IAmShedeOne
JF-Expert Member
- Jul 2, 2015
- 202
- 385
- Thread starter
- #21
RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA KUMI NA NNE
Alipofika usawa wa jengo la ofisi ndogo ya posta tawi la uwanja wa sabasaba, John Doe alitaka kukata kushoto ili apotelee kwenye uchochoro mwingine mdogo. Jaka alijua kuwa akifanikiwa tukuingia kwenye uchochoro ule hatoweza tena kumpata. Pia alihisi kuwa huenda John Doe akawa ana wenzake kule upande wa pili wa uchochoro ule ambao wangeweza kumdhuru.
Hakumpa nafasi hiyo.
Alijirusha mzima mzima na kumdaka kiunoni kwa mikono yake yote miwili. John Doe aliachia yowe la hamaniko huku akipepesukia mbele, na kwa sekunde kadhaa aliendelea kukimbia kwa kuyumba yumba huku akimburura Jaka nyuma yake.
Huku akigumia, Jaka alihisi mikono yake ikianza kuteleza. Akawa amemng’ang’ania koti yule jamaa huku miguu yake ikiendelea kubururwa kwenye ardhi ile iliyojaa kokoto. John Doe akazidi kupepesuka, kasi yake ikaanza kupungua, naye akijitahidi kujitikisa na kujikung’uta ili Jaka amwachie. Akafanikiwa kumchomoa mkono mmoja, na Jaka akabaki akiwa amemng’ang’ania kwa mkono mmoja huku akibururwa vibaya.
“Sim…ma…ma we…wweee!” Alikuwa akimshinikiza yule mtu mwenye koti refu huku akisota vibaya ardhini akiwa amemng’ang’ania kwa mkono mmoja ilhali kwa ule mwingine akijitahidi kujiinua bila ya kupunguza mwendo.
Ilikuwa ni tafrani ya aina yake.
Ghafla John Doe alimgeukia na kofi kali lililomkosa Jaka na kupitia inchi chache juu ya kichwa chake. Kitendo kile kilisababisha lile koti lichanike ule upande ambao Jaka alikuwa ameung’ang’ania kwa mkono wake wa kulia huku John Doe akizidi kukukuruka kwa nguvu ili ajinasue kutoka mikononi mwake. Jaka akamng’ang’ania mguu kwa nguvu na hapo wote wawili wakapiga mweleka mzito. Jaka hakuuachia ule mguu hata kidogo. Sasa John Doe alikuwa anagaragara pale chini huku akijaribu kuunasua mguu wake, wakati Jaka akizidi kuung’ang’ania huku akiutumia kama nyenzo ya kujivutia juu ili amlalie yule jamaa pale chini na kumdhibiti kikamilifu.
Katikati ya rabsha ile John Doe alimfyatulia teke kali sana la uso kwa mguu wake uliokuwa huru. Yowe la maumivu lilimtoka Jaka huku akisukumwa pembeni na mikono ikamlegea. John Doe akajichomoa na kumshindilia kwa soli ya kiatu chake kifuani akiwa bado amelala pale chini, na Jaka akagaragazwa hovyo pale chini huku akigumia kwa maumivu na hasira.
John Doe alikurupuka kutoka pale chini na kutaka kukimbia, lakini Jaka nae alikuwa ameshainuka na aliwahi kumdaka ukosi wa koti lake kwa nyuma kabla hajafika mbali.
“Tulia weweee! Unan’natakia nini mim...” Alianza kumfokea, lakini hapo John Doe alimgeukia kwa konde zito lilitua sawia kwenye “solar plexus”, sehemu nyeti sana iliyopo baina ya pale kifua kinapoishia na tumbo linapoanzia. Jaka alienda chini bila kupenda na kupiga goti moja ardhini huku akipatatapa kutafuta pumzi bila mafanikio. Lilikuwa ni konde zito sana lililomlegeza maungo yote na hakuelewa kwa nini pigo lile lilimfanya vile.
Kwa mbali aliweza kumsikia Clara akiita jina lake huku akikimbilia pale walipokuwa. Aliinua uso wake kumtazama yule jamaa, na kuona kuwa John Doe alikuwa amemsimamia katika ile “honor stance” ya kibondia, kama kwamba alikuwa akimsubiri ainuke ili waendelee na pambano iwapo Jaka angekuwa tayari kuendelea. Lakini ile ngumi ilikuwa kali sana na Jaka hakuwa na nguvu kabisa ya kujiinua kutoka pale chini. Alibaki akiwa amejikunja kwa maumivu huku akimtumbulia macho ya kukata tamaa yule jamaa.
