Simulizi: Kiu ya talaka

Simulizi: Kiu ya talaka

SEHEMU YA 41

"Ni kweli kabisa uyasemayo, lakini mume wangu ameonesha jinsi gani alivyo chukizwa na uamuzi wa baba yake wa kumfukuza mwanamke wake ndani ya nyumba na kuamua kumdharau baba yake kwa kumuondoa mkewe na kumfuata huko aliko mpeleka na yeye kuniachia nyumba.
“Sasa dada inawezekana labda shemeji yako anajua mimi namng’ang’ania kwa ajili ya jumba, la hasha.

Dada nina nyumba mbili, labda utajiri wake. Sikwenda kuomba msaada wa kunioa, pia sikutoka pangoni nitapambana na maisha. Mbona kuna wanamke hawana wanaume na maisha yanasonga?” "Hapana usifanye hivyo, tena ndiyo vizuri kurudi kwa mkweo kumweleza dharau aliyo ionesha mumeo."

"Dada hakuna mapenzi ya kulazimishana kwa sasa mume wangu hana mapenzi na mimi, anaona aibu kumjazia machangudoa na mabaa medi utawaweka wapi? “Kwa hali hiyo siwezi kumlazimisha mume wangu kwa shinikizo la baba mkwe. Kama amemdharau baba yake bado narudi kwao labda lao moja ukali wa baba yake ilikuwa tisha toto."

"Mmh! Sasa mdogo wangu ulikuwa na uamuzi gani?"
"Dada sina jinsi zaidi ya kubwaga manyanga, naomba safari hii niache usiingize mdomo wako kwa kuwa yote umeyashuhudia kwa macho, kama ameshindwa baba yake mkali kama pilipili.

Kama nilivyosema kwanza hata yeye simuamini huenda lao moja hawezi kutoa mkwara mzito mwanaye asishtuke."
"Mmh! Kwa kweli mdogo wangu mpaka hapo uamuzi nakuachia mwenyewe. Yaani kila nikikuangalia nakuonea huruma ukipata mwili kidogo matatizo yanajitokeza.

“Mdogo wangu ndoa umekupurua mwili, mpaka hapo uamuzi nakuachia mwenyewe najua maisha hayatakushinda kwa kuwa ulijiandaa mapema." *** Jioni shemeji mume wa dada aliporudi alielezwa na dada hakusita kunipa pole kwa yote yaliyonisibu na uvumilivu nilio uonesha mwisho alimalizia kwa kusema:

"Unajua umejitahidi na kuyafanyika kazi yote tuliyo kueleza na umeonesha uvumilivu wa hali ya juu, ambao kwa dunia ya leo ni nadra kupatikana kwa wasichana wa sasa.

Umejitahidi vya kutosha kwa kweli ndoa yako imekuwa sawa na sikio la kufa lisilo sikia dawa na siku zote la kuvunda halina ubani na kila chenye mwanzo hakikosi mwisho."
 
SEHEMU YA 42

“Lakini mume wangu ndoa hii imefungwa kanisani?” dada alimkumbusha shemeji aliyekuwa upande wangu.

“Sawa, hii tutaivunja mahakamani, ingekuwa ya kiislamu ingekuwa nyepesi.”
“Itabidi tufanye hivyo mwishowe ndoa hii itamtoa roho. Kila likitoka hili ilinaingia hili mwisho wake nini. Lini mdogo wangu atafurahia ndoa yake?”

dada alisema kwa uchungu. **** Nilikaa kwa dada kwa muda wa wiki nzima huku nikijifikiria kama mume wangu akitokea na kuniomba radhi nitachukua uamuzi gani? Japokuwa moyo wangu haukuwa tayari kumsamehe na kuwa tayari kuishi maisha ya upeke kwa kujua heri maskini huru kuliko tajiri mtumwa.

Lakini moyo wangu uligawanyika pande mbili, upande mmoja haukuwa radhi kumsamehe mume wangu lakini upande mwingine ulikuwa bado ukimuhitaji sana mume wangu.

Hivyo nilijikuta njia panda katika maamuzi yangu pindi atakapotokea mume wangu. Wiki ilikatika bila kuiona sura ya mume wangu, najua alipata taarifa za kuondoka kwangu hata kukataa kuipokea pesa aliyo nitumia kwa matumizi.

Baada ya kuamini mume wangu aliamini shida yangu ilikuwa kula na nyumba, nilikataa msaada wake. Nilipomuomba dereva asiniletee chochote atakachopewa na mume wangu.

Baada ya wiki ya pili kukatika nilihamia kwenye nyumba yangu na kuyaanza maisha yangu mwenyewe. Mwanzo naweza kusema ulikuwa mgumu sawa na kumeza mfupa. Nyumba niliiona kubwa na upweke ulikuwa mara dufu.
Nilipata wakati mgumu sana kwa vile nilikuwa nimezoea kuishi chini ya mtu tena kwa amri.

