*MKUFU WA MALKIA WA GOSHEN -- 30*
*Simulizi za series*
ILIPOISHIA
Mfalme akapendezwa na wazo hilo, akamshukuru kijakazi wake na kumtaka aendelee na kazi zake kama ada. Akabaki mwenyewe chumbani.
Akaendelea kutafakari juu ya ndoto ile kiasi kwamba mpaka kunakaribia kukucha ndipo akapata usingizi. Alipoamka akawapa ujumbe watumishi wake kwenda kuwaita wazee wa baraza waje hekaluni mara moja.
Baada ya nusu saa, wazee wakawa wamewasili, watano kwa idadi, wakiwa na hamu ya kujua kilichomo ndani ya wito huo wa ghafla.
ENDELEA
"Nimewaita hapa maana nimeota ndoto kuu ya kutisha. Nami najua ninyi ni wazee, mmeona mengi, hamuwezi mkakosa neno," Phares akafungua kikao kwa haja yake.
Alikuwa ameketi mbele kabisa wakati wazee wa baraza wakiwa wameizingira meza kumtazama. Juu ya meza kulikuwa kuna matunda ya kila aina, pamoja pia na divai. Nyuma ya wazee hao walikuwa wamesimama vijakazi wakingojea kuagizwa ama kuhudumia.
Phares akiwa na hisia kali, akaanza kupambanua ndoto yake. Ameota ndani ya usiku wa giza totoro, akiwa amelala usingizi mzito, akasikia kelele kali toka nje ya hekalu lake.
Akakurupuka kwa hofu, na moja kwa moja akawaza pengine kuna vita imejiri.
Basi kabla hajafanya jambo, mlango wake ukafunguliwa na mwanajeshi wake akazama ndani. Akiwa ana sura yenye hofu, akamwambia wamevamiwa! Na afanye haraka amtoroshe kabla hajatiwa nguvuni.
Hakuwa na muda wa kujiuliza. Mwanajeshi wake akamnyaka mkono na kumkimbizia nje. Huko akaona anga likiwa jeusi ti! Na sasa sauti za yowe na makelele zikivuma huku na huko kwa karibu masikioni mwake.
Ajabu ni kwamba kila alipomuuliza mwanajeshi wake wamevamiwa na nani, hakusema, akazidi tu kusihi waondoke eneo hilo haraka iwezekanavyo.
Wakampanda farasi na kwenda mbio mno. Wakiwa wameliacha jengo kwa mbali, akakunja shingo kutazama nyuma. Ajabu, akaona jengo likimezwa na rundo kubwa la ndege, ambao moja kwa moja aliwafahamu ni popo.
Akiwa kwenye bumbuwazi hilo, mara akashangazwa, hata mbele yake, kufumba na kufumbua, rundo kubwa la popo likaibuka na kuwameza!
"Ikawaje?" Akauliza mzee mmoja kwa shauku. Phares akameza kwanza mate kabla ya kuendelea kusimulia.
Hakujua kilichotukia ni nini baada ya hapo, ila alistaajabu akija kuupata ufahamu akiwa mwenyewe. Amebaki na nguo za ndani tu! Alikuwa mchafu mno, hatamaniki.
Akaangaza huku na huko, hakuona kitu wala yeyote. Goshen ilikuwa imegeuka nusu jangwa. Alipotembea, akaishia kuona mifupa ya watu ikiwa imezagaa.
Akahofu.
Hata jengo lake la kifalme kilikuwa limegeuka kuwa ghofu. Mito ilikuwa inatiririsha damu na mabwawa yakiwa yananuka kifo.
Miti ilikuwa imekauka. Nyasi zimekuwa za njano. Huku na kule kulikuwa kumepatapakaa mabaki ya miili ya watu, haikuwezekana kukanyaga ardhi kwa hatua tatu!
Akashangazwa. Ni kwa muda gani mambo hayo yametukia? Mbona yanaonekana yamechukua karne ilhali alifumba na kufumbua tu macho?
Akiwa bumbuwazini, mara akaona tena kundi la popo angani. Akakimbia kwa nguvu zake zote lakini hakufanikiwa, akamezwa tena na popo hao lukuki!
Akatokomea kizani.
Aliporudi kwenye mwanga, ndipo akawa amekurupuka kuamka.
"Sasa ndoto hii maana yake nini?" Akauliza.
Wazee wakatazamana kwa nyuso za bumbuwazi.
"Bila shaka janga kubwa laja!" Akasema mzee mmoja. "Nashauri tuchukue hatua za haraka."
"Hatua zipi hizo?" Akauliza mzee mwingine. Alikuwa ni Baba yake na Oragon na Ottoman. "Hatua zitakuja baada ya kujua tatizo. Tulijue kwanza ndipo tutafute namna ya kulikabili."
"Lakini popo si ishara nzuri kabisa," akasema mzee mwingine. Yeye alikuwa ni mzee zaidi kuliko wote. "Popo humaanisha giza maana huishi nyakati za usiku. Popo humaanisha kisanga maana ni ndege na wakati huo huo mnyama anayebeba mimba!
Nakumbuka, kipindi cha mfalme Gayun, aliota popo ndani kwake. Hakudumu hata siku mbili, akaumwa ugonjwa wa ajabu, akafa akiwa amekakamaa. Baadae tukaja kugundua kumbe kilikuwa ni kisasi cha Jayit kwani mfalme Gayun alikuwa amedhamiria kuivamia Devonship."
Mada ikawa moto zaidi. Lakini ubaya hamna yeyote miongoni mwao aliyefanikiwa kutoa maelezo ya kueleweka. Basi mfalme akatoa kazi kwa wazee hao kusaka majibu ya ndoto yake hiyo ndani ya siku mbili.
Kwa atakayefanikiwa, basi atapewa zawadi nono. Lakini pia kwa atakayefikisha taarifa za uongo, ataadhibiwa vikali! Kikao kikafungwa kila mtu akiwa ana hamu na zawadi hiyo ya mfalme. Lakini pia wakiwa na hofu na mkono mzito wa adhabu.
Isipokuwa baba yake Oragon tu.
Yeye aliamini zawadi hiyo likuwa ni ya kwake. Aliapia ndani ya moyo wake lazima aipate kwa njia yoyote ile.
Ya kheri ama ya shari!
***
Joto lilikuwa kali mno!
Hakukuwa na dalili zozote za upepo wala mawingu angani. Anga lilikuwa la bluu na katikati yake likiwa limesimama jua linalomimina miale kwa fujo.
Hakukuwa na mti wa kujikingia kivuli wala ukuta wa kuuegemea. Hakukuwa hata na tone la maji ardhini, wala mmea wowote uliochipukia.
Palikuwa panatisha.
Palikuwa ni jangwa la kifo mezani! Ndani ya jangwa hili, mtu alikuwa anakamuliwa haswa maji yote mwilini na jua kali kisha anaachwa chini amekauka kama mbao!
Ndani ya jangwa hili, hauwezi kutembea zaidi ya nusu saa. Mwili unakuwa upo hoi mno kupambana na mchanga wa jangwa wenye kina kirefu.
Ndani ya jangwa hili, haikuwa inawezekana kuona mbele zaidi ya hatua thelathini. Utaona maruweruwe kwa mvuke wa jua.
Ndani ya jangwa hili, ndipo walikuwamo Malkia na wenziwe!
"Haya maji hayawezi yakatutosha kabisa kabisa," alisema Seth aliyekuwa mgongoni mwa farasi akiwa anatazama vijidumu vidogo walivyokuwa wamebebelea.
Wenzake wote walikuwa wanatembea kwa miguu isipokuwa yeye kwasababu ya majeraha.
Majasho yalikuwa yanawatiririka, na vinywa vyao vilikuwa vikavu kama pamba. Macho yao yalionyesha wapo hoi. Mwendo wao haukuwa na nguvu ndaniye.
Kulikuwa kimya akosekane hata wa kumwongelesha Seth. Kila mtu alikuwa anapambana na hali yake.
Wakatembea kwa dakika kadhaa, lakini ghafla Fluffy akadondoka chini kama mzigo! Wakatahamaki. Wakamjulia hali lakini mwanamke huyo alikuwa hawezi hata kuongea.
Wakamnywesha maji kulainisha koo lake kavu. Lakini bado hakuwa na nguvu ya kusema kitu. Macho yake yalikuwa yanaeleaelea kama mtu aliyebwia mihadarati.
Basi Ghaut, jitu la Azeth, likamnyanyua mwanamke huyo na kumpakiza kwenye mgongo wa farasi wa Malkia, wakaendelea na safari.
"Tumechoka. Inapasa tupumzike," alisema Zura kwa sauti kavu.
"Lakini tutapumzikia wapi wakati kote ni juani?" Akauliza Malkia. Wakaangaza huku na huko, huku na huko.
"Kule!" Seth akaponyooshea kidole upande wake wa mashariki. "Kutakuwa kuna mapango katika ile miamba. Twendeni!"
Hakuna aliyebishia wazo lake. Wakaongozana kwenda huko. Kweli wakakuta mapango, hatimaye wakapumzisha miili yao dhidi ya jua lenye hasira.
Wakanywa maji kidogo kidogo kulowanisha tu vinywa.
Basi kwasababu za uchovu, wakapitiwa na usingizi.
Lakini je, makazi haya waliyoyapata. Hayakuwa na wenyewe? Ni kweli waliyakuta matupu yaliyokaa hapo kwa bahati tu?
***