Kamati Kuu CCM yabaini mkataba wa jengo la Vijana una kasoro saba
Na Kizitto Noya
TUHUMA zilizotolewa na mwanasiasa kijana, Nape Nnauye dhidi ya mkataba wa uendeshaji wa jengo la makao makuu ya Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM), zinaonekana kuwa na nguvu baada ya Kamati Kuu ya chama hicho kukataa kuupitisha mkataba huo.
Akiongea na waandishi wa habari baada ya kuchukua fomu za kugombea uenyekiti wa UVCCM Julai 15, Nape, ambaye ni mtoto wa mwanasiasa aliyekuwa na heshima ndani ya CCM, Moses Nnauye, alidai kuwa mkataba huo unanuka rushwa na kumashambulia mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini la vijana, Edward Lowassa, mwenyekiti wa wake Dk Emmanuel Nchimbi na aliyekuwa katibu mkuu Amos Makalla kuwa walihusika.
Na juzi ilibainika kuwa mkataba huo una matatizo na hivyo kuifanya Kamati Kuu, maarufu kama CC, kusita kuupitisha baada ya kikao chake kilichoisha usiku mwingi mjini Dodoma.
Habari zilizolifikia gazeti hili jana kutoka vyanzo vilivyo ndani ya kikao hicho kilichofanyika kwa awamu mbili kuanzia juzi alasiri, zinasema CC imegoma kupitisha mkataba huo kwa kuwa una kasoro kuu saba na imeagiza ukaangaliwe upya na kufanyiwa marekebisho kabla ya kusainiwa.
Kwa mujibu wa habari hizo, baada ya kuutupa mkataba huo, kamati imeunda tume ya watu watatu kuchunguza mazingira ya namna ulivyoingiwa na kuuboresha ili uwe wa faida.
Vyanzo hivyo vya habari vimewataja wajumbe wa tume hiyo kuwa ni Pindi Chana, Andrew Chenge na Abdalah Kigoda.
"Ni kweli mkataba leo (jana) umejadiliwa lakini haukupitishwa na imeundwa tume kwa ajili ya kuuchunguza na kuuboresha ili uwe wa faida," alisema mmoja wa wajumbe wa kikao hicho ambaye hakutaka kutajwa gazetini.
Taarifa zilieleza pia kwamba tume hiyo haitafanya kazi peke yake bali itafanya kazi kwa pamoja na viongozi wa Umoja wa Vijana, hatua kwa hatua na watakapomaliza suala hilo litakabidhiwa kwa kamati ya utekelezaji na hatimaye Baraza Kuu na hatimaye Kamati Kuu tena.
Mkataba huo uliwasilishwa katika kikao cha CC kwa ajili ya kusomwa, kupitiwa, kukubalika na baadaye kusainiwa, lakini baada ya kusomwa na kupitiwa, haukukubalika na wajumbe wakataka usisainiwe.
Habari zaidi zinasema wajumbe wa CC walitaka mkataba huo usisainiwe hadi ufanyiwe marekebisho katika vipengele saba ambavyo waliona kuwa vinautia kasoro, lakini kasoro hizo saba hazikuwekwa bayana.
Habari zaidi zinasema kuwa kutupwa kwa mkataba huo jana, kulimpa wakati mgumu katibu mkuu wa CCM, Yusuf Makamba, ambaye alilazimika kuitisha kikao cha dharura cha Sekretarieti ya chama hicho kujadili uamuzi huo wa CC.
Makamba amekuwa mstari wa mbele kuelezea kitendo cha Nape kukosoa mkataba huo kuwa ni utovu wa nidhamu na alimwita kijana huyo ofisini kwake na kumuweka kiti moto mara baada ya kutangaza hisia zake kuwa kuna harufu ya ufisadi katika uingiaji wa mkataba huo.
Makamba pia aliwaambia waandishi mapema wiki hii kuwa demokrasia inaheshimiwa pale tu watu wanapokuwa na nidhamu, akimaanisha kuwa kitendo cha Nape kukikosoa chama nje kuwa ni cha utovu wa nidhamu.