Amini usiamini maisha yalikuwa magumu sana.Kama mume wangu angetokea kwa muda ule nilikuwa radhi kumsamehe na kurudi kwangu.
Nyumba niliiona kubwa kama bahari japokuwa haikuwa kubwa kama ya mume wangu ambayo iliizidi yangu ukubwa mara nne. Lakini kwa mume wangu nilikuwa na matumaini huenda atatokea.

Moyo wangu taratibu ulianza kupoteza ujasiri, nilijutia uamuzi wangu wa kuondoka bila kusikiliza ushauri wa dada wa kurudisha malalamiko kwa baba mkwe.
Kila alipokaa peke yangu nilipomkumbuka mume wangu. Kila siku nilisali kumuomba Mungu amrudishe mume wangu na kumpa moyo wa mapenzi kwa mkewe.
 
SEHEMU YA 43

Nilitamani nimtafute na kumuomba msamaha ili turudiane hata kwa kukaa nyumba moja na mimi kuwa chini ya mwanamke wake.

Lakini nilishangaa na kujiuliza ni moyo gani dhaifu nilio uonyesha kwa kipindi kifupi.
Nilimuomba Mungu anipe ujasiri ili niweze kumsahau mume wangu hasa ndoto za usiku nilipoota nipo na mume wangu na nilipozinduka usingizini kujikuta peke yangu.

Hapo niliumia mara mbili na kujikuta nalia peke yangu usiku kucha. Asikuambie mtu mazoea ni ugonjwa mbaya sana unaomchukua mtu muda kupona.

Lakini sikuchoka kumuomba Mungu kunipa farijiko kipindi chote kile. Nakiri kilikuwa kipindi kigumu maishani mwangu chenye maumivu makubwa na kuwa na mtihani mzito juu ya uamuzi wangu na kiapo nilicho jiapiza.

Huwezi kuamini kila hodi iliyopigwa nyumbani kwangu niliomba awe mume wangu amekuja kuniomba radhi au kunifuata, lakini wapi. Ile hali ilipozidi ilinifanya nirudi kwa dada kuomba ushauri.

“Dada, mdogo wako nitakufa kwa kihoro, hali ni mbaya sana nyumba yangu mwenyewe naiona kama kaburi. Kwa ajali ya kumkosa mume wangu.
“Naweza kufa kwa presha au kuwa mwendawazimu. Nilifikiri kuondoka ingekuwa afadhali lakini maumivu yamekuwa mara mbili yake.

“Heri nyumbani ningeweza kumuona hata mara moja akija kubadiri nguo. Lakini kwangu sidhani kama atafunga safari, naamini yule mwanamke kamteka mume wangu,” nilijikuta nikilia. "Mdogo wangu pole sana najua kiasi gani unavyoumia hii hali ina tofauti kidogo na dada yako Cathy."

"Samahani dada kwani na da Cathy alifanya nini nakumbuka kuna kipindi alirudi nyumbani, kwa muda aliokaa nyumbani alikonda sana kama mgonjwa wa tibii na kuna siku alinituma nipeleka barua kwa mumewe. “Huwezi kuamini sikukubali kumuacha shemeji kwa hali aliyokuwa nayo dada na kumlazimisha turudi wote..

“Lakini baada ya kurudi kwa mumewe sasa hivi mzima wa afya njema tena amenenepa mpaka amechusha," Nilikumbuka kisa cha dada alichokutana nacho kwenye ndoa yake wakati huo mimi nilikuwa nimemaliza kidato cha tatu.

"Mdogo wangu dada yako naye alikumbana na mazito ukimpigia simu atakueleza mwenyewe kwa ufasaha.
 
SEHEMU YA 44

"Ila nataka nikueleze kitu kimoja, ndoa ni bahati nasibu, kila mmoja kwenye familia yetu ana mitihani yake ya ndoa. Ndio maana nikasema maisha ya ndoa ni nje ndani.Wa ndani wanataka kutoka na waliotoka hawataki kurudi au waliotoka wanatamani kurudi tena.

Vile vile walio nje wanatamani kuingia hata kwa kupitia kwa waganga wa kienyeji."
“Mdogo wangu najua yote yanayokutokea yanatokana na kukaa sehemu moja. Hebu jiweke bize haichukui muda utamsahau mume wako.”

Baaada ya kushauriwa na dada ambao sikukubaliana kwa asilimia mia. Kuanzia hapo nilijishughulisha katika moja ya maduka yangu si kwa kukaa tu bali kuwahudumia, kitu kilichonifanya niwe bize muda wote .

Nilijikuta nakuwa bize muda mwingi na nikirudi nyumbani huwa nimechoka kama mtu aliye kunywa pombe.
Nilipoamka ilikuwa siku ya pili, nilioga na kuelekea kwenye shughuli zangu. Nilianza kwa kuwaacha watoto kwa dada .

Baadaye wanangu niliwatafutia mfanyakazi ambaye aliwalea vizuri.
Mtoto mkubwa nilimpeleka darasa la kwanza na wadogo zake niliwanzisha kindagate. Kila siku walipitiwa na gari la shule na kurudishwa jioni. Ubize wa kujishughulisha na shughuli za dukani ulinifanya nimfute mume wangu taratibu japokuwa ilikuwa kazi kubwa.

Kila ilipoitwa jina linalifanana na mume wangu au kumuona mtu anayefanana naye moyo ulinilipuka. Lakini Mungu alituahidi hakuna mateso yasiyo na mwisho. Ubize ulinifanya nimfute taratibu mume wangu japo si moja kwa moja, nilimkumbuka.

Baada ya duka kupanuka na kuzoeleka na watu wengi. Tulijikuta tunagawana majukumu na mtoto wa dada yangu kwa mimi kujaribu kufuata bidhaa nje ya nchi kwa kusafiri kufuata mizigo ya biashara Dubai na China.

Mungu anaye alileta heri zake biashara zangu zilitanuka na kufungua duka lingine katikati ya mji. Biashara zangu zilitanuka na mambo yalikwenda kama yalivyopangwa bila msaada wa mwanaume.

Huwezi kuamini nilijikuta namsahau kabisa mume wangu na akili yangu yote niliielekeza kwenye biashara. Kipindi kile sikuwa na mawazo ya kutafuta mwanaume, akili yangu yote niliielekeza kwenye maisha yangu japokuwa walitokea wanaume walionitaka kwa gharama yoyote .
 
SEHEMU YA 45:

Nilinenepa na kupendeza, siku moja nikiwa nimeinama dukani kwangu nikipiga mahesabu. Ndani ya duka wateja walikuwa wachache, kutokana na ubize wateja walioingia sikuwaona.

Kila aliyenunua vitu alikuja kulipa kwangu, nikiwa bado nimeinama, msichana wangu wa kazi aliniambia.
“Dada huyo mama atakulipa laki mbili na nusu nimempunguzia elfu ishirini na tano.”

Wakati huo mteja alikuwa ameisha zimeweka fedha mbele yangu. Nilizichukua na kuanza kuzihesabu huku nikinyanyua uso. Nilijikuta nikitazamana uso kwa uso na mwanamke aliyenitoa ndani.

Moyo ulinipasuka kama nimeonana na jini, lakini nilijitahidi kuificha hofu yangu. Naye aliponiona alishtuka mpaka simu aliyoishika mkononi ikamdondoka. Aligeuka na kuchukua vitu vyake bila kusema kitu na kutoka nje ya duka bila kuomba risiti. Sikufanya lolote nilimsindikiza kwa macho mpaka alipotoka nje ya duka.

Nilimtuma msichana wa kazi akamwangalie amekuja na nani. Baada ya muda alinieleza alikuwa mwenyewe, ameingia kwenye gari na kuondoka.
Baada ya kuondoka moyo uliniuma sana na kuona kama amekuja kunitonesha kidonda kilichoanza kupona.

Lazima niseme ukweli yule mwanamke alikuwa amenenepa na kupendeza. Mwilini alikuwa amechafuka kwa vitu vya dhahabu.
Lakini nilimuomba Mungu anipe moyo wa subira na ujasiri ili niweze kuyashinda majaribu yote. ***

Siku nazo zilisonga nami nilijikuta nimeyazoea maisha ya upweke. Siku moja nikiwa nje ya duka langu. Nilishituliwa na mtu aliyeniita kwa jina langu.

“Ni wewe Eliza?” Alipogeuka nilikutana na shoga yangu wa zamani aliyekuwa akiniletea taarifa za mume wangu ambazo nilikataa kuziita umbea kwa sababu zilikuwa na ukweli.
Hakuamini kuniona nipo kwenye hali nzuri aliyonikuta nayo.

“Ha! Shoga ndiyo mimi.” “Hata siamini!” alisema huku akinishangaa.
Niliamini katika akili yake baada ya kuondoka kwa mume wangu alitegemea kunikuta nimekwisha kama sio kubakia mfupa na ngozi kwa ugumu wa maisha na niliyotendewa na mume wangu.
Aliponiona alionekana amepigwa na butwaa na kutoamini macho yake nilimzindua kwa kumwambia.
 
SEHEMU YA 46

Aliponiona alionekana amepigwa na butwaa na kutoamini macho yake nilimzindua kwa kumwambia. "Usishangae shoga ni mimi Eliza Kijoki yuleyule wa zamani."

"Mmh! Siamini kweli Mungu mkubwa na hulipa dunia kabla ya mauti." Kauli ile ilinishtua na kutaka kujua ina maana gani? na kutaka kuja kwa nini amesema vile.

“Kauli yako ina maanisha nini?” "Eliza yaani yote aliyokutendea mumeo yamemtokea puani," kauli ile ilinishtusha zaidi kwa kuogopa mzazi mwenzangu kukutwa na matatizo ambayo yangeiathiri hata familia yangu kwa kujua malezi ya watoto ni wazazi wote hata wakiwa mbali maadamu wazima.
"Mungu wangu! Mume wangu amefanya nini tena?"

"Yaani we’ mtu wa ajabu unamuonea huruma mtu aliyekutenda vile?" shoga yangu alinishangaa.

"Shoga eleza yaliyotaka kuniambia mengine hayakuhusu...Amefanya nini?" nilijikuta nikiwa na hamu ya kujua mume wangu amepatwa na nini japokuwa tumetengana muda mrefu.
"Mbona amekubwa na aibu ya mwaka!"
"Aibu gani hiyo tena?" nilizidi kushtuka na moyo kinienda mbio.

"Mumeo kauziwa mbuzi kwenye gunia!"
"Hebu niweke wazi umekuwa kama umetoka kwenye ngano za kiswahili. Unaniacha njia panda hebu nidadavulie," nilitaka kujua kwa undani.

"Mumeo alipewa mtoto si wake!"
"Si wake una maana gani?"
"Kumbe alilea mimba na mtoto wa mwanaume mwenzake ambaye alikuwa gerezani kwa kufungwa.

“Baada ya kuondoka yule mwanaume kwenda gerezani. Huku nyuma ndipo alipokutana na mumeo na kumbambikia ujauzito ule." Habari zile zilifanya nihisi kama tumbo la kuharisha na kujikuta namuonea huruma mume wangu wadogo zake ambao ni wifi zangu na mama mkwe.

Niliiona picha wakiwa mbele ya baba mkwe wakiomba msamaha huku wakifukuzwa kama mbwa. "Vipi shoga naona umekwenda mbali?"
"Ni kweli habari hizi ni nzito nawaonea huruma watu wazima wameadhirikaje!"
"Basi yule mwanamke nasikia nyumba yake ilikuwa ndiyo inamaliziwa kujengwa.

Ilichelewa kuisha baada ya mumeo kusimamishwa kazi kwa ubadhifu wa fedha kazini kwake, Huwezi kuamini kupata yule mtoto familia ya mumeo ilikuwa kama watumishi wa ndani kwa yule mwanamke walimtetemekea kama Mungu kwa vile kamleta mrithi wa familia .”
 
SEHEMU YA 47

“Mungu wangu!” Nilishtuka na kushika kifuani, nilijikuta nikiumia kama bado tupo nyumba moja.
“ Basi shoga inasemekana mzazi mwenzio aliuliza moja ya gari lake ili amalizie nyumba ya hawala yake.

Kwa bahati nzuri au sijui niseme yule mwanaume alitumikia kifungo kwa miaka miwili na baada ya kukata rufaa na kushinda. Si ndipo aliporudi nyumbani na kumkosa mkewe, alielekezwa na wasamalia wema alipo.

“Ndipo alipokwenda moja kwa moja wanapokaa mumeo. Inasemekana mwanaume alipofika alikuwa mtaarabu hakutaka shari na mtu alimuomba mwanaye ili amuachie mumeo yule mwanamke.

“Hukuwepo malaika wako alikuwepo, hapo ndipo mumeo na mwanamke wake walipoumbuka. Mumeo hakukubali na kuamua kumshtaki yule bwana, kutokana na kuwa na pesa yule bwana alikamatwa na kuwekwa ndani.

“Baada ya yule bwana kusurubiwa bila kosa, ilibidi aseme ukweli wa mambo. Yule bwana, mtoto na mumeo wakaenda kupima damu DNA. Japokuwa picha halisi ilionesha mtoto si wa mumeo, lakini bado alikuwa king’ang’anizi. “Majibu ya vipimo vilikuwa vilevile kuwa mumeo mtoto si wake. Hapo mbona lilipowashuka, nasikia shoga sikuwepo lakini waliofuatilia kwa karibu walipofika nyumbani yule mwanamke alifukuzwa kama mbwa.

“Sasa hivi kuna mtafaruku kati ya mama mkwe na baba mkwe juu ya yale yaliyotokea vilevile sasa hivi wifi zako na mumeo ni chui na paka." "Japokuwa moyo unaniuma lakini hayo ni malipo ya duniani siku zote malipo ni duniani, ahera kwenda hesabu."

"Basi shoga kwa ufupi ni hayo mengine siyajui."
“Kwani balaa hili limewatokea muda gani sasa?”

“Huu unakatika mwezi wa tatu au wa nne. Kweli shoga uko bize, mbona lilikuwa gumzo la mtaa na watu kukuonea huruma kwa kitendo walichokufanyia.”
"Sawa shoga nashukuru kwa yote ila tusamehane kwa yote," nilichukua nafasi ile kumuomba msamaha shoga yangu kutokana na kumfukuza na maneno yake.

"Shoga mbona mimi nilikusamehe mapema, nilijua ulikuwa umechanganyikiwa. Kwanza sikuamini kukutata umetakata kiasi hiki. Nilijua ungekuwa kama mpira wa makaratasi uliochoka."
 
SEHEMU YA 48

"Kila kitu kinapangwa na Mungu, sisi wanadamu hatuyajui ya kesho kama tungejua yatakayo tutokea tungekuwa makini."
"Au umeisha pata mzee mwenzio?" alinichokoza.

"Wala ni kulizika na maisha na kuyasahau yaliyopita." Niliagana na shoga yangu na kuniacha na mawazo mazito kila nilichojiuliza kilikosa jibu.

Nilikuta nikimuonea huruma mume wangu kwa yote yaliyo msibu kwa pigo mujarabu alilolipata kwa kuuziwa mbuzi kwenye gunia kumbe mbwa.

Lakini sikuwahurumia sana kwa kuwa kila mchuma janga hula na wa kwao. Habari zile zilinifanya nikose raha hata sijui kwa nini ziliniweka kwenye hali ile.

Hata hamu ya kufanya kazi ilinishinda na kuamua kurudi nyumbani mapema. Nikiwa nyumbani nikikumbuka walivyo nitenda familia ya mume wangu na aibu iliyowakuta. Nilijua lazima kwa vile nyuso zao hazina haya watakuja kuniomba msamaha kama mwanzo. Lakini niliuapiza moyo wangu kwa mara ya pili kuwa katu sitakubali kurudi kwa mume wangu hasa baada ya kuyazoea maisha ya upweke na uhuru iliojiwekea.

Sikuwa radhi kuurudisha moyo wangu kifungoni tena , wala kujiingiza kwenye mateso ya kujitakia.

Nilijikuta nikikumbuka siku niliyoletewa yule mwanamke ndani kwa makeke,Nilijikuta nikilia kwa kuona nilionewa bila kosa na kuonekana sina thamani kwenye familia ya mume wangu.
Mwanzo nilionekana mgumba, Mungu akawaumbua nikapata mtoto tena si mtoto mmoja bali watoto wanne.

Hawakuridhika wakanitafutia sababu nyingine, eti nimewajazia mitoto ya kike. Lakini Mungu mkubwa aliwaumbua sijui watanitazama vipi usoni. Mmh! yangu yalikuwa macho na kusubiri nione kitakachoendelea.

Kama atatafuta mwanamke mwingine kwangu ilikuwa sawa au atarudi kwangu. Japo moyo wa kumsamehe mume wangu ulikuwa wazi, lakini sehemu kubwa sikuwa radhi kugeuzwa Punda wa Dobi asiye na moyo wala masikio.
 
SEHEMU YA 49

Kama kila siku natendelewa mabaya naendelea kurudi mwisho wake nilijua ni mauti. Mwanzo walinitenda kuwa sizai na nikaamua kuondoka, baadaye walikuja kuniomba msamaha na kurudi kama Punda wa Dobi aliyejeruhiwa na Simba.
Kwa vile nilikuwa sina moyo wala masikio nilirudi kwa mume wangu.

Lakini yaliyonikuta siwezi kuyasahau mpaka naingia kaburini. Leo hii tena waje tena kuniomba msamaha nikubali kama sio kufuata kifo ni nini?

Taarifa zile nilimpelekea dada ambaye alikuwa na jibu fupi kuwa malipo ni duniani. Basi baada ya kukaa kwa mwezi toka nipate habari zilizoushtua moyo wangu za mume wangu kuuziwa mbuzi kwenye gunia.

Nilipata ujumbe kutoka kwa dada kuwa ananitaka kwake nikitoka kwenye shughuli zangu nipitie kwake.

Nilitii amri baada ya shughuli zangu nilipitia kwa dada, nilipofika aliniambia ana mazungumzo na mimi. Nilimkubalia na kusubiri nilichoitiwa, muda niliofika ilikuwa majira ya saa kumi na moja za jioni. Majira ya saa kumi na mbili kasoro niliitwa na dada sebuleni.

Niliingia ndani nilipofika sebuleni, nilishtuka japokuwa si sana kutokana na jambo lile kuliwaza kabla alijatokea. Sebuleni nilimkuta baba mkwe baba wa mume wangu.

Nilijua ni yaleyale niliyokuwa nayawaza baada ya kuzipata zile habari za kuumbuliwa mume wangu mchana kweupe. Nilipofika mbele ya baba mkwe nilisabahi na kukaa pembeni yake lakini kochi la pili. "Karibu baba," nilimkaribisha japokuwa hapakuwa kwangu.

"Asante mwanangu, wake zangu hawajambo?”
“Hawajambo.”
“Kwanza pole kwa yote."
"Nimepoa baba, namshukuru Mungu ni mwema."

"Mbona mama yalitokea mambo kinyume siku ile hukuja kunieleza?"
"Baba nina imani kwa kauli kali uliyoitoa siku ile na mume wangu kuidharau.

Sikuwa na haja ya kurudi tena kwako."
"Kwa nini mama?" "Baba, mume wangu nilikuwa nampenda sana tena mapenzi ya dhati nikuwa tayari kumsamehe kwa makosa yake. Mwanzoni nilimsamehe tena bila mashrti japokuwa alilonitendea lilikuwa zito.

”Nilirudi kwake na kuonesha mapenzi mazito na kuyasahau yote ikiwepo na kuwasamehe wifi zangu na mama mkwe kwa kuwaonesha mapenzi bila kuwabagua wala kuwawekea kinyongo.
 
SEHEMU YA 50

“Kumbe ilikuwa wazi mimi sitakiwi katika familia ya mume wangu, likatafuta la kutafuta na kufanikiwa kunitoa ndani."

"Hapana mwanangu bado hujatolewa ndani," nilimshangaa baba mkwe kukataa kuwa sijatolewa ndani.

“Baba imepita miaka mingapi leo ndiyo uje uhoji, kama kweli ulikuwa hujui kilichoendelea, uliwahi kuja kuhoji kilichoendelea?” nilimuuliza huku nikimkazia macho.

“Pamoja na hayo, bado mama ulitakiwa kurudi kwangu kama kuna kitu kimekwenda tofauti na maagizo yangu.”
"Kwa wewe mzazi wangu utasema hivyo, hebu fikiria toka siku ile ulipomuamuru mume wangu amtoe ndani yule mwanamke wake mpaka leo hii sijamtia machoni. Kweli mimi ni mke wake wa ndoa au anakuheshimu wewe mzazi wake?

“Baba, mama mkwe wifi zangu na mume wangu hawanipendi hivyo siwezi kuishi kwa shinikizo lako. Je, ukifa nani atakuwa mtetezi wangu, baba akumulikae mchana usiku atakuchoma."

"Ni kweli mwanangu, lakini mumeo amelipata funzo sidhani atarudia upuuzi wake."
"Baba siwezi kuwa Punda wa Dobi kamwe."
"Mwanangu ile ni hadithi tu," majibu ya baba ilionesha aliijua hadithi ya zamani kisa cha punda wa dobi.

"Lakini iliyotolewa makususi kwetu wanadamu, wamenikosa mara mbili ya tatu ni mauti yangu siwezi kuyakimbilia mauti nayaona mbele ya macho yangu."
"Hapana mwanangu huu mguu ni wa mumeo anaomba umsamehe na kuyasahau yote ili muwalee wenenu."

"Baba nakuapia maisha ya ndoa mimi tena basi, kurudi kwa mume wangu au kwenye familia yako siwezi labda maiti yangu. Lakini nikiwa mzima navuta pumzi katu abadani." nilisimamia msimamo wangu.

"Hapana mama mrudie bwana Mungu wako, msamehe mumeo amefanya makosa kama mwanadamu wala si malaika."

"Ni kweli, lakini sitarudi kwa mume wangu siwezi kuwa Punda wa Dobi mwambie amfaute mwanamke mwingine amuoe. Mwisho kabisa baba sipendi kuongea sana kwa vile nachubua madonda yaliyoanza kupona.

“Nakuheshimu sana mzazi wangu naomba tuishie hapa naogopa kuropoka maneno mazito ambayo lazima nitakuvunjia heshima.

“Sitaki mzazi wangu nikuvunjie heshima, katika watu duniani ninao waheshimu na sitawasahau na kuwaona ni kiumbe wa kipekee waliojaliwa na Mungu, wewe ni mmoja wao.
 
Sehemu ya 51

Lakini umekosa familia bora yenye muongozo thabiti.
“Naomba tena mzazi wangu unisamehe kwa hilo, kamwambie katu abadani sitarudi kwake.

Hivi nisingepata mtoto ningekuwa wapi? “Nimeteseka kabla ya kupata mtoto Mungu kasikia kilio changu. Hilo halikutosha nimeonekana nawajazia mabaa medi na machangudoa. Lakini Mungu hamfichi mnafiki kawaumbua mchana kweupe.

“ Kama yule mtoto wa kiume angekuwa wake kweli ingekuwaje? Leo baba ungefunga safari kuja kuniambia haya unayoniambia? Thamani yangu ipi katika nyumba yako? “Sina mayai ya kiume mnataka niongeze machangudoa na mabaa medi ndani ya familia yenu?

Baba naomba mniache, mateso na maumivu niliyoyapata nayajua mwenyewe. “Nakuheshimu na nitaendelea kukuheshimu ila mume wangu mama mkwe na mawifi zangu sitawasamehe na sitawasahau mpaka nakufa." Maneno yangu yalimfunga mdomo baba mkwe alinyanyuka na kuondoka kwa aibu.

Baada ya kuondoka dada alikuja kuniuliza nimefikia wapi? Nilimweleza yote bila kuacha hata moja baada ya kunisikiliza aliniuliza: "Kwa hiyo mdogo wangu umeamua kabisa kutorudi kwa mumeo?"
"Si mimi ila wao, na kamwe siwezi kuwa Punda wa Dobi."

"Mmh! Kwa hilo siwezi kukuingilia uamuzi wako usije sema bila mimi yasingenikuta." Baada ya mazungumzo na dada nilirudi nyumba nikiwa na hasira hata kuwa karibu na wanangu kwa siku ile sikutaka japokuwa haikuwa kawaida yangu kulala bila kuonana na wanangu hata kama nimechoka vipi.

Nilimuagiza mtumishi wangu wa ndani aniletee vidonge vya maumivu. Badala ya kumeza kimoja nilimeza vitatu na kujilaza hadi asubuhi.

Siku ya pili nikiwa ofisini alikuja mume wangu dukani mwangu na kuniomba tuongee. Sikutaka kumkatalia kwa sababu ni mzazi mwenzangu, vile vile sina kinyongo naye.

Baada ya kuweka mambo yangu vizuri nilitoka dukani,Tulikwenda kwenye kibanda kinachouza vinywaji baridi na kutafuta meza ya pembeni iliyokuwa tupu na wakati ule watu hawakuwa wengi sana.
Baada ya kukaa aliagiza vinywaji, kabla ya mazungumzo nilimtazama mume wangu na kugundua kitu.

ITAENDELEA.....
 
SEHEMU YA 52

Baada ya kukaa aliagiza vinywaji, kabla ya mazungumzo nilimtazama mume wangu na kugundua alikuwa amepungua sana. Nilijikuta nikimuonea huruma, niliyaanzisha maongezi kwa kujua mwanzo kwa mume wangu ungekuwa mgumu.
"Ndiyo mume wangu za siku?"
"Nzuri hongera kwa hatua uliyofikia."

"Asante nashukuru."
"Vipi watoto hawajambo?"
"Buheri wa afya."
"Mke wangu najua nimekukosea mengi."
"Ni kweli,"nilimjibu kwa sauti ya upole.
"Mke wangu nakiri makosa yangu mbele yako na kukubali adhabu yoyote kwako ili mradi tu urudi kwako."

"Mume wangu najua ndoa yetu imefungwa mbinguni hakuna mwanadamu atakaye weza kuivunja..uongo kweli?"
"Ni kweli kabisa mke wangu,"alijibu mume wangu. "Lakini siku zote usipende pasipo penzi na usilazimishe mapenzi pasipo na penzi. Ni kweli kufanya kosa ni kosa na kurudia kosa ni kudhamilia.

Siku zote hitimisho la karibu ni tatu baada ya moja, mbili mwisho ni tatu, uongo kweli?"

"Una maana gani?" niliniliza huku macho yamemtoka pima.
"Kama leo nitakusamehe na kurudi kwako lazima itakuwa umetimia tatu ambayo huwa mbaya zaidi ya yote."

"Una maana gani kusema hivyo?"
"Ya kwanza ulinitendea nikavumila na kukubali kurudi kwako ya pili ikawa mbaya zaidi ambayo nilikuwa sawa na kinyesi nisiye hitajika moyoni mwako wala usoni, si mimi hata damu yako ambayo ameinyanyapaa kwa kuwaona ni machangudoa na mabaa medi.

“Leo hii unataka nirudi kwako ili unimalize kabisa mume wangu, hata mimi amani ya moyo naitaka vile vile bado natamani kuishi japokuwa sijui siku yangu itakuwa lini.
Kwa vile sijui siku yangu ya kufa bado nina hamu ya kuendelea kuishi."

"Mke wangu siwezi kukufanyia baya lolote unalolifikiria, nimejifunza kutokana na makosa. Nitakuwa mume mwema na mwenye mapenzi kwako na kwa familia yangu," mume wangu alisema kwa sauti ya upole yenye kuchanganyikana na majuto.

"Yaani mume wangu una bahati yote ni kutokana na kuwa mzazi mwenzangu, lakini bila hivyo kila nikikumbuka roho inaniuma kama moyo upasuke na maumivu yake ni makubwa.

Wewe ni mnafiki mkubwa leo hii ndio umeniona mzuri mzazi mwenzi kwa sababu umeumbuka..eeeeh...
 
SEHEMU YA 53

"Huu msamaha ungeuomba lini kama yule mrithi uliyekuwa ukimtafuta angekuwa damu yako wala si magumashi. Basi kwa taarifa yako mimi kurudi kwako sahau kabisa moyoni kwako kwanza hunipendi nirudi kufanya nini? “Si wewe tu, familia nzima mnataka kuniambia baada ya kuumbuliwa ndiyo mapenzi yenu yamekuja kwangu?

“Nakuomba kuanzia leo unione kama mbingu na ardhi ila tutashirikiana kwa jambo lolote si mapenzi na ukinikuta na bwana muheshimu kama mume mwenzio," nilizumgumza kwa hasira hapokuwa moyo ulinisuta na kuwa tayari kumsamehe.

"Mama Jacky!" maneno yangu yalimfanya mume wangu macho yamtoke pima. Kama ingekuwa siku ya kwanza kumuona nisingejifikiria kumsamehe alikuwa akitia huruma. "Ndio mimi baba Jacky."

"Sikubali lazima utarudi kwa nguvu kwa hiyari," mume wangu alikuja juu na kutoa mkwala mzito huku akisimama.
"Jaribu uone!" nami sikuonesha kushtuka nilionesha msimamo wangu japokuwa woga uliniingia kwa mbali.

Baada ya mume wangu kuniona sitishwi na mkwala mbuzi aliondoka akiwa amefura.Sikumuonea huruma kwa kuwa nilijua alitaka kunigeuza kuchaka cha kumalizia haja zake pale anaposhikika. ***

Kuanzia hapo sikusikiliza la mtu yeyote, mume wangu hakukata tamaa alihaha kama kuku anayetaka kutaka. Alirudi tena kwa dada ambaye aliniita na kuniweka chini ili nibadili uamuzi lakini nilisimamia msimamo wangu wa kutogeuka nyuma.

Hakuishia hapo aliwatuma mpaka wazee wa kanisa ambao nilikuwa nawaheshimu sana. Nao niliwajibu kuwa kama mzazi wake alishindwa kumsikiliza hakuna wa kusikiliza. Mwisho nilimalizia na hadithi ya Punda wa Dobi ambayo iliwaacha midomo wazi na kukosa la kuongezea na kuniacha na maamuzi yangu.

Tokea siku ile maisha ya ndoa naliyachukia walio ndani ya ndoa kama yangu niliwapa pole na waliokuwa katika ndoa kama ya dada niliwapa hongera.
Siku zilisonga huku wanangu wakiendelea kusoma katika malezi mazuri japokuwa ya upande mmoja. Moyoni nilipanga wakiwa wakikubwa watakuwa na haki ya kwenda kwa baba yao japokuwa sikuwa tayari kupanda chuki mioyoni mwake kutokana na kauli za udhalilishaji toka kwa baba yao.
 
SEHEMU YA 54

Pia nilikuwa radhi aje nyumbani kwangu kuwaona watoto wake lakini si kuondoka nao au akipata mwanamke mwingine awachukue na kuwalea. Kwa upande wa shughuli zangu japokuwa kulikuwa na ugumu fulani kutokana na kuongezeka kwa wafanya biashara za aina moja, lakini fedha ya kula na kujikimu ilipatikana.

Katika maisha yangu nami nilikuwa na hamu ya kumiliki gari langu hata la milioni tatu. Kwa bahati nzuri shoga yangu mmoja tuliyekuwa tukifanya biashara pamoja ambaye nilikukutana naye mara ya kwanza dubai.

Baada ya hapo tulijenga ushoga, na ndiye aliyenifanyia mpango wa duka katika ya jiji. Aliambia anauza gari aina ya Toyota Lav4 alilokuwa akiendesha baada ya kuletewa gari jingine na mpenzi wake aina ya Toyota Harrier Lexus.

Kutokana na kuona gharama yake kubwa nami nilitaka gari lisilozidi milioni tano nilimwambia siwezi kununua. Lakini asema ataniuzia kwa milioni nane kwa kutanguliza milioni sita na zingine ningemlipa taratibu.

Kwa vile alitaka nami nimiliki gari langu, alisema amenipa kwa fedha ya kutupa ili tu nami niwe na gari. Kwa vile gari alikuwa amenipunguzia sana nilikubali kununua kwa milioni nane kwa kutanguliza sita na kudaiwa mbili.

Baada ya kujibana niliweza kufikisha milioni sita ambazo ndizo tulizokubaliana nitangulize. Nilimpigia simu shoga yangu na kumweleza nimefikisha kiasi tulichokubaliana kutanguliza. Kwa vile alikuwa mkoani alinieleza nikachukue gari nyumbani kwake atawapigia simu kuwajulisha.

Kuhusu fedha alisema atazikuta kwangu kwa vile alikuwa akiniamini sana.
Baada ya makubaliano, nilimwita msichana aliyekuwa akinisaidia kuuza dukani ili nimuachie maagizo niwahi kwa shoga yangu kuchukua gari.

Wakati najiandaa kutoka baada ya kumuachia maagizo msichana wangu, moyo ulishtuka kumuona shoga yangu ambaye mara nyingi huja na habari za kushtusha.

ITAENDELEA KESHO
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom