MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN --007
Simulizi za series
Sasa Jayit alikuwa anataka nguvu hiyo; nguvu ya kizazi chao; nguvu ya babu na bibi yake. Ingawa alikuwa ana nguvu zake binafsi lakini bado kwake haikuwa inatosha kabisa. Alitaka nyongeza. Alitaka zaidi!
Alitaka kutawala tawala zote nyakati za usiku!
Alibwia unga wa wa mafuvu ya babu na bibi yake akiwa ameuchanganya na madawa kadhaa. Aliumung’unya unga huo na kuumeza kana kwamba anakunywa dawa ya klorokwini, alikuwa amekunja sura akiusikilizia unga ukizama mwilini. Alipotulia baada ya sekunde tatu tu akaanza kubadilika mwili kuwa mtu wa ajabu zaidi!
Rangi yake ya mwili wake iligeuka na kuwa nyekundu. Mkia ulichomoza ukiwa na kishungi cha simba. Kwenye paji lake la uso, pembe mithili ya za ng’ombe zikachomoza. Alitisha! Lakini zaidi ya hapo, alikuwa na nguvu mno kiasi kwamba alipokuwa anakanyaga sakafu ilipasuka ama kutitia.
Wazee tisa walipiga magoti wakamsujudia. Si tu hao, hata raia wake wasioleweka ni watu wa aina gani nao wakapiga magoti ya kusujudu kumkaribisha kiongozi wao mpya.
“Sasa ni muda wetu!” Alifoka Jayit, umati wa watu wake ukimsikiliza vizuri. “Ni muda wa Devonship kutawala tawala zote! Ni muda wa Devonship kutawala nyatakati zote za usiku!” alisisitiza maneno hayo kwa kuyarudia mara tatu.
Alinyoosha mikono yake membamba juu radi nyekundu zikapiga kwa fujo. Wafuasi wake walifurahia na kupiga nderemo. Wote waliimba:
“Wasaa umewadia! … wasaa wa kutwaa vilivyo vyetu!”
Jayit alimlisha pia farasi wake madawa, mnyama huyo akawa wa ajabu. Macho yake yaligeuka kuwa mekundu na misuli yake ikakamaa kana kwamba alikuwa ananyanyua vyuma. Nywele zake za shingoni zilikuwa ndefu zaidi na meno yake yakachongoka mithili ya mnyama chui!
Hapo Jayit akajikuta anatabasamu kwa furaha. Moyoni alishajua hakuna atayeweza kumzuia, hakuna atakayediriki kunyanyua kiungo chake chochote kuziba njia yake kwahiyo basi kwanini ajinyime furaha? Kama kuna siku njema kwake, basi ile ilikuwa ni mojawapo.
“Mkuu, tunangojea tu amri yako,” alisema mwanaume mmoja mrefu mweusi mwenye kipara. Alikuwa ni mmojawapo wa wanajeshi wa Jayit, tena kiongozi mkuu kwa vyeo.
Uso wake ulikuwa mpana wenye makovu mbalimbali ya kuchanwachanwa kiasi kwamba alikuwa kama kapeti iliyochoka. Kwa jina alizoeleka kuitwa Tititat japokuwa jina lake kamili ni Titus Titanium.
“Ngoja kwanza Tititat,” alisema Jayit akiwa anakunywa damu ndani ya bilauri la kioo. “Wala halihitaji papara hili jambo. Huyu kuku ni wa kwetu, hatuna haja ya manati!”
.
.
.
.
.
***
.
.
.
.
Tangu pale kifo cha Fursa kilipotokea, Rhoda hakuwa na furaha tena. Mara nyingi alijikuta akiwa amekunja uso wake, amejikunyata na kukaa mbali na watu. Macho yake yalijaa machozi na hata urembo wake ukaanza kutiwa doa kwa kutojijali.
Yote hayo si tu kwamba yalisababishwa na kutokuwa na uwezo wa kujihudumia vema, bali pia mawazo juu ya kesho yake. Japokuwa alikuwa amejishikiza kwa kufungua mgahawa mpya wa chakula kutokana na pesa alizozichuma toka kwa Fursa, bado aliona maisha ni magumu mno.
Hakukuwa na mtu yeyote anayejuana naye serikalini, hili lilikuwa ni tatizo kwake na kwa biashara, na pia hakuwa mzoefu wa kuchakarika kutafuta pesa bali kupewa.
Maisha yaligeuka chini juu, juu chini. Alitokea kuwa na kinyongo kikali dhidi ya malkia Veda kwani alijua fika huyo ndiye aliyemuua Fursa. Alijikuta anamchukia mwanamke huyo mno, lakini bahati mbaya hakuwa na chochote cha kufanya zaidi tu ya kuungulia kifuani.
Akiwa anapika chakula cha wateja wa mchana kwenye mgahawa wake mpya unaosuasua, wateja watatu, wanaume, waliingia na kuketi.
Walikuwa wanaongea kwa sauti kubwa na isingekuwia vigumu kujua ya kwamba walitoka kunywa kwanza kabla ya kupitia pale. Walikuwa wanacheka hovyo, macho yao yalikuwa mekundu wakinukia pombe kana kwamba pafyumu ya Kurusumu.
Pasipo kuficha, walikuwa wanaonyesha chuki zao za wazi kwa malkia Veda wakimuita ni malaya aliyemuua mume wake na amedhamiria kuwaua na wao pia.
“Hivi kweli tumeshindwa kabisa kumtoa huyo mwanamke madarakani?” Aliuliza mlevi mmoja. “Yani siamini kabisa kama inakaribia juma moja sasa.”
“Nani wa kumtoa?” Akauliza mwingine. “Ni mshirikina mno, we hujaona Fursa na wenzake walivyonyongwa kama kuku?”
“Sasa kama mshirikina, kwanini hakupelekwa Tanashe kwa wachawi?” Aliuliza mlevi mwingine.
“Ukute mme wake pia alikuwa anajua!”
“Una maanisha marehemu mfalme wetu?”
“Ndio. Mbona hakupelekwa huko? Ni kwasababu alikuwa mke wa mfalme.”
“Unamaanisha kwamba mfalme naye alikuwa mchawi?”
“Ndio! Na watakuwa waligombana, mke akamuua mume wake. Sasa alivyoona Fursa amechukua madaraka, akaamua amuue!”
Mlevi mmoja akatikisa kichwa chake kwa masikitiko.
“Aibu iliyoje hii kuongozwa na mchawi? Yaani nikiwa huko nje nitaona hata aibu kusema nimetokea Goshen. Si wataniona mchawi!”
“Lakini Malkia wetu ameenda wapi?”
Aliuliza mlevi mmoja. Swali hilo likazua mtafaruku mkubwa. Hakuna aliyekuwa anajua wapi alipo Malkia Sandarus, waliamini atakuwa amekufa kwani kama angekuwa hai basi wangepata kusikia habari yake.
Walevi hao walipiga kelele haswa lakini Rhoda hakuzisikia hata kidogo. Alikuwa amezama kwenye mawazo asipate muda wa kusikiliza chochote huko nje.
Hata hakujua kama kuna wageni mpaka pale aliposhituliwa na walevi hao wakimtuhumu kutowajali.
“Samahani sana wateja wangu,” alinyenyekea Rhoda. Walevi walimpuuza wakaagiza chakula. Baada ya muda mfupi chakula kililetwa mezani walevi wakawa wanakula. Walimaliza na Rhoda akadai pesa yake.
“Mbona bei ghali hivyo?” Alilalama mlevi mmoja.
“Jamani si mnajua kodi zimepanda,” Rhoda alieleza. “Wakulima nao wamepandisha bei ya mazao yao, kila kitu sasa kimekuwa ghali!”
“Ah! Ah! Hatuwezi kulipa hiyo pesa!” akasema mlevi mmoja akinyanyuka. Wote walisimama na wakakataa kulipa pesa.
Rhoda alipambana apate pesa yake lakini hakuweza. Bei ilikuwa juu na walevi hawakutaka kuelewa sababu ya hilo. Japokuwa pia walipotoka kunywa pombe bei ilikuwa imepanda vilevile, hawakuwa wamejali hilo isipokuwa tu kwenye chakula.
Walimpiga kikumbo Rhoda, wakadhihaki na kushombo:
“Katafute bwana huko! Hii kazi si yako.”
“Au kama unataka twende tukalale wote nikupe pesa!”
Walicheka wakaondoka zao.
Rhoda alijikusanya akawahi chakula chake kinachoungua jikoni kabla ya kuja kuketi kuwaza na kuwazua akitoa chozi.
Mwishowe aliamini kweli ile haikuwa kazi yake, upishi na kuuza mgahawa, na inambidi afanye juhudi za kutafuta kazi nyingine anayoiweza zaidi.
Mawazo yake yalimtuma amtafute mwanaume mwingine anayejiweza kwa mali na hali. Akimpata mwanaume huyo aombe ndoa, ama basi amchune vya kutosha asimbakize hata harufu ya damu ili apate pesa za kutosha kufanya mambo mengine na si kuuzia chakula masikini wenzake waliojaa maudhi, makwazo na majaribu.
.
.
.
.
.
*** .
.
.
.
.
Ndani ya siku tatu bado wanaendelea na safari. Kuamkia siku ya nne ndipo Malkia Sandarus na Zura walitia miguu ndani ya tawala ya Osheni – tawala ya masonara.
Hakuwa na mwenyeji yeyote huko hivyo basi ikawalazimu kutafuta msamaria mwema atakayewakarimu baada ya kutokuwa na pesa za kukodi chumba. Walimpata mwanaume mmoja, sonara mdogo, aliyewapa chumba kimoja wapate kujikusanyia humo. Wakapumzika kwa masaa kadhaa kisha wakaoga na kula chakula kidogo walichopewa.
“Mbona mmetoka mbali hivyo kuja hapa?” Aliuliza msonara yule mkarimu. Alikuwa ni mwanaume mnene mwenye nywele ‘rafu’. Nguoze zilikuwa zimechoka na si nadhifu.
“Tumekuja kutafuta taarifa juu ya mkufu,” alijibu Malkia. Alimueleza kila kitu msonara yule mdogo juu ya mkufu wake. Akajaribu pia na kuuchora chini ili apate kumtengenezea taswira kuhusu nini anaongelea.
“Siujui kusema ukweli. Na sifahamu ni wapi waweza kupata taarifa yake,” alijibu msonara mdogo kwa masikitiko.
“Hamna yeyote ambaye unadhani anaweza akatusaidia?” Aliuliza Zura.
Msonara alifikiria kwa muda mfupi, akasema:
“Labda naweza nikawaelekeza kwa wasonara fulani wa kati. Pengine wanaweza wakawa na taarifa.”
Msonara huyo mdogo aliwaelekeza Malkia na Zura wapi watawapata wasonara hao wa kati ambao walikuwa watatu kwa idadi. Pasipo kupoteza muda, Zura na Malkia wakawaendea wasonara hao kuelezea haja zao.
Lakini hata huko napo hawakupata kitu. Hakuna aliyekuwa anafahamu kuhusu huo mkufu, wala hakuna aliyeamini kama Sandarus ni malkia. Labda kutokana na mwonekano wake usioonyesha kama kweli ni malkia.
Walirudi kwa msonara mdogo na kumpasha habari. Msonara huyo alisikitika sana. Alijua sasa kazi itakuwa kubwa na huku upenyo wa kufanikiwa ukiwa mdogo sana.
“Hao niliowaambia ni masonara maarufu wa kati. Sasa hapo hakuna tena cha kufanya zaidi ya kwenda kwa msonara wa juu. Itakuwa ajabu sana kama na yeye hatokuwa na taarifa ya kitu kikubwa kama hicho kwenye fani hii ya usonara.”
Matabasamu yakajaa kwenye nyuso za Malkia na Zura.
“Ila si rahisi kabisa kumpata msonara huyu. Anafanya biashara za juu na uongozi wa tawala mbalimbali. Ratiba yake ni ngumu na kazi zenye faida kubwa zimepangana kwake.”
Matabasamu yakajifinya.
“Na ukizingatia, hamna atakayeamini wewe ni malkia,” alimalizia msonara.
“Tutaenda tu kujaribu,” alisema Malkia. Msonara mdogo pasipo na hiyana akawaelekeza wapi watampata mtu huyo.
“Ni maarufu sana, hamwezi mkapotea.”
Japokuwa ilikuwa inaelekea jioni, Malkia na Zura hawakutaka kukoma kuendelea kusaka. Walielekea kule walipoelekezwa, kwa msonara mkubwa, huko walikuta nyumba kubwa mno yenye fensi kubwa ya mawe. Mlangoni kulikuwa kuna walinzi wawili, warefu wenye sura kavu za kazi, waliobebelea mapanga marefu yanayometameta.
Walieleza haja yao kwa walinzi hao ili waruhusiwe kuingia ndani. Walinzi waliangua kicheko na kuwataka wapotee eneo hilo haraka iwezekanavyo.
“Embu tutoleeni uchafu hapa!” Aliamuru mlinzi mmoja kwa sura ya ukali. “Hapa wanakuja watu wakubwa tu, watu wenye heshima zao!”
Malkia na Zura walijitetea lakini hawakusikilizwa wala hawakuaminiwa, mwishowe walinyakuliwa wakaenda wakamwagiwa mbali.
“Ole wenu tuwaone tena!” Mlinzi alitoa kitisho kabla hawajarejea lindoni mwao upesi.
Malkia na Zura walirudi kwa msonara mdogo wakiwa na huzuni. Mioyo ilikuwa imewavunjika wasiwe na matumaini. Msonara aliwakaribisha akiwataka wavute subira kwani waweza wakafanikiwa.
“Msijali, hiko chumba kipo tu wazi tangu mwanangu afariki dunia mwaka jana,” alisema msonara mdogo. “Nipo mpweke sana, mke wangu pia alifariki, nafurahia nyie kuwepo hapa maana mnanipa faraja.”
Wanawake hao walipika chakula cha usiku huo, wakala na kulala. Walidumu hapo kwa siku nne pasipo kufanikiwa. Hawakupata nafasi ya kumuona msonara mkubwa, kila siku walipojaribu waliishia kukimbizwa na walinzi.
Waliwaza kukata tamaa, lakini je kufanya hivyo si nikumaanisha muda wote huo waliotumia kuhangaika ni bure? Walipowaza hapo basi wakajipa moyo wa kuendelea kuvuta subira. Walikuwa nyumbani kwa msonara wakifanya kazi za hapa na pale.
Kwenye siku ya tano, majira ya jioni, msonara alikuja nyumbani akawapasha habari.
“Kesho kuna ujio mzito kwa msonara mkubwa, Mfalme toka Uarabuni anakuja. Hiyo inaweza ikawa nafasi yenu ya kuingia ndani na kukutana na msonara huyo!”
Taarifa hiyo ilikuwa njema, lakini ilikuwa imebeba hatari ndani yake, hatari ambayo inaweza pia kuukwapua uhai wa mtu. Malkia na Zura walitokea kulitambua hilo na hivyo basi wakadhamiria kujiandaa.
Kuna mambo kadhaa waliyaomba toka kwa msonara, bahati nzuri msonara akaahidi kuwasaidia.
Kesho ilipowasili, kwenye majira ya alasiri, msafara mkubwa wa farasi wa Mfalme toka Uarabuni ulijongea ndani ya himaya ya Osheni. Kwa idadi ya harakaharaka kulikuwa kuna farasi themanini na ushenzi. Farasi wanne wanaovuta kitoroli kilichojifunga vema, ndio walimbebelea mtawala. Farasi wengine wakiwa ni wa walinzi na wanawake walioongozana na Mfalme huyo.
Ni katikati ya farasi hao waliowabebelea wanawake, ndipo Malkia na Zura wakajichomeka. Walikuwa wamejivika kufunika sura zao wakiacha macho tu, nguo ambayo ilivaliwa na wanawake wote msafarani hivyo hawakugundulikana kwa upesi.
Lakini pia tendo hilo lilifanyika kwa wepesi mno kiasi kwamba halikukamata ‘atensheni’ ya watazamaji wala walinzi.
Malkia na Zura waliingia ndani ya jengo la msonara wanayemlenga. Na wakati msonara huyo akimkaribisha mgeni wake, wao walishuka toka farasini wakazunguka nyuma ya nyumba kwa siri na tahadhari.
Walitaka kujitunza humo kwa muda mrefu unaowezekana huku wakiwinda nafasi ya kuonana na msonara mkubwa.
Walijua fika wageni wale, toka uarabuni, watalala pale kutokana na muda waliongia jengoni, lakini pia waliamini ndani ya muda huo watapata tu fursa ambayo msonara atakuwa mpweke, na hiyo ndiyo itakuwa nafasi yao.
Lakini je watadumu humo jengoni mpaka kumuona msonara wakiwa hawajakamatwa? Hapo ndio palikuwa shida.
Kutokana na nyumba hiyo kuwa kubwa mno, walifanikiwa kujificha mara kwa mara pale walipohisi usalama wao upo mashakani.
Waligundua ndani ya nyumba ile, ama jumba, ulinzi haukuwa mkubwa sana kama vile ilivyokuwa kule nje. Basi kwa kutumia mwanya huo, waliweza kujificha mpaka pale katikati ya usiku.
Mfalme toka uarabuni alikuwa amelala, hata wapambe wake pia. Msonara naye alikuwa amelala ndani ya chumba chake kilichojaa samani akiwa na wanawake wale aliokuja nao Mfalme.
Akiwa humo anatafuta usingizi, mlango wa chumba chake ulifunguliwa akaingia Malkia Sandarus, na punde Zura naye akazama. Msonara alishituka akiwatazama wanawake hao.
Alihofia usalama wake. Hata wanawake aliokuwa amelala nao, walikurupuka wakiwa na nyuso zenye mashaka. “Tafadhali naomba usipige kelele,” alisema Malkia Sandarus. “Nimekuja hapa tokea Goshen, nimekuja kuonana na wewe unisaidie.”
“Nikusaidie nini?”
“Ni kuhusu mkufu fulani!”
“Mkufu upi? Unadhani mimi najua mikufu yote duniani?”
“Haujui yote, ila utakuwa unaujua huu!”
Msonara, pasipo kujali, alipaza sauti yake kuwaita walinzi. Malkia alitaka kukimbia lakini Zura akamzuia. Walinzi walifika wakawatwaa wanawake hao. .
.
.
.
.
Lako jicho!