Mwakyembe awa mbogo
Atoboa siri ya ugomvi wake na Mwakipesile
Adai kiongozi huyo anafanya kazi ya mafisadi
Ataka atambue kwamba yeye ni RC na siyo MC
Na Gladness Mboma
MBUNGE wa Jimbo la Kyela mkoani Mbeya, Dkt. Harrison Mwakyembe amesema kuwa tatizo analoliona kati yake na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Bw. John Mwakipesile ni harakati zake za kutaka kumng'oa katika jimbo la Kyela, jambo ambalo hataweza.
Alisema kuwa kazi anayoifanya Bw. Mwakipesile katika jimbo lake ni sawa na kuuza kofia za polisi ambazo hazinunuliki na kwamba anajisumbua, anajidhalilisha na kujifedhehesha licha ya kutumwa na mafisadi kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.
Dkt. Mwakyembe alitoa kauli hizo za kejeli alipozungumza na gazeti hili kujibu hoja za Bw. Mwakipesile kuwa mbunge huyo anapotoshwa na wapambe wake wanaompa taarifa za uongo na kwamba hajawahi kuwaomba wazee wa Mbeya ili wawapatanishe.
"Ni lazima Bw. Mwakipesile atambue kuwa yeye ni RC na siyo MC kwa maana ya msema chochote. Mkuu wa mkoa mmoja kati ya wakuu wa mikoa 21 kuzungumza magazetini kila siku akiwarukia wabunge wanaopambana na ufisadi ni dalili ya kuweweseka.
"Ninalazimika kusema kuwa mwenzetu anahitaji ushauri nasaha, waandishi mchunguzeni Bw. Mwakipesile ili kujua anapatana na mbunge gani mkoani Mbeya?" alisisitiza Dkt. Mwakyembe.
Dkt. Mwakyembe aliongeza kuwa, kila mtu anatambua kuwa Bw. Mwakipesile anashinda Kyela kufanya kampeni za kuhakikisha kuwa, anamuondoa mwaka 2010 katika uchaguzi mkuu na kwamba Serikali inatambua jambo hilo.
"Hili tatizo halinipi tabu hata kidogo kwa sababu kazi anayofanya ni kama kuuza kofia za polisi mali ambazo hazinunuliki anajisumbua, anajidhalilisha na kujifedhehesha," alisema.
Dkt. Mwakyembe alisema kuwa alipata kura asilimia 93 katika uchaguzi mkuu mwaka 2005, lakini anashangazwa na kauli aliyoitoa Bw. Mwakipesile katika gazeti hili kwamba wapambe ndio wanaompotosha na kumtaka atambue kuwa wapambe hao ni wananchi wote wa Kyela.
"Tatizo la Bw. Mwakipesile anadanganywa sana na mafisadi ambao wanamtumia kama wakala, hiyo kazi waliyompa kwa Kyela ni ngumu kwelikweli, ni sawa na kuuza kofia za polisi kwa wananchi hivyo ni lazima atambue kuwa mimi ni mti mkavu usiochimbwa dawa," alisisitiza Dkt. Mwakyembe.
Alisema kuwa yeye alikuwa nje ya nchi na amerudi juzi ndipo alipomkuta mwenzake akiongea hovyo katika vyombo vya habari huku akitoa malalamiko kwamba yeye ndiye anayekwamisha maendeleo ya Mkoa wa Mbeya.
Alipoulizwa kiini cha mgogoro kati yake na Bw. Mwakipesile unasababishwa na nini, Dkt. Mwakyembe alisema kuwa yeye hana mgogoro wowote na mkuu huyo wa mkoa, bali yeye RC huyo anayekwamisha maendeleo ya mkoa huo kutokana na muda wote kukaa Kyela kwa lengo la kumwondoa mbunge mwaka 2010.
Akizungumzia madai ya kutaka kuuawa alisema kuwa huo ni uongo na kwamba anaokoteza maneno barabarani na kuyafanyia kazi.