Riwaya:Mtuhumiwa

Riwaya:Mtuhumiwa

RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA ARUBAINI NA MOJA
“Lakini Moze...Joakim alikuwa ni rafiki yangu...tulishapatana siku chache kabla ya kifo chake…wakati nilipokuwa nimelazwa pale hospitali!” Jaka alimambia kwa hamaniko.
Moze alisimama ghafla na kutulia tuli. Kisha aligeuka taratibu na kumtazama kwa macho yaliyokuwa na mchanganyiko wa mshangao, kutoamini na fadhaa.
“Joakim alikuwa rafiki yako tangu lini, Jaka?” Alimuuliza kwa sauti ya upole huku akimshangaa waziwazi.
Jaka aliguna na kutikisa kichwa kwa kukata tamaa. Aliona wazi kuwa hakuna atakalosema ambalo Moze atalielewa katika hali ile.
“Sasa kama rafiki yako ndiyo umemfanya vile...haya mie unayeniita mpenzi wako utanifanya nini...?” Moze alimuuliza kwa uchungu.
Heh!
Jaka alibaki akimtazama yule binti kwa simanzi, hakuamini kama ni kweli mpenziwe alikuwa amemgeuka ghafla namna ile.
“Jaka unataka kunifanya mimi mjinga...? Unasema uongo hivi hivi bila haya? Joakim angekuwa rafiki yako mimi nisingejua? Leo hii unategemea mimi nikuamini ukiniambia kuwa alikuwa rafiki yako...?”
Hata wakati akiyasikia maneno yale ya kunyong’onyeza moyo yakitamkwa, majuto na simanzi vilimshukia Jaka kutokana na uamuzi wake wa kutomueleza Moze tangu hapo awali kuhusu yale maongezi yake na Joakim ya siku ile Joakim alipokwenda kumtemebelea pale hospitali.
Laiti angejua kuwa haya yangekuja kutokea!
Ama kweli usilolijua, usiku wa kiza.
Sasa ni nani atamuamini akisema kuwa Joakim hakuwa adui yake wakati wa kifo chake?
Chuki aliyoiona machoni kwa Moze wakati akimueleza maneno yale ya kukatisha tamaa ilikuwa ni kubwa sana, na hilo lilimtisha pasina kifani. Na wakati akimuangalia yule binti akimsemesha yale maneno ya kunyong’onyeza moyo kwa chuki kubwa namna ile, ilimfunukia wazi kuwa kitu kilichokuwa kikiwaunganisha na kuwaweka pamoja siku zote, kilikuwa kimekatika, hakikuwepo tena. Alichokiona wakati ule machoni mwa yule msichana kilikuwa ni chuki iliyoelekezwa kwake yeye...macho ambayo siku zote yalikuwa yakimuangalia kwa upendo, sasa yalikuwa yakimuangalia kwa chuki ya hali ya juu. Hakukuwa na penzi hata kidogo kwenye macho yale! Ilikuwa ni chuki, chuki, chuki...
Mungu wangu! Jaalia hii iwe ndoto tafadhali...
“Moze...” Jaka alitaka kusema zaidi lakini Moze alimkatisha kwa kutikisa kichwa chake kwa nguvu kutoka upande mmoja kwenda mwingine.
“Jaka...kila mtu anajua kuwa wewe na Joakim hamkuwa marafiki...lakini tulishakubaliana kuwa hakuna haja ya kutaka kulipiza kisasi wala kuendeleza uhasama…”
“Na hivyo ndivyo ilivyokuwa Moze…hebu nisikilize basi kwanza nikueleweshe kilichotokea…”
“Kilichotokea ni kwamba umemuua Jaka…umeua mtu wewe! Kuna nini tena cha kuelewesha hapo, eenh?” Moze alimkatisha kauli kwa jazba huku akitikisa kichwa na akifumba macho kama kwamba alikuwa hataki hata kuendelea kumuona.
Jaka alibaki akimshangaa. Moze akafumbua macho na kumtazama Jaka kwa muda.
Walitazamana.
“Unanidanganya Jaka! Unanidanganya...kwamba Joakim alikuwa rafiki yako...!
“Moze wewe huelewi...inabidi unisikilize, la sivyo hutaelewa kabisa...”
“Haitosaidia kitu Jaka! Kuelewa au kutoelewa hakutobadilisha ukweli wa jambo hili Brown...sina haja ya kuelewa tena! Sina haja ya kuelewa kwa sababu huu ndio mwisho wa mapenzi yangu kwako! Sina tena upendo na wewe na sitaki kukuona tena maishani mwangu kwa sababu wewe ni muuaji Jaka...muuaji mkubwa!” Moze alifoka kwa hasira huku macho yake yakionesha kuumia kwa kiasi kikubwa sana.
“Ndio maana Rose alikuwa akijaribu kunitahadharisha kwenye ile barua yake…kumbe alijua kuwa wewe ni mtu wa namna gani! Je, na Joakim ulimuua kwa sababu alikugundua kuwa u- muuaji Jaka?” Moze aligongelea msumari wa moto kidondani.
“Eeenh?” Jaka alibaki mdomo wazi. Alihisi kitu kama msumari wa moto kikichoma kati kati ya moyo wake. Alitaka kusema kitu zaidi lakini sauti haikutoka tena. Alijaribu kumeza mate lakini mate yalikuwa yamemkauka. Alifumba macho kwa nguvu na kuyafumbua.
“Moze...!” Ndilo neno pekee lililotoka kinywani mwake baada ya hapo.
“Wewe ni muuaji Jaka. Tena muuaji wa watu wasio na hatia! Siwezi kupendana na muuaji Jaka, samahani sana...na naomba kuanzia sasa tusijuane!” Moze alifoka na kukimbia kutoka kwenye chumba kile huku akibubujikwa na mchozi. Jaka alikurupuka kutoka kwenye benchi alilokuwa amekalia na kujaribu kumsimamisha.
“Subiri Moze! Usiondoke tafadhali...tafadhali usiniache...sio sasa hivi! Unakosea sana Moze...yote unayoamini sivyo yalivyo...!” Alimpigia kelele, lakini Moze alikuwa ameshatoka nje ya chumba kile. Akabaki akiwa amesimama katikati ya chumba kile asijue la kufanya. Alijishika kichwa na kuinua uso wake kutazama juu, kisha akaachia ukelele mkubwa sana uliokuwa chanzo cha kilio kikubwa cha uchungu na kuomboleza. Alijibwaga pale sakafuni na kubaki akiwa amepiga magoti huku akiwa amejishika kichwa chake kwa mikono yake yote miwili kabla ya kujiangusha sakafuni kwa kishindo akitanguliza mikono na uso wake.
Mwili wake ulikuwa ukirukaruka kwa kilio cha kwikwi hali akiwa amesujudu pale sakafuni. Maneno ya Raymond Mloo yalimrudia tena na tena kichwani mwake huku akilia kwa sauti.
“...msichana anaweza kukupenda sana, lakini pia anaweza kukuchukia sana...na hapo ndipo utakapojuta kuzaliwa...”
Machozi yaliendelea kumbubujika akiwa pale chini huku akihisi uchungu usio kifani. Hakujua afanye nini. Maneno ya kwenye shairi alilomtungia Moze kwa ajili ya siku yake ya kuzaliwa yalimjia na kumzidishia uchungu maradufu.
... When your love is gone, my tears will flow.
…Siku penzi lako litakapoisha, machozi yatanibubujika...
Hajui alikaa pale kwa muda gani. Hatimaye alijizoazoa na kukaa pale sakafuni akiwa ameegemea ukuta. Kwa namna fulani maneno kutoka kwenye ule wimbo wa Roxette ambao siku zote ulikuwa ukimliza Moze yalimjia kichwani.
It must have been love, but it’s over now...
Bila shaka lilikuwa ni penzi, lakini sasa limekwisha...
Alianza kulia upya.
__________________
Sehemu nyingine ya jiji, Raul aliinua uso wake na kumtazama Kamishna Msaidizi wa Polisi Albert Bangusillo kwa macho yake ya kuogofya.
“Kwa hiyo unataka kuniambia kuwa huyo kijana anajua juu ya biashara inayofanyika hapa?” Alimuuliza, na Albert Bangusillo hakufanya haraka kumjibu. Alipeleka kinywani sigara iliyokuwa mkononi mwake na kuvuta moshi wa tumbaku kutoka kwenye sigara ile na kuupuliza juu kwa madaha.
Walikuwa nyumbani kwa Raul, maeneo ya Upanga, jijini Dar.
“Kwa mujibu wa maelezo yake, hiyo ndiyo maana yake…na kwa vyovyote atataka kutumia hilo kama njia ya kujisafishia jina lake na kuachiwa huru.” Hatimaye alimjibu.
Raul alimkazia macho kwa hasira.
“Lakini si tayari ana kesi ya mauaji? Sio rahisi kwake kuachiwa hivi hivi tu eti kwa kuwa amegundua njama za biashara ya kulevya…” Alimwambia.
“Yeah…ni kweli, lakini yule kijana siye aliyeua Raul…sheria ina namna ya kutambua jambo kama hilo. Unadhani akipata wakili mzuri itakuwa vigumu kumkwamua kutoka kwenye tuhuma feki kama hizo?”
Raul Pinto Garcia alimtazama kwa jicho la ghadhabu zaidi.
“Hapati wakili wa kumkwamua! Ataangamia tu!” Alikoroma.
“Hivyo ndivyo tunavyotarajia…lakini iwapo itatokea vinginevyo, italazimisha uchunguzi wa kina ufanyike kwenye hayo madai yake na pia kwa kumtafuta muuaji halisi…jambo ambalo litaleta usumbufu mkubwa kwa biashara yote. Hiyo haitasaidia lolote katika biashara, na mambo yakifika hapo Raul, sio siri…sitaweza tena kuyadhibiti!” Bangusillo naye alimkoromea.
Raul aliguna na kubaki akimtazama kwa muda bila ya kusema neno, na alipoongea ilikuwa dhahiri kuwa mjadala ule ulikuwa umefikia mwisho.
“Huyo kijana atazibwa mdomo milele Albert, iwe kabla au baada ya hukumu, it doesn’t matter….vijana wangu watahakikisha kuwa anapatwa na maafa fulani, na wewe kazi yako kama kawaida itakuwa ni kuhakikisha kuwa polisi hawaingilii mipango yangu, Okey?”
Albert Bangusillo aliafikiana naye kwa kichwa.
“Usiwe na shaka na upande wangu…ila sasa na wewe usipomdhibiti huyo Tony atakuja kututia wote kwenye balaa…” Alimwambia.
“Sipendi mtu yeyote anifundishe nini nifanye na nini nisifanye…shughuli hizi sikuzianzia hapa! Kitu pekee kinachonifanya nimtumie Tony ni kuwa popote anapokwenda anajulikana yeye ni mtoto wa nani na hivyo huwa hakuna maswali, na wewe unaelewa hilo!” Raul alimjibu kwa ghadhabu.
“Hilo liko wazi Raul, ila ni lazima nikukumbushe kuwa tatizo sio Jaka tu kwa hapa tulipo…na Tony naye pia ni tatizo…na wote wawili ni juu yako kuwadhibiti. Mimi mchango wangu kwako uko pale pale…n’taendelea kuhakikisha kuwa polisi haiingilii mipango yako, mengine ni juu yako!” Bangusillo alimjibu.
“Basi tuko sawa. Fanya jukumu lako…nami niache nifanye yangu!” Raul alimkoromea.
Waliagana, Bangusillo akiondoka na bahasha nene iliyosheheni noti nyingi.
_________________
Muda mfupi baada ya Moze kuondoka pale kituo cha polisi, Raymond Mloo alifika na kumkuta Jaka akiwa katika hali mbaya sana. Baada ya kumbembeleza sana, hatimaye kwa uchungu na taabu kubwa Jaka alimueleza kila kilichojiri baina yake na Moze pale mahabusu. Habari ile ilimsikitisha sana Raymond.
“Yaani…Dah! Moze huyu huyu…?”
“Ndiyo rafiki yangu…Moze kanigeuka kaka!”
“Yaani, aisee!” Raymond alijikuta akiishiwa na maneno ya kusema.
Walikaa kimya mle ndani kwa muda mrefu sana mpaka yule askari aliyekuwa zamu alipokuja na kumtaka Raymond aondoke kwani Jaka alikuwa ametembelewa na wageni wengine. Raymond alimtazama rafiki yake kwa huzuni, kisha walikumbatiana, na bila kuongea lolote akatoka huku akijipangusa machozi.
Baada ya Raymond kutoka, Mama Jaka aliingia akiwa ameongozana na msichana mmoja ambaye Jaka alikisia kuwa na umri wa kati ya miaka ishirini na nane ua thelathini hivi. Alikuwa amevaa suti nzuri nyeusi iliyokuwa na sketi fupi sana iliyoonesha mapaja yake mazuri na miguu yake mirefu. Mkononi alikuwa amebeba mkoba maalum wa kiofisi, maarufu kama briefcase.
“Naitwa Abiah…Abiah Byabato…nimeajiriwa na mama yako nikutetee kwenye kesi inayokukabili. Unajisikiaje?” Yule msichana alijitambulisha huku akimpa mkono na kumuwashia tabasamu zuri sana. Jaka alijitahidi kutabasamu kidogo huku akiupokea mkono ule laini. Alizitazama kucha ndefu na nzuri za vidole vya yule binti zikiwa zimepakwa rangi ya damu ya mzee na kukumbuka vidole vya mpenzi wake Moze.
“Sijambo…wewe ni wakili?” Jaka aliijibu salamu ya yule binti na kumtupia swali. Abiah aliafiki kwa kichwa huku akitabasamu.
“Unadhani utaweza kunisaidia dhidi ya tuhuma hizi?”
“Hakuna kisichowezekana kaka’angu…vipi huo uso wako, umepigwa?” Abiah alimjibu na kumtupia swali, akimakinika ghafla.
Jaka aliafiki kwa kichwa. Abiah alimtazama na kumuuliza tena.
“Umepigwa ukiwa chini ya ulinzi?”
Jaka akaafiki tena kwa kichwa. Umakini uliojengeka usoni kwa yule binti uliongezeka. Alimwita yule askari wa zamu, na kwa dakika kumi zilizofuata, alimtetemesha vibaya sana yule askari kwa kumnukulia vifungu kadhaa vya kisheria vinavyopinga mtuhumiwa kupigwa akiwa chini ya ulinzi bila ya sababu maalum. Yule askari alibabaika mno na alijitahidi kujitetea kuwa yeye hakuwa zamu wakati mambo hayo yanatokea.
“Basi mkuu wako wa kituo atajibu shutuma hizo mahakamani, kwani mimi na mteja wangu tutawafungulia kesi ya police brutality, halafu ndio utajua nani alikuwa zamu na nani hakuwepo!” Abiah alimchachamalia zaidi yule askari huku akiandika kwenye kijitabu kidogo alichotoa kwenye mkoba wake, akimaanisha kuwa atalifungulia jeshi la polisi kesi ya “ukatili wa kipolisi” huko mahakamani.
Jaka alivutiwa na jinsi yule binti alivyokabiliana na yule askari na akajua kuwa angalau alikuwa amepata wakili makini na mwenye kuielewa kazi yake.
“Jambo la kwanza tunalotakiwa kufanya kaka Jaka ni kukupatia dhamana ili utoke katika makazi haya mabaya. Halitakuwa jambo rahisi kutokana na uzito wa tuhuma zenyewe, lakini kutokana na mazingira haya ya kupigwa kwako, tunaweza kushawishi hadi ukapata dhamana, Okay?” Abiah alimwambia huku akirudisha tena ile sura yake nzuri yenye tabasamu.
Jaka aliafiki kwa kichwa.
“Sasa naomba unieleze mkasa wote ulivyokuwa hata ukajikuta katika tuhuma hizi…na naomba unieleze ukweli wako wote. Mimi ni wakili wako na ndiye msiri wako mkuu kuanzia sasa mpaka mwisho wa kesi hii.”
Jaka alikaa kimya kwa muda, kisha akaanza kumueleza. Alimuaelezea kisa chote tangu mwanzo hadi mwisho wakati Abiah akimrekodi maelezo yake kwa kutumia redio kaseti ndogo aliyokuja nayo. Jaka alipomaliza kutoa maelezo yake, Abiah alikaa kimya kwa muda huku akimtazama.
“Mnh! Pole sana Jaka…lakini naomba nikuhakikishie kuwa hii sio kesi ngumu kwako kama inavyoonekana. Kwanza lazima tuhakikishe unafunguliwa mashitaka…au unaachiwa huru bila kushitakiwa, ila huwezi kuendela kuwa mahabusu tu hapa bila sababu. Kesi ikiwa mahakamani ndio inakuwa rahisi kwetu kuivunjavunja na kuibuka washindi…”
“Nakubaliana nawe, lakini…unadhani kesi iliyo na vidhibiti kama hivi, japo vya kupandikizwa…it
akuwa rahisi kuivunjavunja kama unavyodai?” Jaka alihoji, na mama yake akitikisa kichwa kukubaliana na swali lile.
“Oh, Yes…ila…itanibidi nipitie vifungu kadhaa vya sheria na nionane na baadhi ya wanasheria wenzangu, na baada ya hapo tutakuwa tayari kupambana mahakamani…kama wataifikisha mahakamani.” Abiah alimwambia huku akitabasamu.
“Kwa hiyo ndiyo kusema…” Jaka aliuliza kwa matumaini kidogo, na Abiah alirudisha tena ile sura yake ya umakini.
“Sitaki kukupa matumaini hewa Jaka, lakini kutokana na maelezo yako, hii ni kesi nzuri sana kwetu. Tuna nafasi kubwa sana ya kushinda na kudai fidia ya mamilioni baada ya hapo, ila kuna vipengele fulani vya sheria ambavyo nahitaji kuvihakiki kwanza kabla sijawa na uhakika juu hilo…” Alimwambia kwa uangalifu. Jaka alimtazama na kuafiki maelezo yale kwa kichwa.
Muda mfupi baadaye Abiah aliaga na kuahidi kurudi tena siku iliyofuata saa nne asubuhi akiwa na maelekezo juu ya dhamana na uhakika juu ya vile vipengele muhimu vya sheria.
Jaka alibaki na mama yake kwa muda zaidi, kabla naye hajaondoka na kumuacha na majonzi yake pale mahabusu.
__________________
Wakili Abiah Byabato alitazama saa ya ukutani pale sebuleni kwake na kupiga mwayo. Ilikuwa ni saa nane za usiku na alihisi uchovu mkubwa. Alishusha miguu yake mirefu kutoka juu ya meza ndogo iliyokuwa imetapakaa vitabu na makabrasha kadhaa ya sheria na kusimama huku akijinyoosha
 
RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA ARUBAINI NA MBILI.
Wakili Abiah Byabato alitazama saa ya ukutani pale sebuleni kwake na kupiga mwayo. Ilikuwa ni saa nane za usiku na alihisi uchovu mkubwa. Alishusha miguu yake mirefu kutoka juu ya meza ndogo iliyokuwa imetapakaa vitabu na makabrasha kadhaa ya sheria na kusimama huku akijinyoosha.
Ile kesi ya Jaka ilikuwa ni kesi nzuri sana. Sasa alikuwa na uhakika kuwa alikuwa ana uwezo wa kushinda kesi ile iwapo itafikishwa mahakamani. Mwili ulimsisimka kwani alijua kuwa kushinda kesi ile kungempatia umaarufu mkubwa na kumfanya kuwa miongoni mwa mawakili wa kutumainiwa nchini.
Na maisha yake yatabadilika.
Akiwa amevaa suruali ya kulalia ya kitambaa cha hariri hali akiwa kifua wazi, alichukua ile redio kaseti yake ndogo iliyorekodi maelezo ya Jaka na kupachika visikilizio vya redio ile masikioni. Alizima taa ya pale sebuleni na kuelekea chumbani kwake ambako alizima taa ya kawaida na kuwasha taa ya rangi ya buluu, akajibwaga kitandani huku akisikiliza kwa mara nyingine tena yale maelezo ya Jaka. Aliyasikiliza upya yale maelezo hadi mwisho, kisha akayarudia tena. Kabla ile kaseti haijafika mwisho katika ile mara ya pili, alipitiwa na usingizi mzito.
Muda mfupi baada ya kupitiwa na lile lepe zito la usingizi, alihisi kitu kikimbana kwa nguvu mdomoni. Alishtuka kutoka usingizini na moyo ulimlipuka vibaya sana alipoona sura ya mtu asiyemjua ikiwa imemuinamia karibu sana na uso wake. Alitaka kupiga kelele lakini mkono wa yule mtu ulikuwa umembana mdomo kwa nguvu. Alijaribu kujiinua kutoka pale kitandani huku akitupa mikono na miguu, lakini vyote vilikuwa vimebanwa kwa nguvu. Alibaki akiikodolea macho ile sura ya duara uliyokuwa ikitabasamu.
Nani?? Unataka nini…?
Ingawa ile sura ilikuwa ikitabasamu, macho mekundu yaliyokuwa na nyama zilizolegea chini ya macho yale yalikuwa hayatabasamu hata kidogo. Yalikuwa ni macho maovu na wakili Abiah Byabato aliishiwa nguvu kwa woga.
“HuSsshhh, mwanasheria…kimya!” Yule mtu alimnong’oneza, halafu akaendelea huku akimuwekea mdomo wa bastola fupi kwenye paji la uso, “Nitatoa mkono wangu mdomoni mwako taratibu, nawe utaendelea kubaki kimya hivyo hivyo…la sivyo natawanya ubongo wako…sawa?”
Abiah aliitikia kwa kichwa haraka haraka huku akiwa ametumbua macho vibaya sana.
Yule mtu alimuachia mdomo wake taratibu huku akimdidimizia ile bastola kwenye paji la uso. Abiah alibaki kimya huku akifumba macho yake kwa nguvu, kisha aliyafumbua taratibu akitaraji kujikuta peke yake pale kitandani, lakini bado yule mtu alikuwepo, akiendelea kumtazama huku akitabasamu.
Heh!
“Un…unataka nin…we’ nani….?” Abiah aliuliza kwa kitetemeshi.
Yule mtu aliendelea kumtazama tu huku akiwa amemuwekea bastola kwenye paji la uso. Na hapo ndipo Abiah alipomuona mtu mwingine akitokea nyuma ya mtu yule.
Wako wawili!
Ingawa taa ya rangi iliyokuwa ikiwaka chumbani kwake haikuwa na mwanga wa kutosha kuona vizuri, aliweza kuona kuwa sura nyembamba ya yule mtu wa pili ilikuwa imetapakaa alama nyingi za ndui. Yule mtu mrefu mwenye sura ya ndui alianza kumfunga mikono na miguu yake kwa kamba. Abiah hakuthubutu kupiga kelele kwani bastola bado ilikuwa kwenye paji lake la uso. Baada ya kumfunga kamba kwa nguvu pale kitandani, yule mtu mwenye sura ya ndui alitoa plasta kubwa kutoka kwenye mfuko wa suruali yake na kumbandika mdomoni.
Yule mtu mwenye tabasamu aliondoa bastola usoni kwa Abiah na kuanza kutembeza macho yake kwenye sehemu ya juu ya kiwiliwili cha yule msichana. Aliyatazama matiti mazuri na madogo ya yule binti kwa muda, kisha akateremsha macho yake taratibu hadi kwenye kitovu cha yule binti.
Mungu wangu…wanataka kunibaka…!
Wakili Abiah aliwaza kwa kihoro huku akitokwa na machozi.
“Hapana mrembo wangu…hatuna haja ya kukubaka….” Yule mtu mwenye tabasamu la kuogofya alimwambia kwa sauti ya kuchobeza, kama kwamba alikuwa ameyasikia mawazo yake.
Oooh, sasa mnataka nini jamani? Mmeingiaje humu ndani…?.
“Abiah…Abiah…Abiah…kwa nini unataka kujiharibia maisha yako bure? Mtoto mrembo kama wewe…” Yule mtu mwenye tabasamu alimnong’oneza huku akivuta meza ndogo iliyokuwa mle chumbani na kuiweka kando ya kitanda na kuketi. Abiah alibaki akitembeza macho huku moyo ukimdunda kwa woga na kihoro.
Kwani nimefanya nini jamani…? Mmejuaje jina langu…?
Wale jamaa walikuwa wakifanya wayafanyayo kwake kimya kimya, na Abiah alipandwa kihoro pale alipomshuhudia yule mtu mwingine akimpandia pale kitandani na kumpigia magoti juu yake, akikiweka kiwiliwili chake katikati ya miguu yake.
Ooh, mungu wangu! Mnanibaka nyieee…!
Abiah alibaki akilia kwa kukata tamaa, akitembea macho tu kufuatilia kile alichokuwa akifanyiwa. Na hata pale lile wazo lilipokuwa linapita akilini mwake alimuona yule mtu mwembamba akimuwekea ncha ya kisu chembamba na kirefu katikati ya matiti yake mazuri. Mwili ulimsisimka, taharuki ikamtawala. Huku akimtazama usoni kwa macho ya kutisha, yule jamaa alitembeza ncha ya kisu kile taratibu kutoka kifuani kwa yule binti hadi kitovuni. Hapo kisu kile kilitulia na yule jamaa akijiweka vizuri pale kitandani. Kufikia hapo Abiah alikuwa akilia kama mtoto mdogo huku akitoa miguno hafifu kutokana na kuzibwa mdomo na ile plasta aliyobandikwa mdomoni. Alizungusha macho kule kwa yule mtu mwingine, na kuona kuwa alikuwa akitazama mambo yale huku akitabasamu. Mwili ulimuingia baridi. Lilikuwa ni tabasamu la kutisha kuliko yote aliyowahi kuyaona maishani mwake.
Ghafla alihisi yule mtu aliyekuwa pale kitandani akiishika kwa nguvu suruali yake ya kulalia na kwa tendo moja la haraka sana aliichana ile suruali kwa kisu chake kikali. Mguno wa woga ulimtoka huku akijitahidi kupiga kelele bila mafanikio. Yule mtu alivuta kwa nguvu mabaki ya suruali ile na kuitupa kando bila kujali.
Wakili Abiah Byabato alibaki uchi, kwani huwa havai chupi wakati wa kulala.
Eeeh, Mungu wangu…!
Yule jamaa alimtazama kwa dharau akiwa amelala uchi wa kuzaliwa pale kitandani, na Abiah alijihisi anakaribia kufa.
Ni nini hasa mnachokitaka jamani…kwa nini mnanidhalilisha namna hii?
Yule jamaa alikitembeza tena kile kisu taratibu kuelekea kwenye sehemu ya uuke wake, na Abiah alihisi ubaridi ukimtambaa mwili mzima, akawa analia waziwazi huku kamasi zikimvuja. Kile kisu kilisimama kwa muda katika lile eneo la uuke wake, kisha yule jamaa akafanya kama kwamba alikuwa akijaribu kumnyoa nywele zilizokuwa eneo lile kwa kisu kile.
Abiah akajikojolea bila ajizi.
Jamaa hakuonekana kujali hali ile, badala yake alikipandisha tena kisu kile taratibu na kukituliza kwenye titi la yule binti na kumtazama usoni kwa macho yake yaliyojaa unyama wa hali ya juu.
Huku akilia kwa uchungu Abiah alijikukurusha pale kitandani kujaribu kujikomboa, lakini kila alivyofanya hivyo ncha kali ya kile kisu ikawa inamcoma kwenye titi, akabaki akijinyonganyonga tu pale kitandani huku akimtupia macho ya kuomboleza yule mtu mwenye tabasamu lisilokauka, machozi yakimbubujika, akitoa sauti za kilio kilichobanwa.
Ndipo yule mtu mwenye tabasamu alipoinama na kumuwekea mdomo wake sikioni, kisha akamnong’oneza kwa ile sauti yake ya kubembeleza huku akimchezea rasta zake kimahaba.
“Mambo yote haya umejitakia mwenyewe Abiah…huyu bwa’ mdogo hapa alisema kuwa tuje tukuue tu halafu twende zetu…lakini mi’ n’kamwambia kuwa haitakuwa busara kulipotezea taifa rasilimali-mtu kama hii, Abiah…au wewe unaonaje? Kukuua si kutalipunguzia taifa idadi ya rasilimali-watu, eeeennh?”
Abiah alijikuta akiitikia kwa kichwa haraka haraka huku akiwa ametumbua macho, moyo ukimwenda mbio.
“Safi sana! Mi’ n’lijua kuwa tutaelewana tu Abiah…” Mzee wa matabasamu alimwambia huku akimpigapiga kichwani kwa namna ya kumbembeleza, kisha akaendelea, “…kwa hiyo tukakubaliana kuwa badala ya kuja kukuua, tuje tukueleze tu mawazo yetu halafu tukuachie wewe uyatekeleze, na…ukiyatekeleza basi hutatuona tena maishani mwako na utaendelea kuishi…”
Kufikia hapo mzee wa matabasamu alipiga kimya na kubaki akimtazama tu, tabasamu likiwa limeganda usoni kwake. Alikaa vile kwa dakika nyingi kiasi cha kumjaza wahka Abiah.
Mnataka kunieleza nini kwani ndugu zangu…? Nielezeni basi muende zenu…!
Yule mtu mwingine alimtembezea tena ncha kali ya kisu chake tumboni, na Abiah alijihisi kupoteza fahamu huku mkojo aliojikojolea ukimuwasha mapajani.
“…lakini ukiamua kuwa mkaidi, basi…itabidi tufanye kama bwa’ mdogo hapa alivyopendekeza
….” Hatimaye yule mzee mwenye tabasamu lisilokauka akamalizia kauli yake, na safari hii lile tabasamu lake likaishia kwenye kicheko chepesi, kisha akapiga kimya tena, akawa anajishughulisha kuisafisha-safisha bastola yake kwa kutumia shuka ya kile kitanda.
Abiah alimtazama kwa woga akamgeukia yule mtu mwembamba aliyemkalia juu yake pale kitandani, ambaye sasa alikuwa anatumia kile kisu chake kujikunia kidevu chake, kama kwamba hana habari naye tena.
Abiah alitamani awasemeshe wale watu lakini alikuwa amezibwa mdomo. Walibaki katika hali ile kwa dakika kadhaa, ambazo Abiah aliziona ni masaa.
Sasa mnataka nini kwani jamani??? Semeni basiii!!!
Aliwakemea nyuma ya miguno aliyokuwa akiitoa huku akihangaika pale kitandani. Nahapo ayule mtu mwenye tabasamu la mfululizo alimgeukia ghafla na kuwambia huku akimazama moja kwa moja usoni na tabasamu lake likiwa imara usoni kwake.
“Jaka ni habari mbaya sana Abiah!”
Khah!
“Na mtu yeyote anayejihusisha naye anakutwa na mabaya zaidi ya haya unayoyaona hapa sasa hivi Abiah…so kaa mbali na Jaka bi mdogo. Hayo ndiyo mawazo tuliyokuja kukupa usiku huu wakili.” Mzee wa matabasamu alimalizia kwa sauti yake ya kuchombeza huku akimvutavuta zile rasta zake.
Haa! Kumbe ndio hilo! Jaka…!? Oh, Mungu wangu…!
Wakili Abiah Byabato alilia kama mtoto mdogo. Matabasamu aliendelea tu kumueleza kwa ile sauti yake ya kuogopesha, japo mwenyewe ndio alikuwa anaifanya iwe ya kuchombeza.
“Kama umetuelewa juu ya hilo Abiah, sisi tutaondoka nawe utaendelea kuishi. Ila ukijitia kupiga simu au kutoa taarifa polisi tu, ujue huo ndio mwisho wako…tutakutokea popote pale ulipo na tutakuua taratibu sana hadi utatubembeleza tukuue haraka haraka, upo hapo?”
Doh!
Abiah aliitikia kwa kichwa huku akiwa amemtumbulia macho yule mtu. Macho ya yule mtu sasa yalikuwa makatili kweli kweli na bado lile tabasamu lake lilikuwa palepale.
“Lazima ukumbuke juu ya mawazo yetu kuhusu Jaka Abiah, sawa?”
Kwa mara nyingine Abiah aliitikia kwa kichwa haraka haraka, macho yakimtembea, machozi yakimbubujika, akili ikimzunguka. Matabasamu alimkazia macho, na alipotaka kugeuza uso wake alimkamata kidevu kwa nguvu na kumgeuza ili waendelee kutazamana, kisha akamgeukia yule mwenzake mwenye sura ya ndui.
“Hebu muoneshe Abiah mfano wa yatakayompata iwapo atasahau haya mawazo yetu juu ya Jaka.” Alimwambia, na kwa mara ya kwanza tangu wamuibukie mle chumbani mwake, Abiah aliona tabasamu likichanua usoni kwa yule mtu mwenye uso wa ndui, kisha kwa kihoro kikubwa alimshuhudia yule mkatili akimkamata kidole cha shahada na kumuwekea kile kisu kwenye pingili ya kidole kile kwa muda.
Mungu wangu, ananikata kidole!
Kisha kama aliyebadili mawazo, yule jamaa alikihamishia kisu kile kwenye kucha ya kile kidple na kuanza kuikata taratibu sana kama kwamba kile kisu kilikuwa ni wembe.
Oooooh!
Alipomaliza kumkata ile kucha alihamia kidole kingine…na kingine…na kingine. Kile kisu kilikuwa kikali kuliko wembe. Yalikuwa ni mateso makubwa sana kwa Abiah, ambaye alibaki akilia huku akiziona kucha zake za mikononi alizozipenda na kuzitunza sana zikikatwa na yule mtu ambaye sasa alijihakikishia kuwa alikuwa mwehu. Na kila kucha iliyokatwa mwili ulimsisimka kwa kuhofia kukatwa kidole na kisu kile kikali. Alipomaliza vidole vyote vya mikononi, yule mtu alihamia miguuni na kumkata kucha zote za miguuni. Aliifanya ile kazi kwa utaratibu wa hali ya juu kiasi kwamba Abiah alitamani kumpigia kelele kuwa afanye haraka amalize ili apate kupumua.
Ilikuwa ni hali ya kuogopesha sana.
Hatimaye yule mtu alimaliza.
“Vizuri sana dogo!” Matabasamu alisema baada ya yule jamaa kumaliza kazi yake, kisha akamgeukia Abiah. “Na huo Abiah, ni mfano tu wa kuhakikisha kuwa hutasahau juu ya haya tuliyokueleza…kaa mbali na Jaka…kaa mbali sana na Jaka…Jaka ni habari mbaya sana kwako!” Alimwambia. Abiah alianza kutulia kwani alijua kuwa karibu wale watu wataondoka. Lakini mambo yalikuwa bado. Yule mtu alibaki akimtazama tu baada ya kumwambia yale maneno.
Sasa mbona hamuondoki…?
“Sasa tunataka kukuonesha kuwa hatutanii juu ya haya tuliyokuja kukueleza Abiah. Utakapokwenda kinyume na maelekezo yetu, utapatwa na madhila makubwa kuliko haya utakayoyapata hivi punde.”
Nhah? Nini tena…? mbona sielewi…kuna madhila gani tena zaidi ya haya ndigu zangu? Eeh Mungu wangu nisaidie mie….!
Abiah alipagawa.. Na hapo yule jamaa mwembamba aliyemkata kucha kwa namna ya kutisha kabisa, alimkamata kidole chake cha shahada cha mkono ya kushoto na kuanza kukikeremsha taratibu kisu cha kuelekea kwenye kidole kile.
Oooh, sasa nd’o wanan’kata kidole!
Alijikukurusha kwa nguvu pale kitandan huku akigumia kwa taabu, mate yakimpalia kooni kutokana na kuzibwa mdomo na ile plasta kubwa. Alilia kwa uchungu na maumivu ya hali ya juu wakati yule jamaa akimng’oa kucha yake ya kidole kile kwa kutumia kile kisu.
Lilikuwa ni tendo lililohitaji roho mbaya sana kulitekeleza, lakini yule jamaa alikuwa akilitekeleza kama kwamba alikuwa akimpaka rangi ya kucha tu, uso wake ukiwa mtulivu, usioonesha hisia yoyote.
Lah!
Mwanamama alilia kwa sauti iliyokuwa ikitoka kwa miguno isiyoeleweka huku mate yakizidi kumpalia, alishuhudia kucha yake iking’olewa huku damu ikimwagika kwa wingi sana. Alifumba macho lakini bado uchungu ulikuwa palepale.
Jamani si bora nife tu…!
Maumivu yalikuwa ni makali mno kuvumilika. Wakili Abiah Byabato akapoteza fahamu.
____________________
Alipozinduka wale watu hawakuwepo. Huku akihisi maumivu makali mkononi, alijitahidi kujiinua kutoka pale kitandani na kukaa. Zile kamba alizokuwa amefungwa hazikuwepo na ile plasta aliyobandikwa mdomoni ilikuwa imetolewa. Redio kaseti yake ilikuwa imetupwa sakafuni ikiwa wazi, kaseti iliyokuwa na maelezo ya Jaka haikuwemo.
Shuka lake pale kitandani lilikuwa limetapakaa damu.
Wakili Abiah Byabato alijikunyata pale kitandani na kuanza kulia kwa sauti. Alilia kwa muda mrefu sana huku akitetemeka.
Wale ni watu gani?
Kwa nini walitaka Jaka aadhibiwe kwa kosa ambalo hakulifanya?
Iwapo wameweza kumnyofoa ukucha bila hata ya kuonesha kujali hata kidogo, watashindwa kumuua?
Alijikongoja hadi bafuni ambako alijisafisha na kujifunga kile kidole kilichoathiriwa kwa bandeji iliyokuwa mle ndani mwake, kisha usiku ule ule aliwasha gari na kujipeleka hospitali, machozi yakimbubujika njia nzima.
Kulipopambazuka na akiwa tayari ameshapata matibabu ya lile jeraha aliloachiwa an wale watu, alimuelekeza katibu muhtasi wake kuandika barua ya kujitoa uwakili wa Jaka kwa sababu za matatizo ya kiafya.
 
RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA ARUBAINI NA TATU.
Mwanamama alilia kwa sauti iliyokuwa ikitoka kwa miguno isiyoeleweka huku mate yakizidi kumpalia, alishuhudia kucha yake iking’olewa huku damu ikimwagika kwa wingi sana. Alifumba macho lakini bado uchungu ulikuwa palepale.
Jamani si bora nife tu…!
Maumivu yalikuwa ni makali mno kuvumilika. Wakili Abiah Byabato akapoteza fahamu.
____________________
Alipozinduka wale watu hawakuwepo. Huku akihisi maumivu makali mkononi, alijitahidi kujiinua kutoka pale kitandani na kukaa. Zile kamba alizokuwa amefungwa hazikuwepo na ile plasta aliyobandikwa mdomoni ilikuwa imetolewa. Redio kaseti yake ilikuwa imetupwa sakafuni ikiwa wazi, kaseti iliyokuwa na maelezo ya Jaka haikuwemo.
Shuka lake pale kitandani lilikuwa limetapakaa damu.
Wakili Abiah Byabato alijikunyata pale kitandani na kuanza kulia kwa sauti. Alilia kwa muda mrefu sana huku akitetemeka.
Wale ni watu gani?
Kwa nini walitaka Jaka aadhibiwe kwa kosa ambalo hakulifanya?
Iwapo wameweza kumnyofoa ukucha bila hata ya kuonesha kujali hata kidogo, watashindwa kumuua?
Alijikongoja hadi bafuni ambako alijisafisha na kujifunga kile kidole kilichoathiriwa kwa bandeji iliyokuwa mle ndani mwake, kisha usiku ule ule aliwasha gari na kujipeleka hospitali, machozi yakimbubujika njia nzima.
Kulipopambazuka na akiwa tayari ameshapata matibabu ya lile jeraha aliloachiwa an wale watu, alimuelekeza katibu muhtasi wake kuandika barua ya kujitoa uwakili wa Jaka kwa sababu za matatizo ya kiafya.
Pamoja na barua ile, aliambatanisha maelekezo yaliyopata kurasa tatu ambayo yalimpa Jaka kipengele muhimu cha kutumia katika utetezi wake dhidi ya tuhuma zinazomkabili, iwapo kesi yake itafikishwa mahakamani. Alimpa maelezo juu ya kipengele alichokielezea kuwa kinahusiana na Evidence beyond reasonable doubt.
Ushahidi usio na shaka hata kidogo.
Ingawa yaliyomkuta usiku uliopita asingeweza kuyasahau kamwe, alijua kuwa yatabaki kuwa siri yake maisha yote.
___________________
Mchana wa siku ile barua iliwasilishwa kwa Jaka, na baada ya kuisoma alichanganyikiwa vibaya sana. Kila kitu kilionekana kumong’onyoka mikononi mwake. Ilikuwa ni wazi kuwa alikuwa amekamata njia kuu kuelekea kwenye maangamizo, na hilo lilimuuma sana. Alielewa wazi kuwa swala la wakili Abiah kujitoa kwenye utetezi wake lilikuwa ni matokeo ya njama za akina Tony, hususan wale washirika wake aliomuona nao kule kwenye lile jengo la St. Stanza, kwa lengo la kuhakikisha kuwa anatiwa hatiani kwa kosa la mauaji ya Joakim.
Masikini wakili Abiah…sijui naye amekutwa na yepi huko. Mungu amsaidie!
Alikubali matokeo.
Siku iliyofuata, alifunguliwa rasmi mashitaka ya mauaji na siku hiyo hiyo akahamishiwa gerezani Segerea.
Siku tatu baadaye alifikishwa mahakama ya Kisutu kusomewa rasmi shitaka lake. Siku hiyo aliteremshwa kutoka kwenye gari la kubebea mahabisu na washitakiwa kutoka kule gerezani pamoja na washitakiwa wengine, yeye akiwa amefungwa pingu mikononi. Alilishtushwa na umati wa watu waliojaa nje ya mahakama ile. Wapiga picha wa magazeti mbali mbali walianza kumpiga picha bila ya mpangilio naye akalazimika kujiziba uso kwa mikono yake yenye pingu. Wengi wa waliokusanyika pale walikuwa ni wanafunzi wenzake, naye aliweza kuwatambua baadhi yao wakati akipitishwa kuelekea ndani ya jengo la mahakama, ambamo aliwekwa pamoja na mahabusu wengine kwenye chumba maalum kusubiri muda wa kesi yake kuitwa.
Hatimaye kesi yake iliitwa naye akapandishwa kizimbani na kusomewa shitaka lake. Kutokana na mahakama ile kutokuwa na mamlaka ya kusikiliza na kuendesha kesi za mauaji, hakutakiwa kujibu lolote kwenye shitaka lile na akafahamishwa kuwa kesi ile itahamishiwa mahakama kuu ambako itapangiwa siku ya kusikilizwa. Kabla ya kurudishwa kwenye kile chumba cha kusubiria kurejeshwa Segerea alipata nafasi ya kutembeza macho yake ndani ya kile chumba cha mahakama kilichofurika. Alimuona rafiki yake Raymond Mloo akiwa ameketi kwenye safu za mbele kabisa ndani ya korti ile. Macho yao yalipokutana, Raymond alitabasamu. Naye alijitahidi kutabasamu kidogo na kiasi alifarijika kwa tendo lile. Mama yake alikuwa nyuma kidogo ya Raymond. Walitazamana kwa huzuni na mama yake kwa muda, na hatimaye Jaka alifanikiwa kumtupia tabasamu hafifu. Yule mama alijibu tabasamu lile kwa tabasamu hafifu zaidi huku akibubujikwa na machozi.
Pamoja na wanafunzi wengi wengine aliwatambua pale mahakamani, Tony na wale wenzake wawili pia walikuwepo, wakiwa wamevaa nguo nyeusi tupu kwa ishara ya kuomboleza msiba wa “rafiki” yao.
Wanafiki wakubwa.
Jaka aliwatazama mmoja baada ya mwingine bila ya kuficha hisia zake dhidi yao. Aligonganisha macho na Tony, wakatazamana kwa chuki huku Jaka akitamani amrukie kutoka pale alipokuwa amesimama, lakini hakuweza kufanya hivyo. Alibaki akimtupia chuki kwa macho yake. Tony akamchanualia tabasamu la kejeli. Jaka alihamisha macho yake uapnde mwingine wa chumba kile cha mahakama.
Ndipo alipomuona Sajenti John Vata.
Alikuwa amekaa kwenye kona kabisa ya chumba kile akiwa katika mavazi ya kiraia miongoni mwa raia wengine waliokusanyika ndani ya mahakama ile. Walitazamana, na Jaka akaona huzuni kubwa machoni mwa yule askari ingawa alikuwa kijitahidi kuficha hisia zake. Walizidi kutazamana kwa muda, na Jaka hakujua iwapo alitakiwa atabasamu au akasirike. Alihamisha macho yake kutoka kwa yule askari na ndipo yalipotua kwa Moze. Moyo ulimlipuka na kuanza kumwenda mbio. Alihisi koo likimkauka na machozi yakimchonyota.
Walitazamana kidogo sana ilitosha kumfanya ajutie kitendo kile kwani katika sekunde zile chache walizotazamana, aliona chuki kubwa machoni mwa Moze. Chuki ile ilikuwa imeelekezwa kwake.
Iliuma sana. Ilikuwa haivumiliki.
Aliinamisha macho.
Hakuyainua tena hadi alipotolewa nje ya mahakama ile…
 
RIIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA ARUBAINI NA NNE

Alihamisha macho yake kutoka kwa yule askari na ndipo yalipotua kwa Moze. Moyo ulimlipuka na kuanza kumwenda mbio. Alihisi koo likimkauka na machozi yakimchonyota.
Walitazamana kidogo sana ilitosha kumfanya ajutie kitendo kile kwani katika sekunde zile chache walizotazamana, aliona chuki kubwa machoni mwa Moze. Chuki ile ilikuwa imeelekezwa kwake.
Iliuma sana. Ilikuwa haivumiliki.
Aliinamisha macho.
Hakuyainua tena hadi alipotolewa nje ya mahakama ile…
___________________
Kesi yake iliunguruma mahakama kuu wiki mbili baadaye, na kudumu kwa miezi mitatu. Ilikuwa ni miezi mitatu ya machungu na madhila mazito sana kwake wakati akisota gerezani Segerea huku akizidi kuendelea na kesi. Mama yake na Raymond walishamtembelea mara kadhaa akiwa kule Segerea, pamoja na baadhi ya rafiki zake wachache kutoka kule chuoni. Si Moze, wakili Abiah wala Sajenti Vata aliyeenda kumtembelea kule gerezani katika kipindi kile…
_____________

Gari la magereza aina ya Land Rover lilikuwa likienda kwa mwendo wa kasi sana, kuelekea Dodoma. Sehemu ya nyuma gari lile, Jaka alikuwa ameketi kwa kujiinamia kwenye benchi lilikuwa mle garini, akiwa amefungwa pingu mikononi na miguuni. Pamoja naye kule nyuma safari hii kulikuwa kuna askari wawili wa magereza ambao hakuwa amewatilia maanani tangu anapakiwa ndani ya gari lile. Alijua tu kuwa mmoja wa wale askari alikuwa ameketi pembeni yake, wakati yule mwingine alikuwa ameketi mbele yake. Roho ilimuuma sasa, kwani ingawa aliona kuwa hakimu alijitahidi kutoa hukumu kwa haki kadiri alivyoweza, bado kulikuwa kuna walakini kwa kuwa yeye alikuwa anaadhibiwa kwa kosa ambalo hakulifanya. Mama yake alishukuru kuwa angalau atakuwa hai, lakini kwake lile bado lilikuwa ni tatizo.
Kwa nini muuaji aachiwe hivi hivi tu?
Kwa nini madai yake yasifanyiwe uchunguzi na akina Tony wakatiwa mbaroni?
Alijua sasa hatoweza tena kuendelea na masomo yake na hilo ndilo lililomuuma kuliko vyote.
Akiwa amejiinamia pale kando ya yule askari, aliweza kuiona bastola fupi na nene ikiwa inaning’inia kwenye mkoba maalum uliopachikwa kiunoni kwa yule askari, na hivyo ile bastola ilikuwa katikati yake na yule askari.
Alipeleka macho yake kwa yule askari aliyekuwa mbele yake na hapo hapo moyo wake ukamlipuka na akahisi ubaridi ukimtambaa kwa kasi mgongoni. Yule askari alikuwa akimtazama kwa makini hali uso wake ukiwa umepambwa na tabasamu pana!
Lile tabasamu na macho ya yule askari havikuwa vigeni kwake.
Jaka alikumbuka siku ile alipokuwa akichungulia kwenye dirisha ndani ya jengo la St. Stanza Canned Fish Company na kumuona Tony akiwa amekaa kando ya mtu mfupi, mnene, aliyekuwa amevaa tai iliyompendeza sana ambaye alikuwa akitabasamu bila ya sababu maalum.
...smiling face...
Ni yeye! Tabasamu ni lile lile!
Jaka alibaki akimtazama yule askari aliyekuwa akitabasamu mbele yake na aliyaona tena yale macho. Ni macho yale yale yaliyokuwa yakimchungulia kutoka kwenye vitundu viwili vilivyotobolewa kwenye soksi iliyouficha uso wa mtu yule siku moja tu iliyopita.
Ah! Huyu ni yule yule muuaji aliyetaka kuniua jana...! Vipi leo yumo ndani ya gari hili akiwa kama askari...?
Mungu wangu! Jana alinikosa, sasa ndio amekuja kunimaliza kabisa!
Woga wa ajabu ulimgubika.
Yaani hawa watu walikuwa wamedhamiria kumuua kiasi hiki? Waliwezaje kupata nafasi ya kuwa naye ndani ya lile gari pamoja naye namna ile? Yule mtu aliendelea tu kumtazama huku mdomo wake ukiwa umeachia tabasamu pana. Yaani alikuwa analiona tabasamu la kifo mbele ya uso wake na hakuwa na la kufanya.
Alishusha macho yake taratibu na kumgeukia yule askari aliyekuwa pembeni yake na moyo ukamtumbukia nyongo.
Uso wa yule askari aliyeketi pembeni yake ulikuwa umetapakaa alama nyingi za ndui!
Oh, Mungu wangu…Klaus Kinski!
Hapo alielewa kuwa wale jamaa hawakuwa askari wa kweli na kwamba walikuwa naye mle garini kwa lengo moja tu la kumuua.
Watamuuaje? Na wapi?
Na hata wakati mawazo haya yakipita kichwani kwake, alimuona yule jamaa mwenye uso wa ndui akitoa sigara na kuanza kuipeleka taratibu mdomoni mwake. Akili ilimcheza, macho yalimtembea. Alizungusha jicho na kuitazama ile bastola iliyokuwa katikati yake na yule askari.
Ghafla, kabla yule “askari” hajaifikisha kinywani ile sigara yake, alijitia kupiga chafya kwa nguvu huku akiinua mikono yake kujiziba mdomo. Kiwiko cha mkono wake kilimgonga kwa nguvu kidogo yule askari na kumfanya aiangushe ile sigara. Haraka alijitia kuomba samahani kwa woga huku akiinama kutaka kuiokota ile sigara taratribu.
“Hebu tulia wewe!” Yule mtu mwenye tabasamu pana alimkaripia na kumuamrisdha atulie kama alivyokuwa. Ndilo jambo alilokuwa akilitaka. Alitulia na yule askari aliyekuwa pembeni yake aliinama na kuanza kuiokota ile sigara. Hiyo ndiyo nafasi aliyokuwa akiitarajia.
Haraka sana Jaka alijigeuza na kuichomoa ile bastola kutoka kiunoni kwa yule askari kabla hajainuka. Don Sibazosi aliliona tendo lile na kutoa tusi kali huku akipeleka mkono wake kiunoni kutoa bastola yake, lakini alichelewa.
Jaka alikuwa ameikamata ile bastola kwa mikono yake yote miwili na kuikandamiza kwa nguvu kisogoni kwa Puzo Vurumai, yeye akimjua kama Klaus Kinski.
“No! Nyie nd’o mtulie!” Jaka alifoka kwa kitetemeshi huku akiwa amemkazia macho Don Sibazosi na bastola bado ikiwa kisogoni kwa Puzo ambaye alibaki akiwa ameinama vile vile, mkono wake mmoja ukielea juu ya ile sigara iliyolala pale chini ndani ya gari. Don Sibazosi alibaki akiwa ameduwaa na bastola yake mkononi.
“Unafanya kosa kubwa kijana...sisi ni askari...na hapa tunaiwakilisha Jamhuri...” Alisema huku akimtazama Jaka machoni kwa makini na mdomo wake bado ukiwa na tabasamu pana.
“Kimya!” Jaka alimfokea huku akiwa amekunja uso wake kwa ghadhabu, kisha akaendelea kwa kitetemeshi, “Weka chini hiyo bastola yako...taratibu mno!”
Don Sibazosi alitii huku macho yake yakionesha ghadhabu zisizo kifani na mdomo wake ukiwa una tabasamu pana. Jaka alikiri kuwa yule jamaa alikuwa ni mtu hatari na wa ajabu sana.
“Sasa…Sasa nataka…unifungue pingu za miguuni...kwa utulivu mno! Nikihisi mtikisiko wowote usiohitajika natawanya ubongo wa huyu mwenzako hapa, sawa?” Jaka alimuamuru tena kwa ukali, safari hii bila kitetemeshi.
Bila ya kujibu kitu, Don Sibazosi alitoa funguo kutoka kwenye mfuko wake wa shati na kuanza kumfungua zile pingu taratibu mno. Alipomaliza alibaki akimtazama kwa hasira kubwa huku bado mdomo wake ukiwa una tabasamu pana. Jaka alimwamuru arudi mahala alipokuwa amekaa hapo mwanzo na aziache zile funguo pale chini. Yule muuaji alitii.
Gari liliendelea kwenda tu.
Taratibu Jaka aliitembeza ile bastola mwilini kwa Puzo Vurumai na kuikandamiza ubavuni kwa yule jamaa.
“Sasa wewe nataka uokote hizo funguo hapo chini na unifungue pingu za mikononi...ukit
etereka kidogo tu, nakushindilia marisasi!” Alimwambia huku bado macho yake yakiwa yamemuelekea Don Sibazosi.
Puzo Vurumai alitekeleza amri ile huku akitetemeka kama bwege. Baada ya kumaliza Jaka alimwamuru naye aende kukaa kule alipokuwa yule mwenzake.
Sasa wakawa wanatazamana, Jaka kwenye benchi la upande mmoja wale wauaji la uoande mwingine, huku safari ikiendelea.
“Nyie sio askari wala nini...ni wauaji tu nyie!” Aliwaambia. Jamaa walibaki wakimtazama tu. Alimnyooshea Don Sibazosi ile bastola.
Don Sibazosi alibaki akimtazama kwa macho ya ghadhabu huku kinywa chake bado kikiwa kimechanua kwa tabasamu pana. Jaka alikuwa akifikiri haraka haraka afanye nini baada ya kufikia hatua ile. Alikuwa akiuliza yale maswali kwa kupitisha muda wakati akifikiri. Alitupa jicho kwenye dirisha dogo lililozibwa kwa wavu na nondo, na kuona kuwa walikuwa wameshafika maeneo ya Manzese. Alijua kuwa Manzese kulikuwa kuna msongamano mkubwa wa watu, hivyo kama alitaka kufanya kitu ni vyema afanye akiwa katika eneo lile.
Huku akiwa amewaelekezea wale watu ile bastola kwa mkono wake wa kulia, aliokota mkoba wake uliokuwa chini ya miguu yake na kuupachika begani.
“Hutafika popote kijana...” Don Sibazosi alimwambia.
“Kimya!” Jaka alimkemea, na hapo hapo aligeuka na kuipiga risasi loki ya mlango wa nyuma wa gari ile, bastola ikitoa mlipuko mkubwa mle ndani, lakini aliikosa. Akapiga risasi nyingine na loki ikisambaratika vibaya, mlango ukafunguka na kujibamiza tena kwa nguvu.
Don Sibazosi na Puzo Vurumai walikurupuka kutaka kuiwahi ile bastola iliyokuwa pale chini, lakini Jaka aliwageukia na kuwanyooshea ile bastola iliyokuwa mkononi mwake.
“We! Weeee! Tulia kama mlivyo, pumbavu!”
Jamaa walisita, na hapo gari lilianza kupunguza mwendo likielekea kusimama baada ya dereva kusikia ile milipuko ya bastola kutokea kule nyuma. Bila ya kufikiri zaidi Jaka alimtupia Puzo ile bastola kwa nguvu. Puzo aliikwepa na wakati huo huo Don Sibazosi alijirusha chini kuiwahi ile bastola nyingine wakati Jaka akijitupa nje ya gari lile na kudondokea barabarani. Gari lililokuwa nyuma ya ile Land Rover lilifunga breki ghafla baada ya dereva wake kuona mtu akidondoka barabarani kutokea kwenye gari lililokuwa mbele yake, na wakati huo huo Jaka alijibiringisha pembeni huku akisikia mayowe ya watu na honi za gari zikiambatana na misuguano ya matairi kwenye lami na baadaye kishindo kikubwa. Lile gari lililomkosa liliigonga kwa nyuma ile Land Rover ya Magereza.
Tafrani!
Jaka aliinuka kutoka kando ya barabara na kutupa jicho kule yale magari yaliyogongana na kuona watu wengi wakikimbia kuelekea kule. Alimuona Puzo Vurumai akiwa ameinua juu bastola yake akijaribu kupenya kwenye ule msongamano wa watu kumfuata kule alipokuwapo. Aligeuka na kuanza kutembea kwa mwendo wa haraka kuondoka katika eneo lile, akipishana na watu waliokuwa wakikimbia kuelekea kule ilipotokea ajali.
“Simama! Mkamate huyo…mfungwa anatorokaaa!” Amlisikia Don Sibazosi ikipaaza sauti nyuma yake. Aliongeza kasi huku akigeuka na kuwaona wale wauaji wawili wakikimbilia, bastola zao zikiwa zimeinuliwa juu ya vichwa vyao na vya watu wengi waliokuwa wamesongamana katika eneo lile, kelele za kishabiki na honi za magari zikirindima kutokana na msongamano uliotokana na ajali ile.
Alianza kukimbia kurudi kule lile gari lao lilipokuwa limetokea.
Don Sibazosi na Puzo Vurumai, wakiwa katika mavazi ya kiaskari wa magereza, bastola mikononi, walimkimbiza huku wakipamiana na watu waliokuwa wamezagaa eneo lile.
Jaka aliongeza mbio.
“Simama we! Kamata huyooo!”
Jaka alizidi kutimua mbio kwa kasi zaidi.
“Kamata huyooo! Mwiziii!”
Oh, Mungu wangu!
Jaka aliongeza kasi.
Wapita njia na wachuuzi wa bidhaa mbali mbali waliozagaa eneo lile walianza kumtafuta mwizi, huku wengine wakijiunga kupiga kelele za “mwizi...mwizi...” bila hata ya kujua ni nani hasa anayekimbizwa. Jaka aliendelea kutimua mbio, akilini akijua kuwa tayari alikuwa mdomoni kabisa mwa mauti, kwani kuitiwa mwizi katika eneo la Manzese ni kifo cha wazi wazi. Mbele yake aliliona daraja la Manzese naye alitimua mbio kulielekea.
“Jakkaaa! Simamaaaa! Tutakupiga risasi!” Don Sibazosi alimpigia kelele huku akimkimbiza, na Jaka akazidisha kasi. Puzo Vurumai alisimama na kutanua miguu yake huku akichukua shabaha kumlenga Jaka kwa bastola aliyoishika kwa mikono yake yote miwili. Watu wengi waliokuwa wakikimbia hovyo katika eneo lile huku wakipiga kelele za “Mwizi…! Mwizi…!” walimkinga asiweze kupata shabaha vizuri. Alisonya kwa sauti na kuteremsha mikono yake. Alitazama uelekeo aliokuwa akichukua Jaka, kisha akatimua mbio huku akiikata ile barabara kuelekea upande wa pili.
“Toka njianiii! Polisi..!” Alibwata huku akikimbilia upande wa pili wa ile barabara akiwa ameinua bastola yake hewani.
Kule alipokuwa Jaka alibakiza hatua chache tu kulifikia lile daraja, na hapo alitokea mtu mmoja mbele yake aliyetaka kumdaka huku akipiga kelele za mwizi. Jaka alimpiga kibega na kumuacha akisambaratika barabarani naye akaendelea kutimua mbio. Yaani sasa alikuwa kama jogoo anayekimbizwa ili achinjwe...kukamatwa kwake kulimaanisha kifo.
Hatua kadhaa mbele yake jamaa mwingine alijitokeza akimwendea kasi huku akiwa ameinua fimbo kubwa tayari kumtandika. Bila kufikiri Jaka aliruka juu na kumshidilia soli ya kiatu chake kifua, na yule mtu akatupwa nyuma huku akitoa yowe na ile fimbo ikimtoka. Lile pigo lilimpoteza uelekeo Jaka na alipepesuka vibaya, akisota kwa mikono huku miguu yake ikiendelea kujisukuma mbele ili aendelee kukimbia kisha akafanikiwa kisimama tena wima na kuendelea kutimua mabio.
Aliziparamia kwa pupa ngazi za lile daraja huku Don Sibazosi akiwa mbali nyuma yake. Juu ya daraja lile alitimua mbio kuelekea upande mwingine wa barabara huku akipishana na watu kadhaa waliokuwa wakipita juu ya daraja lile. Don Sibazosi alifika juu ya daraja na kumuona Jaka akikimbia kuelekea upande wa pili wa barabara. Aliinua bastola yake na kupiga risasi mbili hewani.
“Wote lala chiniii!” Alipiga kelele kuwambia watu waliokuwa wakipita pale darajani baada ya kuachia ile milipuko miwili iliyozua taharuki isiyosemekana pale juu ya daraja.
Mara ile ile watu wote waliokuwa wakitembea juu ya daraja lile walijitupa chini huku wakipiga kelele kwa woga. Mlio wa risasi si jambo la kawaida kwa wakaazi wa jiji la Dar, na hakuna aliyetaka kuwa wa kwanza kupigwa risasi.
Jaka alisimama ghafla aliposikia ile milio ya risasi, na wakati huo huo aliona watu wote wakilala chini huku wakipiga kelele za woga. Aligeuka nyuma haraka, na kumuona Don Sibazosi akimsogelea taratibu huku akiwa amemnyooshea bastola, akitweta kwa nguvu na jasho likimtiririka hali macho yake yakiwa yamemwiva kwa hasira na mdomo wake ukiwa umepambwa na tabasamu lake pana, pua zikimtanuka na kumsinyaa kila alipopumua.
Jaka naye hakuwa katika hali tofauti sana na ile ya Don Sibazosi, kwani alikuwa amelowa jasho huku akihema kwa taabu kutokana na kutimua mbio. Alimtazama Don Sibazosi na akajua kuwa mwisho wake ulikuwa umewadia. Aligeuka nyuma na kutazama kule alipokuwa akijaribu kukimbilia hapo awali.
Kutokea upande ule, alimuona Puzo Vurumai akimsogelea huku akiwa amemnyooshea bastola kwa mikono yake yote miwili, naye alikuwa ametota jasho huku akihema kwa nguvu.
Dah!
Alichanganyikiwa.
 
RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA ARUBAINI NA TANO
Alimtazama Don Sibazosi na akajua kuwa mwisho wake ulikuwa umewadia. Aligeuka nyuma na kutazama kule alipokuwa akijaribu kukimbilia hapo awali.
Kutokea upande ule, alimuona Puzo Vurumai akimsogelea huku akiwa amemnyooshea bastola kwa mikono yake yote miwili, naye alikuwa ametota jasho huku akihema kwa nguvu.
Dah!
Alichanganyikiwa.
Taratibu aliinua mikono yake juu na kumgeukia Don Sibazosi huku akitamani kulia na kupiga kelele.
“Utafanyaje sasa Jaka?” Don Sibazosi alimfokea huku akimsogelea,“ Unataka kukimbia? Kimbia tu...kimbia!”
Jaka alibaki akiwa amesimama huku mikono yake ikiwa juu. Kando yake alisikia vilio vya akina mama na watoto waliokuwa wamelala chini pale darajani. Aliangalia kulia kwake chini
ya lile daraja. Magari yalikuwa yakipita chini ya daraja lile. Hakuwa na njia yoyote ya kujiokoa kutoka katika mtego ule. Alikuwa amenasa.
Alitazama kushoto kwake.
Kingo za daraja lile zilikuwa karibu sana naye kwa upande wake wa kushoto kuliko kulia. Aligeuka tena kulia. Kutokea upande wa magari yatokeayo Ubungo aliliona lori kubwa la mchanga likija taratibu mno huku likipiga kelele nyingi. Lile Lori lilikuwa wazi nyuma na kutoka pale alipokuwa amesimama, Jaka aliweza kuona jinsi mchanga ulivyokuwa umejirundika kule nyuma. Lile Lori lilikuwa likikaribia kupita chini ya daraja.
“Nyie sio askari! Ni wauaji tu nyie!” Jaka alimpigia kelele Don, na yule muuaji aliachia cheko ya kebehi.
“Piga magoti hapo chini mafungwa! Mbinu yako ya kutaka kutoroka imegonga mwamba!” Don alimkoromea kwa sauti ili watu wote pale wamsikie.
Haraka haraka Jaka alipima umbali uliokuwepo kabla lile lori halijapita chini ya lile daraja, moyo ukimwenda mbio, na mabango makubwa ya matangazo pale juu ya daraja yakimkinga asione vizuri.
“Mnataka kuniua!” Alibwata kumjibu Don, huku taratibu akianza kutembea kuelekea kule alipokuwa Puzo, akiwa ameinua mikono yake juu. Don Sibazosi nae aliendelea kumsogelea huku akimtazama kwa makini, bado akiwa amemlengeshea bastola. Kutokea pale aliposogea, Jaka aliweza kuona vizuri zaidi kule chini barabarani. Lile Lori sasa lilikuwa chini ya daraja, na kwa kadiri alivyopimia, lilikuwa moja kwa moja chini ya pale alipokuwa amesimama. Alisimama akimtazama Don Sibazosi huku akijitahidi kutomfikiria Puzo Vurumai aliyekuwa nyuma yake.
“Sasa huna ujanja mfungwa...utakwenda na sisi kwa upole au kwa mabavu? Uamuzi ni wako!” Don Sibazosi alimwambia huku akimuashiria kwa ile bastola kuwa akae chini. Wala Jaka hakumtilia maanani. Akili yake ilikuwa ikifanya kazi kwa kasi sana, moyo wake ukimuenda mbio kwa kasi zaidi. Alijua ni jambo gani alikuwa anataka kulifanya na alihisi miguu ikimwishia nguvu, naye akajitahidi kutoitilia maanani hali hiyo.
Aligeuka kidogo kushoto kwake, na kutokea pale juu alikiona kichwa cha lile Lori kikitokeza upande wa pili wa daraja kule chini, barabarani.
Mungu nisaidie!
Ghafla alishusha mikono yake, akapiga hatua moja kushoto na kukamata kingo za daraja lile kwa mikono yake na kujirusha juu, akiitupa miguu yake juu ya kingo za lile daraja huku akiiachia mikono yake.
Alielea hewani kudondokea upande wa pili wa lile daraja, ambako, kiasi cha futi zisizopungua kumi na tano kwenda chini, ililala ile barabara ya Morogoro na magari mengi yakipita juu yake.
E bwana we!
Kilikuwa ni kitendo cha haraka na cha hatari sana, kilichohitaji udiriki kwa hali ya juu.
Don Sibazosi hakuamini macho yake wakati akimshudia yule kijana akijirusha kutoka juu ya lile daraja, na tusi kubwa kwa mshangao lilimtoka huku akimtupia risasi.
Alichelewa kwa sekunde tu na risasi yake ikaambulia patupu.
Puzo Vurumai naye aliliona tendo lile lisilotarajiwa, na aliachia ukelele wa kutoamini huku hapo hapo naye akimtupia Jaka risasi mbili za haraka haraka, lakini naye pia alichelewa. Risasi zake zilipita sehemu ile wakati Jaka akiwa tayari ameshapotelea upande wa pili wa ukingo wa daraja lile.
Jaka alipiga kelele huku akidondoka kutoka juu ya daraja lile, akisikia milio ya bastola na mayowe ya taharuki kutoka kwa watu, na kwa sekunde chache alipata hisia kuwa ule ulikuwa ndio mwisho wake.
Hesabu zake zilikuwa sahihi.
Alidondoka kwa kishindo kwenye rundo la mchanga nyuma ya lile lori, vumbi jingi likitimka na kupeperuka hewani, maumivu makali yakimtabaa mwilini kutokea ubavuni alipoangukia pale mchangani, lakini hakujali. Lile lori lilikuwa likiendelea tu na safari yake polepole huku likipiga kelele nyingi. Jaka alijigeuza haraka pale mchangani na kutazama kule darakani.
Kutoka pale alipokuwa, aliweza kuwaona wale wauaji wawili wakiwa wamesimama nyuma ya kingo za kushoto za daraja la Manzese wakilitazama lile Lori likitokomea taratibu, yeye akiwa ndani yake.
Na hata alipokuwa akiwatazama wale wauaji wakizidi kuonekana wadogo kadiri lile lori lilivyokuwa likizidi kutokomea, alijua kuwa alikuwa ameshinda pambano tu, lakini sio vita. Wale jamaa wangeendelea kumfuatilia tu.
Sasa aende wapi…?
_____________________
Lile lori liliposimama kwenye taa za kuongozea magari zilizokuwa kwenye makutano ya barabara ile ya Morogoro na ile ya Kawawa, aliruka nje kutoka nyuma ya lile Lori bila ya hata dereva wa gari lile kuelewa kilichokuwa kimeendelea. Alianza kutembea haraka bila ya uelekeo maalum kando ya ile barabara ya Kawawa.
Kichwa chake kilikuwa kimezingirwa na mawazo huku akijiuliza ilikuwaje hata akapata ujasiri wa kujirusha kutoka pale juu ya daraja namna ile. Mwili ulimsisimka alipojaribu kufikiri matokeo yangekuwaje iwapo angelikosa lile Lori.
Ingawa mvua ilikuwa ikinyesha kwa nguvu na watu walikuwa wakikimbia huku na huko kujikinga na mvua ile, yeye alikuwa akitembea tu kama kwamba ile mvua haikuwepo au ilikuwa haimhusu. Aliangalia saa yake na kuona kuwa ilikuwa ni saa kumi na moja na nusu za jioni.
Ilikuwaje hata wale wauaji wakafanikiwa kuingia pamoja naye ndani ya lile gari la magereza bila ya kugundulika kuwa hawakuwa askari wa kweli?
Au ina maana kuwa jambo hili linahusisha watu wengi katika ngazi za juu kiasi kwamba hakuna namna ya yeye kujikwamua katika balaa hili…? Au ndio maana hata hakimu aliamua kunipa adhabu hii, akijua kuwa hata huko Dodoma sitafika…?
Mawazo hayo na mengine kama hayo yalikuwa yakipita kichwani mwake wakati akitembea kuifuata ile barabara, sasa akitembea kwa mwendo wa taratibu sana huku akihisi uchovu wa hali ya juu.
Aliamua kwenda nyumbani kwa mama yake huko msasani bila ya kujali kuwa huenda huko akakutana na balaa likimsubiri, lakini aliona ni lazima aonane na mama yake, kwani alijua kuwa muda mfupi tu ulikuwa umebaki kwa yeye kuendelea kuwa hai.
Alipoifikia nyumba yao alikuwa amechoka na ametota kwa mvua vibaya sana. Akili yake ilimtuma afungue tu mlango na aingie ndani ajibwage kitandani huku akijua kuwa ataonana tena na mama yake. Wazo la kumuona tena mama yake wakati hakuwa na matarajio ya kumuona tena kwa siku nyingi zijazo nusura limtie tena mikononi mwa polisi, kwani alikuwa akipeleka mkono wake kufungua mlango ule, kisha katika sekunde ya mwisho kabisa alisita. Alinyata kuzungukia ubavuni mwa nyumba ile na kuchungulia sebuleni kwao kupitia dirishani.
Moyo ulimlipuka kwa mshituko na kihoro, kwani kupitia pale dirishani aliweza kuwaona askari wa jeshi la polisi wawili wakiwa wamekaa kwenye kochi kubwa wakitazamana na mama yake aliyekuwa amekaa kwenye kochi ndogo mbele yao. Askari mwingine alikuwa amesimama kando ya lile kochi alilokalia mama yake. Wale askari walionekana kuwa walikuwa wakimuuliza maswali fulani mama yake, ambaye alikuwa akitikisa kichwa chake kutoafikiana na yale waliyokuwa wakimueleza huku machozi yakimtiririka. Aliwatazama wale askari kwa makini, lakini hakuwa amepata kuwaona kabla na hakuwa na njia yoyote ya kuweza kujua iwapo walikuwa ni askari wa kweli au ni miongoni mwa wale wa bandia wanaotaka kumuua.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom