RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA ARUBAINI NA NANE
Mzee Januari Mwakaja alitulia huku akiendelea kuendesha, kisha akajaribu kutia jeuri huku akiongeza mwendo wa gari.
“Nadhani unaelewa kuwa ukiitumia hiyo silaha sasa hivi sote tutakufa, kwa sababu gari litapinduka na hutakuwa na uhakika kama wewe utatoka salama…” Alimwambia.
“Unataka tujaribu?” Ile sauti ilimuuliza, na Mzee Mwakaja akajua kuwa hakuwa na ujanja. Alibaki kimya huku akijaribu kumtazama yule mtu kwa kutumia kioo cha kutazamia magari yatokayo nyuma kilichokuwa mbele yake mle garini. Hakuweza kumuona vizuri kutokana na kiza, lakini aliweza kuona kofia pana iliyofunika sehemu kubwa ya uso wa yule mtu. Hapo hapo alikumbuka maelezo ya Jaka juu ya mtu aliyekuwa akimfuata fuata anayevaa koti refu na kofia ya pama.
Ndiye huyu…?
“Unataka nini?” Hatimaye alirudia swali lake la kwanza.
“Endelea kuendesha!”
Mzee Mwakaja alitii amri ile. Baada ya mwendo fulani, ile sauti ilimwamuru aegeshe gari kando ya barabara na atulize mikono yake kwenye usukani. Januari Mwakaja akatii amri ile huku akibaini kuwa yule mtu alimwamuru asimamishe gari sehemu ambayo ilikuwa mbali sana na nyuma za raia.
“Maongezi ninayotaka kuongea nawe ni ya siri sana ndio maana imenibidi nitumie njia hii ya kijasusi, bila shaka utaelewa.” Ile sauti ilimwambia kutokea kule nyuma huku muongeaji akimkabidhi kitambulisho kutokea kule nyuma. Mzee Mwakaja alikipokea na kuwasha taa ya ndani ya gari kukiangalia. Haikuwa mara yake ya kwanza kuona kitambulisho cha aina ile. Kilikuwa ni kitambulisho cha afisa wa usalama wa taifa.
“Sawa bwana Jeff Bijhajha…nimekiona kitambulisho chako, lakini sijui kuwa sura iliyoko huko nyuma ndiyo haswa ya huyu mtu anayeonekana kwenye hiki kitambulisho.” Alisema huku akirudisha kile kitambulisho bila ya kugeuka nyuma.
“Unaweza kugeuka nyuma taratibu sana kuniangalia.” Jamaa alimwambia huku akikipokea kile kitambulisho chake. Januari Mwakaja aligeuka na kumtazama. Walitazamana. Hakuwa amepata kumuona kabla ya wakati ule, lakini sura iliyokuwa kwenye kitambulisho kile ilikuwa ndiyo haswa aliyokuwa akitazamana nayo wakati ule.
“Umeridhika?” Jeff Bijhajha aliuliza, na mzee Mwakaja aliafiki kwa kichwa.
“Nadhani sasa unaweza kuzima taa ya gari ili tuongee.”
Mzee Mwakaja alizima taa ya ndani ya gari na yule afisa wa usalama wa taifa alianza kueleza.
“Sasa hivi kumetokea wimbi kubwa la biashara ya madawa ya kulevya hapa nchini, na katika miaka miwili iliyopita serikali, ikivitumia vyombo vyake vya dola, imekuwa ikijitahidi bila ya mafanikio kukabiliana na wimbi hili…
“…tatizo kubwa limekuwa kwamba pamoja na kuwa inajulikana wazi kuwa biashara hiyo inafanyika humu nchini, kiini cha bidhaa hiyo haramu kimeendelea kuwa kitendawili…swala la nani hasa anayehusika na kuyaingiza hapa nchini na kwa kutumia njia gani ndilo limekuwa gumu mno kwa serikali na idara zake zote za kudhibiti madawa ya kulevya.”
“Ah, Lakini mbona kuna watu, hasa vijana, wengi tu wanaokamatwa na madawa hayo kila kukicha? Ina maana imeshindikana kuwabana wote hao hata wakataja ni wapi wanapata bidhaa hiyo?” Mzee Mwakaja alidakia.
