SEHEMU YA TISINI NA NNE
Asubuhi na mapema Samson aliamka mapema lengo aanze kazi ili walau kujiweka kwenye mazingira mazuri asije akaonekana huwa mvivu, lakini baada ya kutoka nje alishangaa kumuona Mama yake mzazi akiwa ameshaamka, wakiwa na dada wa kazi Sarah wakitimiza majukumu ya kazi asubuhi ile.
Mama shikamoo, mbona umeamka mapema sana, ni Bora ungeendelea kupumzika tu hizi kazi tutafanya Mimi na aunt Sarah. aliongea Samson akishangazwa namna mama yake alivyojihimu.
Haina shida mwanangu wala hakuna maana kulala wakati tayari kumekucha, nimeona ni afadhali niamke tu, lakini mwanangu Jana Kuna kauli nimeisikia toka kwa shemeji yangu (Mzee Mgaya)japokuwa alikatishwa na mkewe lakini tayari nilimwelewa,
Wanasema yule mtoto wa yule Binti ni wa kwako? unajua haya masuala yamesababisha nikose usingizi kabisa kwani Kila nikiwaza nimekosa majibu. Najua nitaambiwa lakini wewe ni mwanangu napaswa nikusikilize kwanza wewe.
aliweka kituo mama mzazi wa Samson huku akimwangalia Samson Kwa kumkazia macho.
Wanasema ni mtoto wangu ila Mimi naendelea na masomo yangu kama kawaida. alijibu kifupi Samson.
(Mama yake Sam akacheka kwa kumuhudumia mwanaye) Kisha akaendelea....
Wanasema akina nani, kwahiyo wewe huna uhakika kama ni mwanao? Hivi wewe mtoto mbona unakosa akili timamu ya kulinganisha maisha haya ya wenzetu na maisha ya kule kijijini kwetu.
Halafuuuu mmmmh nashindwa kuelewa kwakweli, kwanza Kuna barua tulipokea tangu mwezi wa tisa kuhusu malalamiko ya huyu Mama lakini hatukuitilia maanani tukahisi labda ni mgongano wa kawaida na hata nilivyoambiwa nije nilipuuza.
Lakini pia mwezi wa kumi na moja tulipokea simu kutoka kwa baba yako mkubwa Mzee Mgaya, kiukweli masikitiko yaliyoandikwa mule yalitunyong'onyesha kiasi cha baba yako kuniruhusu nije maana yeye kabanwa na shughuli za shamba. lakini tayari mwanga nimeshapata , halafu wewe unaniambia eti wao wanasema kuwa ni mtoto wako kwakuwa wewe hujui siyo.
Mama yake Sam aliongea kiasi cha kuifanya sauti iwe juu, ila Samson alimsihi mama yake atulie.
Heeeeh shoga yangu mbona mapema tena, kwanza habari za uchovu, nilitegemea ulale dada yangu lakiniiiiiiii... alishindwa kumalizia sentensi yake Mama Kulwa huku akijifunga nguo zake vizuri.
Hakuna haja ya kufanya kazi dada yangu wewe, wewe pumzika tu tunaye mtu ambaye yupo kwa kazi za hapa. aliongea mama Kulwa na kuingia na mgeni ndani.
Samson alibaki nje, huku akiwa na wasiwasi fulani juu ya maneno ya mama yake mzazi, aliendelea na mishe zake huku akiwa ana hamu ya kumuuliza mama yake habari za kijijini japo alijua mama akipata full mkanda wa habari zake, basi amani itapotea.
Breakfast time ilifika huku watu wote wakiungana kwenye meza moja, kasoro mama Kulwa na mama yake Samson ambao walikuwa pamoja muda wote wakiongea na kucheka mambo fulani huku Samson akitamani angekuwepo mahali walipo ili asikie kinachoongelewa lakini haikuwezekana.
Hebu toa hivyo vyombo, siyo kila kitu afanye Sarah wakati mwingine inabidi wewe mwenyewe ujue Nini unapaswa ufanye acha kuwa mvivu.
Mzee Mgaya aliongea kwa ukali kiasi cha kumshangaza Samson akitaka kujua Nini kinaendelea.
Baada ya muda watu wote walikuwa pale sebuleni wakiwa na kikao cha dharula ambacho kiliitishwa na mzee Mgaya kwaajili ya kumweleza mgeni tabia za mwanaye Samson.
Kwanza nikushukuru kwa mara nyingine shemeji yangu kwa kuacha shughuli zako na kuamua kuja kuitika wito wetu hakika ni jambo zuri sana, lakini moja kwa moja kwakuwa ni haraka kidogo ningeomba mke wangu aeleze kile alichodai Jana si vizuri kukwambia lakini nadhani huu ni muda sahihi kuweza kufahamu mambo ya kijana wetu.
Mzee Mgaya alifungua kikao kile.
Unaelekea mwaka wa nne tangu tumpokee huyu mtoto, lakini alivyonikinai utasema tumekaa naye miaka zaidi ya kumi,
Samson ni kijana mpole tu ukimwangalia lakini ni mtu mwenye kujisahau sana, ni mtoto ambaye anaweza kurudia kosa moja zaidi ya mara tano kwa muda mfupi, mwaka wa kwanza nilikaa naye miezi michache lakini tukakosana, ikabidi aende kwa mke mwenzangu ambako Nako kulimshinda akaona ni nafuu hapa kwangu, lakini kosa kubwa alilofanya ni kutuletea hiki kiumbe ,
Hakika ni dharau kubwa na aibu aliileta kwenye familia hii, nadhani mengi nimekueleza lakini si vibaya nikarudia.
Kutokana na kuwa ni mzazi wa kwanza huyu Binti alininyanyasa sana kiasi cha Mimi kusitisha baadhi ya kazi zangu yote kuhakikisha afya na usalama wa huyu Binti.
Kweli kuishi kwingi ni kuona mengi, na mambo nimeyaona , Samson amenipa somo nimelea watoto wangu mpaka Sasa ni wakubwa Lakini hawajawahi kuwa na makosa ya kujirudiarudia kama huyu.
Nimegeuka mlezi wa mtoto maana kama unavyomuona huyu Binti umri wake, hajafikia kutambua dalili zozote za mtoto kuwa kwasasa anataka nini au nini, mtoto akilia na yeye analia kwahiyo unajua jinsi gani nahitaji kuwa karibu na huyu Binti,
aliweka kituo mama Kulwa.
Kisha mama yake Samson akajibu.....
Na Mimi nawashukuru kwa kuweza kukaa na huyu kijana mpaka Sasa, lakini niwashukuru zaidi kwa uvumilivu wenu juu ya yote yaliyojitokeza kwa huyu (akitaja tusi)
Mmeweza kudharau na kukuta ni lazima muishi naye japo kwa kumsukuma, Kisha akamgeukia Samson,
Kwani mwanangu una malengo gani mpaka muda huu maana tabia na mwenendo wako umenistua na umetutia aibu Mimi na baba yako tuonekane tulikulea vibaya kiasi cha wewe kuwa si mwenye kusikia, je una mawazo gani juu ya hatma yako?
mama Samson aliuliza.
Mimi nitaendelea na shule kama kawaida Sina mpango wala njia nyingine zaidi ya kuwaza shule, kwani tayari nawashukuru walezi wangu wameweza kunitafutia shule nzuri ambayo itanikuza kitaaluma.
alijibu kiufupi Samson.
Siyo shule ambayo itakukuza kitaaluma, ni kwamba tuligundua shule unayosoma hutakiwi na ndiyo maana tukaamua kukuhamisha mapema vinginevyo ungefukuzwa kabisa. dada yangu, mwanao tabia yake imeenea mtaa mzima kwanza hakuna anayemtaka kuanzia huko shuleni kwao, walimu hawampendi kutokana na tabia zake Lakini yote hayo sisi tulisamehe na kuchukulia kama ni ya kawaida. alidakia mama Kulwa.
***************************************
Samson baada ya kusoma nyuso za wakubwa wake aliamua kupiga magoti katikati huku akianza kuwaomba msamaha Mzee Mgaya na mkewe kisha akamuinamia mama yake mzazi na kukiri makosa yake yote, huku akiahidi kubadilika.
Jamani binafsi Mimi namsamehe ni kijana, ni mtoto wetu pia ni hatua za makuzi yake , watoto hawawezi kufanana kila mmoja huwa na namna yake ya ukuaji hivyo binafsi nikitakie utekelezaji mzuri kwa uliyoahidi mbele yetu. aliongea Mzee Mgaya huku kauli ikiungwa mkono na watu wote mle ndani.
Baada ya hapo stori za kawaida zilifuata huku furaha, utani na mengine ya kufurahisha yakiendelea huku wakipokezana mtoto wa Rahma Kila saa ila Kila wakikutanisha macho Kati ya Samson na mama yake mzazi, Kuna kitu Samson aligundua mama yake alijikaza tu mbele ya wenyeji wake na lakini inaonesha alikuwa na donge likimkaba akionesha kutoridhishwa na yale aliyoambiwa,na namna yalivyoisha.
Samson na mama waliendelea kukwepana hususan Samson alikuwa anaona aibu hata kumuuliza mama yake habari za kijijini, alitamani afanye hivyo lakini aligundua mama hataki kuongea naye chochote ikabidi afanye habari zake.
Siku iliisha na Samson aliamini Kila kitu kipo sawa, lakini baadaye baada ya kupata chakula cha jioni waligawana vyumba kama kawaida na yeye damson kuingia ndani kwake, lakini baada ya kama masaa mawili huku usingizi Ukiwa unamchukua alisikia mlango ukigongwa, aliamka na kufikiri ni Rahma huku akiwa kashajiandaa kumpa makavu yake kwanini amuaibishe mbele ya uwepo wa mama yake.
Lakini baada ya kufungua alikutana na sura ya mama yake mzazi,
Mama vipi mbona ni usiku Kuna shida gani? aliuliza Samson
Mama hakujibu badala yake aliingia ndani na kufunga mlango Kisha akatoa fimbo yake ambayo inaonesha aliindaa tangu mchana, mfano wa bakora, akaanza kumshushia kipigo Kizito Samson akiwa hachagui pa kupiga licha ya Samson kupiga makelele ya kuomba msamaha na msaada lakini mama yake hakuonesha hata chembe ya huruma , mama Kulwa, Rahma pamoja na Sarah walionesha wameshafika mlangoni na kumsihi mama Samson aamuache mwanaye lakini hakusikia,
Mama mwenye nguvu za kijijini mwenye kutumia jembe la mkono zaidi ya miezi mitatu kuanzia kulima, kupalilia mpaka mavuno, alikuwa akitoa dozi kwa mwanaye ambapo Samson alijikunja mithili ya mtu aliyepoteza tumaini.
Licha ya mama Kulwa kumbembeleza mgeni wake kuwa amuache mwanaye atamuumiza lakini hali ilikuwa mbaya, ni Samson mwenyewe baada ya kugundua kuwa akijilegeza atakufa alifungua mlango kwa taabu huku akikimbilia sebuleni ambapo paji la uso na sehemu zingine za kichwa zilikuwa zikivuja damu. Maana haikuwa fimbo ya kawaida.
Watu wote watatu mama Kulwa, Rahma na Sarah walimwanfalia mama yake Samson kwa uoga huku akiwapita na kuingia kwenye chumba chake huku akimuita mama Kulwa Kwa ishara.
Pole vipi umeumia sana? Au tukupeleke hospital. Rahma alimwambia Sam huku akimfuta damu, na Sarah naye akiwa anafuta damu zilizodondokea sakafuni. Mama yake Sam kuona vile Rahma anamfuta damu Samson, alirudi kwa kasi na kuanza kumshambulia Rahma huku akitoa matusi mazito sana.
Jamani leo imekuwaje na hivi Mume wangu hayupo nawezaje kuituliza hii hali,halafu dada huyu Binti ni mgonjwa mgonjwa hajatengamaa bado utamuumiza.
alilalamika mama Kulwa huku akishindwa la kufanya kumuokoa Rahma ndani ya mikono ya mama yake Samson.