Katika tuhuma zake, Nape alienda mbali zaidi kwa kuwataka Lowassa, Nchimbi na kaimu katibu mkuu wa UVCCM, Frank Isaack kuwajibika kutokana na ama uzembe au kuhusika moja kwa moja na mkataba huo.
Alisema Lowassa kwa mamlaka yake ya kuwa mwenyekiti wa bodi ya wadhamini ya UVCCM alishindwa kutekeleza majukumu yake ya kusimamia mali za jumuiya hiyo.
Alisema mkataba huo una kasoro nyingi, ikiwemo mkataba huo kuwa wa maisha na kipengele kinachosema mwekezaji atamiliki asilimia 75 ya hisa wakati UVCCM wataambulia asilimia 25.
Nape alitaja kasoro nyingine za mkataba huo kuwa ni mwekezaji kukosa mtaji wake na kutumia hati za jengo la UVCCM kwenda kuomba fedha benki, jambo alilosema kuwa hata UVCCM yenyewe ingeweza kulifanya.
Alibainisha kuwa mradi wa jengo hilo ni mkubwa lakini una mikono ya vigogo ambao wamepanga kukata majina ya baadhi ya wagombea watakaokuwa na msimamo wa kuuhoji.
Siku moja baada ya Nape kutoa kauli hiyo, Makamba alimwita ofisini kwake kwa nia ya kumkaripia na kueleza kuwa Baraza la Wadhamini halipaswi kuwajibika kuhusu mradi huo kwa kuwa limetimiza wajibu wake, tena kwa kuvuka mpaka kwa sababu limelifikisha suala hilo katika vikao vya chama kwa ajili ya kuona linafanyika kwa uhakika.
Makamba alisema baada ya Baraza hilo kupelekewa na uongozi wa UVCCM mapendekezo ya mkataba huo, iliyapitia na kufanya marekebisho ambayo imeyaona yanafaa na kuyafikisha ofisini kwake Julai 7 mwaka huu ili ayapeleke kwenye vikao vya juu vya chama hicho.
Hata hivyo, kauli ya Makamba ilipingwa na baadhi ya wajumbe wa baraza la UVCCM ambao kwa nyakati tofauti walisema mkataba huo ni batili kwa kuwa hakuna kikao cha baraza hilo kilichoupitisha.
Wajumbe hao walisema asilani hawajabariki mkataba wa jengo hilo jipya na kusisitiza kuwa taratibu za kuupitisha zilikiukwa na kwamba ujenzi wake unasukumwa na vigogo wenye maslahi binafsi
Utata wa kauli ya Makamba ulianza kujitokeza pale aliposhindwa kueleza sababu za mwekezaji kusogeza vifaa eneo la ujenzi na kuanza kazi wakati alisema kuwa mkataba huo haujasainiwa.
Makamba alishindwa kueleza suala hilo na kuwatupia mpira viongozi wa UVCCM ambao hadi leo wanashindwa kuondoa utata huo, akidai kuwa hahusiki na masuala ya ujenzi.
Mwenyekiti wa UVCCM anayemaliza muda wake, Dk Emmanuel Nchimbi alikwepa kuzungumzia utata huo kwa maelezo kuwa yeye si mtendaji wa taasisi, bali kiongozi wa vikao vya taasisi hiyo.
Naye kaimu katibu mkuu wa UVCCM, Francis Isack alisema suala la mwekezaji kusogeza vifaa eneo la ujenzi kabla ya mkataba kusainiwa, ni la kawaida katika mikataba.
Kauli ya Nape kwamba baadhi ya vigogo wamepanga kukata majina ya wagombea wa uchaguzi wa UVCCM watakaohoji uhalali wa makataba huo, imeanza kujidhihirisha baada ya Baraza Kuu la UVCCM kumvua uanachama na kupendekeza kwa CCM kumvua nyadhifa zote ndani ya CCM kwa tuhuma za kusema uongo kuhusu mkataba huo.
Mbali na maamuzi hayo ya Baraza Kuu, tayari Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM imemwekea alama E inayomaanisha hafai kuwa kiongozi kwa kigezo cha umri.
Mkataba huo umeshaamsha mvutano mkubwa ndani ya UVCCM ambayo tayari wanachama wake wamegawanyika kwa misimamo ya Nape.
Source: Mwananchi
Na Kizitto Noya
TUHUMA zilizotolewa na mwanasiasa kijana, Nape Nnauye dhidi ya mkataba wa uendeshaji wa jengo la makao makuu ya Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM), zinaonekana kuwa na nguvu baada ya Kamati Kuu ya chama hicho kukataa kuupitisha mkataba huo.
Akiongea na waandishi wa habari baada ya kuchukua fomu za kugombea uenyekiti wa UVCCM Julai 15, Nape, ambaye ni mtoto wa mwanasiasa aliyekuwa na heshima ndani ya CCM, Moses Nnauye, alidai kuwa mkataba huo unanuka rushwa na kumashambulia mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini la vijana, Edward Lowassa, mwenyekiti wa wake Dk Emmanuel Nchimbi na aliyekuwa katibu mkuu Amos Makalla kuwa walihusika.
Na juzi ilibainika kuwa mkataba huo una matatizo na hivyo kuifanya Kamati Kuu, maarufu kama CC, kusita kuupitisha baada ya kikao chake kilichoisha usiku mwingi mjini Dodoma.
Habari zilizolifikia gazeti hili jana kutoka vyanzo vilivyo ndani ya kikao hicho kilichofanyika kwa awamu mbili kuanzia juzi alasiri, zinasema CC imegoma kupitisha mkataba huo kwa kuwa una kasoro kuu saba na imeagiza ukaangaliwe upya na kufanyiwa marekebisho kabla ya kusainiwa.
Kwa mujibu wa habari hizo, baada ya kuutupa mkataba huo, kamati imeunda tume ya watu watatu kuchunguza mazingira ya namna ulivyoingiwa na kuuboresha ili uwe wa faida.
Vyanzo hivyo vya habari vimewataja wajumbe wa tume hiyo kuwa ni Pindi Chana, Andrew Chenge na Abdalah Kigoda.
"Ni kweli mkataba leo (jana) umejadiliwa lakini haukupitishwa na imeundwa tume kwa ajili ya kuuchunguza na kuuboresha ili uwe wa faida," alisema mmoja wa wajumbe wa kikao hicho ambaye hakutaka kutajwa gazetini.
Taarifa zilieleza pia kwamba tume hiyo haitafanya kazi peke yake bali itafanya kazi kwa pamoja na viongozi wa Umoja wa Vijana, hatua kwa hatua na watakapomaliza suala hilo litakabidhiwa kwa kamati ya utekelezaji na hatimaye Baraza Kuu na hatimaye Kamati Kuu tena.
Mkataba huo uliwasilishwa katika kikao cha CC kwa ajili ya kusomwa, kupitiwa, kukubalika na baadaye kusainiwa, lakini baada ya kusomwa na kupitiwa, haukukubalika na wajumbe wakataka usisainiwe.
Habari zaidi zinasema wajumbe wa CC walitaka mkataba huo usisainiwe hadi ufanyiwe marekebisho katika vipengele saba ambavyo waliona kuwa vinautia kasoro, lakini kasoro hizo saba hazikuwekwa bayana.
Habari zaidi zinasema kuwa kutupwa kwa mkataba huo jana, kulimpa wakati mgumu katibu mkuu wa CCM, Yusuf Makamba, ambaye alilazimika kuitisha kikao cha dharura cha Sekretarieti ya chama hicho kujadili uamuzi huo wa CC.
Makamba amekuwa mstari wa mbele kuelezea kitendo cha Nape kukosoa mkataba huo kuwa ni utovu wa nidhamu na alimwita kijana huyo ofisini kwake na kumuweka kiti moto mara baada ya kutangaza hisia zake kuwa kuna harufu ya ufisadi katika uingiaji wa mkataba huo.
Makamba pia aliwaambia waandishi mapema wiki hii kuwa demokrasia inaheshimiwa pale tu watu wanapokuwa na nidhamu, akimaanisha kuwa kitendo cha Nape kukikosoa chama nje kuwa ni cha utovu wa nidhamu.
Katika tuhuma zake, Nape alienda mbali zaidi kwa kuwataka Lowassa, Nchimbi na kaimu katibu mkuu wa UVCCM, Frank Isaack kuwajibika kutokana na ama uzembe au kuhusika moja kwa moja na mkataba huo.
