SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

textgram_1505928279.png


Hapatoshi [emoji91][emoji91][emoji91]
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II -- 31*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Wakanywa maji kidogo kidogo kulowanisha tu vinywa.

Basi kwasababu za uchovu, wakapitiwa na usingizi.

Lakini je, makazi haya waliyoyapata, hayakuwa na wenyewe? Ni kweli waliyakuta matupu yaliyokaa hapo kwa bahati tu?

ENDELEA

Hakuna mtu aliyewaza hayo. Kila mmoja alikuwa hoi. Walitazamia kupumzika tu wapate kupooza miili yao iliyomchemshwa na jua.

Lakini japokuwa walikuwa kivulini, bado wakaendelea kutota kana kwamba wamemwagiwa ndoo za maji, ama wapo mvuani.

Kama kuna mahali utakapokiri pasipo kulazimishwa kuwa maji ni uhai, basi ni hapa. Utahitaji maji muda wote. Kila saa ulimi wako utakwangua mdomo kama taulo.

Ndani ya pango hili , miale ya jua haikuwa inafika, ila joto lake lilikuwa kali mno kana kwamba tanuri la kuchomea mkaa. Lakini utafanyaje? Bado palikuwa ni kheri.

Basi wakauvuta usingizi.

Lakini kwenye pango hilo walilokuwa wamelala, ndani kabisa kule kizani, ni siri kulikuwa kuna mifupa ya wanyama na hata binadamu. Mifupa hii ilikuwa mingi ikirundikwa kutengeneza kichuguu!

Na hata pangoni hapo ukitazama vema ardhi yake ngumu, utagundua kulikuwa kuna nyayo za miguu ya kiumbe!

Miguu hii haikuwa ya kawaida. Ilikuwa ni myembamba yenye vidole virefu. Ikiachana kwa umbali mkubwa hatua kwa hatua.

Zaidi ya hapo, kiumbe huyu alikuwapo ndani. Ndani ya pango. Kwenye kina cha pango. Macho yake yalikuwa yanang'aa kama yale ya paka akiwa gizani.

Macho haya yalikuwa makubwa, na yakifanana haswa kimuonekano na bundi.

Kiumbe huyu alikuwa ni nani? Si tu kwamba hakuna anayemjua, bali hakuna hata aliyekuwa anafahamu kama yupo hapo!

Kiumbe huyu alikuwa anawaona vema wageni wake japo wao walikuwa hawamwoni wala kumhisi. Alikuwa anawatazama wageni kimawindo akiwapigia mahesabu kwa namna atakavyopata mifupa yao kuongezea idadi ya ile aliyokuwa nayo.

Basi kutimiza adhma yake hiyo, kuwatafuna na kuwapembua mifupa wageni ambao hakutoa jasho kuwatafuta, akaanza kuwajongea.

Kitu pekee ambacho kingekufanya ukajua anajongea, ni kusogea kwa macho yake yaliyokuwa yanang'aa. Na sauti za mifupa aliyokuwa akiikanyaga ikivunjikavunjika taratibu.

Kiumbe huyu alikuwa mjawa wa akili pia. Pale alipohisi mmoja wa mgeni wake atashtuka kwa sauti ya kusogea kwake, basi akasimama na kuvuta muda. Kisha akaendeleza safari baada ya kuona mazingira ni mazuri.

Sasa akawakaribia wageni wake akiwa amebakiza hatua chache tu kuwatia kinywani. Hapo akaanza kuonekana angalau kwa mbali. Rangi yake ilikuwa nyeupe.

Akapiga hatua tena, lakini ghafla akasita. Bado alikuwa kizani. Aliutokeza mguu wake kwenye mwanga, ila kwa haraka mno akaurudisha gizani.

Aliungua!

Akangurumia kooni kwa maumivu. Mara Seth akakurupuka na kuangaza. Hakuona kitu. Kiumbe kile hakikuwapo tena pale kilipokuwa. Haikujulikana kimeyoyomea wapi!

Seth asikubali kwamba hamna kitu, akaendelea kurusha macho yake, ila mwishowe akachoka na kuamua kulaza kichwa chini. Lakini hakulala tena usingizi. Kuna shaka alilipata.

Baadae jua lilipopungua makali, wakaamua kusonga na safari yao. Bado walikuwa wana mwendo mrefu wa kwenda. Walishapumzika na kupata nguvu mpya.

Wakatembea mpaka usiku ukawafikia. Angalau wakawa wamevuta mguu kwa kiasi chake. Kwa siku hiyo ikawa imetosha sasa, wapumzike kwa ajili ya kesho yake.

Wakatandika juu ya mchanga na kulaza miili yao baada ya kula akiba ndogo ya chakula.

Kulikuwa kuna baridi sasa. Upepo ulikuwa unapuliza kwa fujo na hata mara nyingine ukisomba mchanga. Usingedhani kama eneo hili ndilo lilikuwa lina joto la pasi wakati wa mchana.

Wakati watu wote wakiwa wamelala, kupo kimya, wamepotelea usingizini, yeye Malkia alikuwa anakodoa macho. Hakuwa na usingizi. Kichwa chake kilikuwa kimebanwa na mawazo kadha wa kadha.

Alikuwa anawaza wapi watapata maji. Wapi watapata chakula. Ni wazi walivyokuwa navyo visingeweza kumaliza hata siku tatu. Sasa itakuaje? Watafia jangwani?

Akageukia kila upande, akiwaza asiwazue. Hakupata majibu pasipo kujali alijikakamuaje. Mwishowe, akajilazimu kuamini njia itapatikana japo hakujua ni kwa namna gani.

Angalau sasa usingizi ukaanza kumnyemelea. Akalala.

Hakujua ulipita muda gani akiwa usingizini, ila mara akasikia sauti ya mtu kwa mbali ikiwa inaita. Mwanzo akadhani ni ndoto. Lakini sauti hiyo ikaendelea kuita tena na tena! Akashtuka na kuangaza.

Ajabu, upande wake wa magharibi akamwona mtu akiwa anazama mchangani. Moyo wake ukapiga fundo kubwa - bumm! Na kuanza kukimbia harakaharaka - bum! bum! - bum! bum! - bum! bum!

Wenzake wote walikuwa wamelala. Hamna aliyekuwa na habari. Lakini miongoni mwao, hakuwapo mmoja. Naye ni Ghaut - jitu la Azeth!

Malkia akaamsha wenzake upesi na kuwahabarisha. Kwa haraka wakanyanyuka, isipokuwa Seth mwenye majeraha, wakakimbia kwenda kumsaidia Ghaut aliyekuwa anamezwa na shimo la mchanga.

Lakini ajabu ni kwamba Ghaut huyo hakuwa akipiga makelele wala kufanya jitihada zozote za kujikomboa. Hakuwa katika fikra wala fahamu zake kamili. Masikioni mwake alikiwa anasikia sauti tu iliyompumbaza.

Wenzake wakabahatika kumdaka mkono mmoja. Mwili wake wote ulikuwa umemezwa tayari. Wakajaribu kumvuta kwa nguvu zao zote. Wakashindwa.

Ghaut akaenda mbele ya macho yao!

Wakajaribu kufukua lakini wapi. Hakukuwa hata na dalili ya shimo. Wakaketi wakiwa wamebaki na majonzi na maswali vichwani.

"Nilisikia sauti nikiwa usingizini," Malkia aliteta. "Ilikuwa inaita Ghaut Ghaut, lakini nikadhani ni ndoto. Kumbe ndiyo ilikuwa inamchukua!"

Wakastaajabu sana. Hawakutarajia kama lile jinamizi la majina lingeendelea kumuwinda Ghaut mpaka kule jangwani. Walidhani waliliacha msituni. Hawakutarajia pia kama shimo lile limezalo watu lingejiri mpaka mchangani.

Usiku ukawa mbaya kwao. Wakapoteza hamu yote ya kulala. Wakaketi ama kujilaza wakijikunyata. Ilikuwa ni kama ndoto ndani ya dakika chache tu kumpoteza mwenzao asionekane hata mwili!

Kukawa kimya. Sauti ya upepo pekee ndiyo ikivuma na kupuliza huku na huko.

Usiku ukazidi kusonga.

Zikiwa zimepita kama dakika thelathini tangu Ghaut amezwe na mchanga, Seth akawashtua tena wenzake baada ya kuona kitu cha ajabu kwa mbali.

Kilikuwa ni kile kiumbe kilichokuwamo ndani ya pango! Sasa jua lilikuwa kimetokomea, anaweza kuringa na kutamba. Sasa ulikuwa ni muda wake. Alikuwa amekuja kudai mifupa ya wageni wake.

***
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN II -- 32*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Kukawa kimya. Sauti ya upepo pekee ndiyo ikivuma na kupuliza huku na huko.

Usiku ukazidi kusonga.

Zikiwa zimepita kama dakika thelathini tangu Ghaut amezwe na mchanga, Seth akawashtua tena wenzake baada ya kuona kitu cha ajabu kwa mbali.

Kilikuwa ni kile kiumbe kilichokuwamo ndani ya pango! Sasa jua lilikuwa kimetokomea, anaweza kuringa na kutamba. Sasa ulikuwa ni muda wake. Alikuwa amekuja kudai mifupa ya wageni wake.

ENDELEA

Kiumbe huyu alikuwa mwembamba mwenye rangi nyeupe ya kufifia. Kichwa chake kisichokuwa na nywele kilikuwa cha duara inayokaribia pembe tatu, macho yake makubwa rangi ya kijani, kifua chake kimechomoza mbavu, mikono mirefu na mipana.

Alikuwa anatembea kilevi lakini akionyesha mwenye nguvu. Miguu yake ilikuwa inatawanya michanga ya jangwa kana kwamba maji. Mdomo wake mdogo wenye meno ya paka ulikuwa wazi akiwatazama walengwa wake anaotaka kuwatia kinywani.

Na mate yalikuwa yanamchuruza.

Kiumbe gani hiki? Wakajiuliza wakina Malkia wakitumbua macho. Hawakuwa wanaamini wanachokiona. Hawakujua kiumbe hicho kinataka nini lakini kwa haraka wakaamini hakijaja pale kwa kheri.

"Wewe ni nani?" Seth akapaza sauti. "Unataka nini?"

Kiumbe kile wala hakikuongea, kikazidi kusonga kuwajongea kana kwamba hakijasikia. Seth akabadilisha lugha takribani nne akimuuliza kiumbe kile maswali hayohayo, hatimaye akafanikiwa!

Aliongea lugha anayoielewa. Lugha hii ilikuwa ni ki-injin, lugha inayozungumzwa na idadi ndogo sana ya watu waishio mabarafuni. Ilikuwa na maneno machache, na endapo ukiiskiliza vema utatambua inarudiarudia sana maneno lakini kumaanisha maana tofauti.

"Kukluf kazif tekop, meshan kabac tubuknova," akateta kiumbe yule akiwa anazidi kusogea.

"Anasema nini?" Zura akawahi kuuliza kwa hofu. Macho yake yalijawa woga, mikono yake ilikuwa inatetemeka.

Seth, kwa haraka, akawakalimania kwamba kiumbe yule anaitwa Kazif na amekuja hapo kuchukua kilicho chake.

"Kipi hicho?" Malkia akawahi kuuliza. Alimgeuzia uso Seth lakini macho yakiwa kwa yule mgeni wao anayezidi kujongea.

Seth akamuuliza tena yule kiumbe kwa lugha anayoielewa, hapo amekuja kufuata nini hicho kilicho chake? Kiumbe kile pasipo hiyana, akasema mifupa. Anahitaji kwenda kujaza pango lake zaidi.

Malkia akataka kunyanyua panga, Seth akawahi kumtazama na kumzuia kwa ishara ya kumwonyesha kiganja.

"Acha tuongee naye kwanza."

Kisha akamwomba kiumbe yule aketi chini wapate kuteta. Wao hawana maana ya kuzua shari. Kwa kusikia ombi hilo, kiumbe kile kikaketi kikiwatazama. Zura na Fluffy wakazidi kupata hofu. Kiumbe hicho hakikuwa kinavutia kukitazama hata kidogo.

Kadiri kilivyosogea basi kingekufanya tumbo likusokote kwa woga. Miguu ife ganzi. Na haswa kikikutazama, ungeweza kupata haja zote kwa mpigo!

Tangu kiumbe hichi kiliposogea hapo, hali ya hewa ikageuka na kuwa baridi zaidi. Ungemtazama vizuri ungebaini alikuwa anafuka moshi. Moshi wa barafu.

Si bure hakuwa anapatana jua maana angeweza kuyeyuka.

Basi Seth akamwomba awabakizie uhai wao, na watakaporejea toka safari yao ya mbali watampatia zawadi kama fadhila. Kiumbe hicho kikakataa na kusema:

"Habaq quatta kilim meshan, juata himas!" Akimaanisha kama wamemkatalia ombi lake basi wacheze naye mchezo. Seth akamuuliza mchezo gani huo, Kazif akamwambia unaitwa 'Yuaj si Kobil' - maji ama damu.

Akauelezea mchezo huo. Atawauliza mafumbo matatu na endapo wakiyakokotoa atawapatia maji, na endapo wakishindwa basi wao watampatia damu.

Hiyo ndiyo njia pekee ya kuweka nao makubaliano.

"Hapana," Malkia akakataa. "Hatuwezi kucheza naye mchezo huo wa hatari kiasi hicho. Tupambane naye!"

"Lakini vipi kama tukapoteza zaidi kwa kupambana naye kuliko njia hii ya kidiplomasia?" Akauliza Seth. "Vipi kama tukashinda, tukabaki salama na maji akatupatia? Si rahisi kupambana na kiumbe hiki!"

Lakini bado Malkia akawa na woga. Seth akamsihi wachague mchezo huo, na kwa pamoja watashirikiana kufumbua mafumbo hayo. Vichwa vitano si sawa na kimoja.

Basi wakamruhusu kiumbe yule aanze kuuliza mafumbo yake. Hapa chini kama yalivyotafsiriwa:

La kwanza, kikapu kina matufaha matano na nina watoto watano. Nitayagawanyaje haya matufaha matano kwa watoto wangu na kwa wakati huo tufaha moja likabaki kapuni?

"Tumekwisha!" Akasema Fluffy akitoa macho. "Mbona anauliza maswali ambayo hayawezakani!"

Seth akasafisha koo lake kisha akafikiri kidogo. Akajibu atawapatia matufaha manne kwa wale watoto wa nne, alafu mtoto wa tano atampatia tufaha likiwa limebaki ndani ya kikapu.

Wakastaajabu mojawapo ya chupa yao imejawa na maji. Walikuwa wamepata!

La pili, anayekitengeneza, hakihitaji. Anayekinunua hakitumii. Anayekitumia hawezi kukiona wala kukihisi. Ni nini hicho?

Seth akatabasamu, haraka akajibu ni sanda. Basi chupa lao la pili likajawa na maji. Wakafurahi. Kile kiumbe kikang'ata meno yake kwa hasira. Sasa akadhamiria kuuliza fumbo gumu la mwisho ili angalau asiwe amepoteza muda wake bure.

La tatu, nyakati za mchana huzitumia dirishani, nyakati za chakula naenda mezani, nyakati za usiku najificha hamnioni. Mimi ni nani?

Seth akatabasamu tena, upesi akajibu ni nzi. Bobo lao moja lilio tupu likajaa maji! Alikuwa amepata! Sasa kiumbe huyu akawa ameshindwa kutimiza adhma yake. Lakini kwa ukaidi, akasema anaongezea swali moja la mwisho.

Seth na wenzake wakatahamaki. Malkia akasema yule kiumbe hakuwa anataka kuwaacha hai, inabidi wapambane. Lakini Seth akawatoa hofu, hawakuwa na haja hiyo. Wamwache huyo kiumbe atupe turufu yake ya mwisho.

La nne, kuna wadada wawili: mmoja anamzaa huyo wa pili, alafu naye huyo wa pili anamzaa huyo wa kwanza. Hawa wadada wawili ni wakina nani?

Seth akamtazama Malkia kisha Fluffy na baadae Zura. Akawauliza kama wana majibu, wote wakasema hawana. Wakajawa pia na hofu baada ya kuona Seth anawauliza wao. Walikuwa wanamtegemea yeye kwenye hili.

Lakini mara Seth akatabasamu, akamtazama kiumbe yule na kumjibu dada hao ni usiku na mchana.

Kiumbe kile kikakasirika mno. Alikuwa ameshindwa! Akasaga meno yake na kupiga ngumi kiganja chake. Akamwambia Seth kwamba ameshinda kwa leo lakini anajua itawachukua siku kadhaa kumaliza jangwa hilo kwahiyo kila siku usiku atakuwa anawatembelea na kuwauliza mafumbo kadhaa.

Hawatayapata siku zote hizo, aliamini na kuwaaminisha. Akaenda zake akiwa ameghafirika.

"Uliyajuaje mafumbo yote yale?" Fluffy akamuuliza Seth akiwa na kimuhe. Seth akamwambia baba yake alikuwa akimuuliza sana akiwa mtoto, vile vile vitabu vingi alivyovisoma. Wakampongeza sana kwani alisaidia kupata maji ambayo hawakujua wangeyapatia wapi.

Lakini kwa wakati huo, yule kiumbe, akiwa amepania kwa dhati, akaenda kukesha usiku mzima kupitia mafumbo yake aliyoyaandika kwenye kuta za pango. Hata kula hakutaka!

***
 
Uuuuwiiiih. Hicho kiumbe kimeniogopesha hadi mie huku. This is an art of writing.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom