SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

SIMULIZI: Mkufu wa Malkia wa Goshen

Dah nimekuja nduki nkajua nimechelewa[emoji16][emoji16][emoji16]kumbe majamaa bado mpo na arosto zenu.
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 28*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Mzee asiseme kitu, akashusha pumzi ndefu. Akawataka wanawe wakapumzike. Wote wakaondoka na kumwacha mwenyewe.

Usiku kwake ukawa mgumu.

ENDELEA

Akafikiria sana, mwishowe akaenda zake kujilaza kitandani. Huko akaendelea kuwaza na kuwazua mpaka pale usingizi ulimpokwapua.

Hata hivyo usingizini akawa anakurupuka na majinamizi.

**

Baada ya kusema maneno matatu, mlango ukafunguka.

Giza lilikuwa limenoga haswa, na jengo zima lilikuwa jeusi ti!

Vikongwe wakazama ndani na kuangaza angaza kukagua mali yao. Bado walikuwa ndani ya mwili wa Rhoda. Mkononi walikuwa wamebebelea kifurushi kidogo cha kitambaa cheusi.

"Hatimaye tupo nyumbani!" Wakasema Rhoda akitabasamu.

Hawakudumu ndani ya mwili huo, wakauvua na kuuacha kitini ili wapate wasaa wa kutengeneza na kufanya kilichowaleta Tanashe.

Ndani ya kifurushi walikuwa wamejaza dawa walizozipitia na kuzichuma maeneo mbalimbali ndani ya Tanashe. Kwasababu ya kazi hiyo, hawakupata wasaa wa kutia mguu nyumbani kwao tangu wazame ndani ya himaya hiyo masaa mengi tu yaliyopita.

"Ila nimechoka haswa," akasema kikongwe mmoja. Acha tuwatofautishe kwa idadi ya macho yao. Huyu aliyesema hii kauli alikuwa na jicho moja, mwenzake akiwa na mawili kamili, ambapo moja alikuwa amelitohoa toka kwa yule mwenzao waliyemuua.

"Umeanza uvivu wako!" Akasema huyu mwenye macho mawili. Wakati huo alikuwa amebebelea chungu kikubwa akikipeleka uani.

"Siku nzima tumekuwa tukiinamisha migongo huko. Hujachoka?" Akauliza kikongwe wa jicho moja. Mwenzake hakumjibu kwa haraka, alikuwa anakagua kile chungu alichokileta akiwa amezamisha kichwa ndani.

Alipokitoa akamuuliza mwenziwe:

"Umechoshwa na nini?" Pasipo kumtazama. Alikuwa anaendelea na shughuli zake za maandalizi.

Mwenziwe akalalama kuchoka, mwili mzima unamuuma, hawezi kumpa mkono wa msaada kwa muda huo. Basi yule kikongwe mwenye macho mawili akabakia akipambana na zoezi hilo. Sasa hawakuongea kwa muda kidogo.

Alipokamilisha nusu ya kila kitu, mafiga, vyombo na kuviweka hapo vitu vyote vitakavyotumika, akamtazama mwenzake. Akamkuta amekwisha lala!

Akaishia kusonya na kisha akatafuta mwanya naye ajipumzishe. Akilini hakuwa na msongo kwani alishajua amemaliza kupanga kila kitu.

Dakika kama tano zikapita wote wakiwa wamelala.

Lakini punde, kule kwenye dirisha la upande wa kushoto, popo akatua.

Popo huyo, akiwa amebinuka kichwa chini miguu juu, akawasha macho yake makubwa kumulika mazingira ya sebuleni.

Akakaa hapo kwa dakika moja, na mara akawasha mbawa zake kutimka!

**

Popo akatua kwenye bega la kulia la kaka yake Venin, mwanaume mweupe mwenye macho makubwa mekundu, nywele ndefu nyeupe mithili ya sufi.

Mwanaume huyo jabali alikuwa ameketi kwenye kiti chake cha enzi akiwa amevalia joho lake zito jeusi. Kwenye kola kulikuwa na ufito wa rangi nyekundu iliyokolea.

Alionekana bora kuliko hapo awali.

Uso wake wa kutisha ulikuwa umetulia tuli, macho yake yakionyesha hayupo karibu kimawazo.

Popo yule aliyemtulia begani, akamnong'oneza jambo sikioni, na mara mwanaume huyu akatabasamu kuonyesha meno yake mabaya rangi ya njano kisha akasimama na kunyoosha mikono yake yote miwili angani.

"Wakati umefika!" Akapaza sauti. "Wakati umefika! Wakati umefika!" Kisha akanyamaza akitazama dari.

Na kwa sauti ya chini akasema:

"Muda wa kulipa kisasi ..." huku akitikisa kichwa. "muda wa kumwaga damu ... muda wa Venet!" Na kumbe hili ndilo lilikuwa jina lake.

Venet.

Kaka wa mlozi Venim. Mwanaume aliyebeba kisasi cha kumuua mdogo wake kwa kumtuhumu kumsaliti, na hata kumgeuka pindi alipotakiwa amtumie watu wa kumtoa Tanashe.

Mwanaume aliyepigwa zongo dakika za mwisho na vikongwe kwa kufanikiwa kuondoka na mwili wa Rhoda.

Sasa ilikuwa zamu yake.

Kufumba na kufumbua akageuka kundi kubwa la popo kiasi kwamba mwanga uliokuwa eneo hilo wote ukamezwa na kuwa giza!

Mara popo hao wakatoka nje kwa fujo! Hao wakayoyoma. Hao wakayoyoma!

Wakielekea kule lilipo jengo la vikongwe.

***

Usingizi ulikuwa mzito na mtamu mno kunyanyua kope. Unaweza kusema hivyo kwani kwa sasa walikuwa wanakoroma kwa mbali.

Ni kweli walikuwa wamechoka mno kwa kazi waliyoifanya siku nzima. Walilala kwa amani zote wakiwa wamejawa na matumaini.

Matumaini ya kwenda kuiteka Goshen na kuiweka kwenye viganja vyao. Matumaini ya kuwa walozi wa kwanza kutawala himaya ya binadamu. Wafanye wanavyotaka. Wafanye inavyowapendeza.

Lakini hawakujua matumaini haya yalikuwa hatiani sasa. Yalikuwa mashakani, tena mashaka makubwa!

Hawakujua hata muda huo walikuwa tayari wameshatiwa nguvuni. Hawakuwa kwenye nyumba yao kama pengine walivyokuwa wanadhani vichwani mwao.

Hawakujua kwa muda huo, Venet alikuwa yu mbele yao akiwatazama!

Venet akiwa ameketi kwenye kiti chake, akaliza vidole vyake vya mkono wa kushoto. Mara wakatokea popo huko wasipojulikana. Venet akawaelekeza popo hao kwa kidole kwenda kwa wale vikongwe ambao walikuwa wamefungwa mikono na miguu kwa minyororo.

Popo wakawavamia wale vikongwe na kuwakurupusha toka usingizini. Wakastaajabu sana kujikuta pale. Wakaogofya sana kumwona Venet mbele yao.

Sasa wakajua wamekwisha!

Venet akatabasamu.

"Karibuni, warembo!" Akasema kwa dhihaka. "Mpo mahala sahihi!"

Kisha akanyanyuka na kuanza kusonga hatua za taratibu kuwafuata wale vikongwe waliokuwa wameshikiliwa na minyororo kutani.

"Nisingependa kuongelea ya nyuma, hayo yashapita na yamekwenda. Ila naona mliona haitapendeza endapo msiponipatia nami nafasi, sio?" Akauliza Venet akimpigapiga vikofi kikongwe mwenye macho mawili.

Alikuwa anatabasamu, alikuwa ana furaha kifuani mwake.

Akacheka sana. Akawadhihaki sana wale vikongwe. Akawatambia sana. Na mwishowe akawahabarisha wawe tayari kwa ajili ya kafara lake kwani mwezi ulio mzima utaonekana angani ndani ya siku tatu zijazo.

"Punde mwezi huo utakavyotawala anga, hakuna kati yenu atakayesalimika. Kiu yangu itakatwa!"

Akaendea kioo chake cha kilozi na kumtafuta mdogo wake Venim. Akampatia ujumbe mfupi, anakuja yu njiani.

Ajiandae kwa kifo chake.

"Labda unipatie sababu ya muhimu ya kukubakizia uhai wako. La sivyo ..."

Akapotea kiooni.

**

Asubuhi ...

Baada ya kupata kifungua kinywa, Tattiana akiwa mwenyewe mezani, akatazama nje kwa kupitia dirishani. Hakukuwa na mtu.

Nyumba nzima alikuwa yeye mwenyewe. Alichelewa kuamka. Hakujua baba na mama yake wameenda wapi wala Fanty.

Akajiuliza kuwahusu hao. Akanywa chai taratibu akiwaza. Alipomaliza akawa ameboreka kwa kutokuwa na shughuli ya kufanya.

Hapo ndipo wazo likamjia. Kama yupo mwenyewe nyumbani kwanini asijue kile ambacho wengine hawataki akijue?

Alipambana sana na hili wazo. Ni kama vile mwili wake ulikuwa hautaki wakati akili inataka. Akajaribu kujizuia, ila mwishowe akashindwa. Akanyanyuka na kupitia mlango wa nyuma aende stoo.

Alikuwa anataka kwenda kuchungulia vile vitu ambavyo vililetwa na Oragon na Ottoman. Vilikuwa ni vitu gani hivyo ambavyo hataki kuelezwa?

Akafungua stoo na kuzama ndani. Kulikuwa ni giza, kuona vema ilimbidi akazane kukodoa macho.

***
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 29*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Alipambana sana na hili wazo. Ni kama vile mwili wake ulikuwa hautaki wakati akili inataka. Akajaribu kujizuia, ila mwishowe akashindwa. Akanyanyuka na kupitia mlango wa nyuma aende stoo.

Alikuwa anataka kwenda kuchungulia vile vitu ambavyo vililetwa na Oragon na Ottoman. Vilikuwa ni vitu gani hivyo ambavyo hataki kuelezwa?

Akafungua stoo na kuzama ndani. Kulikuwa ni giza, kuona vema ilimbidi akazane kukodoa macho.

ENDELEA

Akakapekua huku na huku. Akashika hiki na kile na kukifunua lakini hakuona kitu zaidi ya majani ya farasi. Akakasirika.

Akasema pengine mzigo huo unaweza ukawa kwenye stoo ya pili. Basi akiwa amejawa matamanio ya kutaka kujua, akatoka ndani ya ile stoo ya kwanza na kwenda ya pili.

Alikuwa mwangalifu mno.

Akafungua mlango na kuzama humo, napo akaanza kupekua kama alivyo fanya kwenye stoo ya kwanza.

Hakumaliza zoezi, akasikia geti huko likifunguliwa! Akashtuka. Pengine wazazi wake walikuwa wamerejea.

Basi haraka, akaenda kwenye mlango wa stoo na kuchungulia akiwa anaomba ujio huo uwe ni wa Fanty. Moyo wake ulikuwa unaenda mbio kuliko kawaida. Alianza kujuta kwanini alienda kule stoo.

Kwa macho yake akamwona baba na mama yake wakiwa juu ya farasi wanajongea kuja zilipo stoo. Huko ndipo banda la farasi lilipo. Akapata woga pengine wanaweza kuingia stoo ama kutuma vijakazi wachote nyasi kwa ajili ya farasi.

Hapo ndipo itajulikana kuwa yupo humo.

Atasema alikuwa anafuata nini mule? Akachanganyikiwa. Alifahamu wazi wazazi wake watajua lengo lake lilikuwa ni kutafuta kile Oragon na Ottoman walicholeta.

Hawakuwa wajinga kutolitambua hilo.

Moyo wake ukazidi kwenda mbio kadiri wazazi wake walivyojongea. Akajificha kwenye manyasi akiomba asikamatwe na huku akijilaumu kwa kujitakia shida.

Wazazi wake wakawafungia farasi wao, kisha Melkizedek akamtala kijakazi awalishe farasi hao mara moja. Kijakazi akatii agizo hilo na akazama stoo kuchukua manyasi.

Mbaya akaingia stoo aliyokuwamo Tattiana! Mwanamke huyo akajikunyata apotelee nyasini. Kijakazi akanyofoa nyasi kwa wingi kuzijaza mikononi, kabla hajaondoka, akaona viatu vya mtu.

Akashtuka.

Akazimwaga nyasi pembeni na kutazama viatu hivyo. Akagundua kuna mtu hapo. Mara Tattiana akajitokeza akiwa anavuta hewa kana kwamba ametoka chini ya maji.

"Binti wafanya nini nyasini huku stoo?" Kijakazi akauliza kwa kustaajabu. Tattiana akamsihi apunguze sauti yake.

Kisha kabla hajajibu, akanyanyuka na kwenda kuchungulia wazazi wake kama wameenda ndani. Hakuwaona. Akamtazama kijakazi na kumwambia asimwambie yoyote yule juu ya tukio lake la kukutwa nyasini.

"Sawa?" Akamtolea macho kijakazi, kisha upesi akazama ndani.

Akaenda kuketi sebuleni akiwa mwenyewe akizuga kuwa na kikombe cha kunywa maji. Ndani ya muda mfupi mama akatokea chumbani mwa Tattiana na kumwona binti huyo sebuleni.

Mama akajongea kumfuata akiwa analinyanyua gauni lake refu rangi ya samawati. Alikuwa anatembea kwa maringo kama msichana wa juzi. Akaketi na kusalimiana na mwanaye.
"Ulikuwa wapi?" Mama akauliza.

Tattiana akatabasamu kiuongo.

"Nilikuwa nipo ndani, tumepishana kidogo tu," Tattiana akajibu. Mama akamtazama kwa jicho la mashaka.

Uso wake ulitosha kuonyesha hakumwamini Tattiana. Lakini hakubangaiza kumlazimisha aseme kweli, akatabasamu.

"Ni vema. Tuliondoka asubuhi ukiwa bado umelala. Tuliona usumbufu kukuamsha."

"Mlienda wapi?"

"Kuonana na baadhi ya wafanyabiashara ... makubaliano kadhaa kadhaa, si unajua."

"Mlienda na Fanty?"

"Ndio. Unajua tunamuandaa kuwa mrithi wa biashara zetu. Anatakiwa kuanza kuvaa hivyo viatu sasa."

"Na vipi kuhusu mimi? Hamna mpango huo?"

Mama akatabasamu.

"Wewe unaenda kuwa mke wa mfalme, si mfanyabiashara."

Tattiana hakusema kitu. Alikabwa na fikira kadhaa kichwani. Ulimi wake ulikuwa mzito kunena. Hakuwa na tabasamu usoni.

"Unahitaji kujifunza siasa," mama akamwambia. "Upate kujua namna gani siasa za kila himaya zilivyo ili umsaidie mfalme kutawala."

Bado Tattiana akawa kimya. Mama yake akanyanyuka, akamtazama na kisha kwenda zake chumbani pasipo kumuaga.

"Hatakiwi aendelee kukaa hapa," mama akasema akiufunga mlango wa chumbani. Melkizedek alikuwa ameketi kitandani.

"Kadiri atakavyokaa hapa, na matatizo yatakuja," mama aliendelea kuongea, ila Melkizedek akiung'ata ulimi wake.

"Ameenda leo kupekua kule stoo, ni wazi alikuwa anatafuta ule mzigo. Kama usingekuwa umesafirishwa asubuhi ya mapema, angeuona!"

"Umejuaje alienda huko?" Melkizedek akauliza.

"Nywele zake zimejaa nyasi za farasi!" Mama akajibu akiketi kitandani.

"Hatujui ni lini pia kaka yake atamweleza. Najua Fanty hataweza kukaa na kitu hiki kifuani kwa muda mrefu."

Melkizedek akashusha pumzi ndefu. Akakuna ndevu zake akiwaza.
"Sasa tunafanyaje?" Akauliza.

"Inabidi Tattiana aende kwenye hekalu la mfalme akaishi huko," mama akapendekeza. "Hiyo ndiyo njia pekee itamweka Tattiana mbali na hapa lakini kwa wakati huo karibu zaidi na mfalme."

"Unadhani inawezekana?" Melkizedek akamtazama mkewe.

"Ndio inawezekana!" Mama akajibu kwa kujiamini. "Tumtumie yule mzee, atalifanyia wepesi."

Melkizedek akashika kichwa chake kama dafu. Hakupenda hili wazo.

***

Katikati ya usiku wa manane...

Baada ya kuota ndoto mbaya ya kutisha, Phares akashtuka akiwa anahema kwanguvu! Alikuwa kifua wazi, shuka akiwa amelitupia kando.

Akatazama kushoto na kulia kwake. Chumba kizima hakikuwa na mtu isipokuwa yeye. Punde mlango ukafunguliwa akaingia mwanajeshi akiwa ameelekezea mkuki mbele.

Akamuuliza mfalme kama kuna shida. Mfalme akamweleza ilikuwa ni ndoto tu, hakuna cha ziada.

"Mfalme wangu, una uhakika?"

"Ndio, hakika. Nashukuru."

Mwanajeshi yule kwa mashaka, akaushika mlango aufunge kwenda zake lakini mfalme akamwita na kumshirikisha juu ya ndoto yake.

"Unajua maana yake ni nini?" Mfalme akamuuliza kijakazi wake huyo ambaye naye alikuwa amepigwa na butwaa la hofu.

"Hapana, mfalme, sitambui maana yake," akajibu kijakazi. "Ila itakuwa na maana nzito sana, ni kheri ukawashrikisha wazee wa baraza wanaweza wakakupa neno," akashauri.

Mfalme akapendezwa na wazo hilo, akamshukuru kijakazi wake na kumtaka aendelee na kazi zake kama ada. Akabaki mwenyewe chumbani.

Akaendelea kutafakari juu ya ndoto ile kiasi kwamba mpaka kunakaribia kukucha ndipo akapata usingizi. Alipoamka akawapa ujumbe watumishi wake kwenda kuwaita wazee wa baraza waje hekaluni mara moja.

Baada ya nusu saa, wazee wakawa wamewasili, watano kwa idadi, wakiwa na hamu ya kujua kilichomo ndani ya wito huo wa ghafla.

***
 
*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 30*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Mfalme akapendezwa na wazo hilo, akamshukuru kijakazi wake na kumtaka aendelee na kazi zake kama ada. Akabaki mwenyewe chumbani.

Akaendelea kutafakari juu ya ndoto ile kiasi kwamba mpaka kunakaribia kukucha ndipo akapata usingizi. Alipoamka akawapa ujumbe watumishi wake kwenda kuwaita wazee wa baraza waje hekaluni mara moja.

Baada ya nusu saa, wazee wakawa wamewasili, watano kwa idadi, wakiwa na hamu ya kujua kilichomo ndani ya wito huo wa ghafla.

ENDELEA

"Nimewaita hapa maana nimeota ndoto kuu ya kutisha. Nami najua ninyi ni wazee, mmeona mengi, hamuwezi mkakosa neno," Phares akafungua kikao kwa haja yake.

Alikuwa ameketi mbele kabisa wakati wazee wa baraza wakiwa wameizingira meza kumtazama. Juu ya meza kulikuwa kuna matunda ya kila aina, pamoja pia na divai. Nyuma ya wazee hao walikuwa wamesimama vijakazi wakingojea kuagizwa ama kuhudumia.

Phares akiwa na hisia kali, akaanza kupambanua ndoto yake. Ameota ndani ya usiku wa giza totoro, akiwa amelala usingizi mzito, akasikia kelele kali toka nje ya hekalu lake.

Akakurupuka kwa hofu, na moja kwa moja akawaza pengine kuna vita imejiri.

Basi kabla hajafanya jambo, mlango wake ukafunguliwa na mwanajeshi wake akazama ndani. Akiwa ana sura yenye hofu, akamwambia wamevamiwa! Na afanye haraka amtoroshe kabla hajatiwa nguvuni.

Hakuwa na muda wa kujiuliza. Mwanajeshi wake akamnyaka mkono na kumkimbizia nje. Huko akaona anga likiwa jeusi ti! Na sasa sauti za yowe na makelele zikivuma huku na huko kwa karibu masikioni mwake.

Ajabu ni kwamba kila alipomuuliza mwanajeshi wake wamevamiwa na nani, hakusema, akazidi tu kusihi waondoke eneo hilo haraka iwezekanavyo.

Wakampanda farasi na kwenda mbio mno. Wakiwa wameliacha jengo kwa mbali, akakunja shingo kutazama nyuma. Ajabu, akaona jengo likimezwa na rundo kubwa la ndege, ambao moja kwa moja aliwafahamu ni popo.

Akiwa kwenye bumbuwazi hilo, mara akashangazwa, hata mbele yake, kufumba na kufumbua, rundo kubwa la popo likaibuka na kuwameza!

"Ikawaje?" Akauliza mzee mmoja kwa shauku. Phares akameza kwanza mate kabla ya kuendelea kusimulia.

Hakujua kilichotukia ni nini baada ya hapo, ila alistaajabu akija kuupata ufahamu akiwa mwenyewe. Amebaki na nguo za ndani tu! Alikuwa mchafu mno, hatamaniki.

Akaangaza huku na huko, hakuona kitu wala yeyote. Goshen ilikuwa imegeuka nusu jangwa. Alipotembea, akaishia kuona mifupa ya watu ikiwa imezagaa.

Akahofu.

Hata jengo lake la kifalme kilikuwa limegeuka kuwa ghofu. Mito ilikuwa inatiririsha damu na mabwawa yakiwa yananuka kifo.

Miti ilikuwa imekauka. Nyasi zimekuwa za njano. Huku na kule kulikuwa kumepatapakaa mabaki ya miili ya watu, haikuwezekana kukanyaga ardhi kwa hatua tatu!

Akashangazwa. Ni kwa muda gani mambo hayo yametukia? Mbona yanaonekana yamechukua karne ilhali alifumba na kufumbua tu macho?

Akiwa bumbuwazini, mara akaona tena kundi la popo angani. Akakimbia kwa nguvu zake zote lakini hakufanikiwa, akamezwa tena na popo hao lukuki!

Akatokomea kizani.

Aliporudi kwenye mwanga, ndipo akawa amekurupuka kuamka.

"Sasa ndoto hii maana yake nini?" Akauliza.

Wazee wakatazamana kwa nyuso za bumbuwazi.

"Bila shaka janga kubwa laja!" Akasema mzee mmoja. "Nashauri tuchukue hatua za haraka."

"Hatua zipi hizo?" Akauliza mzee mwingine. Alikuwa ni Baba yake na Oragon na Ottoman. "Hatua zitakuja baada ya kujua tatizo. Tulijue kwanza ndipo tutafute namna ya kulikabili."

"Lakini popo si ishara nzuri kabisa," akasema mzee mwingine. Yeye alikuwa ni mzee zaidi kuliko wote. "Popo humaanisha giza maana huishi nyakati za usiku. Popo humaanisha kisanga maana ni ndege na wakati huo huo mnyama anayebeba mimba!

Nakumbuka, kipindi cha mfalme Gayun, aliota popo ndani kwake. Hakudumu hata siku mbili, akaumwa ugonjwa wa ajabu, akafa akiwa amekakamaa. Baadae tukaja kugundua kumbe kilikuwa ni kisasi cha Jayit kwani mfalme Gayun alikuwa amedhamiria kuivamia Devonship."

Mada ikawa moto zaidi. Lakini ubaya hamna yeyote miongoni mwao aliyefanikiwa kutoa maelezo ya kueleweka. Basi mfalme akatoa kazi kwa wazee hao kusaka majibu ya ndoto yake hiyo ndani ya siku mbili.

Kwa atakayefanikiwa, basi atapewa zawadi nono. Lakini pia kwa atakayefikisha taarifa za uongo, ataadhibiwa vikali! Kikao kikafungwa kila mtu akiwa ana hamu na zawadi hiyo ya mfalme. Lakini pia wakiwa na hofu na mkono mzito wa adhabu.

Isipokuwa baba yake Oragon tu.

Yeye aliamini zawadi hiyo likuwa ni ya kwake. Aliapia ndani ya moyo wake lazima aipate kwa njia yoyote ile.

Ya kheri ama ya shari!

***

Joto lilikuwa kali mno!

Hakukuwa na dalili zozote za upepo wala mawingu angani. Anga lilikuwa la bluu na katikati yake likiwa limesimama jua linalomimina miale kwa fujo.

Hakukuwa na mti wa kujikingia kivuli wala ukuta wa kuuegemea. Hakukuwa hata na tone la maji ardhini, wala mmea wowote uliochipukia.

Palikuwa panatisha.

Palikuwa ni jangwa la kifo mezani! Ndani ya jangwa hili, mtu alikuwa anakamuliwa haswa maji yote mwilini na jua kali kisha anaachwa chini amekauka kama mbao!

Ndani ya jangwa hili, hauwezi kutembea zaidi ya nusu saa. Mwili unakuwa upo hoi mno kupambana na mchanga wa jangwa wenye kina kirefu.

Ndani ya jangwa hili, haikuwa inawezekana kuona mbele zaidi ya hatua thelathini. Utaona maruweruwe kwa mvuke wa jua.

Ndani ya jangwa hili, ndipo walikuwamo Malkia na wenziwe!

"Haya maji hayawezi yakatutosha kabisa kabisa," alisema Seth aliyekuwa mgongoni mwa farasi akiwa anatazama vijidumu vidogo walivyokuwa wamebebelea.

Wenzake wote walikuwa wanatembea kwa miguu isipokuwa yeye kwasababu ya majeraha.

Majasho yalikuwa yanawatiririka, na vinywa vyao vilikuwa vikavu kama pamba. Macho yao yalionyesha wapo hoi. Mwendo wao haukuwa na nguvu ndaniye.

Kulikuwa kimya akosekane hata wa kumwongelesha Seth. Kila mtu alikuwa anapambana na hali yake.

Wakatembea kwa dakika kadhaa, lakini ghafla Fluffy akadondoka chini kama mzigo! Wakatahamaki. Wakamjulia hali lakini mwanamke huyo alikuwa hawezi hata kuongea.

Wakamnywesha maji kulainisha koo lake kavu. Lakini bado hakuwa na nguvu ya kusema kitu. Macho yake yalikuwa yanaeleaelea kama mtu aliyebwia mihadarati.

Basi Ghaut, jitu la Azeth, likamnyanyua mwanamke huyo na kumpakiza kwenye mgongo wa farasi wa Malkia, wakaendelea na safari.

"Tumechoka. Inapasa tupumzike," alisema Zura kwa sauti kavu.

"Lakini tutapumzikia wapi wakati kote ni juani?" Akauliza Malkia. Wakaangaza huku na huko, huku na huko.

"Kule!" Seth akaponyooshea kidole upande wake wa mashariki. "Kutakuwa kuna mapango katika ile miamba. Twendeni!"

Hakuna aliyebishia wazo lake. Wakaongozana kwenda huko. Kweli wakakuta mapango, hatimaye wakapumzisha miili yao dhidi ya jua lenye hasira.

Wakanywa maji kidogo kidogo kulowanisha tu vinywa.

Basi kwasababu za uchovu, wakapitiwa na usingizi.

Lakini je, makazi haya waliyoyapata. Hayakuwa na wenyewe? Ni kweli waliyakuta matupu yaliyokaa hapo kwa bahati tu?

***
 
Shunie mama ungeongeza km viwili kufidia pengo LA Steve!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom