RIWAYA: MKOLONI MZAWA—2
MTUNZI: HASSAN MBONECHE
SEHEMU YA 16.
Jioni, timu ya Luteni Jenerali Kipozi ilikutana Ngowe kama ilivyo ada. Awamu hii Makamu wa Rais, Lilian, IGP Lukanga na Jenerali Namkumba hawakuwepo. Alikuwepo Luteni Jenerali Kipozi, Babigamba, Ndalama, Luteni Mwaipeta, Koplo Namaya na Konstebo Babaa. Walikuwa wameketi sofani, kwa kuizunguka meza iliyowekwa ule ujumbe ulioachwa nyumbani kwa Babigamba juu yake.
“Vijana, tunafanyaje kuiokoa familia ya mwenzetu?” Luteni Jenerali Kipozi aliuliza.
Konstebo Babaa alidakia, baada ya kupita ukimya kwa muda mfupi toka Luteni Jenerali Kipozi aulize, “Huu ni mtego. Na naamini, sote hapa tunamfahamu muhusika aliyetega. Azma ya kufanya hivi, ni kumuona Babigamba hashiriki kwenye kinyang’anyiro, sasa je, tupo tayari kuona hilo likitokea?”
Wengine walijibu kwa pamoja, isipokuwa Babigamba pekee. Muda wote alikuwa kimya. “Hapana.”
“Una maoni gani?” Luteni Jenerali Kipozi alipachikia ulizo.
“Mmmmmh! Nadhani itakuwa vyema Babigamba akatii agizo lao.”
“Unamaanisha awapigie simu?”
“Yeah!”
“Huoni kuwa tukifanya hivyo tutapoteza dhamira yetu jumla? Maana ataamriwa apeleke na fomu aliyoichukua.”
“Sote hapa ni makamanda. Hatuwezi kuruhusu aende peke yake...”
Luteni Jenerali Kipozi alidakia, “Nahisi kukuelewa. Kwamba aende, halafu wengine wawe nyuma yake kwa ulinzi...”
Konstebo Babaa naye alidakia kabla Luteni Jenerali Kipozi hajamalizia kauli yake, “Na ndiyo watakaokuwa sehemu ya ukombozi. Familia haitodhurika, na fomu itabaki mikononi mwetu.”
“Good idea,” Ndalama alipongeza.
Kama walivyokubaliana, Babigamba alipiga simu kwa ile namba. Haikuchukua muda mrefu ikapokelewa, sauti nzito iliyojaa ngurumo ikasikika upande wa pili.
“Babigamba?” Sauti ya upande wa pili iliuliza. Sauti ya kiume.
Babigamba aliitikia kwa sauti iliyojaa unyonge. Wenzie wakiwa makini kumsikiliza, “Ndiyo ni mimi.”
“Nakusikiliza.”
“Nipo tayari kutii agizo lenu.”
Mtu wa upande wa pili alicheka kwa kebehi kwa muda, kisha alitokwa na kauli, “Fika Nufa Tower. Saa tano usiku.”
“Hamna shida. Nitakuwa hapo muda huo.”
“Msisitizo.”
“Ndiyo.”
“Njoo peke yako. Usitoe taarifa sehemu yoyote, na la mwisho...” alisema na kutulia.
Babigamba akadakia, “Ndiyo.”
“Usisahau fomu.” Akakata simu kabla Babigamba hajajibu.
Wenzie wakamvaa kwa wajihi ulio pomoni kwa shauku ya kutaka kufahamu alichoambiwa. Hakuwa na budi, aliwaeleza maagizo yote aliyoambiwa.
Baadaye Luteni Jenerali Kipozi aliwataarifu Makamu wa Rais, IGP na Jenerali Namkumba kuhusu hatua waliyofikia. Nao hawakupinga, walibariki wazo hilo huku wakitoa msisitizo wa umakini, ili mambo yasiangukie pua.
***
Ilivyowadia saa tano usiku tayari Babigamba alishawasili Nufa Tower. Akiwa amebeba bahasha yenye ile fomu ndani yake. Muda wote mwili ukimtetema, kutokana na mawazo yaliyokuwa yanakinzana pasi na kuyapatia ufumbuzi. Nguo alizovaa; prova yenye rangi nyeusi, kadeti rangi ya hudhurungi na raba alizozifunga vyema miguuni havikumfanya ajione yupo huru. Alijihisi yupo uchi, kwa namna ambavyo alikosa amani. Kwa kuamini kila mmoja anafahamu matatizo apitiayo.
