Riwaya: Mkoloni Mzawa

Riwaya: Mkoloni Mzawa

RIWAYA: MKOLONI MZAWA—2
MTUNZI: HASSAN MBONECHE
SEHEMU YA 27.

IMEPITA miaka mitatu na miezi tisa, tangu ahukumiwe kifungo cha maisha jela kwa kosa la kufanya mauaji ya kukusudia ya halaiki waliyopo kwenye maandamano jijini Nufaiko. Mazingira ya magereza yakambadilisha, kwa kupoteza muonekano wa sura na umbo kwa ujumla. Hakuwa yule aliyezoeleka kuonekana machoni mwa watu wengi. Brigedia Jenerali Mstaafu Bakari Kiboko.

Mkasa ulioibua kisa cha kwenda gerezani ni mahusiano. Mahusiano aliyoyaanzisha na kigogo mmoja wa wilaya. Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Butu. Binti, mwali, m-dada akadiriwaye miaka thelathini na nne. Afahamikaye kwa jina la Siwema Ndomondo.

Hisia zake kwa binti huyu zilimponza. Kwani aliingilia kati penzi la pembeni la mtawala wa taifa lao, Rais Sharabu. Alionywa, lakini hakuwa radhi kuonyeka. Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko aliweka kibri, kilichopelekea manyanyaso mwisho wa siku. Alipata manyanyaso kwenye familia, akapata manyanyaso kazini. Ya kazini yakaleta chuki, iliyomshikiniza kustaafu jeshi kwa hiyari.

Alistaafu, huku akiwa na kisasi dhidi ya Rais Sharabu na serikali yake kwa ujumla. Kwa kifupi, penzi lilimjutisha. Penzi lilimfanya afilisike na kumpotezea heshima mtaani.

Ilikuwa ijumaa, siku moja nyuma kabla ya kufikia siku ya uchaguzi mkuu wa Tuleane. Mazingira ya gereza kuu la Nufaiko yalibadilika. Siku hiyo kulikuwa na ulinzi mkali wa askari wa jeshi la Magereza kuzunguka viunga mbalimbali. Palikuwa na kikao cha maafisa waandamizi kutoka Makao Makuu ya jeshi hilo na wengine kutoka pale Magereza.
“Nadhani mulipokea wito kutoka makao makuu...” kiongozi wa kile kikao alisema.

Waandamizi kutoka pale magereza walijibu kwa kutingisha kichwa; juu-chini.

“Hivyo atasafirishwa mchana wa leo hii. Mkuu wa gereza, andaa utaratibu mapema, ili huyu mtu awasilishwe kwa wakati katika lile gereza lingine.”

Mkuu wa gereza aliinuka alipoketi, alipiga saluti na kutokwa na kauli, “Hamna shida afande. Tumeshafikia hatua ya mwisho ya maandalizi yetu. Nakuhakikishia, kufikia mchana wa leo, saa saba, tutakuwa tumeianza safari.” Akaketi.
“Musipoteze miadi.”

Kikao kikahitimishwa.

Baadaye wale maafisa waandamizi kutoka makao makuu waliondoka. Maafisa waandamizi wa pale pale magereza wakaanza kuwajibika juu ya kile kilichokuwa kinajadiliwa kikaoni.

Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko alipaswa kuhamishwa gereza.

***

Saa saba mchana ilivyowadia tayari Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko alitolewa gerezani na kupakizwa ndani ya gari, basi. Ambalo hutumika mara kwa mara kusafirisha wafungwa. Zaidi yake, kulikuwa na askari wanne kutoka kitengo maalumu cha kutuliza ghasia magerezani, pamoja na dereva.

Achilia mbali askari hao, kulikuwa na magari manne ya usindikizaji; mbele mawili, nyuma mawili, yote yakiwa yamesheheni askari wa ulinzi, waliokamatia bunduki mbalimbali za kivita. Na kufanya jumla ya msafara wa magari matano.

Saa 7:15 mchana safari ilianza, kwa mwendo kasi uliosafishiwa njia na ving’ora. Kila mmoja akimuomba Mwenyezi Mungu, wawe na mwisho mwema wa safari yao.

Ilikuwa ni safari yenye kutumia kilomita mia nne, kutoka gereza kuu Nufaiko hadi kufikia ukomo, gereza kuu Liamba. Gereza lililoaminika na kusifika kuwa ndilo gereza pekee gumu nchini Tuleane. Baada ya mwendo wa takribani nusu saa, waliuacha mkoa wa Nufaiko na kuingia mkoa wa Ndwika, hata kabla hawajaifikia Maswera, msafara ukavamiwa.

Ulivamiwa na maharamia, waliojidhatiti ki-mashambulizi ya kutumia bunduki.

“Tumevamiwa. Take cover, take cover,” mmoja kati ya askari magereza aliwaamrisha wenzie. Waliteremka kwenye magari na kutafuta maficho yatakayowasaidia dhidi ya wapinzani wao. Ambao walikuwa wanne tu.

Namna walivyojipanga wavamizi iliwarahisishia kupeleka moto mkali kwa maadui zao. Waliwashambulia wale askari magereza utadhani hawana mafunzo yoyote ya kimedani. Ndani ya dakika mbili tu, waliwamaliza wote ambao walikuwemo kwenye gari za usindikizaji. Wakasalia wale wa kwenye basi.

Kabla hawajateremka, walimsaili kwanza Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko pale alipofungwa. Naye aliwarudishia jicho la namna hiyo hiyo ambalo wao walipata kumtolea. Ki-ujumla walishangaana. Nini sababu ya tukio hilo kutokea?

Pasi na papara, ijapokuwa walikuwa wenye hofu tele, wale askari walipiga hatua hadi mlangoni ikiwa njia ya kujiokoa kwa upande wao.

Likawa kosa.

Kwani muda huo huo, wavamizi wawili walitoka kwenye pointi zao na kusogea hadi usawa wa mlango. Wakatega kilipuzi na kusogea pembeni.

Kule pembeni hawakukaa kizembe. Walikaa mkao wa uvamizi mara tu kilipulizi kitakavyolipuka. Ikawa hivyo. Haikuchukua muda mrefu, ulitokea mlipuko mdogo ulioambatana na kishindo kuelekea ndani ya gari. Pasi na kusahau moshi.

Wavamizi walitumia nafasi hiyo kuingia ndani, na walivyokuwa makini, hawakuwaacha wale askari magereza wajitafutie pumzi kutokana na ule moshi. Waliwawasha chuma, baadaye walimfungua Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko pale alipofungwa, wakatoka naye nje.

Moja kwa moja walienda kumpakiza garini mwao. Ambayo waliiegesha mita chache kutoka eneo la mapambano.
“Mpe ulinzi. Asikukimbie, sisi tunaenda kusafisha eneo la tukio,” mvamizi mmoja wapo alisema. Akimwambia mwenzie aliyeketi nyuma ya usukani.
“Hamna shida mkuu, nipo makini, hivyo hawezi kunitoka kizembe.”

Wavamizi watatu wakarejea eneo la tukio.

Usafi walioufanya eneo la tukio ni kuondoa miili ya wafu. Waliibeba na kutupia maporomokoni, walifuatia kuyasukumizia magari na kurusha makombora kadhaa kuyaelekezea.

Walivyojiridhisha pako shwari walielekea lilipo gari lao, dereva aliungurumisha injini na kuondoka.

Muda mchache baadaye, ulioruhusu kusambaa kwa habari za tukio hilo, kisa cha tukio kikageuzwa. Kila chombo cha habari kilitangaza kuwa msafara huo umepinduka na kusererekea maporomokoni. Huko kilifuatia kitendo cha kulipuka. Wahusika wa uvamizi waliratibu hili kwa umakini wa hali ya juu, hawakutoa nafasi ya aina yoyote ya shaka.

Uhalisia wa tukio haukuelezwa, ukizingatia muda wa tukio hakukuwa na pita pita za vyombo vingine vya usafiri. Viluzuiliwa na askari wa usalama barabarani maeneo ya mjini, kwa kisingizio cha kuepusha usumbufu kwa msafara husika.

***

Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko alifikishwa kwenye jengo la kifahari ndani ya jiji la Nufaiko maeneo ya Bondeni. Hakuisha kuwa mwenye mshangao, na maulizo mengi aliyoshindwa kuyapatia ufumbuzi, lakini kamwe hakukenua kingo za mdomo kuwatupia swali wale wavamizi.

Klichomfanya ashindwe kuwauliza alifahamu, watu hao sio wabaya kwa upande wake. Kwani laiti kama wangelikuwa wabaya, wasingelimuokoa na kuendelea kumfanya aishi. Kama hiyo haitoshi, wavamizi hawakumsemesha jambo lolote toka mwanzo wa safari hadi hapo walipofikia.

Muendelezo wa imani ya kuwa watu hao sio wabaya, walimpatia huduma nzuri ya malazi. Huduma iliyomfanya ang’ae na kuonekana kama nuru gizani.
“Jiandae ki-akili, kesho kuna mtu utaenda kuonana naye,” kiongozi wa kundi la wavamizi aliongea. Wakati huo Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko akiwa amestopisha hatua alizokuwa anazipiga kuelekea chumbani kulala. Aliitafakari kauli hiyo, akaitafakari pia siku aliyoelezwa; siku mahususi kwa zoezi la upigaji kura. Siku ya uchaguzi.
“Ndiyo muhusika wa huu mpango?” Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko aliuliza.
“Hujapewa nafasi ya kuzungumza, hivyo acha kimuhe muhe.”

Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko alimsaili yule mvamizi aongeaye kisha aliondoka. Hakumpatia picha, huku akiwa mwingi wa shauku ya kumfahamu huyo atakayeenda kuonana naye, na nini sababu ya kuokolewa.

Asubuhi kulivyopambazuka, hata kabla hawajapata stafutahi, wale wavamizi walimtwaa Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko wakaondoka naye. Safari yao haikuwa mbali sana na pale walipokuwa awali. Ulikuwa kama umbali wa mita mia mbili themanini, wakaegesha gari lao ndani ya nyumba ya kifahari yenye mfanano na ile waliyotoka.

Walimteremsha Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko, kisha waliongozana naye hadi ndani ya jengo. Ukomo wao ulikuwa sebuleni.

“Karibuni sana,” mwenyeji wao aliwalaki.
“Tumeshakaribia bosi,” kiongozi wa wavamizi alijibu kwa niaba.

Mwenyeji aliwaonyesha sehemu ya kuketi, lakini wale wavamizi hawakutaka kuketi. Walimuongoza Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko wapi aketi, baadaye waliondoka.

“Karibu sana kamanda,” yule mwenyeji aliongea, akiwa anamkabidhi Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko kikombe cha chai ya kahawa. Naye kuipokea, mboni kazitumbua pima kumsaili mwenyeji wake.

Hakuamini!

Kama zoezi lote lililofanyika ni kwa ajili ya kukutanishwa na huyo mtu. Rais Sharabu.

Akapandwa na hasira. Ambazo zilifahamika kwa haraka akilini mwa Rais Sharabu. Hasira zilizomfanya afikirie, kutolewa kwake gerezani ni kwa sababu maalumu yenye manufaa kwa Rais Sharabu. Mtu ambaye amemfanya aishi kwa tabu na kufikia hatua aliyopo, anaanzaje kumsaidia?
“Punguza jazba ili tuelewane,” Rais Sharabu alifungua uwanja wa mazungumzo.
“Umesahau nini maishani mwangu?”
“Tulia. Tulia, sasa sio muda wa wewe na mimi kuwa maadui.”
“Una maanisha nini? Au kuna yeyote ambaye kwake jua limezama mapema hivyo haitaji kuona likichomoza siku ya kesho?”
“Ndiyo maana nimekuhitaji.”
“Sio muumini wa ushiriki wa hizo kazi kwa sasa. Na kingine, ewe ndiyo adui yangu pekee hapa duniani.” Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko alisema na kugida funda kadhaa za chai.
“Okay! Tuachane na hayo. Nina zawadi nahitaji nikupatie,” Rais Sharabu alichomoa mkanda wa CD, kutoka kwenye begi ndogo aliloliweka jirani na pale alipoketi, akamkabidhi Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko. Kisha aliendelea na kauli, “Nenda kaitazame, ukishamaliza, utanipatia majibu ya kile utakachokutana nacho. Pasi na kusahau hitajio langu.”

Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko alinyanyuka na kuondoka. Alipofikia mlango Rais alitokwa na kauli iliyosheheni msisitizo, “Endapo utaafikiana nami, kupitia hicho utakachokiona, mjulishe mlinzi atakayekuwa anasimamia usalama wako huko utakakopelekwa.”

Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko hakujibu. Aliishia kumwangalia, baadaye aliendelea na safari. Alivyofika nje, aliingia ndani ya gari waliyotumia awali kisha aliwaamuru wale wavamizi wamrudishe. Nao hawakuwa na hiyana, walimrudisha kwenye lile lile jengo la awali.

Alirudi akiwa mwenye kughafirika. Hakupendezwa na dhihaka alizofanyiwa na Rais Sharabu. Yaani juu ya utu uzima wote alionao, anataka amuendeshe kama mtoto mdogo!

Jambo la kwanza mara baada ya kuwasili aliweka ule mkanda wa CD kwenye deki na kuangalia picha jongefu iliyopo. Alistaajabu alichokiona, familia yake ilishikiliwa. Fika akafahamu, Rais Sharabu ndiye mwamuzi wa mipango yote hiyo.

Alichanganyikiwa.

Kiasi cha kutomaliza kuitazama, akaamua kumfuata mlinzi na kuomba miadi ya kukutanishwa na Rais Sharabu.
“Mwambieni huyo mbwa wenu, nahitaji kuonana naye haraka iwezekanavyo na asifanye jambo lolote kwa familia yangu,” Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko alisema akionekana mwenye jazba isiyotatuzuka.
“Ujumbe wako umefika. Hivyo urudi ukapumzike pindi unafanyiwa kazi.”

***

Uchaguzi ulifanyika kwa amani. Babigamba akaibuka kidedea. Nafasi ya wabunge na madiwani, chama tawala na kile cha upinzani vikatofautiana idadi ndogo ya uwakilishi. Ijapokuwa chama tawala ndicho kiliongoza.

Baada ya siku kadhaa iliandaliwa hafla ya uapisho. Hafla iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa ndani na nje ya nchi. Rais Sharabu alikuwa mmoja wao. Alihudhuria akiwa na kijiba cha roho. Lakini kabla hajaelekea eneo la tukio alikutana na Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko kwenye ile ile nyumba waliyokutana siku zilizopita.
“Nina uhakika tayari umeshatazama?” Rais Sharabu alifungua mjadala wa mazungumzo.

Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko hakujibu kwa uharaka. Alijitafakarisha kwa sekunde chache, huku akiuma uma kingo ya chini ya mdomo na kutikisa kichwa. Baada ya sekunde chache, tafakuri yake ilipoisha ndipo alijibu, “Yeah!” Sauti ikiwa kavu. Sura kaikunyata mithili ya katuni wa kuchorwa.
“Jibu halijajitosheleza.”
“Nipo tayari. Lakini acha kucheza na familia. Acha kucheza na familia yangu wewe mbwa.”

Rais Sharabu aliangua cheko la dhihaka. Kwa muda mfupi kisha alimgeukia Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko. Alipiga hatua moja mbele, alipomfikia, alitumia moja ya mkono wake kukamata bega.
“Usijali. Chukua hii,” Rais Sharabu alisema na kumkabidhi Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko kikaratasi kidogo kilichokunjwa.

Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko alikikunjua kile kikaratasi, akakumbana na maandishi machache yaliyompigisha moyo kite kwa mshangao. Aliinua uso, akamwangalia Rais Sharabu kwa sekunde chache kisha alirejea kuangalia yale maandishi.
“Kama kweli unahitaji heshima kwa familia yako. Hauhitaji kuchezewa, huna budi kutekeleza hilo.” Rais Sharabu akaondoka kuelekea kwenye sherehe za uapisho.

Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko akabaki kutumbulia yale maandishi.

***

Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko aliandaa vijana na kuwapatia mafunzo ya medani za kivita. Mafunzo hayo yalifanyika kwenye moja ya msitu mkubwa uliopo mkoani Ndonya. Juu ya hilo, yalifanyika usiku kucha. Huku washiriki wengi wakianzia umri wa miaka kumi na mbili na mwisho mwenye umri wa miaka thelathini na tano.
“Tufanye haya maazoezi kwa morali ya juu, ili siku tutakayoenda mjini, tuuonyeshe uhodari wetu,” mara kwa mara Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko aliwaasa vijana wake.

Hakika, hayakuwa mazoezi ya kizembe. Yalikuwa mazoezi haswa, yaliyohusisha mbinu zote za kijeshi na matumizi ya silaha za kivita. Kwani sio bunduki, risasi, mabomu wala makombora, kwao yalisheheni. Mtu ambaye alikuwa nyuma ya Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko, hakuwa wa mchezo. Ni zaidi ya mwenye mamlaka na ukwasi wa kutosha.

Baada ya miezi kadhaa, Brigedia Jenerali Mstaafu Kiboko alifanya tathmini ya mafunzo kwa vijana wake. Aliangalia maonyesho mbalimbali yaliyoandaliwa, alivyomaliza, alienda ofisini kwake, alifungua moja ya droo akachukua kile kikaratasi alichopatiwaga na Rais Sharabu. Ambaye kwa wakati huo alikuwa mstaafu. Akarudia kusoma yaliyoandikwa.
“Sitaki kuona Babigamba akitawala kwa amani. Hivyo hakikisha, Tuleane inanuka kwa matendo ovu yaliyobeba ugaidi.”

Baadaye alikigeuza na kuangalia upande wa nyuma. Alikutana na maandishi mengine, yaliyobeba mikakati anayopaswa kutekeleza. Alichukua kalamu na kuweka tiki kwenye mkakati wa kwanza, kuonyesha tayari ameshaufanyia kazi.

ITAENDELEA...

HABARI NJEMA

KITABU CHA RIWAYA YA NENDA SASA KINAPATIKANA RENICS BOOKSHOP TAWI LA MOSHI KWA GHARAMA YA TSH. 10,000/= MAWASILIANO: 0767826134
Ni shida juu ya shida
 
AFRIKA YANGU

MTUNZI: HASSAN MBONECHE

Mwanga wa kibatari haukuweza kuleta nuru chumbani. Mwanga mdogo, ulioashiria utambi umeshindwa kunyonya mafuta ya kutosha kwa sababu ya upungufu. Mafuta yalikuwa yanaelekea kuisha.

“Mwanangu, chukua hii bahasha, na ufanye hima kuondoka hapa nchini. Kilichomo ndani ndiyo mkombozi wa maisha yako, usikipuuzie,” ilisikika sauti kutoka kwa mama aliyelala kitandani ndani ya kile chumba. Maneno ya nasaha kumwendea bintiye aliyeketi chini kando ya kitanda. Ilikuwa sauti iliyojaa unyonge.

“Mama, si tuondoke wote.”

“Nitaenda wapi na hii hali mwanangu?”

“Sasa nami nitawezaje kutoka? Kwanza nitaelekea wapi?”

“Tanzania.”

“Tanzania!”

“Ndiyo. Huko kuna amani ya kutosha ambayo tunaililia hapa.”

“Mmmh! Mama, siku zote ulikuwa unaniepusha na kifo dhidi ya hawa mabaradhuli, sasa nikitoka humu ndani si ndiyo nitauwawa? Na nitafikaje Tanzania ilhali mimi ni wa hapa hapa usiku kucha?”

“Mwanangu. Naomba unielewe, hayo yaendeleayo huko nje sisi ndiyo chanzo, hasa baba’ako. Sasa ameshauwawa, wabaya wake wamegeuzia majeshi kwetu wakiamini kile walichokuwa wanakihitaji kwake kipo kwetu...”

“Wanahitaji nini?”

“Ndiyo maana ninakuhitaji uende Tanzania...” yule mama hakumalizia kuongea, mwanaye akamkatisha.

“Tanzania, sehemu gani?”

“Kigoma. Kambi ya wakimbizi Nduta.”

“Mama, napata hofu, una uhakika nitafika salama?”

“Kwa uwezo wake Mwenyezi Mungu. Na ukishafanikiwa, kamtafute mtu anayeitwa Richard Mugaza.”

“Halafu?”

“Utamkabidhi hiyo bahasha.”

“Mama.”

“Hakuna jinsi mwanangu, yakupasa uondoke.”

Binti alizungumza chozi likimtiririka, “Kwa hiyo, kwa hiyo hutaki nikuone...”

“Ondoka haraka, wasije wakakukuta.”

Binti hakuwa na hiyana. Ijapokuwa alikuwa mwingi wa unyonge pindi anatekeleza alichoambiwa. Alinyanyuka alipoketi, akaiweka vyema khanga aliyojifunga kwa mtindo wa chingolingoli na kupiga hatua hadi dirishani. Dirisha lililofunikwa kwa pazia ya kitenge. Ile bahasha aliikamatia mkono wake wa kushoto.

Alisimama pale dirishani takribani dakika moja. Muda wote akionekana kutafakari jambo, lililomshinikiza kutega masikio vyema asikilize kitendekacho nje.

Kulitawala makelele.

Baadaye alifunua lile pazia na kushuhudia kilichochangia makelele aliyoyasikia. Alipigwa na butwaa, namna raia wa kijiji chao walivyokuwa wanahangaishwa kutoka kwenye makazi yao na kusundikwa sehemu moja. Sehemu ya uwazi.

Heri tolewa hiyo ingelikuwa ya amani. Lakini haikuwa hivyo. Walikuwa wanapigwa, na kuangushiwa maswali lukuki, ambayo wengi wao jibu lilikuwa moja tu, hatufahamu walipo.

Watu waliokuwa wanafanya hayo hawakutofautiana na wapiganaji wa mwituni, mavazi na zana walizobeba ziliwatambulisha. Walikuwa wamebeba mapanga, rungu na silaha chache za kienyeji.

“Familia ya Ndiyashena inaishi wapi?” aliuliza mmoja wa wale wapiganaji wa msituni. Swali kwenda kwa mama aliyemkamata pasi na kujali kama anavunja staha na thamani ya yule mama. Alimtoa ndani akiwa amevaa chupi pekee.

Mapambo ya hubani yakiwa yamejiachia. Lilikuwa fungu la kutosha. Shanga!

Lile tukio liliteka akili ya binti. Kiasi kwamba hakuwa makini na mengineyo. Mama’ke ndiyo alimgutusha kutoka kwenye hali hiyo, “Mwewe akosapo kifaranga windoni, huondoka na kitu chochote kilichopo jirani.”

Binti akafunika pazia na kumgeukia mama yake.

Alimtupia swali akiwa anapiga hatua za kumfuata, “Unamaanisha nini?”
“Kama nilivyokuambia mwanzo, wabaya wa baba’ako hawawezi kutuacha salama.”

“Lakini mama...” binti aliongea, kabla hajahitimisha sauti ya kukitwa kwa kitu kizito ikasikika mlangoni. Sauti iliyoashiria mlango unavunjwa.

Kwa pamoja, walishtushwa na ile hali. Kwani hata yule mama alijiinua kidogo pale kitandani na kuzitupa mboni za mashaka kwa bintiye.

Wakatazamana kwa muda.

Haikuzidi dakika moja, mtazamo uliotoa picha kila mmoja yupo kwenye mafikirio ya kile kiendeleacho nje ya mlango wao. Walivyokuja kuzinduka, binti alipiga hatua chache za haraka hadi kilipo kibatari, akakizima.

“Unataka kufanya nini?” mama’ke aliuliza kwa unong’ozi. “Nilishakuambia ondoka ukaleta ukaidi. Unaona sasa matokeo yake?”

Binti hakujibu. Badala yake alinyata taratibu hadi usawa wa mlango, akaweka tuo pembezoni, wakati huo hofu na ujasiri vimemkumbata kwa pamoja.

Jirani na pale aliposimama kulikuwa na mwichi, aliuvuta na kuukamatia kwa umahiri kabisa. Lengo, yule atakayethubutu kuingia, kipigo kiwe halali yake.

Kweli.

Mlango ulivyofunguka tu, alimuona mtu akiingia kwa kunyata mle ndani. Alivyopiga hatua moja kutoka mlangoni, yule mvamizi aliwasha tochi kufukuza kiza kilichopo.

Mwanga ukambainisha mama wa yule binti pale kitandani. Alikuwa amekaa kwa kutojiweza.

“Waaoooh!” mvamizi alipiga ukunga wa ushindi, na kunuia kupiga hatua kumfuata.

Kabla mguu haujatua, binti akatii dhamirio lake. Aliuinua ule mwichi na kuupigiza kichwani kwa mvamizi. Mvamizi akatoa mguno na kupata shinikizo la kuangalia kipigo kilipotokea. Aligeuka nusu, binti akapigiza mwichi kwa mara nyingine. Ukatua kwenye pembe ya jicho la kulia la mvamizi.

Hakuyahimili maumivu, na msukumo wa kile kipigo, alianguka chini, tochi nayo ikijipigiza na kuzima.

“Ondoka sasa mwanangu,” mama alimsihi bintiye.

“Tuondoke wote mama.”

“Tukiondoka wote hatutofika mbali, watatukamata.”

Kauli ya mama’ke ilimfikirisha kwa muda kabla hajachukua maamuzi. Alikuja kuzinduliwa na sauti itokayo nje, nyumba jirani na pale walipo. Sauti ya kiume iliyosikika ikiita. Muito uliompa utambuzi anayeitwa ni yule aliyelala pale chini akiugulia.

“Mugoo! Mugoo!” iliendelea kusikika ile sauti kutoka nje. Awamu hii ilisikika karibu zaidi.
“Ndinaa ondoka,” yule mama akapaza sauti kwa kujikakamua. Kwani hali yake kiafya si ya kumlazimu kutumia nguvu kwenye matumizi ya aina yoyote.

Mwambiwa, yule binti, afahamikaye kwa jina la Ndinaa alitoka kasi pale alipo hadi kitandani, na kumshushia mvua ya mabusu mama’ke.

“Mwenyezi Mungu akulinde mama’ngu. Naamini, kwa uwezo wake, tutaja kuonana kwa mara nyingine.” Ndinaa akaondoka. Lakini sio kwa mapendo ya dhati nafsini mwake.

Alivyofika nje hakujali yaendeleayo. Alikata kona na kupotelea nyuma ya nyumba yao. Mwendo wake ulikuwa mbio. Mbio zilizoshinikiza hofu kumtawala nafsini mwake, kwa kuamini nyuma kuna anayemfuatilia. Yule mtu aliyekuwa anamwita mwenzake.

Akiwa umbali kama wa mita mia moja na ishirini alisimama ghafla na kujikuta akivuta hisia. Kuna milio ilisikika. Milio iliyomwaminisha ni milio ya risasi. Risasi zinazotua kwenye mwili wa mama’ke.

“Mama! Mama! Mama!” Ndina aliita, taratibu akiketi chini pasi na uridhiaji. Machozi yakimlenga, mate yakimjaa mdomoni. Nafsi ikitukuta kwa maumivu.

***

Ubaridi wa kiyoyozi ulikonga nyoyo za viongozi waandamizi wa mataifa ya Tanzania na Burundi ndani ya ukumbi wa mikutano Ikulu ndogo mkoani Kigoma. Iliyopo maeneo ya Bangwe mjini Ujiji.

Viongozi waliopata kuwepo ni marais wa mataifa yote mawili; Tanzania na Burundi-Cosmas Luambano na Franké Nibizi. Wengine; Mawaziri, wa Burundi na Tanzania.

Kwa upande wa Burundi, walikuwepo Waziri wa mambo ya nje na maendeleo ya kimataifa, Jean Mutazi, Waziri wa ulinzi, Galus Ndirako na Waziri wa mambo ya ndani, maendeleo ya jamii na usalama wa umma, Albert Shingizi.

Tanzania, waliwakilishwa na Waziri wa mambo ya ndani, Ndg. Khatib Nalimuka na Waziri wa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa, Mariam Batani. Pasi na kuwasahau wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama.

“Bwana Nibizi, karibu sana Tanzania,” Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania, Cosmas Luambano alisema.

“Nimeshakaribia mheshimiwa. Sio mara yangu ya kwanza kuja hapa, hivyo ni mwenyeji.” Wote wakaangusha tabasamu.

“Tusipoteze muda...” Rais Luambano alishauri, kabla hajamalizia kauli yake, Rais Nibizi akamkatisha.

“Kama nilivyopata kuteta nawe hapo awali, nina mpango wa kudumisha amani nchini kwetu. Hivyo nahitaji warundi wote waliopo kwenye mataifa mengine wawe sehemu ya kufurahia amani ya taifa lao.”

Rais Luambano akaingilia kati, “Ina maana unahitaji wakimbizi wote warudi nchini?”

“Sahihi,” Rais Nibizi aliitikia na kukazia kwa utingishaji wa kichwa.

“Ni wazo zuri. Na hongera sana kwa kuamua jambo hilo.”

“Nashukuru. Lakini kuna harufu inayofukuta ambayo imenilazimisha kuhitaji msaada kwako.”

“Ipi?”

“Baadhi ya viongozi waandamizi wa serikali yangu nadhani hawajafurahishwa na uamuzi huu. Vilevile viongozi wachache kutoka Rwanda.”

“Kwa nini unahisi hivyo?”

“Kuuwawa kwa Jenerali Ndiyashena.”

Rais Luambano alivuta pumzi na kuzitua kwa nguvu, kisha alitoa ulizo. “Kwa hiyo unahitaji tukupatie msaada gani?”

“Usalama.”

Jibu alilopatiwa Rais Luambano lilimshinikiza awasaili wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama kisha kuwatazama mawaziri wa Burundi. Kitendo kilichozalisha ukimya kwa muda mfupi.

“Wanapata wapi nguvu hao watu unaohisi wanapinga wazo lako?” Rais Luambano aliuliza.

“Hakika sifahamu,” Rais Nibizi alijibu kwa sauti yenye mchanganyiko wa aibu.

Jibu hili lilitengeneza ukimya kwa mara nyingine, uliomfikirisha Rais Luambano.

“Nakuomba,” Rais Nibizi alisema na kumtoa Rais Luambano tafakurini. “Msaada wako ni wa muhimu kwetu. Tusaidie, kama ilivyo desturi yako ya kuona bara zima linakuwa tulivu.”

“Mmh, siwezi kukupatia jibu la moja kwa moja. Nipe muda, at least one second to think it. Na vipi, ulijaribu kuwasiliana na wakuu wa serikali ya Rwanda kuhusu hao maafisa wao?”

“Hawajatoa ushirikiano wa kuniridhisha ndiyo maana tumekuja kwako.”

“Okay, tuachie.”

***

Alikuwa ameshajitayarisha kulala kabla hajakatishwa na muito wa simu’ke ya mkononi ambayo aliihifadhi juu ya meza ikichajiwa. Awali aliipotezea, lakini ilivyoita kwa awamu nyingine, alijiaminisha ni simu ya umuhimu ndiyo maana mpigaji amerudia mara ya pili.

Ile imani ya umuhimu, ikamfanya ainuke kitandani hadi alipoihifadhi. Alilisaili kwa muda jina la mpigaji, na kumfanya asisimkwe mwisho wa usaili wake. ‘Chief' ndivyo lilivyosomeka jina la mpigaji.

“Leo imekuwa tofauti!” yule mtu alisema mara baada ya kupokea. Alikuwa mwanaume; aliyepambwa kwa rangi nyeusi, mrefu wastani, mnene kiasi.

“Nakuhitaji jijini Dar es salaam siku ya kesho,” ilisikika sauti ya mtu wa upande wa pili. Sauti iliyojaa amri.

“Ku’nini?” aliuliza, lakini hakujibiwa. Mtu wa upande wa pili akakata simu.

Hakuwa na budi, aliirejesha simu ilipokuwa awali, huku wajihi ukibadilika taratibu kutokana na amri aliyopatiwa. Ilionekana kumfikirisha.
“Maelekezo ya leo yamekuwa yakibabe sana,” alijisemeza, akiwa anapiga hatua taratibu. Ukomo, ulikuwa mbele ya kabati. Alitekenya kidogo ufunguo, upande mmoja wa mlango wa kabati ukafunguka.

Aliangalia kwa muda kile kionekanacho, baadaye alipiga hatua moja mbele na kuanza kukishika shika. Lilikuwa vazi nadhifu, chini lilipoishia, kulikuwa na kitabu cha biblia na rozali. Alitumia takribani dakika mbili, baadaye aliufunga ule mlango na kurejea kitandani. Akausaka usingizi.

***

Mnamo saa 8 adhuhuri siku iliyofuata yule mtu aliyepigiwa simu, akiwa kwenye yale mavazi aliyoyashika shika jana usiku aliteremka ndani ya basi kituo kikuu cha mabasi yaendayo mikoani, Ubungo, jijini Dar es salaam.

Alikuwa amefunga safari kutoka mjini Mtwara.
Mkononi alikuwa amekamatia begi dogo jeusi, ambalo lilitoa ubainisho halina vitu vingi ndani. Kwani lilipwaya.

“Tumsifu Yesu Kristo,” ilisikika sauti kutoka upande wa kushoto pale aliposimama pindi akiyaangazia mazingira ya kituo.

“Milele amina,” yule mtu alijibu huku akigeuka kumwangalia aliyemsabahi. Alikuwa kijana wa makamo.

“Nipo kwa mapokezi yako Askofu,” yule kijana alimtaarifu.

“Ooh, nashukuru sana.” Akamkabidhi kile ki-begi yule kijana. Baada ya hapo wakapiga hatua taratibu za uondokaji.

Mavazi aliyovaa msafiri yalimbainisha kuwa yeye ni Askofu. Na hakika ilikuwa hivyo. Alikuwa Askofu. Askofu wa Dayosisi ya Mtwara. Akifahamika kwa jina la Ponera Haule.

Ukomo wa safari yao ulikuwa eneo la maegesho la magari madogo mle mle ndani ya kituo. Wakaelekea kwenye moja ya gari, aina ya Toyota Hilux double cabin rangi nyeupe, iliyopambwa kwa maandishi yenye wino mweusi ubavuni, CATHOLIC ARCHDIOCESE OF DAR ES SALAAM, wakaingia na kuyaacha mazingira ya pale kituoni.

“Naona mazingira ya jiji yanazidi kubadilika kila uchao,” Askofu Ponera alisema baada ya kupita kitambo kidogo cha ukimya.

“Ipo siku ukitoka mkoa na kuja hapa utapotea,” yule kijana alichangia hoja, na kujikuta wakiangusha tabasamu.

“Lakini ndiyo maendeleo.”

“Nasi yatubidi tuende na wakati kama dunia itakavyo. Tusibaki pale pale pa siku zote.”

Maongezi yalikoma walipowasili eneo kusudiwa. Kwenye moja ya nyumba ya kifahari maeneo ya Sokoine Drive 40. Hapo waliteremka garini, na kupotelea ndani ya jengo lilipo mbele yao. Jengo la ghorofa mbili.

Akiwa katika pilika pilika za kusabahiana na wenyeji wake, muito wa simu ulimpoozesha Askofu Ponera na kufanya aikumbuke alipoihifadhi. Aliitoa mfukoni, na kuisaili. Ulikuwa ujumbe.

Akaufungua.

“Leo, saa 5 usiku, Kijitonyama. Bila kukosa.” Ulisomeka ujumbe aliotumiwa.

Haukumfikirisha, badala yake aliirejesha simu alipoihifadhi hapo awali, akarudi tena maongezini.

***

Ilikuwa ofisi kubwa, iliyopambwa na vitu vichache na kufanya sehemu kubwa iwe wazi. Ukiachilia mbali meza ya mbao yenye umbo la msitatili, viti viwili, sofa liwezeshalo kukaa watu wawili, kabati na jokofu hakukuwa na vitu vingine.

Katikati ya ile meza na kabali palikuwa kiti kilichokaliwa na m-baba wa makamo, akadiriaye miaka arobaini na tisa. Fadhy Njau, ndivyo anavyotambulika na wengi. Afisa operesheni ndani ya Idara ya Usalama wa Taifa (TSS-Tanzania Security Service) aliyeumbwa kwa umbo nene wastani, mrefu, mweusi.

Mbele yake, aliketi Askofu Ponera. Mwanga hafifu kutoka kwenye taa iliyofungwa moja ya kuta ikitoa ubainisho wa namna walivyo. Rangi ya nguo walizovaa, na mandhari yote kwa ujumla mle ndani ya ofisi. Ofisi iliyobebwa kwenye jengo la ghorofa moja maeneo ya Kijitonyama.

Muda huo Askofu Ponera alikuwa amevaa kiraia.

“Wito wako ulinishangaza sana ile jana,” Askofu Ponera alisema. Akiwa amevunja mzungu wa nne kitini.

“Ilinilazimu kufanya hivyo. Sikuwa na budi,” Fadhy alimfafanulia.

“Kuna tatizo?”

“Tena kubwa sana.”

Askofu Ponera akatoa mboni zake pima kwa mshangao. Mshangao uliotoa mkazo wa kumtaka Fadhy aendelee.

Fadhy akaendelea, “Mheshimiwa Rais ametutaka tuendeleze desturi tuliyorithishwa na baba wa Taifa, kusaidia mataifa mengine yawapo matatizoni. Nadhani umesikia mnyukano uliopo Burundi...” akatulia.

Kwa msisitizo wa utingishaji wa kichwa, Askofu Ponera aliitikia, “Yeah.”

“Kwa taarifa za ndani, Rais wa sasa wa Burundi ana nia ya kuwarudisha wakimbizi wote nchini kwao. Lakini waandamizi wachache ndani ya serikali yake na nchi jirani ya Rwanda hawajaafikiana na wazo hili...”

Askofu Ponera akamkatisha, “Kwa nini?” Akazidi kuuvaa umakini wa usikilizaji.

“Nadhani kuna maslahi wayapatayo. Hivyo kumekuwa na hisio, kwamba yanaweza yakatokea machafuko yatakayopelekea azma ya Rais isitimilike,” Fadhy alieleza na kutulia kwa mara nyingine.

Ilikuwa pindi anataka aendelee kuzungumza, pale Askofu Ponera alipoingilia kati, “Ukiachana na waandamizi wa Rwanda, kuna wengine wanaoleta msukumo kutoka bara la Afrika wanaohitaji huo mpango usifanikiwe?”

“Hawakosekani, ijapokuwa bado sina uhakika zaidi. Maana si unafahamu, hao watu hawapendi sisi tujitawale kwa amani?”

“Nafahamu. Hawafurahii kabisa tukiwa shwari,” Askofu Ponera alijibu.

“Ndiyo uhalisia. Hivyo tunakuhitaji ukahubiri amani ndani ya Burundi. Tusiwape nafasi ya kututawala tena. Mwanzo waliweza kwa sababu wengi wetu tulikuwa hatujitambui. Lakini leo hii tuna elimu za kutosha vichwani, bado tu wanataka waturudishe enzi zile? Za ukoloni? Hapana,” Fadhy alisema kwa sauti iliyojaa uchungu.

“Askofu, msaada wako ni wa muhimu sana kwa kipindi hiki,” Fadhy alikazia.

Kwa namna maelezo yalivyomwingia Askofu Ponera alikosa neno la kuzungumza. Badala yake alimsaili Fadhy kwa sekunde kadhaa kabla hajatua kwa nguvu viganja vya mikono yake mezani na kuinuka.

Alivyokuwa wima, alipiga hatua taratibu hadi kwenye moja ya dirisha. Alisogeza pazia pembeni na kuyasaili mandhari ya jiji yalivyopambwa kwa mataa ya kila rangi usiku ule. Akilini, maneno ya Fadhy yakiendelea kumtafakarisha.

TUKUTANE TOLEO LIJALO
 
AFRIKA YANGU—02

MTUNZI: HASSAN MBONECHE.

Ubaridi wa kiyoyozi ulikonga nyoyo za watu sita waliopo ndani ya ukumbi mkubwa wa mikutano kwenye hoteli ya Club Du Lac Tanganyika iliyopo eneo la Chaussee D'uvira jijini Bujumbura.

Kwa pamoja waliizunguka meza kubwa ya mbao iliyonakshiwa vyema, iliyozungukwa na viti ishirini na nne. Na kufanya viti kumi na nane kuwa wazi ukiachilia mbali vilivyokaliwa na wao.

Kiongozi wa kikao kile alikuwa m-mama, mwenye asili ya bara la Ulaya akadiriaye miaka hamsini na moja. Umbo lake lilipambwa kwa wembamba wa kati, mrefu. Alifahamika kwa jina la Wilhelmina Filippo. Ni mmoja miongoni mwa maafisa wanaoshughulika katika shirika la wakimbizi (UNHCR- United Nations High Commission of Refugees) nchini Burundi.

Wengine, ambao ndiyo wajumbe wa kikao kile walikuwa watu wenye asili ya bara la Afrika. Walikuwa weusi; wanne kati yao walionekana kuwa makamanda wa kijeshi kutoka jeshi la FDN (Force de Defense nationale) jeshi la nchini Burundi. Mmoja aliyebakia alikuwa amevaa kiraia. Afisa idara inayoshughulikia wakimbizi nchini Rwanda. Alifahamika kwa jina la François Kinigi.

Kwa pamoja, wajumbe hawa walikuwa wanaume.

“Kamanda, operesheni yetu imefikia wapi mpaka sasa?” Wilhelmina aliuliza. Lilikuwa swali kwenda kwa mjumbe wa kwanza aliyeketi kiti cha kwanza mkono wake wa kuume.

“Ondoa hofu, bado ipo kwenye mstari utakiwao. Tumeshafanikiwa kumuondoa duniani Jenerali Ndiyashena, na vijana wameshaanza kufanya kazi kule Gitega. Hivi niongeavyo sasa damu inanuka kiasi cha kukerehesha nafsi. Kamwe, nia ya Frankè haiwezi kutimia,” yule mtu aliyedhamiriwa na lile swali alijibu. Alikuwa mtu mwenye umbo la miraba minne, cheo kilichopo begani kilimtambulisha kuwa yeye ni Brigedia Jenerali. Aliitwa Prosper Buyoya.

“Ili tuzidi kujinoofisha na pesa za umoja wa mataifa ni lazima wakimbizi waendelee kujitokeza kila uchao. Kinigi, assurez-vous qu'il n'y a pas de pression sur les réfugiés qui doivent venir ici.” Wilhelmina alisema kwa mkazo, akimtaka na Kinigi ahakikishe hakuna shinikizo kutoka kwa wakambizi wanaohitaji kurudi Burundi kutoka nchini Rwanda.

“Hilo halina shaka,” Kinigi alihakikisha.

“Brigedia, vipi kuhusu familia ya huyo Jenerali na Mugaza?” Wilhelmina aliuliza kwa mara nyingine.

Familia ya Jenerali ilikimbilia Gitega, ndiyo maana tumeanzia huko kufanya machafuko, ikiwa ni mbinu moja wapo ya kuifuatilia. Kuhusu Mugaza ripota wetu ametuambia huyu mtu hayupo nchini. Inasadikika, amekimbilia Tanzania. Lakini hatutampatia nafasi ya kujitawala, tutamfuata huko na kumzimisha, kama tulivyomzimisha mwenzake,” Brig. Jen. Buyoya alijibu.

Wanajeshi wengine wakatingisha kichwa kuafiki. Ambao ni; Meja Ezekiel Uwizeye, aliyepambwa kwa umbo refu, mwembamba. Luteni Domitien Bazombanza, aliyepambwa kwa umbo fupi na nene kiasi. Koplo Alain Rumera, huyu ni mrefu, mwembamba.

“Niwapongeze, lakini nizidi kuwapa msisitizo, nguvu iongezeke. Ongezeni nguvu, ikiwezekana Burundi yote inuke damu,” Wilhelmina alikazia.

“Hilo halina shida,” Brig. Jen. Buyoya alitii. Kamanda wa operesheni ndani ya jeshi la FDN. Vilevile mdhamini wa kundi la wapiganaji wa msituni lifahamikalo Red Tabala.

Kufikia mafanikio katika utekelezaji Brig. Jen. Buyoya aliigawa timu yake. Alimtaka Meja Uwizeye aende Tanzania kufuatilia habari za Mugaza. Wakati huo huo aliwaamuru Luteni Bazombanza na Cpl Rumera waelekee yalipokuwa makazi ya Jenerali Ndiyashena kufanya upekuzi kama watapata kitu kitakachowasaidia kufuta nyayo zao.

***

Ndege aliyomo Askofu Ponera iliwasili jijini Bujumbura katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Melchior Ndadaye saa 10 jioni, ambayo ni sawa na saa 11 jioni nchini Tanzania.

Kama alivyoingia na kupokelewa jijini Dar es salaam, ndivyo ilivyokuwa huku pia. Akiwa ndani ya yale mavazi yake ya ki-Askofu, alipokelewa na msaidizi wa Askofu Dayosisi ya Bujumbura wakaelekea sehemu ya mafikio, Kanisa kuu la Dayosisi, lifahamikalo Regina Mundi, lililopo umbali wa mita kadhaa kutoka makutano ya barabara ya Chaussee de Gitega, Boulevard du Japan na Ave des Mimosas.

Ulipojengwa mnara wa monument du soldat inconnu.

Uwepo wa Askofu Ponera ndani ya jiji hili ulikuwa na kazi moja tu, kutimiza dhima ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyopatiwa na Fadhy Njau. Kuhakikisha amani inarejea. Hivyo utekelezaji wa dhamira hiyo ilimpasa Askofu Ponera asafiri hadi nchi husika, na kusomeka ameingia kushiriki kongamano la kidini lililoandaliwa na kanisa hilo alilofikia.

Sio pekee aliyeingia kwa minajili ya kongomano hilo. Walikuwepo maaskofu wengine pia kutoka mataifa mbalimbali. Huku likipangiwa juma moja la kufanyika.

Siku ya kwanza ya kongamano hilo, ambayo ni siku iliyofuatia baada ya kuwasili, lilihudhuriwa na watu wengi sana. Sio viongozi wa kiserikali wenye nyadhfa mbalimbali, wala walala hoi, kwa pamoja walijumuika kumtukuza Mungu aiwezeshe Burundi inadumu kwenye amani.

Uhitaji wa kudumisha amani ulikuwa mkubwa sana kwa wakati huo. Hawakuhitaji ididimie, juu ya uwepo wa dhahama chache zilizojichipua.

Karibu na hitimisho kwa siku hiyo pindi maaskofu wanatoa salamu za baraka kwa waumini, Askofu Ponera alipokea bahasha ya wastani kwa siri kutoka kwa kijana mmoja akadiriaye miaka ishirini na saba. Yule kijana hakuwa mgeni kwake, alimfahamu, kwa sababu haikuwa mara ya kwanza kuonana mahali hapo.

Mmoja miongoni mwa maafisa wa ubalozi wa Tanzania nchini Burundi.

Kitu cha kwanza kufanya ndani ya chumba alichofikia kwa kulala mara baada ya kongamano kuhitimisha aliifungua ile bahasha. Akakutana na vitu viwili ndani yake; karatasi ndogo iliyoonekana kuwa na ujumbe ikakunjwa kunjwa pamoja na bastola. Aina ya Glock 17.

Alivutika kwanza na ile karatasi.

Aliikunjua na kusoma yaliyomo.

Kinanira 2, King David Avenue, block 55.

Ndivyo yalivyosomeka yale maandishi.

Maelezo haya yalimfahamisha wapi anakopaswa aanzie misheni yake. Baadaye aliivuta bastola akaichunguza. Kwa kusaili ujazo wa risasi kwenye kisanduku chake, ulaini wa mitambo; kwa kukoki, mwisho, kifyatulio (trigger).

“Uchaguzi makini,” Askofu Ponera alijisemeza, pindi akikirudisha kisanduku cha risasi mahali pake. Akimaanisha mtu aliyemchagulia ile bastola alifanya chaguo sahihi kwa matumizi yake.

***

Ni usiku wa saa sita, Askofu Ponera alipoacha makazi aliyofikia akiwa amevaa kiraia na kula moja moja uelekeo ulikomtaka ule ujumbe kufika.

Muda huo alikuwa amevaa suruali ya jinzi rangi nyeusi, fulana rangi ya njano iliyofifia, kapelo rangi nyeusi, prova rangi ya kijivu na buti kubwa chini rangi nyeusi pia. Kiunoni, alikuwa ameisundika ile bastola yake ikizuiliwa na fulana na prova lililoishia chini kidogo ya kiuno.

Mbele kidogo toka pale yalipo makazi aliyofikia aliita teksi na kumwamuru dereva amfikishe kwenye ule mtaa.

Dereva alitii hitajio lake kwa kuzidisha mwendo ili wawahi kufika, ijapokuwa kuna muda hakuacha kumsaili kupitia kioo cha juu kilichomo mle ndani ya gari.

Baada ya mwendo wa dakika kadhaa dereva aliegesha gari kando ya barabara na kumtaarifu Askofu Ponera tayari wameshawasili eneo kusudiwa. Askofu Ponera alifanya malipo kwa pesa za Burundi, faranga, kisha aliendeleza moja moja akipotelea kwenye uchochoro.

Lengo la kufanya hivi ni kumpoteza dereva teksi. Kwani alipojihakikishia ameondoka baada ya kusikia ngurumo ya gari, alirudi tena barabarani kuitafuta nyumba pasa.

Halikuwa zoezi gumu kwa upande wake kuitambua ile nyumba. Nyumba aliyokuwa akiishi Jenerali Ndiyashena enzi za uhai wake. Kabla hajaifikia, aliangaza huku na kule kama hakuna mtu anayefuatilia nyendo zake kisha akaikaribia kwa uchunguzi wa namna atakavyoingia ndani.

Ilikuwa nyumba iliyojengwa kwa mtindo wa kawaida, lakini ilibeba sifa zote za ufahari. Ilikuwa nzuri mno, ijapokuwa uchakavu ulianza kuinyemelea kwa ukosefu wa matunzo, uliomfahamisha Askofu Ponera kwa wakati huo haina mkazi.

Sambamba na hilo, kiza kiliikumba nyumba hiyo. Kiza cha kuogofya kwa rika lolote lile atakaye kuingia.

Baada ya kujihakikishia ni mwenyewe ndiye aliyopo mahali hapo aliruka uzio uliouzunguka nyumba hiyo na kutua kwa mshindo mdogo uani. Pale alipotua hakuchelea, alijiinua na kutembea kwa haraka hadi ilipo varanda upande wa nyuma wa jengo hilo.

Akajibanza ukutani na kupimia.

Kuna yeyote?

Alivyoona kimya kinazidi kushika hatamu alipiga hatua hadi mlangoni. Kulikuwa na mlango mdogo uliomfahamisha ni wa dharura. Akachomoa glavu kutoka kwenye mfuko wa prova, akazivaa.

Tayari kwa kuanza shughuli.

Alianza kwa kuusaili ule mlango kwa kukinyonga nyonga kitasa, akabaini umefungwa.

Ataingiaje?

Akatoa lundo la funguo kutoka kwenye mfuko wa suruali, akajaribu funguo moja baada ya nyingine, alivyoijaribishia ya nne, kitasa kikajipa. Kwa kutoa sauti ya wastani iliyomwashiria kimeshafunguka. Hakuchelea, alikinyonga na kufungua mlango.

Mlango ulivyokuwa wazi alisubiri kwa sekunde kadhaa ili mgandamizo wa hewa uliopata kuwemo upungue. Masubirio hayo yalikuwa kwa sekunde chache tu, baada ya hapo aliingia ndani.

Kwa kutumia tochi yake ya kijasusi, aina ya Uv Zaklamp, iliyo pamoja na kamera, aliwezesha mwanga mle ndani ya nyumba kwa kuiwasha kwa sekunde kadhaa kabla hajaizima.

Hivyo akawa anawasha na kuzima kila baada ya muda fulani, apitapo kwenye vyumba kwa ukaguzi.

Alikuwa kwenye chumba cha tatu. Chumba kilichomfahamisha kilikuwa kinalaliwa na Jenerali Ndiyashena na mkewe, huku viwili alivyopita awali akitoka kapa pasi na kupata kitu chenye umuhimu katika nyendo zake, akili ikiwa imelala kwenye upekuzi wa saraka, alishtuka kusikia kitasa cha mlango chumba alichopo kikitekenywa.

Moyo ukapiga kite kwa hofu. Wakati huo saraka ilishafunguka na kubainisha vilivyomo ndani. Alivyowasha tochi kuviangalia, juu kabisa alikumbana na karatasi yenye rangi nyeupe ikiwa na maandishi machache yaliyoandikwa kwa wino wenye rangi nyeusi.

Alivyopitisha mboni zake kwa haraka haraka kilimvuta kile kilichoandikwa, akaivuta ile karatasi kwa uharaka na kuihifadhi kwenye mfuko wa suruali. Baadaye alilirudishia lile saraka namna lilivyo, kabla hajazima tochi na kukimbilia usawa wa mlango.

Pale mlangoni purkushani za kitasa kufunguliwa zilizidi kumchanganya akili na kuinua kiwango cha hofu kwa kiasi kikubwa kwa Askofu Ponera, kiasi kwamba kuna muda, aliihisi haja ndogo kumkurubia.

“Kuna watu wameshahisi nyendo zangu?” Askofu Ponera alijiuliza, mapigo ya moyo yakimwenda kasi.

Kilichomfanya awe hivyo ni kutotambua nguvu ya mtu aliyefanya uvamizi kwa wakati huo.

“Huyu mjinga japo amefariki, lakini bado anazidi kutuchanganya akili,” ilisikika sauti kutoka nje ya kile chumba.

“Vibaya mno,” ilisikika sauti ya mtu mwingine akichangia hoja.

“Mkewe si ameshawekwa hatiani, lakini?” ilijirudia sauti ya mtu wa kwanza.

“Anaweza asitupatie ushirikiano wa kutosha. Hivyo inabidi tuanze, ili baadaye...” yule mtu wa pili alijibu, kabla hajamalizia kauli yake, akakatishwa na mshindo mdogo wa sauti kutokana ndani ya kitasa, ulioashiria kimeshafunguka.

Walikuwa Luteni Bazombanza na Koplo Rumera, ndani ya mavazi ya kiraia. Lakini namna miili yao ilivyojengeka ilitoa utambulisho kwa mtu yeyote ni watu walio na mafunzo ya kijeshi.

TUKUTANE TOLEO LIJALO.
 
AFRIKA YANGU—3

MTUNZI: HASSAN MBONECHE.

Yalishapita masaa mawili na dakika kadhaa, toka Ndinaa apitiwe na usingizi baada ya kitambo cha robo saa kilichomfanya aangushe kilio pale alipokaa. Kilio kwa ajili ya mama yake ambaye muda huo aliamini hayupo tena duniani.

Alikuja kuzinduka baada ya kusikia sauti mfululizo ya ukohozi na purkushani za hatua. Hatua zilizokuwa zinaelekea usawa ule aliopo. Hakusita kuwa mwenye hofu kwa muda, huku akisikilizia kwa makini mienendo ya hatua hizo, ambazo alifahamu fika, wasababishao hatua hizo ni watu.

Umakini aliouumba ukampa jibu kwa kuvuta mazungumzo ya wahusika.

“Huyu mbwa aombe tusimpate. Tukimpata, atajuta kwa nini alizaliwa mwanamke,” ilisikika sauti yenye ngurumo kidogo.

“Najaribu kuvuta picha namna nitakavyombambia,” sauti ya mtu mwingine ikachangia hoja.

Kikusidiwacho kikamvumbua. Kuwa aongelewaye hapo ni yeye na hao ni wale wavamizi wa kijijini kwao.

“Oooh! Ee Mola nisaidie mja wako,” Ndinaa alisema akijiinua pale alipoketi.

Alivyoinuka, alisikilizia kwa mara nyingine mienendo ya zile hatua, zilizidi kumsogelea. Kitendo kilichompa hadhari akiwa mzembe anaweza kufikiwa na kuwafanya wabaya wake wafurahie ushindi wa mezani.

Hakuta hilo.

Hivyo alianza kwa kuihakiki bahasha kama ipo mahali alipoihifadhi. Alipojihakikishia ipo, alipiga hatua ndogo ndogo zenye uharaka huku akipambanua namna atakavyokuwa huru dhidi ya mabaradhuli hao.

Alivyoona mwendo huo unamkawiza, alianza kukimbia. Lakini hakufika mbali, pale alipojikwaa kwenye kisiki na kutoa ukunga wa nguvu kutokana na anguko na maumivu aliyoyapata. Hamu ya kusonga mbele ikamwisha. Akaketi chini kwa muda kutathmini namna atakavyoyapunguza maumivu.

Pindi yeye anachukua majukumu ya kujiganga ili aendelee na safari, ule ukunga aliopiga na mshindo wa anguko uliwabainisha maadui kuwa lindo lao halipo mbali.

“Amepita huku,” kiongozi wa lile kundi alisema, huku akionyesha kwa mkono uelekeo wanaopaswa kuuchukua.

Lilikuwa kundi la watu wanne.

Pindi kundi la maharamia likiongoza kasi, Ndinaa alikuwa amemaliza kufuta damu kwa majani ya mti kisha kurudi upya kwenye mwendo. Awamu hii kasi ilipungua. Hakuwa na uwezo tena wa kukimbia kwa ustadi, badala yake alifanya mbio kwa mchechemeo.

Hata hivyo hazikumridhisha. Akaketi chini kwa mara nyingine na kuwazua afanyaje asiweze kufikiwa. Wakati anawazua mboni zake zililala kwenye kidole gumba cha mguu wa kuume. Kilikuwa kinavuja damu.

“Nisipoidhibiti hii damu haiwezi kukata,” Ndinaa alijisemeza, huku akiifuta futa ile damu inayozidi kutiririka kwa kijiti.

Alihisi kupatikana.

Ghafla, alikuwa kama mtu aliyepigwa shoti ya umeme, alivyoingiwa na wazo jipya akilini na kulitekeleza. Alichana sehemu ndogo ya khanga aliyovaa akajifunga pale kidoleni.

Kidogo, akahisi atapata ahueni katika utembeaji.

Alitumia takribani dakika tatu kuhitimisha zoezi hilo. Baada ya hapo ndipo alirudi kwa mara nyingine mwendoni kukimbia mawindo ya adui, ambayo yalikuwa zaidi ya hatari.

Kama alivyohisi awali, awamu hii ahueni ilikuwepo. Ijapokuwa kasi haikufanana na ile pindi yu'mzima wa afya.

***

Ndinaa alifanikiwa kuifikia barabara kuu ielekeayo Ruyigi, na kujichanganya kwenye halaiki ya watu wenye rika mbalimbali waliokuwa wameyakimbia makazi yao kwenda kutafuta sehemu ya kuishi.

Machafuko yaliyoshika kasi, familia yao ikiwa chanzo ilimfanya awaonee huruma wale wengine. Hasa wenye watoto wadogo, ambao muda huo walipaswa kuwa shule.

“Eeh, Mola, tupe mioyo yenye uvumilivu na subira kukipita kipindi hiki salama,” Ndinaa alijisemeza, akijitahidi kukatiza awe mbele zaidi.

Utulivu wa mioyo ya wanaburundi kwa wakati huo ulikuwa chini yake. Akabidhishe bahasha kwa mkusudiwa aliyoambiwa. Jambo ambalo kwa upande wake lilikuwa ngumu, kwa sababu hamfahamu huyo mtu. Kwani hakuwahi kubahatika kumuona japo kwa siku moja.

Zilipita dakika tano, toka Ndinaa ajichanganye kwenye ile halaiki vijana wamfukuzao nao walijichanganya. Walikuwa ni vijana wa makamo, wasiozidi hata umri wa miaka ishirini na miwili.

Asilimia kubwa wote walikuwa wembamba wenye vimo vya kati. Huku makoti makubwa yaliyoshuka hadi magotini yakizuia silaha; bunduki aina ya AK 47 waliyokata sehemu ya kitako ili iwe fupi na kufichika kwa urahisi. Pasi na kusahau mapanga waliyoyasundika kiunoni.

Ijapokuwa kiza kilishika hatamu wale vijana walikaza mboni zao juu juu kumwangalia Ndinaa. Lakini isivyo bahati, mboni zote nane, zilizokazwa kama watafuta shilingi ya malipo ya ada, hawakufua dafu.

“Tuhakikishe tunampata huyu kinyaragosi,” mmoja wa wale vijana, ambaye ndiye kiongozi alisema. Sauti ikiwa imesheheni ghadhibiko.

“Na atakuwa yuko humu humu,” kijana mwingine alikazia.

“Sasa sikilizeni...” yule kijana wa mwanzo alisema na kutulia kwa muda. Alivyojihakikishia wenzake wamevaa umakini kumsikiliza, aliendelea, “Tusitembee pamoja namna hii. Tujigawe; wengine waelekee mbele, na wengine tusalie uwanda huu huu.”

Kiongozi wao alivyohitimisha utekelezaji ulifuatia. Hakuna aliyepinga. Wawili kati yao walielekea mbele, waliobakia walisalia usawa uleule. Na kwa kutaka kufanya kazi yao kwa urahisi zaidi, yule kiongozi alipiga risasi kadhaa hewani na kuzua mshindo wenye taharuki iliyowafanya watu wakimbie ovyo ovyo.

Utulivu wa safari ukakosekana.

Kwani ile kimbia kimbia ilitengeneza utengano uliowasaidia wale vijana kufanya uchunguzi wao kwa urahisi. Kuendeleza urahisi, walichomoa tochi walipozisundika na kuziwasha.

Lahaula!

Ule mwanga pale ulipotua ulikuwa kwa mtu wamkusudiaye.

“Yule pale,” mmoja wa kijana aliyopo mbele alimtaarifu mwenzake.

Kweli, alikuwa Ndinaa.

Akapiga mbinja kuwajulisha waliopo nyuma kuwa windo lao limeshaonekana.

Wenzao walipowafikia waliunga nyuma yake huku wakiendelea kummulika asiwapotee. Lakini kitendo hicho kilimpa ishara fulani Ndinaa ya kumtaarifu yu'matatizoni zaidi, baada ya kuona ile miali haiendi sehemu nyingine tofauti na pale alipo.

Hatua ya kwanza aliyojiamini inaweza kuwa ya uokozi ni kuongeza mwendo. Akafanya hivyo. Akaongeza mwendo, na wale vijana pia waliongeza mwendo.

“Anataka kukimbia huyu mjinga,” kijana mdogo kuliko wote aliwavumbua wenzake. Nao kuafiki, baada ya kumuona Ndinaa akijitahidi kujipenyeza katikati ya kundi la wa-mama waliobeba vifurushi kichwani.

Ilikuwa anataka kumalizia mguu wake wa kulia apotelee kwenye lile kundi la wa-mama, pale kiongozi wa kundi la wale vijana alipochomoa bunduki yake na kutupa mitupo ya risasi kadhaa mwilini mwa Ndinaa.

Zilitua risasi mbili mwilini mwake, na kumtupa umbali wa mitaa kadhaa, huku akiharibu kwa mara nyingine utulivu wa safari. Kwani sio mlio wa risasi, wala mshindo wa anguko, ulioweza kuwazuia wasaka makazi purkushanini kwa mara nyingine.

Haraka sana, yule aliyepiga risasi baada ya kumaliza aliirejesha bunduki mahali alipokuwa ameihifadhi na kuwahimiza wenzake wakimbie wakamuangalie mtu wao. Cha kushangaza, walipofika eneo ambalo Ndinaa walimuona ameangukia hakukuwa na mtu.
Wakapigwa na butwaa.

Butwaa lililowashinikiza waanze kwa mara nyingine zoezi la kukodoa mboni zao kumtafuta. Walipatwa na hisio, baada ya lile anguko aliinuka na kujivuta vuta.

Walivyoangaza kwa makini walibaini mbururo walioutilia shaka. Wakaamua kuufuatilia, kwa kupiga hatua za wastani huku mwanga wa tochi ukiwaongoza. Hawakufika umbali mrefu, ule mburuzo ulikata na hawakufanikiwa kumuona Ndinaa.

“Inawezekanaje?” kiongozi wa lile kundi la vijana aliuliza, sauti ikiwa imesheheni mkoromo ulioonyesha kiwango cha chuki alichonacho.

Alichukia, kama ilivyo desturi ya wakosa mawindo.

***

Askofu Ponera ndivyo anavyofahamika na wengi. Lakini hilo sio jina halisi alilopatiwa na wazazi wake baada ya uzao. Jina alilopatiwa na wazazi ni John Chiwa. Isivyo bahati, jina hili lilipotea ghafla, pale alipoanza shule ya msingi. Kwa shinikizo kutoka serikalini, wazazi walilazimika kubadili jina masikioni mwa jamii na kupatiwa Ponera. Ilikuwa ni sehemu ya kazi kutoka kitengo nyeti serikalini.

Akiwa Ponera, hujulikana kama Askofu. Ilhali akiwa John Chiwa, hujulikana Luteni Kanali wa jeshi la wananchi Tanzania. Sifa moja wapo ilikuwa ya kutengenezwa na idara, kama walivyomtengenezea jina siku za nyuma.

Utawazwa wa kuwa Askofu ulitengenezwa na idara ya usalama wa Taifa baada ya kufukuzwa jeshi kwa geresha akiwa na cheo cha PTE (Private). Akatengenezewa nafasi mbalimbali za uongozi wa dini ndani ya dhehebu, mwisho akasimikwa rasmi kuwa Askofu Dayosisi ya Mtwara.

“Chiwa, hizi nafasi utazitumikia zote. Lakini moja ni kama kiremba kwa ajili ya kuficha nafasi nyingine,” ilikuwa kauli ya m-baba mmoja mwenye mvi nyingi ndani ya ofisi kubwa akiteta na Chiwa mara baada ya kuhitimu kidato cha sita.

“Utaenda jeshini. Na utakuwa Askofu. Lakini kazi yako kuu ni...” yule m-baba aliendelea kusema. Kabla hajahitimisha Chiwa akamkatisha.

“Spy.”

“Sahihi. Tunahitaji uwe jasusi tegemezi ndani ya taifa letu.”

“Sasa huoni kuwa upande wa dini utanizuia kufanya matendo hatarishi ya kijasusi?”

“Tunahitaji uwe kiongozi wa dini ili ukatulize mihemko ya waumini dhidi ya serikali pale watakapochochewa na watu hatarishi kwa taifa letu. Kama vile wanasiasa.”

Hivyo ndivyo ilikuwa.

Jasusi kuwa na kofia ya u-Askofu.

***

Luteni Bazombanza aliufungua mlango kwa uwazi, Koplo Rumera akiwa pembeni yake. Hakuwa na shaka yoyote kwamba anaweza kuwepo mtu ndani, hasa baada ya mhusika wa nyumba kutowepo duniani. Kabla hawajapiga hatua kuingia, Koplo Rumera aliwasha tochi na kufanya wajionee vyema mazingira ya mle chumbani.

Vumbi, lililoshika hatamu likawashinikiza wapige chafya. Huku mwanga wa tochi ukiwabainishia dama za buti sakafuni.

“Kuna mtu aliingia humu ndani,” alijisemeza Luteni Bazombanza. “Atakuwa nani?” akafuatia kujitupia ulizo. Wakati huo hofu ikimchonyota na hadhari ikimkwiva.

Vivyo hivyo kwa Koplo Rumera.

“Hili ni tatizo lingine. Tulikuwa tumekaa kwa kujiachia sana kwamba hakuna anayefuatilia nyendo zetu. Sasa huyu aliyeingia sio wa kumbeza,” Koplo Rumera alitoa wazo.

Hadhari ilivyokuwa komavu ndipo waliingia mle chumbani. Waliingia wakiwa wenye machale, kwani waliielekeza tochi huku na kule kwa uchunguzi. Wakati huo huo, wakiwezesha kurekodi video kupitia ile tochi. Kwani ilikuwa tochi ya kijasusi.

Juu ya kuangaza pande zote mle ndani lakini hawakumuona mtu. Wakahisi, yumkini ameshatoka. Au, mhusika wa zile dama hakuingia siku ile.

Wakarejea kwenye zoezi lililowaleta, upekuzi.

Kwa uharaka, wenye umakini wastani, walipekua kila pande ya chumba hicho. Hawakuacha kitu chochote ambacho waliamini kinahusika kwenye uhifadhi. Lakini juu ya jitihada zote hizo, hawakupata wala kuona kitakachowafutia hatua zao, au kufahamu mienendo ya Mugaza ndani ya Tanzania.

Muda wote huo Askofu Ponera alikuwa juu ya dari ameyatega masikio vyema asipitwe na neno. Hakujali hali ya huko, hasa joto, lililomshinikiza muda mwingine atamani kupata japo hewa, lakini ilishindikana. Kwani kupata habari kutoka kwa hao watu lilikuwa jambo la muhimu zaidi. Aliamini itamwezesha kusogea hatua nyingine zaidi katika misheni yake.

Juu ya muda wote waliotumia Luteni Bazombanza na Koplo Rumera kwenye lile zoezi hawakuambulia chochote. Mwisho, walighadhibika. Ghadhibiko lililowaamuru kusitisha na kuchukua maamuzi ya kuondoka.

Ilikuwa pindi wanaondoka, pale Luteni Bazombanza alipositisha hatua baada ya kuona kitu mbele yake.

“Kuna tatizo?” Koplo Rumera aliuliza.

Luteni Bazombanza badala ya kujibu, alichutuma na kukiokota kile kitu. Alivyoinuka, alianza kukisaili. Lilikuwa kacha livaliwalo mkononi. Kacha lililotungwa kwa shanga na kurembwa kwa berenda ya Tanzania.

“Limeingiaje humu ndani?” Luteni Bazombanza alijiuliza. Koplo Rumera akalisikia swali hilo kutokana na sauti iliyomtoka Luteni Bazombanza. Sauti ya wastani.

“Yumkini ndiyo mhusika wa hizi hatua,” Koplo Rumera alijibu.

“Nami nina wasiwasi huohuo.”

“Tunaweza kulitumia kumpata mhusika?”

“Mmmmh! Yeah, lakini tulifikishe kwanza mikononi mwa wakuu, yawezekana watakuwa na wazo bora zaidi yetu.”

“Hamna shida.”

Wakaondoka.

***

Yalikuwa makutano ya dharura usiku ule baina ya Wilhelmina, Kinigi na wale makamanda wa kijeshi wakiongozwa na Brigedia Jenerali Buyoya. Makutano yao yalichagizwa na hali waliyoikuta kina Luteni Bazombanza na Koplo Rumera kule nyumbani kwa hayati Jenerali Ndiyashena.

Makutano yao yalifanyika kwenye nyumba ya ghorofa moja katikati ya mtaa wa Buyenzi.

Kabla mazungumzo hayajaanza walipata nafasi ya kupitia video zilizorekodiwa, mara baada ya hapo ndipo utetaji ulianza. Utetaji uliojaa hasira kwa sababu ya ukosefu wa mafanikio.

“Nimeingiwa na mashaka dhidi ya hili jambo” Wilhelmina alisema.

“Tena ni makubwa sana,” Brigedia Jenerali Buyoya aliingilia kati. “Hii inatoa picha kwamba hatupo peke yetu. Kuna mtu, au watu wanaotafuta ukweli wa yanayojiri,” Brigedia Jenerali Buyoya alikazia.

“Hisio lenu la kwanza mnalipeleka wapi?” Wilhelmina aliuliza.

Kilipita kitambo kidogo cha ukimya kabla swali hili halijajibiwa. Kitambo kilichotoa picha makamanda wapo kwenye zoezi la ufikiriaji. Meja Uwizeye ndiye alikuja kuufukuza.
“Tanzania.”

“Why Tanzania? Kwani haiwezekani mtu wa hapa Burundi kuvaa kacha la taifa lingine?” Wilhelmina aliuliza kwa mara nyingine.

“Hakuna mzalendo wa kweli avaaye kacha la taifa lingine badala ya taifa lake,” Meja Uwizeye aliweka wazi jibu lake.

Brigedia Jenerali Buyoya akaingilia kati, “Ulichozungumza Uwizeye kipo sahihi. Huyu aliyetumwa kufuatilia hii ishu hawezi kuwa raia tu wa kawaida. Ni lazima awe mtu aliyepitia majeshini. Kama amepitia majeshini, mimi ndiye Kamanda wa operesheni ndani ya jeshi letu, hakuna operesheni yoyote iliyoanzishwa kuhusu hii mambo.

“Ingelianzishwa, ningelikuwa na taarifa. Hivyo basi...” Brigedia Jenerali akaachwa kauli yake ikielea baada ya kukatishwa na Wilhelmina.

“Ni lazima vyombo kama polisi na usalama wa Taifa wafanyapo operesheni zao wewe ufahamu?”

Brigedia Jenerali Buyoya akajibu, “Kimsingi ni hivyo. Kwani inasaidia uchangiaji wa mawazo katika ufanikishaji.”

“Kwa hiyo, Tanzania ni nani hadi aingilie mambo ya Taifa lenu?” Wilhelmina aliuliza, sauti ikibeba hali ya chukizo, wakati huo huo akimsaili mmoja baada ya mwingine.

Waulizwa walishindwa kulijibu hili swali. Kitendo kilichozalisha ukimya kwa sekunde kadhaa kabla Wilhelmina hajauondoa.

“Buyoya, wewe ni kamanda wa kijeshi, unafahamu miiko ya mtu wa majeshi kuingia nchi nyingine pasi na kibali,” akatulia kwa muda na kumsaili Brigedia Jenerali Buyoya apokeavyo kauli yake. “Fanya jitihada usiku na mchana kumsaka huyo aliyejiingiza kufuatilia nyendo.

“Fanya jambo, ukweli uzidi kubaki kwetu. Fanyeni jambo tusije kuhaibika. Na fanyeni jambo kuwaonyesha Tanzania si lolote, si chochote. Tumeelewana?”

“Hiyo ni sehemu ya kiapo chetu kwenye hii misheni,” Brigedia Jenerali Buyoya alijibu kikakamavu.

TUKUTANE TOLEO LIJALO
image_search_1605889931327.jpg
 
AFRIKA YANGU—4

MTUNZI: HASSAN MBONECHE

Askofu Ponera alisubiri kwa sekunde chache pale darini baada ya Luteni Bazombanza na Koplo Rumera kuondoka, naye ndipo aliteremka na kuchukua uelekeo yalipo makazi aliyofikia.

Hata kabla hajapoa, aliitoa ile karatasi aliyoichukua sarakani na kuisoma kwanza kabla hajaendelea na mambo mengine.

Gitega ndiyo sehemu salama ya kuishi kwa sasa. Fikeni hapo, na uhakikishe bahasha ndogo inamfikia Mugaza kwa ukombozi wa maisha yenu. Mpendwa wenu sina tena nafasi ya kuendelea kuishi. Nawapenda sana.

Ndivyo ulivyosomeka ujumbe ulioandikwa kwenye ile karatasi.

Ujumbe uliomfungua jambo, anapaswa kukutana na baadhi ya watu ili kitendawili chake kiteguliwe. Nao ni Mugaza, na mhusika aliyeipokea ile bahasha. Ambaye ni mke wa hayati Jenerali Ndiyashena.

“Kwa mujibu wa huu ujumbe, Jenerali alikuwa anatoa taarifa kwa watu wengi,” Askofu Ponera alijisemeza akiwa anayasaili yale maandishi. “Yumkini ni familia yake. Na aliwaelekeza Gitega ni sehemu salama ili iwe rahisi kwa wao kukabidhi hiyo bahasha ndogo. Ilikuwa na nini hiyo bahasha?” mwisho alijitupia ulizo lililomtafakarisha kwa muda mrefu.

“Nitakwenda Gitega siku ya kesho kulipembua hili,” Askofu Ponera alijisemeza mwisho wa tafakuri yake.

Siku iliyofuata kulivyopambazuka aliitii ratiba yake namna ilivyopangwa. Asubuhi alielekea kwenye shughuli za kongamano. Usiku ulivyowadia alihamia kwenye uhalisia wake wa kimaisha. Alipigilia mavazi ya kazi, na kuyaacha makazi kwa mwendo mdogo mdogo kabla hajaruka ukuta na kutokomea.

Alivyofika kijiwe cha teksi, aliingia moja ya gari na kumshtua dereva aliyekuwa ameanza kutekwa na usingizi.

“Nifikishe Gitega,” Askofu Ponera alimwamuru yule dereva.

“Gitega sehemu gani?” dereva alimuuliza, akiwa anajinyoosha nyoosha kuweka mwili sawa.

Askofu Ponera alifikiria kwa muda kabla hajajibu swali hili. Alipojiridhisha na akitakacho ndipo alijibu, “Mjini.”

Idhini ya Askofu Ponera ilimshinikiza dereva aungurumishe injini huku akimtajia kiwango cha nauli anachopaswa kulipa.

“Hamna shida kuhusu malipo. Kikubwa endesha gari kwa uharaka tuwahi kufika,” Askofu Ponera alimtoa hofu.

“Hali ya barabara ikiwa shwari itatuchukua muda wa saa moja na nusu hadi mbili kuwasili.”

“Na haya mavurugu...” Askofu Ponera alimchombeza. Lakini kabla hajaingia kwenye kina, dereva akamkatisha.

“Inavyoonekana hili taifa lililaaniwa toka uumbaji wake.”

“Kwa nini unasema hivyo?”

“Kwa sababu hatujawahi kufurahia uhuru tulioachiwa na mkoloni.”

“Mna uhakika ipo siku mtafurahia?”

“Tumeumbwa kuwa na imani. Hivyo tuna imani hiyo, japo hatufahamu itakuwa lini.”

Safari ile ilisongeshwa na ladha ya taarifa mbalimbali kutoka redioni. Taarifa zilizobeba matukio yatendekayo.

“Unaingia Gitega kufanya nini kiongozi na haya machafuko?” dereva teksi aliuliza wakiwa wameshatembea umbali wa kilomita kadhaa.

“Naenda kucheki ndugu zangu. Ikibidi niwachukue.”

“Ni jambo zuri sana. Maana watu wanaopaswa kutulinda ndiyo wanaofanya maisha yetu kuwa mashakani. Inasikitisha sana kwa kweli,” dereva alisema kwa sauti iliyopoa kidogo.

Kwa muda mfupi wa safari Askofu Ponera alitengeneza urafiki na yule dereva teksi wenye lengo la kumrubuni ampatie machache anayoyafahamu kuhusu machafuko yaendeleayo.

Machafuko yaliyobeba picha ya ki-biashara.
Baada ya mwendo wa makadirio aliyoyatoa dereva hatimaye waliwasili Gitega. Wakaegesha gari nje ya moja ya mgahawa mtaa wa Nyamugari, ufahamikao chez maman bonheur, kisha waliingia ndani kupata chakula.

“Vipi, nikikuambia ufanye subira hadi nimalize shughuli zangu, utaweza?” Askofu Ponera aliuliza, taratibu chakula apatacho kikiweka sawa hali ya tumbo.

Dereva alimeza kwanza tonge lililopo kwenye kijiko ndipo alijibu, “Ni hela yako tu. Hata ukisema tukae huku mwezi mzima, kama tutaafikiana malipo nitakayofurahishwa nayo.”

Wakaangua tabasamu.

Tabasamu lile lilikatizwa na mshindo wa viatu vilivyokuwa vinasikika kwa nguvu vikinyanyasa sakafu. Askofu Ponera akageuka kuangalia ule upande utokeao sauti. Aliona vijana wawili walioonekana kuwa na haraka kwenye matembezi yao.

Moyo ukapiga kite kwa hofu. Akilini akawa kama amepigiziwa filimbi ya kumtaarifu jambo. Jambo lenye hatari.

“Kuna tatizo bosi?” dereva teksi aliuliza huku akigeuka kuangazia kule kule aangaliako Askofu Ponera.

“Hapana. Aaah, hakuna shida,” Askofu Ponera alijibu kwa kubabaika, huku akizirudisha mboni zake kwenye sahani ya chakula.

Alipiga kijiko kimoja na kukitupia mdomoni kwa haraka, nafsi ikimsuta, kwamba asiwaachie watu wale kirahisi wakipotea mbonini mwake.

Kilichoshinikiza hilo ni namna wale vijana walivyo. Walikuwa vijana wa makamo wenye ukadirio wa umri wa miaka thelathini. Warefu, wembamba, wakipambwa na rangi nyeusi. Mavazi waliyovaa, kidogo yalishabihiana. Walivaa makoti makubwa ya kujikinga na mvua, suruali ya jeshi la FDN na buti fupi.

Yale makoti waliyoyavaa walionekana kuficha kitu fulani kilichopo ndani kwa upande wa mgongoni. Askofu Ponera alilibaini hilo wale vijana walipofikia mlango na kupotelea nje. Na hisio la haraka lilikuwa bunduki. Walikuwa wameficha bunduki kule mgongoni.

“Naomba unifiate,” Askofu Ponera alimwamuru dereva huku akitupa kijiko kwenye sahani na kuinuka pale alipoketi.

Dereva alistaajabu. Hakumwelewa kabisa Askofu Ponera ukizingatia chakula hakikuisha.

“Haa! Si tumalizie kwanza chakula!” dereva alishauri.

Askofu Ponera alijibu pendekezo la dereva teksi akiwa ameshafikia sehemu ya kaunta kufanya malipo, “Tutakula sehemu nyingine.”

“Hata kama wewe ndiyo tajiri, hiki ulichokifanya sio kitu kizuri. Umenikiririsha bhana,” dereva teksi alilalama, tayari akiwa ameshainuka na kumfuata Askofu Ponera.

Hadi wanaingia garini dereva teksi alionekana kuchukizwa na kitendo cha alichofanyiwa. Namna mdomo ulivyofura ndivyo ulivyotoa ubainisho wa jambo hilo.

“Ifuatilie ile gari. Fanya vyovyote uwezavyo isitupotee,” Askofu Ponera alimwamuru dereva. Wakati huo gari kusudiwa ikiwa umbali wa mita kadhaa ikichanja mbuga. Dereva alivyoungurumisha injini na kuanza kuiondoa, Askofu Ponera akampatia nasaha, “Msisitizo,” alisema na kumsaili dereva kwa muda. Dereva naye aligeuka na kujikuta wakitazamana, “Isitupotee ile gari.” Dereva akaurejea umakini wake.

Vijana waliokuwa wanawafuatilia walikuwa wamepanda nyuma ya gari ndogo aina ya Nissan Navara Pick-up. Kuipa utulivu miili yao, walizivua bunduki wakazitandaza chini.

Mwendo walioenda nao ulikuwa wa yange yange, wakati huo vurugu zikiendelea mitaa mbalimbali. Kwani hazikuacha kusikika sauti za milipuko na kuchomwa moto vitu tofauti tofauti.

“Ujue ndugu sikuelewi. Au hawa ndiyo ndugu zako ulionitaarifu?” dereva teksi aliuliza, mguu wa kulia ukizidi kukanyaga pedeli ya kuongeza mwendo.

“Ndiyo wenyewe. Lakini sihitaji uwasogelee zaidi. Umbali huu huu tulioutengeneza unatosha,” Askofu Ponera alimuongopea.

Dereva hakuwa na la kuongeza, badala yake alifanya vile alivyoamriwa.

***

Ukomo wa safari yao ulikuwa nje ya mji, mbele ya nyumba kuu kuu iliyobeba hali ya uduni wa kimaisha kwa mhusika. Askofu Ponera alikuwa ametega kwenye moja ya mti takribani mita tisini toka ile nyumba ilipo. Dereva teksi alimwacha mita hamsini nyuma, kwa makubaliano amsubiri hapo kwa dakika kumi na tano, asipotokeza, aendelee na ratiba zake.

Kwa msaada wa mwanga hafifu kutoka nyumba za majirani Askofu Ponera alishuhudia na kuyaelewa baadhi ya mambo yaendeleayo. Mbele ya uga wa ile nyumba iliegeshwa ile gari Nissan waliyokuwa wanaifuatilia, na vijana wawili waliobeba bunduki wakizunguka huku na kule kuhakikisha ulinzi wa eneo hilo. Vijana hawa walikuwa tofauti na wale waliokuwa wanawafuatilia kuanzia kule mgahawani. Wale wa mgahawani walipotelea ndani ya ile nyumba.

Ilichukua zaidi ya dakika nane kwa masubirio, ilivyoelekea dakika ya tisa, ndipo wale vijana waliopotelea ndani walitokeza wakiwa wanasukuma kitanda cha magurudumu kitumikacho hospitalini, juu alilazwa mwanamama aliyeonekana kuteswa sana.

Walipolifikia gari, walimtua yule mama garini na kukirejesha kile kitanda ndani, wakafuatia wenyewe baadaye. Hawakuchelea, gari liliungurumishwa na kuanza mwendo.

Pindi vijana waliokuwa wanawafuatilia wanaondoka, wale waliokuwa wanadumisha ulinzi walimwaga mafuta juu ya paa ya ile nyumba kisha kuwasha moto. Hawakusubiri ukolee, nao waliondoka mahali pale kwa gari nyingine aina ile ile waliyotumia vijana wa awali.

Mwendo walioondoka nao ulikuwa wa kasi mno. Wakichukua uelekeo waliouchukua wenzao.

Askofu Ponera hakuona haja ya kuendelea kupoteza muda. Alirudi kwa kasi alipomwacha dereva na kumtaka aifuatilie gari hiyo. Aliamini, ielekeako ndiko ilipoelekea gari ya mwanzo.

“Kuna usalama lakini utokako?” dereva teksi aliuliza.

“Wajinga sana hawa watoto. Jitahidi tuwawahi,” Askofu Ponera alimsisitizia katika uendeshaji badala ya kujibu swali aliloulizwa.

“Mbona unanifanya nianze kuingiwa na mashaka kukuhusu!” dereva teksi alisema, huku akipunguza mwendo na kutumbua mboni zake kwa Askofu Ponera.

***

Usiku ule ule yule mama aliyechukuliwa kwenye nyumba kuu kuu aliteremshwa mbele ya jengo la kifahari la ghorofa moja mtaa wa Buyenzi, jijini Bujumbura. Akapakizwa kwenye kitanda cha magurudumu na kuingizwa ndani ya nyumba ile.

Pindi hayo yanaendelea Askofu ponera alikuwa jirani na wigo uliozunguka ile nyumba. Hivyo alishuhudia kila liendelealo kwa msaada wa mwanga utokao kwenye taa zilizofungwa kwenye nguzo za wigo.

Miongoni wa aliyoyashuhudia, ni watu sita walioonekana vigogo mahali ukiachilia mbali wale vijana aliokuwa anawafuatilia. Na m-mama waliyemleta pale alikuwa mama Ndinaa.

“Hawa ndiyo mabosi wao,” Askofu Ponera alijisemeza huku akizidi kukaza mboni kusaili.

Alimsaili mtu mmoja baada ya mwingine. Kati yao alikuwepo Brigedia Jenerali Buyoya, Meja Uwizeye, Luteni Bazombanza, Koplo Rumera, Wilhelmina na Kinigi.

Brigedia Jenerali Buyoya na wenzie walikuwa wamevaa half combat. Hii ilimwezesha Askofu Ponera athibitishe maneno aliyokwishawahi kuambiwa pindi anakabidhiwa jukumu hilo na Fadhy. Kwamba kuna waandamizi wa serikali, wasiolitakia mema taifa kwa maslahi yao binafsi ya kujinoofisha.

Ushiriki wa waandamizi hao kwenye kadhia iliyopo ilimfanya ajawe hasira iliyomtamanisha, aruke ule wigo na kwenda kuwararua raua. Ilimuumiza sana. Umivu lililomshinikiza atoe tochi ya kijasusi kwenye moja ya mfuko wa suruali yake na kuwapiga picha.

Aliwapiga picha, moyo ukimchonyota kwa maumivu makali.

“Sitoruhusu mpige hatua nyingine ya harakati zenu,” Askofu Ponera alijisemeza pindi akiirejesha ile tochi mfukoni.

TUKUTANE TOLEO LIJALO.
 
AFRIKA YANGU—5

MTUNZI: HASSAN MBONECHE

Mlio wa mashine ya nukushi iliyokuwa inatoa ujumbe uliotumwa kutoka mahali, ulimwinua Fadhy kitini ndani ya ofisi yake maeneo ya Kijitonyama na kupiga hatua za wastani hadi ilipo mashine. Kwa tahadhari kubwa aliitoa ile karatasi na kurejea alipoketi awali. Akajipa zoezi la usaili.

Ujumbe uliomo kwenye ile karatasi ulikuwa picha mnato. Ambayo haikuweza kuonekana kwa ufasaha kutokana na muda uliotumika kupiga, usiku. Sura za wahusika hazikuweza kuonekana vizuri. Zilijaa ukungu, jambo ambalo lilimkerehesha nafsi kwa sekunde chache kabla hajasaili anuani ya mtuma ujumbe.

Ulitumwa kutoka ofisi ya ubalozi wa Tanzania nchini Burundi.

“Askofu,” alijisemeza pindi akiitua ile karatasi mezani.

Alikuwa ameshalowea kwenye ufikiriaji, pale alipoinuka na kwenda kusimama usawa wa dirisha lile lile alilopata kusimama Askofu Ponera siku zilizopita. Kwa jicho kavu, akaanza kuyasaili mandhari ya jiji. Ikiwa ni sehemu ya kuliondoa ghadhibiko lililoshika hatamu nafsini kwa kukosa ufumbuzi wa picha aliyotumiwa.

“Kwa tafsiri ya haraka wale ni sehemu ya machafuko yaendeleayo Burundi. Ni kina nani hawa? Na kwa nini wameamua kufanya hivi?” Fadhy alijiuliza, moja ya mkono wake ameshikilia kidevu.

Bado hakupata muafaka wa ufikiriaji. Purkushani ya jiji ilionekana kuzidi kumchanganya tofauti na alivyowaza awali.

Baadaye alitoa mche mmoja wa sigara kampuni ya Embassy kutoka kwenye pakiti aliyoihifadhi mfuko wa suruali na kuibandika kwenye kingo za mdomo. Dakika moja mbali, aliiwasha na kuiteketeza kwa mikupuo ya taratibu iliyoonekana kuchangamsha mwili.

Ulivyoteketea nusu mche, alirudi mezani akachukua ile karatasi ya ujumbe na faili lenye rangi ya khaki, kisha alirejea tena usawa wa dirishani. Lile faili na karatasi alivitua kingo ya chini ya dirisha. Karatasi chini, faili juu.

Karibu na mche kumalizika, alishtushwa na sauti ya mlango ukifunguliwa. Kwa mwingine, angelazimika kugeuka kumwangalia aingiaye. Lakini ilikuwa tofauti kwa Fadhy. Hakushawishika kugeuka. Aliendelea kusaili mandhari ya jiji, viwambo vikinata kwa umakini wa hali ya juu sauti ya mtembeo wa mtu aingiaye.

Alikuja kugeuka alivyofukizwa harufu nzuri ya uturi iliyobadilisha hali ya mle ofisini. Kwani aliamini yule aliyeingia ameshamfikia pale alipo.

Kweli.

Yule aliyeingia alikuwa hatua chache tu toka aliposimama. Mwanaume mwenye umbo nene kiasi, mrefu, maji ya kunde. Harufu ya uturi iliyofukiza iliendana na suti rangi nyeusi aliyokuwa amevaa. Pasi na kusahau miwani imkingayo dhidi ya miale ya jua. Alifahamika kwa jina la Benson Lau, Mkurugenzi idara ya Usalama wa Taifa nchini (TSS).

“Karibu sana chief,” Fadhy alimlaki. Aliuchomoa mche wa sigara na kuizima kwa kuifinyanga finyanga na viganja vya mkono, kisha akaiangushia chini kupitia pale dirishani.

“Nimeshakaribia. Kuna jipya?” Benson alijibu, na kusimama usawa aliopo Fadhy.

Fadhy hakujibu, badala yake aliliinua lile faili, ishara kwa Benson ajionee ile picha. Naye alikielewa kitendo kile kwa haraka. Aliichukua ile karatasi, na kufanya yaliyokwisha wahi kufanywa na Fadhy hapo awali, kuisaili.

“Hayo ndiyo mafanikio ya Askofu,” Fadhy alimpasha jambo.

Benson hakuchangia neno, alitingisha tu kichwa; juu-chini kisha alimkabidhi Fadhy ile karatasi.

Fadhy aliipokea, wakati wote mboni akiziangazia nje, huku akisubiri kuambiwa neno kutoka kwa mkuu wake. Kilipita kitambo kidogo pasi na kusemeshana, baadaye Fadhy alilifunua lile faili na kupachika ile karatasi. Akalifunika. Juu ya lile faili kulikuwa na maandishi machache yaoneshayo utambulisho. Yalisomeka AFRIKA YANGU.

Kitambo cha ukimya kilivyokaribia kushika hatamu, Benson akaufukuza, “Burundi lazima iwe salama.” Akageuka kumwangalia Fadhy, kisha aliuinua moja ya mkono wake akamshika bega na kumminya minya kidogo. “Hilo lazima lifanikiwe kwa gharama yoyote ile,” alikazia, na kupiga hatua taratibu akijiondoa ofisini.

***

Ndinaa alikuwa anatweta kwa hofu chini ya mti mkubwa umbali wa mita kadhaa kutoka pale alipopigwa risasi. Risasi alizopigwa; moja ilimpata pajani na nyingine sehemu ya bega. Pembeni yake aliketi mama mwenye rika apatalo miako arobaini na ushee akimpatia huduma ya kwanza. Hasa kwa kuzuia damu nyingi iliyokuwa inamtririka-huyu ndiye aliyemtorosha pale alipoangukia.

Kilio kilichotokana na maumivu kikaelezea hisia apitiazo kwa wakati huo. Alikuwa analalama sana, ijapokuwa sauti ilisikika katika mfumo wa ugugumiaji.

“Pole sana binti, vumilia kwa muda tu, hali itakuwa sawa,” yule mama amhudumiaye Ndinaa alimliwaza. Mama aliyepambwa kwa sura ya kikarimu. Hata sauti imtokavyo wakati wa uzungumzaji ilionyesha hivyo.

“Nasika maumivu makali,” Ndinaa alilalamika.
“Sawa. Endelea kuyavumilia, kwani baada ya muda yatapungua.”

“Oooh, ewe Mola nisaidie. Mungu nisaidie mimi hawa watu wasinifikie,” Ndinaa alilalama kwa mara nyingine. Wakati huu, moja ya kiganja chake cha mkono akipiga piga ardhi, sehemu ya mgongo ameupindisha kidogo.

Neno wasinifikie lilikita kwa nguvu mtimani mwa yule mama na kumpa mtetemo mdogo uliomtaka afahamu jambo kutoka kwa Ndinaa.
“Kwa nini unasema wasikufikie? Ni kina nani hao ambao huitaji wakufikie?” yule mama aliuliza.

“Wao.”

“Kina nani?”

“Walionipiga risasi.”

“Bado sijakuelewa, unamaanisha nini?”

Kwa wema uliofanywa na yule mama Ndinaa hakuona haja ya kumficha yaliyomsibu. Tena dhana hiyo ilikuwa komavu pale alipojihakikishia anaweza kumtumia zaidi kupata uokozi. Hivyo alimhadithia.

Alimhadithia mkasa mzima.

“Hee, wewe ni mtoto wa Jenerali Ndiyashena?” yule mama alipigwa na butwaa. Huku akipozi kwa muda ile shughuli aliyokuwa anaifanya.

“Marehemu Jenerali Ndiyashena,” Ndinaa alimrekebisha.

“Pole sana.”

“Nimeshapoa mama.”

Hadithi aliyohadithiwa ilimfanya yule mama apumbazike kwa muda kama zezeta. Alipokuja kuzinduka, ndipo alirejelea kazi ya kumhudumia Ndinaa. Alihudumu kitambo cha ukimya kikichukua nafasi.

“Nataka nikuombe jambo,” Ndinaa aliufukuza ule ukimya.

Yule mama aliinua kichwa akamwangalia, ishara tosha iliyomfahamisha Ndinaa aendelee.

“Nahitaji msaada wako,” Ndinaa alisema na kutulia kwa sekunde chache. Akakaza mboni kumsaili yule mama kwa sekunde kadhaa, kisha aliendelea, “Unaweza kuambatana nami hadi tunaingia Tanzania?”

Yule mama hakujibu kwa haraka. Alijipa fikirio kwa sekunde chache, alivyojipatia muafaka, alijibu, “Hamna shida. Nipo tayari kwa lolote kuhakikisha nakulinda kuanzia sasa.”

Ndinaa akajisikia mwenye fariji. Mtima ukashinikiza mwili mzima kumsisimka kwa jibu hilo.

Shughuli ilivyohitimika walipumzika kwa muda ili wapate nguvu zaidi kabla hawajaendelea na safari. Iliwachukua zaidi ya dakika ishirini, hadi pale walipoona linaanza kuwachosha ndipo walinuia upya kuianza safari. Safari iliyokosa matumaini ya kufika salama.

***

Meja Uwizeye aliungana na vijana wamfuatiliao Ndinaa baada ya kuondoka kwenye mapokezi ya mama Ndinaa kule Buyenzi. Hakuwa amevaa kijeshi. Alivaa kiraia, ili iwe rahisi kwa upande wake kufanya akitakacho.

Kabla hawajasonga mbele, kiongozi wa lile kundi alimpatia mrejesho wa hatua walizopitia. Nini wamefanya, na matokeo yake ni yapi. Jambo lililomshtua Meja Uwizeye ni lile la Ndinaa kushambuliwa kwa risasi halafu hakuonekana alipopotelea. Haikumwingia akilini kabisa kila alivyojaribu kufikiria.

Inawezekanaje?

Alijiuliza swali hili zaidi ya mara tatu pasi na mafanikio.

“Mlijaribu kukagua maeneo ya jirani na pale mlipomuona akiangukia?” Meja Uwizeye aliuliza.

“Tulilifanya hilo kiongozi,” kiongozi wa lile kundi la vijana alijibu.

Wakati huo walikuwa wameweka kituo mahali.

“Siku zote hakunaga uchawi kwenye risasi. Sasa huyo binti amewezaje kupotea?” Meja Uwizeye aliuliza kwa mara nyingine. Swali lililoumba ukimya kwa sekunde chache kabla hajajijibu mwenyewe. “Au kuna mtu alimsaidia mara baada ya kuanguka.”

Kijana mmoja wapo akadakia, “Inawezekana.”

“Kulikuwa na umbali kiasi gani kutoka alipoangukia nanyi mlipokuwa wakati mnamshambulia?”

“Palikuwa na umbali kia...” kiongozi wa kundi la vijana alijibu, kabla hajamalizia akakatishwa na Meja Uwizeye.

“Basi. Kuna mtu amemsaidia huyo kunguni.”

“Kwa hiyo itakuaje?”

“Lazima tuendelee kumtafuta.”

Walivyohitimisha mazungumzo waliendelea na safari. Safari iliyosheheni mwendo wa kikamanda huku wakizidi kusaili kila mtu wampitaye. Kuna muda walifanya vurugu za hapa na pale kutokana na hasira na kutofanikiwa kwa nia yao.

Hadi Walivyokaribia kuingia mpakani mwa Tanzania hawakubahatika kumpata wala kumuona Ndinaa. Hasira ikawazidi. Hasira waliyoidhihirisha wajihini kwa kuielezea iliyopo mtimani. Walifura, huku wakionekana kuwa na nadhiri endapo watamkamata Ndinaa watamtafuna tafuna mzima mzima.

“Kwa hizi zana hatuwezi kuingia Tanzania kwa kutumia njia halali,” Meja Uwizeye alishauri.

“Kwa hiyo itakuaje?” kijana mmoja wapo aliuliza.

“Tutatumia njia ya panya kuingia,” Meja Uwizeye alisema na kutulia kwa muda. Lengo kupima wampokeavyo. Baadaye aliendelea, “Lakini mmoja wetu lazima aingie Tanzania kwa njia halali. Huyu atakayeingia kwa njia halali kazi yake itakuwa moja tu, kuendelea kufanya upelelezi wa kufahamu Ndinaa anapatikana wapi.

“Tutakaopita njia ya panya tutakuwa tunasubiri ripoti kutoka kwa yule aliyeingia kwa njia halali,” Meja Uwizeye alihitimisha ufafanuzi.

“Sasa, huyo atakayeingia kwa njia halali atatupatiaje ripoti pasi na kufahamu sisi tulipo?” kiongozi wa lile kundi la vijana aliuliza.

“Nafahamu vizuri mazingira ya Tanzania, hasa Kigoma. Vile vile baadhi ya shughuli za wakimbizi kwenye makazi yao...”

Meja Uwizeye akaachwa kauli yake ikielea. Kiongozi wa lile kundi la vijana alimkatisha, “Ina tutam-direct aende kwenye kambi maalumu? Maana tunaweza tusijue akapangiwa kambi gani.”

Ukimya ukashika hatamu.

Swali lilionekana kuwa gumu kwa Meja Uwizeye. Muda wote ambao ukimya ulichukua hatamu alijipa fikirio namna gani wafanye kwa huyo mtu watakayemtuma apite njia halali. Kiongozi wa wale vijana aliongea jambo la msingi sana. Makambi ya wakimbizi yapo mengi, sasa huyo mtu wao watamtuma kambi ipi?

Ilichukua takribani dakika tano ule ukimya ukiendelea kudumu. Hadi wakaanza kusailiana mmoja baada ya mwingine.

“Ndu,” Meja Uwizeye alisema na kutulia, kama hakuwa na uhakika na akisemacho. Baadaye aliendelea, “Nduta. Mtu tutakayemtuma ahakikishe anaenda huko. Nasema hivi kwa sababu moja kubwa, kuna mtu mwingine tofauti na Ndinaa ambaye anapaswa apatikane kwa udi na uvumba.”

“Nani? Na yuko wapi?” kiongozi wa vijana aliuliza.

“Richard Mugaza. Rafiki mkubwa wa marehemu Ndiyashena. Na ni afisa wa idara ya usalama wa Taifa, SNR (Service National de Renseigment). Huyu yupo Tanzania kwa muda mrefu. Alikimbilia huko mara baada ya kifo cha Ndiyashena. Hivyo lazima apatikane ili ukweli uendelee kubaki kwetu,” Meja Uwizeye alijibu.

“Umesahau kufafanua jambo moja.”

“Lipi?”

“Makutano.”

“Kuna shughuli za soko hufanyika karibu na maeneo ya makambi ya wakimbizi. Hivyo ripota wetu atakuwa anatuletea ripoti hapo kila siku ya soko.”

Vijana wakatingisha vichwa kuashiria wamemwelewa vyema.

TUKUTANE TOLEO LIJALO
 
AFRIKA YANGU—6

MTUNZI: HASSAN MBONECHE

Ilikuwa alasiri, Wilhelmina alipoongoza kikao cha watu wa nne; Brigedia Jenerali Buyoya, Luteni Bazombanza, Koplo Rumera na Kinigi kwenye lile jengo la kifahari pale Buyenzi. Kabla hawajaingia kikaoni walipitia kumwangalia mama Ndinaa chumbani alipohifadhiwa, yu’hali gani ndipo walielekea ukumbi wa kikao.

“Huyu mtu ni lulu kwetu,” Wilhelmina alisema na kutulia. Aliwasaili wajumbe wake kwa muda kisha aliendelea, “Inabidi tuhakikishe anakuwa mzima ili ateme kile alichomezeshwa. Naamini sote tunakubaliana, ana kitu alichoambiwa na marehemu kabla ya umauti wake.” Akawasaili wajumbe wake kwa mara nyingine.

Akawaona wakitingisha vichwa juu chini, ishara ya kukubaliana naye.

Akaendelea, “Ili akiseme, tuyaokoe maisha yake kwanza kufikia uwezo wa kuzungumza. Au mnashaurije?”

“Upo sahihi,” Brigedia Jenerali Buyoya alidakia. “Tumtafute daktari, amtibu, akisharejewa na ahueni, ndipo zoezi letu lianze.”

“Kinigi, unashaurije?” Wilhelmina aliuliza.

“Naungana na Brigedia Jenerali Buyoya. Ushauri wake una mashiko sana,” Kinigi alijibu.

“Rumera na Bazombanza, mna lolote?”

Koplo Rumera akadakia, “Lulu huenziwa. Ikishapoteza uthamani wake hutupwa.”

Wote wakaangua vicheko.

Mwisho wa kikao hiki ulifuatia utekelezaji. Utekelezaji wa kumtafuta daktari atakayemhudumia mama Ndinaa kwa matibabu. Jukumu hilo lilikuwa chini ya Brigedia Jenerali Buyoya.

Brigedia Jenerali Buyoya ndiyo alimtafuta daktari. Na wala hakuhangaika sana, alimrubuni mmoja wa madaktari kutoka hospitali ya kijeshi Kamenge.

“Unajua huu utaratibu sio mzuri kwa ajira yangu itakapokuja kubainika?” daktari alishauri, wakiwa ndani ya gari Land cruiser Prado wakikata mitaa kuelekea Buyenzi. Nyuma ya usukani aliketi Brigedia Jenerali Buyoya.

“Nafahamu, ndiyo maana nimekutajia donge nono,” Brigedia Jenerali Buyoya alimtoa hofu. “Nami nataka nikuombe kitu,” akamsaili daktari. Naye kwa utii, aligeuka kumwangalia Brigedia Jenerali Buyoya. Hiyo ilikuwa ishara iliyomshinikiza Brigedia Jenerali Buyoya kuendelea, “Utunze siri ya mteja wako.”

Alivyohitimisha kuzungumza hilo Brigedia Jenerali Buyoya alikuwa anaegesha gari eneo la maegesho kwenye ile nyumba pale Buyenzi. Walitulia kwa sekunde kadhaa mle garini pasi na kuteremka. Walionekana kuteta jambo, walivyojiridhisha, waliteremka na kupotelea ndani ya ile nyumba.

Moja kwa moja waliweka ukomo chumba alichopo mama Ndinaa.

“Huyu ndiyo mgonjwa mkusudiwa,” Brigedia Jenerali Buyoya alimueleza huku akimwonesha kwa mkono kama msisitizo. Wakati huo mama Ndinaa alifunikwa mfuko mweusi usoni, lengo asionekane sura. “Tibu haya majeraha. Sharti, usimfunue huu mfuko ukaona sura yake.”

“Hamna shida kuhusu hilo,” daktari alikubaliana naye. Akageuka, wakatazamana na Brigedia Jenerali Buyoya kisha walikutanishana mikono yao.

***

Kwa Kudra za Mwenyezi Mungu kongamano liliendelea kwa usalama mpaka siku ya mwisho. Siku iliyoshushwa maombi ya nguvu yaliyojaa utakaso. Kuhitimika kwa kongamano hilo ilikuwa kama ruhusa kwa wahubiri waendelee na ratiba zao. Waliotoka mataifa ya nje, warudi makwao. Na wale wa pale pale Burundi, wayarejee makazi yao.

Ilikuwa sawa kwa wahubiri wote; isipokuwa Askofu Ponera. Atarudije nchini pasi na kutimiliza majukumu ya upande wa pili? Ukizingatia hilo ndilo kiini cha safari yake?

“Inabidi nimpate yule mama. Yule mama wanayemshikilia. Yumkini ni sehemu ya familia ya hayati Jenerali Ndiyashena,” Askofu Ponera alijinadhiri, akiwa chumbani kwake akipanga vitu begini. “Ni lazima awe mikononi mwangu leo hii hii ili niondoke naye asubuhi ya kesho,” alijisititizia.

Utekelezaji wa dhamirio alilojiwekea lilifanyika usiku kama ilivyo ada. Alijikoki kwa mavazi yake ya kikamanda, akaisundika bastola kiunoni, kisha aliacha makazi mara baada ya kuruka ukuta. Hatua kadhaa mbele alikifikia kituo cha teksi. Akaingia moja ya gari na kumwamuru dereva ampeleke Buyenzi.

Walipoikaribia ile nyumba, Askofu Ponera alimwamuru dereva teksi aegeshe gari pembeni, naye kutii.

“Nahitaji uniache hapa,” Askofu Ponera alisema akiwa anajipapasa papasa mfukoni kutafuta pesa. Alivyoipata, alimpatia yule dereva.

“Nashukuru sana,” dereva teksi alisema akiwa anapokea.

“Sawa. Nakutakia kazi njema.” Askofu Ponera akateremka garini.

Dereva teksi alivyogeuza gari kurudi watokako, Askofu Ponera alipiga hatua ndogo ndogo na za taratibu kulisogelea lile jengo. Kulikuwa na umbali takribani mita mia mbili kutoka aliposhukia, na alifanya hivyo makusudi. Lengo kubwa ayasome vyema mazingira yazungukayo nyumba hiyo.

Wakati anaielekea nyumba hiyo alikuwa anaitazama upande wa mbele. Baadaye aliona sio vyema kwenda moja kwa moja kupitia upande huo. Akanuia kubadilisha. Atumie upande mwingine utakaomrahisishia kuingia. Ilikuwa pale alipodhamiria abadili uelekeo, aielekee nyumba hiyo kwa upande wa nyuma, aliposikia muungurumo wa kitu nyuma yake.

Akashawishika kugeuka.

Akakumbana na miali ya mwanga iliyomfahamisha inatoka kwenye gari. Mjumulisho wa ule muungurumo ndiyo uliomfanya ajawe na uhakika. Kwa namna fulani hakupendezwa na kile kitendo, akachepukia kando ya barabara na kujificha kwenye moja ya chochoro.

Alirejea barabarani gari lilivyompita. Tena alirejea akiangusha tusi zito la nguoni kwa mtu aliyomo ndani ya gari kwa kumharibia umakini wake.

Japo Askofu Ponera alijihakikishia ushindi wa kumpiga chenga mhusika aliyomo ndani ya gari, lakini haikuwa hivyo kwa wahusika wawili waliomo ndani ya gari; Luteni Bazombanza na Koplo Rumera. Walimuona pindi anamalizikia kuiacha barabara kwenda kujificha.

“Anakusudia nini yule mtu?” Luteni Bazombanza aliuliza.

“Yumkini hataki aonwe,” Koplo Rumera alijibu, akiwa nyuma ya usukani.

“Unahisi kwa nia njema?”

“Duh! Sidhani,” Koplo Rumera alijibu, wakiuacha ule uchochoro aliopotolea Askofu Ponera.

“Hebu niache hapo, nijaribu kumchunguza,” Luteni Bazombanza alimwamuru wakiwa umbali wa mita kadhaa kutoka uchochoro aliopo Askofu Ponera.

Koplo Rumera alitii kwa kupunguza mwendo kidogo tu, kisha Luteni Bazombanza alichumpa chini na kujiviringisha mara kadhaa. Kule alipofikia hakuchelea, aliinuka kwa haraka na kwenda kujificha kwenye wigo wa maua uliozunguka moja ya jengo.

Askofu Ponera akalipita lile eneo pasi na kumuona.

Alimsubiri afikie umbali wa mita kadhaa, ndipo Luteni Bazombanza alijiondoa pale mafichoni na kuunga nyuma ya Askofu Ponera.

Alipoona mlengwa wake amechukua uelekeo wa moja kwa moja kwenye makazi yao machale yakamcheza. Kwamba huyo sio mtu salama kwa upande wao. Akabana mahali kuzidi kumsaili zaidi.

Wakati huo Askofu Ponera alikuwa upande wa nyuma wa lile jengo. Akaangaza huku na kule, alipoona hakuna mtu au kitu chenye kutilia mashaka alisogea karibu na wigo akaanza kuupanda.

“Hii kunguni anataka kuingia ndani,” Luteni Bazombanza alisema, akiwa anawasiliana na mtu wa upande wa pili kwa njia ya simu. Akatulia kwa muda mfupi kusikilizia majibu kutoka kwa mtu wa upande wa pili kisha akaendelea, “Sasa tufanye jambo kumrahisishia,” akatulia tena. Mara hii ilikuwa muda mfupi zaidi kabla hajaendelea, “Zimeni umeme ili tumrahisishie akitakacho.”

Simu ikakatwa.

Haikumchukua muda mrefu Askofu Ponera kuupanda ule wigo na kutua chini. Aliponuia kuamka ili apige hatua kulisogelea jengo umeme ukakata. Alisita kwa muda, na kuihimiza halmashauri ya kichwa chake ihisi jambo. Kabla hajalithibitisha, akaangaza nyumba zilizopo jirani ajionee kama nazo hazina umeme. Lakini haikuwa hivyo.

“Kutakuwa na tatizo?” Alijiuliza akiwa vile vile namna alivyotua pale chini.

Kilipita kitambo kidogo cha kutafuta muafaka, kabla hajajiaminisha hiyo ndiyo nafasi pekee itakayomfanikishia jambo lake kwa wepesi.

Akainuka na kupiga hatua kulielekea jengo.

Kwa ule upande wa nyuma kulikuwa na mlango mdogo alioutambua kuwa ni wa dharura. Na aliuhitaji autumie huo kuingia ndani. Hivyo alichomoa kurunzi yake ya kijasusi, akaiwasha kwa sekunde chache kukisaili kitasa kisha aliizima.

Alivyoirejesha kurunzi mfukoni alitoa rundo la funguo na kuzijaribu kufungua kwenye kile kitasa. Halikuwa zoezi jepesi, kiasi kwamba jasho lilimtoka chapa chapa mithili ya mwanariadha wa mbio ndefu.

Wakati Askofu Ponera akiwa ameuvaa umakini kwenye zoezi hilo Luteni Bazombanza alikuwa ameshatua ndani ya wigo na kusimama moja ya pembe akimpimia.

***

Baada ya jitihada za muda mrefu Askofu Ponera alifanikiwa kufungua mlango na kuingia ndani. Kwa msaada wa kurunzi, aliyoiwasha na kuizima kila baada ya sekunde kadhaa, ilimwezesha kuingia chumba kimoja baada ya kingine na kufanya upekuzi.

Lakini vyote alivyovipitia, havikumwezesha kupata kitu chenye msaada katika misheni yake, lau kumuona mama Ndinaa.

“Itakuwa wamemuhifadhi juu,” Askofu Ponera alijisemeza, pindi akiurudishia mlango mara baada ya kuhitimisha upekuzi chumba cha mwisho sakafu ya chini.

Akanuia kuianza sakafu ya juu.

Alikuwa ameshafikia vidato vya ngazi kuianza safari ya kuelekea sakafu ya juu pale umeme uliporudi. Moyo ukapiga kite kwa mshangao na kumfanya aduwae kwa muda asijue nini afanye. Lilikuwa fumanizi la aina yake.

Kwani alipokuja kuzinduka, alijikuta amezungukwa na watu watatu waliovaa half combat. Juu ya ngazi, kule aelekeako alisimama mmoja, Koplo Rumera. Chini atokako walisimama wawili; Brigedia Jenerali Buyoya na Luteni Bazombanza.

“Hawa wajinga sana. Kumbe ulikuwa mtego?” Askofu Ponera alijiuliza, huku akitafakari namna ya kujiokoa. “Lazima nifanye jambo,” alijisititizia huku akimsaili Koplo Rumera alivyojiketisha.

Bahati, kichwani alikuwa amevaa kapelo. Hivyo iliwawia ugumu wapinzani wake wamtambue kwa haraka. Akapimia, yule wajuu alikuwa mbali kwa makabiliano. Lakini wale wa chini, walikuwa jirani tu toka aliposimama.

Akanuia kuanza nao.

Taratibu, aliurudisha mguu aliokuwa ameutanguliza mbele uwe sawa na ule wa nyuma huku akijigeuza ili afurumushe ngumi mmoja kati ya wale waliopo nyuma, lakini alijikuta hila yake ikiishia kati pale alipopigwa ngumi ya mbavu na Luteni Bazombanza.

Ilikuwa ngumi iliyotua kwa mshindo wa nguvu kiasi cha kumpa maumivu makali. Mgugumo wa sauti iliyochanganyikana na ukohozi ilidhihirisha hilo. Hasira zikampanda, zilizomshinikiza ajitutumue kwa mara nyingine kujitetea. Kwani alirusha ngumi kumwendea Brigedia Jenerali Buyoya, lakini ilionwa. Hivyo Brigedia Jenerali Buyoya alirudi nyuma hatua moja na kuifanya ngumi iliyopangwa ikakite chini ya taya ipite kapa.

Nguvu alizotumia Askofu Ponera kuirusha ile ngumi ilimyumbisha kidogo kwa kuelekea mbele, wakati anajirudi akae sawa, akakumbana na ngumi nzito ya kichwa kutoka kwa Luteni Bazombanza iliyomyumbisha na kwenda kumpigiza kwenye kingo ya vidato vya ngazi na kusererekea chini.

Ile kapelo ikamvuka. Na kufanya abainike.

“Oooh! Askofu,” Brigedia Jenerali Buyoya alimwita, akimsogelea pale alipoangukia.

“Alaaah!” Luteni Bazombanza akashangaa.

Koplo Rumera naye akateremka kule juu.

Kwa pamoja walivyomfikia, kila mmoja alitumia kiungo alichoona kinamfaa kumshushia kipigo Askofu Ponera pale chini. Baadaye Luteni Bazombanza na Koplo Rumera walimtwaa Askofu Ponera juu juu na kumfunga kwenye kiti baada ya kumfanyia upekuzi na kumchukulia vitu vyake vyote.

“Mmnh! Askofu, umefuata nini himayani kwetu?” Brigedia Jenerali Buyoya aliuliza. Moja ya mguu wake ameukanyagia pajani kwa Askofu Ponera. Ambaye uso ulifura kwa kipigo.

Badala ya kujibu Askofu Ponera alikodoa mboni zake kumwangalia Brigedia Jenerali Buyoya namna anavyojisongondoa songondoa. Wakati huo akilini alikuwa na wazo moja tu, atoke salama mahali hapo na amuokoe mama Ndinaa.

Ilikuwa lazima iwe.

Lakini atawezaje?

“Askofu, ulitumwa kuja kufanya kongamano? Au ulikuja kwa lengo la kutupeleleza. Na kuanzia lini Askofu akawa mpelelezi?” Brigedia Jenerali Buyoya aliuliza kwa mara nyingine. Awamu hii aliinua juu moja ya mkono wake lengo ashushe pigo. Lakini kabla hajafanya hivyo, alisitishwa na kitendo cha mlango wa kuingilia hapo sebuleni kufunguliwa.

Wote wakaziangazia mboni zao mlangoni.

Waliingia wazungu wawili; Wilhelmina na Clement Markel-afisa kutoka Umoja wa Mataifa anayehudumu nchini Burundi.

“Tumebahatika kutembelewa na ugeni,” Brigedia Jenerali Buyoya alisema huku akigeuka kuwalaki wageni wake.

Wilhelmina na Clement wakaangua tabasamu.

“Mumepata chochote kutoka kwake? Maana ni maajabu makubwa Askofu kuwa hivi,” Wilhelmina alitoa dukuduku lake.

“Ndiyo tunataka tulifanyie kazi muda huu.”

“Basi hakikisheni na yule mwenzie, mke wa Ndiyashena...” Clement alisema na kusita, muito wa simu ya Brigedia Jenerali Buyoya ilimpa ghairisho hilo.

“Uwizeye,” Brigedia Jenerali Buyoya aliita mara baada ya kupokea. Aliiweka ile simu katika mfumo wa upazaji sauti. “Nipe hali ya uwanja huko.”

“Yako vyema. Tumefanikiwa kuwaona hawa watu mahali walipo,” ilisikika sauti ya upande wa pili. Sauti ya Meja Uwizeye.

“Wote wawili?” Brigedia Jenerali Buyoya aliuliza kwa mkazo.

“Ndiyo; Richard Mugaza na mtoto wa Ndiyashena, Ndinaa.”

“bon travail,” Brigedia Jenerali alisema, akimaanisha kazi nzuri, huku akiwa amekenua kingo za mdomo na kuonyesha meno yaliyoacha asili ya rangi yake, na kuchukua rangi ya shaba. “Sasa wako wapi?”

“Kibondo. Hivyo tunafanya jitihada za kuwaweka himayani.”

“Liwe zoezi la haraka iwezekanavyo.”

“Hamna shida kamanda.”

Simu ikakatwa.

Taarifa hii ilikuwa kama limao ubongoni mwa Askofu Ponera. Ilimchachua, na kumfanya awazue namna ya kujiokoa ili aiwasilishe ofisini kwao.

Alikuja kuondolewa mafikirioni Clement alivyochukua nafasi ya kuzungumza.

“Hakikisheni hawa wawili wana mioyo myeupe.”

“Hilo halina shida.”

“Iwe myeupe pee. Kusiwe na chochote ambacho wanaweza kukitumia kutuhusu,” Clement alisisitiza.

Askofu Ponera alielewa nini Clement amaanichasho. Kwamba wafanywe vyovyote; yeye na mama Ndinaa hadi watoe siri zilizopo ndani ya mioyo yao.

Watazitoaje?

Akafahamu inakuja ngwe nyingine ya kusulubiwa.

ITAENDELEA...
 
AFRIKA YANGU—7

MTUNZI: HASSAN MBONECHE.

Asylum seeker (mwombaji hifadhi) ndiyo hatua ya awali aliyoipitia Ndinaa kabla hajarasimishwa rasmi kuwa mkimbizi. Na watu wengine pia walioyaacha makazi yao Burundi. Hatua hii waliipitia mpakani baina ya Tanzania na Burundi kwa upande wa Kibondo.

Hapo walisailiwa, kisha walisambazwa kwenye makambi mbalimbali.

Ndinaa bahati ililala upande wake. Alichaguliwa kuyaendeleza maisha yake ndani ya kambi ya Nduta. Alishindwa kuruka juu kushangilia tu, lakini moyoni alikuwa na furaha ya ajabu pale alipoambiwa anaelekea kambi ya wakimbizi Nduta. Lile agizo la mama’ke aliliona linaenda kukamilika. La kwenda kumkabidhi ile bahasha Richard Mugaza.

“Kwanza bahasha yenyewe ina nini?” Ndinaa alijiuliza pindi wakisubiri magari yatakayowasafirisha-kutoka pale mpakani kwenda kwenye makambi husika.

Akashawishika kuisaili.

Aliifungua, na kuchunguza vilivyomo; kulikuwa na flash na karatasi ndogo iliyokunjwa. Akavutwa kwanza na ile karatasi. Aliikunjua na kusoma yaliyomo. Alikuta orodha ya majina tu. Majina ya watu sita; Clement Markel, Wilhelmina Filippo, François Kinigi, Brigedia Jenerali Prosper Buyoya, Meja Ezekiel Uwizeye, Luteni Domitien Bazombanza na Koplo Alain Rumera.

Alistaajabu.

Kwa kushindwa kufahamu kusudio la kuorodheshwa kwa majina hayo.

“Au ndiyo wahusika wa machafuko yaliyojitokeza nchini?” Ndinaa alijiuliza, huku akiikunja na kuirejesha ile karatasi bahashani.

Baadaye aliisaili ile flash kwa sekunde chache kisha kuirejesha.

Muda uliopangwa safari kuanza utekelezaji ulichukua nafasi. Wahusika waliingia kwenye magari-malori aina ya Volvo kisha kila msafara ulichukua uelekeo wake.

Ewaaah.

Ndinaa aliuacha moyo utulie. Baada ya kujiaminisha huo ndiyo mwisho wa masahibu. Atarejea Burundi mara baada ya kukamilisha alichoombwa na mama’ke, amtafute Mugaza amkabidhi ile bahasha na pale machafuko yatakapokoma.

Utulivu wa moyo ukamshurutisha atumbukie kwenye kundi la watu waliotekwa na mandhari ya mkoa wa Kigoma kwa ujumla. Waliokuwa wanaangaza huku na kule kusaili uoto uliopo. Alivyorejesha mboni garini, akajikuta akitazamana na kijana aliyekaa umbali mfupi kutoka pale alipo.

Matazamano yao yalichukua sekunde kadhaa, kiasi kwamba Ndinaa alijikuta akimuonea huruma yule kijana kwa namna wajihi wake ulivyonyongeka. Hakuonekana kuwa na furaha. Alionekana kuwa mtu aliyekaribia kuangua kilio kwa kumbukizi za mapitio ya kimaisha.

“Pole sana,” Ndinaa alijisemeza. Liwazo kwa yule kijana, akadiriaye miaka kumi na saba, akipambwa kwa umbo refu, mwembamba na rangi nyeusi.

Akazirudisha mboni zake kwenye ushangaaji kwa mara nyingine. Alivyochoka kushangaa na kurejesha mboni garini zikatua kwa yule yule kijana. Hadi ikawa kawaida, iliyopelekea kujenga hisio moyoni mwake.

***

“Naitwa Ndinaa. Mwenzangu unaitwa nani?” Ndinaa aliuliza, swali kwenda kwa yule kijana mara baada ya kuteremka garini walivyowasili mahali husika.

“Herimana,” muulizwa alijibu, sauti ikiwa imesheheni unyonge uliobeba uhalisia wa hali ya moyo wake. Alikuwa yule kijana aliyeshangaana na Ndinaa ndani ya gari. Wakati huo walikuwa wamesimama hatua chache kutoka walipoteremkia.

“Hujafurahia kuja huku?” Ndinaa aliuliza kwa mara nyingine.

Herimana alimtupia Ndinaa jicho pande la usaili ndipo akajibu, “Sijawahi kuishi mbali na nyumbani hata siku moja.”
“Unatokea sehemu gani?”

“Bujumbura.”

Ndinaa alimshika Herimana moja ya bega na kumbinya mbinya taratibu ishara ya kumliwaza. “Pole sana, kwani maisha ndivyo yalivyo. Vumilia ipo siku yale machafuko yataisha na tutarejea kwa mara nyingine nchini kwetu.” Akamtazama Herimana apokeavyo, kisha aliendelea, “Umekuja na wazazi wako?”

Herimana alishindwa kujibu swali hili kwa haraka, alitengeneza kitambo cha ukimya, kilichomshinikiza Ndinaa asiondoe mboni wajihini kwake. Katika hali isiyotarajiwa, sekunde chache zijazo Herimana alianzwa kutokwa na machozi yaliyomfahamisha Ndinaa ameumizwa na lile swali.

“Wewe ni mwanaume. Jikaze,” Ndinaa alimliwaza.

Lakini lilikuwa liwazo la bure kwa Herimana.
Alidondosha kilio, kilichovuta hisia za watu wengine.

***

Historia za mapitio yao na rika walilonalo ilitoa msukumo kwa Ndinaa na Herimana kuwa marafiki. Historia ya Herimana haikutofautiana sana na ya Ndinaa. Naye wazazi wake waliuwawa usiku aliouwawa Jenerali Ndiyashena. Sio kwa hilo tu, kingine kilichochangia ni kazi ya wazazi wao, wote walikuwa wanajeshi.

Hivyo walikuwa na muunganiko mkubwa mno wa kiurafiki. Muunganiko ulioshinikiza shughuli nyingi pale kambini wafanye pamoja. Walitokea kuelewana, kiasi kwamba watu wengine waliwahisi ni ndugu, ijapokuwa kuna muda walijitambulisha hivyo walipoulizwa.

Wengine hisia zao walizipeleka mbali zaidi, kuwa wao ni wapenzi. Kitendo walichokitekeleza siku zilizofuata baada ya Herimana kuzidiwa na hisia nyingi za uhitaji wa Ndinaa kuwa karibu naye zaidi. Ukaribu utakaomweka huru na mwili kwa lolote atakalolihitaji ambalo halina madhara yatakayosababisha kifo kwa makusudio.

“Herimana kipenzi changu,” Ndinaa aliita, wakiwa wameketi umbali mdogo kutoka hema waishilo.

“Niambie.”

Ndinaa alimsaili kwanza Herimana ndipo akaendelea kuzungumza, “Kuna jambo nahitaji unisaidie.” Akutulia kwa muda, huku akimsaili kwa mara nyingine na kujipa fikirio kama ni sahihi kumshirikisha kile anachotaka kumwambia.

“Mbona huendelei kuzungumza?” Herimana aliuliza, akionekana kujawa na shauku ya kufahamu kinachomsuta mpenziye.

“Nataka unisaidie jambo fulani,” Ndinaa alisema, sauti ikiwa imepoa kidogo.

“Lipi?”

“Kumtafuta mtu mmoja hivi humu kambini anaitwa Richard Mugaza.”

“Ni nani wako?” Herimana aliuliza kwa sauti ya wivu wivu.

“Rafiki wa baba’ngu.”

Herimana alifikiria kwanza kabla hajatoa mrejesho. Kama kazi hiyo ataifanya, ama la. Fikirio lake halikuchukua muda mrefu. Muda mfupi tu, baada ya hapo alimjibu.

“Hamna shida. Nitaifanya hiyo kazi. Lakini nipe dondoo chache kumhusu yeye namna alivyo.”

“Pasi na kukuongopea, sifahamu anafananaje huyo mtu. Kwa sababu sijawahi kuonana naye ana kwa ana, wala picha yake. Nalifahamu jina tu.”

“Okay, sio kesi, nitatumia maarifa yangu kufanikisha hili. Lakini nawe yakupasa uwe unaulizia ulizia ili liwe zoezi fupi.”

“Wala usijali,” Ndinaa aliafikiana naye na kushusha mvua ya mabusu shavuni kwa Herimana.

***

Meja Uwizeye aliongoza timu yake pori kwa pori hadi wakafanikiwa kuifikia ardhi ya Tanzania. Hadi wanakusudia kupumzika baada ya kuchukua muda mwingi wa kutembea umbali mrefu, wale vijana walisalia watatu tu; kiongozi wa kundi, na manyokaa wawili. Wapi mmoja alipo? Wala hawakuwa na habari naye.

Kwa sababu walikuwa na uchovu mwingi, uliotokana na kiasi kikubwa cha maumivu ya miguu, haikuwachukua muda mrefu kupitiwa na usingizi. Wakaangusha midomo ikiwa juu juu, ili wapate urahisi wa kuzitua pumzi.

Ulikuwa usingizi mzito. Uliowatorosha na mengi yaendeleayo.

Walikuja kuzinduka masaa matatu baadaye. Tena sio kwa kupenda, bali kwa shinikizo la sauti ya ukohozi na uuguliaji wa maumivu umbali wa mita kadhaa kutoka walipo. Kwani ile sauti kwao ilikuwa inasikika kwa mbali.

Wakainuka, na kutega viwambo kusikilizia kwa umakini. Lengo, wafahamu upande itokako, na ni ya nani; mtu, au mnyama?

Zoezi hilo lilichukua dakika tatu kuhitimika. Na hitimisho la pamoja walilolipata sauti hiyo ilikuwa ya mtu, na haikutoka umbali mrefu sana toka wao walipo.

“Jamani eeh, twendeni tukafanye usamaria wema kwa huyo mtu,” Meja Uwizeye alishauri.

Hakuna aliyepingana naye. Waliinuka, wote walivyokuwa tayari, walielekea kule sauti isikikako.

Pindi hayo yanajiri ilikuwa ni mapambazuko. Mwanga ulishaanza kujichukulia nafasi, kiza kikitoweshwa kwa ulazima na kufanya ubainisho wa kitu chochote hata kiwe mbali.

Hivyo Meja Uwizeye na watu wake walivyofikia umbali wa mita kadhaa walimuona mtu aliyekuwa anaitoa ile sauti iliyowashawishi kuifuatilia; mwanaume, aliyepambwa kwa umbo fupi, mnene wastani, mweusi. Alikuwa amejiegemeza kwenye mti mkubwa, pembeni yake kukiwa na fuko dogo lililotuna kiasi.

Kwa muonekano wa mwili yule mtu alionekana kutojiweza kwa lolote. Alinyong’onyea sana, wakati kila akikohoa, akitema, kohozi huambatana na damu. Alikuwa anakohoa damu. Na ndiyo iliyoonekana kumnyong’onyeza zaidi, achilia mbali njaa na maumivu ya miguu, iliyojaa vidonda unyayoni.

Kitendo cha maugulio kilimwanzia katikati ya usiku mnene hadi palipokucha. Hivyo kwa wakati huo wa asubuhi, mboni zilimlazimisha kufunga angalau alale, ili akiamka, awe na utulivu utakaomwezesha kufanya jambo.

Alikuwa ameshaanza kusogeza kidogo miguu nyuma tayari kwa kujinyoosha alale, pale alipoona watu wakielekea usawa ule aliopo. Akaghairisha zoezi alilolikusudia, na kujipa zoezi jipya la usaili wa wale watu. Kina Meja Uwizeye. Kila walivyopiga hatua kumsogelea ndivyo alivyoonekana kuzidiwa na hofu nafsini mwake. Hasa alivyowaona wamebeba bunduki. Hisio likamjaa, kuanzia muda ule atakuwa chini ya ulinzi mkali wa vyombo vya usalama kwa kuingia nchini Tanzania kinyemela, baada ya kujiaminisha watu hao wanatoka kwenye chombo kimoja wapo cha ulinzi.

Lakini wazo hili lilikuja kukatika ghafla, alivyobaini miongoni mwa wale watu wamevaa nguo za kijeshi za Burundi. Hapo moyo ukakita kwa hofu. Mashaka yakamkithiri na kumlazimisha aongeze umakini wa kuwasaili.

“Hawa sio watu wema,” yule mtu alijisemeza. Alikuwa mwenye rika la kati, akadiriaye miaka arobaini na ushee.

Alikuja kujihakikishia hisio lake pale alipomtambua Meja Uwizeye. Alikuwa anamfahamu. Inakuaje ameingia kwa njia za panya? Tena ameambatana na vijana wasioeleweka?

Alamu ya hatari ikalia mara mbili kichwani mwake. Aondoke, kabla hajafikiwa.

Hakujua wapi nguvu zimetokea, pale alipoinuka kwa haraka, akavuta lile fuko na kuondoka. Alianza kuondoka kwa uzuri. Kosa likawa hatua kadhaa baada ya kuuanza mwendo huo. Alionwa. Na kuwahimiza kina Meja Uwizeye waongeze kasi. Alivyogeuka nyuma na kukuta anazidi kufuatiliwa kwa haraka, alijibidiisha kupepea. Alitoka nduki, lakini isiyo na kasi.

“Anakimbia,” kijana mmoja wao aliwashtua wenzake.

Meja Uwizeye alitaka kughairisha zoezi, pale alipoona wakifanyacho sicho kilichowaleta. Hivyo kama yule waliyekuwa wamepanga kumsaidia anakimbia msaada wao, basi waachane naye.

“Kama anakimbia asisaidiwe haina haja ya...” Meja Uwizeye aliwashauri wenzie. Lakini hakuhitimisha kauli yake na kuiacha ikielea baada ya kuona jambo lililomshtua kwa yule mtu akimbiaye.

Wenzie wakabaki na shauku ya kuhitaji mwendelezo.

“Mugaza! Richard Mugaza!” Meja Uwizeye alistaajabu.

“Yule ndiyo mlengwa mwingine?” kijana mmoja wapo aliuliza.

Badala ya kujibu, Meja Uwizeye aliivuta bunduki yake AK 47, akaipachika kwenye nyama ya bega na kuruhusu mitupo ya risasi alipo yule mtu awakimbiaye. Richard Mugaza!

***

Herimana alionekana mwenye furaha alivyomfikia Ndinaa aliyekuwa ameketi nje ya hema karibu na machweo baada ya mihangaiko ya siku. Bashasha aliyooneshwa ikamfanya naye aambukizwe na kuchanua tabasamu ambalo halikudumu muda mrefu kwa kujawa na shauku ya ulizo la kutaka kufahamu kilichomchangamsha Herimana.

“Kulikoni?” Ndinaa aliuliza.

“Nimekamilisha kile kikufanyacho mnyonge muda wote,” Herimana alijibu kwa madaha.

Ndinaa aliinuka kwa haraka na kutaka kumkumbatia. Lakini hatua moja aliyopiga Herimana kurudi nyuma ndiyo iliyozuia jaribio hilo kufanikiwa.

“Haina haja ya haraka. Tulia, nitakupasha habari taratibu,” Herimana alimtuliza, akiwa ameshika mabega ya Ndinaa akimsukumia aketi mahali pake.

Wote wakaketi.

“Mmnh! Nijuze,” Ndinaa alionesha shauku ya wazi aliyonayo.

“Nimefanikiwa kupata habari za Mugaza.”

Ndinaa akauliza mshangao ukiwa umejaa, “Wapi?”

“Humu humu ndani.”

“Ina maana tunaishi naye humu ndani?”

“Hapana. Ni sehemu nyingine.”

“Amesema tutaonanaje?”

“Atatupeleka.”

“Lini?”

Herimana alijibu kwa madaha, “jours pas beaucoup.” Akimhakikishia Ndinaa wataenda kuonana na Mugaza siku si nyingi.

Ilikuwa ni jumamosi, Herimana, Ndinaa na wakimbizi wengine walivyoliacha kambi na kwenda sehemu iliyoandaliwa kwa soko la ujirani mwema ndani ya mji wa Nduta, uliopo takribani kilomita sitini na nne kutoka Kibondo. Soko linalojumuisha wafanyabiashara mbalimbali kutoka ndani na nje kambi.

Waliwasili sokoni pindi upoozi ukichukua nafasi kwenye jua. Hivyo halikuwapa shuruba ya kuchosha miili yao juu ya kitambo cha mwendo walichotembea.

Lengo la ujio wao mahali hapo lilikuwa moja tu, kuonana na Mugaza kama walivyokubaliana siku zilizopita. Kwa mujibu wa mtoa taarifa, Herimana alielekezwa mahali hapo ndipo anaweza kumpata mtu wake.

“Ulielekezwa ni sehemu gani huwa anapenda kukaa?” Ndinaa aliuliza, wakiwa wanapiga hatua ndogo ndogo huku wameambatana kwa mfuatano ulioruhusu mara kwa mara miili yao kugusana.

“Kule hivi,” Herimana alijibu, huku akimwoneshea na msisitizo wa kumuelekezea mkono uelekeo wanaopaswa kwenda.

Baada ya mwendo wa hatua kadhaa, waliliacha kidogo soko na kujielekeza kwenye kichaka chenye nyasi fupi fupi.

“Kwenye lile banda pale,” Herimana alisema na kumfanya Ndinaa akaze mboni zake kuangalia pale alipoambiwa.

Kilikuwa kibanda kidogo kilichojengwa kwa miti na kufunikwa na maturubai. Ndani ya banda alikuwepo mwanaume mmoja aliyeketi juu ya gogo pasi na shughuli yoyote.

“Karibuni,” yule mwanaume aliwakaribisha Herimana na Ndinaa walivyolifikia lile banda.

“Ahsante,” waliitikia kwa pamoja.

Baadaye nao waliketi gogoni kisha kusabahiana na utambulisho juu. Huku sehemu kubwa ya utambulisho ikibebwa na Ndinaa. Alijieleza vyema, wakati wote akimsaili yule mtu.

Ndiyo mwenyewe?

Swali hili lilielea kila muda kichwani mwake pindi anajieleza.

“Tumshukuru Mungu kwa kutuwezesha kuonana kwa haraka. Hicho ulichonacho ni sehemu ya ukombozi wa wanaburundi. Baba yako alikuwa makini sana, na hakukubaliana na wadhalimu ndiyo maana...” yule mwanaume alisema na kusita mara baada ya Ndinaa kumaliza kujieleza, sauti ikiwa imesheheni unyonge huku kwa mbali machozi yakimlenga mbonini. Alionekana kuumizwa na aelezacho. Aliendelea baada ya kufuta chozi, “Baba yako hakuwa na kosa lolote. Wamemuua bure.” Akatokwa machozi kwa mara nyingine, na sauti ya kilio juu.

Hali ya mwanaume huyo ilimwambukiza hadi Ndinaa. Alianza kujihisi mnyonge na kutoneshwa kumbukizi za mapitio yake. Naye akaanza kububujikwa na machozi.

Kitendo kilichowasukuma kukumbatiana kwa muda wakiwa wamekaa vile vile kwa lengo la kupoozana. Walivyoachiana, yule mwanaume alitokwa na ulizo.

“Iko wapi hiyo bahasha?”

Badala ya kujibu, Ndinaa alifanya vitendo.

Ilikuwa pindi Ndinaa alivyoingiza mkono wa kushoto usawa wa matiti kuitoa bahasha aliyoombwa, pale alipoona kwa ibio dole gumba la mkono wa kushoto wa yule mwanaume, likionesha ishara ya shega kwenda kwa Herimana. Moyo ukampiga kite kwa nguvu na kufanya msisimko wa hofu umtawale kwa kasi.

Kabla hajafahamu kwa nini amepatwa na hali hiyo, kengele ya hatari ikakesha kulia akilini mwake. Na kuhisi alipoingia sio sehemu salama.

Alivyokaza macho kwa umakini kuangalia nyuma ya yule mwanaume, ambako lile turubai lilitoboka na kutoa mwanya wa kushuhudia mazingira, aliwaona vijana kadhaa walioonekana kucheza cheza michezo asiyoielewa mboni zao zikitua walipo wakati tofauti tofauti.

Hofu ikamzidi. Alivyohisi vijana wale wako timu moja na mtu aliyopo mbele yao.

Hata Herimana?

Alijiuliza pasi na jibu.

“Naweza nikapata sehemu nijisadie haja ndogo? Nahisi bahasha niliihifadhi huku...” Ndinaa aliomba, kauli yake akiiachia inaelea, na kuangua tabasamu bandia asishtukiwe, ilhali ule mkono aliouelekeza kwenye matiti ukiwa umetua juu juu tu.

Yule mwanaume kauli ile ilimpa badiliko la ghafla wajihini na mtimani. Mapigo ya moyo yakamwenda kasi, matuta ya viazi yakajiviriga pajini. Lakini tabasamu alilolichanua likamfanya ajioneshe hana kinyongo, ijapokuwa ilimchukua muda kutafakari ili atoe jibu sahihi la ombi.

Hakuwa mwingine, bali ni Meja Uwizeye. Meja Uwizeye ndiye aliyekuwa mbele ya Ndinaa na Herimana wakati ule.

ITAENDELEA...
 
AFRIKA YANGU—7

MTUNZI: HASSAN MBONECHE.

Asylum seeker (mwombaji hifadhi) ndiyo hatua ya awali aliyoipitia Ndinaa kabla hajarasimishwa rasmi kuwa mkimbizi. Na watu wengine pia walioyaacha makazi yao Burundi. Hatua hii waliipitia mpakani baina ya Tanzania na Burundi kwa upande wa Kibondo.

Hapo walisailiwa, kisha walisambazwa kwenye makambi mbalimbali.

Ndinaa bahati ililala upande wake. Alichaguliwa kuyaendeleza maisha yake ndani ya kambi ya Nduta. Alishindwa kuruka juu kushangilia tu, lakini moyoni alikuwa na furaha ya ajabu pale alipoambiwa anaelekea kambi ya wakimbizi Nduta. Lile agizo la mama’ke aliliona linaenda kukamilika. La kwenda kumkabidhi ile bahasha Richard Mugaza.

“Kwanza bahasha yenyewe ina nini?” Ndinaa alijiuliza pindi wakisubiri magari yatakayowasafirisha-kutoka pale mpakani kwenda kwenye makambi husika.

Akashawishika kuisaili.

Aliifungua, na kuchunguza vilivyomo; kulikuwa na flash na karatasi ndogo iliyokunjwa. Akavutwa kwanza na ile karatasi. Aliikunjua na kusoma yaliyomo. Alikuta orodha ya majina tu. Majina ya watu sita; Clement Markel, Wilhelmina Filippo, François Kinigi, Brigedia Jenerali Prosper Buyoya, Meja Ezekiel Uwizeye, Luteni Domitien Bazombanza na Koplo Alain Rumera.

Alistaajabu.

Kwa kushindwa kufahamu kusudio la kuorodheshwa kwa majina hayo.

“Au ndiyo wahusika wa machafuko yaliyojitokeza nchini?” Ndinaa alijiuliza, huku akiikunja na kuirejesha ile karatasi bahashani.

Baadaye aliisaili ile flash kwa sekunde chache kisha kuirejesha.

Muda uliopangwa safari kuanza utekelezaji ulichukua nafasi. Wahusika waliingia kwenye magari-malori aina ya Volvo kisha kila msafara ulichukua uelekeo wake.

Ewaaah.

Ndinaa aliuacha moyo utulie. Baada ya kujiaminisha huo ndiyo mwisho wa masahibu. Atarejea Burundi mara baada ya kukamilisha alichoombwa na mama’ke, amtafute Mugaza amkabidhi ile bahasha na pale machafuko yatakapokoma.

Utulivu wa moyo ukamshurutisha atumbukie kwenye kundi la watu waliotekwa na mandhari ya mkoa wa Kigoma kwa ujumla. Waliokuwa wanaangaza huku na kule kusaili uoto uliopo. Alivyorejesha mboni garini, akajikuta akitazamana na kijana aliyekaa umbali mfupi kutoka pale alipo.

Matazamano yao yalichukua sekunde kadhaa, kiasi kwamba Ndinaa alijikuta akimuonea huruma yule kijana kwa namna wajihi wake ulivyonyongeka. Hakuonekana kuwa na furaha. Alionekana kuwa mtu aliyekaribia kuangua kilio kwa kumbukizi za mapitio ya kimaisha.

“Pole sana,” Ndinaa alijisemeza. Liwazo kwa yule kijana, akadiriaye miaka kumi na saba, akipambwa kwa umbo refu, mwembamba na rangi nyeusi.

Akazirudisha mboni zake kwenye ushangaaji kwa mara nyingine. Alivyochoka kushangaa na kurejesha mboni garini zikatua kwa yule yule kijana. Hadi ikawa kawaida, iliyopelekea kujenga hisio moyoni mwake.

***

“Naitwa Ndinaa. Mwenzangu unaitwa nani?” Ndinaa aliuliza, swali kwenda kwa yule kijana mara baada ya kuteremka garini walivyowasili mahali husika.

“Herimana,” muulizwa alijibu, sauti ikiwa imesheheni unyonge uliobeba uhalisia wa hali ya moyo wake. Alikuwa yule kijana aliyeshangaana na Ndinaa ndani ya gari. Wakati huo walikuwa wamesimama hatua chache kutoka walipoteremkia.

“Hujafurahia kuja huku?” Ndinaa aliuliza kwa mara nyingine.

Herimana alimtupia Ndinaa jicho pande la usaili ndipo akajibu, “Sijawahi kuishi mbali na nyumbani hata siku moja.”
“Unatokea sehemu gani?”

“Bujumbura.”

Ndinaa alimshika Herimana moja ya bega na kumbinya mbinya taratibu ishara ya kumliwaza. “Pole sana, kwani maisha ndivyo yalivyo. Vumilia ipo siku yale machafuko yataisha na tutarejea kwa mara nyingine nchini kwetu.” Akamtazama Herimana apokeavyo, kisha aliendelea, “Umekuja na wazazi wako?”

Herimana alishindwa kujibu swali hili kwa haraka, alitengeneza kitambo cha ukimya, kilichomshinikiza Ndinaa asiondoe mboni wajihini kwake. Katika hali isiyotarajiwa, sekunde chache zijazo Herimana alianzwa kutokwa na machozi yaliyomfahamisha Ndinaa ameumizwa na lile swali.

“Wewe ni mwanaume. Jikaze,” Ndinaa alimliwaza.

Lakini lilikuwa liwazo la bure kwa Herimana.
Alidondosha kilio, kilichovuta hisia za watu wengine.

***

Historia za mapitio yao na rika walilonalo ilitoa msukumo kwa Ndinaa na Herimana kuwa marafiki. Historia ya Herimana haikutofautiana sana na ya Ndinaa. Naye wazazi wake waliuwawa usiku aliouwawa Jenerali Ndiyashena. Sio kwa hilo tu, kingine kilichochangia ni kazi ya wazazi wao, wote walikuwa wanajeshi.

Hivyo walikuwa na muunganiko mkubwa mno wa kiurafiki. Muunganiko ulioshinikiza shughuli nyingi pale kambini wafanye pamoja. Walitokea kuelewana, kiasi kwamba watu wengine waliwahisi ni ndugu, ijapokuwa kuna muda walijitambulisha hivyo walipoulizwa.

Wengine hisia zao walizipeleka mbali zaidi, kuwa wao ni wapenzi. Kitendo walichokitekeleza siku zilizofuata baada ya Herimana kuzidiwa na hisia nyingi za uhitaji wa Ndinaa kuwa karibu naye zaidi. Ukaribu utakaomweka huru na mwili kwa lolote atakalolihitaji ambalo halina madhara yatakayosababisha kifo kwa makusudio.

“Herimana kipenzi changu,” Ndinaa aliita, wakiwa wameketi umbali mdogo kutoka hema waishilo.

“Niambie.”

Ndinaa alimsaili kwanza Herimana ndipo akaendelea kuzungumza, “Kuna jambo nahitaji unisaidie.” Akutulia kwa muda, huku akimsaili kwa mara nyingine na kujipa fikirio kama ni sahihi kumshirikisha kile anachotaka kumwambia.

“Mbona huendelei kuzungumza?” Herimana aliuliza, akionekana kujawa na shauku ya kufahamu kinachomsuta mpenziye.

“Nataka unisaidie jambo fulani,” Ndinaa alisema, sauti ikiwa imepoa kidogo.

“Lipi?”

“Kumtafuta mtu mmoja hivi humu kambini anaitwa Richard Mugaza.”

“Ni nani wako?” Herimana aliuliza kwa sauti ya wivu wivu.

“Rafiki wa baba’ngu.”

Herimana alifikiria kwanza kabla hajatoa mrejesho. Kama kazi hiyo ataifanya, ama la. Fikirio lake halikuchukua muda mrefu. Muda mfupi tu, baada ya hapo alimjibu.

“Hamna shida. Nitaifanya hiyo kazi. Lakini nipe dondoo chache kumhusu yeye namna alivyo.”

“Pasi na kukuongopea, sifahamu anafananaje huyo mtu. Kwa sababu sijawahi kuonana naye ana kwa ana, wala picha yake. Nalifahamu jina tu.”

“Okay, sio kesi, nitatumia maarifa yangu kufanikisha hili. Lakini nawe yakupasa uwe unaulizia ulizia ili liwe zoezi fupi.”

“Wala usijali,” Ndinaa aliafikiana naye na kushusha mvua ya mabusu shavuni kwa Herimana.

***

Meja Uwizeye aliongoza timu yake pori kwa pori hadi wakafanikiwa kuifikia ardhi ya Tanzania. Hadi wanakusudia kupumzika baada ya kuchukua muda mwingi wa kutembea umbali mrefu, wale vijana walisalia watatu tu; kiongozi wa kundi, na manyokaa wawili. Wapi mmoja alipo? Wala hawakuwa na habari naye.

Kwa sababu walikuwa na uchovu mwingi, uliotokana na kiasi kikubwa cha maumivu ya miguu, haikuwachukua muda mrefu kupitiwa na usingizi. Wakaangusha midomo ikiwa juu juu, ili wapate urahisi wa kuzitua pumzi.

Ulikuwa usingizi mzito. Uliowatorosha na mengi yaendeleayo.

Walikuja kuzinduka masaa matatu baadaye. Tena sio kwa kupenda, bali kwa shinikizo la sauti ya ukohozi na uuguliaji wa maumivu umbali wa mita kadhaa kutoka walipo. Kwani ile sauti kwao ilikuwa inasikika kwa mbali.

Wakainuka, na kutega viwambo kusikilizia kwa umakini. Lengo, wafahamu upande itokako, na ni ya nani; mtu, au mnyama?

Zoezi hilo lilichukua dakika tatu kuhitimika. Na hitimisho la pamoja walilolipata sauti hiyo ilikuwa ya mtu, na haikutoka umbali mrefu sana toka wao walipo.

“Jamani eeh, twendeni tukafanye usamaria wema kwa huyo mtu,” Meja Uwizeye alishauri.

Hakuna aliyepingana naye. Waliinuka, wote walivyokuwa tayari, walielekea kule sauti isikikako.

Pindi hayo yanajiri ilikuwa ni mapambazuko. Mwanga ulishaanza kujichukulia nafasi, kiza kikitoweshwa kwa ulazima na kufanya ubainisho wa kitu chochote hata kiwe mbali.

Hivyo Meja Uwizeye na watu wake walivyofikia umbali wa mita kadhaa walimuona mtu aliyekuwa anaitoa ile sauti iliyowashawishi kuifuatilia; mwanaume, aliyepambwa kwa umbo fupi, mnene wastani, mweusi. Alikuwa amejiegemeza kwenye mti mkubwa, pembeni yake kukiwa na fuko dogo lililotuna kiasi.

Kwa muonekano wa mwili yule mtu alionekana kutojiweza kwa lolote. Alinyong’onyea sana, wakati kila akikohoa, akitema, kohozi huambatana na damu. Alikuwa anakohoa damu. Na ndiyo iliyoonekana kumnyong’onyeza zaidi, achilia mbali njaa na maumivu ya miguu, iliyojaa vidonda unyayoni.

Kitendo cha maugulio kilimwanzia katikati ya usiku mnene hadi palipokucha. Hivyo kwa wakati huo wa asubuhi, mboni zilimlazimisha kufunga angalau alale, ili akiamka, awe na utulivu utakaomwezesha kufanya jambo.

Alikuwa ameshaanza kusogeza kidogo miguu nyuma tayari kwa kujinyoosha alale, pale alipoona watu wakielekea usawa ule aliopo. Akaghairisha zoezi alilolikusudia, na kujipa zoezi jipya la usaili wa wale watu. Kina Meja Uwizeye. Kila walivyopiga hatua kumsogelea ndivyo alivyoonekana kuzidiwa na hofu nafsini mwake. Hasa alivyowaona wamebeba bunduki. Hisio likamjaa, kuanzia muda ule atakuwa chini ya ulinzi mkali wa vyombo vya usalama kwa kuingia nchini Tanzania kinyemela, baada ya kujiaminisha watu hao wanatoka kwenye chombo kimoja wapo cha ulinzi.

Lakini wazo hili lilikuja kukatika ghafla, alivyobaini miongoni mwa wale watu wamevaa nguo za kijeshi za Burundi. Hapo moyo ukakita kwa hofu. Mashaka yakamkithiri na kumlazimisha aongeze umakini wa kuwasaili.

“Hawa sio watu wema,” yule mtu alijisemeza. Alikuwa mwenye rika la kati, akadiriaye miaka arobaini na ushee.

Alikuja kujihakikishia hisio lake pale alipomtambua Meja Uwizeye. Alikuwa anamfahamu. Inakuaje ameingia kwa njia za panya? Tena ameambatana na vijana wasioeleweka?

Alamu ya hatari ikalia mara mbili kichwani mwake. Aondoke, kabla hajafikiwa.

Hakujua wapi nguvu zimetokea, pale alipoinuka kwa haraka, akavuta lile fuko na kuondoka. Alianza kuondoka kwa uzuri. Kosa likawa hatua kadhaa baada ya kuuanza mwendo huo. Alionwa. Na kuwahimiza kina Meja Uwizeye waongeze kasi. Alivyogeuka nyuma na kukuta anazidi kufuatiliwa kwa haraka, alijibidiisha kupepea. Alitoka nduki, lakini isiyo na kasi.

“Anakimbia,” kijana mmoja wao aliwashtua wenzake.

Meja Uwizeye alitaka kughairisha zoezi, pale alipoona wakifanyacho sicho kilichowaleta. Hivyo kama yule waliyekuwa wamepanga kumsaidia anakimbia msaada wao, basi waachane naye.

“Kama anakimbia asisaidiwe haina haja ya...” Meja Uwizeye aliwashauri wenzie. Lakini hakuhitimisha kauli yake na kuiacha ikielea baada ya kuona jambo lililomshtua kwa yule mtu akimbiaye.

Wenzie wakabaki na shauku ya kuhitaji mwendelezo.

“Mugaza! Richard Mugaza!” Meja Uwizeye alistaajabu.

“Yule ndiyo mlengwa mwingine?” kijana mmoja wapo aliuliza.

Badala ya kujibu, Meja Uwizeye aliivuta bunduki yake AK 47, akaipachika kwenye nyama ya bega na kuruhusu mitupo ya risasi alipo yule mtu awakimbiaye. Richard Mugaza!

***

Herimana alionekana mwenye furaha alivyomfikia Ndinaa aliyekuwa ameketi nje ya hema karibu na machweo baada ya mihangaiko ya siku. Bashasha aliyooneshwa ikamfanya naye aambukizwe na kuchanua tabasamu ambalo halikudumu muda mrefu kwa kujawa na shauku ya ulizo la kutaka kufahamu kilichomchangamsha Herimana.

“Kulikoni?” Ndinaa aliuliza.

“Nimekamilisha kile kikufanyacho mnyonge muda wote,” Herimana alijibu kwa madaha.

Ndinaa aliinuka kwa haraka na kutaka kumkumbatia. Lakini hatua moja aliyopiga Herimana kurudi nyuma ndiyo iliyozuia jaribio hilo kufanikiwa.

“Haina haja ya haraka. Tulia, nitakupasha habari taratibu,” Herimana alimtuliza, akiwa ameshika mabega ya Ndinaa akimsukumia aketi mahali pake.

Wote wakaketi.

“Mmnh! Nijuze,” Ndinaa alionesha shauku ya wazi aliyonayo.

“Nimefanikiwa kupata habari za Mugaza.”

Ndinaa akauliza mshangao ukiwa umejaa, “Wapi?”

“Humu humu ndani.”

“Ina maana tunaishi naye humu ndani?”

“Hapana. Ni sehemu nyingine.”

“Amesema tutaonanaje?”

“Atatupeleka.”

“Lini?”

Herimana alijibu kwa madaha, “jours pas beaucoup.” Akimhakikishia Ndinaa wataenda kuonana na Mugaza siku si nyingi.

Ilikuwa ni jumamosi, Herimana, Ndinaa na wakimbizi wengine walivyoliacha kambi na kwenda sehemu iliyoandaliwa kwa soko la ujirani mwema ndani ya mji wa Nduta, uliopo takribani kilomita sitini na nne kutoka Kibondo. Soko linalojumuisha wafanyabiashara mbalimbali kutoka ndani na nje kambi.

Waliwasili sokoni pindi upoozi ukichukua nafasi kwenye jua. Hivyo halikuwapa shuruba ya kuchosha miili yao juu ya kitambo cha mwendo walichotembea.

Lengo la ujio wao mahali hapo lilikuwa moja tu, kuonana na Mugaza kama walivyokubaliana siku zilizopita. Kwa mujibu wa mtoa taarifa, Herimana alielekezwa mahali hapo ndipo anaweza kumpata mtu wake.

“Ulielekezwa ni sehemu gani huwa anapenda kukaa?” Ndinaa aliuliza, wakiwa wanapiga hatua ndogo ndogo huku wameambatana kwa mfuatano ulioruhusu mara kwa mara miili yao kugusana.

“Kule hivi,” Herimana alijibu, huku akimwoneshea na msisitizo wa kumuelekezea mkono uelekeo wanaopaswa kwenda.

Baada ya mwendo wa hatua kadhaa, waliliacha kidogo soko na kujielekeza kwenye kichaka chenye nyasi fupi fupi.

“Kwenye lile banda pale,” Herimana alisema na kumfanya Ndinaa akaze mboni zake kuangalia pale alipoambiwa.

Kilikuwa kibanda kidogo kilichojengwa kwa miti na kufunikwa na maturubai. Ndani ya banda alikuwepo mwanaume mmoja aliyeketi juu ya gogo pasi na shughuli yoyote.

“Karibuni,” yule mwanaume aliwakaribisha Herimana na Ndinaa walivyolifikia lile banda.

“Ahsante,” waliitikia kwa pamoja.

Baadaye nao waliketi gogoni kisha kusabahiana na utambulisho juu. Huku sehemu kubwa ya utambulisho ikibebwa na Ndinaa. Alijieleza vyema, wakati wote akimsaili yule mtu.

Ndiyo mwenyewe?

Swali hili lilielea kila muda kichwani mwake pindi anajieleza.

“Tumshukuru Mungu kwa kutuwezesha kuonana kwa haraka. Hicho ulichonacho ni sehemu ya ukombozi wa wanaburundi. Baba yako alikuwa makini sana, na hakukubaliana na wadhalimu ndiyo maana...” yule mwanaume alisema na kusita mara baada ya Ndinaa kumaliza kujieleza, sauti ikiwa imesheheni unyonge huku kwa mbali machozi yakimlenga mbonini. Alionekana kuumizwa na aelezacho. Aliendelea baada ya kufuta chozi, “Baba yako hakuwa na kosa lolote. Wamemuua bure.” Akatokwa machozi kwa mara nyingine, na sauti ya kilio juu.

Hali ya mwanaume huyo ilimwambukiza hadi Ndinaa. Alianza kujihisi mnyonge na kutoneshwa kumbukizi za mapitio yake. Naye akaanza kububujikwa na machozi.

Kitendo kilichowasukuma kukumbatiana kwa muda wakiwa wamekaa vile vile kwa lengo la kupoozana. Walivyoachiana, yule mwanaume alitokwa na ulizo.

“Iko wapi hiyo bahasha?”

Badala ya kujibu, Ndinaa alifanya vitendo.

Ilikuwa pindi Ndinaa alivyoingiza mkono wa kushoto usawa wa matiti kuitoa bahasha aliyoombwa, pale alipoona kwa ibio dole gumba la mkono wa kushoto wa yule mwanaume, likionesha ishara ya shega kwenda kwa Herimana. Moyo ukampiga kite kwa nguvu na kufanya msisimko wa hofu umtawale kwa kasi.

Kabla hajafahamu kwa nini amepatwa na hali hiyo, kengele ya hatari ikakesha kulia akilini mwake. Na kuhisi alipoingia sio sehemu salama.

Alivyokaza macho kwa umakini kuangalia nyuma ya yule mwanaume, ambako lile turubai lilitoboka na kutoa mwanya wa kushuhudia mazingira, aliwaona vijana kadhaa walioonekana kucheza cheza michezo asiyoielewa mboni zao zikitua walipo wakati tofauti tofauti.

Hofu ikamzidi. Alivyohisi vijana wale wako timu moja na mtu aliyopo mbele yao.

Hata Herimana?

Alijiuliza pasi na jibu.

“Naweza nikapata sehemu nijisadie haja ndogo? Nahisi bahasha niliihifadhi huku...” Ndinaa aliomba, kauli yake akiiachia inaelea, na kuangua tabasamu bandia asishtukiwe, ilhali ule mkono aliouelekeza kwenye matiti ukiwa umetua juu juu tu.

Yule mwanaume kauli ile ilimpa badiliko la ghafla wajihini na mtimani. Mapigo ya moyo yakamwenda kasi, matuta ya viazi yakajiviriga pajini. Lakini tabasamu alilolichanua likamfanya ajioneshe hana kinyongo, ijapokuwa ilimchukua muda kutafakari ili atoe jibu sahihi la ombi.

Hakuwa mwingine, bali ni Meja Uwizeye. Meja Uwizeye ndiye aliyekuwa mbele ya Ndinaa na Herimana wakati ule.

ITAENDELEA...
Mkuu alosto inatutesa,tukumbuke kidogo.
 
RIWAYA: MKOLONI MZAWA—2
MTUNZI: HASSAN MBONECHE
SEHEMU YA 14.

Taifa lilizizima.
Kila kona ilienea habari moja tu, kuanza kwa mchakato wa kuwatafuta wawakilishi katika kinyang’anyiro cha uchaguzi mkuu. Sio chama tawala, wala chama cha upinzani, Maendeleo Tuleane (MATU) ambacho kilikaa pasi na kushughulikia jambo hili. Lengo, wapate wagombea makini wanaokubalika kwa wananchi.
Kwa upande wa Matu, walikuwa na watu wawili tu wenye nguvu. Na ndiyo ambao waliingia kwenye kinyang’anyiro; Prof. Geugeu Makashata, mwanachama aliyejiunga na chama hicho siku chache zilizopita akitokea chama tawala. Mwingine ni Mwenyekiti wa chama, Masabi Wakwetu-lakini mwenyekiti ndiyo alikuwa na uhakika zaidi wa kupita. Masabi!
“Kuna mazingira yoyote yaliandaliwa kuhusu watu wa upinzani?” Makamu wa Rais, Lilian alimtupia swali Luteni Jenerali Kipozi.
“Nina hakika hilo lipo.”
“Ina maana nawe hauna uhakika?” Jenerali Namkumba alikazia.
“Kamishna...” Luteni Jenerali Kipozi alijibu. Lakini kabla hajamaliza alikatishwa na muito wa simu.
Alitoa alipoihifadhi na kupokea.
Wote wakawa kimya kumsikiliza anenacho.
“Hallo!” Luteni Jenerali Kipozi aliita mara baada ya kuipokea ile simu.
“Masabi naongea.”
“Ndiyo.” Akatoa simu sikioni na kuipazisha sauti. Kila mmoja apate kusikia atakachozungumza Masabi.
“Nina ujumbe kutoka kwa Kamishna Ndirimwe.”
Wote wakasogea jirani na Luteni Jenerali Kipozi.
“Endelea.”
“Naweza kuonana nawe?”
Luteni Jenerali Kipozi akasita kwa muda. Akaangalia nyuso za kila mmoja ndipo akafuatia kujibu, “Yeah!”
“Basi nipe uelekeo.”
Nusu saa baadaye Masabi alijumuika na timu ya kina Luteni Jenerali Kipozi.
“Ni jambo la kushangaza,” Masabi alisema baada ya salamu.
“Yeah! Na haupaswi kuondoka na mshangao. Inabidi uuache hapa hapa.”
Wakaangua kicheko.
“Twende kwenye hoja,” Jenerali Namkumba aliamuru.
“Nina ujumbe kutoka kwa Kamishna Ndirimwe.”
“Usisite, uweke wazi.”
“Aliniambia nikuone wakati chama chetu kikielekea kwenye mchakato wa uchaguzi.”
Wakahamaki.
Na kuwafanya wenye tafakuri kwa muda.
“Vipi?” Masabi aliuliza.
“Kamishna Ndirimwe hakunipatia ujumbe wowote kuhusu wewe.”
“Kwa hiyo niondoke?”
“Hapana.”
“Sasa nitabaki kufanya nini?”
“Naamini kuna sehemu yako. Keti nasi tujadiliane tuone namna gani tunafikia muafaka.”
“Kama hatutofikia?”
“Itakuwa ishu nyingine. Ambayo kwa upande wetu hatutokuwa tayari kuiona inatoka nje. Lakini nina hakika haitofikia huko.”
“Una maanisha nini?”
“Chukua nafasi tuzungumze.”
Wakaketi pamoja kwa majadiliano zaidi.
***
Upande wa Chautu walikesha kwa vifijo na nderemo kuwa Rais Sharabu ndiye pekee anayeenda kuchukua fomu na kupeperusha bendera ya chama. Hakuna aliyehisi, kama kuna mwingine atakayejitokeza. Hasa kwa imani ya siku zote, mgombea anayefanikiwa kuongoza muhula wa kwanza, ndiye huyo huyo atakayechaguliwa kwa muhula ujao.
Hivyo milango ilivyofunguliwa Rais Sharabu alijitokeza mapema tu kuchukua fomu. Tena hakuacha zake mbwembwe, na mikogo ya kujiona yupo sahihi muda wote. Ile ya kucheza cheza na kujipitisha pitisha kwa watu wa daraja la chini wamuone naye ni mtu wa aina kama yao.
Alivyokamilisha taratibu aliirejesha, kisha akatega macho na masikio kutazamia nani atasema mbovu juu yake. Sambamba na atakayeleta kiherehere cha kuwania nafasi hiyo.
***
Baada ya maongezi ya muda mrefu, Masabi aliafikiana na kina Luteni Jenerali Kipozi. Awe kivuli cha mipango yao. Agombee, lakini asiweke nia ya dhati.
“Kwa maana hiyo nitakosa uwakilishi kwa wananchi?” Masabi aliuliza.
“Sahihi. Lakini tutakutengenezea mazingira ya kuhakikisha hii nia baada ya awamu ijayo inatimia.”
“Ina maana mtanisaidia kuwa Rais?”
“Pasi na shaka. Kwani tunaamini, tukimweka huyu tumtakaye atamaliza kila hitajio tunalolitaka.”
“Oooh! Natamani ningeliifahamu mipango yenu mapema.”
“Ni makini. Na yenye kuleta nuru kwa wote.”
“Lakini...”
Luteni Jenerali Kipozi akadakia, “Tutakupoza kiasi katika hili. Na kukupa uhakika wa utekelezaji wa nia yako. Tuache tumweke msafisha njia, ukishaingia madarakani userereke tu.”
Wakaangua kicheko.
“Ewe ni Rais ajaye. Tuamini.”
Maongezi yalivyohitimika waliondoka. Waliondoka, kila mmoja akiwa na deni nafsini mwake, ya kuhakikisha mipango haiyumbi.
***
Ilikuwa jumatatu usiku wa saa tano, Babigamba alivyowasili nchini akitokea Marekani. Akapokelewa na Luteni Jenerali Kipozi kisha waliongozana kuelekea kwenye jengo lao la maficho.
“Hatuna haja ya kupoteza muda. Pumzisha mwili, ukishajiona uko fit, ingia kati uanze mapambano,” Luteni Jenerali Kipozi aliongea.
“Mambo yatakaa sawa? Maana nina hakika bwana mkubwa macho yake yote yapo huko.”
“Nakuhakikishia, ni lazima uchukue fomu. Na utakuwa Rais wa nchi yetu kupitia uchaguzi ujao.”
“Ninachohitaji ni ulinzi wangu. Pasi na kusahau familia.”
“Katika hili hawezi kukugusa kwa ubaya. Huko alipo amejawa na imani, akifanya hivyo ataharibu picha yake kwa wananchi. Hivyo inabidi tutumie hapo kuzidi kumpiga.”
Siku iliyofuata Ndalama aliwakumbusha watu wake aliowashawishi wajiandae, tayari kwa mpango. Baadhi walishikwa na sintofahamu. Hawakuamini amini.
“Hueleweki?”
“Ndiyo maana awali niliwaambia muniamini. Huu ndiyo muda sahihi wa kuanza kumwangusha Sharabu.”
“Kwa namna ipi?”
“Yatupasa tuende na mpinzani atakayejitokeza ndani ya chama.”
“Mbona unatuletea ndoto za alinacha? Nani atajitokeza kushindana na Sharabu?”
“Vuteni subira. Hiyo siku yaja.”
Muda wa kuchukua fomu ulivyokaribia kufikia hitimisho, ndipo Babigamba alijitokeza kwenda kuchukua fomu za kuwania kinyang’anyiro cha kupeperusha chama katika kiti cha urais. Mtoa fomu, Katibu Mkuu, alishikwa na kigugumizi. Aliiwazua ile taarifa mara mbili mbili pasi na kupata jibu.
“Mzee! Ni nini unataka kufanya? Utaratibu wa chama si unaufahamu?” Katibu Mkuu wa chama cha Chautu aliuliza. Wakati huo bado akiwa na fukuto nafsini mwake. Imekuaje Babigamba kaamua kufanya hivyo.
Babigamba akajibu kishujaa, “Nafuata katiba ya chama, na sio utaratibu wa kiholela.”
“Bhana! Upo timamu kweli? Unataka kufanya nini? Muache Sharabu amalizie muhula uliosalia.”
“Wewe huna mamlaka ya kunizuia, nipe fomu, mkutano mkuu ukaamue kama nafaa au sifai.”
“Siwezi kukupa fomu,” Katibu Mkuu aliongea huku kijasho cha woga kikimtiririka. Akanyanyuka alipoketi na kupiga hatua zilizokosa uelekeo mule ofisini. Alienda na kurudi zaidi ya mara sita. Vidole viwili vya mkono wa kuume kakamata kidevu.
Pindi Babigamba na Katibu Mkuu wanazidi kulumbana Jackson alitumia nafasi yake kurahisisha kazi kwa Babigamba. Aliachia taatifa mtandaoni. Kwa njia ya picha mnato na jongefu. Taarifa ilisema ‘Babigamba, kuchuana vikali na Rais Sharabu katika kinyang’anyiro cha kuwania tiketi ya kuwakilisha chama kwenye nafasi ya urais.’
Moja ya picha; ile ya mnato, ilimuonesha pindi akiteremka ndani ya gari. Wakati picha jongefu ilimuonesha akiingia ndani ya jengo la chama, hadi ndani ya ofisi ya Katibu Mkuu. Ikajenga shangwe kwa wapinzani wa Rais Sharabu kiitikadi.
Rais Sharabu alivyofikwa na taarifa alikasirika. Hasira zilizomshinikiza atengeneze kisasi cha nguvu dhidi ya Babigamba.
“Sheenz! Yaani mimi nilikuwa nakulea lea kumbe mwenzangu...” Rais Sharabu alijisemeza huku akiiangalia ile picha jongefu imuonyeshayo Babigamba.
Baada ya kuiangalia kwa muda mrefu na hasira kupoa kwa kiasi, alimpigia simu Katibu Mkuu.
“Mpe akitakacho,” Rais Sharabu alisema, mara baada ya simu kupokelewa. Akakata simu. Kabla ya mtu wa upande wa pili kujibu.
Akampigia mtu mwingine. Killa.
“Nahitaji Babigamba ashughulikiwe haraka iwezekanavyo. Familia yake isisahaulike. Ili udhibiti uwe na nguvu.”
Kupitia amri ya Rais Sharabu Babigamba alikabidhiwa fomu na kuondoka ofisini. Nje, akakuta tuksi la waandishi wa habari waliokuwa wanamsubiri kwa hamu. Wakamvaa kwa maswali.
“Kulikoni Makamu?”
“Mheshimiwa Makamu Mwenyekiti, imekuaje uchukue fomu ya kuwania kuwakilisha chama katika kinyang’anyiro cha urais wakati utaratibu wenu ni...”
Waandishi wa habari waliuliza maswali hayo huku wakipiga hatua za kasi kuendana na mwendo wa Babigamba. Ambaye alionekana kupotezea nia ya wanahabari. Alivyoifikia gari yake alisimama na kujibu yale maswali.
“Tulieni. Haina haja ya kuwa na jazba, kwa sababu nilichofanya ni kitu cha kawaida sana. Nimetimiza matakwa ya katiba ya chama.”
“Lakini haijazoeleka ndani ya chama chenu kuwa na tukio la namna hii?” mmoja wa waandishi alimtupia swali.
“Nimevunja mwiko ambao watu wengi walikuwa wanauogopa kuuvunja. Vile vile, huu ni wakati sahihi wa hiki nilichokifanya kwa hali ya taifa letu ilipofikia. Hivyo niwaombe wanachama wenzangu wanipokee kwa mikono yote.” Akaingia ndani ya gari na kuondoka.
Mtaani kukapasuka.
Kila mmoja alipokea kwa namna yake hili tukio. Wapo waliombeza na kumpongeza. Lakini mwenyewe aliziba masikio asisikie lolote kutoka kwao. Alichojalisha ni kile kilichopo kwenye mkakati wa kufanikisha azma yao.

ITAENDELEA...

HABARI NJEMA

KITABU CHA RIWAYA YA #NENDA KINAPATIKANA RENICS BOOKSHOP TAWI LA MOSHI KWA GHARAMA YA TSH. 10,000/= WASILIANA KWA 0767826134 KUJIPATIA NAKALA YAKO.View attachment 1541164
Iko poa sana

Sent from my SM-A207F using JamiiForums mobile app
 
AFRIKA YANGU—8

MTUNZI: HASSAN MBONECHE

Chumba kilikuwa kidogo. Kiza kilitamalaki vya kutosha, kwani kidirisha kidogo kilichopo mlangoni hakikuweza kuingiza mwanga mwingi wa kumfanya aliyomo ndani aweze kufurahia uwepo wake.

Chumba kile kilibebwa kwenye jengo la ghorofa moja maeneo ya Buyenzi. Ndani yake alikuwemo Askofu Ponera akiwa mwingi wa maumivu yaliyotokana na kipigo. Kipigo cha mbwa mwizi kutoka kwa Brigedia Jenerali Buyoya, Luteni Bazombanza na Koplo Rumera.

Sehemu kubwa ya mwili wake ilitawaliwa majeraha yaliyomnyongesha mwili na kumnyima uhuru wa kuchangamka. Mbali na majeraha, miguuni na mikononi alifungwa kamba nene maalum kwa kuendelea kumnyima uhuru wa kufanya jambo litakalokuwa hatari kwa watesi wake.

Juu ya yote hayo aliyofanyiwa, ni sehemu moja tu ambayo ilimfanya kwa kiasi fulani ajisikie kuwa huru. Akilini. Hakuiruhusu akili ilale. Aliichakarisha ifanye kazi kwa ukawaida wake na muda wote.

“Ni lazima nitoke hapa,” Askofu Ponera alijisemeza, akiwa amejilaza kwenye moja ya kona. “Zile taarifa nilizozinasa lazima nizifikishe kwa Chief. Chifu lazima apate ile taarifa kwa namna yoyote ile.” Alijisisitizia.

“Lakini nitazifikishaje?” alijiuliza, na kujipa tafakuri ya kulijibu swali hilo.

Kabla hajapata mwafaka wa ulizo lake, sauti fulani yenye purkushani ilimshtua. Akakatisha fikirio na kuihimiza akili iruhusu viwambo inase kwa umakini ile sauti.

Aliisikia sauti laini iliyomwaminisha ni ya kike ikilalamika.

Hivyo haraka sana, akapeleka fikra moja kwa moja kumhusu mama Ndinaa.

“Atakuwa ndiye mwenyewe,” alijisemeza, huku akijibidiisha kuamka.

Zoezi lile halikuwa gumu kwa upande wake. Alitoka mlaloni na kufanikiwa kuketi. Akaruhusu kwa mara nyingine kusikilizia ile sauti. Iliendelea kulalama, awamu hii ikiwa imeongezeka kidogo.

Ijapokuwa alikuwa hakifahamu azungumzacho, lakini kupitia maugulio yalimfanya Askofu Ponera aanze kumuonea huruma mama Ndinaa. Hasa baada ya kukumbuka namna alivyopigwa, na kuhusudu upigaji wa watesi wake kwa maumivu ayasikiayo, vipi kwa mama Ndinaa. Alikuwa na uwezo wa kuvumilia?

“Hapana, hawezi kuyamudu maumivu ya namna ile,” alijisemeza. “Na kama ameshindwa kuyamudu, basi atakuwa amewaeleza wakitacho,” aliendelea kujenga hisia.

Lakini zilibaki kuwa hisia tu, kwa sababu hakufahamu uhalisia. Kupata uhalisia ilimpasa akutane na mama Ndinaa kwa namna yoyote ile.

Matamanio hayo yalimsukuma Askofu Ponera ainamishe kidogo kichwa chake usawa lilipo fundo la kamba alilofungwa mikononi na kuanza kulifungua kwa kutumia meno. Meno ya mbele yalifanya kazi sana katika zoezi hilo. Hatua kwa hatua, na kumfanya achukue takribani dakika saba kuhitimisha.

Baadaye aliipara para ile mikono sehemu ambayo kamba ilipita, kutuliza kwa kiasi maumivu kisha aliifungua kamba ya miguuni. Kamba ya miguuni haikumchukua muda mwingi kuifungua, alivyokamilisha alipooza sehemu ambayo fundo lilipita kisha aliruhusu kuwazua hatua inayofuata.

Hakujali tena maumivu ayapatayo, kwani baada ya hitimisho la uwazaji alijivuta vuta kwa msaada wa ukuta hadi usawa wa mlango. Akaketi hapo kwa masubirio.

Alikuwa ameshaanza kutekwa na usingizi pale aliposikia purkushani za kufuli mlango wa chumba alichopo. Akajua unafunguliwa. Na ndicho alichokuwa anakihitaji, akajiinua kwa haraka na kusimama. Ijapokuwa haukuwa usimamaji wenye uhimilivu. Mtetemo wa maumivu ya majeraha yalimsumbua hasa.

Zile purkushani zilipokoma alishuhudia mlango ukifunguliwa. Hapo akapata nafasi ya kuushuhudia mwanga wa kutosha kwa mara ya kwanza ukiingia ndani toka alivyoingizwa. Zilipita sekunde kadhaa, ndipo akaanza kuzisikia hatua za mfunguzi akinyanyasa sakafu kuingia mle ndani. Alivyouacha mlango hatua kadhaa, akamuona akifanya purkushani fulani zilizomfahamisha anataka kuwasha tochi ili amwangalie upande aliopo.

Kwa hofu, na mapigo ya moyo yakimwenda kasi, hakuridhia kitendo hicho kitimilike. Hivyo alirusha teke tepetevu lililotua kwenye mkono wa mfunguzi uliokuwa unajishughulisha na tochi.

Tochi ikadondoka na mfunguzi kuyumba kidogo.

Hakumpa nafasi ajipange, akavuta hatua moja kwa tabu kumfuata mfunguzi alipoyumbia na kukamata ukosi wa shati lake. Hapo ndipo mfunguzi alipopata kutambua, mateka wao hayupo tena katika hali ile ya awali pindi wanamleta chumbani.

Alikuwa amefikia kupiga kelele kuwataarifu wenzie waje wamsaidie, kabla hajatulizwa na ngumi ya chembe kidevu iliyotua kwa nguvu na kumpa mshindo uliomgugumiza kama mbuzi dume. Maumivu makali yakamtawala kichwani.

Askofu Ponera alitulia kwa sekunde chache tu, toka alivyorusha ile ngumi, akarusha makonde mengine mawili yaliyotua sehemu ile ile. Maumivu yakamzidi mara mbili, kiasi kwamba alishindwa kuipa akili nafasi kufikiri namna ya kujikwamua. Baadaye alimchapa ngwara iliyomdondosha chini kama fuko la pumba. Kwa namna alivyomwachia na kufikia chini kwa utangulizi wa kisogo, akafahamu hawezi kuwa na hali nzuri.

Ndiyo.

Hakuweza kufurukuta pale alipoangukia.

Baadaye Askofu Ponera alijipa dakika moja tu ya masubirio, alivyomuona yule mtu hajihangaishi, alimfanyia upekuzi. Haukuwa upekuzi wa muda mrefu, alitumia sekunde chache sana kukamilisha, akachukua vitu alivyoviamini ni vya muhimu vinavyoweza kumwokoa mahali hapo; bastola na lundo la funguo.

Hakupoteza muda, alivyovimiliki vyema mkononi alipiga hatua ndogo ndogo kuondoka ndani ya chumba kile. Hadhari ikiwa imemtawala, aliufuata ushoroba kuelekea chumba alichopo mama Ndinaa. Alivyokifikia, alizihimiza zile funguo kufungua kufuli kubwa alilolikuta ili apate nafasi ya kuingia ndani. Lakini isivyo bahati, hakukuwa na ufunguo uliofungua.

Akaona amepoteza.

Atamuokoaje?

Ulizo lilipita kwa haraka akilini mwake, huku sauti ya mama Ndinaa ikiendelea kusikika akiugulia maumivu.

Ile sauti ya uuguliaji ikazidi kumwongezea hamasa ya kuhakikisha hamwachi ndani ya nyumba hiyo.

Naam!

Dhamirio hilo lilitekelezwa kwa haraka baada ya kukoki bastola na kuruhusu mitupo ya risasi kulielekea kufuli. Alivyositisha, tayari kufuli lilikuwa limeachia, lakini sauti ya mama Ndinaa haikusikika tena. Kuna muda alihisi, yumkini zile risasi alizopiga zimempata na kuchukua uhai wake. Alivyokumbuka mtindo alioutumia kupiga, akaipotezea mbali hisia iliyomkumba.

“Zile risasi zilikuwa haziingii ndani,” Askofu Ponera alijisemeza akiwa anafungua mlango.

Kwa nguvu aliyotumia alifahamu wenzie yule aliyomzimisha watazuru muda wowote kutokana na milio ya zile risasi. Hivyo aliingia ndani kwa haraka moja kwa moja alipo mama Ndinaa. Tofauti na chumba alichohifadhiwa yeye, hiki kilikuwa kikubwa, na kiliwashwa taa ya ufifiaji.

“Nipo kwa ajili ya msaada wako,” Askofu Ponera alimtoa hofu mama Ndinaa alipomfikia. Alikuwa amelazwa kwenye kitanda cha magurudumu manne, majeraha machache yakijibainisha. Na ndiyo yaliyooneka kumsumbua.

“Mimi ni mtu mwema kwako. Nimekuja kukuokoa,” Askofu Ponera aliendelea kumtuliza.

Kwa kiasi fulani mama Ndinaa alishawishika na kauli za Askofu Ponera. Alipunguza hofu, na kumwamuru amsaidie kuondoka mahali pale.

Idhini hiyo ilimsukuma Askofu Ponera kufungua kamba alizofungwa mama Ndinaa kisha kumwinua pale kitandani.

“Pole sana,” Askofu Ponera alimliwaza.

“Siwezi kupoa, ilhali nimetenganishwa na watu wa karibu,” mama Ndinaa alijibu, sauti ikiwa nyongefu. Wakati huo wakijikokoteza kuondoka mle chumbani.

Walivyotaka kutokeza ushorobani, viwambo vikaruhusu kusikika kwa vishindo vilivyowafahamisha ni upandaji wa ngazi. Kuna watu wanapanda ngazi. Mama Ndinaa akaingiwa na uzito wa kuendelea na mwendo. Kwani alipunguza kasi.

“Usiwe na hofu, tutatoka salama mahali hapa,” Askofu Ponera alimhakikishia.

Kabla hawajatua miguu yao ushorobani, Askofu Ponera alitokeza kichwa kwanza kuangalia hali ya uwanja. Kulikuwa shwari. Ni sauti tu zile za upangaji ndizo ziliendelea kusikika. Akajiaminisha, hadi watu hao watokeze walipo, itakuwa wamepiga hatua kadhaa zitakazowasaidia kwenye makabiliano. Haikufaa wafikiwe mle chumbani, itawawia ugumu kujitetea.

Hivyo Askofu Ponera alimkumbata vyema mama Ndinaa kwa moja ya mkono, mwingine alikamatia bastola kisha wakajitosa ushorobani. Walikuwa wamekiacha kile chumba kwa hatua kadhaa, pale wasababisha vishindo walivyovisikia walipoanza kujitokeza pasi na umakini walivyomaliza ngazi, mama Ndinaa akaanza upya kuleta purkushani kwa sababu ya hofu, kuruhusu hilo, ilikuwa ni kuhalalisha mazingira magumu ya ukombozi kwa upande wao, na Askofu Ponera hakutaka hilo litokee kwa wakati huo. Akambana kwa uthabiti karibu na kwapa kisha kuruhusu mitupo ya risasi kwenda kwa wale watu.

Hawakuwa na ujanja wa kuepuka, ziliwafika sehemu walizolengwa na kuhimitisha historia yao duniani. Askofu Ponera akazidi kutumia nafasi hiyo kusonga mbele, na kila walivyokutana na watesi wao hakuwapa nafasi ya kujishughulisha wawashambulie. Aliwawahi kwa haraka.

Hadi wanaifikia sakafu ya chini, Askofu Ponera aliwazimisha walinzi kadhaa na kutengeneza njia nyeupe iliyowapa uhakika wa kuondoka. Na kilichowaaminisha zaidi ni ukimya ulivyotamalaki. Ikamfahamisha watesi wake wameshamalizika.

Kwa mwendo ule ule wa kujivuta, walipiga hatua hadi eneo la maegesho, wakaelekea kwenye moja ya gari. Ilivyo bahati, haikufungwa.

“Kaa hapa, mimi narudi kukamilisha kazi,” Askofu Ponera alisema pindi akimketisha mama Ndinaa.

“Kazi ipi tena? Tuondoke, wasije wakatukuta wenzao,” mama Ndinaa alimuasa akiwa mwenye hofu tele.

Askofu Ponera hakusubiri kumjibu. Aliondoka vile vile kwa mchechemeo wenye kasi kidogo na kupotelea ndani ya lile jengo.

Upande wa mama Ndinaa, akabaki kuwa mwenye hofu. Hofu iliyomlazimisha kumwona Askofu Ponera anawahi kurejea.

Haikumchukua muda mrefu Askofu Ponera kurudi. Alirudi akiwa amekamatia bunduki aina ya AK 47 na visanduku viwili vya risasi vya ziada.

“Ulifuata nini?” mama Ndinaa aliuliza, wakati huo tayari Askofu Ponera alishaketi nyuma ya usukani na kuanza makeke ya kuliungurumisha gari-Toyota Hilux pick up.

“Kinga.” Askofu Ponera alijibu, ile bunduki aliitua kwenye uwazi kati yake na mama Ndinaa.

“Kinga!”

“Ndiyo. Maana huwezi jua hali ya barabara ilivyo. Ikiwa mbaya, hii itatupatia ukombozi.”

Pindi anahitimisha kujibu walishalifikia lango, Askofu Ponera aliteremka garini, akalifungua, kisha kurejea garini na kuliondoa kwa kasi.

Kidogo, wakajawa na ahueni, ukombozi, unawakurubia.

Hiyo ilikuwa ni usiku. Usiku mnene, uliofanya jiji maeneo mengi kuwa kimya.

***

Luteni Bazombanza, Koplo Rumera na vijana kadhaa walikuwa ndani ya gari, Nissan Navara pick-up wakikata mtaa kwa kasi maeneo ya De I’OUA kufuata uelekeo waliouchukua kina Askofu Ponera. Wote, walikuwa na bunduki, AK 47. Sura zao zikionekana kujawa hasira kiasi kwamba wao kwa wao hawakusemezana.

Walivyowasili maeneo ya Bujumbura Mairie walichukua uelekeo wa Chaussee du peuple Murundi, Koplo Rumera aliyeketi nyuma ya usukani akijitahidi kuongeza kasi kila baada ya dakika kadhaa, lengo waifikie gari iliyopo mbele yao. Gari waliyopo Askofu Ponera na mama Ndinaa.

“Mbona kama tunafuatiliwa?” mama Ndinaa aliuliza. Ulizo lililomsukuma Askofu Ponera athibitishe.

Ilikuwa pindi anageuka, pale aliposikia mkwaruzo ukipita kwa kasi ubavuni na kwenda kukita kwa nguvu pembezoni mwa boneti usawa wa tairi. Kabla hajakaa sawa kujijibu ni kitu gani, mshindo mwingine uliovunja kioo cha mbele kwa kupita katikati yao kutokea nyuma, ndiyo ulimpa hakikisho.

“Inama,” Askofo Ponera alimwamuru mama Ndinaa. Wakati huo akiibia kwa kuangalia nyuma kupitia vioo vya pembeni. Aliiona gari iwafuatiliayo ikiwa kasi.

“Wajinga sana hawa jamaa,” alijisemeza, pindi akivuta bastola. Usukani ukabaki kumilikiwa na mkono mmoja.

Alivyoimiliki vyema ile bastola mkononi wala hakujadili. Alitokeza kichwa kidogo tu na kuruhusu mitupo kadhaa ya risasi kulielekea lile gari. Lakini shabaha yake haikuzaa matunda. Mitupo ilipita kapa, na kumfanya ajipange upya.

Rasmi, likaibuka zoezi la makabiliano ya piga, nikupige. Wakati wote huo, mama Ndinaa akiwa mwenye hofu pale alipojilalia kiasi cha kumwaga haja ndogo.

“Usiwe na hofu, hawatoweza kutufikia,” Askofu Ponera ikambidi amtulize.

“Una uhakika?”

“Ndiyo. Kikubwa uwe makini. Usiinue kichwa chako.”

Baada ya kutumia jitihada nyingi za kuongeza mwendo, angalau iliweza kuwasaidia kuwa mbali na kina Luteni Bazombanza. Askofu Ponera akaona hiyo bingo, inayoweza kumsaidia kupata mawili matatu kuhusu misheni iliyomleta.

“Unaweza kunipa utambulisho wako?” Askofu Ponera aliuliza.

“Naweza kuinuka kwanza ili nikujibu vizuri?”

Askofu Ponera aligeuka kuangalia mazingira ya nyuma yapoje, alivyojionea ushwari umetawala, akamruhusu. “Sawa.”

Mama Ndinaa akainuka na kumsaili Askofu Ponera. Kitendo kilichotengeneza ukimya kwa muda. Baadaye aliufukuza, “Mke wa marehemu Jenerali Ndiyashena.”

“Pole sana.”

“Nilishakujibu mwanzo, kuwa siwezi kupoa kirahisi hivyo ilhali nimetanganishwa na familia yangu.”

“Unawafahamu hao wanaotufuatilia? Na sababu ya kufanya hivyo?”
“Siwafahamu.”

Askofu Ponera akaingilia kati, “Sababu ya kufanya hivyo?”

“Nayo sijui.”

Askofu Ponera akafunga breki kwa nguvu ghafla na kumsaili mama Ndinaa. Aliona anamchezea shere, “Nitakuacha hapa usiponieleza ukweli. Nimeyatoa maisha yangu ili nikusaidie, ya nini unifiche?”

Kauli hii ikamfanya mama Ndinaa awe mwenye haya. Nafsi ilimsuta.

“Teremka kwenye gari,” Askofu Ponera alimkazia.

“Hee! Mbona umekuwa wa ajabu hivyo? Unataka nielekee wapi nikiteremkia hapa?”

“Huu ndiyo mwisho wa msaada wangu.”

Mama Ndinaa akazidi kumtupia jicho la usaili. Usaili uliojaa tathmini mtu aliyopo mbele yake anafananaje.

“Haya. Twende basi, nitakueleza.”

Askofu Ponera akachochea mwendo upya.

Hakuwa na budi, mama Ndinaa alifunguka kile anachokifahamu kuhusu mkasa huo. Alihadithia namna mumewe alivyouwawa, na wanavyowindwa kusaka kile kilichoachwa na marehemu mumewe.

“Hivyo vilivyoachwa uliviona?” Askofu Ponera aliuliza.

“Hapana. Nilimkabidhi mwanangu akamtafute mtu niliyoelekezwa ampatie.”

“Mugaza?”

Mama Ndinaa aligeuka kumwangalia, wajihi ukiwa wenye mshangao ndipo akajibu, “Ndiyo. Umemfahamuje?”

“Niliwasikia wenyewe wakimtaja. Umemwambia akamtafutie wapi?”

“Nduta. Kambi ya wakimbizi Nduta nchini Tanzania.”

Majadiliano haya yaliwafanya wajisahau kama wapo mbilingeni. Kwani Askofu Ponera alipunguza mwendo, na kuendesha wa ki-bibi harusi.

Mshindo wa mkito wa kombora lililokita mita kadhaa mbele yao nje kidogo ya barabara ndilo lililowavumbua wapinzani wao wameshawasogelea. Hofu ikarejea upya kwa mama Ndinaa, kiasi alimkumbatia Askofu Ponera kwa nguvu hadi alitaka apoteze uhimili wa kuendesha. Aliyumba kidogo.

“Tulia. Tulia, tu...” Askofu Ponera alimtuliza, lakini kabla hajahitimisha kauli yake mkito wa nguvu ukatua garini.

Haikuchelea.

Mkito ule uliotoa mshindo uliolirusha lile gari umbali wa mita kadhaa ukifuatia mlipuko mkubwa wa moto.

Ilipita dakika moja tu, toka ule mlipuko uanze, Koplo Rumera aliegesha gari hatua chache kutoka eneo la tukio. Hawakukawia, waliteremka kwa haraka garini na kulisogelea gari lilipoangukia. Katika angaza ya huku na kule, walimuona mama Ndinaa akigaa gaa kupambania uhai wake.

“Mtafuteni yule kunguni mwingine, ndiyo mwenye umuhimu kwa sasa,” Luteni Bazombanza aliamuru. Na wote kujigawa kila upande kulizunguka lile gari kwa utekelezaji.

ITAENDELEA...
 
AFRIKA YANGU—9
MTUNZI: HASSAN MBONECHE
MAWASILIANO: 0673056571

Ulikuwa ni usiku mnene, Fadhy alivyoyabarizi mandhari ya jiji kupitia lilelile dirisha alilosimama siku kadhaa zilizopita. Moja ya kingo ya dirisha, ya chini, kulikuwa na lile faili lenye utambulisho wa AFRIKA YANGU. Kuna ujumbe aliupokea, na ndiyo uliomsukuma aondoke nyumbani kwake kwa haraka kuja kuufanyia kazi.

Pindi anawasili, hali ya wingu usiku ule lilikuwa ang’avu. Upepo mdogo ulipiga pande zote na kufanya asilimia kubwa wafurahishwe kwa sababu joto lilipungua kwa kiasi fulani. Hali ya jiji ilibadilika haswa, kiasi kwamba naye hakupata msukumo wa kuwasha kiyoyozi ukizingatia dirisha lilikuwa wazi.

Baadaye aliutoa mche wa sigara kutoka pakitini aliyoihifadhi kwenye mfuko wa kaptura aliyoivaa, akaubandika mdomoni, na kuhangaika kwa muda kutafuta alipohifadhi kiberiti. Alipokipata na kukimiliki vyema mkononi hakusita kukiwasha. Ilikuwa pindi anaupeleka mkono usawa wa mdomoni akaiwashe ile sigara, pale aliposikia mlango wa ofisi ukifunguliwa. Akauzima moto kwa kutingisha mkono kiasi kisha kumwangalia aingiaye.

Mkurugenzi Idara ya usalama wa Taifa, Benson Lau.

“Karibu sana,” Fadhy alimlaki.

“Tufanye ulichoniitia,” Benson alisema.
“Kuna tatizo?”

“Mama watoto kajaa kinoma.”

Fadhy aliutoa ule mche wa sigara na kuangua kicheko.

Benson alipomfikia Fadhy aliweka tuo usawa lilipo lile faili. Na bila kuchelea, alilitwaa na kupiga hatua kurudi vilipo viti. Akaenda kuketi kilipo kiti kiashiriacho hukaliwa na kiongozi wa ofisi ile. Fadhy aliketi kiti cha mgeni.

Alilitua lile faili mezani na kulifunua.

Karatasi ya mwanzo tu, baada ya kulifunua lile faili ilikuwa na maandishi machache yaliyomchukua Benson kuyasoma kwa haraka na kuinua kichwa kumwangalia Fadhy ishara amweleweshe yanahusu nini.

“Ujumbe kutoka ubalozini nchini Burundi,” Fadhy alimfafanulia.

Akayarudisha macho yake karatasini.

Karatasi ile iliandikwa orodha ya majina. Majina mawili tu; Richard Mugaza na Ndinaa Ndiyashena.

“Hilo lenye mkolezo wa rangi na kuwekewa hizo nyota linaashiria huyo mtu sio wa kubebzwa,” Fadhy alizidi kumfafanulia. “Na sio salama kwa taifa letu.”

“Kwa...” Benson akakatishwa na kuachwa kauli yake ikielea.

“Ni mtu, au alikuwa mtu ndani ya idara ya usalama wa Taifa, na kwa sasa yupo nchini. Hivyo moja kwa moja kwetu hiyo ni hatari, hata kama ameingia kwa nia njema.”

“Tunampataje? Na vipi kuhusu huyu mwingine?” Benson aliuliza.

“Ndiyo maana nimekuhitaji chief, kwani ni ngumu mno kuliamulia peke yangu. Huyo mwingine si mtu mwenye madhara kwa usalama wa nchi yetu. Ni mtoto wa marehemu Jenerali Ndiyashena.”

Benson akainua kichwa na kumsaili Fadhy. Wakabaki wakitazamana kwa muda. Matazamano yaliyotoa shauku ya kupata mwafaka kwa haraka.

***

Mashambulizi yalizidi kumfuata Mugaza. Meja Uwizeye na vijana wake hawakufanya uzembe hata kidogo ambao wangeliutumia baadaye kujilaumu. Walisongesha mashambulizi kwa kasi pasi na kupumzika. Kila sekunde iendayo hawakusita kuruhusu mitupo ya risasi kumfuata Mugaza akimbiliapo.

Katika mitupo yote ya risasi zipo zilizompata na nyinginezo kumkosa. Nyingi zilimkosa. Chache zikamfikia. Na zile zilizomfikia, hazikumfikia sehemu hatarishi yenye kukatisha maisha yake muda huohuo. Nyingi zilimpata begani.

“Wanahitaji kufuta ushahidi wote,” Mugaza alijisemeza, akiwa amechukua maficho kwenye mti mkubwa huku akihema juujuu, damu nyingi ikimtiririka.

Alisimama pale kwenye mti kwa sekunde chache tu, baadaye akaanza upya kuchanja mbuga kutafuta sehemu sahihi ya kujihifadhi. Wakati huo hisio la maumivu likimtafuna kwa kasi. Yale majeraha yalianza kumpatia matokeo, yaliyopelekea kubadilisha hatua za utembeaji, mwisho, nguvu zilimwishia na kuanguka.

Alipoangukia palikuwa shimoni. Shimo la wastani lililopo umbali wa mita chache kutoka kwenye mti.

Akaanza kuugulia maumivu, huku akifanya bidii ya kujiganga damu isimtoke kwa wingi.

Zoezi hilo alilisitisha alipohisi michakacho ya hatua ikisogelea usawa aliopo. Akabana pumzi na kuzuia sauti isimtoke kwa nguvu. Michakacho ilivyozidi kusogea naye ndivyo alivyojizuia wanaokuja wasibaini uwepo wake. Ambao aliamini, kwa namna yoyote watakuwa wale wamfuatiliao.

Kweli.

Hatua zile zilikuwa za watu wamfuatiliao, Meja Uwizeye na vijana wake. Na walimpita kwa kasi pale alipo. Hatua za nguvu zenye mshindo uliomtanabaisha wapo katika riadha. Walivyompita, kidogo akapata ahueni. Lakini sio sana, ijapokuwa alipata nafasi ya kuwazua atumie namna gani azidi kujinusuru.

“Sipaswi kubweteka,” Mugaza alijisemeza, taratibu akijiinua kuchungulia wale watu walikokimbilia. Alichungulia kwa sekunde chache tu, lakini hakubahatika kuwaona. Akajirudi tena. “Nifanye jambo litakalonifanya niwe huru zaidi. Nifanye jambo nijiweke mbali na hawa. Lazima nifanye jambo litakaloniweka mbali nao.”

Meja Uwizeye na wale vijana hawakwenda umbali mrefu toka walivyompita Mugaza pale shimoni. Wakaweka tuo, mihemo ikiwa juujuu, baada ya kuona windo lao limewapotea katika mazingira yasiyoeleweka.

“Ametutorokaje torokaje huyu mjinga?” Meja Uwizeye aliuliza.

“Yawezekana tumemwacha huku nyuma. Au tayari amekwisha kata moto kwa yale mashambulizi tuliyompelekea,” kijana mmoja wao alitoa wazo.

“Angelikuwa amekata moto tungelimwona,” kijana mwingine alishauri. “Huyo itakuwa kuna sehemu amechepukia hukuhuku nyuma tutokako.”

“Turudi kumwangalia huku nyuma,” Meja Uwizeye alishauri. “Lakini tujigawe, ili tu-kave sehemu kubwa.”

Hakuna aliyepingana naye. Na kwa sababu miili ilishapoa kidogo, walitekeleza ushauri huo kwa haraka mno.

Msako wa kumtafuta Mugaza ukashika hatamu. Muda mwingi mboni wameziangazia chini na kwenye pande mbalimbali zilizopambwa kwa vificho vidogo vilivyotengeneza hifadhi ya mtu kutoonekana.

Katika pitapita za hapa na pale, na namna walivyokuwa wanachakua Mugaza alizisikia zile harakati. Moyo ukabaki kumpwita pwita muda wote, kijasho cha nguvu kikamtiririka, yote, kuomba maficho yake yasigundulike.

“Ewe Mola, niepushie mbali hawa mabaradhuli,” Mugaza alijisemeza, huku akijaribu kuibia ibia kuangalia kwa juu kama kuna yeyote akatizaye.

Ilikuwa pindi amejiandaa kuinua kichwa aangalie kwa nje, pale alipohisi hatua zikisogea kasi kuja alipojificha, akarudi chini kwa haraka na kupimia. Punde, akaona kiza kimeongezeka mle shimoni, ishara iliyomwaminisha kuna kitu kimesimama hatua chache kutoka pale shimoni. Hakuwa na haja ya kujihangaisha, moja kwa moja akafahamu kimesababishwa na mpiga hatua. Ambaye aliweka ukomo hatua chache kutoka shimo lilipo.

Akawa anaangaza huku na kule.

“Hii inaweza kuwa njia yangu ya uokozi,” Mugaza alijisemeza, taratibu akijiinua kutoka mlaloni.

Alivyoinuka kwa kupiga goti, akakihimiza kukipandisha kichwa kwa hadhari ampimie yule mtu. Akafanikiwa. Kwani alitokeza kidogo tu, kisha kukirejesha ndani. Kilikuwa kitendo cha sekunde chache, lakini chenye mafanikio makubwa kwa upande wake. Alimuona jinsi alivyosimama yule mtu. Alikuwa kijana, akadiriaye miaka ishirini na mbili. Moja ya bega amebeba bunduki aina ya AK 47.

“Aghalabu sasa, nalazimika kutumia taaluma na mafunzo kujihakikishia uwepo wangu duniani,” Mugaza alijisemeza akijiinua kwa mara nyingine.

Awamu hii alivyotoa kichwa alimwona yule kijana akichunguza mazingira ya upande wake wa kushoto. Kitendo kilichotoa nafasi nzuri kwa Mugaza azidi kumlea rada. Kiasi kwamba hadi alipata nafasi ya kuitandaza mikono yake ardhini na asibainike.

Yule kijana alitumia takribani dakika nne kuangaza pande za kulia na kushoto kwake. Aliporidhishwa na matokeo, akanuia kuianza safari. Ni nafasi ya pekee iliyosubiriwa kwa hamu kubwa na Mugaza. Kwani pindi moja ya mguu wake ukielea juu ili akautue, Mugaza alisafirisha mikono yake kwa uharaka akaenda kuikamata miguu ya yule kijana.

Akastaajabishwa.

Na pindi anataka kufahamu nini kilichomshikilia kwa kuinamisha kichwa aangalie, Mugaza aliivuta ile miguu kwa nguvu kuielekezea alipo. Kwa sababu kijana alikosa uhimili, alijikuta akikubaliana na kitendo kile kwa kupata anguko lililomsafirisha moja kwa moja hadi shimoni.

Anguko alilolifikia lilimfanya afikie kifudifudi na kutoa ugugumiaji wa nguvu kiasi uliosababisha sauti iwafikie wenzie. Namna ilivyosikika ikawapa mashaka, na kuwahimiza watege masikio kwa makini kusikilizia kama itasikika kwa mara nyingine. Walivyoona kimya kinashika hatamu, mashaka yakawazidi.

“Mutabazi,” Meja Uwizeye aliita kwa sauti ya nguvu. “Mutabazi, Il y a un problème?” alizidi kupaza sauti. Na ulizo juu, lililomtaka aeleze kama kuna tatizo.

Lakini juu ya jitihada zote hizo, hakukuwa na mrejesho kutoka kwa mlengwa. Kwani yule kijana aliyefahamika kwa jina la Mutabazi pale shimoni alibananishwa vilivyo na Mugaza kwa kabari moja takatifu iliyomdidimiza ardhini kiasi cha kushindwa kupumua. Mwisho alikata moto. Hapo ndipo Mugaza akamwachia na kuchukua vitu alivyoviona ni msaada kwa upande wake. Hasa bunduki.

Mara alivyoimiliki vyema mikononi aliichunguza kwanza. Kwa kuiangalia ilivyoundwa undwa, kisha alihamia kwenye kisanduku cha risasi. Aliitoa mahala pake na kujihakikishia ujazo kwa kushindilia na kidole kabla hajathibitisha kupitia tundu lililopo pembeni.

“Sasa ninacho cha kujivunia. Ni mwendo wa jino kwa jino,” Mugaza alijisemeza, pindi akirudishia kisanduku mahali pake. Baadaye aliikoki, na kujiinua pale shimoni tayari kwa kujiondoa akakate mbuga zitakazomweka huru.

Pindi Mugaza anainuka pale shimoni, Meja Uwizeye naye aliiruhusu timu yake ielekee ilikosikika sauti ya Mutabazi. Mwendo walioondoka nao haukuwa legelege, walikaza miguu na kuchanganya miondoko, kitendo kilichowafanya watumie muda mfupi kufikia mahali husika.

Walimkuta Mugaza akiishia kupanda ili aivae tambarare, wakati huo bunduki ikiwa umbali mfupi toka ulipomalizikia mkono anaotumia kujishikizia ili atoke.

***

Hakuhitaji ashtukiwe mapema, ijapokuwa alifura kwa hasira kutokana na ile ruhusa aliyoombwa. Hakuitarajia. Wala hakutaraji kama kutatokea mazingira yatakayoleta ukinzani, au viashiria vya ukinzani. Alichoamini hila yake ingelitiki muda huohuo, kisha kujichukulia ubingwa kwa urahisi.

Hivyo alimruhusu Ndinaa akafanye alichoomba kwa shingo upande.

Ile ruhusa ilimwondoa Ndinaa pale bandani na kwenda kuweka tuo umbali wa takribani mita kumi. Wakati huo moyoni akiwa na dhamirio moja tu, kuwaachia nyoya.

Hivyo alijihangaisha kwa muda pale alipofikia, kwa kufanya hiki na kile ilhali akiwatupia jicho mkengezo kuwasoma walivyojiachia na kujipa matumaini ya kurejea kwake. Akabaini itakuwa ngumu kuwachomoka. Hasa alivyobaini wote wamemwangazia yeye. Jambo lililomzalishia hisia zenye maumivu. Kwa kuhisi alichoagizwa na mama’ke hakitotimilika.

Imani hii iliyeyuka ghafla, pale alipokumbuka pilikapilika za soko. Akajiaminisha, akikimbia kuelekea vilipo vibanda vya biashara itakuwa nusura.

Hakujipa muda wa kutafakari dhamirio hili mara mbili. Alivyohitimisha tu, awamu hiyohiyo ya kwanza, akafungua riadha kuelekea vilipo vibanda vya biashara.

Cha kufia nini? Meja Uwizeye na kundi lake nao wakaunga nyuma wakiwa wenye staajabiko. Imekuaje awakimbie?

Walijiuliza, ijapokuwa jibu la moja kwa moja walishalihisi, kwamba amewabaini kuwa sio watu wazuri kwa upande wake.

Na mbio alizotokana nazo Ndinaa zilikuwa na kasi haswa. Kasi iliyowavuta waliopo pembeni wavutike kumfuatilia. Alivuta macho ya wengi. Na alivyojichanganya katikati ya watu waliopo katika pilikapilika za ununuaji mabandani ndiyo kuzidi. Kwani aliwaparamia hata kuwasukuma baadhi ili apate nafasi ya kupita.

Alivyofikia umbali fulani aliouhisi amewaacha hatua nyingi wamfuatiliao, aligeuka nyuma kuwaangalia. Bado walikuwa wanamfuatilia. Tena wakiwa na nyuso zenye uchu.

Kosa lililofanywa na Ndinaa ni kuliacha eneo la soko na kuutafuta uelekeo kambi lilipo. Hiyo ikawa nafasi mujarabu kwa kundi la Meja Uwizeye. Na wala hawakutaka kusumbuka, kwani walipunguza mwendo huku mmoja wao akichomoa bunduki alipoisundika na kuruhusu mitupo kadhaa ya risasi.

Risasi zilizopigwa zikakatiza mwendo wa Ndinaa. Zilikuwa risasi tatu, zote alipigwa pajani mguu wa kulia. Na kufanya bila mapendo, aanguke chini huku akiugulia maumivu.

Kwa wahusika wengine wa tukio, baada ya kufanya ushambuliaji wa namna hiyo wangelikimbia eneo la tukio kusalimisha maisha yao. Lakini haikuwa hivyo kwa Meja Uwizeye na kundi lake. Hawakutetereshwa na kilio cha Ndinaa wala watu walioanza kulizingira eneo la tukio kuwa sehemu ya mashuhuda. Walizidi kusonga mbele kumfuata Ndinaa pale alipoangukia.

Walivyomfikia hawakuchelea, walimtwaa juujuu na kujiondoa eneo hilo kishujaa kwa kupiga risasi kadhaa hewani kuwapa utisho watu walionza kujijenga kwa zingiro. Na hakuna aliyethubutu kukaa, wengi wao walitoka nduki ili wazidi kufaidi mema ya duniani. Huku wakitoa urahisi kwa kina Meja Uwizeye kuondoka eneo hilo.

ITAENDELEA...
 
Back
Top Bottom