RIWAYA; MTUHUMIWA
MTUNZI; HUSSEIN TUWA
SEHEMU YA ARUBAINI NA MBILI.
Wakili Abiah Byabato alitazama saa ya ukutani pale sebuleni kwake na kupiga mwayo. Ilikuwa ni saa nane za usiku na alihisi uchovu mkubwa. Alishusha miguu yake mirefu kutoka juu ya meza ndogo iliyokuwa imetapakaa vitabu na makabrasha kadhaa ya sheria na kusimama huku akijinyoosha.
Ile kesi ya Jaka ilikuwa ni kesi nzuri sana. Sasa alikuwa na uhakika kuwa alikuwa ana uwezo wa kushinda kesi ile iwapo itafikishwa mahakamani. Mwili ulimsisimka kwani alijua kuwa kushinda kesi ile kungempatia umaarufu mkubwa na kumfanya kuwa miongoni mwa mawakili wa kutumainiwa nchini.
Na maisha yake yatabadilika.
Akiwa amevaa suruali ya kulalia ya kitambaa cha hariri hali akiwa kifua wazi, alichukua ile redio kaseti yake ndogo iliyorekodi maelezo ya Jaka na kupachika visikilizio vya redio ile masikioni. Alizima taa ya pale sebuleni na kuelekea chumbani kwake ambako alizima taa ya kawaida na kuwasha taa ya rangi ya buluu, akajibwaga kitandani huku akisikiliza kwa mara nyingine tena yale maelezo ya Jaka. Aliyasikiliza upya yale maelezo hadi mwisho, kisha akayarudia tena. Kabla ile kaseti haijafika mwisho katika ile mara ya pili, alipitiwa na usingizi mzito.
Muda mfupi baada ya kupitiwa na lile lepe zito la usingizi, alihisi kitu kikimbana kwa nguvu mdomoni. Alishtuka kutoka usingizini na moyo ulimlipuka vibaya sana alipoona sura ya mtu asiyemjua ikiwa imemuinamia karibu sana na uso wake. Alitaka kupiga kelele lakini mkono wa yule mtu ulikuwa umembana mdomo kwa nguvu. Alijaribu kujiinua kutoka pale kitandani huku akitupa mikono na miguu, lakini vyote vilikuwa vimebanwa kwa nguvu. Alibaki akiikodolea macho ile sura ya duara uliyokuwa ikitabasamu.
Nani?? Unataka nini…?
Ingawa ile sura ilikuwa ikitabasamu, macho mekundu yaliyokuwa na nyama zilizolegea chini ya macho yale yalikuwa hayatabasamu hata kidogo. Yalikuwa ni macho maovu na wakili Abiah Byabato aliishiwa nguvu kwa woga.
“HuSsshhh, mwanasheria…kimya!” Yule mtu alimnong’oneza, halafu akaendelea huku akimuwekea mdomo wa bastola fupi kwenye paji la uso, “Nitatoa mkono wangu mdomoni mwako taratibu, nawe utaendelea kubaki kimya hivyo hivyo…la sivyo natawanya ubongo wako…sawa?”
Abiah aliitikia kwa kichwa haraka haraka huku akiwa ametumbua macho vibaya sana.
Yule mtu alimuachia mdomo wake taratibu huku akimdidimizia ile bastola kwenye paji la uso. Abiah alibaki kimya huku akifumba macho yake kwa nguvu, kisha aliyafumbua taratibu akitaraji kujikuta peke yake pale kitandani, lakini bado yule mtu alikuwepo, akiendelea kumtazama huku akitabasamu.
Heh!
“Un…unataka nin…we’ nani….?” Abiah aliuliza kwa kitetemeshi.
Yule mtu aliendelea kumtazama tu huku akiwa amemuwekea bastola kwenye paji la uso. Na hapo ndipo Abiah alipomuona mtu mwingine akitokea nyuma ya mtu yule.
Wako wawili!
Ingawa taa ya rangi iliyokuwa ikiwaka chumbani kwake haikuwa na mwanga wa kutosha kuona vizuri, aliweza kuona kuwa sura nyembamba ya yule mtu wa pili ilikuwa imetapakaa alama nyingi za ndui. Yule mtu mrefu mwenye sura ya ndui alianza kumfunga mikono na miguu yake kwa kamba. Abiah hakuthubutu kupiga kelele kwani bastola bado ilikuwa kwenye paji lake la uso. Baada ya kumfunga kamba kwa nguvu pale kitandani, yule mtu mwenye sura ya ndui alitoa plasta kubwa kutoka kwenye mfuko wa suruali yake na kumbandika mdomoni.
Yule mtu mwenye tabasamu aliondoa bastola usoni kwa Abiah na kuanza kutembeza macho yake kwenye sehemu ya juu ya kiwiliwili cha yule msichana. Aliyatazama matiti mazuri na madogo ya yule binti kwa muda, kisha akateremsha macho yake taratibu hadi kwenye kitovu cha yule binti.
Mungu wangu…wanataka kunibaka…!
Wakili Abiah aliwaza kwa kihoro huku akitokwa na machozi.
“Hapana mrembo wangu…hatuna haja ya kukubaka….” Yule mtu mwenye tabasamu la kuogofya alimwambia kwa sauti ya kuchobeza, kama kwamba alikuwa ameyasikia mawazo yake.
Oooh, sasa mnataka nini jamani? Mmeingiaje humu ndani…?.
“Abiah…Abiah…Abiah…kwa nini unataka kujiharibia maisha yako bure? Mtoto mrembo kama wewe…” Yule mtu mwenye tabasamu alimnong’oneza huku akivuta meza ndogo iliyokuwa mle chumbani na kuiweka kando ya kitanda na kuketi. Abiah alibaki akitembeza macho huku moyo ukimdunda kwa woga na kihoro.
Kwani nimefanya nini jamani…? Mmejuaje jina langu…?
Wale jamaa walikuwa wakifanya wayafanyayo kwake kimya kimya, na Abiah alipandwa kihoro pale alipomshuhudia yule mtu mwingine akimpandia pale kitandani na kumpigia magoti juu yake, akikiweka kiwiliwili chake katikati ya miguu yake.
Ooh, mungu wangu! Mnanibaka nyieee…!
Abiah alibaki akilia kwa kukata tamaa, akitembea macho tu kufuatilia kile alichokuwa akifanyiwa. Na hata pale lile wazo lilipokuwa linapita akilini mwake alimuona yule mtu mwembamba akimuwekea ncha ya kisu chembamba na kirefu katikati ya matiti yake mazuri. Mwili ulimsisimka, taharuki ikamtawala. Huku akimtazama usoni kwa macho ya kutisha, yule jamaa alitembeza ncha ya kisu kile taratibu kutoka kifuani kwa yule binti hadi kitovuni. Hapo kisu kile kilitulia na yule jamaa akijiweka vizuri pale kitandani. Kufikia hapo Abiah alikuwa akilia kama mtoto mdogo huku akitoa miguno hafifu kutokana na kuzibwa mdomo na ile plasta aliyobandikwa mdomoni. Alizungusha macho kule kwa yule mtu mwingine, na kuona kuwa alikuwa akitazama mambo yale huku akitabasamu. Mwili ulimuingia baridi. Lilikuwa ni tabasamu la kutisha kuliko yote aliyowahi kuyaona maishani mwake.
Ghafla alihisi yule mtu aliyekuwa pale kitandani akiishika kwa nguvu suruali yake ya kulalia na kwa tendo moja la haraka sana aliichana ile suruali kwa kisu chake kikali. Mguno wa woga ulimtoka huku akijitahidi kupiga kelele bila mafanikio. Yule mtu alivuta kwa nguvu mabaki ya suruali ile na kuitupa kando bila kujali.
Wakili Abiah Byabato alibaki uchi, kwani huwa havai chupi wakati wa kulala.
Eeeh, Mungu wangu…!
Yule jamaa alimtazama kwa dharau akiwa amelala uchi wa kuzaliwa pale kitandani, na Abiah alijihisi anakaribia kufa.
Ni nini hasa mnachokitaka jamani…kwa nini mnanidhalilisha namna hii?
Yule jamaa alikitembeza tena kile kisu taratibu kuelekea kwenye sehemu ya uuke wake, na Abiah alihisi ubaridi ukimtambaa mwili mzima, akawa analia waziwazi huku kamasi zikimvuja. Kile kisu kilisimama kwa muda katika lile eneo la uuke wake, kisha yule jamaa akafanya kama kwamba alikuwa akijaribu kumnyoa nywele zilizokuwa eneo lile kwa kisu kile.
Abiah akajikojolea bila ajizi.
Jamaa hakuonekana kujali hali ile, badala yake alikipandisha tena kisu kile taratibu na kukituliza kwenye titi la yule binti na kumtazama usoni kwa macho yake yaliyojaa unyama wa hali ya juu.
Huku akilia kwa uchungu Abiah alijikukurusha pale kitandani kujaribu kujikomboa, lakini kila alivyofanya hivyo ncha kali ya kile kisu ikawa inamcoma kwenye titi, akabaki akijinyonganyonga tu pale kitandani huku akimtupia macho ya kuomboleza yule mtu mwenye tabasamu lisilokauka, machozi yakimbubujika, akitoa sauti za kilio kilichobanwa.
Ndipo yule mtu mwenye tabasamu alipoinama na kumuwekea mdomo wake sikioni, kisha akamnong’oneza kwa ile sauti yake ya kubembeleza huku akimchezea rasta zake kimahaba.
“Mambo yote haya umejitakia mwenyewe Abiah…huyu bwa’ mdogo hapa alisema kuwa tuje tukuue tu halafu twende zetu…lakini mi’ n’kamwambia kuwa haitakuwa busara kulipotezea taifa rasilimali-mtu kama hii, Abiah…au wewe unaonaje? Kukuua si kutalipunguzia taifa idadi ya rasilimali-watu, eeeennh?”
Abiah alijikuta akiitikia kwa kichwa haraka haraka huku akiwa ametumbua macho, moyo ukimwenda mbio.
“Safi sana! Mi’ n’lijua kuwa tutaelewana tu Abiah…” Mzee wa matabasamu alimwambia huku akimpigapiga kichwani kwa namna ya kumbembeleza, kisha akaendelea, “…kwa hiyo tukakubaliana kuwa badala ya kuja kukuua, tuje tukueleze tu mawazo yetu halafu tukuachie wewe uyatekeleze, na…ukiyatekeleza basi hutatuona tena maishani mwako na utaendelea kuishi…”
Kufikia hapo mzee wa matabasamu alipiga kimya na kubaki akimtazama tu, tabasamu likiwa limeganda usoni kwake. Alikaa vile kwa dakika nyingi kiasi cha kumjaza wahka Abiah.
Mnataka kunieleza nini kwani ndugu zangu…? Nielezeni basi muende zenu…!
Yule mtu mwingine alimtembezea tena ncha kali ya kisu chake tumboni, na Abiah alijihisi kupoteza fahamu huku mkojo aliojikojolea ukimuwasha mapajani.
“…lakini ukiamua kuwa mkaidi, basi…itabidi tufanye kama bwa’ mdogo hapa alivyopendekeza
….” Hatimaye yule mzee mwenye tabasamu lisilokauka akamalizia kauli yake, na safari hii lile tabasamu lake likaishia kwenye kicheko chepesi, kisha akapiga kimya tena, akawa anajishughulisha kuisafisha-safisha bastola yake kwa kutumia shuka ya kile kitanda.
Abiah alimtazama kwa woga akamgeukia yule mtu mwembamba aliyemkalia juu yake pale kitandani, ambaye sasa alikuwa anatumia kile kisu chake kujikunia kidevu chake, kama kwamba hana habari naye tena.
Abiah alitamani awasemeshe wale watu lakini alikuwa amezibwa mdomo. Walibaki katika hali ile kwa dakika kadhaa, ambazo Abiah aliziona ni masaa.
Sasa mnataka nini kwani jamani??? Semeni basiii!!!
Aliwakemea nyuma ya miguno aliyokuwa akiitoa huku akihangaika pale kitandani. Nahapo ayule mtu mwenye tabasamu la mfululizo alimgeukia ghafla na kuwambia huku akimazama moja kwa moja usoni na tabasamu lake likiwa imara usoni kwake.
“Jaka ni habari mbaya sana Abiah!”
Khah!
“Na mtu yeyote anayejihusisha naye anakutwa na mabaya zaidi ya haya unayoyaona hapa sasa hivi Abiah…so kaa mbali na Jaka bi mdogo. Hayo ndiyo mawazo tuliyokuja kukupa usiku huu wakili.” Mzee wa matabasamu alimalizia kwa sauti yake ya kuchombeza huku akimvutavuta zile rasta zake.
Haa! Kumbe ndio hilo! Jaka…!? Oh, Mungu wangu…!
Wakili Abiah Byabato alilia kama mtoto mdogo. Matabasamu aliendelea tu kumueleza kwa ile sauti yake ya kuogopesha, japo mwenyewe ndio alikuwa anaifanya iwe ya kuchombeza.
“Kama umetuelewa juu ya hilo Abiah, sisi tutaondoka nawe utaendelea kuishi. Ila ukijitia kupiga simu au kutoa taarifa polisi tu, ujue huo ndio mwisho wako…tutakutokea popote pale ulipo na tutakuua taratibu sana hadi utatubembeleza tukuue haraka haraka, upo hapo?”
Doh!
Abiah aliitikia kwa kichwa huku akiwa amemtumbulia macho yule mtu. Macho ya yule mtu sasa yalikuwa makatili kweli kweli na bado lile tabasamu lake lilikuwa palepale.
“Lazima ukumbuke juu ya mawazo yetu kuhusu Jaka Abiah, sawa?”
Kwa mara nyingine Abiah aliitikia kwa kichwa haraka haraka, macho yakimtembea, machozi yakimbubujika, akili ikimzunguka. Matabasamu alimkazia macho, na alipotaka kugeuza uso wake alimkamata kidevu kwa nguvu na kumgeuza ili waendelee kutazamana, kisha akamgeukia yule mwenzake mwenye sura ya ndui.
“Hebu muoneshe Abiah mfano wa yatakayompata iwapo atasahau haya mawazo yetu juu ya Jaka.” Alimwambia, na kwa mara ya kwanza tangu wamuibukie mle chumbani mwake, Abiah aliona tabasamu likichanua usoni kwa yule mtu mwenye uso wa ndui, kisha kwa kihoro kikubwa alimshuhudia yule mkatili akimkamata kidole cha shahada na kumuwekea kile kisu kwenye pingili ya kidole kile kwa muda.
Mungu wangu, ananikata kidole!
Kisha kama aliyebadili mawazo, yule jamaa alikihamishia kisu kile kwenye kucha ya kile kidple na kuanza kuikata taratibu sana kama kwamba kile kisu kilikuwa ni wembe.
Oooooh!
Alipomaliza kumkata ile kucha alihamia kidole kingine…na kingine…na kingine. Kile kisu kilikuwa kikali kuliko wembe. Yalikuwa ni mateso makubwa sana kwa Abiah, ambaye alibaki akilia huku akiziona kucha zake za mikononi alizozipenda na kuzitunza sana zikikatwa na yule mtu ambaye sasa alijihakikishia kuwa alikuwa mwehu. Na kila kucha iliyokatwa mwili ulimsisimka kwa kuhofia kukatwa kidole na kisu kile kikali. Alipomaliza vidole vyote vya mikononi, yule mtu alihamia miguuni na kumkata kucha zote za miguuni. Aliifanya ile kazi kwa utaratibu wa hali ya juu kiasi kwamba Abiah alitamani kumpigia kelele kuwa afanye haraka amalize ili apate kupumua.
Ilikuwa ni hali ya kuogopesha sana.
Hatimaye yule mtu alimaliza.
“Vizuri sana dogo!” Matabasamu alisema baada ya yule jamaa kumaliza kazi yake, kisha akamgeukia Abiah. “Na huo Abiah, ni mfano tu wa kuhakikisha kuwa hutasahau juu ya haya tuliyokueleza…kaa mbali na Jaka…kaa mbali sana na Jaka…Jaka ni habari mbaya sana kwako!” Alimwambia. Abiah alianza kutulia kwani alijua kuwa karibu wale watu wataondoka. Lakini mambo yalikuwa bado. Yule mtu alibaki akimtazama tu baada ya kumwambia yale maneno.
Sasa mbona hamuondoki…?
“Sasa tunataka kukuonesha kuwa hatutanii juu ya haya tuliyokuja kukueleza Abiah. Utakapokwenda kinyume na maelekezo yetu, utapatwa na madhila makubwa kuliko haya utakayoyapata hivi punde.”
Nhah? Nini tena…? mbona sielewi…kuna madhila gani tena zaidi ya haya ndigu zangu? Eeh Mungu wangu nisaidie mie….!
Abiah alipagawa.. Na hapo yule jamaa mwembamba aliyemkata kucha kwa namna ya kutisha kabisa, alimkamata kidole chake cha shahada cha mkono ya kushoto na kuanza kukikeremsha taratibu kisu cha kuelekea kwenye kidole kile.
Oooh, sasa nd’o wanan’kata kidole!
Alijikukurusha kwa nguvu pale kitandan huku akigumia kwa taabu, mate yakimpalia kooni kutokana na kuzibwa mdomo na ile plasta kubwa. Alilia kwa uchungu na maumivu ya hali ya juu wakati yule jamaa akimng’oa kucha yake ya kidole kile kwa kutumia kile kisu.
Lilikuwa ni tendo lililohitaji roho mbaya sana kulitekeleza, lakini yule jamaa alikuwa akilitekeleza kama kwamba alikuwa akimpaka rangi ya kucha tu, uso wake ukiwa mtulivu, usioonesha hisia yoyote.
Lah!
Mwanamama alilia kwa sauti iliyokuwa ikitoka kwa miguno isiyoeleweka huku mate yakizidi kumpalia, alishuhudia kucha yake iking’olewa huku damu ikimwagika kwa wingi sana. Alifumba macho lakini bado uchungu ulikuwa palepale.
Jamani si bora nife tu…!
Maumivu yalikuwa ni makali mno kuvumilika. Wakili Abiah Byabato akapoteza fahamu.
____________________
Alipozinduka wale watu hawakuwepo. Huku akihisi maumivu makali mkononi, alijitahidi kujiinua kutoka pale kitandani na kukaa. Zile kamba alizokuwa amefungwa hazikuwepo na ile plasta aliyobandikwa mdomoni ilikuwa imetolewa. Redio kaseti yake ilikuwa imetupwa sakafuni ikiwa wazi, kaseti iliyokuwa na maelezo ya Jaka haikuwemo.
Shuka lake pale kitandani lilikuwa limetapakaa damu.
Wakili Abiah Byabato alijikunyata pale kitandani na kuanza kulia kwa sauti. Alilia kwa muda mrefu sana huku akitetemeka.
Wale ni watu gani?
Kwa nini walitaka Jaka aadhibiwe kwa kosa ambalo hakulifanya?
Iwapo wameweza kumnyofoa ukucha bila hata ya kuonesha kujali hata kidogo, watashindwa kumuua?
Alijikongoja hadi bafuni ambako alijisafisha na kujifunga kile kidole kilichoathiriwa kwa bandeji iliyokuwa mle ndani mwake, kisha usiku ule ule aliwasha gari na kujipeleka hospitali, machozi yakimbubujika njia nzima.
Kulipopambazuka na akiwa tayari ameshapata matibabu ya lile jeraha aliloachiwa an wale watu, alimuelekeza katibu muhtasi wake kuandika barua ya kujitoa uwakili wa Jaka kwa sababu za matatizo ya kiafya.