Ilivyogota saa 5:05 usiku alipiga simu kwenye ile namba. Ilivyopokelewa alitaarifu uwepo wake mahali hapo.
“Kuwa na subira. Acha papara Makamu,” mtu wa upande wa pili wa simu aliongea kwa kebehi. Mwisho wa kauli alimalizia cheko dogo lenye mguno.
Dakika saba baadaye toka alivyopiga simu iliwasili gari ndogo mbele yake. Noah. Aliikumbuka, ni ile ile waliyotumia watu waliomvamia mchana. Mmoja kati ya watu waliomo ndani ya gari aliteremsha kioo, na kumpa ishara Babigamba aingie. Mlango ulifunguliwa. Babigamba akaingia.
Safari ilipamba moto.
Akiwa ndani ya gari, Babigamba alifungwa kitambaa cheusi na kizito usoni. Lengo, asifahamu uelekeo wa safari aendayo. Hivyo baada ya pita pita za hapa na pale zilizowachukua takribani saa mbili, hatimaye walifikia ukomo wa safari. Bondeni. Karibu na mpaka wa kuingia mkoa wa Makong’onda.
Babigamba aliteremshwa na kuingizwa ndani ya mjengo fulani wa kifahari, ambao hauleti mashaka kwa wapita njia, kama unahusika kuficha maovu. Hasa watendewayo wapingaji wa utawala wa Rais Sharabu. Lilikuwa jengo la ghorofa moja.
Walivyofikia ukomo mule ndani, Babigamba alifunguliwa kile kitambaa. Akapikicha macho apate kuona vyema. Alishtuka kuwaona mkewe na mwanaye wamefungwa kwenye viti huku wakitokwa na machozi. Uchungu ukachipua upya. Nafsi ilitokota kwa hasira maradufu, kiasi kwamba alitamani awe na nguvu za miujiza apambane na wapinzani wake.
“Tulia, hupaswi kuwa na papara kupambana nao,” kuna sauti aliisikia ikimuonya. Akatua pumzi kwa nguvu.
Ukiachilia mbali familia yake, mwingine ambaye alikuwepo mule ndani ni Shida. Ikamfanya afahamu, huyo ndiye aliyehusika kuwateka. Alitokea kumchukia, na kujipa kazi ya kumsaili anafananaje na uhalifu anaoufanya.
“Endapo nitatoka hapa salama, sitowaacha hai mbwa ninyi,” alijisemeza. Taratibu mboni zikilengwa na machozi.
Baadaye aliingia Maua mule ndani. Hakuamini, kama naye ni sehemu ya timu. Akafuatwa hadi pale aliposimama.
“Oooh! Mgombea,” Maua aliita kwa kejeli. Akiwa amesimama takribani umbali wa mita moja, toka aliposimama Babigamba. Babigamba akamtupia jicho la shari.
“Acha nikuweke wazi, tuna uwezo wa kukufanya lolote na hakuna mtu atakayetuongelea kwa ubaya huko nje. Kwa usalama wako, usijihusishe na hiki ukitakacho kukifanya. Umenielewa?”
Babigamba hakujibu. Maua akaona isiwe shida, akaendelea kuzungumza. Muda wote, mikono yake kaiweka mifukoni mwa koti alilovaa. Koti kubwa la manyoya manyoya. Kichwani alivaa boshori.
“Hivyo tupatie fomu yetu, kisha tukurudishie familia yako.”
Wakati wote huo, mkewe na mwanaye walikuwa wanalia kwa uchungu, huku kilio kikiomba huruma yake katika maamuzi.
Airudishe fomu aikomboe familia? Ili aachane na mpango kama alivyoambiwa. Ama atafute namna ya kupambana nao vitu vyote vibaki mikononi mwake. Alikuwa na wakati mgumu wa kuamua.
***
Luteni Mwaipeta, Koplo Namaya na Konstebo Babaa walikuwa mita chache toka kwenye ule mjengo alioingizwa Babigamba. Mjengo ulizongukwa na wigo mrefu kiasi. Lakini haukuzuia baadhi ya mazingira kuonekana, kutokana na urembo uliopo.
Muonekano wao ulikuwa wa ki-komando zaidi. Kwani walivaa kombati za mtumba rangi ya khaki ya majeshi ya nje, walibeba bunduki kubwa za kimapigano ya mbali, pasi na kusahau mapeki mgongoni. Bunduki walizobeba ni jamii ya SMG; Luteni Mwaipeta alibeba M21, Koplo Namaya alibeba M21S na Konstebo Babaa alibeba M21BS.
