Simulizi: Kazi ya Kutengeneza Majeneza

Sehemu ya 31.

Nilimwambia bibi umenikumbusha, kuna kitu nataka kuongea na wewe, lakini naomba iwe kesho.

"Haya mimi sina neno, nipo. Ukiwa tayari utanitafuta," alisema bibi kwa sauti yake yenye lafudhi ya pwani.
Nilikwenda kutafuta chakula, nilipomaliza kula nilirudi nyumbani nikaoga, nikapanda kitandani kulala.

Nadhani siku hiyo nililala saa tatu usiku, wakati siku zote huwa nalala saa nne au saa tano. Na pia hata kama sijalala mara nyingi nakuwa ndani kwangu tu. Yaani kifupi sikujaaliwa kuwa mtembezi au mtu wa kutumia. Pombe sinywi, sikuwa napenda wanawake kwa hiyo hakukuwa na sababu ya kutotulia nyumbani kwangu.

Siku hiyo nililala salama mpaka asubuhi. Niliwahi kuamka na kujiandaa kisha nikaenda kazini kwangu.

Njiani nilijipongeza sana kwa uamuzi wangu wa kutaka kumwambia bibi yanayonisibu. Niliamini kuwa bibi kama yule, aliyekula chumvi nyingi (kuishi miaka mingi). Kwa vyovyote angeweza kunipa ufumbuzi wa tatizo langu.
Nilifika kazini na kufungua geti salama usalimini. Siku hiyo au asubuhi hiyo sikusikia sauti mbaya yoyote ile kama ilivyokuwa jana yake.

Nilianza kazi zangu kama kawaida. Ilipofika saa nne kama na nusu hivi, wale watu wa jeneza walitokea na kuchukua jeneza lao. Wakaondoka zao.
Lakini siku hiyo hiyo nikaamua kuchonga mengine ambayo yalikuwa hayana 'oda' na mtu.

Sasa hapo nilianza kutumia mawazo yangu na ule ushauri wa yule mama jirani, kwamba ili kuondoa haraka haraka inayonitokea niwe nachonga kwa vipimo vyangu na kuyaweka tayari kwa kununuliwa na wateja.

Mpaka saa nane na nusu mchana nilimaliza jeneza moja, lilibaki kupakwa vanishi tu. Nilitandika mbao nikachukua kamba na kuzungusha kisha nikaliburuza mpaka ndani. Hiyo ndiyo ilikuwa staili yangu ya kuingiza ndani na kutoa nje majeneza bila kuomba msaada kutoka kwa watu.

Baada ya hapo nilianza kuweka sawa mbao za kile kitanda cha yule kijana. Nilianza kuchonga na kurembesha kama alivyotaka mwenyewe.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 32.

Saa kumi kamili jioni, kuna watu wakaja wanataka jeneza la mwanamke. Walinipa vipimo kisha wakaniomba walifuate kesho yake. Waliomba mpaka saa sita ya kesho yake liwe tayari, kwani wana gari ambalo wakibeba tu, breki ya kwanza kwenye mwili wa marehemu ambapo walisema ulikuwa umehifadhiwa hospitali ya Amana.

Niliwahakikishia itakuwa hivyo walivyotaka.
Niliacha kazi ya kitanda na kuanza kupasua za jeneza. Kwangu haikuwa kazi kutengeneza jeneza. Sasa sijui ilikuwa ni nguvu zile mbaya au nini.

Nilifanya kazi hadi kwenye saa kumi na mbili na robo, nikakumbuka kuwa nilitakiwa kuonana na yule bibi ili nimsimulie mambo yangu. Na alikuwa na tabia ya kulala mapema zaidi kuliko mwingine yeyote ndani. Wakati mwingine saa mbili kasoro usiku utasikia amelala. Sababu ya uzee.

Nikawa ndani ya banda langu, nilichukua msasa na kopo la vanishi kwa lengo la kuviingiza ndani ya jeneza lile ambalo nililimaliza toka saa nane mchana. Lakini wakati nalifungua tu mfuniko wa lile jeneza, ghafla nilishtuka nimeshikwa shingo na kuingizwa ndani ya jeneza kisha likafungwa na kukawa na giza totoro humo ndani ya jeneza.


Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 33.

Hofu kuu ilinipata kuhusu tukio lile, ilibaki kidogo tu mapigo ya moyo yasimame kwa mshtuko nilioupata kwa kujikuta nimo ndani ya jeneza nililolitengeneza mwenyewe. Hewa ilianza kuwa nzito kutokana na kukosa nafasi ya kupitisha hewa.

Niligusa mfuniko ili kuusukuma juu hata uanguke mbali ili mradi niweze kutoka au nipate hewa nzuri. Lakini ghafla! Mkono wangu ulishikwa na uzito wa kumudu kufanya hivyo nilivyofikiria kufanya.

Nilihisi lile ni tatizo jingine kwani ilinipa picha kuwa, lengo la mimi kufikwa na tukio lile lilikuwa ni kuniua kabisa.
"Jam......," nilitaka kusema jamani naombeni mniache lakini niliishia kusema hivyo tu, jam...!

Sasa hali yangu ya mwili ilibadilika, nilianza kulowa jasho kwa muda mfupi tu tangu kuingia ndani ya jeneza.
Hapo nilijigundua kuwa nilikuwa nimelala chali, wakati nawaza hivyo ghafla! Nilisikia geti kubwa likifungwa tiiii. Halafu kukafuatiwa na mlio wa kitasa kufungwa kufuli.

Ulipita ukimya wa ajabu mie ndani ya jeneza na chumbani kwa ujumla. Nilijiuliza mwenyewe kwamba, je, nini kitatokea kufuatia tukio lile?

"Nyaaau....nyaaau," nikasikia mlio wa paka ukitokea jirani kabisa na lilipo jeneza ambalo mimi nilikuwa ndani yake.
Mara nilisikia jeneza likiguswa na kuparuliwa na kucha za miguu ya paka huyo huku sauti ikiendelea kusikika kila wakati.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 34.

Mara nilisikia jeneza likiguswa na kuparuliwa na kucha za miguu ya paka huyo huku sauti ikiendelea kusikika kila wakati.
Nilikuwa nikitetemeka mwili mzima kwa hofu. Nilikuwa nikihema kwa nguvu huku nikifanya jitihada za kuzuia sauti yangu isisikike nje ya jeneza nikiamini kuwa, huenda sikuwa nikijulikana kama mimi nimo ndani ya lile jeneza.

Punde tena nilisikia yule paka akipainua juu ya lile jeneza. Hapo sikumbuki nini kiliendelea kumbe nilipoteza fahamu ghafla. Nilipokuja kuzinduka jeneza lilikuwa wazi. Halikuwa na mfuniko pia kulikuwa na hali fulani kama ya mwanga ndani ya kile chumba. Nikiwa bado nimelala chali nilifumbua macho zaidi ili nione ni nini kinaendelea.

Baadhi ya mabati yalikuwa na matundu madogo madogo yaliyoniwezesha kuona nje kwa juu angani. Kulionekana mwanga mkubwa ambao ulinifanya nitambue mara moja kuwa jua linawaka.

Niliinuka taratibu na kukaa lakini mle mle ndani ya jeneza nikagundua hata geti kubwa la kuingilia ndani ya kibanda changu lilikuwa wazi kiasi kwamba niliweza kuona moja kwa moja nje jua likiwaka sana.

Nikiwa bado nimekaa ndani ya jeneza huku nikiangalia kila kona na kila upande wa lile banda langu. Akili ikiniambia kuwa nilikuwa nimelala ndani ya lile jeneza toka jana yake mpaka muda huo nashtuka.

"Hivi ni kweli?" nilijiuliza mwenyewe, halafu pia wakati naangalia mle ndani chumbani, nikagundua kuwa ule mfuniko haukuwemo ndani ya kile kibanda.

Hilo nalo lilinishangaza sana, nakiri kuwa sikuwa na ujasiri wowote wa kupambana na yale yote yaliyokuwa yananitokea bali ni Mungu mwenyewe alinipa ujasiri wa kuvumilia na kuonekana kama vile nilikuwa jasiri.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 35.

Nilikuwa bado natetemeka nilitembea kwa kunyata mpaka nje. Kitu cha kwanza ambacho macho yangu yalikutana nacho ni mfuniko wa lile jeneza.