“Hao unaowasema wewe ni wale wasambazaji wadogo wadogo tu ambao hawakuwa na msaada wowote wa maana mpaka sasa. Wengi wao wamekuwa wakitoa mtiririko wa habari zilizoishia hewani tu, hazifikii hasa pale kwenye shina kuu la biashara hii nchini…yaani hizi mbinu za kuendesha biashara hii ni za uficho sana kiasi kwamba ni vigumu kuwatia mkononi wale mapapa na manyangumi wa biashara hii. Tunaishia kukamata vijidagaa tu…wale watekelezaji wa mwisho kabisa ambao huwa hata hawaelewi hao mabosi wa biashara hii ni akina nani hasa…it’s very complicated…”
“Yote nayajua hayo…inahusu nini kuniinyatia garini mwangu usiku wote huu na kunieleza hayo?” Januari Mwakaja alitia hoja.
“Isitoshe, wengi wa hao wanaokamatwa ni watumiaji wadogo wadogo tu ambao huwa hawajali ni nani anayewaletea bidhaa hiyo, wanachojali wao ni kupata tu hiyo bidhaa, basi...” Jamaa aliendelea kama kwamba hakulisikia swali la yule mkuu wa polisi wa mkoa, na akaendelea, “…na wengine ni wale wanaokuja na bidhaa hiyo moja kwa moja kutoka nje ya nchi, kama vile Pakistan, Uturuki na nchi za Afrika ya Kusini na magharibi, wale wanaomeza paketi za unga huo na kukamatwa hapa uwanja wa ndege. Hawa mara nyingi huzitaja nchi walizotoka na unga huo kuwa ndio chanzo cha biashara hiyo. Wote hawa hawakuwa na msaada wa maana katika kuwafikia yale manyangumi ya biashara hii humu nchini.”
“Nimekuelewa. Lakini bado hujanielewesha ni jinsi gani swala lote hilo linahusika na mkoa wangu hadi ifikie hatua ya sisi kuongea katika mazingira kama haya.”
“Swali zuri…hapa ndipo utakapoelewa ni jinsi gani wewe unaingia…” Jeff Bijhajha alimjibu kisha akavuta pumzi na kutulia kidogo kabla ya kuendelea, “Kiasi cha kama mwaka mmoja uliopita, ujumbe maalum kutoka kikosi cha kupambana na madawa ya kulevya cha marekani, kijulikanacho kama D.E.A…”
“Drug Enforcement Agency…” Januari Mwakaja alidakia.
“Yeah…Drug Enforcement Agency…ujumbe kutoka D.E.A. ukiongozwa na balozi wa Marekani hapa nchini ulimtembelea Rais Ikulu na kumkabidhi ripoti kuhusu biashara ya madawa ya kulevya hapa nchini. Ripoti hiyo ilionesha kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kushiriki kwa viongozi wa ngazi za juu aidha serikalini au ndani ya jeshi la polisi katika uendeshaji wa biashara haramu ya madawa ya kulevya hapa nchini. Ingawa taarifa hii ilikuwa ngumu kukubalika mara moja, lakini ilileta maana kutokana na ukweli kwamba jitihada zote za serikali za kupambana na biashara hii zimekuwa zikigonga mwamba, na mara nyingi ilionekana kama kwamba hao wanaoendesha biashara hii, walikuwa wanapata taarifa zote za nini serikali ilikuwa inapanga na hivyo kuwawia rahisi kwao kukwepa mitego ya serikali.”
Mzee Januari Mwakaja alikaa vizuri huku akisikiliza kwa makini maelezo yale. Ile sauti nzito iliendelea kueleza kwenye kiza cha mle garini.
“Ni kutokana na ripoti hii ndipo rais alipounda tume maalum kuchunguza undani wa swala hili. Hii ni tume ya siri sana kiasi kwamba hata watu wa ngazi za juu kabisa serikalini hawajui juu ya uwepo wake. Mimi ni mmoja kati ya watendaji wa tume hii, na mpaka sasa tuna orodha ya baadhi ya askari wakubwa wanaoshukiwa kujihusisha na biashara hiyo, ingawa bado hatujafanikiwa kukitambua kiini cha uendeshaji wa biashara hiyo hapa nchini mpaka sasa.”
“Sasa bwana mdogo mbona unaniambia yote haya?” Januari alidakia tena.
“Hewaa! Nakueleza haya kwa sababu tume imenielekeza nije nikueleze habari hii, na nimetakiwa nikueleze habari hii ili uone umuhimu wa kunipa ushirikiano kwenye jambo lililonileta hapa Dodoma…”
“Mnh, okay. Ni jambo gani hasa lililokuleta hapa Dodoma bwana Bijhajha?” Januari Mwakaja aliuliza huku akiwa makini sana .
“Kijana aitwaye Jaka Brown Madega.”
“Whaat? Jaka…! Jaka si mhalifu aliyeletwa hapa kutumikia kifungo cha nje kwa kosa la mauaji!” Januari Mwakaja aliuliza kwa mshangao.
“Inaweza ikawa kweli amefanya hayo makosa…lakini pia inawezekana ikawa amepakaziwa tu kwa sababu ya kulinda maslahi ya watu fulani…” Jeff alimjibu.
“Kwa hiyo…?”
“Bila kutafuna maneno mzee kuna kila sababu za kuamini kuwa Jaka anaweza kuwa na taarifa nyeti zinazoweza kutusaidia kwenye kulifikia shina la biashara hii haramu hapa nchini.”
Mzee Januari Mwakaja aliduwaa.
“Kwa hiyo…?” Aliuliza tena, akili ikimzunguka, kile alichokuwa kikihisi kuhusu Jaka kikijidhihirisha katika zile taarifa alizokuwa anapokea wakati ule.
“Nimepewa kibali maalum cha kumtumia Jaka Brown Madega kwa namna yoyote ile nitakayoona inafaa katika kutekeleza uchunguzi wa tume niliyokuelezea,ili kuhakikisha kuwa tume inatimiza kazi iliyotumwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano.” Bijhajha alimalizia na kutulia.
Kwa mara nyingine Januari Mwakaja alilazimika kuwasha taa ya ndani ya gari ile na kusoma karatasi aliyokabidhiwa na yule mtu ambaye kitambulisho chake cha kazi kilimtambulisha kama Jeff Bijhajha. Ile karatasi ilikuwa inatoa kibali kwa Jeff Bijhajha kumtumia Jaka Brown Madega katika kutekeleza majukumu aliyokabidhiwa na tume ya siri ya kuchunguza uhusikaji wa maafisa wa polisi na viongozi wa juu serikalini katika uendeshaji wa biashara ya madawa ya kulevya nchini.
Kile kibali kilikuwa kina nembo ya rais na kusainiwa na waziri wa mambo ya ndani kwa niaba ya rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania.
Januari Mwakaja alijikuta akipiga mbinja kwa mshangao na kustajaabia jambo lile.
“ Dduh! Imetoka moja kwa moja Ikulu hii!” Alisema kwa mastaajabu.
Jeff Bijhajha hakujibu. Aliichukua ile karatasi na kuihifadhi kwenye mfuko wa ndani wa koti lake refu.
“Kwa hiyo unadhani kuwa Jaka anaweza kuwa na msaada kwako?”
“Tukio la leo asubuhi pale sokoni linazidi kunihakikishia hivyo.”
“Kwa hiyo, wewe ndiye uliyekuwa ukimfuatilia nyendo zake yule kijana?” Mwakaja aliuliza, na kabla Bijhajha hajajibu, akaendelea, “Sasa kwa nini ulimtwanga mangumi kule uwanja wa sabasaba siku kadhaa huko nyuma?”
Badala ya kumjibu, Jeff akacheka kidogo, kasha akwamwambia, “Tuachane na hayo. Nadhani sasa umeshaelewa kuwa siko hapa kwa ubaya dhidi yake. Sasa, Mi’ nitahitaji kwenda Dar kwa siku mbili kabla ya kuja kuongea rasmi na Jaka. Katika siku mbili hizo, nakuomba sana mzee uhakikishe kuwa Jaka anaendelea kuishi hadi hapo nitakaporudi. Baada ya hapo atakuwa chini yangu.”
Alifungua mlango, akateremka na kuanza kutokomea kizani.
“ Hey! Jeff!” Januari Mwakaja alimwita, na Jeff akarudi na kuchungulia dirishani.
“Unasemaje?”
“Sasa tutaonana vipi tena? Huu utaratibu wa leo si mzuri bwana…”
“Nikikuhitaji nitakupata tu mzee…si unaona nilivyokupata leo?”
“Hii sio namna nzuri ya kukutana…”
“Lakini ndio salama zaidi…”
Akatoweka.
Januari Mwakaja alitia gari moto na kuondoka eneo lile huku akiwa na mawazo tele kichwani.
Siku iliyofuata, Clara alisafiri “kikazi” kuelekea Dar es Salaam kwa gari la kampuni. Dereva aliyekuwa akimuendesha na wafanyakazi wengine wote pale ofisini kwao, walijua kuwa ile ilikuwa ni moja kati ya safari zake nyingi za kikazi kuelekea Dar es Saalaam. Kama jinsi ambavyo wale askari waliowekewa kuwalinda pale nyumbani kwao walivyoelewa.
Ni wao pekee ndio walioijua dhima ya safari ile.
___________________
Akiwa ofisini kwake siku ile Jaka alikuwa akifanya kazi huku akili yake ikiwa kwa Clara tu aliyekuwa safarini wakati ule. Alikuwa na wahka mkubwa wa kujua iwapo atafanikiwa kuipata ile simu yake na iwapo ile simu itakuwa na ufumbuzi walioutarajia. Mawazo haya yalikuwa yakimjia na kuondoka huku akijitahidi kufanya zile kazi kadiri alivyoweza.
Hatimaye akili yake ikazama moja kwa moja kwenye zile kazi na kusahau kuhusu safari ya Clara kwa muda. Mlango wa ofisini kwake ulifunguliwa taratibu na kufungwa tena, naye akiwa na uhakika kuwa aliyefungua mlango ule alikuwa ni mhudumu wa ofisi akileta barua za kikazi au vocha za malipo ya madereva wa ile kampuni ya usafirishaji, aliendelea kushughulika na kazi zake kwa muda kabla hajainua uso wake kumsikiliza.
La Haula!
Moyo ulimlipuka na hapo hapo ukaanza kumwenda mbio huku akili ikikataa kabisa kuamini alichokuwa akikiona mbele ya uso wake.
Mbele yake mle ndani walikuwa wamesimama watu wawili ambao aliamini kuwa hatowaona tena maishani mwake.
Don Sibazosi, ambaye yeye alimtambua kama “mzee wa matabasamu”, alikuwa amesimama katikati ya ofisi ile hali akiwa amemuelekezea bastola ambayo alishawahi kuiona mikononi mwa muuaji yule hapo awali. Llama Automatic ilikuwa imemuelekea moja kwa moja usoni. Nyuma ya yule mtu mwenye tabasamu la kutisha kabisa alilopata kuliona, Puzo Vurumai, ambaye yeye alikuwa akimtambua kama “Claus Kinski” mwenye sura yenye alama za ndui, alikuwa amesimama akiwa ameegemea ukuta kando ya mlango hali mikono yake ikiwa imezama kwenye mifuko ya koti la suti nyeusi aliyovaa huku akimtazama kwa macho makali.
Jaka alibaki mdomo wazi.
Wale jamaa walikuwa amevalia suti ghali sana zilizowafanya waonekane kama aidha ni wafanyabiashara wenye mafanikio au ni maafisa wa maana sana kiasi kwamba Jaka hakuwalaumu walinzi waliowaruhusu kupita hadi pale ofisini kwake. Wakati Puzo alikuwa amepiga suti kali nyeusi, Don Sibazosi alikuwa amevaa suti safi sana ya kijivu iliyomkaa vyema sana.
Don Sibazosi alikuwa akimsogelea pale mezani huku akimlengeshea ile bastola iliyofungwa kiwambo cha kuzuia sauti hali mdomo wake ukiwa umefanya tabasamu na wakati huo huo macho yake yakionesha chuki ya hali ya juu.
Heh!
“Unadhani unaweza kuwakimbia Don Sibazosi na Puzo Vurumai halafu uishi kwa raha mstarehe hapa duniani Jaka?” Don Sibazosi alimuuliza, na ndio kwa mara ya kwanza Jaka alipoyasikia majina ya wale wauaji, ingawa kwa pale alipokuwa hakuwa na namna ya kujua yupi ni yupi kati yao. Alibaki ameduwaa.
Weekend njema Chiefs