii,” alisema Dickson.
“Nimepooza Dickson!”
“Najua! Ninakupenda katika hali hiyohiyo uliyokuwanayo,” alisema.
Alimaanisha, moyoni mwake hakukuwa na msichana aliyekuwa na nafasi zaidi ya Nandy, alikuwa tayari kufanya kila kitu katika maisha yake lakini si kumuacha msichana huyo.

Aliongea naye mambo mengi kitandani pale, yale machozi yakakauka na kuanza kucheka pamoja mahali hapo kitu kilichowafurahisha wazazi wao.
Siku zikaendelea kukatika, kila siku madaktari walikuwa wakiingia na kuangalia hali ya Nandy. Walichokifanya ni kumnunulia Nandy kiti cha mataili ambacho walimtaka kukitumia katika maisha yake.

Hiyo ikawa nafasi ya Dickson kumtoa na kuanza kuzunguka naye huku akimuendesha kwenye kiti kile. Kila siku hiyo ndiyo ilikuwa ratiba yao, walitoka asubuhi na kwenda kwenye bustani, huko walizungumza mambo mengi huku wakipanga mipango yao ya maisha ya baadaye.

“Nandy!” aliita Dickson.
“Abeee.”
“Will you marry me?” (utakubali nikuoe?) aliuliza Dickson, hapohapo akapiga magoti mbele ya Nandy na kumuonyeshea pete iliyokuwa kwenye kikabati chake.

Nandy alipoiona, akashindwa kuvumilia, palepale alipokuwa akaanza kulia, hakuamini kuona mwanaume huyo akiwa na shauku ya kutaka kumuona japokuwa alikuwa kwenye hali mbaya kama aliyokuwa nayo.

Alitamani kuinyanyua mikono yake na kumkumbatia lakini alishindwa kusogeza kiungo chake chochote kile. Akakubaliana naye huku akilia, akatingisha kichwa chake na kumwambia kwamba alikuwa tayari kuolewa na yeye lakini bado kulikuwa na tatizo kwamba alikuwa amepooza.

“Sijali!”
“Ila sitoweza kufanya mapenzi na wewe!”
“Sijali!”
“Sitoweza kukuzalia watoto!”
“Pia sijali!”
 
SEHEMU YA 75 •


“Dickson! Kwa nini usitafute mwanamke mwingine?”
“Siwezi! Nilianza kukupoteza Nandy! Kwa sasa, sitoweza kukupoteza tena. Kwako sihitaji watoto, sihitaji kufanya mapenzi, nikiwa na wewe tu najisikia amani, najisikia furaha, najiona kukamilika kama mwanaume,” alisema Dickson, akachukua mkono wa Nandy na kumvisha pete ya uchumba huku wazazi wao wakiwa kwa mbali wakiangalia.

Ulikuwa ni ushujaa mkubwa kwa Dickson, kwake hakutaka kujali kitu chochote kile, alichokuwa akikiangalia ni kuwa na msichana huyo tu.
Baada ya kukaa miezi miwili, wakaondoka na kurudi nchini Tanzania. Njiani walikuwa wakizungumza mambo mengi mno, walikuwa wakifurahia pamoja japokuwa kwa msichana Nandy hakuweza kufanya kitu chochote kile.

Walipofika, maisha yakaanza upya. Dickson hakutaka kuona Nandy akikaa peke yake, alichokifanya ni kumuhamisha nyumbani kwao na kuanza kuishi na yeye. Hakutaka kusoma tena, alichokifanya ni kusimamia biashara za baba yake.
Akamuajiri msichana wa kazi za ndani aliyeitwa Maria ambaye huyo alitakiwa kukaa na Nandy na kumuhudumia kwa kila kitu.

Wakati akiwa ameishi nchini Tanzania kwa siku tatu, ghafla akashtukia akipokea ugeni kutoka katika Kituo cha Polisi cha Osterbay na kuambiwa kwamba alikuwa akihitajika huko kwa kuwa kulikuwa na kesi ya kubaka iliyofunguliwa.
“Nilibaka?” aliuliza, alisahau kabisa kuhusu Amina.

“Ndiyo!” alijibu polisi mmoja na kumfunga pingu, wakaanza kuelekea kituoni.
Wakati akiwa ndani ya gari la polisi ndipo kumbukumbu ya tukio hilo lilipomjia kichwani mwake. Alikumbuka namna alivyotumiwa video akiwa anafanya mapenzi na Amina ambaye alionekana kama alikuwa akimbaka.

Moyo wake ukawa na hasira zaidi na Linda kwani aliamini kwamba msichana huyo ndiye aliyekwenda kituoni na kufungua kesi hiyo.

Alipofikshwa huko, akatupwa selo na kuambiwa asubiri kwani kesi yake hiyo nzito ilikuwa ikiandaliwa tayari kwa kupelekwa mahakamani ambapo ingeanza kusikilizwa na kama angekutwa na hatia, alitakiwa kufungwa gerezani kwa miaka isiyopungua thelathini.

JE, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 76

Wazazi wa Dickson walipewa taarifa juu ya kile kilichokuwa kimetokea, walishangaa, kwao lilionekana kuwa jambo geni kwa mtoto wao kukamatwa na kupelekwa polisi huku akishutumiwa kwa kosa la ubakaji alilokuwa amelifanya miezi mitatu iliyopita.

Wakaondoka na kuelekea katika kituo hicho ambapo huko wakajitambulisha kwa polisi na kutaka kujua kile kilichokuwa kimetokea.
Polisi hao waliwaambia kwamba kulikuwa na msichana mmoja aliyekwenda kituoni hapo kufungua kesi ya ubakaji aliyokuwa ameifanya miezi mitatu iliyopita.

Walichokitaka ni kuonana na msichana huyo na kuzungumza naye kwani kitu hicho kwao kilionekana kuwa kigeni na hawakuwa na uhakika kama mtoto wao alifanya kosa hilo kwa kuwa walimwamini, alikuwa mcha Mungu ambaye aliishi katika mazingira ya dini kila siku.

Linda akapigiwa simu na kuambiwa kwamba mwanaume aliyekuwa amemfungulia kesi tayari alikuwa amekamatwa na hivyo kwenda katika kituo hicho.

Msichana huyo aliposikia hilo, moyo wake ukawa na furaha, akawa na amani na kuona kwamba alikuwa amemaliza kila kitu na hivyo kitu kilichokuwa kimebaki kilikuwa ni kuzungumza na Amina ili amwambie kwamba alitakiwa kujiandaa.

“Kila kitu tayari, yule mwanaume amekamatwa,” alisema Linda.
“Mwanaume gani?”
“Dickson! Yaani umesahau?” aliuliza Linda.

Amina alisahau kila kitu kilichotokea, siku hiyo alipoambiwa kuhusu mwanaume huyo, kumbukumbu zake zikaanza kurudi nyuma na kuikumbuka sura ya mwanaume huyo.

Bado alikuwa mzuri, alihisi kabisa kwamba kama angekwenda mahakamani na kutoa ushahidi kwamba alibakwa kitu ambacho hakikuwa kweli, aliona kabisa maisha yake yasingekuwa kama yalivyokuwa, yangebadilika kwa kuwa nafsi yake kila siku ingekuwa ikimsuta.
“Siwezi! Siwezi kutoa ushahidi wa kumfunga,” alisema Amina.

Hilo ndilo alilopanga, hakutaka kumwambia Linda, mwanamke huyo alitumia kiasi kikubwa cha pesa kuhakikisha kila kitu alichopanga kinakwenda kama kilivyotakiwa hivyo kama angekataa kwamba hakubakwa basi alihisi kungekuwa na jambo baya ambalo lingetokea.

Wakati akifikiria kuhusu hayo, Linda akampigia simu na kumwambia kwamba walitakiwa kuonana kwa kuwa kuna mambo mengi walitakiwa kuyazungumza kabla ya kupanda mahakamani.
 
Thanks shunie
Sasa mamii naomba unitag ile hadithi ya binti kipofu aliyezuzuka na raha za dunia hii
 
Upo vzr bibie, yaani tangu nianze kufuatilia hadithi zako kuanzia Mkufu wa Malkia wa Ghoshen.! Sitaki kukosa tena uhondo. Tupia zaidi. I wish ningekuwa na namba yako ningeliknunulia bundle kabisaaa.!!
 
Asanteee. Naitafuta sasa hivi. Maana huwa zinaniondolea uchovu kabisaaaa nikitoka kwenye mihangaiko yangu jioni.!! Ubarikiwe sana mpendwa.!!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom