Riwaya: Scolastica Temu

Riwaya: Scolastica Temu

SEHEMU YA 48




ILIPOKOMEA...
Kwa sauti alisema, "Nilivyokwambia kuwa PAK ilikuwa ikiuzwa katika maduka makubwa, makubwa tu, sikuwa na maana kuwa nayajua maduka hayo. Namaanisha kuwa thamani ya PAK siyo ndogo. Ni vigumu kwa mtu mwenye kijiduka chake cha dawa kule Manzese, kuweka PAK akitarajia kuiuza ndani ya miezi sita."
***SASA ENDELEA***
"PAK inatengenezwa Athens, Ugiriki. Mwagizaji hana budi kuagiza katoni moja au zaidi, ikitegemea uwezo wake. Katoni moja ina chupa kumi na mbili za PAK. Mwagizaji analipa shilingi elfu sitini kwa chupa, na hapo bado hatujaweka vijiushuru vya bandari. Kwa jumla zitamgharimu pesa nyingi mwagizaji, si chini ya laki nane kwa katoni moja tu! Hapo sasa nd’o maana nakwambia kuwa siyo rahisi kwa muuzaji wa daraja la kati au la chini kuweza kuagiza PAK, kitu ambacho mauzo yake yanakwenda taratibu sana. Umenielewa?"
"Nimekuelewa, dokta," Ndonya alijibu kwa unyonge. Kisha akasimama bna kuanza kutoka. Mara tu alipogusa mlango, aligeuka na kusema, "Dokta, nashukuru sana kwa msaada wako. Mungu akipenda tutaonana tena."
"Ok."
Muda mfupi baadaye Ndonya alikuwa akivuka makutano ya barabara za India na Morogoro. Akawa akitembea kwa mwendo wa kikakamavu zaidi, akizidi kutokomea katikati ya mitaa hiyo ya Uhindini.
Hatimaye, baada ya kuyadharau maduka mawili ya dawa, aliingia katika duka la dawa lililokuwa Mtaa wa Kitumbini. Lilikuwa ni duka kubwa, zaidi ya maduka mengine mtaani hapo yaliyouza dawa kwa mfumo wa rejareja na jumla.
Wateja wasiopungua kumi walikuwa wakihitaji huduma kutoka kwa Mwasia mmojja mwenye tumbo kubwa. Ndonya alisimama, akiwa ni kati ya wateja hao ambao wengi wao walionesha dhahiri kuwa ni wanunuzi wa jumla. Kulikuwa na pilikapilika nyingi, kila mteja akionesha kuwa na haraka zaidi ya mwingine.
"Nipe katoni mbili za Panadol ya Kenya!”
“Oyaa…lete katoni moja ya Dakika Tatu!” wa pili ni kama alikuwa kifoka.
Mwingine alipaza sauti, “Paracetanol zipo?" hakusubiri jibu. Papohapo alinyoosha mkono wenye noti kadhaa huku akiamuru, "Toa katoni tatu haraka!"
Ndonya alikuwa miongoni mwa walioongeza idadi dukani humo, lakini hakuwa miongoni mwa wateja wa kawaida, waliohitaji bidhaa za kawaida. Yeye alikuwa na lake jambo. Akaishia kuziona bidhaa ambazo macho yake yalikwishazizoea na kinywa kilishazikinai. Zilikuwa ni dawa za kutibu maradhi, wala hakuiona hata sumu ya kuua panya, mende au wadudu wowote warukao au watambaao.
Akaendelea kuangaza huku na kule mithili ya mteja wa kawaida kama hao wateja wa kawaida. Hatimaye akaamua kumwita kijana mmoja ambaye jukumu lake kubwa lilikuwa ni kufuata ghalani katoni zilizoagizwa na mteja.
Kijana huyo alipomsogelea, Ndonya alitamka kwa mnong’ono, "Mkifunga duka saa saba, unikute pale kwa muuza mihogo ya kukaanga."
"Pale kwenye makutano ya mitaa ya Mosque na Mshihiri?"
"Hapohapo. Utapata lunch yako ya nguvu, siyo ile mihogo. Sawa?"
"Poa."
Kichwani mwa kijana huyo hakuwa na kumbukumbu yoyote kuhusu Ndonya. Hakumbuki aliwahi kuimwona wapi. Ni shinikizo tu la moyo wake kumtaka akubaliane na wito, japo alikuwa akihitaji kuhoji zaidi. Na aliamua kutohoji zaidi kwa wakati huo kwa kile alichoamini kuwa kitendo hicho kingezua hisia tofauti kwa bosi wake, mhindi yule mwenye tumbo kubwa.
*****
KWA Ndonya, utaratibu wa kula mihogo ya kukaanga ambayo hutayarishwa sehemu mbalimbali jijini Dar, hususan kando ya barabara, alishaucha tangu alipopata ajira yenye mshahara mnono na marupurupu kibao.
Sasa yeye alikuwa ni mtu wa kuingia katika migahawa yenye gharama kubwa, migahawa amayo mamilioni ya Watanzania wengine hawathubutu hata kuisogelea.
Lakini kwa siku hii, akizingatia kuwa tayari ameshawasiliana na yule kijana wa duka la dawa,alilazimika kuzikumbuka zile enzi zake. Ili aweze kuketi hapo kwenye biashara ya mihogo, ilimlazimu kuwa mteja halisi, jambo ambalo alilifanya.
"Mihogo miwili," aliagiza.
Dakika mbili au tatu hivi baadaye alikabidhiwa sahani ya mihogo iliyopondwapondwa na kuwekwa kachumbari juu yake. Hakuonesha kushangazwa na masizi yaliyoganda hapa na pale katika sahani hiyo. Ashangae? Ashangae halafu wateja wengine wanaokula mihogo hiyo nao wamshangae? Alikandamiza moyoni mshangao wake na kukiepuka kinyaa kilichomnyemelea kwa kasi ya kutisha. Akala mihogo hiyo taratibu, akivua muda katika kumsubiri kijana huyo.
Ni saa saba na robo kijana huyo alipotokea. Na Ndonya hakumchelewesha, aklimwita kando na kumnong’oneza, “Mtafungua saa ngapi?”
“Saa tisa kamili.”
Ndonya akachomoa noti ya shilingi 5,000 na kumpatia huku, kwa mnong’ono uleule, akisema, “Kuna suala moja muhimu. Tangulia pale Kili Hotel. Ukifika agiza chochote.”
“Poa.”
Dakika tano baadaye walikuwa pamoja Kili Hotel. Makoo yao yalikuwa yakishusha soda baridi matumbini mwao.
“Sasa nadhani tusipoteze muda,” Ndonya alianza. “Kuna kitu ambacho nakihitaji, na n’nadhani dukani kwenu kipo. Na kama hakuna hapo kwenu nadhani wewe utanipa mwangaza wapi pa kukipata.”
Kijana huyo alikunja uso na kumtazama Ndonya kwa mshangao. “Ni kitu gani hicho?” hatimaye aliuliza.
“PAK,” Ndonya alishusha sauti. “PAK inayotengenezwa Athens, Ugiriki. Unaifahamu?”
Kijana huyo alikuna kichwa huku akikodoa macho mezani. Kisha akamtazama Ndonya. “Naifahamu.”
“Naiweza kuipata?” Ndonya alimdaka.
Kijana akaguna. “Ni ngumu. Si unajua serikali I’shaipiga stop?”
"Hilo nalijua sana, dogo," Ndonya aliachia tabasamu la mbali. "Lakini pia najua kuwa bado ipo kwa wauzaji ingawa haiwekwi hadharani. Mimi naihitaji sana kama vile kuuhitaji Ufalme wa Mbinguni. Naitaka kwa gharama yoyote ile!"
Yalikuwa ni maneno yaliyomwingia vilivyo kijana huyo na kuchambuliwa akilini mwake kwa umakini wa hali ya juu. Picha ya noti nyingi za shilingi elfu kumi, kumi ikamjia akilini, noti ambazo angezimiliki baada ya mtu huyo kupata akitakacho.
"Naweza kuipata?" Ndonya alimshtua.
"Unaweza kuipata," kijana huyo alizinduka na kujibu kwa kujiamini.
"Una hakika?"
"Siku tanii. Mfuko wako tu."
Tabasamu la matumaini likachanua usoni pa Ndonya. Akanyanyua chupa ya Cocacola na kuipeleka kinywani. Akanywa mafunda machache kisha akairejesha mezani. Hatimaye, huku tabasamu likiendelea kuchanua, akasema, "Kama nilivyokwambia awali, ninaihitaji PAK kama ninavyotamani kuingia Paradiso. We nipe uhakika kama unaweza kuipata leo hii!"
"Unaweza kuipata!" kijana yule alisisitiza. “Kuipata s’o tatizo. S’o tatizo kabisa. Muhimu ni mkwanja tu!”
“Kiasi gani?”
“Siyo nyingi, fanya milioni tu.”
Ndonya alitokwa macho. Mwonekano wa kijana huyu haukuwa wa mtu wa kutamka kiwango hicho. Ndonya alitarajia kuambiwa atoe labda shilingi laki moja au mbili tu. Kiwango alichotajiwa, aliona ni kikubwa sana.
"Milioni moja?!" alimuuliza kijana huyo kwa mshangao.
"Nd’o maana'ake."
"Hapana, shusha kidogo mdogo wangu. Nitakupa shilingi laki tatu."
Kijana huyo akaachia cheko la dhihaka, cheko la kujiamini. “Sifanyi biashara hiyo, kaka. Kwa laki tatu labda kazunguke kwingine, labda utabahatisha. Na ukienda kichwakichwa kuuliza kwa kila mtu, utajikuta unadakwa na askari.”
Ndonya alikunja uso kidogo. Akamtazama kijana huyo kwa makini na kuubaini msimamo mkali uliodhihirika usoni pake. “Siki’za dogo,” hatimaye alisema kwa mnong’ono uleule “Hili ni dili lako we’ binafsi. Hakuna cha mhindi wako wala nani. Upo?”
***ITAENDELEA***

Sent using Jamii Forums mobile app
 
huyu jamaa ki-ndonya ana bahati mbaya ya kupoteza hela zake, wakati scola ana mpango wa kutoroka ye anagharamia sumu huku
kweli dua la kuku halimpati mwewe
 
SEHEMU YA 49



ILIPOKOMEA...
Ndonya alikunja uso kidogo. Akamtazamqa kijana huyo kwa makini na kuubaini msimamo mkali uliodhihirika usoni pake. “Siki’za dogo,” hatimaye alisema kwa mnong’ono uleule “Hili ni dili lako we’ binafsi. Hakuna cha mhindio wako wala nani. Upo?”
SASA ENDELEA..
“Siyo kwamba sijui kuwa hili ni dili langu,” kijana huyo alisema. “Najua sana. Lakini si unaijua bei ya PAK kabla haijapigwa marufuku?"
"Naijua. Ilikuwa ikiuzwa kati ya shilingi elfu hamsini na sitini."
"Hujakosea. Lakini sasa mimi na wewe tunafanya magendo. Tena biashara yetu ni hatari kama vile kujihusisha na biashara ya ‘unga.’
"Serikali i’shatangaza kuwa yeyote atakayekutwa na kitu hicho, hakutakuwa na mambo ya kupelekwa mahakamani; atatupwa
jela, akae huko hadi kufa kwake. Hebu fikiria, mimi hapa sijatimiza miaka thelathini, halafu eti leo niende kufia jela!"
Akiamini kuwa uwezekano wa kuipata sumu ya PAK ni mdogo, zaidi ya kwa huyo kijana, Ndonya alilazimika kuafikiana naye.
"Ok, tusiende mbali," hatimaye alisema. "Suala la pesa lisituchukulie muda. Siyo tatizo. Panga muda na jinsi ya kuwasiliana. Hapo utambue kuwa mambo yatakuwa mkono kwa mkono. Unanipa mzigo wangu, nakukabidhi kikokotoo chako. Tuko pamoja?"
"Nakusoma," kijana alijibu kwa kujiamini.
"Kwa hiyo?" Ndonya alikuwa na haraka.
“Nipe kitu kama saa mbili hivi.”
“Kuanzia?”
“Kuanzia pale tu nitakaporipoti tena kazini.”
"Yaani kuanzia saa… "
"Tisa kamili."
"Kwa hiyo nd’o tuseme…" Ndonya alisita kidogo. "Yaani kati ya saa kumi u nusu na saa kumi na moja, PAK itakuwa katika himaya yako, si nd’o maana’ake?"
Ndivyo itakavyokuwa. Amini, usiamini."
"Una hakika?" Ndonya alikuwa na shaka.
“Sikutanii, bro.”
Ndonya alimtazama kwa makini kijana huyo na kujisikia
kumwamini kwa kiwango kikubwa. Akashusha pumzi, kisha akamuuliza, “Tutaonana saa ngapi na wapi?”
"Kituo cha daladala cha pale AKIBA, saa kumi na moja u nusu.”
*****
ILIKUWA ni saa tisa kasorobo alasiri, wakati mteja mwingine alipoingia dukani kwa Mwasia Vinod Khan na kuagiza bidhaa mbalimbali kwa viwango vya katoni. Alikuwa ni mteja mzuri kwa Vinod Khan kwani alikuwa akinunua bidhaa zenye thamani ya takribani shilingi milioni tatu.
Kwa kuonesha kuwa anamjali sana mteja huyo, mhindi huyo alimhimiza kwa ukali, mfanyakazi wake, Kijicho, atoe katoni hizo haraka stoo.
Kijicho naye hakuwa mzembe. Alikuwa akiingia stoo haraka na muda mfupi baadaye anatoka na katoni moja ya dawa. Lakini alikuwa makini, kila alipoingia humo stoo aliangaza macho huku na kule, akilitafuta lile boksi ambalo bosi wake aliagiza lifutikwe pembezoni mwa bidhaa nyingine mara tu serikali ilipopiga marufuku uagizaji na uuzaji wa sumu ya PAK.
Pia serikali iliwataka wale wote waliokuwa na sumu hiyo madukani au stoo, waikabidhi mara moja serikalini kwa ajili ya kuiangamiza.
Kichwani mwake alikumbuka kuwa bosi wake hakuwa tayari kuisalimisha PAK serikalini, na ndiyo maana aliagiza ihifadhiwe mahali fulani, tofauti na bidhaa nyingine, lakini iwe ndani ya stoo hiyohiyo.
Alipoona muda unazidi kwenda, na kila anapoingia humo kuchukua bidhaa halioni boksi hilo, ndoto ya kupata pesa ikaanza kuyoyoma.
Huku jasho chepechepe likimtoka, alifumbata mikono na kuomba Mungu kimoyomoyo, bosi wake amtume tena huko stoo. Aliamini kuwa boksi hilo halijahamishwa, ni yeye tu ambaye hajafanikiwa kuliona.
Labda Mungu alikisikia kilio chake, kwani dakika chache kabla ya kufunga duka mara mteja mwingine akaingia. Huyo aliagiza katoni tatu za dawa aina tofauti. Na ni hilo alilolihitaji Kijicho.
Safari hii hakuzembea. Alitwaa katoni hii na kuiweka huku. Katoni ile akaiweka kule, ile nyingine ikatupwa kule, ilimradi alizipangua bidhaa hizo zilizofurika humo huku ile ndoto ya pesa ikimjia sekunde hadi sekunde.
Ulikuwa ni mchakato mgumu, lakini aliutekeleza kwa umakini wa hali ya juu. Ingawa katoni zilizohitajika angeweza kuzibeba kwa mara moja, hata hivyo aliamua kutumia mbinu ili afanikishe mpango wake.
Akawa anatoa katoni moja, moja. Na kila aliporudi stoo, hakufikia kuchukua katoni nyingine papohapo, bali kwanza alitumia muda akilisaka lile boksi, ilhali kichwani mwa Vinod Khan ilichukuliwa kuwa katoni nyingine inatafutwa.
Ni pale alipopaswa kupeleka katoni ya mwisho, ndipo alipokuwa makini zaidi katika upekuzi wake. Akagusa kila sehemu. Hatimaye macho yakakiona kile kilichoisumbua akili yake.
Lilikuwa ni boksi dogo, lililofungwa kamba madhubuti. Hakuhitaji kutumia hata sekunde mbili kulitambua boksi hilo.
Huku mapigo ya moyo yakiongeza kasi, na kichwani akiziwaza milioni moja alizoahidiwa au kukubaliana na Ndonya, hakutaka kuzembea hata kidogo.
Alikitwaa kisu na kuzikata kamba zile haraka, kisha akalifungua boksi hilo na kutoa chupa moja ya PAK. Bila ya kuchelewa, akaipachika katika mmoja wa mifuko mikubwa ya suruali yake pana. Kilichofuata ni kuitwaa katoni ya mwisho ya dawa na kuipeleka dukani.
******
AKIWA amesimama katika kituo cha daladala cha AKIBA, Ndonya alikuwa akitazama saa kila baada ya muda mfupi. Alifanya hivyo mara nyingi na ilipotimu saa kumi na moja na nusu, akaacha kutazama saa. Sasa akawa akiangaza macho huku na kule, akitarajia kumwona Kijicho akitokezea upande wowote.
Dakika kumi baadaye, Kijicho alifika kituoni hapo. Watu waliokuwa wakisubiri usafiri walikuwa wengi, hivyo alilazimika kuangaza macho huku na kule, sura ya Ndonya ikiwa imemganda akilini.
Hata hivyo, ni Ndonya aliyetangulia kumwona Kijicho. Akamfuata ma kumgusa begani. Kijicho akashtuka na kugeuka.
“Vipi, umefanikiwa?” Ndonya alimwahi.
“Kama nilivyokuahidi.”
“Ok, tusogee pembeni.”
Walijitenga na kundi la abiria waliokuwa wakisubiri usafiri. Wakahamia upande wa pili wa barabara. Wakasogea hadi katika makutano ya barabara hiyo ya Bibi Titi Mohame na Zanaki.
Hapo hakukuwa na watu wengi. Kijicho akaitoa chupa ya PAK na kumkabidhi Ndonya kwa usiri mkubwa. Ndonya naye kwa usiri huohuo akaichunguza chupa hiyo kwa makini na kuridhika kuwa ni PAK halisi. Chupa hiyo ilikuwa imefungwa kwa lakiri.
Muda mfupi baadaye waliachana, kila mmoja akashika njia yake, huku kitita cha shilingi milioni moja kikiwa kibindoni mwa Kijicho, ilhali PAK ikiwa katika himaya ya Ndonya.
*****
ILIKUWA ni siku njema kwa Ndonya. Kufanikiwa kuipata sumu kali aina ya PAK, kwake hakutofautisha na kuruhusiwa kupenya katika lango kuu la Paradiso. Na kwa furaha aliyokuwqa nayo, hatua chache tu baada ya kuachana na Kijicho, alikodi bodaboda iliyompeleka Leaders Club, Kinondoni.
Akiwa njiani alitwaa simu na kuongea na Kapamba, akimtaka wakutane hapo Leaders Club. Pia akamwambia awasiliane na Kipini ili wote wakutane hapo saa kumi na mbili jioni.
Pendekezo lake lilikubaliwa. Saa kumi na mbili wote walikuwa hapo, katika meza moja, chini ya mkusanyika wa miti iliyotengeneza vivuli vya kuburudisha.
Kila mmojawao alikuwa na chupa ya bia mbele yake. Lakini siku hiyo, Kapamba na Kipini walishangazwa na uchangamfu uliooneshwa na Ndonya.
Huyu hakuwa yule Ndonya waliyemfahamu, Ndonya ambaye kwa muda mfupi sana anatabasamu na kuongea kwa uchangamfu kabla hajabadilika tena na kuurejesha ule uso wenye mikunjo.
****ITAENDELEA ****
 
SEHEMU YA 50



ILIPOKOMEA...
Huyu hakuwa yule Ndonya waliyemfahamu, Ndonya ambaye kwa muda mfupi sana anatabasamu na kuongea kwa uchangamfu kabla hajabadilika tena na kuurejesha ule uso wenye mikunjo.
***SASA ENDELEA***
“VIPI leo? Mbona mwenzetu uko tofauti?” Kapamba alimuuliza.
“Kwa nini?” Ndonya naye aliuliza badala ya kujibu.
“Unaonekana mwenye furaha tofauti na siku zilizopita,” Kapamba alijibu huku kamkodolera macho.
Kicheko kikamtoka Ndonya. “Ndiyo, nina furaha kiasi, na nina sababu ya kufurahi.”
“Sababu gani? Kwani shem wetu kakufanyia nini zaidi ya wanawake wengine unaowachukuaga?” Kipini naye akauendeleza uchokozi.
“Hapana,” Ndonya alikunja uso ghafla. Ile furaha yake ikatoweka mithili ya moshi angani. “Ninayo sababu ya kunifanya niwe hivi. Shemeji yenu hahusiki hata kidogo na furaha yangu.”
Kwa mara nyingine tabasamu likarejea usoni pake. Akawatazama kwa zamu Kipini na Kapamba. Kisha akayapeleka macho mezani. Akaitwaa glasi ya bia na kuipeleka mdomoni. Akanywa mafunda kadhaa kisha akairejesha mezani.
Akawatazama tena. “Leo,” akasita kidogo. Kisha, kama tabasamu lake lilivyorejea usoni muda mfupi uliopita, sasa likatoweka tena. Macho yake mekundu yakawaganda rafikize.
“Leo nina suala jipya," hatimaye alisema kwa sauti ya chini. "Kwanza napenda kuwashukuru sana kwa ile kazi, ile operesheni ya majuzi. Nawashukuru sana, tena sana, japo mliitekeleza kwa makubaliano maalum.
“Lakini pia niwaombeni mnivumilie kidogo, kwa kuwa sasa nataka kupasua jipu. Nataka niwe mkweli.”
Kufikia hapo akatulia kidogo huku akiangaza macho huku na kule. Akameza funda la mate na kuendelea, “Nakumbuka nyote mlishangazwa na hatua yangu ya kugharimia kiwango kikubwa cha pesa katika kuhakikisha yule mwanamke anaiepuka kesi yake. Si nd'o maana’ake?”
“Ni kweli ulitushangaza,” Kapamba alisema. "Tulihisi kuwa kuna malaria inayokujia kwa nguvu kubwa."
"Nilijua hivyo," Ndonya alitabasamu kidogo. ”Nilijua kuwa mtadhani nimekuwa chizi. Lakini sasa naomba mtambue kuwa sikuwa mwendawazximu hata kidogo. Huo nd’o ukweli. Nilikuwa na mambo yangu kichwani. Nilijua nafanya nini."
Akatulia kidogo akiwatazama wenzake kwa zamu. Kisha akaendelea, "Nyote mnaitambua kazi aliyoifanya yule mwanamke, kazi iliyowatoa roho watu watatu ndani ya saa zisizozidi sabini na mbili. Mmoja kati ya hao ni kaka yangu, tumbo moja. Baba mmoja, mama mmoja! Marehemu Machemba!
"Kitendo alichokifanya yule mwanamke kilinichoma sana moyo Na hadi leo donda hilo halijapona. Pia kuna uwezekano mkubwa wa kuwa ni donda lisilopona hadi mwisho wa uhai wangu hapa duniani. Hivyo ndivyo ilivyo!
"Sasa," akasita. "Nilichowaitia leo, ni kuwataarifu kuwa nilichohitaji kwake nimekwishakipata. Na kwa kweli nimefaidi vya kutosha kiasi cha kwamba kwa sasa baaaas! Nimemchoka! Kilichobaki ni kumtimua na halafu nusu saa baadaye n’takuwa ni'shamchomea utambi polisi na atakamatwa tena!
"Nini?!" Kapamba alimtolea macho. "Kwa nini umchomee utambi tena ilhali tayari gerezani kuna mtu anayejulikana kwa jina la SCOLASTICA TEMU?"
"Hiyo si hoja," Ndonya alisema kwa kujiamini. "Atakapotiwa pingu kwa mara nyingine ndipo atakapojua kuwa maharage ni mbegu au mboga daaaaadek!"
Kapamba aliguna. "Lakini huo hautakuwa ubinadanmu, Ndonya. Elewa kuwa huenda muda huu, na katika siku zote hizi, Scola amekuwa akikuthamini na kukushukuru kimoyomoyo kwa kumtoa kule jehanamu. Iweje umfukuze ghafla hivyo? Unadhani atajisikiaje au atakuonaje?"
Ndonya alicheka. Kisha, kwa sauti iliyojaa dharau, akasema, "Sijali kuwa atanionaje au atajisikiaje. Hilo litakuwa juu yake. Kapamba, tambua kuwa nilitokea kukipenda kiuno chake tu na si vinginevyo!"
"Lakini… "
"Hakuna cha ‘lakini’ Kapamba!" Ndonya aliwaka. "Malaya mmoja ka’ yule asikusumbue kichwa! Ni muuaji Ya nini kumwonea huruma leo wakati siku ile nyie wote mlilipinga wazo langu la kumtoa huko rumande?"
*KUMEKUCHA! UNADHANI NI KIPI KITAENDELEA?
 
SEHEMU YA 51




ILIPOKOMEA...
"Hakuna cha ‘lakini’ Kapamba!" Ndonya aliwaka. "Malaya mmoja ka’ yule asikusuimbue kichwa! Ni muuaji. Ya nini kumwonea huruma leo wakati siku ile nyie wote mlilipinga wazo langu la kumtoa huko rymnande?"
SASA ENDELEA
“Hapana Ndonya,” Kipini aliibuka. “Asemayo Kapamba ni kweli tupu. Kiubinadamu, uamuzi unaotaka kuuchukua siyo mzuri. Ingekuwa ni vizuri kama ungemwacha asote Keko, na hizi gharama ulizotumia katika kumtoa rumande, ndizo ungetumia kwa kufanya apate hukumu kali zaidi, ikibidi iwe ni hukumu ya kifo.”
Hayakuwa maoni yaliyoulegeza msimamo wa Ndonya. Dhamira yake ilikuwa palepale! Ni nani ambaye angeubadili msimamo wake? Na kwani amewaita kwa ajili kuhitaji maoni na mapendekezo yao? Mbona walishindwa kuubadili msimamo wake katika mpango wa awali, itakuwa leo?
Akachekea moyoni kisha akawauliza, “Nyie si ni wanaume marijali? Kati yenu hakuna anayemtamani mwanamke huyo hata kidogo?"
Ukimya wa sekunde chache ulitawala, Kipini na Kapamba wakitazamana kisha wakamkodolea macho Ndonya. "Una maana gani?" hatimaye Kapamba alimuuliza Ndonya.
"Nina maana kwamba ile ni mboga yenu."
"Mboga yetu?" Kipini alidakia. "Mboga yetu kivipi?”
“Kwa anyehitaji akachukue na akale!”
“Hujaeleweka,” Kapamba alisema.
Kwa mara nyingine kimya kikatawala. Kisha Ndonya akaifafanua kauli yake. Akawaambia kuwa alitaka siku inayofuata, wote watatu washiriki kumbaka Scolastica Temu na kwamba baada ya tukio hilo atawapa pesa ya shukurani. “Hilo ndilo nililowaitia. Na baada ya hapo, kinachofuata hakiwahusu, Ni mimi na yeye. Semeni, mko tayari?”
Haikuwa rahisi kuapatikana jibu la haraka. Kapamba na Kipini hawakutarajia kuambiwa hivyo. Kila mmojawao alipokuja hapo, hakuwa na hisia za kupokea ujumbe kama huo, ujumbe unaoweza kumstaajabisha mwendawazimu na kumtisha mwenye akili timamu. Isitoshe, uso wa Ndonya ulikuwa umebadilika. Sasa alionesha dhahiri kupandwa na chuki iliyokwea hadi kileleni mwa Mlima Everest!
Alitisha!
Ni mabadiliko hayo yaliyomfanya Kapamba amtilie shaka. Imani kuwa kila alichosema ni cha kweli ikaanza kumtoka kwa kasi. Kama alidiriki kuwahaadaa, akidai alikuwa akimpenda sana Scolastica na kwamba ndiyo maana alitaka atoke rumande na amuoe, atashindwa nini kuunda uongo mwingine kitaalamu na kisha akawamwagia mithili ya mwigizaji mahiri wa tamthiliya?
Kitu fulani kikamnong’oneza moyoni, ‘huyu ana lake jambo.’ Na sasa akaamua kuwa makini akiepuka kupingana naye ili tu ajue mwisho wa mkakati wake.
“Mko tayari?” Ndonya aliwauliza tena.
“Hilo ni jambo dogo,” Kapamba alijibu.
“Hapana, mimi siko tayari,” Kipini alitamka kwa msisitizo.
“Unaogopa?” Ndonya alimkazia macho.
“Niogope nini? Siogopi kitu, ila sipendi tu!"
Kapamba alimtazama KIpini kisha akaachia tabasamu kubwa. Akamgeukia Ndonya. “Ok, usimlazimishe. Mambo ya aina hii yanahitaji hiyari ya mtu. Unajua, watu wengine hujisikia kinyaa kupishana huyu baada ya huyu katika mchezo huo. Inahitaji roho ngumu! Lakini mimi sina noma, niko tayari. Sema tu nije lini na saa ngapi?”
Bia zilikwishaanza kufanya kazi katika mishipa ya fahamu ya Ndonya. Haja ndogo ilimbana. Hivyo, kabla ya kutamka chochote, alisimama na kuelekea msalani. Huku nyuma Kipini alimtazama Kapamba na kumuuliza, “Hivi kweli unaweza?”
“Tulia,” Kapamba alimwambia kwa sauti ya chini, macho yake yakimtazama kwa makini. “Kuna jambo ni’logundua. Nitakueleza kwa kirefu tutakapoondoka. Kwa kifupi ninaamini kuna jambo zaidi ya jambo katika mpango wake. Mengine anayotusimulia hapa, hayatofautiana na hadithi nzuri ya kubuni. Tuliza boli. Kikao kitakapokwisha tuagane naye bila ya kufuatana. Hapo ndipo tutakapoongea kwa kina.
*****
WALIONDOKA Leaders Club saa moja kasoro dakika chache, giza likiwa limeanza kuingia. Walikubaliana kuwa siku inayofuata saa tatu au nne usiku, Kapamba awe amefika kwa Ndonya, Mtaa wa Kazima, Kinondoni. Walikubaliana hivyo na Ndonya aliamini kikao chao kimeisha vizuri, hakuna kitakachoharibika.
Aliwaamini na kuwaheshimu Kipini na Kapamba. Imani na heshima hiyo vilikomaa baada ya kuwapa jukumu la kufanikisha mpango wa Scolastica Temu kutoka rumande. Ni kipi kimfanye awatile shaka?
Ndiyo, aliwaamini, aliwaheshimu. Lakini yeye hakuwa Mungu. Ni binadamu kama binadamu yeyote mwinginie mwenye nyama. Ni kati ya mabilioni ya wanadamu waliotapakaa chini ya jua.
Hakuna binadamu aliyezaliwa na mwanamke, anayeweza kumtazama binadamu mwenzake na kubaini kuwa anawaza nini, ana malengo gani na ana kiasi gani cha pesa mifukoni mwake.
Yeye ni miongoni mwao; hakuwa na uwezo wa kuisoma mioyo ya hao rafiki zake hususan moyo wa Kapamba.
Ukweli ni kwamba, Kapamba alichanganyikiwa pindi tu alipomwona Scolastica ile siku alipokwenda na Latifah gereza la Keko. Alivutiwa na sura yake, akalipenda umbo lake. Japo ule mng’aro wake ulianza kufifia kwa kasi, hata hivyo bado machoni mwa Kapamba, alikuwa ni mwanamke mzuri machoni mwa yeyote apendaye wanawake wazuri. Aliamini kuwa siku chache tu za kuishi uraiani, zingetosha kuurudisha ule mwonekano wake wa awali.
Na katika maongezi ya pale Leaders Club jioni hiyo, Kapamba alimsikia Ndonya akitamka kuwa Scolastica kapendeza sana ndani ya siku chache tu. Eti ngozi yake imenawiri na mwili umejazia kike!
Kama yule Scolastica ambaye Kapamba alimwona akiwa anavutia wakati akiwa rumande siku ile, basi sasa kuwa mwanadamu wa kawaida aliyezaliwa chini ya jua. Kapamba aliamini hivyo. Ni imani hiyo iliyomfanya apandwe na shetani wa uzinzi. Japo alijisikia kumpenda Scolastica, lakini zaidi alimtamani. Aliuhitaji mwili wake!
Ni shetani huyo aliyemfanya ayashtukie maelezo ya Ndonya, na sasa akaamua kuweka bayana kwa kumwambia Kipini kuwa hayuko tayari kushiriki mpango huo.
"Kwa nini?" Ndonya alimshangaa. "Mbona umebwata mbele yake kuwa uko tayarti?”
“Ndiyo, nimemkubalia, lakini kwa kweli siko tayari. Pale mbele yake nililazimika kuwa mnafiki tu.”
“Mnafiki”
“Ndiyo! Nilitumia unafiki tu kwa kuwa sikupenda kumuudhi palepale. Nilitaka tuachane kwa kirafiki zaidi. Si unajua anatuamini sana?"
"Najua."
"Sasa kitendo cha wewe kupingana na pendekezo lake, kama na mimi ningefuatia, sidhani kama angejisikia vizuri. Ukweli ni kwamba angekasirika na angetuona sisi ni wasaliti. Umenielewa?"
"Hapo nimekuelewa."
"Basi kama uimenipata ngoja nikwambie sababu kuu ya kuwa mnafiki pale kikaoni." Kapamba alimwambia wakati wakiliacha geti la eneo la viwanja hivyo na kuifuata Barabara ya Tunisia.
“Nampenda Scola.”
“Nini?” Kipini alisita kutembea, akamtazama Kapamba kwa macho yasiyoamini alichokisikia.
“Acha kushangaa-shangaa, twende,” Kapamba alianza kuvuta hatua tena. "Nimekwambia kuwa nampenda Scola. Na ujue kuwa kwa jinsi alivyo, mwanamume yeyote aliyekamilika lazima ama ampende au amtamani. Ni miongoni mwa wanawake wachache sana duniani ambao wanaweza kumvutia rijali kutokana na sura au maumbo yao.
“Huyu Scola alinivutia siku nilipokuwa nikimpeleka hawara yako, Latifah, kuchukua nafasi yake kule Keko. Na sasa jamaa anadai kuwa kapendeza maradufu. Naweza kuiamini kauli hiyo kwa kuwa Scola sasa yuko kwenye kijigereza kingine, kijigereza cha uraiani. Sasa ni mtu wa kukaa ndani tu; anakula anachotaka, anakunywa anachopenda, runinga mbele yake.
"Kwa nini asibadilike kwa muda mfupi wakati hata usiku huutupa mwili wake kitandani, huenda kwenye godoro zuri na kupata usingizi wa starehe? Kwa nini asinawiri ilhali anapohitajii mwanamume wa kumburudisha, Ndonya huwa tayari usiku kucha?”
Akasita kidogo, akakunja uso na kutupa macho angani. Akamshika mkono Kipini huku akimtazama kwa macho makali. Kisha, kwa sauti nzito, ya chini, yenye msisitizo mkali, akasema, “Ipo haja ya kumwokoa Scolastica Temu! Kuna kila dalili ya janga zito mbele yake.
“Sasa nakwambia hivi, kwa kuwa kanikaa moyon,i sina budi kulivalia njuga suala la kuyalinda maisha yake piga, ua! Lije jua, ije mvua! Nitafanya kila liwezekanalo na kulazimisha hata lisilowezekana, ili kuhakikisha kuwa SCOLASTICA TEMU hadhuruki!”
Wanaume hao wakabaki wakitazamana, kimya kikitawala kwa muda.
***HAYA , KAPAMBA KAAMUA ...LIJE JUA, IJE MVUA!! NI KIPI KITAFUATA?***
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom