RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA THELATHINI NA MBILI
“Wacha niongeze chai, inaelekea kikao kitakuwa kirefu.” Raymond alisema huku akichukua birika la umeme wanalotumia kuchemshia chai.
Nusu saa baadaye, akiwa ameshasikia kila kitu kuhusu Tony na kundi lake, na historia mbaya baina yao na Jaka, Sajenti John Vata aliinuka na kupeana mikono na wale vijana. Aliwashukuru kwa msaada wao na kukumbusha kuwa iwapo kutatokea tatizo au taarifa nyingine yoyote mpya, wawasiliane naye.
Waliagana.
___________________
Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Poisent Ndimbalema, mkuu wa kitengo cha kudhibiti madawa ya kulevya katika wilaya ya Kinondoni, aliisoma kwa mara ya pili ripoti iliyowasilishwa mezani kwake na Sajenti John Vata, na kwa mara nyingine tena alijikuta hajui la kufanya.
Ilikuwa ni ripoti nzuri na kwa kanuni na misingi ya kazi, jambo alilotaka kulifanya Sajenti Vata lilikuwa ni sawa kabisa. Lakini Mrakibu Mwandamizi Poisent Ndimbalema, akiwa na umri wa miaka arobaini na minane alielewa zaidi jinsi mambo yalivyokuwa yakiendeshwa kuliko Sajenti John Vata ambaye bado alikuwa mgeni katika jeshi la polisi.
Mzee Athanas Wanzaggi alikuwa ni mtu mkubwa sana sio tu jijini Dar es Salaam, bali pia nchini kote. Ingawa hakuwa Waziri wala kiongozi yoyote serikalini, utajiri wake ulifahamika na kila mtu nchini, mawaziri na viongozi wakubwa serikalini wakiwemo. Yeye pamoja na viongozi wake wa kazi walimtambua mzee Wanzaggi ni nani na ana uwezo gani katika nchi hii. Ndimbalema alijua kuwa kutokana na ripoti ile, John Vata alitakiwa amuweke chini ya ulinzi kwa mahojiano mtoto wa mzee Wanzaggi. Pia alitakiwa aende nyumbani kwa mzee Wanzaggi na afanye upekuzi katika chumba cha mtoto yule ambaye bado alikuwa chini ya himaya ya baba yake.
Alijaribu kufikiria jinsi magazeti yatakavyoiandika habari ile na mwili ulimsisimka. Waandishi wa habari wana namna ya kunusa mambo kama haya…sijui wananusaje…na wakishanusa huwa hawana simile…
Aliiweka pembeni ile ripoti ya kurasa ishirini na kuzitupia macho karatasi mbili zilizokuwa mezani kwake ambazo ziliidhinisha kufanyika kwa matendo ambayo Sajent Vata alipendekeza yafanyike katika ripoti ile yake.
Karatasi moja ilikuwa ni “Search Warrant” iliyomuidhinisha Sajenti John Vata kwenda kupekua vyumba vya Anthony Wanzaggi, kile cha nyumbani kwa baba yake na kile anachotumia pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Karatasi ya pili ilikuwa ni “Arrest Warrant”, ambayo ilimpa Sajenti John Vata idhini ya kumkamata na kumuweka chini ya ulinzi Anthony Wanzaggi kwa tuhuma za kuhusika na kifo cha Rose na kwa mahojiano kuhusu kiasi cha unga wa dawa za kulevya kilichokutwa chumbani kwa Rose.
John Vata asingeweza kuzitumia idhini zile bila ya yeye, Mrakibu Mwandamizi Poisent Ndimbalema, kusaini katika sehemu zinazostahili kwenye karatasi zile. Ni saini zake ndizo zilizokuwa zinasubiriwa ili kumfanya John Vata aweze kutekeleza kazi yake ambayo kwa hakika alikuwa ana ari nayo sana.
Mrakibu Mwandamizi Poisent Ndimbalema alikunja uso na kufikiri kwa muda mrefu, kisha alishusha pumzi ndefu na kuchukua simu yake ya kiganjani, akaanza kumpigia mkubwa wake wa kazi, mkuu wa Idara ya kudhibiti madawa ya kulevya wa Mkoa wa Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi (ACP) wa Polisi, Albert Bangusillo.
_____________________
“Kwa sasa hivi usifanye jambo lolote, Poisent. Umefanya vizuri sana kunitaarifu juu ya habari hii kabla ya kuchukua hatua yoyote...” Albert Bangusillo alitoa maelekezo kupitia kwenye simu baada ya kusikiliza maelezo ya Mrakibu Mwandamizi Poisent Ndimbalema, kisha akaendelea, “… nitakupigia simu baada ya muda mfupi kukupa maelekezo zaidi juu ya nini cha kufanya, na asijue mtu mwingine yeyote kuhusu hiyo ripoti ya Vata na swala zima hilo mpaka hapo utakapoelekezwa vinginevyo, sawa?” Akakata simu.
“Sawa mzee…” Albert alijibu, lakini simu ilikuwa imeshakatwa.
Upande wa pili wa simu ile, ACP Albert Bangusillo alifikiria kwa muda mfupi kisha akaitumia tena simu yake kupiga namba fulani. Upande wa pili simu ile ilipokelewa na Bangusillo aliisikia sauti aliyoitarajia, sauti iliyotulia, iliyotoka kama kwamba mwenye sauti ile alikuwa amepaliwa na moshi.
“ Hallo… Raul hapa…”
Dakika kumi baadaye simu ya Mrakibu Mwandamizi Poisent Ndimbalema iliita. Poisent alipoiinua simu ile, alipokea maelekezo kutoka kwa ACP Albert Bangusillo kuhusiana na Sajenti John Vata.
__________________
Upande mwingine, mapenzi baina ya Jaka na Moze yaliendelea kama kawaida, ingawa kwa siku za mwanzo baada ya kifo cha Rose yalilegalega kutokana na Moze kutokuwa katika hali yake ya kawaida na kujilaumu sana kwa kutokuwa pamoja na rafiki yake siku ile aliyokumbwa na maafa yale ambayo wao wangeweza kukisia tu yalikuwa ni makubwa kiasi gani, kwani ni Rose pekee ndiye aliyejua ukubwa wa maafa yale. Lakini kadiri siku zilivyopita, ndivyo hali ilivyozidi kurudi kama hapo awali.
Kufikia wakati huu hakukuwa na shaka tena baina yao juu ya nani aliyemfanyia Rose unyama ulioishia kwenye kifo chake kwani fumbo lililokuwa kwenye maneno ya mwisho ya Rose lilishafumbuliwa na wote waliamini kuwa baada ya muda mfupi, mkono mrefu wa sheria ungemtia Tony mbaroni kama jinsi Sajenti Vata alivyoahidi na alivyoonesha kudhamiria.
Waliamua kuwasahau Tony na wenzake na kuyaacha nyuma yaliyomtokea rafiki yao Rose, na kuangalia mbele.
____________________
Wiki mbili baadaye Raymond Mloo aliyeonekana mwenye wasiwasi na asiyekuwa na raha aliingia chumbani kwao pale chuoni na kumkuta Jaka akijisomea. Jaka alimuuliza kulikoni.
“Inakuwaje mpaka leo Tony bado anatemebea huru tu, Jaka?” Ray aliuliza kwa hasira, kisha akendelea, “Yaani…nilitegemea tangu siku ile yule sajenti alipokuja kutuuliza maswali yake hapa agalau angekuwa ameshakamatwa na kuhojiwa kikamilifu, sio…?”
“Sasa Ray, una hakika gani kuwa bado hajahojiwa na polisi mpaka sasa?”
Raymond alitupa mikono yake hewani na kwa kukata tamaa.
“Aakh! Kila kitu kiko wazi…ile sio tu kesi ya madawa ya kulevya, bali ni ya mauaji pia…usitake kuniambia kuwa ameweza kutoa maelezo ya kutosha kuwafanya polisi wamwachie kwa tuhuma zote mbili Jaka…yule wameamua kumuachia tu bwana!” Alimaka.
“Hizo ni tuhuma nzito sana Ray, sio rahisi kuachiwa hivi hivi tu bila ya kuchukuliwa hatua….”
“Eee..enhe-e? Then welcome to the world my friend…hivi ndivyo dunia ilivyo siku zote! Kinyume na utaratibu, kinyume na matarajio!” Alitoka tena nje kwa hasira na kubamiza mlango. Kwa muda mrefu Jaka alibaki akiwa anaukodolea macho ule mlango akiyatafakari yale maneno ya Raymond Mloo…
Wiki moja baadaye Jaka alimuona Tony.
Ilikuwa ni kiasi cha saa tatu za usiku hivi wakati alipokuwa akitoka maktaba kujisomea. Ingawa ilikuwa usiku, aliweza kumtambua mara moja kutokana na mwendo wake. Tony alipita kama hatua kumi mbele yake bila ya kumjua akielekea sehemu ya kuegesha magari iliyoko kando ya duka la vitabu la pale Chuoni. Huku moyo ukimwenda mbio, Jaka aliongeza hatua na kuanza kumfuata kwa nyuma, ingawa hakujua angemfanya au angemwambia nini pindi akimfikia–akilini mwake alikuwa akiyakumbuka maneno ya Raymond Mloo kuhusiana na swala zima la Tony kutochukuliwa hatua yoyote na polisi. Tony alipita ubavuni mwa jengo la ofisi ya posta lililokuwa jirani na duka la vitabu pale chuoni, na Jaka alipita upande wa pili wa lile jengo ambako ndio kulikuwa na njia ya wapitao kwa miguu, kwani ni wenye magari yaliyoegeshwa kwenye ule uwanja wa kuegeshea magari tu ndio waliopita upande ule aliopitia Tony. Kutokea pale alipokuwa aliweza kumuona Tony akiwa katika harakati za kufungua mlango wa gari lake lililokuwa limeegeshwa katika uwanja ule.
Kulikuwa kuna gari jingine moja lililoegeshwa kando ya lile la Tony, na mbele zaidi kulikuwa kuna Baa ya wanafunzi ambako muziki ulisikika ukitokea upande huo. Mara, kama aliyekumbuka kitu, Tony aligeuka kuangalia upande ule ulipokuwa ukitokea ule muziki, halafu aliondoka kuelekea kule Baa huku akiacha mlango wa gari lake ukiwa wazi. Haraka sana Jaka aliuruka uzio wa mabomba uliouzunguka uwanja ule na kukimbia upesi hadi ubavuni mwa gari la Tony. Kwa jinsi lile gari lilivyoegeshwa, ule mlango wa dereva ulikuwa upande ilipokuwa ile Baa.
Taratibu aliweka vitabu vyake chini na kukiweka kwenye mfuko wake wa shati kijitabu chake kidogo cha anuani, kisha alijiinua taratibu na kuanza kuchungulia ndani ya lile gari kwa kupitia dirishani. Kwenye kiti cha abiria kando ya kile cha dereva kulikuwa kuna mkoba mdogo wa kiofisi, au Briefcase, ambao hakuweza kung’amua mara moja ulikuwa wa rangi gani kutokana na mwanga hafifu katika eneo lile. Alitupa jicho kule alipoelekea Tony na kumuona akiongea na jamaa wengine wawili nje ya ile Baa hali wanafunzi wengine wachache wakiwa wamezagaa nje ya Baa ile, wengi wao wakiwa wanasubiri chipsi na mishikaki vilivyokuwa vikiuzwa pale nje.
Alirudisha macho yake kwenye kiti cha nyuma ndani ya lile gari na mara moja alibonyea tena ubavuni mwa gari lile baada ya kusikia sauti za watu zikielekea pale alipokuwa kutokea nyuma yake. Lilikuwa ni kundi la wanafunzi waliokuwa wanatoka kwenye mijadala ya kujisomea kwa makundi, na wengine, kama yeye walikuwa wanatoka maktaba. Lile kundi la wanafunzi lilipita kwa vicheko na maongezi ya sauti za juu. Jasho lilianza kumtiririka mgongoni na usoni huku moyo ukimwenda mbio kwa wasiwasi. Wale jamaa walisimama mbele ya duka la vitabu kwa kama dakika mbili hivi wakati mmoja kati yao akisimulia kituko fulani kabla ya wote kuangua kicheko kingine kikubwa sana na kuendelea na safari yao huku wakicheka na wengine wakikimbia. Na hapo sauti ya Tony ilimfikia wazi wazi kutokea kule kwenye baa, akicheka kwa sauti na baadhi ya watu wengine kule, kisha akawapazia sauti wale watu aliokuwa akicheka nao.
“Okay, see you tomorrow guys…mi’ naenda down town mara moja, you know what I’m sayin’!”
Jaka alimakinika pale alipojibanza.
Town saa hizi…?
Bila ya kufikiri zaidi, Jaka alipeleka mkono wake na kuvuta sehemu iliyofungua buti la lile gari na kule nyuma buti likafunguka. Alitambaa chini chini hadi nyuma ya lile gari na kuingiza mkono wake ndani ya buti kulizuia lisijifunge na kujibana, kisha akabaki akimchungulia Tony kupitia kwenye dirisha la nyuma la lile gari. Alimuona Tony akiwa amekaa kwenye kiti cha dereva huku akiwa anaongea na simu ya kiganjani. Kisha Tony aliweka simu yake pembeni na kuanza kutia gari moto. Jaka aliliinua lile buti na kujitumbukiza ndani na kabla hajajifungia kabisa ndani ya lile buti, alipachika tambara alilolikuta mle ndani kwenye loki ya buti ili lisijibane wakati yuko mle ndani akashindwa kutoka. Gari lilirudi nyuma na kugeuza kabla ya kuondoka kwa kasi kutoka eneo lile, yeye akiwa ni abiria asiyetakiwa ndani yake.
Safari haikuwa nzuri kwake, kwani alilazimika kujikunja mle ndani ya buti la gari huku akiwa amelalia ubavu, na akiwa ameukamatia kwa ndani ule mlango wa buti ili usiwe unajibamiza-bamiza naye akitupwatupwa kila gari lilipokuwa likizidi kukata mitaa kuelekea kusipojulikana. Kiasi cha kama dakika ishirini na tano baadaye Jaka aliinua taratibu mlango wa lile buti na kuchungulia. Walikuwa kwenye daraja la Salenda. Alishusha mlango ule taratibu na kujilaza tena ndani ya buti lile. Hakujua ni kitu gani kilichomfanya aamue kumfuatilia Tony kiasi cha kujikuta katika hali ile, lakini alijua kuwa kwa pale alipofikia, hakuweza kurudi nyuma tena.
Mwendo mfupi na kona kadhaa baadaye, alihisi lile gari likisimama na akasikia honi. Akajua wamefika walipokuwa wakielekea. Alisubiri kidogo kisha akainua mlango wa buti na kuchungulia. Hakuweza kuelewa pale walikuwa wapi. Aliona magari yakipita kwa mbali na alihisi kusikia harufu ya bahari, lakini hakuwa na uhakika. Gari lilianza kwenda tena kwa mwendo mdogo na Jaka alijifungia tena ndani ya buti. Mwendo mfupi baadaye gari lilisimama tena. Kwa mbali Jaka aliweza kusikia sauti za watu wakiongea, ikiwemo ya Tony, kisha gari likaondoka tena kwa mwendo wa kasi kidogo na baada ya mwendo mwingine mfupi na kona moja lilisimama na kuzimwa. Alisikia mlango wa gari lile ukifunguliwa na kufungwa. Aliendelea kutulia kwa kama dakika tano zaidi, kisha taratibu alilifungua lile buti na kuchungulia nje.
Mbele ya macho yake, kiasi cha kama mita hamsini hivi, aliona ukuta mrefu uliozungushiwa nyaya za misumari kwa juu. Eneo lote kutoka pale alipokuwa hadi pale kwenye ukuta, kulikuwa kuna majani yaliyokatwa vizuri na vichaka vidogo vya maua vilivyotapakaa hapa na pale katika eneo lile.
Alizungusha macho kulia kwake, ambako ndiko geti la kuingilia ndani ya eneo lile lilikuwapo na aliona njia safi ya lami iliyopinda na kupotelea kulia zaidi, hivyo kumfanya mtu aliyeko kule getini asiweze kuona yaliyokuwa yakitokea pale alipokuwapo.
Aligeuza macho yake kushoto. Kiasi cha hatua tano hivi kutoka pale lilipoegeshwa lile gari kulikuwa kuna gari jingine aina ya Land Rover Discovery. Mbele zaidi ndipo alipoliona lile jengo. Kwa pale alipokuwa, aliweza kuona sehemu ya juu tu ya lile jengo, ambayo ilimjulisha kuwa lilikuwa ni jengo la ghorofa moja. Kwa mbele zaidi kushoto mwisho wa ukuta ule, kulikuwa kuna taa kubwa iliyotoa mwanga mkali kutoka juu ya kona ya ukuta ule kuangaza jengo lile. Kulikuwa kuna taa nyingine kama ile kwenye kona nyingine ya ukuta ule iliyopo kulia kwake.
Kwa nini Tony aje kwenye jengo hili saa kama hizi?
Kwanza hili ni jengo gani…Ofisi...? Ofisi gani hii ya kutembelewa usiku?