Ndani ya mapeki waliweka vilipuzi na mabomu kadhaa ya mkono, yatumikayo kutulizia ghasia. Hasa mabomu yenye moshi mwingi unaowasha. Vilevile waliweka kamba ngumu, ambazo mara nyingi hutumika kuvukia vikwazo.
Pasi na kusahau holster. Zilizofungwa pajani zikiwa na bastola.
Hivyo ndivyo vifaa vya kazi walivyobeba. Wakati kwenye mavazi, ukiachana na kombati, chini walipigilia buti, vidoleni walivaa glavu na kichwani boshori, ambazo walizishusha hadi usoni, huku zikiwa na tundu kadhaa zilizowawezesha kuona na kupumua.
Kwa haraka haraka waliweza kufahamu, mjengo huo upo chini ya ulinzi mkali. Walibaini kupitia kamera za CCTV zilizofungwa kona mbalimbali. Na juu ya ule wigo, kulikuwa na nyaya zenye mionzi ya umeme. Ikawapatia wakati mgumu wa kuwazua mbinu watakayotumia kuingilia.
“Daima majengo ya namna hii haikosi milango ya nyuma,” Konstebo Babaa aliongea. Mboni zake kazitupia kwa udadisi mkubwa mjengoni.
“Kwa hiyo unashaurije?” Luteni Mwaipeta aliuliza.
“Tutumie mlango wa nyuma kuingia. Tukitumia huku mbele tutawashtua mapema na kupelekea walengwa wetu kuwaweka kwenye hatari zaidi.”
“Kama hakuna mlango?”
“Hauwezi kukosa.”
Walivyoafikiana walipiga hatua za mnyato huku wakizikwepa kamera hadi upande wa nyuma wa lile jengo. Hakika, ulikuwepo mlango mdogo wa dharura. Wakatabasamu. Wakiwa takribani umbali wa mita sitini toka wigo ulipo.
“Koplo Namaya,” Luteni Mwaipeta aliita.
“Ndiyo afande wangu.”
“Ewe ndiyo mlinzi wetu. Hivyo hautopaswa kuingia ndani. Take camouflage, and you will be our sniper.”
Koplo Namaya alijibu kwa kutingisha kichwa.
“Kingine...” Luteni Mwaipeta alisema na kutulia kwa muda. Koplo Namaya akamtumbulia pima mboni zake kumwashiria aendelee kuzungumza anamsikiliza. Luteni Mwaipeta akaendelea, “...hakikisha unatulinda dhidi ya kamera zote zilizopo upande huu.”
“Hamna shida. Kwangu ni utekelezaji.”
Dakika tatu zijazo Koplo Namaya alikuwa juu ya mti wa muembe uliopo umbali wa takribani mita mia moja na nusu toka jengo lilipo. Akatega moja ya tawi, kisha akaanza shughuli ya kuangaza mazingira yote yazungukayo jengo kupitia darubini iliyofungwa juu ya bunduki. Kila kamera aliyoiona hakuacha kufanya alivyoambiwa. Alizishambulia, zikapoteza uelekeo wa kurekodi matukio, zingine zilikatika na kuanguka chini.
“Njia nyeupe kwenu,” Koplo Namaya aliwataarifu wenzie kwa kutumia redio maalumu za mawasiliano. Ambazo walichomeka waya na kubandika visikilizio masikioni.
“Vipi ndani?” Luteni Mwaipeta aliuliza.
“Kwa upande wa nyuma nako ni kweupe. Sijajua upande wa mbele maana siuoni.”
“Okay! Endelea kutupa ulinzi.”
Baada ya mrejesho huo Luteni Mwaipeta na Konstebo Babaa walifungua mapeki na kutoa kamba, ambazo upande mmoja ilifungwa nondo iliyotengenezwa mfano wa ndoano. Wakazirushia ndani ya wigo usawa wa ule mlango. Ambao juu yake hakukuwa na zile nyaya za umeme.
Walifuatia kuzivuta kidogo na kugota sehemu. Ndicho walichokitaka, hivyo sekunde kadhaa baadaye walikuwa wanapanda kwa msaada wa mlango kuingia uani. Walivyofika juu walirukia chini na kuziondoa zile kamba kwa haraka wakazirejesha pekini.
Hawakupoa, kitendo hicho kilifanyika kwa muda mfupi sana, walivyomaliza walipiga hatua taratibu zenye mshindo mdogo hadi mlango wa nyuma wa jengo. Wakajibanza ukutani, mbele akiwa ametangulia Luteni Mwaipeta, nyuma Konstebo Babaa.
Pele mlangoni walisikilizia kwa muda mfupi, kuona kama watasikia mshindo wowote aidha kutoka ndani, au upande mwingine hapo uani.
Ukimya ulitamalaki.
Walivyojihakikishia kupo shwari, Luteni Mwaipeta alichomoa kilipuzi kutoka kwenye moja ya mfuko wa suruali akapachika pale mlangoni, usawa wa kitasa kilipo.
Wakaanza kuzihesabu sekunde, ilivyogota kumi, ulitokea mlipuko wenye mshindo mkubwa ulioambatana na moshi mwingi. Hawakusubiri ule moshi upungue, waliingia vivyo hivyo, wakiwa wamejigawa na mitutu ipo juu usawa wa ulengaji.
***
Vijana wawili waliopo chumba cha kuongozea kamera za lile jengo waliwaona kina Luteni Mwaipeta wanavyoingia mara baada ya mlango kulipuka. Walinaswa na kamera iliyotegwa moja ya kona, kabla Konstebo Babaa hajaishambulia.
Hawakuvumilia tukio hilo. Haraka sana, mmoja wao alivuta kiwambo cha simu ya mezani na kubonyeza vitufe kadhaa kisha alikisogeza kile kiwambo sikioni. Iliita kwa sekunde chache, ilivyopokelewa na mtu wa upande wa pili, Killa, wakawa kwenye mazungumzo.
“Tumebaini uwepo wa wavamizi pale mjengoni. Wamefanikiwa kuingia ndani kupitia mlango wa nyuma,” yule kijana alimtaarifu.
“Ahsante kwa taarifa.” Killa alijibu na kushusha kiwambo mahali pake.
Killa aliipokea ile taarifa kwa mshtuko sana. Hao wavamizi alioambiwa wamewezaje kupafahamu mahali hapo? Alitatizika. Na kumfanya aghadhibike, kwa sababu hakuwa na matarajio ya kupata habari ya namna hiyo.
“Babigamba unajifanya mjanja? Unajifanya don-town?” alijiuliza akiwa anabonyeza bonyeza kwenye simu janja yake. Baada ya muda, alikuwa kwenye maongezi na mtu wa upande wa pili. Mmoja ya walinzi wa lile jengo.
“Kuna wavamizi wameingia kwa kutumia mlango wa nyuma. Hakikisheni hawafiki juu.”
“Sawa bosi.” Akakata simu.
Akaunga mawasiliano kwa mtu mwingine. Maua.
“Usimchekee huyo mbwa.”
“Kuna’ni?” Maua aliuliza akimtupia Babigamba mboni za kumsaili kulingana na maelezo anayopatiwa.
“Hapo hajaja peke yake.”
Simu ikakatwa. Maua akaongeza usaili kwa Babigamba. Wa awamu hii ulijaa dhihaka.
“Ooooh! Babi...” alimuita kwa ufupi na kutulia kwa sekunde chache. Akaendelea, “...unadhani utaweza kutoka salama kwa huo mchezo ulioufanya?” akapiga hatua taratibu kumfuata Babigamba aliposimama.
Babigamba hakumjibu. Aliishia kumwangalia kwa aibu huku akitafakari kauli aambiwayo.
Killa alivyomaliza maongezi alijiandaa kwenda kuongeza nguvu. Wakati vijana wa ulinzi; wawili, waliopo geti la mbele, walitoka nduki wakiwa wamekamatia vyema bastola zao mikononi kuelekea walipoelekezwa. Upande wa nyuma wa jengo, ambao Luteni Mwaipeta na Konstebo Babaa wametumia kuingilia.
Vilevile Maua hakukaa nayo ile taarifa, aliwatonya Kinyonga na Shida. Nao chap, walibeba zana za kazi na kuteremka chini kwa kunyemelea. Hatua taratibu zisizo na mshindo, mboni zikikesha huku na kule, walipeleka kila kona, tena kwa uangalifu mkubwa ili wasipate kuhadhirika dhidi ya maadui zao.
Haikuchukua muda mrefu Killa kuwasili. Aliwasili kwa mingi mihemko, ya kuhakikisha hakuna atakayetoka salama katika watu hao waliovamia mjengoni mwao. Ambao alifahamu fika, lengo la ujio wao ni kumuokoa Babigamba na familia yake.
ITAENDELEA...
HABARI NJEMA.
KITABU CHA RIWAYA YA #NENDA KINAENDELEA KUPATIKANA #RENICS_BOOKSHOP TAWI LA MOSHI KWA GHARAMA YA TSH. 10,000/= MAWASILIANO: 0767826134