SEHEMU YA 53
Mzee Gwamaka hakumpenda Dickson, alimchukia kwa kuwa alimuumiza binti yake lakini kwenye hali kama aliyokuwanayo, hakuwa na jinsi, akaungana naye na kuanza kwenda huku na kule kumtafuta msichana huyo.
Ilipofika majira ya saa sita usiku, wakaamua kuzunguka kwenye hospitali mbalimbali na kuulizia kama alifikishwa huko akiwa maiti. Wakaelekea katika mochwari za hospitali zote lakini hakukuwa na majibu.
“Twende Muhimbili,” alisema Dickson.
Wakaelekea huko, sehemu ya kwanza kabisa kufika ilikuwa ni mochwari ambapo huko wakaenda na kuanza kumtafut Nandy, walimkosa, hilo liliwachanganya sana na kwenda kuulizia kwa manesi ndipo wakapewa taarifa kuhusu wagonjwa walioletwa hospitalini hapo siku hiyo.
“Kuna msichana?” aliuliza mzee Gwamaka.
“Wapo sita hivi.”
“Majina?”
Akawatajia lakini akawaambia kwamba wawili hawakuwa wakijulikana. Wakataka kuwaona hao wawili, wakapelekwa kwa mmoja, walipomwangalia, hakuwa Nandy.
“Na huyo mwingine?”
“Huyo yupo mahututi, tangu aletwe hospitali hajanyanyuka, alipata ajali mbaya sana,” alisema.
“Ajali mbaya?”
“Ongeza sana.”
Wakataka kumuona msichana huyo. Hawakuruhusiwa kumuona kwa kipindi hicho mpaka baada ya daktari kufika kwa lengo la kumjulia hali.
Akawaambia kuhusu watu hao kwamba walitaka kumuona mgonjwa huyo kwani walikuwa wakimtafuta ndugu yao aliyekuwa amepotea na mpaka muda huo, saa nane usiku hawakujua mahali alipokuwa.
Kwa kuwa walikuwa wamechoka na walionekana kutaka kujua kuhusu ndugu yao, wakachukuliwa na kupelekwa katika chumba hicho.
Kwa mbele walimuona msichana akiwa kitandani, hakuwa akitingishika, aliwekewa dripu huku akipumua kwa kutumia mashine ya gesi. Kichwa chake kilizungushiwa bandeji, kwa kumwangalia pale alipokuwa ilikuwa rahisi sana kugundua kwamba mtu huyo alikuwa mahututi.
Wakaanza kumsogelea, walipomfikia na kumwangalia usini. Alikuwa Nandy. Mzee Gwamaka akahisi miguu yake ikipigwa ganzi, hakuweza kusimama, akajikuta akikaa chini na kuanza kulia.
Dickson, hakuamini alichokuwa akikiangalia, kwanza akahisi kwamba alikuwa akiota, Nandy, msichana aliyekuwa akimpenda kwa moyo wote hakuamini kama siku hiyo angekuwa katika hali aliyokuwanayo kipindi hicho.