SEHEMU YA SABINI NA SITA
Mama Kulwa aliingiza gari lake ndani Kisha Samson akawa wa kwanza kushuka ili afunge geti kabisa,
Aliingia ndani na huku akishangaa shangaa kama mgeni, wakati huo mama Kulwa hakuongea chochote na Samson akaingia tu chumbani kwake . Samson aliingia ndani kwake na kuweka begi lake chini kabisa kwasababu lilikuwa chafu sana kutokana na misukosuko aliyoipata.
Alirudi pale sebuleni akiwa kama mgeni mpya licha ya njaa kumuandama, lakini hakuthubutu kumuuliza yeyote Wala kulisogelea poti la Chakula kuona kama kuna chochote kitu ili apoze njaa, akabaki katulia tu.huku akishangaa mbona Rahma haonekani lakini hakuwa na jibu ikabidi atulie tu, huku akitafakari juu ya lile tukio ambalo huenda asingekuwepo Duniani maana aliponea kwenye tundu la sindano.
Akiwa kwenye lindi la mawazo huku akiwa hajui kwanini mama Kulwa anamkwepa na kwenda chumbani kwake akasikia honi nje na kwenda kufungua alikuwa ni Mzee Mgaya kushoto akiwa ni Rahma, walishuka huku gari likiachwa nje kabisa ya fence, wakaja ndani huku Mzee Mgaya akipitiliza Moja kwa moja hadi chumbani kwake.
Pole sana Samson, pole kwa yale yaliyokukuta jana, vipi ulilala wapi kwani? Na nimemsikia baba anasema eti polisi walikukamata wakidhani ni mwizi kwani ulifanyaje? aliuliza maswali Rahma huku wakitoka nje ili wawe huru kuongea
Lakini juu ya yote nikupe pole sana hata Mimi nilifukuzwa jana ileile , nashukuru baba alinikuta hapo nje akiwa anatoka kwenye safari yake, ndipo aliponirudisha ndani akauliza sababu ya kufukuzwa, sikumficha nilisema Kila kitu, kwa muda ule alikuwa na hasira sana pengine ungekuwepo angekuumiza sana. Maana alianza kuuuliza uko wapi huku akiingia chumbani kwako kwa kupiga teke mlango, ndipo alipoambiwa umefukuzwa huku akitukana na kusema una bahati na usirudi tena ndani mwake,
Na Mimi nikaambiwa nilale kisha ikifika asubuhi nitafute pa kwenda, lakini ilipofika , alfajiri ya leo nikasikia makelele Kati ya baba na mama huku baba akimwambia mama atoke nje akutafute ulipo, na mama naye akidai atakutafutia wapi kwakuwa hajui ulipoelekea kifupi wamegombana sana, ilipofika asubuhi mama akasema hataki anione ikabidi baba anipeleke kwa mamdogo Tausi ambako Nako nimekataliwa akidai hawezi kuuguza mgonjwa.
Hivyo nilikuwa sehemu tu nimetulia kwa wauza Chakula karibu na pale kwa mamdogo, ni jioni hii nimeshangaa nikiitwa na baba na kuniambia nipande kwenye gari eti mama Kulwa ananiita wakati ni yeye alidai hanitaki. aliweka kituo Rahma.
Wewe Rahma ni mjinga sana, na matatizo yote yaliyonipata chanzo ni wewe kwanini ulinitaja Mimi kwanza una uhakika gani kama ujauzito ni wa kwangu mimi? Ni afadhali ungesingizia kuwa ulibakwa na mtu usiyemfahamu ili utunze siri.aliongea Kwa ukali kidogo Samson.
Weweee ukweli utabaki kuwa ukweli Mimi namuogopa MUNGU licha ya kuwa nimemkosea kwa kuifanya zinaa, lakini aliyenipa ujauzito ni wewe na si mwingine,
Samson, upendo wangu kwako haupimiki haya yaliyotokea ni matunda ya kile ambacho tulionywa kabla , unadhani walezi wetu wangefurahia na kuhalalisha vitendo visivyo vya kimaadili?
Tambua kuwa nakupenda Samson, na najua unanipenda, na tunapendana,Mimi si mwanafunzi kwamba labda umekatisha ndoto zangu, hapana!
Wewe utaendelea na masomo na Kila kitu chako kitakuwa sawa kama ulivyopanga, wewe ni baba mtarajiwa hivyo.............. Kabla hajamalizia sentensi yake Rahma alichapwa kibao.
Yaani wewe sijui nikuiteje, mbona unakuwa kama kichaa namna hii, umeshindwa hata kujua hatari tuliyoitengeneza wewe unataja vitu visivyokuwa na msingi kwanini,
Yaani unawaza juu ya kuzaliwa kwa mtoto usiye na uhakika naye.
Je , umewaza juu ya hatma ya wewe kukaa humu ndani?
Huna hata huruma yaani, unawaza juu yangu baada ya kuvuruga masomo, wazazi wangu ni masikini, angalau nilidhani naweza kuja kuwakomboa kwenye hili janga lakini ndiyo zangu zimefutika , halafu kuanzia leo sitaki unishirikishe juu ya hilo tumbo lako, jua sitaki wa sikuhitaji, aliongea Kwa kujikaza Samson.
Mimi siyo mjinga ila wewe ndiye mjinga kwani ulivyotoka kijijini kwako hukujua kilichokuleta huku,
Unaongea vitu Ukiwa sahihi na Ukiwa timamu ila unasahau kuwa hakuna aliyekushikia panga kunipenda mimi, ulinipenda na kunitamkia wazi unateseka juu yangu, yaani badala uteseke na masomo ujue ni namna gani utaikomboa familia yako kama ulivyosema.
Miezi kadhaa iliyopita nani alikutwa kwenye chumba cha mwenzie , ni Mimi au wewe, jitahidi kuchunga mdomo wako Mimi siyo mtoto mdogo kama wewe. aliongea Rahma huku na yeye akiwa na hasira muda ule ikabidi Samson aondoke, lakini wakati anageuka alishangaa kumuona Mzee Mgaya nyuma yao ambaye anaonekana alisikiliza maongezi yao kwa muda mrefu sana.
Nakuhurumia sana mwanangu, nashindwa kujua una chaguo gani hadi sasa, unachekesha sana juu ya ulichokifanya, sidhani kama una kumbukumbu nzuri sana, halafu mbona ukiambiwa jambo huelewi? unakuwa mwenye kurudia makosa yaleyale kwanini?
Nitawasiliana na wazazi wako ili nijue hatua za ukuaji wako zilikuwaje, isije kuwa nalea mtoto mwenye matatizo ya akili, kwasababu hata usiku wa leo sikulala nikiwaza juu ya mwenendo wako, shida siyo kosa ulilofanya shida ni hali ya kurudia mambo yale yaleyale.
Nina mengi ya kuongea na wewe naijua familia yako, namjua mdogo wangu Elias baba yako wewe, nawajua dada zangu wote asili yetu sisi ni masikini.
Hata mimi bado ni masikini kwakuwa siishi maisha niyatakayo licha ya kuwa ni Mimi pekee niliyebahatika angalau kujaribu kupambana na hawa maadui watatu japo sijafikia hata moja ya kumi siishi maisha wanayoishi watu.
Lakini bado nina nafuu mara mia kuliko yeyote kwenye familia yetu.
aliweka kituo mzee Mgaya. Huku akionesha upole ambao si kawaida yeye kuwa nao.
Samson alipiga magoti kama ishara ya kuomba msamaha na kuonesha kujutia kosa lake lakini Mzee Mgaya akamwambia ainuke huku akimpa swali lingine,
Vipi utaendelea na masomo yako au unawaza nini, au unataka kuwa baba wa familia maana nimemsikia mwenzio anasema wewe ni baba mtarajiwa, aliuliza huku akicheka kivivu Mzee Mgaya.
Kwanza Samson miguu yake ilitetemeka, huku akionesha yupo tayari masomo na asingependa kuwa karibu na Rahma hata kidogo.
Mzee Mgaya akawataka wote waingie ndani, huku mama Kulwa akiamshwa ili aje kwenye kile kikao cha dharula.
Mke wangu kwanza pole sana, ila usiwaze kuhusu yaliyotokea chukulia ni kawaida tu, ni majukumu tumeyabeba wenyewe kwa hiari , kwenye maisha huwezi kuwa sawa kwenye Kila kitu,mambo yenyewe ndiyo haya huyu mtoto ni mjamzito hivyo tuna jukumu la kuhakikisha afya na usalama wake,
Hali kadhalika Samson, tumeshatoa pesa nyingi kwaajili yake, je tunaweza kula ng'ombe mzima ukatushinda mkia? Mzee Mgaya alimuuliza mkewe.
Mama Kulwa hakujibu bali aliitikia kwa kichwa akimaanisha lazima Samson asome.
Hali ya wazazi wake, kuwa wapole vile ni jambo lilimshangaza sana Samson alihisi Kuna kitu kinajificha ambacho hakijui huku akiamini atajua tu kwani wazee wake aliwajua vyema hawawezi kukaa na jambo muda mrefu.
Mzee Mgaya alifunga mjadala huku akimsihi mkewe atulie wala asiwaze badala yake ashukuru MUNGU Kila mtu yupo hai , akatoka huku akimwambia Samson afunge geti kwakuwa hatorudi.
Samson aligundua kuwa mama Kulwa anamkwepa hataki kuwa karibu naye , hakujua sababu ni nini lakini ilikuwa hivyo, aliendelea kutulia pale sebuleni huku Rahma akiwa jikoni akiandaa dinner kwa usiku huo.
Itaendelea....................