“Wew…we nin…nah…nahh…nannii?” Alimbwabwajia kwa taabu yule mtu huku bado akiwa amejikunja pale chini.
“Jaka! Jak…Ni nini tena hiki lakini? Umekuwaje?” Sasa Clara aliwafikia pale walipokuwa na alikuwa akisaili kwa sauti iliyojaa hamaniko.
“Uh…usingekuja huku Clar…” Jaka aligumia kwa taabu, lakini Clara hakumtilia maanani.
“Who are you, mwanaharamu mkubwa wewe? Umemfanya nini huyu wewe, Eeenh?” Clara alimfokea yule jamaa kwa ukali huku akijitahidi kumuinua Jaka kutoka pale chini.
“No, Clara…ondoka ha…hapa! Ni hatari!” Jaka alijilazimisha kuongea huku akishindana na pumzi zilizoonekana kumbana kwa namna ya ajabu kutokana na pigo alilopokea.
John Doe alimtupia macho yule dada, kisha akamtazama Jaka aliyekuwa akihangaika kuinuka kutoka pale chini huku akisaidiwa na Clara, kisha bila ya kujibu akaruka nyuma hatua tatu, akageuka na kutokomea kichochoroni.
Clara akamtupia tusi la nguoni kwa hasira, kisha akamgeukia mpenziwe.
“Jaka! Jaka...vipi, uko salama...? Ni nani yule?” Alimuuliza huku akitweta.
“Yeah! Niko fiti....” Jaka alijibu kwa kujikakamua huku akiyumba. Mate yalimpalia na akakohoa kwanguvu sana, Clara akimpa pole kwa mashaka makubwa. Alitikisa kichwakwa nguvu kamamtu atakaye kuiweka akili yake sawa.
“Pole mpenzi…lakini…ilikuwaje kwani?”
“Ni John Doe yule!” Jaka alimjibukwa taabu huku wakiwa wameshikana mabega wakirudi kule ambako Clara alikuwa ameliacha gari lao, mbele ya jengo la TBC kanda ya kati.
“John Doe?”
“Yeah, ndiye yeye…mshenzi ana ngumi nzito sijapata kuona, bloody fool!”
Hakuwa na namna ya kujua kuwa yule mtu waliyempachika jina la John Doe alikuwa amempiga ile ngumi mahala pale makusudi, akijua kuwa ingemfanya ashindwe kabisa kumbughudhi. Ilikuwa ni ngumi iliyopigwa kwa uzito uliokusudiwa na ikatua mahala ilipokusudiwa.
Clara aliguna.
Hatua chache mbele yao Jaka aliiona kofia ya John Doe ikiwa imeanguka pale chini. Aliiokota na kuikumbatia kwapani kwake huku akiyumba kuelekea nje ya ule uwanja akisaidiwa na Clara.
Kwa nini umekimbia John Doe…?
Unataka nini kwangu wewe lakini…?
___________________
RPC Januari Mwakaja alishusha pumzi ndefu na kubaki akimtazama Jaka aliyekuwa ameketi kwenye kiti kilichokuwa upande wa pili wa meza yake pale ofisini huku akiigonga gonga meza ile taratibu kwa kalamu iliyokuwa mkononi mwake.
“I see...” Hatimaye alisema huku akiendelea kumtazama yule kijana, uso wake ukionesha kuwa bado alikuwa anajaribu kuyatafakari yale aliyokuwa ameambiwa na Jaka muda mfupi uliopita, kisha akaendelea, “...sasa wewe binafsi ulikuwa una mawazo gani hasa juu ya swala hili?”
Ikawa zamu ya Jaka kushusha pumzi ndefu kabla ya kuingea.
“Kitu ninachoomba kieleweke mzee ni kwamba, ingawa mimi nimeletwa hapa kama mhalifu niliyekuja kutumikia adhabu, bado kuna haki ninazopaswa nitendewe. Wakati nasomewa adhabu yangu sikusikia neno lolote kuhusu kuwekewa watu wa kufuatilia nyendo zangu kinyemela, halafu nikijaribu kuuliza kwa nini wananifuata wanipige...”
“Lakini mpaka sasa hakuna ushahidi wowote kuwa mtu huyo ametumwa na vyombo vya dola, kijana! Kama ingekuwa hivyo basi mimi ndiyo ningekuwa wa kwanza kujua...” January Mwakaja alimbishia.
“Sasa kama hivyo ndivyo, basi hiyo inathibitisha kauli yangu ya mwanzo kuwa maisha yangu yamo hatarini hapa Dodoma! Jambo lolote linaweza kunitokea hapa na wewe usiwe na habari mzee.” Jaka alizidi kuweka wazi mashaka yake.
Mzee Januari Mwakaja alimtazama kwa muda mrefu akiwa kimya. Hatimaye alimuuliza swali ambalo siku zote limekuwa likimsumbua kichwani mwake.
“Ni kweli uliua mtu huku ulipotoka?”
Ni swali ambalo Jaka hakulitegemea kabisa. Alipiga kimya kwa muda, akilini akitafakari iwapo lile swali halikuwa mtego.
“Unajua...kuna jaji mmoja huko Marekani aliwahi kusema kwamba, sisi sote tuko chini ya sheria, lakini sheria ni kile ambacho Jaji amesema kiwe...sasa kwa mtazamo huo mzee, iwapo bwana hakimu alisema kuwa mimi nastahili kifungo hiki kutokana na kuhusishwa na kifo cha mtu, kuna haja gani tena kutaka kujua iwapo ni kweli au si kweli niliua?” Hatimaye Jaka alimjibu kwa hisia kali.
Mzee Mwakaja alibaki akimtazama tu kwa muda.
“Oh! I see... Hivi ulifanya nini kule wewe...? Au uliona nini kule mpaka uwe mtu wa kufuatiliwa hivi?” Hatimaye alimuuliza kwa sauti yenye kukwaruza. Jaka aliachia tabasamu dogo la huzuni huku akiguna. Uso wake ulimbadilika na kuwa kama anayevuta kumbukumbu iliyomgusa sana, na ingawa alionekana kumuangalia yule mzee, hakika alikuwa hamuoni na badala yake alikuwa akiona mambo mbali mbali aliyokumbana nayo kabla ya kuletwa kwake pale Dodoma yakipita kwa kasi mno kichwani mwake.
“Ni mengi yametokea mzee...na mengi nimeyaona...tatizo ni kwamba waliotakiwa kuyasikia hawakutakana kufanya hivyo...”
Januari Mwakaja alizidi kumtazama. Tangu akutane na yule kijana, amekuwa akipata hisia kwamba kuna kitu hakikuwa sawa katika kuletwa kwake pale Dodoma. Aliwahi kuhisi kuwa pale alikuwa ameletwa ili apatwe na maafa ya kumtoa duniani, kwani kama ni kweli angekuwa amefanya kosa alilosemekana kuwa amelifanya, ile haikuwa hukumu sahihi.
“Unaweza kunieleza baadhi ya hayo uliyokutana nayo huko?”
Jaka alitikisa kichwa kwa masikitiko.
“Hapana mzee... ni hakika nimeona mengi sana, ila siwezi kukuelezea kwa sasa. Ni machungu sana...”
Mzee Mwakaja alimtazama kwa muda.
“Okay. Ila nina hakika kuwa katika hayo mengi uliyoona, kuna moja au mawili ambayo hukutakiwa kuyaona...” Hatimaye alihitimisha yule mzee.
Kimya kilipita kidogo, kisha Jaka akamuuliza yule mzee swali lililokuwa likimnanga kichwani mwake.
“Sasa baada ya kukuelezea mkasa ulionikuta jana usiku kutoka kwa huyu mtu mwenye koti refu na kofia pana...unaweza kunihakikishia vipi usalama wangu hapa mjini kwako?”
“Hilo swala niachie nilifanyie kazi kwanza kijana. Ninasikitika sana na yaliyokukuta hapa dodoma mpaka sasa ila elewa kuwa usalama wa raia wote wa hapa mjini uko chini yangu, hivyo na wewe pia uko katika himaya yangu. Nitalifanyia kazi kwa karibu sana hilo. Ila nawe saa upunguze kutembea tembea usiku na ujitahidi kuwa kwenye maeneo yenye majumuiko ya watu zaidi kuliko kuwa meneo pweke na peke yako...sawa?” Alimjibu.
Jaka aliafikiana naye kwa shingo upande, kisha akaaga na kuondoka.
Nyuma yake Mzee Januari Mwakaja aliinua mkono wa simu iliyokuwa pale mezani kwake na kumpigia mkuu wa polisi wa kanda maalum ya Dar es Salaam. Kuna mambo kadhaa ambayo alihitaji kufahamishwa.
Wakati ile simu ikiendelea kuita, Osman Mgunya aliingia mle ofisini nayeakairudisha ile simu mahala pake na kumtazama kwa macho ya kuuliza.
“Ulikuwa unahitaji kuniona afande ?” Osman aliuliza.
“Hapana...nikikuhitaji si nitakuita Osman?” Mwakaja alimjibu kwa mshangao.
“Ndio...nilikuwa nimetoka kidogo ofisini, na nilipokuwa narudi nikamuona Jaka akitoka ofisini kwako na simu ya ofisini kwangu ikawa inaita, lakini ilikatika kabla sijawahi kuipokea...hivyo nikadhani ni wewe ndiye uliyekuwa ukinipigia...” Mgunya amlijibu kwa kubabaika kidogo.
“Hapana, endelea na kazi zako.”
“Ndiyo Afande!” Osman alisaluti na kutoka.
Januari Mwakaja alikunja uso kwa mawazo huku akiendelea kukodolea macho pale mlangoni alipotokea Osman Mgunya sekunde kadhaa zilizopita.
Ni kweli alikuja kuulizia alichokuja kukiulizia pale ofisini, au alikuja kuhakikisha kitu...? Kwa nini ameamua kuja pale ofisini baada ya kumuona Jaka akitokea ofisini kwake?
Alikumbuka siku ile alipomkuta akimpiga Jaka kule ofisini kwake na akazidi kukunja uso kwa tafakuri. Alishusha pumzi taratibu, akainua tena mkono wa simu na kuanza kupiga namba za mkuu wa polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam.
__________________
Dakika arobaini baadaye, Mzee Mwakaja alibaki akiwa ameduwaa na simu yake sikioni hata baada ya mtu aliyekuwa akiongea naye kule Dar kukata simu yake. Akiwa bado ameduwa na simu yake sikioni, aliweza kusikia mtu wa upande wa pili wa simu ile akiweka simu yake chini. Alikuwa anataka kuirudisha simu yake chini aliposikia tena mlio wa simu nyingine ikiwekwa chini. Alikunja uso na kuitoa haraka simu ile sikioni mwake na kuitazama, kisha akaiweka tena sikioni.
Kimya.
Aliurudusha mkono wa simu ile mahala pake huku sura yake ikisajili mikunjo mingi kwa mawazo. Alikuwa na hakika kabisa kuwa alisikia simu ya pili ikiwekwa chini baada ya simu ya RPC wa Dar kuwekwa chini...
Januari Mwakaja alikuwa mzoefu sana katika kazi kipelelezi, na ingawa alijua kuwa muda wake wa kustaafu ulikuwa unakaribia, bado alikuwa na imani kubwa sana katika uwezo wake wa kazi.
Kwa hali hiyo, mara moja alijua kuwa kuna mtu mwingine, mtu wa tatu, aliyekuwa akisikiliza mazungumzo kati yake na Kamanda wa Polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam.
Kitu kingine alichojua ni kwamba ile simu ya tatu iliyotumika kusikiliza mazungumzo yale ilikuwa katika jengo lile lile ambamo ofisi yake ilikuwepo. Hiyo inamaanisha mtu aliyekuwa akisikiliza mazungumzo yale alikuwa ndani ya jengo lile lile alilokuwamo.
Ni nani?
Na kwa nini afanye vile?
Aliweza kujijibu swali la “nani” mara moja, au alidhani aliweza. Lakini swali la “kwa nini” bado lilihitaji uchunguzi wa kina.
Mawazo yake yalirudi kwenye maongezi yake na kamanda wa polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam, ambapo alitaka ajulishwe mambo fulani kuhusiana na swala zima la mhalifu Jaka Brown Madega...
Tangu awali kesi ya huyu mtu aitwaye Jaka imekuwa ikimuachia maswali mengi kichwani, na alishindwa kuielewa. Cha ajabu ni kwamba baada ya kuongea kwa zaidi ya dakika arobaini na yule mwenzake wa Dar es Salaam, amejikuta ndio ameongezewa maswali zaidi kuliko majibu kuhusiana na kesi ya Jaka na hivyo kuzidi kutoielewa.
Samson Ramadhani, kamanda wa polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam alimpa jibu ambalo hakulitegemea pale alipomuomba amtumie faili la kesi nambari 08/12582/94/800 inayomhusu mtu aitwaye Jaka Brown Madega.
“Faili hilo limetoweka katika mazingira ya kutatanisha kiasi cha miezi miwili iliyopita...”
Ndilo jibu lililomfanya abaki ameduwaa na simu sikioni...
_________________
Sehemu nyingine ya jengo lile lile, Osman Mgunya alirudisha taratibu mkono wa simu mahala pake baada ya kujihakikishia kuwa January Mwakaja na Kamanda wa kanda maalumu ya polisi ya mkoa wa Dar es Salaam, ambao yeye alikuwa akifuatilia mazungumzo yao ya simu bila ya wao kujua, walikuwa wameshaweka chini simu zao. Alibaki kimya kwa muda huku uso wake mbaya ukiwa umekunjamana kwa tafakuri.
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA KUMI NA NNE
Alipofika usawa wa jengo la ofisi ndogo ya posta tawi la uwanja wa sabasaba, John Doe alitaka kukata kushoto ili apotelee kwenye uchochoro mwingine mdogo. Jaka alijua kuwa akifanikiwa tukuingia kwenye uchochoro ule hatoweza tena kumpata. Pia alihisi kuwa huenda John Doe akawa ana wenzake kule upande wa pili wa uchochoro ule ambao wangeweza kumdhuru.
Hakumpa nafasi hiyo.
Alijirusha mzima mzima na kumdaka kiunoni kwa mikono yake yote miwili. John Doe aliachia yowe la hamaniko huku akipepesukia mbele, na kwa sekunde kadhaa aliendelea kukimbia kwa kuyumba yumba huku akimburura Jaka nyuma yake.
Huku akigumia, Jaka alihisi mikono yake ikianza kuteleza. Akawa amemng’ang’ania koti yule jamaa huku miguu yake ikiendelea kubururwa kwenye ardhi ile iliyojaa kokoto. John Doe akazidi kupepesuka, kasi yake ikaanza kupungua, naye akijitahidi kujitikisa na kujikung’uta ili Jaka amwachie. Akafanikiwa kumchomoa mkono mmoja, na Jaka akabaki akiwa amemng’ang’ania kwa mkono mmoja huku akibururwa vibaya.
“Sim…ma…ma we…wweee!” Alikuwa akimshinikiza yule mtu mwenye koti refu huku akisota vibaya ardhini akiwa amemng’ang’ania kwa mkono mmoja ilhali kwa ule mwingine akijitahidi kujiinua bila ya kupunguza mwendo.
Ilikuwa ni tafrani ya aina yake.
Ghafla John Doe alimgeukia na kofi kali lililomkosa Jaka na kupitia inchi chache juu ya kichwa chake. Kitendo kile kilisababisha lile koti lichanike ule upande ambao Jaka alikuwa ameung’ang’ania kwa mkono wake wa kulia huku John Doe akizidi kukukuruka kwa nguvu ili ajinasue kutoka mikononi mwake. Jaka akamng’ang’ania mguu kwa nguvu na hapo wote wawili wakapiga mweleka mzito. Jaka hakuuachia ule mguu hata kidogo. Sasa John Doe alikuwa anagaragara pale chini huku akijaribu kuunasua mguu wake, wakati Jaka akizidi kuung’ang’ania huku akiutumia kama nyenzo ya kujivutia juu ili amlalie yule jamaa pale chini na kumdhibiti kikamilifu.
Katikati ya rabsha ile John Doe alimfyatulia teke kali sana la uso kwa mguu wake uliokuwa huru. Yowe la maumivu lilimtoka Jaka huku akisukumwa pembeni na mikono ikamlegea. John Doe akajichomoa na kumshindilia kwa soli ya kiatu chake kifuani akiwa bado amelala pale chini, na Jaka akagaragazwa hovyo pale chini huku akigumia kwa maumivu na hasira.
John Doe alikurupuka kutoka pale chini na kutaka kukimbia, lakini Jaka nae alikuwa ameshainuka na aliwahi kumdaka ukosi wa koti lake kwa nyuma kabla hajafika mbali.
“Tulia weweee! Unan’natakia nini mim...” Alianza kumfokea, lakini hapo John Doe alimgeukia kwa konde zito lilitua sawia kwenye “solar plexus”, sehemu nyeti sana iliyopo baina ya pale kifua kinapoishia na tumbo linapoanzia. Jaka alienda chini bila kupenda na kupiga goti moja ardhini huku akipatatapa kutafuta pumzi bila mafanikio. Lilikuwa ni konde zito sana lililomlegeza maungo yote na hakuelewa kwa nini pigo lile lilimfanya vile.
Kwa mbali aliweza kumsikia Clara akiita jina lake huku akikimbilia pale walipokuwa. Aliinua uso wake kumtazama yule jamaa, na kuona kuwa John Doe alikuwa amemsimamia katika ile “honor stance” ya kibondia, kama kwamba alikuwa akimsubiri ainuke ili waendelee na pambano iwapo Jaka angekuwa tayari kuendelea. Lakini ile ngumi ilikuwa kali sana na Jaka hakuwa na nguvu kabisa ya kujiinua kutoka pale chini. Alibaki akiwa amejikunja kwa maumivu huku akimtumbulia macho ya kukata tamaa yule jamaa.
“Wew…we nin…nah…nahh…nannii?” Alimbwabwajia kwa taabu yule mtu huku bado akiwa amejikunja pale chini.
“Jaka! Jak…Ni nini tena hiki lakini? Umekuwaje?” Sasa Clara aliwafikia pale walipokuwa na alikuwa akisaili kwa sauti iliyojaa hamaniko.
“Uh…usingekuja huku Clar…” Jaka aligumia kwa taabu, lakini Clara hakumtilia maanani.
“Who are you, mwanaharamu mkubwa wewe? Umemfanya nini huyu wewe, Eeenh?” Clara alimfokea yule jamaa kwa ukali huku akijitahidi kumuinua Jaka kutoka pale chini.
“No, Clara…ondoka ha…hapa! Ni hatari!” Jaka alijilazimisha kuongea huku akishindana na pumzi zilizoonekana kumbana kwa namna ya ajabu kutokana na pigo alilopokea.
John Doe alimtupia macho yule dada, kisha akamtazama Jaka aliyekuwa akihangaika kuinuka kutoka pale chini huku akisaidiwa na Clara, kisha bila ya kujibu akaruka nyuma hatua tatu, akageuka na kutokomea kichochoroni.
Clara akamtupia tusi la nguoni kwa hasira, kisha akamgeukia mpenziwe.
“Jaka! Jaka...vipi, uko salama...? Ni nani yule?” Alimuuliza huku akitweta.
“Yeah! Niko fiti....” Jaka alijibu kwa kujikakamua huku akiyumba. Mate yalimpalia na akakohoa kwanguvu sana, Clara akimpa pole kwa mashaka makubwa. Alitikisa kichwakwa nguvu kamamtu atakaye kuiweka akili yake sawa.
“Pole mpenzi…lakini…ilikuwaje kwani?”
“Ni John Doe yule!” Jaka alimjibukwa taabu huku wakiwa wameshikana mabega wakirudi kule ambako Clara alikuwa ameliacha gari lao, mbele ya jengo la TBC kanda ya kati.
“John Doe?”
“Yeah, ndiye yeye…mshenzi ana ngumi nzito sijapata kuona, bloody fool!”
Hakuwa na namna ya kujua kuwa yule mtu waliyempachika jina la John Doe alikuwa amempiga ile ngumi mahala pale makusudi, akijua kuwa ingemfanya ashindwe kabisa kumbughudhi. Ilikuwa ni ngumi iliyopigwa kwa uzito uliokusudiwa na ikatua mahala ilipokusudiwa.
Clara aliguna.
Hatua chache mbele yao Jaka aliiona kofia ya John Doe ikiwa imeanguka pale chini. Aliiokota na kuikumbatia kwapani kwake huku akiyumba kuelekea nje ya ule uwanja akisaidiwa na Clara.
Kwa nini umekimbia John Doe…?
Unataka nini kwangu wewe lakini…?
___________________
RPC Januari Mwakaja alishusha pumzi ndefu na kubaki akimtazama Jaka aliyekuwa ameketi kwenye kiti kilichokuwa upande wa pili wa meza yake pale ofisini huku akiigonga gonga meza ile taratibu kwa kalamu iliyokuwa mkononi mwake.
“I see...” Hatimaye alisema huku akiendelea kumtazama yule kijana, uso wake ukionesha kuwa bado alikuwa anajaribu kuyatafakari yale aliyokuwa ameambiwa na Jaka muda mfupi uliopita, kisha akaendelea, “...sasa wewe binafsi ulikuwa una mawazo gani hasa juu ya swala hili?”
Ikawa zamu ya Jaka kushusha pumzi ndefu kabla ya kuingea.
“Kitu ninachoomba kieleweke mzee ni kwamba, ingawa mimi nimeletwa hapa kama mhalifu niliyekuja kutumikia adhabu, bado kuna haki ninazopaswa nitendewe. Wakati nasomewa adhabu yangu sikusikia neno lolote kuhusu kuwekewa watu wa kufuatilia nyendo zangu kinyemela, halafu nikijaribu kuuliza kwa nini wananifuata wanipige...”
“Lakini mpaka sasa hakuna ushahidi wowote kuwa mtu huyo ametumwa na vyombo vya dola, kijana! Kama ingekuwa hivyo basi mimi ndiyo ningekuwa wa kwanza kujua...” January Mwakaja alimbishia.
“Sasa kama hivyo ndivyo, basi hiyo inathibitisha kauli yangu ya mwanzo kuwa maisha yangu yamo hatarini hapa Dodoma! Jambo lolote linaweza kunitokea hapa na wewe usiwe na habari mzee.” Jaka alizidi kuweka wazi mashaka yake.
Mzee Januari Mwakaja alimtazama kwa muda mrefu akiwa kimya. Hatimaye alimuuliza swali ambalo siku zote limekuwa likimsumbua kichwani mwake.
“Ni kweli uliua mtu huku ulipotoka?”
Ni swali ambalo Jaka hakulitegemea kabisa. Alipiga kimya kwa muda, akilini akitafakari iwapo lile swali halikuwa mtego.
“Unajua...kuna jaji mmoja huko Marekani aliwahi kusema kwamba, sisi sote tuko chini ya sheria, lakini sheria ni kile ambacho Jaji amesema kiwe...sasa kwa mtazamo huo mzee, iwapo bwana hakimu alisema kuwa mimi nastahili kifungo hiki kutokana na kuhusishwa na kifo cha mtu, kuna haja gani tena kutaka kujua iwapo ni kweli au si kweli niliua?” Hatimaye Jaka alimjibu kwa hisia kali.
Mzee Mwakaja alibaki akimtazama tu kwa muda.
“Oh! I see... Hivi ulifanya nini kule wewe...? Au uliona nini kule mpaka uwe mtu wa kufuatiliwa hivi?” Hatimaye alimuuliza kwa sauti yenye kukwaruza. Jaka aliachia tabasamu dogo la huzuni huku akiguna. Uso wake ulimbadilika na kuwa kama anayevuta kumbukumbu iliyomgusa sana, na ingawa alionekana kumuangalia yule mzee, hakika alikuwa hamuoni na badala yake alikuwa akiona mambo mbali mbali aliyokumbana nayo kabla ya kuletwa kwake pale Dodoma yakipita kwa kasi mno kichwani mwake.
“Ni mengi yametokea mzee...na mengi nimeyaona...tatizo ni kwamba waliotakiwa kuyasikia hawakutakana kufanya hivyo...”
Januari Mwakaja alizidi kumtazama. Tangu akutane na yule kijana, amekuwa akipata hisia kwamba kuna kitu hakikuwa sawa katika kuletwa kwake pale Dodoma. Aliwahi kuhisi kuwa pale alikuwa ameletwa ili apatwe na maafa ya kumtoa duniani, kwani kama ni kweli angekuwa amefanya kosa alilosemekana kuwa amelifanya, ile haikuwa hukumu sahihi.
“Unaweza kunieleza baadhi ya hayo uliyokutana nayo huko?”
Jaka alitikisa kichwa kwa masikitiko.
“Hapana mzee... ni hakika nimeona mengi sana, ila siwezi kukuelezea kwa sasa. Ni machungu sana...”
Mzee Mwakaja alimtazama kwa muda.
“Okay. Ila nina hakika kuwa katika hayo mengi uliyoona, kuna moja au mawili ambayo hukutakiwa kuyaona...” Hatimaye alihitimisha yule mzee.
Kimya kilipita kidogo, kisha Jaka akamuuliza yule mzee swali lililokuwa likimnanga kichwani mwake.
“Sasa baada ya kukuelezea mkasa ulionikuta jana usiku kutoka kwa huyu mtu mwenye koti refu na kofia pana...unaweza kunihakikishia vipi usalama wangu hapa mjini kwako?”
“Hilo swala niachie nilifanyie kazi kwanza kijana. Ninasikitika sana na yaliyokukuta hapa dodoma mpaka sasa ila elewa kuwa usalama wa raia wote wa hapa mjini uko chini yangu, hivyo na wewe pia uko katika himaya yangu. Nitalifanyia kazi kwa karibu sana hilo. Ila nawe saa upunguze kutembea tembea usiku na ujitahidi kuwa kwenye maeneo yenye majumuiko ya watu zaidi kuliko kuwa meneo pweke na peke yako...sawa?” Alimjibu.
Jaka aliafikiana naye kwa shingo upande, kisha akaaga na kuondoka.
Nyuma yake Mzee Januari Mwakaja aliinua mkono wa simu iliyokuwa pale mezani kwake na kumpigia mkuu wa polisi wa kanda maalum ya Dar es Salaam. Kuna mambo kadhaa ambayo alihitaji kufahamishwa.
Wakati ile simu ikiendelea kuita, Osman Mgunya aliingia mle ofisini nayeakairudisha ile simu mahala pake na kumtazama kwa macho ya kuuliza.
“Ulikuwa unahitaji kuniona afande ?” Osman aliuliza.
“Hapana...nikikuhitaji si nitakuita Osman?” Mwakaja alimjibu kwa mshangao.
“Ndio...nilikuwa nimetoka kidogo ofisini, na nilipokuwa narudi nikamuona Jaka akitoka ofisini kwako na simu ya ofisini kwangu ikawa inaita, lakini ilikatika kabla sijawahi kuipokea...hivyo nikadhani ni wewe ndiye uliyekuwa ukinipigia...” Mgunya amlijibu kwa kubabaika kidogo.
“Hapana, endelea na kazi zako.”
“Ndiyo Afande!” Osman alisaluti na kutoka.
Januari Mwakaja alikunja uso kwa mawazo huku akiendelea kukodolea macho pale mlangoni alipotokea Osman Mgunya sekunde kadhaa zilizopita.
Ni kweli alikuja kuulizia alichokuja kukiulizia pale ofisini, au alikuja kuhakikisha kitu...? Kwa nini ameamua kuja pale ofisini baada ya kumuona Jaka akitokea ofisini kwake?
Alikumbuka siku ile alipomkuta akimpiga Jaka kule ofisini kwake na akazidi kukunja uso kwa tafakuri. Alishusha pumzi taratibu, akainua tena mkono wa simu na kuanza kupiga namba za mkuu wa polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam.
__________________
Dakika arobaini baadaye, Mzee Mwakaja alibaki akiwa ameduwaa na simu yake sikioni hata baada ya mtu aliyekuwa akiongea naye kule Dar kukata simu yake. Akiwa bado ameduwa na simu yake sikioni, aliweza kusikia mtu wa upande wa pili wa simu ile akiweka simu yake chini. Alikuwa anataka kuirudisha simu yake chini aliposikia tena mlio wa simu nyingine ikiwekwa chini. Alikunja uso na kuitoa haraka simu ile sikioni mwake na kuitazama, kisha akaiweka tena sikioni.
Kimya.
Aliurudusha mkono wa simu ile mahala pake huku sura yake ikisajili mikunjo mingi kwa mawazo. Alikuwa na hakika kabisa kuwa alisikia simu ya pili ikiwekwa chini baada ya simu ya RPC wa Dar kuwekwa chini...
Januari Mwakaja alikuwa mzoefu sana katika kazi kipelelezi, na ingawa alijua kuwa muda wake wa kustaafu ulikuwa unakaribia, bado alikuwa na imani kubwa sana katika uwezo wake wa kazi.
Kwa hali hiyo, mara moja alijua kuwa kuna mtu mwingine, mtu wa tatu, aliyekuwa akisikiliza mazungumzo kati yake na Kamanda wa Polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam.
Kitu kingine alichojua ni kwamba ile simu ya tatu iliyotumika kusikiliza mazungumzo yale ilikuwa katika jengo lile lile ambamo ofisi yake ilikuwepo. Hiyo inamaanisha mtu aliyekuwa akisikiliza mazungumzo yale alikuwa ndani ya jengo lile lile alilokuwamo.
Ni nani?
Na kwa nini afanye vile?
Aliweza kujijibu swali la “nani” mara moja, au alidhani aliweza. Lakini swali la “kwa nini” bado lilihitaji uchunguzi wa kina.
Mawazo yake yalirudi kwenye maongezi yake na kamanda wa polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam, ambapo alitaka ajulishwe mambo fulani kuhusiana na swala zima la mhalifu Jaka Brown Madega...
Tangu awali kesi ya huyu mtu aitwaye Jaka imekuwa ikimuachia maswali mengi kichwani, na alishindwa kuielewa. Cha ajabu ni kwamba baada ya kuongea kwa zaidi ya dakika arobaini na yule mwenzake wa Dar es Salaam, amejikuta ndio ameongezewa maswali zaidi kuliko majibu kuhusiana na kesi ya Jaka na hivyo kuzidi kutoielewa.
Samson Ramadhani, kamanda wa polisi wa kanda maalumu ya Dar es Salaam alimpa jibu ambalo hakulitegemea pale alipomuomba amtumie faili la kesi nambari 08/12582/94/800 inayomhusu mtu aitwaye Jaka Brown Madega.
“Faili hilo limetoweka katika mazingira ya kutatanisha kiasi cha miezi miwili iliyopita...”
Ndilo jibu lililomfanya abaki ameduwaa na simu sikioni...
_________________
Sehemu nyingine ya jengo lile lile, Osman Mgunya alirudisha taratibu mkono wa simu mahala pake baada ya kujihakikishia kuwa January Mwakaja na Kamanda wa kanda maalumu ya polisi ya mkoa wa Dar es Salaam, ambao yeye alikuwa akifuatilia mazungumzo yao ya simu bila ya wao kujua, walikuwa wameshaweka chini simu zao. Alibaki kimya kwa muda huku uso wake mbaya ukiwa umekunjamana kwa tafakuri.