RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA ARUBAINI NA SITA
“Nimekuelewa sana mzee na wala sikulaumu kwa uamuzi wako…mimi nitaondoka leo hii hii hapa nyumbani, lakini naomba sana uendelee kumshawishi Clara ahamie kule kwako kwa usalama zaidi. Wema ambao wewe na yeye mmenifanyia ni mkubwa sana na mimi sina haki kabisa ya kutaka chochote zaidi kutoka kwenu…” Alimwambia.
“Hapana Jaka…” Mzee Zaza alimjibu, “…mimi namjua sana mwanangu. Akiamua jambo huwa haamui kipumbavu, huwa amelifikiria…na akishaamua, ni vigumu sana kumshawishi vinginevyo...ni tabia aliyoirithi kutoka kwa mama yake…marehemu mke wangu.” Alivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu. Jaka alitaka kusema kitu lakini mzee Zaza akamuashiria anyamaze.
“Mama yake Clara alijua kuwa iwapo atapata ujauzito na kujifungua, basi maisha yake yangekuwa hatarini na angeweza kupoteza maisha kutokana na afya yake kuwa dhaifu. Lakini alipopata ujauzito alikataa katakata ushauri wa daktari kuwa ile mimba itolewe ili aokoe maisha yake…kwa sababu alikuwa anataka sana kupata mtoto. Na kweli…baada ya kuzaliwa Clara mke wangu mpenzi akaaga dunia…na tangu siku hiyo Clara amekuwa ndiye amekuwa familia yangu…” Aliongea yule mzee kwa huzuni, na Jaka alibaki akimtazama yule mzee tajiri bila ya kujua aseme nini.
“Wacha nikaongee naye tena.” Yule mzee alisema huku akielekea chumbani kwa Clara.
Nusu saa baadaye, mzee Wilfred Mashauri Zaza alirejea pale sebuleni na kusimama kwa muda mrefu kabla ya kuanza kuongea.
“Najua kuwa binti yangu anakupenda sana Jaka, lakini sijui kama amefanya uamuzi wa busara au wa kipuuzi kwa kukupenda. Ninachojua ni kuwa hivyo ndivyo mapenzi yalivyo. Wakati mimi naanza mapenzi na marehemu mama yake, sikuwa tofauti sana na wewe…kwamba Joanna, mama yake Clara alikuwa tajiri sana wakati mimi nilikuwa mfanyabiashara wa kawaida tu, sikuwa na ndugu wala jamaa na sikuwa tajiri kama yeye. Lakini Joanna hakufanya jambo la kipuuzi alipoamua kupendana nami…mimi sikuwa na nia mbaya juu yake.”
Jaka alitulia kimya akimsikiliza.
“Nadhani usalama wa mwanangu unategemea sana na nia yako kwake, Jaka. Kwa sababu yule ni msichana tu aliyetokea kukupenda, I can understand that …sasa wewe ukija kumfanya yeye bwege kwa hilo sitakuelewa kabisa. Usije ukamfanya ajutie uamuzi wake Jaka. Kwa sababu ukimfikisha katika hatua hiyo hutakuwa umemuumiza yeye tu bali na mimi vilevile…”
Jaka aliendelea kumsikiliza kwa makini huku yale maneno yakimwingia vizuri mno.
“Clara ameamua kuendelea kukaa na wewe hapa hapa…hivyo ndivyo mwanangu anavyokupenda Jaka. Yuko tayari kuhatarisha maisha yake kwa ajili yako…sio jambo la mchezo hata kidogo hilo. Mimi nimemkubalia kwa sharti kwamba nitaweka askari wa kuhakikisha usalama hapa nyumbani saa ishirini na nne…na kila atakapokwenda, atasindikizwa na askari. Namna hiyo nadhani kidogo kutakuwa kuna amani japo kidogo, moyoni mwangu.”
“Nashukuru mzee…na sitamfanya ajute hata kidogo.” Jaka alisema, na yule mzee alimtikisia kichwa tu kuafikiana naye, kisha akaiendea simu na kuanza kufanya taratibu za ulinzi kwa kuwasiliana na mkuu wa polisi wa mkoa. Baada ya kufanya hivyo walikaa kimya pale sebuleni hadi dakika ishirini baadaye wakati askari wawili waliporipoti kuanza kazi ya kulinda usalama wa nyumba ya Clara pale Uhindini. Hapo Mzee Zaza alienda chumbani kuagana na mwanaye, kisha akarudi pale sebuleni na kuagana na Jaka.
“Zingatia maneno niliyokueleza kuhusu binti yangu kijana.” Mzee alimwambia.
“Bila shaka mzee…” Jaka alijibu.
Yule mzee akaondoka, akimuacha akiwa amekaa peke yake pale sebuleni.
_____________________
Sasa Jaka aliinuka kutoka pale kwenye kochi na kuchungulia dirishani. Askari mmoja alikuwa amesimama mbele ya nyumba ile. Bastola moja ilikuwa imening’inizwa kiunoni kwake na radio ya mawasiliano ya kipolisi ilionekana kuchungulia kutoka kwenye mfuko wa shati lake. Begani alikuwa amening’iniza bunduki aina ya SMG. Alienda kuchungulia dirisha la nyuma. Nako kulikuwa na hali kama ile ya kule mbele. Alirudi sebuleni na kurudia kujiinamia pale kwenye kochi, bado mawazo mazito yalikitawala kichwa chake.
Ina maana hawa jamaa wamenifuata mpaka huku Dodoma? Kule Dar wamenikosakosa mara mbili bloody fools…kule njia ya Segerea na pale darajani Manzese…sasa hii hali itakuwa hivi mpaka lini?
Alisonya.
Mwishowe wataniua kweli hawa, yaani walikuwa tayari hata kumuua na Clara ambaye hana makosa yoyote? Aaah mi’ naona sasa wakati wa wao kulipa kwa matendo yao umefika…na watajuta! Hivi lini John Doe atatokea? Nina hakika jamaa atakuwa na msaada fulani kwangu, kinyume na nilivyomdhania hapo mwanzo.
Muda huo Clara aliingia pale sebuleni kutokea chumbani kwake na kwenda kuketi naye kimya pale kochini. Jaka alimtazama na kukumbuka maneno ya mzee Wilfred Mashauri Zaza. Moyo wake wote ukamuendea yule binti na alijihisi kumpenda zaidi na zaid. Kitendo cha kuamua kuendelea kuwa naye hata katika kipindi kile kigumu na cha hatari kabisa kilimtia moyo sana Jaka. Alikumbuka jinsi Moze, mpenzi wake wa awali na aliyewahi kumpenda kwa moyo wake wote, alivyomkana na kumuacha katika kipindi ambacho ndio alikuwa akimhitaji sana kutokana na matatizo makubwa aliyokuwamo wakati huo…matatizo yaliyomkuta kutokana na kulitetea penzi lao wenyewe.
Sasa leo huyu binti aliyekaa pembeni yake amekuwa radhi kujitolea maisha yake kuliko kumuacha peke yake katika dimbwi la madhila yale yasiyosemeka…
Alibaki akimtazama tu yule binti kwa upendo uliojaa shukurani.
Clara alimgeukia na wakatazamana. Macho yao yaliongea na kuelewana vizuri sana. Walikumbatiana kwa upendo, na kubaki wakiwa wamekumbatiana pale kwenye kochi kwa muda mrefu.
“Asante sana Clara.” Hatimaye Jaka aliongea.
“Kwa nini…?”
“Kwa kutoniacha peke yangu katika matatizo haya…”
Clara aliinua kichwa chake na kumtazama usoni.
“Kwani kama ungekuwa wewe ungeniacha?”
“Hapana…hata kidogo.”
“Sasa kwa nini unadhani mi’ ningeweza hata kufikiria kukuacha?” Clara alimuuliza, na kuendelea, “Matatizo hayana mwenyewe Jaka, yanaweza kumpata mtu yeyote…na umuhimu wa rafiki…wa mpenzi…unaonekana zaidi pale ambapo mtu uko kwenye matatizo. Mi’ n’takuwa mpenzi wa aina gani kama nitakuacha mpenzi wangu katika kipindi kama hiki Jaka? Halafu matatizo yakiisha nitafanyaje..nitarudi tena kukwambia ‘haya mpenzi sasa tuanze kupendana tena’? Haiwezekani.”
Jaka aliafikiana naye kutikisa kichwa taratibu, akilini akijiuliza ilikuwaje hata Moze akashindwa kuelewa jambo kama lile. Waliendelea kukaa kimya huku wakiwa wamekumbatiana kwa muda mrefu zaidi.
“Ni mambo gani yaliyokutokea huko nyuma hata ukalazimika kuja kizuizini huku Dodoma, Jaka?” Hatimaye Clara alimuuliza.
“Mengi sana Clara…”
“Naomba leo unielezee juu ya mambo hayo mpenzi…ni nini kilitokea mpaka tukakutana siku ile ya mvua kubwa na kiza kizito kule Dar es Salaam, na pia ilikuwaje hata tukaja kukutana tena hapa Dodoma…na mara zote hizo tumekuwa tukikutana katika mazingira ya kutatanisha. Ni wazi kuwa tukio la leo linatokana na mambo yaliyokutokea huko nyuma…”
Jaka alitulia kimya kwa muda kabla ya kumjibu.
“Clara, mi’ naona ni salama zaidi kwako kutoyajua mambo yaliyotokea huko nyuma kuliko kuyajua…”
Clara alijiinua taratibu kutoka kifuani kwake na kuketi huku akimtazama usoni.
“Jaka, tangu tuanze kujuana kwa ukaribu, sijawahi hata siku moja kukuuliza kuhusu maisha yako ya huko nyuma, hasa kuhusiana na mambo yanayohusiana na matatizo haya uliyonayo. Ni kwa sababu nilijua kuwa yaliyotokea huko nyuma hayakunihusu, nami nikaamua kujihusisha na maisha yako niliyokukuta nayo na kuendelea mbele huku nikiamini kabisa kuwa wewe hukufanya hilo kosa linalosemekana kuwa umelifanya hadi ukapewa adhabu ya kufukuzwa jiji la Dar…”
“Clara…”
“Subiri nimalize…mi’ nilishawahi kukueleza kuwa huwezi kuukimbia ukweli Jaka, kwani kuukimbia ukweli ni sawa na kujikimbia mwenyewe. Sasa ukweli umeshadhihirika mpenzi wangu…nao ni kuwa kuazia sasa hauko peke yako kwenye jambo hili…tuko pamoja. Mimi na wewe. Na kama tuko pamoja, basi sasa na mimi nastahili kabisa kuelewa juu ya jambo ambalo saa kadhaa tu zilizopita lingesababisha wewe na mimi tuwe marehemu, kwa sababu lile bomu lisingechagua Jaka..tungekufa sote!”
Duh!
“Dah! Ni kweli Clara, lakini…”
“Lakini nini Jaka? We’ kama unaona kuwa hayo matatizo ni yako peke yako basi hali hiyo ilibadilishwa na ule mlipuko wa bomu asubuhi ya leo. Ule mlipuko umenipa haki ya kujua kila kitu kuhusu yaliyokutokea kule Dar, Jaka. Sasa matatizo haya ni yetu sote, na tunatakiwa tushirikiane katika kukabiliana nayo…na njia nzuri ya kufanya hivyo ni kuanza kueleweshana hali halisi ilivyokuwa tangu mwanzo hadi hapa tulipo…halafu tuone tutaenda vipi huko mbele katika kukabiliana na hali hii.” Clara alimwambia kwa msisitizo.
Jaka hakuwa na hoja tena.
Akamueleza kisa chote cha maisha yake tangu mwanzo. Alimueleza kuhusu Moze, Joakim Mwaga na wenzake na mambo yote yaliyotokea hadi kuuawa kwa Joakim na yeye kutuhumiwa na hatimaye kuhukumiwa kwa mauaji yale. Alimalizia kwa kuelezea matukio yaliyotokea siku ile ambayo usiku wake ndio walikuja kukutana kwa mara ya kwanza kule Dar katika usiku ule wa mvua kubwa na kiza kinene…
_____________________
Clara alibaki mdomo wazi huku akimkodolea macho kwa huruma na mshangao.
“Aisee! Pole sana…dear…yaani, Ah! Hayo mambo huwa nayaona kwenye sinema tu, sikutegemea kabisa kuwa yanaweza kumtokea mtu kikweli kweli, na mtu mwenyewe awe ndiyo wewe…!”
“Yametokea dear…na yamenitokea mimi…nadhani sasa unaelewa ni kwa nini hao watu wataka kuniua.”
“Naelewa sasa…naelewa kabisa!”
Jaka alishusha pumzi ndefu na kutazama pembeni. Walibaki kimya kwa muda, kisha Clara aliuliza, “Kwa hiyo mtu aliyemuua Joakim hajajulikana mpaka sasa…?”
“Sijui kwa kweli…kwa sababu mtu pekee ambaye ningeweza kumhisi ni Tony, lakini Tony na Joakim walikuwa marafiki…” Jaka alijibu kwa mashaka.
Bado Clara alionekana kulitafakari kwa makini lile swala.
“Sasa…na zile glovu zilifikaje chumbani kwako…yaani inawezekanaje mtu aingie chumbani kwako na kupandikiza kitu kama kile bila ya wewe kujua?” Clara aliuliza kwa wasiwasi.
“Mmnh, Clara…! Hapo ndipo panaponishinda…kwa vyovyote vile yeyote aliyeingia na kupandikiza zile glovu chumbani kwangu siku ile, alifanya hivyo katika muda ule ambao mimi nilikuwa kule juu ya jengo nilipomkuta Joakim akiwa tayari ameuawa.” Jaka alijibu huku uso wake akiwa ameukunja kwa kutafakari.
“Kwani ulipotoka hukufunga mlango?”
“Mnh! Sikumbuki sawa sawa…”
“Mnh, Jaka! hebu rudia tena kunielezea kuanzia pale ulipoanza kujirekodi…” Clara alimwambia huku akijiweka vizuri pale kwenye kochi, uso wake ukionesha bashasha ya hali ya juu. Jaka alimtazama kwa mshangao kwani hakuelewa ingesaidia nini au Clara alikuwa na mawazo gani. Hata hivyo, alifanya kama alivyoombwa na kurudia kumuelezea ile sehemu.
Alipomaliza, Clara alibaki akiwa amekunja uso kwa mawazo huku akiangalia upande ule aliokuwapo Jaka ingawa Jaka aliona kabisa kuwa alikuwa hamuoni. Akili yake ilikuwa inafanya kazi kupita uwezo wake, na Jaka alizidi kushangaa ni nini kilikuwa kinapita kichwani mwa yule binti wakati ule.