Sehemu ya 99.
Niliingia huku nikitetemeka sasa kwani akili zangu zilianza kuniambia kuwa, kuna uwezekano mkubwa nakwenda kutolewa uhai na huyu mama kwa sababu ya kukasirika baada ya kugundua nilichungulia ndani kwake na kuona majeneza yaliyorundikana.
"Pita huku," aliniambia yule mama huku akifungua mlango ambao nilibaini haraka sana kuwa ni wa kuingilia chumbani. Lakini usawa wa chumba hicho si kile chenye chumba nilichoona majeneza. Moyoni nilijiambia tutaona huko huko.
Nilipozama ndani ya chumba hicho huku na yeye akiwa ndani kabisa, alinigeukia na kuniuliza.
"Unataka nikuoneshe nini katika mambo unayoyahitaji?"
Sikuwa na jibu lolote kwani sikujua alikuwa na lengo gani.
"Nakuuliza wewe unataka nikuoneshe nini?" alinifokea huku akinikaba koo kwa hasira.
"Hee! Yamefikia huko mama?" nilimuuliza.
"Nani mama yako? Nani mama yako?" aliniuliza kwa ukali ule ule. Macho yake yalitoka na kuwa makubwa kuliko kawaida.
"Basi samahani sana. Nioneshe chochote utakacho," nilimjibu huku nikijaribu kujitetea kujiondoa kutoka kwenye kule kunishika koo kwa nguvu.
"Ona," aliniambia akiwa bado amenishika.
Sikujua nione wapi, kwa hiyo nikawa namshangaa.
"Nimekwambia ona," alisema kwa sauti zaidi. Safari hii akinyoosha kidole kwenye mguu. Nikaona sehemu iliyopona kidonda (jeraha)
Haraka sana, akili yangu ilikumbuka kuwa mguu huo ndiyo ule niliouona nyumbani kwangu usiku mpaka nikashangaa sana.
"Umeona?" aliniuliza.
"Nimeona mama," nilimjibu.
"Njoo huku," aliniita akienda mbele.
Hapo alikuwa ameniachia kule kunishika.
Nilimfuata nyuma nyuma, yeye akikatisha vyumba. Nilishangaa kuiona ile nyumba kwamba, kumbe ni kubwa kiasi kile. Lakini kwa nje haioneshi kama kubwa.
"Ingia," aliniambia huku yeye akifungua mlango kuingia kwenye chumba kimoja ambacho mlango wake ulikuwa na mchoro wa kichwa cha mtu kisichokuwa na nyama (fuvu)
"Angalia humu ndani hadi uchoke, si wakati ule uliangalia kwa kuiba," aliniambia akinipisha niingie vizuri ndani ya chumba kile
Sikutaka kumbishia chochote kile, niliangalia kama alivyotaka. Sikuona kitu chochote.
Nilipogeuza shingo kumwangalia, akaniuliza.
"Umeona nini?"
"Sijaona kitu chochote kile," nilimjibu.
Kufumba na kufumbua mimi na yeye tulikuwa nje ya kibanda changu. Mimi nikiwa napiga nyundo kwenye msumari, yeye amesimama akiwa ameshika kiuno.
"Ukitaka kujua ubaya wangu endelea na tabia hii ya kukagua kagua mambo yangu. Mimi sitaki kabisa, kweli nakwambia bwana," alisema kwa ukali yule mama jirani akiniambia mimi.
"Unakuja kwangu halafu unachungulia, unachungulia nini?" aliendelea kusema.
"Siku zile hivyo hivyo ukaniuliza eti kama nyumbani kwangu naishi na kijana, ule ni upekepeke nisioutaka," alikazana kusema yule mama wa jirani.
Nilishangaa kuona tupo pale tena kwa ghafla, lakini sikusema kitu zaidi ya kumsikiliza tu na kuendelea kumshangaa sana.
Kwa upande mwingine unaweza kusema mpaka pale nilikuwa nimeshapata majibu, kuwa yule mama ndiye mbaya wangu wa siku zote. Ndiye yeye aliyekuwa akinifanyia maajabu yote yale.
Nilikumbuka na ule mguu alionilazimisha kuuangalia na kukuta una lile kovu. Ndiyo kabisa nikawa nimemjua yeye ndiye mbaya wangu.
Kitu kingine ambacho naamini kabisa mpaka leo kwamba ndicho kilichokuwa kikinifanya niendelee kuteseka kwa muda mrefu ni kuwa, inaonekana licha ya kunifanyia mabaya yake, pia alikuwa amenichezea ili kunifunga kinywa nisiseme kwa mtu wala nisiwe na wazo la kutafuta msaada wowote. Lakini hasa kisa kilikuwa nini hadi anifanyie mambo yote yale, sikujua na wala sijaijua mpaka sasa.
Baada ya kunisema sana aliondoka huku akiendelea kusema kuwa, atahakikisha sidumu mahali pale.
Hilo sikujali kabisa, kwani kama angeniingia moyoni mwangu angegundua kuwa, hata mimi nilishachoka kuwa pale kama mahali pangu pa kazi. Tabu na mateso niliyokuwa nikiyapata pale Mungu mwenyewe ndiye anayejua. Na ndiyo maana hata mdogo wangu alishindwa kuvumilia hata kufikisha mwezi mmoja tu, akaaga kurudi nyumbani Tanga. Najua kisa ni vituko tu.
Alipozama tu, kuna mzee mmoja alikuja na kuniambia kuwa, anataka kutengenezewa jeneza la mtoto wa miaka mitano, lakini wakati akitoa kipimo nikamwambia.
"Siku hizi nimeacha kutengeneza majeneza."
Alishangaa sana lakini nilibaki na msimamo huo huo, kwamba siku hizi nimeacha kutengeneza majeneza.
Je, nini kiliendelea?