"Ha!" nilihamaki. Kitu cha pili macho yangu yalikutana nacho ni boksi dogo la mbao ambalo ndani yake mlikuwa na randa, nyundo, msumari na msasa.
Moyoni nikasema ama kweli duniani kuna mambo na mambo yenyewe ndiyo yale yaliyokuwa yananitokea mimi.

"Leo mbona umewahi sana, una kazi za watu nini?" sauti ya yule mama jirani iliniingia masikioni. Haraka sana niligeuza uso kuangalia upande wa nyumbani kwake ambapo ile sauti ilitokea.

"Shikamoo mama," nilimsalimia yule mama bila ya kumjibu swali lake la mwanzo.
"Marahaba lakini hujanibu," yule mama aliniambia akiwa mbali kidogo.
Moyoni nilimuona yule mama jinsi alivyo mnafki. Nilivyochukulia mimi ni kwamba alijua kuwa nililala kibandani kwangu.

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 36.

Moyoni nilimuona yule mama jinsi alivyo mnafki. Nilivyochukulia mimi ni kwamba alijua kuwa nililala kibandani kwangu.
"Yupo baba mmoja jana alisema atakuja mapema sana," nilimjibu.
Wakati huo ilikuwa yapata saa moja na nusu hivi asubuhi.

Yule mama alirudi kwake huku akinipongeza kwa uwezo wa kuamka asubuhi sana, akidai yeye asingeweza.

Mpaka anazama kwake, macho yangu yalikuwa yakimsindikiza huku nikimsikitikia moyoni. Imani na yeye ilinitoka kabisa. Nilijua ndiyo adui yangu mkubwa wa mambo yote yale yaliyokuwa yakinitokea.
Nilikwenda kwenye duka moja la jirani, nikanunua maji madogo, nilirudi na kuyanawa usoni ili kujiweka sawa.

Moyoni nilikuwa nimepania kumsimulia yule bibi mwenye nyumba wangu mambo yangu yote kama nilivyomuahidi kufanya hivyo juzi hivyo usiku. Lakini kwa sababu kulikuwa kuna wateja waliodai wangefika mapema, nilikuwa nikiwasubiria kwanza ndipo nirudi nyumbani kuoga na kubadili nguo kisha kurudi tena.

Lakini kazi ikawa moja, sikujua nianzie wapi kufanya kazi zangu maana bado mwili ulikuwa ukitetemeka. Hata mikono nayo ilikuwa ikitetemeka.

Kuugusa ule mfuniko pale chini moyo wangu ulikataa huku nikiamini kwamba nitakapofanya hivyo kitu kikubwa sana kitatokea.
Niliingia ndani ya banda kisha nikasimama katikati, nikainua mikono juu na kuomba dua kwa Mola.

"Ee Mola nilinde kwa kila kitu," nilisema kwa sauti ya juu. Halafu nikatoka moja kwa moja mpaka kwenye ule mfuniko. Niliugusa kwanza kisha nikaunyanyua baada ya kuona shwari. Nikagundua hakukuwa na lolote baya. Kuanzia hapo nilianza kazi rasmi ya kumalizia kazi ya watu.

Saa saba juu ya alama nilikuwa nyumbani nikijiandaa kuoga. Hapo ni baada ya kujieleza kwa wapangaji wenzangu na bibi yaliyonipata jana yake. Karibu wote hawakuniamini.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 37.

Nilipomaliza kuoga nilimtafuta yule bibi ili niongee naye kuhusu matatizo yangu mwanzo hadi mwisho. Lakini alikataa akidai kwamba hakuwa tayari kuongea na mimi kwa vile yale niliyomgusia tu ya kulala ndani ya jeneza yalionyesha ni jinsi gani nilivyo muongo. Niliumia moyoni kwa mtazamo wake huo.

Alishikilia msimamo huo hali iliyonifanya nimuache na kuondoka zangu kurudi kazini. Umbali mdogo tu kutoka pale nyumbani niliitwa kwa nyuma. Nilipogeuka nilimuona mpangaji mwenzangu akija kwa mbio.
"Unajua kuna mambo uliongea pale nyumbani sijaamini. Lakini baadaye naanza kupata picha kuwa ni kweli," alisema baada tu ya kunifikia.

"Unaweza kupoteza muda wako tukae sehemy tuongee kidogo kuhusu yale maongezi yako?" aliniuliza yule mpangaji. Nilimkubalia, tukaondoka mpaka kwenye mgahawa mmoja.

Huyu mpangaji mwenzangu alinielezea matatizo yake makubwa sana tena ya kutisha. Nayo ni ya ajabu ajabu pia yaliyofanana na yangu. Mwisho akamaliza kwa kuniambia;

"Lakini siku moja mtu mmoja hapa hapa mtaani aliniambia kuwa bibi yetu mwenye nyumba aliwahi kufa akafufuka zamani kabla hatujaamia. Kwa hiyo toka hapo ana vituko vituko. Tujipange sana."

Nilimtumbulia macho kumwangalia yule mpangaji mwenzangu. Niliamini kuwa, hakuwa anajua matatizo yangu kwa undani. Kwani yeye alikuwa akiniambia habari za pale nyumbani, wakati mimi mwenzake nilikuwa nikiteseka na habari za kazini kwangu.

Kwa pale nyumbani toka nimehamia sikuwahi kuona au kuhisi kitu chochote kile ambacho kingenitia wasiwasi juu ya nyumba ile. Kwanza nilikuwa nikilala usiku, hakuna kushtuka mpaka kunakucha asubuhi.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 38.

"Aisee sasa hilo mimi sijalijua. Labda niache nalo nilifanyie kazi," nilimjibu huku nikisimama kwa ishara kuwa, nilikuwa na haraka sana.

"Poa lakini kuwa makini nalo sana. Hakuna aliyekuwa haamini kama mimi lakini siku ya siku nikakubali. Hivi mkataba wangu ukiisha mwezi wa kumi na mbili natafuta nyumba nyingine," alinijibu naye akasimama.
"Siyo kwamba nakataa ila nasema pale nyumbani sijawahi kufanyiwa au kuyaona mauzauza," nilimjibu.

"Kwani mpaka nyumbani, vuta kumbukumbu ni lini hayo mambo yako yameanza kukutokea kama si baada ya kuhamia hapa," aliniambia huku akinipa mkono wa kuniaga kisha akaniambia "Baadaye."

Sikumjibu swali hili, ila tu pale pale nilianza kuvuta kumbukumbu ya kauli yake ya mwisho kwamba ni lini mauzauza yangu yalianza.

Nikiwa njiani kuelekea kazini kwangu, nilikisumbua kichwa changu kwa kuvuta kumbukumbu. Nikagundua kuwa, hakuna ubishi bali ni kweli ni mambo ya ajabu ajabu yalianza kunipata baada ya kuanzisha kibanda cha useremala, lakini nikiwa nimeanza kuishi kwenye nyumba ya yule bibi.

"Ina maana aniachie nyumbani aje kunichezea kazini kwangu? Mbona hajawahi kufika?" nilijiuliza mwenyewe.

Na siku hiyo kwa mara ya kwanza nilijigundua kuwa, nilianza kupungua mwili kwa sababu ya mawazo na matukio yaliyokuwa yakinipata kwa hali ya kawaida ya mwanadamu kama mimi haikuwa rahisi kuyavumilia.

Nilikuwa nimetoboa tundu jipya kwenye mkanda wa suruali.
"Mh usalama wangu wa maisha ni mdogo sana," nilijikuta nikisema.


Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 39.

Na siku hiyo kwa mara ya kwanza nilijigundua kuwa, nilianza kupungua mwili kwa sababu ya mawazo na matukio yaliyokuwa yakinipata kwa hali ya kawaida ya mwanadamu kama mimi haikuwa rahisi kuyavumilia.

Nilikuwa nimetoboa tundu jipya kwenye mkanda wa suruali.
"Mh usalama wangu wa maisha ni mdogo sana," nilijikuta nikisema."Sana," nilisikia kama sauti ikinijibu.

Nilishtuka na kuangalia huku na kule. Lakinu kila mtu alikuwa na shughuli zake na wala hakuna aliyekuwa hata akiniangalia.
"Hii kali," nilisema.

"Tena sana," kama sauti ilinijibu tena.
Nilianza kuogopa hali hiyo. Kwani sasa ilikuwa kama matukio ya kunikabili zaidi mimi na kazi yangu. Niliumia sana moyoni huku nikiendelea kujiuliza ufumbuzi wake ni nini.

Nilipofika kazini kwangu baadhi ya watu niliokutana nao waliniambia kuwa, wakati nimetoka kwenda nyumbani, nyuma kuna watu walifika wakitaka jeneza. Wakanishauri kwamba inabidi nitafute mtu wa pili kwa ajili ya kusaidiana naye kazi ili nitakapokuwa sipo, yeye awe badala yangu.
"Ni kweli na sawa kabisa," nilijibu kukubaliana na mawazo yao.

Lakini kabla sijaanza kazi nyingine yule mama jirani aliniita nyumbani kwake na kuniambia kuwa, hajaniambia tu, lakini ameamua kuniambia.
"Usiku wa kuamkia leo nimekuota wewe," alisema.

"Kivipi mama," nilimuuliza, nikaanza kuingiwa na wasiwasi.
"Eti nimekuota unakwenda kuzikwa,halafu watu waliokuwa wakienda kukuzika makaburini walikuwa wakicheka sana kwa furaha."

Nilibaki nimeyatumbua macho yangu nikimwangalia mama kutokana na hiyo ndoto yake ambayo ilizidisha mapigo ya moyo wangu.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 40.

"Mama we acha tu, mimi mwenyewe nikikwambia mambo utashangaa sana," nilimwambia.
"Enhe...niambie," alisema yule mama huku akijishika kidevu na kukaa sawa ili kusikiliza.
Nilimsimulia tukio zima la mimi kulala ndani ya jeneza. Kila hatua niliyomweleza alionekana kushtuka na kukaa sawa tena na tena.

"We kijana ulikuwa unaota au unaniambia habari za kweli?" aliniuliza.
"Ni kweli kabisa mama."
"Mle kibandani kwako?"
"Ndiyo mama," nilimjibu bila shaka.
"Na hilo jeneza lipo?"

"Ndiyo lile ambalo wenyewe walikuja kulichukua saa zile."
"Kwanini hukupiga kelele?"
"Sikufikiria halafu humo ndani ya jeneza nisingeweza kusikiwa."

"Lakini ungejaribu si ajabu ungepata msaada. Yaani unaniambi habari mbaya sana," alisema mama.
Nilikaa kimya kwa muda kisha nikamsikia yule mama akisema.

"Fanya juu chini uende nyumbani kwenu ukakutane na wazazi wako uwaeleze kila kitu labda kuna mambo ya tambiko ya kimila hayajakaa sawa."
Niliinama nikifikiria maneno yake kisha nikamjibu.

"Sawa mama nitafanya hivyo."
Nikiwa nimesimama kutoka, kwa nje nikasikia sauti ya yule babu wa kwanza aliyetoweka kiajabu (Mzee Jumaa) ikisema.
"Huyu bwana mchonga mbao yuko wapi?"
Kwanza nilishtuka sana kuisikia. Nilimwangalia yule mama ambaye naye alionekana kuisikia sauti hiyo.

Tulitazamana lakini hakuna aliyemwambia mwenzake lolote lile. Kwa sababu sauti yake niliizoea sana, nilitokam mbio ili kuonana naye.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 41.

Hakukuwa na mtu yeyote katika eneo lile kwani sikuona hata dalili ya kuwepo kwa kuku achilia mbali binadamu, au mzee kama yule babu ambaye ndiye aliyesababisha kutoka mbio baada ya kumsikia sauti yake.

"Vipi kama nilimsikia babu yako akiongea hapo nje, si yeye?" alisema yule mama wa jirani huku akiwa amesimama nje ya nyumba yake. Ina maana tulivyoangaliana kila mmoja alijua amesikia nini.

"Hata mimi mama nimesikia hivyo hivyo, ndiyo maana nimetoka mbio," nilimjibu huku miguu ikitetemeka sana kwa woga. Si mchezo.

"Yuko wapi sasa, amekwenda alipoona hakuna mtu?"
"Sijamuona mtu," nilimjibu mama huku mapigo yangu ya moyo yakiwa yanakwenda mbio.

"He! Kweli?" aliniuliza.
"Kweli mama, nilitoka kwa ajili hiyo na mimi," nilimjibu tena kwa kumhakikishia kuwa niliyokuwa nikiyasema ni ya kweli kabisa.
"Maajabu basi," aliniambia yule mama akiwa amesimama nje ya nyumba yake huku amejishika kiuno.

"Mama mambo makubwa. Sidhani kama nina maisha mbele yangu," nilimjibu mama ambaye naye alisimama akinishangaa sana.
Siku hiyo nilirudi nyumbani mapema sana kisha nikalala tu. Ingawa nilikuwa na kazi za watu, lakini sikuona kama kulikuwa na umuhimu wa kuzifanya kutokana na hali yangu kuwa mbaya.
***

Usiku nikiwa nimelala, lakini sijachukuliwa na usingizi moja kwa moja, nilipata mawazo mengi sana. Kwamba asubuhi inayofuata nisafiri kwenda nyumbani Mabawa, Tanga ili nikaelezee matatizo yangu kwa wazazi na ndugu mbalimbali ambao wangeweza kunisaidia kimawazo badala ya kusubiri kifo au matatizo makubwa zaidi ya yale yaliyokuwa yakinitokea.

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 42.

Lakini mawazo yalipingana, kwani kwa upande mwingine niliwaza kutosafiri kabisa, bali nikabiliane na matatizo hayo mwenyewe, lakini mawazo yale ya mwanzo yaliniambia hapana. Lazima nisafiri kwenda nyumbani Tanga ndiko kwenye suluhisho la mwisho la matatizo yangu.
Mpaka kunakucha asubuhi, sikuwa nimepata suluhisho la nisafiri au vipi.

"Leo huendi kazi bwana?" aliniuliza bibi mwenye nyumba aliponiona nikiwa nimesimama nje ya nyumba. Hapo ilikuwa saa mbili na nusu muda ambao mara nyingi nakuwaga sipo nyumbani.

"Nitakwenda bibi lakini pia huenda nikasafiri," nilimjibu.
"Kwenda wapi tena?" aliniuliza.
"Nafikiria kwenda nyumbani," nilimjibu.

"Wapi Tanga?"
"Ndiyo."
"Kuna nini tena?"
"Kusalimia tu bibi," nilimjibu.
Ghafla alisimama na kuingia ndani kwake huku akiniambia nisiondoke mpaka atoke.
Kweli nilisimama nje mpaka alipotoka ambapo alikuwa ameshika kitabu kidogo kisha akakaa kwenye kiti kidogo alichokuwa amekalia toka mwanzo.

"Hiki kitabu changu ni kama cha utabiri. Nikikilalia huwa hakuna mabaya wala mazuri ya mtu ambayo yanaweza kunipata. Uliponiambia kuhusu yaliyokupata kazini kwako kwanza nilikukatalia lakini baadaye nilikuja kukubali baada ya kulala usiku," bibi aliniambia.


Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 43.

Nilishangaa sana lakini sikumuuliza kwanini siku ile niliposema alikataa kwamba si kweli. Kwanini sichukue hicho kitabu na kuangalia kama alivyosema akitumia hicho kitabu anakuwa anajua yote.

Kwa mimi moyoni niliwaza kuwa, huenda ni kweli huyu bibi alikuwa na mambo yake fulani kama alivyoniambia yule mpangaji mwenzangu.

Sasa alihisi kitu baada ya kumwambia huenda nikasafiri kwenda nyumbani. Hayo ndiyo yalikuwa mawazo yangu mimi kama mimi.

"Kwa hiyo bibi unataka kuniambia nini?" nilimuuliza nikiwa bado nimesimama.
Niliamini moyoni mwangu asingeweza kunishauri jambo zaidi ya kuniambia nisisafiri ila nimuombe Mungu.
Kwani kama alihisi kusafiri kwangu ni kwenda kupambana na mtu aliyekuwa akinisumbua, basi ina maana yeye ndiye nitakayekuwa napambana naye.

"Mimi sina cha kukwambia kwa nyinyi watu wa Tanga bwana nani asiyemijua. Nimeanza kusikia sifa za Tanga siku nyingi sana. Tanga kuna wachawi, Tanga kuna mauzauza. Tanga kuna kila....," alipofikia hapo aliishia kusema.
Matumaini mpya yalinijia kuwa, kwa kauli yake bibi lazima aliogopa kitakachotokea baada ya safari yangu.

Pia, niliamini kwa asilimia zote kwamba, bibi ndiye mbaya wangu kama nilivyodokezwa na kama nilivyohisi mwenyewe baada ya kupiga mahesabu ya siku ya kuhamia pale kwake na mauzauza yalipoanza.

"Sasa bibi mbona sijakuelewa, unasema huna la kusema halafu unasema umeanza kuisikia Tanga siku nyingi sana. Na unataja sifa za Tanga huku ukisema umeanza kuisikia zamani, sijakuelewa una maana matukio yangu yanatokana na kuwa mtu wa Tanga au?" nilimuuliza bibi huku nikimsogelea kwa upendo kabisa. Moyoni nilijua nimemmaliza sasa hata kabla sijasafiri.

Na nilipokumbuka habari kwamba eti alikufa akafufuka, nikaona siyo, labda alitaka kufa, kwani kwa mtu aliyekufa akafufuka asingeogopa kusikia mimi nakwenda Tanga kama kweli ndiye aliyekuwa akinifanyia vioja vyote vile.
"Hapana hujanielewa nini sasa? Nimeingia ndani nimetoka na kitabu na kukuelezea kila kitu," aliniambia bibi.

"Kwa hiyo una maana Tanga ndiko yalikonikuta yote hayo?" nilimuuliza kwa mtego.
"Aa, sina maana hiyo, ina maana bado hujanielewa kijana wangu?"

Je nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 44.

"Sijakuelewa bibi, au unataka kusema matatizo yanayonipata yalitokea nyumbani Tanga?"
"Kijana nasema hivi yale uliyosimulia siku ile kwamba yalikutokea huko kazini kwako, yaendee Tanga vipi mpaka nikufafanulie?" alisema bibi.

Hapo tena akawa amebadili mtazamo wangu kuhusu yeye. Wakati mimi nilijua yeye kababaika, kumbe sivyo, amefurahi sana na ushauri wake ni huo.

"Mh," niliguna.
"Unaguna nini sasa?"
"Sijajua nini kinaendelea bibi," nilimjibu.
"Hujajua nini bwana. Kila kitu kiko wazi kabisa. Wewe safiri, kawaambie wazazi wako kila kitu kuhusu matatizo yako. Wao watajua wakufanyie nini, vinginenvyo hapa mjini kijana wangu utakufa siku si zako," alisema bibi.

Niliingia ndani bila kumuaga bibi nilipokuja kutoka, nilikuwa nimeshika begi langu dogo mkononi nikimwambia bibi.
"Bibi labda keshokutwa au mtondogoo ndiyo nitarudi."

"Haya bwana wahakikishie kwamba hawa watu unaokaa wanajua matatizo yako," alisema bibi wakati natoka.

Njiani wakati nakwenda kituoni niliingiwa na mawazo kuwa, bado pengine yule bibi ndiye aliyekuwa mbaya wangu. Na pengine alikuwa akisubiri nifike nyumbani kwetu ili aanze kunifanyia mauzauza.

Nilifika kituo cha mabasi na kupata basi saa nne kamili asubuhi tayari kwa safari ya kwenda Tanga.

Nilifika nyumbani saa nane mchana, baadhi ya ndugu walikuwepo, lakini wengine walikuwa katika mihangaiko yao.
Waliokuwepo nyumbani walinipokea kwa mshangao kwani walisema kuwa, nimebadilika sana.

Nimenenepa sana na kunawiri tofauti na nilivyoondoka kwenda Daresalaam.
Jioni yake mama aliniuliza mambo yangu yanakwendaje Dar? Nikamjibu kuwa nilikuwa niko pale nyumbani kwa makusudi maalum.
"Lakini yaliyonileta siwezi kukwambia mpaka awepo baba," nilimwambia mama.

"Ina maana kuna matatizo, mi nilijua umekuja kusalimia," alisema mama.
"Hapana mama, kuna matatizo tena makubwa sana."

Kwa kauli yangu hiyo, ilibidi mama afanye kazi ya kumtafuta baba kwa kuwatuma watoto sehemu mbalimbali ambazo anapenda kufika, hasa kwenye maeneo wanayocheza bao.

Mara baba alifika haraka sana akisema kuwa, aliweza kuhisi kuna mgeni nyumbani lakini kila alipokuwa akitaka kusimama kurudi nyumbani alikuwa akisikia uvivu.

Je nini kitaendelea?
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom