*MKUFU WA MALKIA II -- 56*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Kabla Oragon na Ottoman hawajapiga hatua kujongea ndani ya nyumba, wakaisikia sauti kali ya mtu akilia! Kunguru wote waliokuwa juu ya paa wakarusha mbawa zao kuruka!
Oragon na Ottoman wakatazamana.
ENDELEA
Walikuwa na hofu mioyoni mwao. Akili yao ilitengeneza picha kubwa Rabis kama bonge la mtu anayeogopeka na hata kuua ama kutesa wanaomkosea. Penngine mawazo yao yalikuwa sahihi.
Ila ni mpaka pale walipoenda kuthibitisha kwa macho yao.
Wakabisha hodi mara mbili mlangoni na punde wakasikia kishindo kizito kikijongea mlango. Huyu ndiye Rabis! Wakatetemeka mioyo.
Mara mlango ukafunguliwa na jibaba kubwa lililoshikilia panga mkononi. Nguo zake zilikuwa chafu zimelowana damu. Alikuwa ana ndevu na nywele lukuki kichwani.
Macho makubwa ya kutisha. Pua ndefu iliyochongoka ila mdomo usionekane kisa kufunikwa na ndevu.
Aliwatazama wakina Oragon pasipo kuteta jambo. Alafu akaufungua mlango wazi waingie. Wakazama humo ndani na kukuta watu kadhaa, kwa haraka kama vile kumi na wawili, wakiwa wamesimama na kila mtu akiwa na mzigo wake, aidha ndani ya kifurushi, ama mkoba.
Lakini humu ndani palikuwa pakubwa sana. Kwa mbali kidogo na watu waliosimama kulikuwa na kama kimadhabahu kidogo. Kuna kiti hapo na mtu mmoja mfupi, miguu hata haigusi chini, alikuwa ameketi.
Alikuwa ana nywele ndefu nyeusi. Vidole vyake vimejawa pete za dhahabu na shingo yake pia. Mikufu inayong'aa!
Chini yake kulikuwa kuna vifurushi kadhaa vikiwa vimewekwa hapo.
Kushoto kwake kulikuwa kuna damu zimetapakaa. Mwili mmoja umelala hapo kimfu. Si bure alikuwa ndiye yule aliyepiga kelele muda si mrefu, kunguru wakawehuka.
Mbali na hapo humo ndani hakukuwa na kitu kingine cha maana zaidi ya samani zilizochoka, mkangafu, japokuwa palionekana ni eneo zuri likifanyiwa matengenezo.
Lile jibaba liliwaelekeza wakina Oragon mahala pa kusimama, kule walipo wenzao, kisha likaenda kusimama kando na yule mtu ambaye ameketi kwenye kiti. Ambaye bila shaka ndiye Rabis!
Akamuagiza,
"Pelekea nguruwe!" Akionyeshea maiti iliyokuwepo hapo chini. Yule jibaba likaunyanyua ule mwili, bado ukiwa unaendelea kuvuja damu, akaenda nao nje.
Si bure wale nguruwe walikuwa wanono kiasi kile. Wanalishwa nyama za binadamu!! Oragon na mwenzake wakatetemeka. Hawakujua ni kwanini mtu yule aliuawa. Pengine nao watauawa kama yule kisha wakalishwe nguruwe!!
Tena lililowapa uoga zaidi, hawakuwa wanamjua Rabis hata punje. Hawakuwa wanajua mwanaume huyo anataka nini, nini miiko yake wala laana!
Basi wakiwa wanameza mate, wakanyamaza watazame namna mambo yanavyoenda.
Wakasonga kwenye ule mstari. Mtu wa kwanza wakamwona akiwa amefikisha mbele kifurushi chake. Rabis akatazama kilichomo ndani na mara akamtikisia kichwa.
Mtu huyo akaenda zake!
Akaja wa pili na wa tatu. Wote hawakuwa na shida. Lakini mmoja aliyefuata alikuwa ameshikilia kifurushi kilichosinyaa. Uso wake ulikuwa na woga. Mikono yake ilikuwa inatetemeka.
Alimkabidhi kifurushi Rabis, Rabis akakitazama kisha akamtazama yule jabali lake la pembeni, mara jabali akamnyaka huyo jamaa na kumsukumia chini. Akamkatakata!!
Kisha kama kawaida akamnyanyua na kwenda kupeleka maiti kwenye banda la nguruwe wamtafune!
Ulipopita muda mfupi, wakina Oragon nao wakafika mbele ya Rabis. Walikuwa wanatetemeka sana. Walimkabidhi Rabis kifurushi chao kisha wakajitambulisha, wao ni wana wa mwewe!
Basi Rabis akawatazama kana kwamba anawapekua. Akatazama na ndani ya kifurushi kisha akabinua mdomo wake.
"Wana wa mwewe!" Akasema kwa kebehi. "Mnajifanya wajanja sio?"
Oragon na Ottoman wakatazamana. Kisha wakatikisa kichwa.
"Yani ushuru wote ninaowadai, muda wote huo, huu ndiyo mmeniletea?" Rabis akauliza akitoa macho.
"Hapana, sisi hata hatujui. Wametukabidhi tulete tu hapa hakuna lolote tunalolifahamu."
Rabis hakuamini. Akamuagiza yule jabali awakamate na kuwashughulikia vijana hao haraka iwezekanavyo!!
Basi wakina Oragon wakadakwa kwa mkono mmoja tu, wakatupiwa chini. Jabali akapandisha panga lake nene juu! Mara
"Msituue! Tuna kingine cha kuwapa!" Akaropoka Oragon.
Rabis akamzuia jabali kutenda kazi yake, kisha akauliza:
"Ni nini hicho?"
**
Sasa alikuwa anafahamu safari yake inaelekea ukingoni. Moyoni alijawa na furaha sana na hakutaka kungoja tena kuijaza zawadi mikono mwake.
Waheed akatabasamu. Mbele yake kulikuwa kuna lango kubwa. Lango kubwa la chuma. Na humo ndani ndimo kuna kofia ya pharao!
Akasogelea lango hilo na kuweka kiganja chake hapo. Mara lango likang'aa na kujiandika maneno kadhaa:
'Ndani mfalme amepumzika. Ni nini unataka?'
Waheed akatabasamu mwenyewe. Alikuwa ana hamu pomoni kushuhudia kwa macho yake kitu ambacho amekuwa amehadithiwa maisha yake yote.
Basi kwa kutumia kidole chake akaandika:
'Nataka kofia ya pharao'
Akangoja majibu. Kimya.
Akaweka tena kiganja chake juu ya lango. Mara maneno yale yaliyotokea awali yakajiandika tena.
'Ndani mfalme amepumzika. Ni nini unataka?'
Waheed akaandika:
"Nataka kofia ya Pharao'
Ikawa kimya tena. Hakupata majibu. Akaweka kiganja kwa mara nyingine. Mara hii akaandika anaomba kofia ya Pharao. Bado majibu yakawa yaleyale. Kimya. Akaweka tena kiganja na sasa akaandika tafadhali naomba kofia ya Pharao.
Majibu hayakubadilika. Kimya.
Akashika kiuno chake akiwaza. Fikra ikamjia kichwani. Akaweka kiganja tena kwenye lango, mara hii akaandika:'
'Nataka kumwamsha Pharao!'
Mara lango likaandika kuuliza:
'Unacho cha kumfanya aamke?'
Waheed akafikiri kwanza. Tamaa ikamzidi hamu akaandika kujibu:
'Ndio.'
Mara lango likafunguka. Waheed akazama ndani na lango likajifunga. Humo ndani kulikuwa na kama kauwanja. Kwa mbele, juu kidogo, kulikuwa na kiti kimoja kikubwa kilichotengenezwa kwa dhahabu.
Kwenye kiti hicho alikuwa kulikuwa kumekaliwa na mifupa ya binadamu. Haikuonyesa chembe ya uhai. Mifupa hiyo ilikuwa ni ya Pharao aliyekufa miaka lukuki huko nyuma!!
Juu ya fuvu ya mifupa hiyo kulikuwa na kofia ya dhahabu! Kofia inayometameta. Kofia ambayo kwa kuitazama ungetambua ni ya thamani kiasi gani!
Japo ilikuwa ya muda mrefu hapo nyuma, kofia hii bado ilikuwa mpya. Inavutia machoni na kushawishi kuinyakua!!
Waheed mate yakamtoka. Sasa kazi kwake ilibakia moja tu. Kwenda kuinyakua kofia ile na kutokomea zake akaitawale dunia.
Lakini kabla hajapiga hatua kuifuata kofia hiyo, akawaza. Li kwapi jeshi la wafu?? Lile alilokuwa anaambiwa habari zake za kutisha kwamba ukizama humo basi utapambana nalo??
Akatazama kando na kando, hakuona kitu! Kakiwanja haka kalikuwa cheupe, mabaki tu ya vitu vya kale hapa na pale. Mbali na mifupa ya Pharao hakukuwa na mifupa mingine ya ziada.
Basi Waheed akaanza kujongea kuelekea kitini. Moyoni alikuwa ana hofu, akawa anatazama nyuma na pembeni yake mara kwa mara.
Akafika kitini hapo. Akameza mate kwanza. Akashika kofia ile na taratibu akainyofoa kichwani kisha akatulia kusikilizia kama kuna lolote litatokea. Kimya. Hakuna kitu!!
Akatabasamu na kushusha pumzi ndefu.
Akakumbatia kofia ile na kuanza kupiga hatua za haraka kwenda langoni. Akaweka kiganja chake hapo, na mara Lango likaulizia ahadi aliyoiweka hapo awali kwa njia ya maandishi.
"Umeshamwasha mfalme?"
Kabla Waheed hajajibu, mara lango likaandika tena:
"Ahsante kwa kutimiza ahadi."
Hapa Waheed akashtuka. Ahadi gani hiyo? Mbona hakumwamsha mfalme??
Kutazama nyuma, hamaki akaona mifupa ile iliyokuwa imeketi pale kitini, imenyanyuka!!
Pharao alikuwa ameamka!
Mara Lango likafunguka, Waheed akataka kukimbia, lakini asiende popote akakutana na JESHI LA WAFU mlangoni!!
Watu hawa wote walikuwa ni mifupa tu. Mikononi mwao walikuwa wamebebelea mapanga yaliyoota kutu. Wengine wakiwa na mikufu shingoni ama pete za dhahabu vidoleni.
Waheed alipotazama vema, akashtuka, kwa kando alimuona Seth, mara akamwona na Alk - jitu la Azeth, mwishowe Fluffy!!
Watu hawa wote walikuwa wafu. Miili yao bado ilikuwa na mabaki ya damu na matundu ya visu walivyokitwa na Waheed.
Nao walikuwa tayari miongoni mwa jeshi la wafu. Macho yao yalikuwa mekundu na makali. Sura zao za kutisha. Sura za kazi!!
**