Alisema Lowassa kwa mamlaka yake ya kuwa mwenyekiti wa bodi ya wadhamini ya UVCCM alishindwa kutekeleza majukumu yake ya kusimamia mali za jumuiya hiyo.
Alisema mkataba huo una kasoro nyingi, ikiwemo mkataba huo kuwa wa maisha na kipengele kinachosema mwekezaji atamiliki asilimia 75 ya hisa wakati UVCCM wataambulia asilimia 25.
Nape alitaja kasoro nyingine za mkataba huo kuwa ni mwekezaji kukosa mtaji wake na kutumia hati za jengo la UVCCM kwenda kuomba fedha benki, jambo alilosema kuwa hata UVCCM yenyewe ingeweza kulifanya.
Alibainisha kuwa mradi wa jengo hilo ni mkubwa lakini una mikono ya vigogo ambao wamepanga kukata majina ya baadhi ya wagombea watakaokuwa na msimamo wa kuuhoji.
Siku moja baada ya Nape kutoa kauli hiyo, Makamba alimwita ofisini kwake kwa nia ya kumkaripia na kueleza kuwa Baraza la Wadhamini halipaswi kuwajibika kuhusu mradi huo kwa kuwa limetimiza wajibu wake, tena kwa kuvuka mpaka kwa sababu limelifikisha suala hilo katika vikao vya chama kwa ajili ya kuona linafanyika kwa uhakika.
Makamba alisema baada ya Baraza hilo kupelekewa na uongozi wa UVCCM mapendekezo ya mkataba huo, iliyapitia na kufanya marekebisho ambayo imeyaona yanafaa na kuyafikisha ofisini kwake Julai 7 mwaka huu ili ayapeleke kwenye vikao vya juu vya chama hicho.
Hata hivyo, kauli ya Makamba ilipingwa na baadhi ya wajumbe wa baraza la UVCCM ambao kwa nyakati tofauti walisema mkataba huo ni batili kwa kuwa hakuna kikao cha baraza hilo kilichoupitisha.
Wajumbe hao walisema asilani hawajabariki mkataba wa jengo hilo jipya na kusisitiza kuwa taratibu za kuupitisha zilikiukwa na kwamba ujenzi wake unasukumwa na vigogo wenye maslahi binafsi
Utata wa kauli ya Makamba ulianza kujitokeza pale aliposhindwa kueleza sababu za mwekezaji kusogeza vifaa eneo la ujenzi na kuanza kazi wakati alisema kuwa mkataba huo haujasainiwa.
Makamba alishindwa kueleza suala hilo na kuwatupia mpira viongozi wa UVCCM ambao hadi leo wanashindwa kuondoa utata huo, akidai kuwa hahusiki na masuala ya ujenzi.
Mwenyekiti wa UVCCM anayemaliza muda wake, Dk Emmanuel Nchimbi alikwepa kuzungumzia utata huo kwa maelezo kuwa yeye si mtendaji wa taasisi, bali kiongozi wa vikao vya taasisi hiyo.
Naye kaimu katibu mkuu wa UVCCM, Francis Isack alisema suala la mwekezaji kusogeza vifaa eneo la ujenzi kabla ya mkataba kusainiwa, ni la kawaida katika mikataba.
Kauli ya Nape kwamba baadhi ya vigogo wamepanga kukata majina ya wagombea wa uchaguzi wa UVCCM watakaohoji uhalali wa makataba huo, imeanza kujidhihirisha baada ya Baraza Kuu la UVCCM kumvua uanachama na kupendekeza kwa CCM kumvua nyadhifa zote ndani ya CCM kwa tuhuma za kusema uongo kuhusu mkataba huo.
Mbali na maamuzi hayo ya Baraza Kuu, tayari Kamati ya Utekelezaji ya UVCCM imemwekea alama E inayomaanisha hafai kuwa kiongozi kwa kigezo cha umri.
Mkataba huo umeshaamsha mvutano mkubwa ndani ya UVCCM ambayo tayari wanachama wake wamegawanyika kwa misimamo ya Nape.
Source: Mwananchi