SEHEMU YA 54
Alishindwa kuyazuia machozi yake, moyo wake ulimuuma mno, akapata hasira kali dhidi ya Linda, japokuwa ilikuwa ni ajali tu lakini akahisi kama yeye ndiye aliyehusika katika ajali hiyo kwa kuwa tu hakumtakiwa kuwa na msichana huyo.
“Nandy!” aliita Dickson huku akimsogelea na kumwangalia vizuri.
Nandy hakuyafumbua macho yake, aliyafumba na kutulia, kwa jinsi alivyokuwa ametulia ilikuwa rahisi sana kusema kuwa msichana huyo alifariki dunia.
“Nandy...Nandy...Nandy! Forgive me,” (Nandy...Nandy...Nandy...nisamehe) alisema Dickson huku akitokwa na machozi.
Dokta hakutaka waendelee kubaki ndani ya chumba hicho, akawachukua na kutoka nao. Akaelekea nao ofisini na kuanza kuwaambia kuhusu mgonjwa wao.
Wote wawili walikuwa wakitokwa na machozi, waliumia, pamoja na kuwa katika hali ya huzuni lakini walitakiwa kuambiwa kitu kingine ambacho kingewatia huzuni zaidi.
“Kuna jambo jingine kuhusu mgonjwa wenu,” alisema Dk. Ndaki huku akiwaangalia kwa zamu.
“Tatizo gani?”
“Mgonjwa wenu....kwanza alipata ajali, donge la damu liliganda kwenye kichwa chake lakini tulifanikiwa kulitoa baada ya kumfanyia upasuaji wa kichwa. Ila kuna tatizo jingine ambalo mnatakiwa kulifahamu,” alisema dokta, hapo, akanyamaza, wote wakabaki wakimwangalia.
“Lipi?” aliuliza Dickson.
“Ni kwamba mgonjwa wenu amevunjika uti wa mgongo,” alisema dokta, wote wakabaki wakimwangalia.
“Uti wa mgongo kwa maana hatoweza.....”
“Kufanya lolote lile, atapooza, maisha yake yote yatakuwa kitandani tu,” alisema daktari, palepale kwenye kiti wote wawili wakaanza kulia kwa sauti kubwa kama watoto wadogo.
Je, nini kitaendelea?