Riwaya:Mtuhumiwa

Riwaya:Mtuhumiwa

RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA THELATHINI NA SABA
Bila shaka Jaka atakuwa chumbani mwake saa hizi.
Hatua kadhaa nyuma yake, Tony alikuwa akimfuata, hali Muddy na Alphonce Ng’ase nao wakiwa wanaelekea kwenye bweni namba tano kwa njia nyingine. Joakim hakuwa na wazo la kugeuka nyuma wala kutazama pembeni kuona kama alikuwa anafuatwa. Akili yake ilikuwa inawaza kuonana na Jaka haraka iwezekanavyo.
Akiwa mbele ya mlango wa lifti ya kupandia kwenye ghorofa za juu za jengo lile alipata wazo jipya. Inawezekana Tony na wenzake nao wakaamua kumfuata Jaka chumbani kwake. Alitembeza macho huku na kule miongoni mwa wanafunzi wachache waliokuwa wakiisubiri ile lifti pamoja naye. Alimuona mtoto mdogo wa kiasi cha miaka kumi na mbili hivi aliyekuwa akiuza karanga mbele ya jengo lile. Alitoa kalamu na kuandika ujumbe mfupi kwenye kijitabu chake cha anuani na kuchana ule ukurasa alioandikia ujumbe ule. Alimsogelea yule mtoto na kumpa shilingi mia tano na ile karatasi yenye ujumbe ambayo aliiandika jina na namba ya chumba cha Jaka. Akamuomba yule mtoto aufikishe ujumbe ule. Yule mtoto alitoka mbio na kuanza kupanda ngazi kuelekea ghorofa ya pili ambako chumba cha Jaka kilikuwepo. Dakika mbili baadaye lifti ilifika pale chini na Joakim alijipenyeza upesi ndani yake. Milango ilifunga na lifti ikaondoka kupanda juu.
Tony alimuona Joakim akimkabidhi yule mtoto ile karatasi na kuingia ndani ya lifti. Kwa mwendo wa haraka alimuwahi yule mtoto kabla hajafika ghorofa ya pili na kumsimamisha. Alimuomba ile karatasi iliyopewa na Joakim, na yule mtoto bila kuelewa alimpa. Tony alisoma ujumbe ulioandikwa kwenye karatasi ile kisha akamrudishia yule mtoto huku uso wake ukifanya tabasamu dogo la ushindi.
“Okay dogo…ipeleke tu hiyo barua mahala ulipoagizwa.” Alimwambia, na yule mtoto bila ya kuelewa, alitimua mbio kupeleka ujumbe ule muhimu. Tony alirudi pale kwenye lifti, na muda mfupi baadaye ile lifti ilirudi tena naye akaingia pamoja na wanafunzi wengine wachache waliokuwa pale chini, wakiwemo Alphonce Ng’ase na Mohammed “Muddy” Shomari.
Ilikuwa ni saa nane kasoro dakika ishirini za mchana.
___________________
Jaka alitazama saa yake na kugundua kuwa ilikuwa ni saa saba na dakika thelathini na tano za mchana. Alikumbuka kuwa ile ilikuwa ndiyo siku ya kuzaliwa kwa mpenzi wake naye aliahidi kumpatia zawadi nzuri atakayoikumbuka daima. Alikuwa amemtungia shairi zuri ambalo aliamua kujirekodi kwenye simu yake ya kisasa akiliimba ikiwa ndio zawadi aliyomuandalia. Lilikuwa ni shairi la mapenzi aliloliandika kwa lugha ya kiingereza waliyozea kutumia pale chuoni na alikuwa na hakika kuwa Moze angelipenda sana.
Aliinuka kutoka kitandani alipokuwa amejilaza chali akilikariri lile shairi akiwa na simu yake pamoja na lile shairi mkononi. Akaketi kwenye kiti kilichokuwa mbele ya meza yake ya kusomea, akaiweka mezani ile simu kisha akalisoma kwa mara ya mwisho lile shairi kabla ya kuanza kujirekodi.
The day I saw you, my love began.
My heart went with you, when my love began.
But the day you said “Yes”, is when my life really began.
Sometimes I wonder, what’s in your love.
That’s such a wonder, in your kind of love.
‘Cause my heart can wander, not ever again.
You make me feel, my world is real.
I know no anger, not anymore.
I know no tears, yet I know.
When your love is gone, my tears will flow.
But until then, my life has just begun,
With our love...
Happy Birthday my love.
Lilikuwa ni sahiri lililoeleza ukweli wa mapenzi yake kwa Moze. Ya kwamba penzi lake lilianza pale tu alipomtia machoni, na siku Moze alipokubali kuwa wake wa maisha ndipo maisha yake yalipoanza.
Ni shairi lililoeleza ni jinsi gani Jaka alivyoliona penzi la Moze kuwa ni la ajabu kiasi kwamba hata moyo wake hautamani msichana mwingine yeyote maishani mwake. Jaka alimalizia shairi lile kwa kumueleza mpenzi wake kuwa penzi lake (Moze) limemfanya asijue kuchukia tena maishani mwake zaidi ya kupenda tu, na kwamba limemfanya asijue tena kutokwa na machozi, lakini pia anakiri kuwa anajua machozi mengi yatamtoka siku Moze takapoamua kuliua penzi lile...lakini mpaka siku hiyo itakapofika, maisha yake ndio kwanza yalikuwa yameanza...kwa penzi lililopo baina yao.
Jaka alitabasamu baada ya kulisoma tena lile shairi, akiwa na hakika kabisa kuwa maneno ya shairi lile yalikuwa ni ukweli uliotoka ndani kabisa ya moyo wake. Aliamini kuwa Moze akiupata ujumbe atakaomtumia kutokea kwenye simu yake ukiwa na sauti yake ikimchombeza kwa vina vya shairi lile, atafurahi sana na ataiona ile kuwa ni zawadi ambayo hataisahau maishani mwake.
Alivuta pumzi nyingi mapafun mwake, na kuzitoa taratibu, kisha huku akitabasamu, alibofya sehemu iliyoiwezesha ile simu kurekodi kile atakachokuwa anakisema, kisha kwa sauti ya kuchombeza alianza kusoma ubeti wa kwanza wa shairi lile.
“The day I saw you, my love began.
My heart went with you, when my love began.
But the day you said Ye...”
Alikatishwa na kishindo cha mlango wake ukigongwa kwa nguvu kutokea nje. Alikunja uso na kugeukia kule mlangoni na wakati huo huo mlango ukagongwa tena kwa nguvu.
“Oi! Nani…? Ingia!” Aliita kwa sauti, lakini mgongaji akazidi kugonga, sauti hafifu ikimfikia pale ndani. Kwa kuwa ile meza ilikuwa kando ya mlango ule, Jaka alijigeuza, akanyoosha mkono wake na kuufungua ule mlango bila ya kuinuka kutoka pale kitini. Alishangaa kumuona mtoto mwenye sinia lenye vipaketi vya karanga akiingia mle ndani na kusimama hatua kama mbili ndani ya kizingiti cha mlango ule.
“Shikamoo.” Yule mtoto alimuamkia.
“Aaam…Marahaba...unasemaje?”
“Jaka yupo?”
“Jaka ndio mimi, unasemaje?”
Yule mtoto alimpa kile kijikaratasi. Jaka alikipokea na yule mtoto akaanza kuondoka.
“Oi! Ngoja kwanza mtoto...nani kakupa hii karatasi...?”
“Simjui!” Yule mtoto alimjibu huku akitoka nje ya chumba kile bila kusubiri maswali zaidi.
Jaka alibaki amepigwa na butwaa.
Aliifungua ile karatasi na kuisoma. Maudhui ya waraka ule yalimfanya ashushe pumzi ndefu na kusajili sura ya kutoelewa. Alisukuma mlango wake kuufunga na kuiweka ile karatasi aliyopewa na yule mtoto juu ya simu yake pale mezani hali uso wake ukiwa kwenye hali ya kukosa uamuzi. Aliichukua tena ile karatasi na kuusoma tena ule ujumbe aliyoandikiwa:
Jaka, tafadhali sana sana fanya hima tuonane sasa hivi juu ya jengo hili.
Naomba uniamini kwani ni jambo la kufa na kupona kaka… kwako na kwangu. Ni mimi,
Joakim Mwaga.
Saa 7:28 Mchana.
Aliangalia saa yake. Ilikuwa ni saa nane kasoro dakika kumi mchana. Kwa hiyo ni dakika zipatazo ishirini na mbili zilikuwa zimepita tangu ujumbe ule uandikwe.
Jambo la kufa na kupona? Ni jambo gani hilo? Na kwa nini tuonane juu ya jengo hili na sio sehemu nyingine yoyote?
Kengele ya hatari ikagonga akilini mwake. Alihisi kuwa ule ulikuwa ni mtego wa akina Tony kutaka kumkamata kwa kumtumia Joakim, kwani kwa Joakim kutaka kuonana naye siku moja tu baada ya yeye kugundua kuwa Tony anajihusisha na biashara ya madawa ya kulevya ilikuwa ni ushahidi tosha juu ya hilo.
Lakini pia iliwezekana kuwa si Joakim aliyeandika ujumbe ule.
Sasa angejuaje?
Kuna njia moja tu ya kujua...kwenda kujionea mwenyewe!
Bila ya kufikiri zaidi, aliitia mfukoni ile karatasi yenye ujumbe, akachukua fulana iliyokuwa pale kitandani na kuivaa haraka haraka huku akitoka nje ya chumba kile akiacha mlango ukijibamiza nyuma yake. Alibonyeza kitufe cha kuiita lifti kisha akabaki akisubiri kwa wahka huku akitazama saa yake.
Saa nane kasoro dakika sita.
Taa nyekundu juu ya mlango wa lifti ile ilikuwa inawaka kwenye namba kumi. Akagundua kuwa tangu amefika pale, taa ile ilikuwa inawaka kwenye namba ile ile. Akaelewa kuwa kuna mtu ameizuia lifti ile kwenye ghorofa ya kumi. Aliendelea kusubiri.
Saa nane na dakika tatu.
Alianza kupata wasiwasi kuwa labda ile lifti ilikuwa mbovu. Wazo la kupanda kwa miguu mpaka juu ya jengo lile lilimfanya asonye kwa hasira. Akaangalia tena saa yake.
Saa nane na dakika saba.
Taa ikazimika kwenye namba kumi. Akajua kuwa sasa lifti ile ilikuwa inakuja. Alitamani sana awaone hao jamaa waliokuwa wameizuia ile lifti kule juu muda wote ule. Taa iliwaka kwenye namba nne kwa muda mfupi na kuzimika tena. Ilikuwa inakuja. Mlango wa lifti ulipofunguka pale chini hakukuwa na mtu yeyote ndani ya lifti ile. Aliingia na kubonyeza namba kumi na lifti ilianza kupanda kuelekea ghorofa namba kumi.
Jengo la bweni namba tano lilikuwa na ngazi tatu za kupanda kwa miguu. Ngazi ndogo kila upande wa jengo lile pana, ambazo mara nyingi zilikuwa zikitumika na wanafunzi walioishi katika vyumba vya pembeni na vile vya kwenye korido fupi za pembeni. Katikati ya jengo lile kulikuwa kuna ngazi kubwa kando ya lifti ambazo mara nyingi zilitumika na wanafunzi waliokuwa wakiishi kwenye vyumba vya kwenye korido fupi za kati na wale wa kwenye vyumba vilivyokuwa kwenye korido ndefu.
Sekunde chache baada ya lifti kuondoka ikiwa na Jaka ndani yake, watu watatu walitoka nje ya jengo lile kwa kutumia ngazi zile.
Tony alitoka kwa kutumia ngazi ndogo zilizokuwa kulia kabisa na kuzunguka nyuma ya jengo lile na kutoweka bila ya kuonekana na mtu.
Alphonce Ng’ase aliokea kwenye ngazi kubwa za katikati na kuambaa taratibu kutoka kwenye jengo lile, wakati Muddy Shomari alitoka kwa kutumia ngazi ndogo zilizokuwa kushoto mwa jengo lile na kutoweka.
_____________________
Lifti ilikuwa inaishia ghorofa ya kumi. Jaka aliteremka na kupanda ngazi zilizoelekea juu ya jengo la lile la ghorofa kumi na mbili. Hatua chache mbele yake kulikuwa kuna mlango uliotokezea kwenye ukumbi mwembamba na mrefu uliofanya paa la zege la jengo lile refu. Kabla ya kuufikia mlango ule, kulia na kushoto mwa ngazi zile alizokuwa akizikwea, kulikuwa kuna mlango mwingine mmoja kila upande. Mlango wa kulia kwake ulikuwa ni wa kuingia kwenye chumba kilichokuwa kina mitambo ya umeme uliotumika kuendeshea lifti ya jengo lile. Mlango wa kushoto kwake ulikuwa ni wa chumba kilichokuwa kina tanki kubwa la kuhifadhia maji kwa ajili ya wakaazi wa jengo lile.
Alichungulia kwenye vyumba vile huku akiita jina la Joakim kwa sauti ya chini huku akiwa makini sana. Hakupata jibu lolote. Alipita kwenye ule mlango uliokuwa mbele yake na kutokea kwenye paa la jengo lile. Alitazama kulia na kushoto. Hakukuwa na mtu.
“Joakim!” Aliita kwa sauti, na kupokewa na kimya tu. Alitembea taratibu kuelekea kushoto kwake. Mbele yake kulikuwa kuna vyumba viwili. Kimoja, kilichokuwa moja kwa moja mbele yake kilikuwa ni cha umeme kwani kilikuwa na nyaya nyingi za umeme zilizotoka kwenye mashine mbili kubwa zilizokuwa ndani ya chumba kile na kutambaa kuelekea ndani ya jengo lile.
Kilikuwa kitupu.
Chumba kingine kilikuwa pembeni ya kile cha kwanza kushoto kwake kiasi kwamba vyumba vile vilifanya herufu “L”. Alifungua mlango wa kile chumba kingine ambacho kilikuwa kina mabaki ya tanki la kuhifadhia maji lililoharibika.
Na chenyewe kilikuwa kitupu.
Wasiwasi ulianza kumtawala, na akaamua kuondoka. Aligeuka na kuanza kuondoka, lakini alipoufikia mlango wa kumrudisha ndani ya lengo lile kutokea kule juu, aliangalia kulia kwake. Kulikuwa kuna chumba kingine kimoja. Alichungulia ndani yake huku akiita jina la Joakim.
Kimya.
Kilikuwa ni chumba cha tanki la kuhifadhia maji sawa na lile aliloliona wakati akipanda ngazi kuelekea juu ya jengo lile.
Alishindwa kuelewa.
Iweje Joakim...au yeyote yule aliyeandika ujumbe ule...amtumie ujumbe wakutane kule juu halafu asitokee? Aliegemea ukuta mfupi uliozunguka eneo lile kuwazuia watu wasianguke kutoka kule juu na kuangalia chini huku akili yake ikijaribu kuelewa hali ile.
Jiji la Dar lilionekana likiwa limejitawanya kwa mapana na marefu kutokea pale juu, lakini akili yake muda ule ilikuwa kwenye ule ujumbe alioletewa pale chumbani kwake na yule mtoto muuza karanga.
Nini maana yake hii? Kama ule ujumbe ulikuwa ni mtego wa akina Tony, mbona hata wao hawapo huku juu?
Ilikuwa haileti maana.
Alisonya huku akigeuka kutoka pale kwenye ule ukuta aliokuwa ameuegemea kwa mbele na kuuegemea kwa mgongo. Alikuwa katika hatua ya kujisukuma kutoka pale ukutani kwa mgongo wake ili aondoke ndipo alipomuona.
ITAENDELEA
 
RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA THELATHINI NA NANE
Nini maana yake hii? Kama ule ujumbe ulikuwa ni mtego wa akina Tony, mbona hata wao hawapo huku juu?
Ilikuwa haileti maana.
Alisonya huku akigeuka kutoka pale kwenye ule ukuta aliokuwa ameuegemea kwa mbele na kuuegemea kwa mgongo. Alikuwa katika hatua ya kujisukuma kutoka pale ukutani kwa mgongo wake ili aondoke ndipo alipomuona.
Naam, alikuwa ni Joakim hasa.
Lakini hakuwa katika hali ambayo Jaka aliitarajia.
Kwenye kona baina ya ukuta wa kile chumba alichotoka kuchungulia punde tu, na ule ukuta uliozunguka ule ukumbi juu ya jengo lile, Joakim Mwaga alikuwa amejikunyata sakafuni, mgongo wake ukiwa umeegemea kwenye kona ile iliyofanya nyuzi tisini. Macho yake yalikuwa yamekodoka kwa mshangao wa kudumu, mdomo wake ulikuwa wazi hali ulimi wake ukining’inia nje. Eneo lote la kifua chake lilikuwa limetapakaa damu kutoka kwenye jeraha lililokuwa shingoni kwake.
Jaka alipiga yowe la mshituko huku miguu ikimwisha nguvu.
Joakima alikuwa ameegemeza kichwa chake kwenye bega lake la kushoto na sehemu ya kichwa kile ilikuwa imeegemea ukuta. Mpini wa kisu ulichomoza kutoka kwenye jeraha lililokuwa upande wa kulia wa shingo ile.
Jaka alipiga hatua tatu za haraka kumsogelea huku akimuita kwa wahka na woga mkubwa.
“Joakim! Joakim! Joakim...” Alizidi kumuita huku akiwa amechutama mbele yake, akimtikisa. Na hapo ndipo alipogundua kuwa ingawa macho yake yalikuwa yakitazama mbele kwa mshangao, Joakim alikuwa haoni, na alikuwa haoni kwa sababu sasa alikuwa marehemu. Joakim hakuwa hai tena. Alikuwa amekufa.
Ameuawa.
Ukelele wa woga ulimtoka Jaka na hapo hapo aliangukia mgongo alipojaribu kurudi nyuma ili awe mbali na ule mwili usio na uhai. Huku akipiga kelele Jaka alijaribu kuinuka huku akirudi nyuma, akadondoka tena. Akajaribu tena lakini kwa mara nyingine tena akadondokea matako. Akabaki akisotea makalio kurudi nyuma huku macho yamemtoka pima akimtazama Joakim kwa woga huku akipiga mayowe.
Hatimaye alifanikiwa kusimama na kujiegemeza kwenye ule ukuta na kubaki akitweta kutafuta pumzi ambazo zilimkaba kooni.
Ilikuwa ndio mara yake ya kwanza kuona mtu aliyekufa, wachilia mbali aliyeuawa, hasa ikiwa mtu huyo ni ambaye alikuwa akimfahamu. Wazo la kwanza lililomjia kichwani mwake lilikuwa ni kwenda kutoa ripoti polisi juu ya tukio lile.
Alikurupuka mbio kutoka pale ukutani kuziendea ngazi za kuteremka kutoka eneo lile. Picha ya Joakim Mwaga, akiwa amejikunyata pale chini, mguu wake mmoja akiwa ameukunja kwa uchungu kiasi kwamba goti lake lilikuwa karibu sana kugusana na bega lake, wakati mguu wake mwingine akiwa ameunyoosha mbele pale sakafuni, mikono yake yote miwili ikiwa imeshikilia kwa nguvu sehemu chini kidogo ya shingo yake, karibu na pale mpini wa kisu ulipochomoza, bado ilikuwa kichwani mwake.
Mambo yote yaliyofuatia kuanzia muda ule yalitokea haraka sana.
Kabla hajaufikia ule mlango, alisikia vishindo vya viatu vikipanda zile ngazi kuelekea kule alipo kuwa. Havikuwa vishindo vya mtu mmoja. Ni watu wengi. Alitaka kugeuka arudi kule alipotokea, akagundua kuwa njia pekee ya kutokea eneo lile ni kupitia kwenye ule ule mlango, kuelekea kule kule vilipokuwa vikitokea vile vishindo. Kabla hajatanabahi, alipatwa na kihoro aliposhuhudia askari wa jeshi la polisi wanne wakiingia pale ju kupitia kwenye ule mlango, wakimlazimisha arudi nyuma bila kupenda, macho yakimtembea, mdomo ukimuanguka.
“Tulia kama ulivyo!” Mmoja wao alimfokea akiwa amemuelekezea bastola.
Jaka alibaki amepigwa na butwaa. Hakutaka kuyaamini macho yake alipoona wale askari wakimzingira huku wakimnyooshea mitutu ya bunduki aina ya SMG. Aliihisi akili ikimsinyaa na miguu ikimwisha nguvu.
“Sio mimi...I mean…sikufanya kitu...amekufa.
..nimemkuta ameuawa!” Aliropoka kwa hamaniko huku akipiga hatua kuwasogelea wale askari. Mara ile ile wale askari walikoki zile bunduki zao na yule aliyemuamuru atulie hapo mwanzo akamfokea.
“Tulia hapo hapo ulipo wewe! Hatua nyingine moja tu utakuwa kilema sasa hivi!”
Heh!
Jaka alikatisha hatua zake na kusimama huku akinyoosha juu mikono yakeiliyokuwa akimtetemeka vibaya sana.
“Kaa kimya!” Yule askari alimwamuru.
Jaka alijikuta akika chini, miguu ikishindwa kabisa kuendelea kumhimili. Macho makali ya yule askari yalimfuata pale pale chini na bila ya kutoa macho yake usoni kwa Jaka aliiita, “Koplo!”
“Afande!”
“Chunguza eneo hili haraka!”
Mmoja wa wale askari waliomzingira Jaka alichomoka na kuelekea kule alipotokea Jaka, mwisho wa ukumbi ule. Jaka alijua ni nini atakachokikuta kule alipoelekea, ila hakujua ni nini kingemkuta yeye baada ya hapo. Sauti ya mshituko ilisikika kutokea kule alipoelekea yule Koplo, na Jaka alifumba macho kama kwamba kufanya hivyo kungemsaidia asisikie maneno ambayo yangefuata.
“Kuna maiti hapa afande…kauawa…kama tulivyotaarifiw
a!” Yule koplo alijibu kwa sauti.
“Mlivyotaarifiwa? Nan…na nani?” Jala alijikuta akiropoka, na hapo hapo alizabwa kofi kali sana la uso, yowe kubwa likamtoka bila kupenda, maumivu makali yakimtawala usoni.
“Kimya wewe! Unaua mtu halafu unajitia kushangaa?” Yule askari alimkemea, kisha alienda kule alipoelekea yule Koplo, wale askari wengine walibaki vilevile wakiwa wamemuelekezea Jaka mitutu ya bunduki zao. Jaka alianza kulia kwa majuto na uchungu, akijua kuwa tayayi alikuwa amebebeshwa kesi ya mauaji. Baada ya muda yule askari kiongozi alirudi na kumuuliza jina lake. Jaka akamtajia.
“Jaka Brown Madega...uko chini ya ulinzi kwa tuhuma ya kuhusika na mauaji!” Yule askari kiongozi alimwambia kwa ghadhabu.
“Sio mimi afande...! Sio mimi...”
Mikono yenye nguvu ilimkamata na kumfunga pingu mikono yake kwa mbele.
“Maelezo yote utatoa kituoni!” Alikemewa.
Mambo yote yaliyofuata baada ya hapo yalikuwa kama ndoto tu kwa Jaka. Wale askari waliwasiliana na askari wengine ambao bila shaka walikuwa chini ya jengo lile kwa redio maalum za mawasiliano na dakika chache baadaye walikuja askari wengine wakiwa na machela ya kubebea maiti. Mwili wa Joakim Mwaga ulipigwa picha ukiwa umejikunyata pale chini kabla ya kubebwa kwenye machela na kuondolewa kutoka eneo lile.
Jaka aliteremshwa haraka haraka kutoka kule juu hali akiwa amefungwa pingu. Ilikuwa ni heka heka baada ya wanafunzi wenzake kumuona akiteremshwa ngazi na askari namna ile. Walikusanyika vikundi vikundi na kuanza kuulizana juu ya mkasa ule ambao wote hawakuuelewa.
Askari walimuamuru Jaka awapeleke chumbani kwake, naye alitii bila ubishi huku kichwa kikimzunguka. Alijitahidi kufikiri lakini hakuna fikra yoyote njema iliyomjia. Mlango wa chumba chake ulikuwa wazi na yule askari alimuuliza iwapo aliuacha wazi kabla ya kutoka nje ya chumba kile.
“Nakumbuka niliubamiza lakini sikuufunga kwa ufunguo...” Jaka alijibu.
“Okay, tuingie ndani humo…!” Askari aliamuru, nao wakaingia na kuacha askari mmoja nje ya mlango wa chumba kile kuwadhibiti wanafunzi waliojaa kwenye korido pale nje ya chumba chake wakitaka kujua kilikuwa kinaendelea.
“Tunapekua chumba chako kutafuta ushahidi wowote tutakaoweza kuutumia katika kuchunguza swala hili, sawa?” Yule askari mwenye bastola, ambayo sasa ilikuwa imehifadhiwa kwenye mkoba maalum ulioning’inia kiunoni mwake alimwambia. Kabla Jaka hajajibu wale askari walianza kupekua chumba kile kwa vurugu. Makabati yalifunguliwa na nguo zilitupwa huku na kule, vitabu vilichakuriwa na kutupwa hovyo sakafuni, kapeti liliinuliwa na kuvutwa bila mpangilio.
Jaka aliangalia mambo yake huku akili ikimzunguka.
“Afande!” Katikati ya upekuzi ule wa fujo, mmoja wa wale askari aliita, naye akapeleka macho yake kule ilipotokea ile sauti. Yule askari mwenye bastola alisogea pale kando ya kitanda cha Jaka alipokuwa amesimama yule askari aliyeita huku akiwa ameinua upande wa godoro la kitanda kile. Jaka naye alisogea taratibu huku akihisi moyo wake ukitaka kumchomoka kutoka kifuani kwake.
Chini ya godoro lile, juu ya chaga za mbao za kitanda chake, kulikuwa kuna glovu mbili za mpira mithili ya zile zinazotumiwa na madaktari wanapofanya upasuaji.
Zile glovu zilikuwa zimetapakaa damu mbichi!
E bwana we!
Jaka alitoa ukelele wa ghadhabu na kutoamini huku akizikodolea macho zile glovu, ukweli kuwa alikuwa ametegwa na amenasa ukimshukia dhahiri fahamuni. Alijirusha juu kwa nguvu akijaribu kugeuka ili atoke nje ya chumba kile.
“Haiwezekani...! Haiwezekani hii! Hii ni njama tu hii1 Nimepakaziwa...! Nimesingiziwa mimi...Hii ni njama kabbisa!” Alibwata kwa hasira. Mikono yenye nguvu ilimshika na kumbana, lakini alizidi kufurukuta.
“Niacheni, niacheni nasema, vibaraka wakubwa nyie!”
Alitwangwa ngumi nzito ya tumboni, na pumzi zikamkatika ghafla, maumivu makali yakimtawala. Alipiga yowe la maumivu huku akienda chini akiwa amejishika tumbo. Aliinua uso kwa ghadhabu kumtazama aliyempiga, akajikuta akiutumbulia macho mtutu wa bastola iliyoelekezwa katikati ya macho yake.
“Tulia kama ulivyo fisi wee! Uko chini ya ulinzi kwa tuhuma za amuaji na sitakukumbusha tena juu ya hilo...fanya tena upuuzi wako uone jinsi nitakavyotawanya bichwa lako kwa risasi, fala we! Unaleta vurugu wakati uko chini ya ulinzi, ebbo!” Yule askari kiongozi alimfokea kwa hasira.
“Lakini mimi sijaua, afande...huoni kama hii ni njama tu?” Jaka alisema kwa kuombeleza huku akiwa amepiga magoti pale chini, machozi yakimbubujika.
“Hakuna aliyekuambia kuwa umeua kijana...kuanzia sasa na kuendelea wewe ni mtuhumiwa tu wa mauaji haya...mpaka hapo mahakama itakapoamua kuwa uwe mshitakiwa namba moja au uachiwe huru, sawa bwana? Kwa sasa nataka ushirikiano wako wa kila hali.” Yule askari alimwambia na kukaa kimya kwa muda kabla ya kuanza kumtupia maswali huku askari mwingine akinukuu kwa maandishi mahojiano yale.
“Hizi glovu ni zako?”
“Hapana...”
“Umeshawahi kuziona kabla ya hapa?”
“Hapana...sijawahi.”
“Unaweza kujua zimefikaje hapa chini ya godoro ?”
“Sijui...”
Yule askari alimtazama kwa muda, na Jaka akajua kuwa alikuwa hamuamini.
“Sawa...” Hatimaye alisema yule askari na kutoa maelekezo kwa wale askari wengine waliokuwamo mle ndani. Zile glovu ziliwekwa ndani ya mfuko maalum wa nailoni na kuchukuliwa kama ushahidi. Jaka alitolewa mkiki-mkiki nje ya chumba kile kuelekea kwenye Land Rover ya polisi iliyokuwa imeegeshwa nje ya jengo lile. Wanafunzi wenzake walikuwa wamejaa pale nje kushuhudia tukio lile huku baadhi wa wanafunzi wa kike wakilia baada ya kuuona mwili wa Joakim Mwaga ulipotolewa hapo awali. Jaka alipitishwa akiwa amefungwa pingu kuelekea kwenye gari ile. Aliangaza huku na kule kwa uso uliohamanika akitarajia kumuona Raymond au Moze katika kundi lile la wanafunzi.
Wote hawakuwepo.
Huku akibubujikwa na machozi, Jaka aliingizwa ndani ya lile gari la polisi, ambalo liliondoka kwa kasi kutoka eneo lile.
12
Raymond Mloo alizipokea habari za kukamatwa kwa Jaka akihusishwa na kifo cha Joakim kwa mshangao na mshituko mkubwa sana. Kama angesikia kuwa Jaka amekutwa akiwa ameuawa, bila shaka asingeshangaa kama jinsi alivyoshangazwa na habari ile. Lakini pamoja na kushangazwa kwake, jambo ambalo alikuwa na uhakika nalo kabisa kichwani mwake ni kwamba zile zilikuwa ni hila za Tony na wenzake za kutaka kumkomoa Jaka na kuhakikisha kuwa anafungwa miaka mingi, au maisha...au kunyongwa kabisa, na hivyo kuwapa wao nafasi ya kuendelea na biashara zao haramu.
Lakini kwa nini Joakim?
Na kwa nini Jaka akutwe eneo la tukio?
Ni maswali ambayo hakuweza kuyapatia majibu mara moja mpaka alipoonana tena na rafiki yake siku mbili baada ya tukio. Na hapo aliweza kupata jibu la swali moja tu kati ya yale mawili: ilikuwaje hata Jaka akakutwa katika eneo la tukio.
Kesi ya mauji!
Ama kweli Tony ni mtoto mbaya...tena mtoto mbaya sana.
Masikini Jaka...nani atamuamini atakaposema kuwa hakumuua Joakim Mwaga? Wanafunzi wengi pale chuoni walijua juu ya uhasama uliojengeka baina yake na Joakim Mwaga. Kuna wanafunzi pale chuoni walioshuhudia kwa macho yao siku Jaka na Joakim walipoamua kurekebisha tofauti zao kwa kutupiana makonde. Na tangu siku ile ilijulikana wazi kuwa hawakuwa na uhusiano mzuri kabisa, jambo lililopelekea Jaka kupewa kipigo kikali kule Club Billicanas na kulamizika kulazwa hospitali kwa siku kadhaa.
Na tangu hapo baadhi ya wanafunzi walikuwa wanasubiri kuona Jaka atajibu vipi mapigo yale...
Na sasa Joakim ameuawa na Jaka amekutwa eneo la tukio.
Masikini Jaka...
___________________
Moze alikuwa akimsikiliza mhadhiri nusu nusu, kwani sehemu ya akili yake ilikuwa ikifikiria juu ya zawadi aliyoahidiwa na mpenzi wake siku ile. Aliangalia saa yake na kugundua kuwa ilikuwa ni saa tisa kasoro robo za alasiri. Ilikuwa imesalia robo saa tu kipindi kiishe, naye alikuwa ana ahadi ya kukutana na mpenzi wake baada ya kipindi kile na aliona kuwa yule mhadhiri alikuwa anamchelewesha tu.
Aliona askari wa jeshi la polisi akiingia mle darasani na kunong’ona na mhadhiri kwa muda. Kimya kilitanda darasani, kila kila mwanafunzi akiwa amemakinika na ujio wa yule askari mle darasani, na muda mfupi baadaye Moze alishangaa kusikia mhadhiri akiita jina lake na kumuomba aende kule mbele. Huku moyo ukimdunda kwa wasiwasi, Moze alienda kule alipokuwa amesimama mhadhiri na yule askari.
“Moze, huyu ni afisa wa polisi...alikuwa anahitaji kukuuliza maswali machache...” Mhadhiri alimwambia kwa upole. Moze alimtazama yule askari kwa mashaka halafu akamtazama mhadhiri, kisha akamtazama tena yule askari.
“Naomba tuongazane kituoni tafadhali.” Yule askari alimwambia. Moze alitaka kubisha, lakini akabadili mawazo. Akiwa haelewi ni nini kinachoendelea, alimfuata yule afisa wa polisi kuelekea kituo cha polisi cha Mlimani. Huko aliingizwa kwenye chumba kidogo na kuombwa asubiri. Alisubiri kwa muda wa nusu saa nzima huku akizidi kuchanganyikiwa juu ya sababu ya kuletwa pale kabla hajatokea mtu yeyote. Ndani ya muda huo mawazo mengi ya mashaka yalimuandama, yote yakiwa ni juu mpenzi wake kufanyiwa madhara na akina Tony.
Wamemfanya nini sasa Jaka wangu hawa watu yarabbi?
Wamemuua kama walivyomuua Rose? Oh Mungu wangu…isiwe hivyo jamani!
Alihamanika vilivyo.
ITAENDELEA
 
RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA THELATHINI NA TISA...
Ndani ya muda huo mawazo mengi ya mashaka yalimuandama, yote yakiwa ni juu mpenzi wake kufanyiwa madhara na akina Tony.
Wamemfanya nini sasa Jaka wangu hawa watu yarabbi?
Wamemuua kama walivyomuua Rose? Oh Mungu wangu…isiwe hivyo jamani!
Alihamanika vilivyo.
Hatimaye askari mwingine aliingia mle ndani alimokuwa amesubirishwa.
“Wewe ndiye Moze Mlekwa?” Aliuliza yule askari huku akikaa kwenye kiti kilichokuwa mbele yake.
“Ye..I mean…ndio. Kwa…kwa nini niko hapa? Kuna nini?” Moze alimjibu na kumtupia maswali huku moyo ukimwenda mbio.
“Jina Jaka Brown Madega...linamaanisha lolote kwako?” Jamaa alimuuliza bila kujisumbua kumjibu yale maswali yale, na Moze alihisi ubaridi ukimtambaa kwa swali lile.
Ni kweli! Kuna jambo limemkuta Jaka!
“Kwa nini unaniuliza hivyo...kwani ni nini kimetokea...?”
“Umekuja hapa kujibu maswali, na sio kuuliza...sasa mimi nitauliza maswali na wewe utatoa majibu, sawa?”
“Kha! Mimi sielewi kwa nini nimeletwa hapa halafu unaniambia nisiulize maswali?”
“Wewe huna haja ya kuelewa...kazi yako hapa ni kujibu maswali yangu halafu uende zako...unafahamu nini kuhusu mtu aitwaye Jaka Brown Madega?”
Moze alimtazama yule askari kwa hasira. Akaamua kuwa hiyo haitamsaidia kitu.
“Jaka...ni mpenzi wangu...amekutwa na nini?”
Yule askari alilidharau swali la Moze na badala yake akamtupia swali jingine.
“Unamfahamu mtu aitwaye Joakim Mwaga?”
“Ndiyo..kwa nini?”
“Uliwahi kuwa na uhusiano wowote wa kimapenzi au vinginevyo na huyu mtu aitwaye Joakim Mwaga?”
Eh! Maswali gani haya?
“Hapana...!” Moze alimjibu kwa mshangao, hakutarajia swali kama lile, “...kwa nini..?” Aliongezea jibu lake kwa swali. Kwa mara nyingine tena yule askari hakujisumbua kumjibu.
“ Kulikuwa kuna uhusiano gani baina ya huyo mpenzi wako Jaka na Joakim Mwaga?”
“Afande naomba unieleze ni nini hasa unachotaka kutoka kwangu...maana sioni sababu ya kunitoa darasani, kunileta huku na kuniuliza maswali kama haya!”
“Ninachotaka kutoka kwako ni jibu la swali ninalokuuliza...” Jamaa lilimjibu kwa utulivu, kisha akaendelea, “…kulikuwa kuna uhusiano gani baina ya Jaka na Joakim...walikuwa marafiki ?”
“Aam, kwa marafiki hawakuwa…”
“Hawakuwa marafiki?”
“Ndiyo!”
“Unaweza kujua ni kwa nini?”
“Walikuwa na tabia tofauti...wasingeweza kuelewana.”
“Sio kwa sababu yako wewe?”
Moze alitikisa kichwa kutokana na hoja ile.
“Sidhani kama hiyo inaweza kuwa ni sababu...ni kweli kuwa Joakim alitaka kuingilia kati uhusiano wetu, lakini hakufanikiwa...”
“Kwa hiyo ni kweli kuwa kulikuwa kuna uhasama baina yao juu yako?”
“Ndiyo...lakini ulikwisha...”
“Hebu nielezee juu ya uhasama huo na jinsi ulivyokwisha.”
Moze alisita kidogo. Bado alikuwa hajaelewa yale maswali yalikuwa yanaelekea wapi. Lakini alijua kuwa polisi wakitaka kujua yaliyotokea baina ya Jaka na Joakim watayajua tu, kwani wanafunzi wengi pale chuoni walikuwa wanaujua uhasama uliopo baina yao. Likini sio kama jinsi yeye anavyouelewa. Hivyo akaamua kumuelezea yule askari juu ya uhasama uliojengeka baina ya Jaka na Joakim. Alimuelezea tangu mwanzo jinsi Jaka na Joakim walivyopambana hadi Jaka alipopigwa vibaya na marafiki wa Joakim kule Club Billicanas na kulazwa hospitalini.
“Tangu hapo uhusiano haukuwa wa kirafiki...ingawa Joakim aliacha kabisa kunifuata fuata na Jaka hakutaka kabisa kuendelea na ugomvi wowote na Joakim wala marafiki zake.” Moze alimalizia.
Yule askari alimtazama kwa muda.
“Baada ya kutoka hospitali Jaka hakuongelea kabisa kuhusu kulipiza kisasi juu ya kipigo alichopewa na marafiki wa Joakim?”
“Hapana.”
“Una hakika?”
“Nina hakika afande...kwa sababu pamoja na mimi kumtaka asifanye hivyo, mama yake pia alimuasa kuhusu jambo hilo.”
Muda wote huu yule askari alikuwa akiandika kwenye daftari alilokuwa nalo pale mezani.
“Hivi ndivyo ulivyojibu maswali niliyokuuliza?” Alimuuliza huku akimsukumia lile daftari.
Moze alilichukua na kuanza kusoma. Aligundua kuwa maswali yote aliyoulizwa yalikuwa yametayarishwa mapema na chini ya kila swali yule askari aliandika jinsi yeye alivyojibu. Alisoma kwa makini, swali kwa jibu, mstari kwa mstari, neno kwa neno.
“Ndiyo. Ndivyo nilivyojibu...sasa naomba nielezwe ni kwa nini nimelazimika kupitia mambo yote haya hapa kituoni?” Moze alimjibu na kumuuliza.
“ Naomba usaini hapo chini.”
Moze alisita kidogo.
Kwa nini asaini?
Yule askari aliuona wasiwasi wake, akamwambia, “Hiyo ni kwa ajili ya kuthibitisha kuwa ni kweli wewe mwenyewe ndiye uliyetoa majibu hayo na kwamba hakiongezewi kitu chochote zaidi ya hapo.”
Moze alisaini kwenye ile karatasi kisha akamtazama yule askari.
“Kwa hiyo sielezwi ni kwa nini nimetolewa darasani na kuja kuulizwa maswali haya hapa kituoni? Jaka amekutwa na nini?” Alimuuliza huku akiwa amemkazia macho makavu.
“Sasa unaweza kwenda Bi. Moze...lakini iwapo ungependa kujua, ni kwamba mtu uliyemjua kama Joakim Mwaga amekutwa akiwa ameuawa muda mfupi uliopita juu ya jengo la bweni namba tano...”
Yale maneno yalimshukia kama pigo la nyundo nzito kichwani.
“Joakim ameuawa!?” Alimaka kwa mshituko huku akimkodolea macho yule askari, akili ikimzunguka.
“Oh, Yes…jamaa marehemu tayari.” Askari alimjbu kama kwamba lilikuwa ni jambo la kawaida tu. Moze alibaki kinywa wazi.
Masikini Joakim.
Alikumbuka siku ile alipomfuata chumbani kwake na kumkemea juu ya tabia yake mbaya wakati Jaka alipokuwa amelazwa hospitali. Alikumbuka jinsi Joakim alivyoumia wakati alipomtamkia kuwa yeye alikuwa hampendi hata akimuua Jaka...na jinsi alimuomba msamaha kwa yote aliyoyafanya na kuahidi kutowabughudhi tena yeye na mpenzi wake...na kweli masikini, hakuwabughudhi tena.
Sasa ni nani tena atakayetaka kumuua Joakim, na kwa nini?
Mawazo hayo yalipita kwa kasi sana kichwani mwake. Na hapo wazo jingine lilimjia.
Kwa nini polisi waje wamuulize yeye kuhusu Joakim...na Jaka...?
Aliinua uso wake na kumtazama yule askari kwa macho makali huku uso wake akiwa ameukunja, utambuzi mbaya ukimshukia kichwani mwake.
“Sasa...sasa...kwani Jaka anahusika vipi na swala hilo?”
“Yeye ndiye anayetuhumiwa kwa mauaji hayo.” Yule askari alimjibu taratibu.
“What? Jaka…?” Moze alimaka, kisha akafoka kwa sauti ya juu zaidi, “Haiwezekani! Haiwez...”
“Unaweza kwenda Bi. Moze..maelezo yako yote kuhusiana na swala hili yako kwenye maandishi haya, kwa hiyo lolote utakalosema sasa halina uzito wowote...”
“Ah, sasa…Jaka yuko wapi? Nataka kumuona…haiweze
kani awe amefanya hivyo…anasingiziwa tu!”
“Mnh! Anasingiziwa wakati amekutwa eneo la tukio, akijaribu kukimbia kutoka mahala ambapo amrehemu amekutwa?”
“Hah!”
“Ndiyo hivyo bibie, kama ulikuwa unagonganisha magari basi sasa matokeo ndio hayo…kijana kamuua mwenzake huko!”
“No! Haiwezekani bwana…! Alikutwaje eneo la tukio wewe? Muongo mkubwa!” Moze alimjia juu yule askari.
“Shika adabu yako bibie! Usitake nikutose ndani na wewe hapa saa hizi! Ondoka hapa, na usicheze mbali maana huenda ukahitajika tena kwa ushahidi mahakamani!” Askari naye alimjia juu.
“Yu-wapi Jaka sasa, eeenh? Yu-wapi? Nataka kumuona kabla sijaondoka…niongee naye! Anihakikishie mwenyewe kuwa…”
“Yuko chini ya ulinzi kwa sasa, na wewe nimekwambia unaweza kwenda zako. Ukitaka kumuona fika hapo kaunta uombe kuonana naye!” Jamaa alimjibu huku akiondoka na lile daftari lake,akapotelea ndani zaidi ya kile kituo cha polisi.
Moze alichanganyikiwa.
Alitoka nje ya kile kituo cha polisi bila ya kujielewa na kuelekea kituo cha basi huku akitokwa na machozi. Mawazo yaliyomkabili kichwani mwake yalikuwa ni mazito sana.
Jaka ameua!
Amemuua Joakim!
Inawezekana kweli?
Na hilo la kukutwa eneo la tukio linakuwaje?
Yaani kumbe aliponiambia kuwa atanipatia zawadi ya siku yangu ya kuzaliwa ambayo sitaisahau maisha…alikuwa anamaanisha zawadi ya kumuua Joakim? Zawadi ya kuniulia mtu? Inawezekana kweli? Nani aliyemwambia kuwa mimi nataka Joakim afe? Yaani kweli Jaka atakuwa ameona kuwa hiyo ndiyo zawadi inayonistahili? Leo hii, siku yangu ya kuzaliwa ndio ameamua kumuua mwenzake?
Aaah, hii haiwezekani kabisa!
Jaka hawezi kufanya ujinga kama huu...ni kweli kuwa alikuwa hampendi Joakim, lakini sio kwa kiasi cha kufikia kutaka kumuua...
Oh! Mungu wangu! Kama ni kweli Jaka atakuwa amemuua Joakim, Mungu wangu, ni jinsi gani nitakavyomchukia! Siwezi kuwa na mapenzi naye tena maishani mwangu...!
Ghafla alisimama. Aligeuja na kuanza kurudi kule kituoni. Alienda moja kwa moja hadi kaunta na kuomba kuonana na Jaka.
“Kwa leo huwezi kumuona dada..labda kesho.” Yule askari wa akaunta alimjibu. Moze alishangaa na kuchanganyikiwa.
“Kwa nini?”
“Hii ni kesi ya mauaji bibie unajua hiyo? Huyo mtu unayetaka kumuona kaua mtu, na hilo sio jambo dogo. Kwa leo hii atakuwa na kazi kubwa ya kujibu maswali huko ndani, sio rahisi kwa mtu yeyote kumuona...we’ bora uje kesho tu.”
Moze aliondoka huku akibubujikwa na machozi kama mtoto mdogo.
__________________
Wakati Moze akijibu maswali ya yule askari, Jaka naye alikuwa kwenye chumba kingine ndani ya jengo lile lile akitoa maelezo yake kuhusiana na tuhuma zilizomuangukia. Sasa aliinua uso wake taratibu kuwatazama wale askari wawili waliokuwa mbele yake ambao walikuwa wakimtazama kwa hasira, meza kubwa ikiwa imekaa baina yake na wake askari. Mmoja kati ya wale askari wawili, ambaye alikuwa mnene, mfupi na mwenye macho makubwa sana, alimsukumia Jaka karatasi iliyokuwa na maelezo yake huku akimfokea.
“Nasema haya maelezo hatuyataki! Andika mengine!”
Jaka aliendelea kumtazama kwa mshangao.
“Mimi nimeshasema hapo mwanzo na ninasema tena...sina maelezo mengine zaidi ya hayo kwa sababu huo ndio ukweli wenyewe! Sasa kama nyie...” Jaka alianza kujibu kwa ukali, lakini hakuwahi hata kumalizia jibu lake, kwani yule askari aliinuka na kumzaba kofi kali la uso na mara ile ile alimkamata nyuma ya shingo yake na kuubabatiza uso wake kwa nguvu pale mezani, yowe la maumivu likimtoka Jaka bila kutarajia.
“Pumbavu! Unataka kuleta mchezo hapa! We’ unaua mtu halafu unategemea sisi tuamini huu upuuzi ulioandika hapa? Unataka kutuchanganya sisi, eenh?”
“Mi’ sina maelezo mengine zaidi ya hayo ndugu zangu, mtaniumiza bure tu jamani!” Jaka alijibu huku akiwa amekandamizwa uso wake pale juu ya meza. Yule askari alimuinua kwa nguvu na kumkwida fulana yake kwa mbele na kumvuta hadi pua zao zikagusana.
“Sikiliza we’ dogo, tena sikiliza kwa makini...tumesh
akabiliana na wababe zaidi yako sisi, na wote walianza na msimamo kama wako lakini hatimaye walisalimu amri!” Alimkoromea.
Jaka alimtazama yule askari bila ya kusema neno, na yule askari aliendelea, “Sasa kwa nini usiseme tu ukweli wako kabla hatujakuchakaza zaidi?”
“Ukweli tayari upo hapo kwenye hiyo karatasi afande...au ukweli gani zaidi unaoutaka wewe?”
Yule askari alimsukuma kwa hasira, na Jaka alipepesuka kwa nyuma, akaangukia kwenye kiti alichokuwa amekalia na kupinduka nacho mpaka sakafuni kwa kishindo kikali.
“Ukweli wa kwamba umemuua Joakim Mwaga kwa sababu unazozijua mwenyewe...na sisi tunazitaka hizo sababu!” Yule askari alimbwatia.
Akiwa amelala chali pale sakafuni, Jaka alihisi mchirizi wa damu ukimtoka puani baada ya kupigizwa uso wake kwenye ile meza. Alijipangusa damu ile kwa mgongo wa kiganja chake huku akijizoazoa kutoka pale sakafuni. Yule askari mwingine alimsaidia kuinuka kutoka pale chini na kumuweka tena kitini. Kisha alichukua ile karatasi iliyokuwa na maelezo ya Jaka na kumueleza, “Sawa, sasa tuanze tena kupitia haya maelezo yako.”
Jaka alikuwa akitazamana na yule askari mnene kwa hasira, na yule askari mwingine akaanza kuongea.
“Kwa mujibu wa maelezo yako uliyoandika...” Alisema yule askari wa pili huku akisoma kutoka kwenye ile karatasi. “...ni kwamba wewe uliletewa ujumbe na mtoto usiyemfahamu leo hii, muda wa saa nane kasoro mchana, kuwa Joakim alikuwa anaomba mkutane juu ya jengo la bweni namba tano, sawa?”
“Sawa.”
“Na kwamba ulipofika kule juu ndio ukamkuta Joakim akiwa tayari ameuawa...”
“Ndiyo.”
“...na kabla hujafanya lolote, askari walitokea na kukuweka chini ya ulinzi.”
Jaka aliendelea kusikiliza.
“Na umeandika kwamba Joakim alikuwa ameuawa na watu wengine ambao walitaka wewe ukamatwe na kuhukumiwa kwa kosa hilo badala ya wao, ili kukufunga mdomo...”
“Ndiyo hivyo...” Jaka alidakia na kutaka kusema zaidi, lakini yule askari alimnyamazisha kwa kumnyanyulia mkono. Aliendelea kusoma.
“Kwamba hata glovu zilizokutwa chumbani kwako zilikuwa zimewekwa makusudi ili kuhakikisha kuwa ni wewe ndiye unayehukumiwa kwa kosa hilo.”
Jaka alikubaliana na maelezo yale kwa kichwa, yule askari aliendelea.
“Kwa hiyo, unaandika, hata huyo mtu aliyepiga simu polisi kutaarifu kuwa kulikuwa kuna mauaji juu ya jengo unaloishi pale chuoni, ni ushahidi tosha kuwa mambo yote hayo yamepangwa, ndio maana huyo mtu aliyepiga simu alijua kuwa wewe ukienda kule juu utaikuta maiti ya Joakim hivyo akaiarifu polisi ili wewe ukamatwe.”
Jaka aliendelea kusikiliza.
“Mwisho unamalizia kwa kuandika kuwa haya yote yamepangwa yakukute kwa sababu wewe umegundua njama za biashara ya madawa ya kulevya, na ili kuhakikisha kuwa hupati nafasi ya kuzitoa njama hizo kwenye vyombo vya dola, wamekupakazia mauaji haya ili kukuharibia sifa yako na kupoteza imani ya Jamhuri juu yako ili kila utakalosema lisitiliwe maanani.”
“Na tayari wameshaanza kufanikiwa katika hilo afande...si unaona hata nyie hamniamini?” Jaka alidakia kwa uchungu.
 
RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA ARUBAINI.
“Mwisho unamalizia kwa kuandika kuwa haya yote yamepangwa yakukute kwa sababu wewe umegundua njama za biashara ya madawa ya kulevya, na ili kuhakikisha kuwa hupati nafasi ya kuzitoa njama hizo kwenye vyombo vya dola, wamekupakazia mauaji haya ili kukuharibia sifa yako na kupoteza imani ya Jamhuri juu yako ili kila utakalosema lisitiliwe maanani.”
“Na tayari wameshaanza kufanikiwa katika hilo afande...si unaona hata nyie hamniamini?” Jaka alidakia kwa uchungu.
Yule askari alimtazama tu bila ya kusema neno, kisha akaendelea kusoma.
“Pia, hapa chini umeandika kuwa mtu ambaye unadhani kuwa anahusika na njama hizo za kukutia wewe hatiani bila makosa ni Anthony Athanas Wanzaggi, au Tony, na washirika wake.”
Askari aliinua macho yake na kumtazama Jaka.
“Una hakika na habari hii?” Alimuuliza.
“Nimeandika nadhani atakuwa anahusika kwa sababu yeye ndiye anayehusika na njama za biashara ya madawa ya kulevya nilizozibaini.”
“Afande huyu anatupotezea muda tu na porojo zake...” Yule askari mnene alidakia. Jaka akamtolea uvivu.
“Oh, Yeah? Sasa kwa nini msiyafanyie uchunguzi mambo ninayowaeleza? Kwa nini msimfuatilie huyo mtu ninaewatajia halafu mkahakikisha iwapo ninasema ukweli au vinginevyo? Au mnamuogopa kama walivyoogopa wenzenu?” Alimfokea.
Loh!
Mara ile ile mkono wa yule askari aliyekuwa akimsomea maelezo yake ulichomoka na kumdaka koo kwa nguvu.
“Kwa sababu hatuelewi ni kwa nini wewe usitoe taarifa juu ya njama hizo za biashara ya madawa ya kulevya mapema, na uje uamue kuzitoa sasa, baada ya kuwa umekamatwa kwa kosa la mauaji...” Alimwambia kwa sauti ya upole huku akiwa amemkaba koo namna ile.
Jaka alibaki akiwa ametumbua macho.
“Na kwa nini hao watu wamuue Joakim na wasikuue wewe ?” Yule askari mnene naye alidakia.
“Sasa hilo ndilo mngepaswa muwaulize hao watu ninaowatajia, mimi nitajuaje?” Jaka alijitutumua kumjibu. Yule askari wa pili alimuachi koo na kurudi kuketi kitini.
“Utetezi wako unanuka Jaka...unasema Joakim alikuandikia huu ujumbe ndio maana ukaenda kule juu, tutahakikisha vipi kuwa huu ni mwandiko wake?”
Jaka aliwatazama wale askari mmoja baada ya mwingine.
“Njia ya kuhakikisha hilo ni ndogo sana sidhani kama mnahitaji mimi niwaelekeze namna ya kulihakikisha hilo…na kama si Joakim mnadhani ni nani atakuwa ameandika ujumbe huo...?” Aliwajibu na kuwauliza.
“Mimi nadhani ni wewe ndiye uliyeandika huu ujumbe Jaka, ili utupoteze maboya...” Yule askari mnene alimjibu kwa jeuri.
Aka!
“Unaongea nini wewe?” Jaka alibwata, kisha akaendelea, “Yaani nijiandikie huo ujumbe ili mkija kule juu mnikute nao halafu niwambie kuwa nimebambikiwa? Hivi kweli inakuingia akilini hiyo afande? Au hutaki tu kukubali maelezo yangu?”
“Ati!? Ongea kwa adabu wewe!” Alifoka yule askari mnene huku akimtupia Jaka kofi kwa nguvu. Safari hii Jaka alikuwa macho, kwani alishaona kuwa wale askari hawakuwa na nia ya kumuelewa makusudi, hivyo kwa mkono wake wa kulia alimdaka mkono yule askari kabla lile kofi halijamfikia.
“Swala la maelezo yangu kuwa hayafai au yanafaa si juu yenu, hiyo ni juu ya hakimu kuamua hapo mtakapoifikisha hii kesi mahakamani. Kwa namna moja mnaogopa kuwa nikifika mahakamani nitatoa siri za biashara haramu na kuhusika kwa huyo mtu niliyewatajia...au na wengine mnaowafahamu...katika biashara hiyo...” Alimwambia huku bado akiwa amemshika ule mkono, na hapo yule askari akamtupia kofi la pili, Jaka akalidaka kwa mkono wake mwingine, na kuendelea,“... mnataka kesi hii ya kufungua na kufunga pindi ifikapo mahakamani siyo? Mnatarajia nikiri kuwa nilimuua Joakim ili iwe open and shut case sio? Basi eleweni kuwa kazi yenu ni kulinda na kutumikia jamii, na jamii hailindwi na haitumikiwi kwa kupigwa makofi na mateke!” Baada ya kusema hayo aliitupa pembeni mikono ya yule askari ambaye muda wote ule alikuwa amepigwa na butwaa. Hajawahi kuona mtu akijiamini kiasi kile akiwa chini ya ulinzi hata baada ya vitisho kama vile.
“Mimi nimeshaandika maelezo yangu, na sababu ya mimi kuwa kule juu ya lile jingo tayari iko wazi kwenye huo ujumbe nilioandikiwa…sasa sioni kwa nini muendelee kuniweka tu hapa kituoni wakati nina mambo kibao ya kufanya...” Jaka alikuwa anaendelea kuwapa vipande vyao, na wale askari ambao kwa sekunde kadhaa hivi walikuwa wamepigwa bumbuwazi. Yule askari aliyemkamata kule juu ya ghorofa alikichukua kile kijikaratasi alichoandikiwa na Joakim.
“Kwa hiyo huu ndio ushahidi unaokutia kiburi, sio?” Alimuuliza huku akimtazama kwa hasira.
“Sio kunitia kiburi..ndio unaeleza kwa nini nilikuwa pale wakati ule…”
“Huu?” Jamaa alimuuliza tena huku akimuoneshea kile kijikaratasi.
“Of Course!” Jaka alimjibu huku amekunja, na hapo hapo uso ulimsawajika pale alipomshuhudia yule askari akikitumbukiza kinywani kile kikaratasi chenye ujumbe kutoka kwa Joakim na kuanza kukitafuna tarattibu huku akiwa amemkazia macho ya hasira.
Hah!
“Pumm-Baaaaaavvvvvv!!!” Alimaka na kukurupuka kutaka kumrukia, na hapo wale askari walimrukia yeye na kumuangushia kipondo kizito. Makofi, mateke, ngumi. Alijaribu kusimama na kujitetea lakini hakuweza. Kipigo kilikuwa kikimuangukia kutoka kila upande na kila kilipokuwa kikiendelea, ndivyo kilivyozidi kuwa kizito.
Hatimaye aliishiwa nguvu na kulala chini huku akimtazama yule askari akimalizia kuutafuna ule ushahidi na kuumeza kabisa.
“Aaaah wanaharamu mmenipotezea ushahidi wangu (akawatukania mama zao) nyieeeee!” Aliwakemea kwa nguvu hafifu. Mapigo yaliendelea kumuangukia kama mvua.
Alipoteza fahamu...
__________________
Mama Jaka alizipokea habari za kukamatwa na kuhusishwa mwanaye na mauji kwa mshituko mkubwa sana. Raymond Mloo ndiye aliyempelekea habari zile za kushtusha na kutatanisha. Mara baada ya kupata habari za kukamatwa kwa rafikiye, Raymond alienda moja kwa moja hadi pale kituoni na kuomba kuonana naye. Alikataliwa kabisa kumuona, lakini kitu kilichomshangaz
a ni kuona kuwa polisi hawakutaka kumuuliza maswali yoyote hata pale aliposema kuwa yeye alikuwa akiishi chumba kimoja na Jaka.
Kama kwamba walikuwa wakimtaka Jaka tu, na sasa wameshampata.
Jioni ile ile alikwenda kumpasha habari mama Jaka.
Kitu kilichomuuma zaidi yule mama ni kule kuzuiliwa kumuona mwanaye siku ile alipoenda pale kituoni baada ya kupata taarifa za kukamatwa kwake.
Siku iliyofuata magazeti yalipambwa na habari za mauaji yale. Picha za Jaka na Joakim zilitokea kwenye ukurasa wa kwanza wa gazeti maarufu nchini likiyanadi mauaji yale kwa kichwa cha habari kilichosomeka: Mauaji ya kutisha Chuo Kikuu: Mtuhumiwa mbaroni.
Habari iliyofuatia kichwa cha habari kile ilielezea jinsi mtuhumiwa alivyokutwa katika eneo la tukio na kutiwa mbaroni “katika harakati za kutoroka kutoka eneo la tukio”, na polisi ambao walipigiwa simu na “msamaria mwema” kuwaarifu juu ya tukio lile “la kinyama” muda mchache kabla ya kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo.
Pia kulikuwa kuna habari ambazo mwandishi wa habari ile alizipata baada ya kuwahoji baadhi ya wanafunzi wa pale chuoni waliowafamu marehemu na mtuhumiwa, kuwa kumekuwa kuna uhasama wa muda mrefu baina ya marehemu na mtuhumiwa na kwamba walishawahi kufanyiana “vitendo vya kiadui” kabla ya tukio hilo la kutisha.
Gazeti la “Daily News” pia liliandika juu ya habari ile chini ya kichwa cha habari kilichosomeka: Terrible murder at the Hill: Suspect under custody.
Haikuwa mpaka siku mbili baada ya tukio ndipo Jaka alipopata nafasi ya kuonana na mama yake. Alikuwa amekonda sana kwa siku mbili zile na uso wake ulikuwa umevimba kutokana na kipigo. Huku akibubujikwa na machozi mama yake alimuuliza iwapo yale aliyoyasikia na kuyasoma kwenye magazeti yalikuwa yana ukweli wowote.
“Hayana ukweli mama...ninasingiziwa tu, na najua ni kwa nini...” Jaka alijibu kwa uchungu.
“Ni kwa nini unasingiziwa jambo kama hili mwanangu? Itakuwa ni yale yale ya akina Tony?” Mama alimuuliza kwa simanzi.
“Ni yale yale tu mama…ni mazito sana mama’angu. Nikipewa nafasi ya kuyaeleza mahala muafaka, nitayaeleza. Ni mazito sana kwa kweli!”
Yule mama alimtazama mwanaye kwa muda.
“Basi usiwe na wasiwasi mwanangu, mimi nilijua kuwa huwezi kufanya jambo kama hilo...na nitahakikisha kuwa sheria inafanya kazi yake nawe unapewa nafasi ya kusikilizwa. Utaachiwa tu.” Alimwambia mwanaye.
Jaka alimtazama mama yake huku akijitahidi kuyazuia machozi yaliyokuwa yakimuelemea.vAlijua kuwa kwa hali aliyoiona mpaka kufikia pale, uwezekano wa yeye kutoka mikononi mwa “sheria” ulikuwa mdogo sana.
“Mimi nataka wewe usiwe na wasiwasi mama...” Alimwambia.
“Wasiwasi lazima niwe nao mwanangu. Kesi ya mauaji sio jambo dogo na najua kuwa hao waliofanya njama ya kukufikisha wewe hapa watafanya kila wawezalo kuhakikisha kuwa unabaki hapo na unapotea kabisa...hivyo na sisi ni lazima tutafute sheria...nina ahadi ya kuonana na wakili mmoja mzuri sana mchana huu, na nadhani jioni ya leo hii atakuja kukuona.”
Jaka alimtazama mama yake na kujaribu kutabasamu.
“Asante sana mama...”
“Unadhani ni nini ambacho mama ataacha kukifanya kwa ajili ya mwanaye?”
Tabasamu la Jaka likatanuka zaidi. Mama na mwana walikumbatiana, kisha mama akaondoka.
Saa mbili baadaye Moze alifika pale mahabusu kumuona.
Walitazama kwa muda bila ya kusemezana lolote, Moze akionekana mnyonge na aliyekata tamaa kabisa. Jaka alijaribu kutafuta maneno ya kumliwaza mpenziwe lakini hakuyapata.
“Kwa nini Jaka?” Hatimaye Moze aliuliza kwa sauti ya chini.
Jaka alimtazama kwa mshangao bila ya kuelewa alikuwa anamaanisha nini.
“Kwa nini...? Unamaanisha nini Moze?” Alimuuliza.
Moze alimtazama kwa muda na Jaka akahisi kuona kitu kama hasira machoni kwake, hakujua hasira ile ilikuwa ni kutokana na mambo yaliyomkuta yeye au ni kitu kingine.
“Kwa nini umemuua Joakim, Jaka? Hicho ndicho ninachomaanisha...”
Hah!
Moyo ulimlipuka Jaka na hapo hapo akaingiwa na unyonge wa hali ya juu.
“Mungu wangu, Moze! Huwezi kuamini kuwa nitakuwa nimemuua Joakim! Ndivyo unavyoamini hivyo? Hata wewe?” Alimuuliza kwa fadhaa kubwa, kisha akaendelea,“Sikumuua Joakim Moze…siwezi kufanya kitu kama hicho kabisa! Na wewe unajua hilo...!”
“Sasa ilikuwaje hata ukakutwa eneo la mauaji?” Moze aliuliza kwa hasira. Jaka alizidi kupigwa na butwaa.
Hata mpenzi wangu naye haniamini!
Kabla Jaka hajajibu swali lile Moze alimtupia swali jingine.
“Na ilikuwaje glovu zilizotumika kwenye mauaji hayo zikutwe chumbani kwako? Tena chini ya godoro la kitanda chako, sio cha Raymond?”
Yaani hadi mpenzi wangu naye anashindwa kuniamini katika hili!
“Moze, we’ unajua kuwa watu tuliokuwa tunapambana nao ni watu aina gani...vyote hivyo vimetegwa makusudi ili nionekane mimi ndiye muuaji, lakini...” Jaka alijaribu kumuelewesha mpenzi wake huku akihisi nguvu zikimwishia kwa kila pumzi aliyokuwa akiitoa katika kufanya hivyo.
“Wacha kusema uongo Brown! Wewe umemuua mwenzako...umemuua kwa sababu siku zote ulikuwa unataka kulipiza kisasi kutokana na mambo waliyokufanyia na wenzake...” Moze alibwata huku akitiririkwa na machozi.
E bwana we!
Jaka aliona kama vile yuko ndotoni.
“Moze…”
“...sikutegemea Jaka, sikutegemea kabisa kama itafikia siku utafanya kitu kama hiki...unamuua mwenzio! Kisa nini? Kisasi? Mapenzi?”
Jamani!
“Moze! Usiwe na mawazo hayo mpenzi...” Jaka alimwambia kwa kuomboleza huku akipeleka mikono yake ili amshike mabega kumpoza. Moze aliisukuma pembeni mikono ile na kusimama kutoka kwenye benchi alilokuwa amekalia, akarudi nyuma kujiweka mbali naye.
“Usinishike!” Alimaka huku akilia.
“Moze, Please!”
“Brown uliposema kuwa unaniandalia zawadi ambayo sitaisahau maishani mwangu kumbe ulikuwa unamaanisha zawadi hii? Zawadi ya kuniulia mtu?”
“Heeeh!”
“Kwani nilikwambia kuwa nataka damu ya mtu ndiyo niamini kuwa unanipenda Brown...?”
Looh!
“Moze...you are over-reacting...” Jaka alijitahidi kumpoza mpenziwe, akimaanisha kuwa alikuwa amepandwa jazba bila sababu tu. Ile kauli ikaonekan kumkera Zaidi Moze.
“N’na over-react miye? N’na Over-React? Kweli? Brown...umemuua mtu in cold blood, for God’s sake, halafu unasema n’na over-react!”
“Moze, unajipandisha jazba bila sababu juu ya hili mpenzi, na ndio maana unashindwa kunielewa...mimi siwezi kuua mtu, na wala sijamuua Joakim...hizo ni njama tu ...kuna mambo nimeyajua ambayo...”
“Sasa nimekuwa nashindwa kukuelewa...kwa nini usisubiri kutoa maelezo yako kwa hakimu Jaka...? Haitosaidia kitu kunieleza mimi hayo maelezo...penzi langu lote kwako...na mambo yote yaliyotupata kwa ajili ya penzi letu, leo hii umeona zawadi ya kunipa kwenye Birthday yangu ni kuniulia adui yako? Sasa ona faida yake...!” Moze alisema kwa masikitiko huku akilia.
Lah!
Mshangao uliomvaa Jaka wakati akimtazama mpenzi wake aliyedhani kuwa alikuwa akimjua vizuri sana ulikuwa ni mkubwa kuliko. Hakuamini kabisa yale aliyokuwa akiyasikia. Sasa hivi ndio alikuwa akiuhitaji sana msaada wa Moze, msaada wa upendo, huruma na kuelewa kutoka kwa mpenzi wake. Badala yake, mpenzi wake mwenyewe ndiye anakuwa wa kwanza kumtupia lawama na kutomwamini! Ni nani tena zaidi ya mama yake na Raymond atakayemuamini?
Nguvu zilimwisha.
“Moze...mbona hiyo siyo zawadi niliyokuwa nimekuandalia? Zawadi yako ilikuwa tofauti kabisa...mimi sikumuua Joakim, na naapa kwa jina la mola wangu kuwa sikumuua...nakuomba sana uniamini mpenzi wangu, kwani imani yako wewe ni nguvu kubwa sana kwangu katika kipindi hiki...naomba uniamini mpenzi...”
Lakini Moze alikuwa kama aliyepagawa. Ilikuwa vigumu sana kwake katika mazingira yaliyokizunguka kifo cha Joakim, kuamini kuwa Jaka hakuhusika na kifo kile.
“Jaka, mimi siwezi kukupenda tena maishani mwangu kutokana na jambo ulilolifanya...kila kitu kinaonesha kuwa ni wewe ndiye uliyemuua Joakim...na mimi najua kuwa unazo sababu nyingi za kutaka kufanya hivyo, nitakachoweza kufanya Jaka ni kukuombea kwa Mungu tu akusamehe, lakini sidhani kama nitaweza tena kuwa na wewe kama nilivyokuwa nawe hapo mwanzo...” Moze alimwambia kwa masikitiko, kasha akageuka na kuanza kutoka nje ya chumba kile.
Jaka alichanganyikiwa.
“Lakini Moze...Joakim alikuwa ni rafiki yangu...tulisha
patana siku chache kabla ya kifo chake…wakati nilipokuwa nimelazwa pale hospitali!” Jaka alimambia kwa hamaniko.
Moze alisimama ghafla na kutulia tuli. Kisha aligeuka taratibu na kumtazama kwa macho yaliyokuwa na mchanganyiko wa mshangao, kutoamini na fadhaa.
“Joakim alikuwa rafiki yako tangu lini, Jaka?” Alimuuliza kwa sauti ya upole huku akimshangaa waziwazi.
Jaka aliguna na kutikisa kichwa kwa kukata tamaa. Aliona wazi kuwa hakuna atakalosema ambalo Moze atalielewa katika hali ile.
“Sasa kama rafiki yako ndiyo umemfanya vile...haya mie unayeniita mpenzi wako utanifanya nini...?” Moze alimuuliza kwa uchungu.
Heh!
 
IAmShedeOne,

Hata kama ujumbe uliotoa ni kwamba anayetaka kusoma na asome na asiyetaka aache lakini sidhani kama lengo lako kuu ni hilo... kwamba "ukitaka, soma or else... sepa!"

Paragraphing kwenye story ndefu kama hii (in fact, any story ) ni muhimu (soma lazima)!

Paragraphing inatoa ventilation kwa story na hivyo kuifanya ipumue vizuri!

Story ikipimua, ina-release Oxygen inayompa pumzi Msomaji aendelee kuisoma!

Hussein Tuwa ndie Mwandishi ninayemkubali zaidi kwa walio hai!

Kwangu mimi, Hussein Tuwa ni mkali kuliko hata Marehemu Ben Mtobwa (RIP Babu... he used to call me babu).

Hussein Tuwa ni mbaya (sifa) kwenye plotting! Ndo vile tu amezidiwa na watu kama akina Elvis Musiba katika kucheza na maneno!

That said, hii story ingevutia sana wasomaji endapo ingepangiliwa vizuri!
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom