Simulizi: Kazi ya Kutengeneza Majeneza

Simulizi: Kazi ya Kutengeneza Majeneza

Sehemu ya 45.

Nilisalimiana na baba kwa furaha sana lakini mama alionekana hana furaha baada ya kumwambia nilikwenda pale kwa matatizo makubwa sana.
"Enhe za huko baba," baba aliniuliza, nikamjibu lakini nikamalizia kwa kumwambia.

"Lakini si nzuri sana baba, nina matatizo ambayo nikiwasimulia mnaweza kukimbia wote humu ndani," nilimwambia baba akakaa vizuri huku akinikazia macho.



Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 46.

"Ni yapi hayo mwanangu, unaweza kunisimulia?" baba aliniuliza.
"Naweza baba," nilimjibu.
"Sawa, nakusikiliza," alisema baba akiweka kiganja cha mkono kwenye kidevu na kuniangalia.

Wakati huo mama naye alikuwa amekaa pembeni akiniangalia kwa umakini sana.
Niliwasimulia baba na mama matatizo yangu yote kutokea mwanzo hadi mwisho huku kila mmoja akinitolea macho pasipo mfano. Walionekana dhahiri kwamba, kila kipengele nilichokuwa nikiongea walikuwa wakiogopa zaidi kuliko nilikoanzia.

Ilifika mahala mama alijiziba uso kwa woga kama vile nilichokuwa nikisimulia yeye alikuwa akikiona machoni pake. Pia kuna wakati aliingiza vidole kwenye masikio ili asisikie.

"Si uondoke kama hutaki kumsikia," baba alimwambia mama.
Lakini mama alijikaza na kubaki ametulia kimya kama vile sasa aliamua kunisikiliza bila woga.

Nilipomaliza kusimulia, baba alisimama akaingia chumbani kwake, alipotoka alikuwa ameshika tasbii akihesabu hesabu kisha akaa kwenye kiti. Akaniuliza.

"Umemaliza mwanangu?"
"Nimemaliza wazazi wangu."
Nilimuona baba akihema kwa nguvu sana kisha akasema.

"Amani kuwa mizimu ya kwetu imekulinda mwanangu. Yote uliyonisimulia kama sio mizimu ya kwetu ungekuwa umekwishaaga dunia. Hayo mambo yote yanatokea sana...!"

Kabla hajamaliza kuongea mama alidakia.
"Sasa badala ya kumsaidia itakuwaje unaanza kumsimulia habari za mizimu ya kwenu. Kwani mimi mizimu ya kwetu haiwezi kumkinga. Mizimu yetu wote imemkinga mtoto."

Baba alionesha uso wa kuchukia lakini hakumjibu kitu, mama akaendea kuniambia.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 47.

"Kinachotakiwa siku zote ni kumuomba Mungu na kumuamini. Pia tena matendo mema unamfanya Mungu kukujua wewe. Maana kuna tofauti kubwa mbili, kuna kumjua Mungu na kujulikana na yeye. Hata majambazi, wachawi, wazinzi, walevi wanamjua Mungu, lakini je, wanajulikana na yeye?"

Sifahamu baba alitoa wapi neno (falsafa) hilo kwani sikuwahi kumsikia siku za nyuma akisema maneno mazuri kama siku hiyo. Akaendelea.

"Sasa itabidi tufanye tambilo la mizimu. Kesho asubuhi, wewe na ndugu zako tutakwenda kwenye kaburi la marehemu babu yako. Tutamsimulia matatizo yako, halafu tukirudi tutapika chakula na kula kwa ajili ya kutusindikiza na tambiko letu. Naamini ukirudi hakutakuwa na hayo matukio ya kutisha tena."
"Sawa baba," nilimjibu.

"Lakini mwanangu kuna kitu kimoja pia nataka ukielewe. Isije kuwa huko Dar umeanza kuingilia ndoa za watu, sasa wenyewe ndiyo wanakuchezea, maana yote uliyonisimulia yanaonekana kama ni mambo ya michezo," mama aliniambia.

"Hapana mama, kama utakuja siku moja ukaona ninavyoishi mwenyewe utanishangaa sana. Nikitoka kazini kwangu nakuwa ndani kwangu mpaka watu wananishangaa,"nilimjibu mama.

Asubuhi ya kesho yake, baba aliamka na homa kali sana. Ilikuwa ni homa iliyomshika sana usiku. Hata mama wakati ananisimulia nilimshangaa kwanini hakutuamsha usiku ule ule ili kutusimulia. Naye akajibu kuwa, alishindwa kufanya vile kwa sababu kila dakika alikuwa akitumaini kuwa, hali itatulia kidogo.

Tulipojadili suala la kumpeleka baba hospitalini, mama alikubali, lakini baba mwenyewe alikataa katakata akisema kuwa, anahisi niliyomsimulia mimi yamemvaa yeye ili tambiko lisiweze kufanyika.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 48.

Sasa itakuwaje habari ya tambiko wakati baba anaumwa? Hilo ndilo swali ambalo nilikuwa nikijiuliza siku hiyo asubuhi.
Kwenye saa tano, baba akawa mzima kabisa kiasi kwamba alinitaka mimi na ndugu zangu twende makaburini kwa ajili ya kufanya tambiko lenyewe.

Nyumbani tulimwacha mama akiandaa chakula kabisa ili tutakaporudi tushiriki chakula hicho ili kukamilisha tambiko hilo.
Tulipofika kule makaburini, kabla baba hajaanza kusema na hiyo mizimu alijikuta sauti haitoki hata chembe.

Kila alipojitahidi kusema sauti ilikataa katakata kutoka. Ilifika mahali ilibidi turudi nyumbani bila baba kuongea chochote.
Tulipofika tu nyumbani, mama alipotupa pole na kamwendo mimi nilimjibu, baba alipotaka kusema sauti ikatoka.
"Si salama sana."
"Vipi tena jamani," aliuliza mama kwa sauti ya mshangao.

Nilimuona baba angeshindwa kumsimulia mama yaliyojiri kula makaburini, hivyo mimi nikaingilia kati kumjulisha.
"Baba alishindwa kuongea. Kwa hiyo tumerudi bila kuwaambia chochote mizimu," nilimwambia mama.

Naye akashangaa sana, lakini hakuongeza kusema kitu. Baba naye alipitiliza kuingia ndani.
"Sasa mama kwa vyovyote vile mimi leo naondoka kurudi nyumbani," nilimwambia mama.

"Kufanya nini? Matatizo hujamaliza halafu uondoke?" mama aliniambia akinishangaa. Lakini hata hivyo niliendelea kushikilia msimamo wangu ule ule kuwa ni lazima niondoke.

Aliingia ndani, nadhani alikwenda hadi chumbani ambako baba aliingia akamweleza kuhusu safari yangu.

Baba alitoka na kusema hilo haliwezekani kamwe kwani katika matatizo niliyomwambia hakuna hata moja nililolitatua. Nimpe siku mbili za kushughulikia suala hilo kikamilifu, niliwajibu.

"Kuna kazi za wateja wengi sijazifanya. Acha niondoke, nitarudi tena baada ya mwezi ili kushughulikia suala hilo kikamilifu," niliwajibu.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 49.

Walinibembeleza sana lakini msimamo wangu ukawa huo. Najua katika kunibembeleza kwao walikuwa na misimamo miwili tofauti. Baba alinibembeleza akiwa hataki kuonekana ameshindwa kunisaidia mimi mtoto wake. Mama yeye alikuwa na uchungu wa matatizo yangu kama mzazi.

"Lakini pia nilitaka kuongea na wewe kitu kimoja mwanangu," alisema mama.
"Kipi hicho mama?" nilimuuliza.
"Kuoa. Sikutaka kukwambia nikijua bado upo, lakini maadamu umeng'ang'ania kuondoka naona nikwambie tu."

Moyoni niliona mama ameniambia suala zito sana. Sikuwa nalifikiria kwa muda ule kutokana na matatizo yangu ya Dar.
"Mama hilo kwanini tusiliweke kiporo?" nilimjibu mama huku nikimwangalia baba.
"Sawa lakini tayari mimi nina chaguo langu.

Yuko msichana ambaye ndiye nataka umuoe," alisema mama, baba akatingisha kichwa kama walishaongea suala hilo, ama kabla sijafika au baada ya kufika.
"Sawa mama lakini naomba muendelee kulishughulikia suala hilo mwisho wa mwezi nikija tutaliweka sawa, sawa?"
"Sawa," alijibu mama.

Nilipobaini hilo limekwisha, niliwaomba niondoke na mdogo wangu niliyemwachia ziwa. Alishamaliza shule na alikuwa hana la kufanya. Wote, baba na mama walinikubalia kwa ombi hilo.


Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 50.

Tulifika Dar saa tisa alasiri. Tulifikia nyumbani moja kwa moja bila kwenda kazini na wala sikuwa na mpango wa kwenda kazini siku hiyo.

Asubuhi na mapema niliamka na kumpa maagizo kadha wa kadha mdogo wangu ingawa na yeye alitaka tuongozane kwenda wote kazini kwangu. Nilimwambia angeanza kesho yake ili kwa siku hiyo akae akiyazoea mazingira ya pale nyumbani.

Nilipofika kazini kwangu tu, kitu cha kwanza kabla sijafungua banda na kuanza kufanya kazi, nilikwenda kumsalimia mama jirani kwani isingekuwa heshima anikute niko kazini tayari wakati na yeye alinipa ushauri wa kwenda nyumbani kulingana na matatizo yangu.

Aliponiona alinichangamkia kwa maana kwamba alikuwa amenikosa kwa siku mbili ambazo sikuwepo kazini kwangu. Aliacha tabasamu akanisalimia.
"Hawajambo wazee lakini?"
"Hawajambo mama, wanakusalimia sana."
"Asante sana, mambo yote yalikwenda salama lakini?" aliniuliza.

"Yote yalikwenda salama mama," nilimjibu.
Mara yule mama aliangalia kule upande wa kibanda changu kama ameona kitu. Na mimi niligeuka kuangalia.

"Fundi sijui yuko karibu?" mtu mmoja aliuliza akiwa amesimama na wengine wengi, wakiwemo wanawake.

Nilikwenda haraka sana huku nikimuaga yule mama kwamba tutaonana baadaye kidogo.
"Sawa baba, tutaongea," aliniambia mama na yeye akiingia ndani kwake.

Wale watu walikuwa ni wafiwa na walikuwa wanahitaji kutengenezewa jeneza la mwanamke mtu mzima.

Walisema maiti wao alikuwa chumba cha maiti Muhimbili, lakini walikuwa wanakwenda kuzika Iringa. Niliwahakikishia kuwa jeneza lao wanaweza kulipata saa tisa na nusu alasiri.

Kwa upande fulani nakiri kuwa, kweli haya mambo yalikuwa yamejaa maajabu kwani spidi niliyokuwa naipata kwenye kutengeneza jeneza si ya kawaida.

Naapa kuwa, kwa wakati ule ningeweza kutengeneza jeneza moja hata kwa saa tatu kama ningeamua. Naamini leo hii kuwa, nilikuwa na nguvu ya ziada, lakini mwenyewe nilikuwa sijui tu.

Walipotoka tu, nilianza kazi. Kama nilivyokwisha kusema, mbao zilikuwepo tayari tena zikiwa zimechongwa na kurandwa. Kazi kubwa kwangu ilikuwa ni kuzipasua tu.

Saa tisa na dakika kama kumi na saba, nilimaliza kazi ya jeneza. Nikaliweka pale pale nje nikiwasubiria wenyewe kuja kulichukua.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 50.

Tulifika Dar saa tisa alasiri. Tulifikia nyumbani moja kwa moja bila kwenda kazini na wala sikuwa na mpango wa kwenda kazini siku hiyo.

Asubuhi na mapema niliamka na kumpa maagizo kadha wa kadha mdogo wangu ingawa na yeye alitaka tuongozane kwenda wote kazini kwangu. Nilimwambia angeanza kesho yake ili kwa siku hiyo akae akiyazoea mazingira ya pale nyumbani.

Nilipofika kazini kwangu tu, kitu cha kwanza kabla sijafungua banda na kuanza kufanya kazi, nilikwenda kumsalimia mama jirani kwani isingekuwa heshima anikute niko kazini tayari wakati na yeye alinipa ushauri wa kwenda nyumbani kulingana na matatizo yangu.

Aliponiona alinichangamkia kwa maana kwamba alikuwa amenikosa kwa siku mbili ambazo sikuwepo kazini kwangu. Aliacha tabasamu akanisalimia.
"Hawajambo wazee lakini?"
"Hawajambo mama, wanakusalimia sana."
"Asante sana, mambo yote yalikwenda salama lakini?" aliniuliza.

"Yote yalikwenda salama mama," nilimjibu.
Mara yule mama aliangalia kule upande wa kibanda changu kama ameona kitu. Na mimi niligeuka kuangalia.

"Fundi sijui yuko karibu?" mtu mmoja aliuliza akiwa amesimama na wengine wengi, wakiwemo wanawake.

Nilikwenda haraka sana huku nikimuaga yule mama kwamba tutaonana baadaye kidogo.
"Sawa baba, tutaongea," aliniambia mama na yeye akiingia ndani kwake.

Wale watu walikuwa ni wafiwa na walikuwa wanahitaji kutengenezewa jeneza la mwanamke mtu mzima.

Walisema maiti wao alikuwa chumba cha maiti Muhimbili, lakini walikuwa wanakwenda kuzika Iringa. Niliwahakikishia kuwa jeneza lao wanaweza kulipata saa tisa na nusu alasiri.

Kwa upande fulani nakiri kuwa, kweli haya mambo yalikuwa yamejaa maajabu kwani spidi niliyokuwa naipata kwenye kutengeneza jeneza si ya kawaida.

Naapa kuwa, kwa wakati ule ningeweza kutengeneza jeneza moja hata kwa saa tatu kama ningeamua. Naamini leo hii kuwa, nilikuwa na nguvu ya ziada, lakini mwenyewe nilikuwa sijui tu.

Walipotoka tu, nilianza kazi. Kama nilivyokwisha kusema, mbao zilikuwepo tayari tena zikiwa zimechongwa na kurandwa. Kazi kubwa kwangu ilikuwa ni kuzipasua tu.

Saa tisa na dakika kama kumi na saba, nilimaliza kazi ya jeneza. Nikaliweka pale pale nje nikiwasubiria wenyewe kuja kulichukua.

Je nini kitaendelea?
huyu atajuta kuondoka kwao bila kufanyiwa tambiko,nahisi jeneza analolitengeneza sasa hivi ndilo atakalozikwa nalo
 
Sehemu ya 36.

Moyoni nilimuona yule mama jinsi alivyo mnafki. Nilivyochukulia mimi ni kwamba alijua kuwa nililala kibandani kwangu.
"Yupo baba mmoja jana alisema atakuja mapema sana," nilimjibu.
Wakati huo ilikuwa yapata saa moja na nusu hivi asubuhi.

Yule mama alirudi kwake huku akinipongeza kwa uwezo wa kuamka asubuhi sana, akidai yeye asingeweza.

Je nini kitaendelea?
Hii hadithi mpaka mimi msomaji ninatetemeka!!!
 
Sehemu ya 51.

Nikaanza kuungaunga mbao nyingine kwa ajili ya kitanda cha yule kijana, kwani siku za kuja kuchukua zilifika.
Saa tisa na dakika thelethini na tano alikuja mmoja kati ya wale watu wenye jeneza lao. Alinisalimia kisha akasema kuwa, hakuja kufuata jeneza ila kutengua kuwa, hawatalichukua siku hiyo.

"Naomba utuhifadhie ndani fundi kwani kumetokea mabadiliko kidogo. Sasa ndugu wote wataagia pale pale mochwari kesho saa nne asubuhi. Hivyo tutakuja kulichukua asubuhi."

Nakumbuka yule mtu alinitamkia hivyo, nikamkubalia huku nikimuomba msaada mwenyewe kuliingiza ndani kwa kusaidiana kulibeba.

Tulipolifikisha tu ndani, akatokea mwenzake mmoja akiwa ameshika mfuko wa rambo mkubwa. Akasema amekuja na maua kwani alikonunulia hakuona sehemu ya kwenda kuyahifadhi hadi kesho yake baada ya mabadiliko ya siku ya kuchukua jeneza kujitokeza.
"Kwahiyo ndugu tuwekee kwako hadi kesho asubuhi tutakapokuja kuchukua jeneza letu," alisema.

Nilimkubalia, nikauchukua ule mfuko wa rambo na kuuweka juu ya jeneza. Kisha wakaaga wakinitakia kazi njema hadi hapo kesho watakapokuja kulichukua jeneza lao.
Niliendelea na kazi nje hadi kwenye saa kumi na moja na nusu hivi, moyoni nikajiambia niwahi kurudi nyumbani kwa sababu ya mdogo wangu hakuwa mwenyeji sana isitoshe angejisikia unyonge kubaki peke yake mpaka giza linaingia.

Nilichukua zana zote kama vile randa, misumeno na vikorokoro vyote nikavitumbukiza ndani ya boksi langu la kazi. Kisha nikalibeba mpaka mlangoni ili kuliingiza ndani. Lakini sikuliingiza moja kwa moja, nikarudi tena kubeba mbao za kile kitanda.

Niliziingiza ndani kwa kadri nilivyoweza kuzibeba. Kule ndani nilizisimamisha kwenye ukuta kisha nikatoka kulichukua lile boksi. Nilibeba mpaka ndani na kuliweka pembeni au tuseme jirani kabisa na tulipoliweka lile jeneza. Ile namaliza kulibwaga chini tu, nikahisi kama kuna mtu anahema kwenye lile jeneza. Niligeuka kuangalia....nikarukia mbali.



Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 52.

Kwa kweli ni mapenzi ya Mungu tu mpaka leo hii niko hai, kwani nilichokiona kama si Mungu ningeanguka na kukata roho pale pale.

Ndani ya jeneza hilo aliyekuwa akihema ni baba yangu mzazi. Alikuwa amelala kama inavyolala maiti, akitumbua macho juu lakini anahema! Mara akatoweka ghafla!

Nilikuwa bado nimesimama pale pembeni, nikiendelea kushikwa na mshangao kuhusu tukio lile. Lakini nikiendelea kutumbulia macho lile tukio, nikasikia sauti ikisema.
"Kila kinachokutokea na kukiona unatakiwa usimwambie mtu. Inaweza kukusaidia kuokoa maisha yako."

Hiyo sauti sikujua ilikotokea, kwani hata nilipozungusha macho kila kona mle ndani sikumwona mtu yeyote yule. Halafu sauti ile ile na maneno yale yale yakajirudia ndani ya kichwa changu.

"Kila kinachokutokea na kukiona unatakiwa usimwambie mtu. Inaweza kukusaidia kuokoa maisha yako."

Niliamini kuwa, ni mwendelezo wa maajabu, lakini kwanini awe baba yangu? Ina maana huko aliko Tanga atakuwa amekufa au? Nilijiuliza huku nikihema kwa nguvu zote na woga juu. Ghafla! Tena nikasikia 'tititii', nikarukia upande mwingine.

Nilipoangalia pale nilipokuwa nimekaa mchanga wenye rangi kama mkaa ulimwagika na kutengeneza kimlima kidogo.
Nikiwa nashangaa hilo nalo, pale pale niliposimama nilidondokewa na maji ya baridi kama vile yalitoka kwenye friji. Nikakimbia na kusimama sehemu nyingine. Nilitaka kupiga kelele lakini nikakumbuka ile kauli.

Mara sijasimama sawa, nikasikia mlio wa kama ndege wanaokula mpunga wakiwa kwa wingi mle ndani. Hapo tena nikaogopa zaidi nikijua ndiyo mwisho wa maisha yangu ya duniani.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 53.

Kwa haraka sana nikajiwa na mawazo kwamba kumbe kuna yanayonitokea lakini bila mimi mwenyewe kujua.

Ndiyo maana ile sauti iliniambia, "Kila kinachokutokea na kukiona...' maana yake ni kwamba kumbe kuna mengine yalikuwa yakinitokea lakini nilikuwa sioni.
Ghafla ulipita ukimya kiasi kwamba hata kelele za nje nilikuwa sizisikii kabisa. Kukawa kimyaa! Mle ndani hakukuwa na kelele hata za mijusi.

Nikaanza kutembea mpaka kwenye ule mchanga. Niliinama kuuangalia lakini sikuushika. Nikageuka kuangalia pale yalipochuruzika maji, yalikuwa yametapakaa chini kwa sehemu.

Nilipoangalia jeneza, lilikuwa liko kama tulivyolibeba kuliingiza na yule mtu aliyekuja kuahirisha siku ya kulichukua. Juu yake kulikuwa na ule mfuko wa rambo wenye maua aliyoyaleta mwenzake na yule aliyekuja mwanzoni.
Hapo nikawa kama nimeingiwa na fahamu iliyotoweka.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 54.

Nilitoka nje haraka sana huku nikiangaza kila sehemu kama kuna mtu aliyekuwa jirani akiona yaliyokuwa yakinitokea.

"Leo umechelewa kufunga," sauti ilisikika. Alikuwa ni yule mama jirani amesimama nje ya nyumba yake akiniangalia huku akitabasamu.
"Nina haraka," nilimjibu hivyo bila kuongeza chochote kile. Lakini nahisi aligundua kuna jambo. Kwank hata sauti yangu ilitoka kwa hofu, halafu nikawa kama simwendekezi.
"Msalimie huko," alisema kisha akaingia ndani.

Kitendo hicho nacho kikanipa wasiwasi.
"Msalimie huko nani? Mbona sikumwambia kama nimekuja na mdogo wangu. Au ni salamu ya kibinadamu tu? Lakini kama ni ya kibinadamu kwanini asiseme 'wasalimie' akasema kwa mtu mmoja? Mbona sikuwahi kumsikia hata siku moja akinipa salamu hiyo? Haho niliyawaza akilini mwangu.

Sikumjibu 'sawa nitamsalimia' wala 'zimedika', kwani kwanza mtu mwenyewe alisema akiingia ndani. Pili sikuwa katika hali ya kuendelea kuongea naye. Nilifunga geti haraka sana na kutoka mbio mpaka kituoni.
Nikiwa ndani ya daladala, kila wakati ile sauti ilinijia, "Kila kinachokutokea na kukiona unatakiwa usimwambie mtu.

Inaweza kukusaidia kuokoa maisha yako."
Hii sauti sasa ikawa kero kwangu. Kwanini inacheza masikioni mwangu? Niliwaza peke yangu huku nikimuogopa kila mtu ndani ya daladala.

Mama mmoja alikaa kiti cha ng'ambo yangu aliponikata jicho, pengine lilikuwa ni la kawaida sana, lakini nilijikuta nikisimama na kusogea mbele karibu na mlango wa kuteremkia.

Nilifika nyumbani na kujitupa kitandani huku mdogo wangu akiniangalia kwa kunishangaa.
"Kaka vipi unaumwa nini?" aliniuliza haraka sana.

"Kila kinachokutokea na kukiona unatakiwa usimwambie mtu. Inaweza kukusaidia kuokoa maisha yako."
Ile sauti ilifanya ghasia tena ndani ya kichwa changu wakati nikiwa najiandaa kumjibu mdogo wangu.

Nilitingisha kichwa kwa ishara ya kukataa kuumwa.

"Mbona umejitupa hivyo, umechoka sana? Poe," mdogo wangu aliniambia.
Nikakubali pole yake kwa kutingisha kichwa kukibetua juu chini.

Je nini kitaendelea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom