SEHEMU YA 73
“Vipi kuna nini?” baba mkwe aliuliza.
“Kawaida tu baba,” mume wangu alijibu.
Mara aliingia bwana mmoja mtanashati aliyekuwa amevaa suti, nilimkumbuka bwana yule alikuwa ni mwana sheria na rafiki ya mume wangu.
“Karibu bwana Swedi.”
“Asante, naona leo matumaini yapo.”
“Siku azilingani.”
“Shikamoo baba, shemeji za siku?”
“Marahaba.”
“Nzuri.”
Baada ya kusalimiana, mume wangu alisema:
“Bwana Swedi nafikiri hatuna muda wa kupoteza tufanye zoezi lile ili uwahi majukumu yako.”
Nilijiuliza zoezi gani linalotakiwa kufanyika muda ule, nilitulia nione mwisho wake.
“Vitu vyote si viko tayari?” Swedi aliuliza.
“Ndiyo,” mume wangu alijibu huku akigeuka na kuchukua bahasha lililokuwa chini ya mto na kumpa.
Baada ya kupitia karatasi zilizokuwa, alimgeukia mume wangu na kusema:
“Nafikiri zoezi lifanyike.”
“Mke wangu, baba,” mume alituita.
Tuliitikia kwa pamoja na kumsikiliza anataka kusema nini.
“Najua hamjui kipi kinatakiwa kufanyika, baada ya kupata nafuu naamini ilikuwa nafasi aliyonipa Mungu ili kuhakikisha mali zangu nazigawa kwa wahusika. Nina imani kila kitu nimeandika kwa akili zangu timamu, unaweza kumpa mke wangu na baba wasome.”
Swedi alitupatia karatasi zilizokuwa zina maelezo ya mume wangu kugawa mali zake, nyumba mbili aliniandikisha mimi na wanaye moja alimuandikisha baba yake. Pia kiwanja kimoja aliniandikisha mimi. Magari matatu aliagiza yauzwe kwa ajili ya kuwasomesha watoto wake na moja ambalo alikuwa amemuazima rafiki yake alimpa baba mkwe.
Baada ya kusoma nilikuwa wa kwanza kuuliza.
“Kwa nini umefanya hivi?”
“Nina sababu yangu, majibu yake utayapata siku chache zijazo.”
“Kwa nini usiniambie leo?”
“Kuwa na subira mke wangu, baba naomba upokee nilichokupa, naheshimu mchango wako katika maisha yangu. Nina imani sasa sitakuwa tena na nguvu za kuweza kutafuta wanangu, nilivyo vigawa ndiyo wanaotakiwa kutazamwa na msimamizi mkubwa ni mama yao.”
“Kwa nini mali zingine hukuacha kwako?” nilimuuliza.
“Naomba swali hili niulize baada ya siku mbili.”
“Mmh! Sawa,” sikuwa na jinsi nilimkubalia.